Showing posts with label biashara. Show all posts
Showing posts with label biashara. Show all posts

SMZ YATAJA MAFANIKIO YA BIMA YA LAZIMA KWA WAGENI

Kajunason June 07, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imetumia Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Karibu-KiliFair 2026 kutangaza mafanikio ya mpango wa bima ya lazima kwa wasafiri, ikieleza kuwa umeimarisha usalama wa wageni na kuchangia ukuaji wa sekta ya afya pamoja na mapato ya utalii visiwani humo.

Mpango huo ulioanza kutekelezwa rasmi Oktoba 1, 2024, unawataka wageni wote wa kimataifa wanaoingia Zanzibar kuwa na bima ya usafiri kabla ya kuwasili. Tangu kuanzishwa kwake, mpango huo umeendelea kuwa chanzo muhimu cha mapato, ukiingiza wastani wa dola za Marekani milioni moja, sawa na zaidi ya Sh bilioni 2.6 kila mwezi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika banda la Shirika la Bima Zanzibar (ZIC) kwenye viwanja vya Magereza jijini Arusha, Ofisa Mauzo wa shirika hilo, Abdul-Halim Muhammad, alisema maonesho hayo yamewapa fursa ya kutoa elimu kwa watalii, wawekezaji na wadau wa sekta ya utalii kuhusu umuhimu wa bima hiyo.

“Tunashiriki Karibu-KiliFair kuongeza uelewa kuhusu bima hii ya lazima na kueleza namna inavyowanufaisha wageni huku ikichangia maendeleo ya huduma muhimu Zanzibar,” alisema.

Kwa mujibu wa utaratibu huo, wageni wengi wa kimataifa hulipa dola 44 za Marekani kwa kila safari ya kuingia Zanzibar, huku wageni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wakilipia dola 22 pekee. Watoto wenye umri wa miaka mitatu hadi 17 hulipa dola 22, huku walio chini ya umri huo wakisamehewa.

Muhammad alisema bima hiyo inawawezesha wageni kupata huduma za matibabu ya dharura na msaada mwingine muhimu wanapokuwa Zanzibar, hatua inayopunguza changamoto za kifedha na kuhakikisha wanapata huduma kwa haraka wanapozihitaji.

Alisema sehemu ya mapato yanayokusanywa kupitia mfuko huo hutumika kugharamia huduma za afya kwa wageni waliokatiwa bima, huku fedha zinazobaki zikielekezwa katika kuimarisha huduma za afya kwa wananchi na wageni kwa ujumla.
“Mpango huu ulianzishwa baada ya mamlaka kubaini kuwepo kwa matukio ya mara kwa mara ya watalii na wawekezaji kuhitaji matibabu ya dharura huku kukiwa na sintofahamu kuhusu nani angegharamia huduma hizo. Sasa mfumo huu umeondoa changamoto hiyo,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa KiliFair Promotions, Dominic Shoo, alisema Karibu-KiliFair 2026 imeendelea kuthibitisha nafasi yake kama maonesho makubwa ya utalii na biashara Afrika Mashariki kwa kuwakutanisha wadau kutoka zaidi ya nchi 40 duniani.

Alisema maonesho hayo yamevutia zaidi ya waoneshaji 500 na wanunuzi wa huduma za utalii wapatao 20,000, hatua inayochochea uwekezaji, ushirikiano wa kibiashara na upanuzi wa masoko ya utalii katika ukanda wa Afrika Mashariki.

“Karibu-KiliFair ni jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania na Afrika Mashariki kimataifa. Kadri wadau wanavyoongezeka kushiriki, ndivyo fursa za biashara, uwekezaji na ukuaji wa sekta ya utalii zinavyozidi kuongezeka,” alisema Shoo. 

MAADHIMISHO YA 11 YA UTAFITI NA UBUNIFU UDSM KUANGAZIA UCHUMI WA KIDIJITALI

Kajunason June 07, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kinatarajia kuadhimisha Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu kuanzia Juni 9 hadi 11, 2026, katika Kampasi ya Mwalimu Julius Nyerere, huku Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, akitarajiwa kuwa mgeni rasmi.

