Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts

DAS KIGAMBONI AZINDUA OFISI YA WILAYA YA KITANESCO YA KIMBIJI

May 05, 2026 Add Comment




📌Asema itapunguza adha wananchi kutembea umbali mrefu kufuata huduma

📌Aipongeza TANESCO kwa maboresho yanayoendelea kufanyika kwa wateja wake

Katibu Tawala Wilaya ya Kigamboni Bi. Upendo Mahalu amezindua Ofisi mpya ya Wilaya ya KiTANESCO Kimbiji ikiwa ni mkakati wa Shirika wa kuendelea kuwahudumia na kusogeza huduma zake karibu na wananchi.
Akizungumza Mei 04, 2026 kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Bi. Upendo Mahalu, amesema uzinduzi wa Ofisi hiyo  umelenga kuboresha utoaji huduma kwa wananchi kadri mahitaji ya nishati ya umeme yanavyozidi kuongezeka.
Ameeleza kuwa hatua hiyo inaakisi maboresho ya kiutendaji yanayolenga kuongeza ufanisi na kupunguza changamoto ya umbali kwa wananchi ambao hapo awali walilazimika kufuata huduma katika ofisi za mkoa zilizopo Tungi Mnadani.
“Lengo la uzinduzi huu ni kuboresha huduma kwa wananchi na kuendana na kasi ya ongezeko la mahitaji ya nishati ya umeme kwa maendeleo ya nchi. Naipongeza Menejimenti ya TANESCO kwa maono ya kusogeza huduma karibu na wananchi,” alisisitiza Bi. Mahalu.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Kigamboni, Mhe. Haran Sanga, ameipongeza TANESCO kwa maboresho makubwa ya kiutendaji na kimtazamo, huku akiwataka wananchi kuwa mstari wa mbele kulinda miundombinu ya umeme, akisisitiza kuwa serikali inawekeza fedha nyingi katika sekta hiyo.
Akizungumza Kaimu Meneja Huduma kwa Wateja, Bw. Shamu Lameck, amesema TANESCO inaendelea kuimarisha huduma zake kwa wateja kwa kutoa elimu na taarifa sahihi kuhusu matumizi ya umeme na miundombinu yake.
“Dhamira yetu ni mteja kwanza. Tunaendelea kuongeza juhudi kuhakikisha kila mteja anafikiwa na huduma bora ya umeme, tunaishukuru sana Serikali kwa kutaoa ushirikiano katika kufikia malengo yetu ya kumuhudumia mteja kwa ufanisi,” alieleza.
Ofisi ya TANESCO Kimbiji itahudumia kata za Kimbiji, Somangila, Pembamnazi na Kisarawe II. Uzinduzi huo pia uliambatana na kukabidhiwa kwa vitendea kazi, yakiwemo magari na bajaji yatakayosaidia kuwafikia wateja kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.


WANANCHI WA DODOMA WAPONGEZA JUHUDI ZA SERIKALI MKAKATI WA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

May 04, 2026 Add Comment

 



Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Wananchi wa Dodoma wamepongeza juhudi za Serikali kupitia mkakati wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, wakieleza kuwa mkakati huo unasaidia kuboresha afya, kuokoa muda na kulinda mazingira.
Hayo yamejiri leo tarehe 4 Mei 2026 katika Soko la Mavunde, Chang’ombe, ambapo wananchi wamepata elimu ya nishati safi ya kupikia kwa nadharia na vitendo, ikiwemo mafunzo ya jinsi ya kutumia nishati hizo kwa usahihi na kwa ufanisi zaidi katika shughuli za upishi wa kila siku.
Baadhi ya wananchi waliohudhuria wamesema kuwa elimu hiyo ya vitendo imewasaidia kuelewa kwa urahisi faida za nishati safi, hususan kupunguza moshi majumbani unaochangia magonjwa ya njia ya hewa na kurahisisha shughuli za upishi.
Aisha Ramadhani, mmoja wa wananchi waliohudhuria na ni mkazi wa Kata ya Chang’ombe, amesema amefurahishwa na kampeni hiyo inayoendelea jijini Dodoma, akibainisha kuwa elimu aliyoipata imemsaidia kubadili mtazamo wake kuhusu matumizi ya nishati, na sasa anaelewa vizuri faida za kutumia nishati safi kama vile kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, kuokoa muda pamoja na kuboresha afya ya familia.
Akizungumza katika eneo hilo, mtaalamu kutoka Wizara ya Nishati, Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia, Nsajigwa Maclean, amesema Serikali inaendelea kutekeleza mkakati kwa kuhakikisha nishati safi ya kupikia inapatikana kwa urahisi, kwa gharama nafuu na kuwafikia wananchi wa makundi yote bila kujali kipato au eneo wanaloishi.
Aidha, amefafanua kuwa serikali imeweka juhudi katika kutoa elimu endelevu kwa jamii kupitia mafunzo ya vitendo, ili kuhakikisha wananchi wanapata uelewa wa kina kuhusu matumizi salama ya nishati safi, pamoja na kuhimiza mabadiliko ya tabia kutoka matumizi ya kuni na mkaa kwenda nishati mbadala inayolinda afya na mazingira.
Wananchi waliohudhuria wameeleza kuridhishwa na juhudi hizo za Serikali na kuahidi kuendelea kuhamasishana juu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo yao wanayoishi.