Maadhimisho hayo yatakayowakutanisha watafiti, wabunifu, wanafunzi, sekta binafsi, taasisi za umma na wadau wa maendeleo, yanalenga kuonesha mchango wa utafiti na ubunifu katika kuharakisha maendeleo ya taifa na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Utafiti, Profesa Nelson Boniface, alisema maadhimisho ya mwaka huu yataongozwa na kaulimbiu isemayo: "Kutumia Utajiri wa Madini wa Tanzania katika Kukuza Nishati Jadidifu, Mageuzi ya Kidijitali na Usalama wa Jamii."

Alisema kaulimbiu hiyo imechaguliwa kutokana na umuhimu wa madini katika maendeleo ya teknolojia za kisasa ikiwemo Akili Mnemba (AI), vituo vya kuhifadhi taarifa (Data Centres), magari ya umeme na nishati jadidifu.

“Tunataka kuonesha namna Tanzania inaweza kutumia rasilimali zake za madini kuchochea mageuzi ya kidijitali, kuimarisha usalama wa nishati na kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi,” alisema Profesa Boniface.

Aliongeza kuwa maadhimisho hayo yatahusisha maonesho ya tafiti na ubunifu, mawasilisho ya kitaaluma, makongamano pamoja na majadiliano ya ushirikiano wa kimkakati yatakayowawezesha washiriki kubadilishana maarifa na kujenga mitandao ya kitaaluma na kibiashara.

Kwa mujibu wa UDSM, maadhimisho hayo yatatoa nafasi kwa watafiti na wabunifu kuonesha suluhisho mbalimbali za kisayansi na kiteknolojia zinazolenga kukabiliana na changamoto za maendeleo nchini katika sekta za madini, nishati, kilimo, afya na uchumi wa kidijitali.

Profesa Boniface alisema chuo kinaendelea kutumia maadhimisho hayo kama jukwaa la kuunganisha taaluma, ubunifu na maendeleo ya taifa kwa kuwafikia wananchi, wawekezaji na wadau mbalimbali wa maendeleo.

"Utafiti na ubunifu ni msingi wa maendeleo endelevu. Tunawaalika Watanzania wote kushiriki katika Maadhimisho ya 11 ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu UDSM 2026 ili kujionea kazi na mafanikio ya watafiti na wabunifu wetu," alisema.

TEMESA NA TOYOTA WAJADILI MAGEUZI YA HUDUMA ZA MATENGENEZO YA MAGARI NCHINI

June 03, 2026 Add Comment

.


Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania - TEMESA, Bw. Kheri Mahimbali, leo tarehe 02 Juni 2026 amekutana na viongozi wa kampuni ya TOYOTA Tanzania katika ofisi zao eneo la Posta, jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine wamejadili kuhusu jitihada za Serikali katika kuendelea kuboresha huduma za matengenezo ya magari hapa Nchini. 

Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Mahimbali amesema TEMESA imejipanga kuhakikisha huduma za ufundi na matengenezo ya magari ya Serikali  zinatolewa kwa viwango vya juu kwa kutumia teknolojia za kisasa na za viwango vya kimataifa.

“TEMESA inaona fursa kubwa katika kuimarisha ushirikiano na TOYOTA kupitia miradi ya pamoja itakayowezesha taasisi hizi mbili kubadilishana utaalamu kwa mafundi na kuongeza ufanisi wa huduma zinazotolewa kwa wadau wetu,” amesema Mtendaji Mkuu.

Kwa upande wake, Meneja Mkuu wa TOYOTA Tanzania, Bw. Jatin Pandya amehakikisha utayari wa kampuni hiyo kuendelea kushirikiana na TEMESA katika mafunzo ya kitaalamu kwa mafundi, ushauri wa kiufundi, matumizi ya teknolojia mpya na kuimarisha mifumo ya usalama wa magari.

“Sisi TOYOTA tunatanguliza usalama wa watumiaji wa magari na ubora wa huduma. Tunaamini ushirikiano huu utachangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha huduma za matengenezo ya magari nchini na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani,” amesisitiza Pandya.

Aidha, mara baada ya kikao hicho, Mtendajji mkuu pia alipata fursa ya kufanya ziara fupi katika karakana za TOYOTA ili kujionea teknolojia mpya zinazotumika katika matengenezo ya magari.

Miongoni mwa mambo waliyojadili katika kikao hicho ni pamoja na uwezekano wa kuanzisha ushirikiano kupitia mfumo wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi - PPP. Hatua inayotarajiwa kuimarisha uwezo wa karakana na kuongeza ufanisi wa huduma katika sekta ya matengenezo ya magari.

Kikao hicho kimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya TEMESA na TOYOTA, huku kikitarajiwa kuwa chachu ya mageuzi makubwa katika sekta ya ufundi wa magari nchini.


JUKWAA LA WANAWAKE NA KODI NI HATUA MUHIMU YA KUENDELEZA USAWA WA KIJINSIA NA KUKUZA UCHUMI SHIRIKISHI -CPA CASTRO

May 14, 2026 Add Comment



 Na Paskal Mbunga, Tanga

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga imesema kwamba Jukwaa la Wanawake na Kodi ni hatua muhimu inayodhihirisha dhamira ya kuendeleza usawa wa kijinsia na kukuza uchumi shirikishi nchini.

Hayo yalisemwa na  Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Tanga, CPA Castro John wakati akifungua Jukwaa la Wanawake na Kodi ambapo  alisema ni dhamira ya dhati ya kujenga mfumo wa kodi unaoshirikisha makundi yote ya jamii, hususan wanawake ambao ni nguzo muhimu ya uchumi wa Taifa.


Alisema takwimu zinaonesha wanawake wanachangia kwa kiwango kikubwa katika shughuli mbalimbali za kiuchumi zikiwemo biashara ndogondogo, kilimo, huduma, viwanda vidogo pamoja na biashara za kati na kubwa.

Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2024/2025, wanawake nchini, wakiwemo wa Mkoa wa Tanga, wanakadiriwa kushiriki katika nguvu kazi kwa asilimia 80, huku wakimiliki asilimia 54 ya biashara ndogo, za kati na kubwa.

“Bila ushiriki wa wanawake, juhudi za kuongeza wigo wa walipa kodi na kuongeza mapato ya ndani haziwezi kufikia malengo yaliyokusudiwa,” alisema CPA Casto John.

Alifafanua kuwa TRA imeanzisha Jukwaa hilo maalumu kwa lengo la kutoa elimu sahihi ya kodi, kusikiliza changamoto za wanawake wafanyabiashara, kujenga ushirikiano wa karibu pamoja na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na kwa wakati.

Aidha, alisema TRA imejikita katika kuboresha huduma kwa kuzingatia ushirikishwaji, uwazi, weledi na urahisi wa upatikanaji wa huduma. Aliongeza kuwa elimu ya kodi na mahusiano bora ni msingi muhimu wa kuongeza utii wa kodi.

Kupitia jukwaa hilo, wanawake watapata nafasi ya kupata ushauri kuhusu masuala ya kodi, kujifunza fursa mbalimbali pamoja na kuelewa wajibu wao wa kikodi.

“Tunataka mwanamke ajisikie salama, aheshimiwe na ashiriki kikamilifu katika mfumo wa kodi bila hofu wala kikwazo chochote,” alisema.

CPA Casto John alisisitiza kuwa kodi ndiyo injini ya maendeleo ya Taifa kwani mapato yake yanagharamia huduma muhimu kama elimu, afya, barabara, maji safi na miradi mingine ya kimkakati.

“Kila mwanamke anayelipa kodi anakuwa mshirika wa moja kwa moja wa Serikali katika kujenga Tanzania yenye uchumi imara na huduma bora kwa wananchi wake,” aliongeza.

Pia aliwataka wanawake kutumia jukwaa hilo kujifunza, kuuliza maswali na kuwa mabalozi wa utamaduni wa kulipa kodi katika jamii zao.