TANZANIA NA JAPAN KUFUNGUA MILANGO MIPYA YA UWEKEZAJI KATIKA SEKTA YA NISHATI

April 30, 2026 Add Comment


Ushirikiano kati ya Tanzania na Japan katika sekta ya nishati unaingia hatua mpya, huku juhudi zikielekezwa zaidi katika kuvutia uwekezaji wa sekta binafsi na teknolojia za kisasa za uzalishaji umeme.

Hatua hiyo imebainishwa jijini Dar es Salaam leo tarehe 30 Aprili,2026 wakati Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia,Dkt.  James Mataragio alipokutana na Mwakilishi Mkuu mpya wa Japan International Cooperation Agency, Dkt. Kuge Katsuya.

Katika kikao hicho Dkt. Mataragio ameweka wazi Mkakati wa Serikali kuifanya sekta ya nishati kuwa kivutio kikubwa cha mitaji ya kimataifa hususan kutoka Japan.

Amesema  kuwa pamoja na historia ndefu ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, hatua inayofuata inapaswa kulenga uwekezaji mkubwa zaidi unaoweza kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa nishati nchini.

“Huu ni wakati wa kuhamasisha kampuni binafsi na taasisi za kifedha kutoka Japan kuja kuwekeza moja kwa moja katika miradi ya nishati Tanzania,” amesisitiza.

Akizungumzia ushirikiano wa Tanzania na Japan Dkt. Mataragio amesema JICA imekuwa mdau wa muda mrefu katika sekta ya nishati nchini na wameshiriki katika miradi ya  Uandaaji wa Mpango kabambe wa Matumizi ya Gesi Asilia Nchini (Natural Gas Utilization Master Plan -NGUMP),  wametoa fursa za kuwajengea uwezo wataalamu katika Matumizi ya gesi asili pamoja na utekelezaji wa Miradi mbalimbali ya umeme.

Aidha Dkt. Mataragio amembushia ahadi ya muda mrefu ya Japan ya kuwezesha Mradi wa umeme wa megawati 300 mkoani Mtwara.

Kwa upande wake, Dkt. Kuge ameashiria mwelekeo mpya wa ushirikiano utakaojikita katika Mafunzo ya teknolojia ya nishati ya nyuklia, Uzalishaji wa umeme kupitia gesi asilia kwa ufanisi mkubwa zaidi na Kuunganisha Tanzania na wawekezaji binafsi kutoka Japan

Ahadi hiyo inaashiria uwezekano wa Tanzania kunufaika na teknolojia za kisasa zaidi za nishati kutoka Japan, moja ya nchi zinazoongoza duniani katika ubunifu wa nishati.

Mkutano huo umeonesha wazi kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Japan hauishii katika misaada, bali sasa unaelekea kwenye uwekezaji mkubwa na ubadilishanaji wa teknolojia  hatua inayoweza kubadilisha kabisa sekta ya nishati nchini

RAIS SAMIA ATAMBULIWA KUWA KINARA WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA AFRIKA

April 30, 2026 Add Comment




📌 Mawaziri wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika wapendekeza Rais Samia kutangazwa rasmi

Umoja wa Afrika umetambua juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuendeleza na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ndani na nje ya nchi, na kumpendekeza kutangazwa rasmi kuwa kinara wa Umoja wa Afrika wa ajenda hiyo.

Hatua hiyo imefikiwa katika Mkutano wa 5 wa Mawaziri wa Nchi wanachama wa Umoja wa Afrika wanaoshughulikia Nishati na Uchukuzi uliofanyika jijini Johannesburg, Afrika Kusini, tarehe 30 Aprili 2026. Katika mkutano huo Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameongoza ujumbe wa Tanzania katika ngazi ya Mawaziri.

Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametambuliwa na kupendekezwa kuwa kinara wa Afrika kutokana na mchango wake mkubwa katika kusukuma sera, mikakati na ushirikiano wa kimataifa unaolenga kupanua upatikanaji wa nishati safi ya kupikia, kupunguza athari za kiafya na kimazingira, pamoja na kuboresha maisha ya waafrika, hususan wanawake na watoto.

Akizungumza katika mjadala kuhusu Programu ya Nishati Safi ya Kupikia Afrika, Waziri Ndejembi amesema kuwa mafanikio ya Tanzania katika sekta hiyo yametokana na uongozi madhubuti wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kusukuma ajenda ya nishati safi ya kupikia ndani na nje ya nchi.

Amesema kuwa chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, nishati safi ya kupikia imepewa kipaumbele cha kitaifa na kuingizwa katika Dira ya Taifa ya 2050, ikiwa ni sehemu muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Katika juhudi za kimataifa, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kuhamasisha agenda ya nishati safi ya kupikia kupewa kipaumbele katika mipango ya mataifa mbalimbali kupitia majukwaa ya kimataifa ikiwemo mkutano wa COP28 mwaka 2023, pamoja na Mkutano wa Nishati Safi ya Kupikia Barani Afrika uliofanyika Paris mwaka 2024, ambapo zaidi ya dola za Marekani bilioni 2.2 ziliahidiwa kusaidia sekta hiyo.

Kutokana na hatua hiyo ya mapendekezo ya Mawaziri yaliyoanzia katika ngazi ya wataalamu wa Umoja wa Afrika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuthibitishwa na kutangazwa rasmi kuwa Kinara wa Umoja wa Afrika wa Nishati Safi ya Kupikia katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika utakaofanyika.




MHE. SALOME ASHIRIKI MKUTANO WA 21 WA MAWAZIRI WA NISHATI AFRIKA MASHARIKI

MHE. SALOME ASHIRIKI MKUTANO WA 21 WA MAWAZIRI WA NISHATI AFRIKA MASHARIKI

April 30, 2026 Add Comment

 





Na Mwandishi Wetu, Cairo

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, ameiwakilisha Tanzania katika Mkutano wa 21 wa Baraza la Mawaziri wa Nishati wa Ukanda wa Mashariki mwa Afrika, uliofanyika Aprili 29, 2026 jijini Cairo, Misri, ukiwa na lengo la kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika sekta ya umeme.

Katika mkutano huo wa nchi wanachama wa Umoja wa Nishati Mashariki mwa Afrika (EAPP), uamuzi muhimu umefikiwa wa kuichagua rasmi Jamhuri ya Kiarabu ya Misri kuwa mwenyeji wa kudumu wa kituo cha uendeshaji wa soko la umeme la pamoja kwa nchi wanachama.

Mkutano huo uliongozwa na Waziri wa Umeme na Nishati Jadidifu wa Misri, Mhe. Dkt. Mahmoud Esmat, ambaye pia ni mwenyekiti anayemaliza muda wake, uliwakutanisha Mawaziri wa Nishati kutoka nchi 13 wanachama kwa lengo la kukamilisha mfumo wa kiutawala na kiuendeshaji wa soko la umeme la pamoja na endelevu.

Mbali na kuichagua Misri, Baraza hilo pia limepitisha nyongeza ya muda wa miezi miwili kwa nchi wanachama kukamilisha mchakato wa kuridhia hati za makubaliano ya ushirikiano baina ya serikali na mashirika ya umeme.

Aidha, mkutano huo umeridhia Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasi ya Ethiopia kuchukua nafasi ya uenyekiti wa Baraza la Mawaziri, kufuatia kumalizika kwa muda wa uongozi wa sasa, kwa mujibu wa katiba ya umoja huo inayotaka uongozi kuzunguka kwa wanachama kila mwaka.

Akihitimisha mkutano huo, Mwenyekiti wa EAPP, Mhe. Dkt. Esmat, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza umoja, ushirikiano, uwazi na kuheshimiana miongoni mwa nchi wanachama ili kufikia malengo ya kuwa na soko la umeme la kikanda lenye tija.

Akizungumza kuhusu mkutano, Mhe. Salome amesema maazimio yaliyofikiwa ni hatua muhimu katika kuleta mageuzi makubwa katika biashara ya umeme na kuimarisha soko la nishati la pamoja kwa nchi za ukanda huo.

Katika mkutano huo, Mhe. Makamba ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Misri, Meja Jenerali Richard Makanzo, Kamishna Msaidizi wa Maendeleo ya Umeme kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Styden Rwebangila, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO anayeshughulikia uzalishaji umeme, Mhandisi Anthony Mbushi, pamoja na wataalamu kutoka Wizara ya Nishati, TANESCO na EWURA.
Shar