Aidha, aliwataka wadau wa sekta mbalimbali pamoja na taasisi za kifedha kuendelea kushirikiana na TRA katika kuwawezesha wanawake kukuza biashara zao kwa kuzingatia misingi ya kikodi.

Kwa upande mwingine, aliwahimiza wanawake wafanyabiashara kujisajili katika mfumo wa kodi na kutekeleza wajibu wao kwa hiari na kwa wakati.

“Kulipa kodi si wajibu wa kisheria tu, bali ni mchango wa moja kwa moja katika kujenga Taifa. Wanawake wakisimama kiuchumi, familia na jamii vinaimarika,” alisema.

Katika hatua nyingine, alisisitiza umuhimu wa kutumia mipaka rasmi ya biashara kwa wafanyabiashara wanaovuka mipaka kupitia maeneo ya Horohoro na Pangani, huku akiwataka kuachana na biashara za magendo na matumizi ya njia zisizo rasmi.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini, JW Ismail Masound, alisema jukwaa hilo lina umuhimu mkubwa kutokana na malengo ya Dira ya Taifa ya mwaka 2050 ambapo sekta binafsi inatarajiwa kuwa mhimili mkubwa wa ukuaji wa uchumi.

Alisema majukwaa hayo yanasaidia kuwawezesha wanawake na wafanyabiashara kufikia malengo ya maendeleo ya Taifa kwa kuongeza ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake Mkoa wa Tanga (TWCC), Aziza Ramadhani, alisema jukwaa hilo litawasaidia wanawake kuelewa umuhimu wa kulipa kodi katika kukuza uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.

“Hivyo ni wajibu wetu kuhakikisha Mkoa wa Tanga unalipa kodi kutokana na umuhimu wake kwa maendeleo ya jamii,” alisema.

Aliongeza kuwa jukumu la jukwaa hilo ni kuwaunganisha wanawake wa Mkoa wa Tanga ili kuwapa nafasi ya kujifunza, kushirikiana na kupata fursa mbalimbali za kiuchumi ndani na nje ya mkoa huo.

Aidha, alisema wamekuwa wakitoa mafunzo mbalimbali ikiwemo kuanzisha mashamba darasa kwa vijana wa kiume na wa kike, huku akiwakaribisha wanawake wajasiriamali kushiriki katika shughuli za maendeleo zinazochangia ukuaji wa uchumi wa Mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.




TANGA YAZIDI KUFUNGUKA KIUCHUMI, WAWEKEZAJI WAMIMINIKA

May 03, 2026 Add Comment


Na Oscar Assenga, Tanga

Mkoa wa Tanga unaendelea kuandika historia mpya ya kiuchumi kufuatia kuongezeka kwa kasi kwa wawekezaji na kuimarika kwa miundombinu, hatua inayotajwa kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa biashara na mapato ya serikali.

Akifungua kikao cha Baraza la Biashara la Mkoa huo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Batilda Burian, alisema lengo la kikao hicho ni kujadili kwa kina namna ya kuboresha mazingira ya biashara ili yawe rafiki na wezeshi zaidi, pamoja na kuibua fursa za uwekezaji na kutafuta suluhisho la changamoto zinazoikabili sekta hiyo.

Alisema serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kuboresha mfumo wa kodi, akieleza kuwa tayari Rais aliunda tume maalum iliyopitia kodi mbalimbali na kutoa mapendekezo.

Alibainisha kuwa mkoa unasubiri utekelezaji wa mapendekezo hayo ili kusaidia kuondoa migongano ya kodi, hususan zile za halmashauri zilizokuwa zikilalamikiwa na wafanyabiashara.

Katika hatua nyingine, Balozi Burian alisema Tanga imekuwa kivutio kikubwa cha uwekezaji, huku Jiji la Tanga likiongoza kwa kupokea wawekezaji wengi zaidi.
 

Aliongeza kuwa uwekezaji huo sasa umeanza kusambaa hadi wilaya za Muheza na Korogwe, ambako kunatarajiwa kujengwa kiwanda kikubwa cha sukari pamoja na kuanzishwa kwa bandari kavu.

Akizungumzia mafanikio ya Bandari ya Tanga, alisema kumekuwa na ongezeko kubwa la shehena ya mizigo kutoka tani 470,000 sasa wanapokea zaidi ya tani milioni 1.3, jambo linalochochea ukuaji wa uchumi.

Alifafanua kuwa kwa sasa takriban meli 60 huingia bandarini kila mwezi, ikilinganishwa na meli 18 hapo awali, huku kila meli ikiingiza Bandarini wastani wa shilingi bilioni 2 kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

“Tunafanya jitihada kuhakikisha ufanisi wa bandari unaongezeka zaidi kwa kupunguza muda wa kuhudumia meli na kuondoa msongamano, ili kuongeza tija kwa sekta binafsi na serikali kwa ujumla,” alisema.

Kuhusu miradi ya kimkakati, Balozi Burian alisema mradi wa bomba la mafuta wa EACOP umefikia hatua za mwisho, huku ukitarajiwa kuanza rasmi kupitisha mafuta kati ya mwezi Juni na Julai.

Alisema mradi huo tayari umetoa fidia ya zaidi ya shilingi bilioni 10 kwa wananchi na kutoa ajira kwa zaidi ya watu 1,700.

Katika sekta ya miundombinu, ujenzi wa barabara ya Tanga–Pangani unaendelea, licha ya changamoto za mvua, huku serikali ikiahidi kuhakikisha shughuli za biashara haziathiriki.

Aidha, uwanja wa ndege wa Tanga unaendelea kuboreshwa kwa gharama ya shilingi bilioni 63, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa jengo la abiria, uzio na upanuzi wa njia ya kurukia ndege ili kuruhusu ndege kubwa kutua.

Kwa upande wa viwanda, serikali ya mkoa kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara inaendelea kufuatlia viwanda vilivyokuwa vimekufa na kuvifufua viwanda vilivyokufa na kuvutia uwekezaji mpya.

Ikiwemo kutaka Maeneo ya uwekezaji yaliyotengwa kupitia TISEZA sasa yanasimamiwa kwa karibu zaidi na kuwekwa alama ili wawekezaji wanapokwenda waweze kuwekeza na tayari mwekezaji mmoja ameonyesha nia ya kujenga kiwanda cha nondo.

Sekta ya utalii nayo imeelezwa kuwa na fursa kubwa, hususan katika maeneo ya fukwe za Pangani na Mking ambapo alisema kwamba Pangani wana maeneo ya Kipumbwi wanayagawa kwa ajili ya uwekezaji kwenye fukwe na Mkinga katika maeneo ya Kwale na maeneo mengine ya Fukwe .


Aliongeza pia kwamba kuna uwekezaji mkubwa katika soko la Samaki na ni juzi tu Rais alizindua Meli kubwa ya Uvuvi wa Bahari ya Kuu na Meli hiyo itavua mpaka Tanga lakini katika meli nne zitakapotimia nadhani moja itakuja kufanya shughuli zake hapa Tanga .


Akisisitiza wana imani wataanza kutumia rasilimali za bahari kwa ufanisi na itakuwa na mchango mkubwa kutokana na kwamba kuwepo na masoko ya Samaki ikiwemo ,Mkinga,Tanga eneo la Deepsea na soko la Samaki la Kimataifa la Kipumbwi.

Sambamba na hilo, uwekezaji katika uvuvi wa bahari kuu unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa samaki na kuimarisha masoko, ikiwemo soko la kimataifa la samaki la Kipumbwi.

Awali, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Mchatta, alisema Baraza la Biashara ni jukwaa muhimu linaloleta pamoja sekta ya umma na binafsi kwa lengo la kujenga mazingira bora ya biashara, kuimarisha uaminifu na kuhakikisha sekta binafsi inakuwa endelevu.


MH. LUSWETULA: TRA IHARAKISHE TATHMINI YA MAHITAJI YA VITUO VYA FORODHA.

April 08, 2026 Add Comment


Na. Saidina Msangi, WF, Dodoma.

Serikali imesema kuwa kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inaendelea kufanya tathmini ya mahitaji ya ujenzi wa Kituo cha Forodha katika Jimbo la Momba, ikiwemo upembuzi yakinifu, upatikanaji na utambuzi wa eneo, gharama za mradi na utayari wa nchi jirani.

Hayo yalisemwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Momba, Mhe. Condester Michael Sichalwe, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itajenga kituo cha forodha katika Jimbo la Momba mkoa wa Songwe.

Alisema eneo hilo linaangaliwa kwa kuzingatia ongezeko la shughuli za biashara na umuhimu wake katika kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato na udhibiti wa biashara mipakani.

’’Ujenzi wa vituo vya forodha, ikiwemo katika Jimbo la Momba, hufanyika kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali, ukamilifu wa taratibu na kanuni za kiforodha, utayari wa nchi jirani tunazopakana nazo, masuala ya kiusalama, upatikanaji wa rasilimali fedha, pamoja na tathmini ya umuhimu wa eneo husika katika shughuli za biashara za mipakani,’’ alifafanua Mhe. Luswetula.

Aliongeza kuwa ujenzi wa kituo hicho utaanza mara baada ya kukamilika kwa maandalizi yote muhimu, ikiwa ni pamoja na kupatikana kwa fedha za utekelezaji wa mradi katika bajeti ya Serikali na kutangazwa kwenye Gazeti la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aidha, Mhe. Luswetula alieleza kuwa TRA inaendelea na maandalizi na itatoa taarifa rasmi pindi ratiba ya utekelezaji wa ujenzi itakapokamilika na kuielekeza TRA kuharakisha tathmini hiyo ambayo iko katika hatua za mwisho.

TANZANIA YANG’ARA KIMATAIFA KWA USIMAMIZI BORA WA DENI LA SERIKALI

March 28, 2026 Add Comment

  Na Joseph Mahumi, WF


Serikali ya Tanzania imeendelea kung’ara katika jukwaa la kimataifa baada ya kuibuka mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.

Ushindi huo mkubwa unatokana na juhudi za Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa deni la umma, ikiwemo kuunganisha vyema mifumo ya kifedha ya Serikali na kuboresha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya maendeleo, ambapo Jopo huru la wataalamu lililochambua mawasilisho kutoka nchi mbalimbali za Jumuiya ya Madola lilizingatia vigezo vya ubunifu, uimara na uendelevu katika kutoa tuzo hizo.

Akifungua hafla ya utoaji tuzo hizo, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal, alisisitiza umuhimu wa nchi wanachama kuendelea kubuni mbinu madhubuti za kusimamia deni la umma ili kulinda uchumi dhidi ya misukosuko ya kifedha duniani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola, Bi. Ruth Kattumuri, aliipongeza Tanzania kwa mageuzi makubwa iliyoyafanya katika kuimarisha usimamizi wa deni la umma.

Alieleza kuwa mafanikio hayo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya nchi katika kujenga uchumi imara na unaostahimili mishtuko ya kiuchumi.

Aidha, Bi. Kattumuri, alisema kuwa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola itaendelea kuisaidia Tanzania katika juhudi zake za kuboresha sera na mifumo ya usimamizi wa deni, sambamba na utekelezaji wa maazimio ya Kikao cha 72 cha Kundi la Mawaziri wa Jumuiya ya Madola.

Mkutano huo wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola uliofanyika kwa muda wa wiki moja uliwakutanisha wataalamu wa usimamizi wa deni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kujifunza na kujadili mbinu bora za kukopa, kusimamia na kulipa deni la umma, na umeandaliwa ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Jumuiya ya Madola wa Deni Imara, Bunifu na Endelevu, ambapo Tanzania imejitokeza kama kinara na mfano wa kuigwa barani Afrika na katika Jumuiya nzima ya Madola.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) akiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal (kushoto) na  Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya hiyo, Bi. Ruth Kattumuri.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama, akionesha tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) Aakiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni washindi wenngine wa tuzo hizo kutoka nchi ya Barbados ambayo iliibuka mshindi wa Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Caribbean na Sri Lanka Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Asia.

AIRTEL TANZANIA YAZINDUA MADUKA 17 YA SMART SHOPS DAR ES SALAM ,KUKUZA HUDUMA ZA KIDIJITALI

March 25, 2026 Add Comment

  Airtel Tanzania, kampuni inayoongoza huduma za mawasiliano nchini, imezindua maduka mapya 17 ya Airtel Smart Shops jijini Dar es Salaam. Maduka haya ni sehemu ya mtandao wa maduka 31 nchini kote, ukiwa na lengo la kupanua huduma za kidijitali na kuongeza ujumuishaji wa kifedha kwa wananchi.


Uzinduzi huo uliofanyika Machi 12, 2026, ulihudhuriwa na Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, pamoja na viongozi wa serikali, wajasiriamali, na vyombo vya habari.

Waziri Kairuki alieleza kuwa uwekezaji huu ni ishara ya nia ya dhati kwa Airtel kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya mawasiliano na kuonyesha imani yake katika mazingira ya biashara Tanzania chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Maduka haya mapya yanaonyesha dhati ya Airtel katika kuleta huduma karibu na wananchi huku yakiboresha uzoefu wa wateja. Pia unaashiria imani thabiti katika mazingira ya biashara Tanzania,” alisema Waziri Kairuki.


Kwa upande wake, Charles Kamoto, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, alisema maduka haya hayako tu kama maduka ya rejareja. Yameundwa kama vituo vya kisasa vya huduma za kidijitali, vinavyotoa usajili wa SIM, intaneti ya kasi, huduma za kifedha kupitia Airtel Money, mauzo ya simu, na suluhisho za kibiashara kwa SMEs.


Maduka haya yamewekwa katika maeneo yenye shughuli nyingi jijini Dar es Salaam, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wakazi na wajasiriamali. Uzinduzi huu ni sehemu ya mpango wa kitaifa wa “Airtel Kila Kona”, unaolenga kufanikisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano hata katika maeneo ya vijijini.

Kampuni pia imewekeza katika kupanua mtandao wake wa 4G, kuanzisha teknolojia ya 5G, na kuongeza uunganishaji wa kimataifa kupitia mfumo wa nyaya za chini ya bahari wa 2Africa Submarine Cable System.



Adriana Lyamba, Mkurugenzi wa Uzoefu wa Wateja Airtel Tanzania, alisema maduka haya yameundwa kutoa huduma haraka, bila karatasi, na kwa ufanisi. Maduka haya yanatarajiwa pia kuunda ajira na kusaidia SMEs na wajasiriamali wa ndani kwa kuwapatia zana za kifedha za kidijitali na huduma za mawasiliano za kisasa.

WAZIRI NANAUKA -SERIKALI ITAENDELEA KUVIPA KIPAUMBELE VIKUNDI VINAVYOREJESHA MIKOPO

March 15, 2026 Add Comment

 

















Na Oscar Assenga,Muheza, Tanga

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka amesema serikali itaendelea kuvipa kipaumbele vikundi vya vijana vinavyoonyesha uwajibikaji kwa kurejesha mikopo wanayopewa ili viweze kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Nanauka aliyasema hayo leo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyotembelea kikundi cha Vijana cha Mali Hai kilichopo wilayani Muheza mkoani Tanga kwa lengo la kukagua shughuli zao za uzalishaji pamoja na miradi iliyopata fedha kupitia mikopo ya halmashauri.

Akiwa kwenye kikundi hicho alionyesha kuridhishwa na juhudi na nidhamu ya kikundio hicho kurejesha mikopo baada ya kufanikiwa kukuza mtaji wake kutoka shilingi milioni 20 hadi kufikia zaidi ya shilingi milioni 50, hatua inayotajwa kuwa mfano bora kwa vikundi vingine vya vijana nchini.

Nanauka alisema kikundi cha Mali Hali ni miongoni mwa vikundi vichache nchini vilivyofanikiwa kurejesha mikopo kwa wakati, jambo ambalo limekifanya kupata nafasi ya kuangaliwa kwa karibu zaidi katika mipango ya kusaidiwa kuongeza mtaji na kupanua shughuli zake.

Alisema katika mchakato unaoendelea wa kusaidia wajasiriamali wadogo na kurasimisha shughuli zao, serikali itaangalia namna ya kukiweka kikundi hicho kwenye orodha ya vikundi vitakavyosaidiwa ili kuimarisha shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, alieleza kuwa serikali inatekeleza maelekezo ya Rais ya kuhakikisha vijana wanaochukua hatua ya kufanya kazi na kuonyesha juhudi wanapatiwa mikopo na serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi na pia kutoa ajira kwa wengine.

“Vijana hawa wameonyesha mfano mzuri kwa watanzania wengine wameanza na mtaji mdogo mwaka 2008,wakapata msaada wa shilingi milioni tano mwaka 2018 na baadaye mkopo wa shilingi milioni 20 mwaka wa fedha 2020/2021. Leo hii wameongeza mtaji wao hadi kufikia zaidi ya milioni 50. Huu ni ushahidi kwamba ndoto kubwa zinaweza kuanza na mwanzo mdogo,” alisema Nanauka.

Aliongeza kuwa serikali itahakikisha vijana wenye juhudi kama hao wanapata fursa zaidi, ikiwemo mikopo mingine, pamoja na kushirikishwa katika zabuni za serikali ili waweze kukuza biashara zao.

Nanauka pia aliwashauri vijana nchini kutokudharau mwanzo mdogo na kuwa na uvumilivu wanapotekeleza ndoto zao za kimaendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Hawa Mchafu, alisema kamati hiyo ipo katika ziara ya kawaida ya kukagua miradi ya maendeleo kabla ya kuanza kwa Bunge la Bajeti, ambapo wamepita katika maeneo mbalimbali kutathmini miradi iliyopata fedha za serikali.

Alisema kamati hiyo imevutiwa na kazi nzuri inayofanywa na kikundi hicho cha vijana, lakini imebaini changamoto ya eneo la uzalishaji kuwa dogo na huenda lisiweze kukidhi mahitaji yao iwapo wataongeza mtaji zaidi.

Kutokana na hali hiyo, kamati imeitaka wizara husika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuhakikisha vijana hao wanapatiwa eneo kubwa zaidi la kufanyia shughuli zao za uzalishaji ili waweze kupanua biashara zao.

“Eneo walilonalo sasa ni dogo ukilinganisha na malengo yao ya kupanua uzalishaji hivyo tunashauri wapatiwe eneo kubwa zaidi na lililopo sasa likibaki kama sehemu ya maonesho ya bidhaa wanazozalisha,” alisema Mchafu.

Pia aliishauri serikali kuangalia uwezekano wa kukipa kikundi hicho mkopo mwingine wa kifedha ili kiweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokikabili, ikiwemo kununua gari kwa ajili ya shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha vijana nchini kutumia fursa zilizotolewa na serikali kupitia mifuko mbalimbali ya maendeleo ya vijana badala ya kujikita kwenye mfuko mmoja pekee.

Mchafu alisema kuwa Rais ametoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vijana kupitia wizara na taasisi mbalimbali, hivyo vijana wanapaswa kuzitumia fursa hizo kujikwamua kiuchumi.

Kamati hiyo pia imeishauri serikali kuhakikisha sheria ya manunuzi ya umma inayotaka asilimia 30 ya zabuni za serikali zitolewe kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu inatekelezwa kikamilifu ili kuwapatia vijana nafasi ya kukua kiuchumi.

Kwa sasa kikundi cha Mali Hali kinadaiwa kuajiri vijana zaidi ya 20 katika shughuli zake za uzalishaji, jambo ambalo limeelezwa kuwa linaunga mkono dhamira ya serikali ya kukuza ajira kwa vijana na kuimarisha uchumi wa wananchi.

Vijana wa kikundi hicho pia wamemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fursa na kuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kufikia ndoto zao za kuanzisha kampuni kubwa inayoweza kutoa ajira kwa vijana wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini.

Mwisho.