HABARI ZETU
Loading...
Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts
 WAHARIRI WAIPONGEZA REA USAMBAZAJI WA GESI ASILIA LINDI NA PWANI

WAHARIRI WAIPONGEZA REA USAMBAZAJI WA GESI ASILIA LINDI NA PWANI

March 08, 2026 Add Comment





Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) wameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kusambaza miundombinu ya gesi asilia kwenye kaya takribani 1000 na shule moja ambapo mradi huo umefadhiliwa na Serikali kwa asilimia 100 kupitia REA.

Hayo yamezungumzwa leo Machi 8, 2026 na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Bw. Deodatus Balile wakati wa ziara ya TEF Kutembelea mradi uliofadhiliwa na REA wa ujenzi wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia kwenye nyumba za makazi mkoa wa Pwani.

Bw. Balile amesema kupitia mradi huo Serikali imepunguza kwa kiasi kikubwa utegemezi wa Nishati nyingine kama mkaa wa kawaida, kuni, na mafuta ya taa na nishati gesi asilia sasa inakua ni chanzo cha nishati ya kupikia.

“REA imefanya kazi kubwa sana ya kufadhili mradi huu, hivyo basi mradi huu utaboresha kiwango cha maisha ya walengwa wa mradi kwa kuokoa gharama na muda wa kupika, mazingira safi afya bora na uwezeshaji wa wanawake kuongezeka, ” Amesema Bw. Balile.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Mradi kutoka REA, Mha. Emmanuel Yessaya amesema kuwa Wakala ulitenga Fedha kwa ajili ya kufadhili mradi ya usambazaji wa gesi asilia kupitia Mfuko wa Nishati Vijijini (REF) ambapo takribani kaya 1000 pamoja na taasisi moja zimenufaika kwa kusambaziwa miundombinu ya gesi asilia kwa ajili ya kupikia majumbani katika mkoa wa Lindi na Pwani.

Mha.Yessaya ameongeza kuwa, Mradi huo ni wa kimkakati kwa ajili ya kupunguza gharama za nishati ya kupikia, kulinda afya za wananchi na kupunguza athari za kimazingira zitokanazo na ukataji wa misitu kwa ajili ya nishati ya kupikia kwa wananchi wanaoishi Vijijini na kwenye vijiji miji.

Kwa upande wake Mhandisi wa mradi huo kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) Mha. Anthony Karomba, amesema kuwa mradi huo wa kuunganisha wateja wa majumbani kwenye mtandao wa gesi asilia umegharamikiwa kwa fedha nyingi na Serikali kupitia REA na hivyo amewasihi wananchi kuendelea kuilinda miundombinu hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wananchi wa Kata ya Kisemvule wameishukuru Serikali kupitia REA kwa kusambaza miundombinu ya gesi asilia ya kupikia katika miji yao. Wameeleza kuwa mradi umenufaisha kaya zao kwa kuokoa gharama, kuongeza muda wa kufanya shughuli za kuzalisha mali, imelinda mazingira, imeboresha afya zao na kuimarisha usawa wa kijinsia kwenye shughuli za kiuchumi.

MRADI WA MALAGARASI WAPELEKA UMEME KWA KAYA 750 KIGOMA

March 07, 2026 Add Comment



Takribani kaya 750 zinazopitiwa na Mradi wa Uzalishaji Umeme wa Malagarasi (MW 49.5) unaotekelezwa mkoani Kigoma zimefaidika na mradi huo, ikiwa ni jitihada za Serikali kuhakikisha kuwa wananchi wanaopitiwa na miradi ya maendeleo wananufaika na miradi husika.


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amewasha umeme katika Kitongoji cha Mdyandelema, Kata ya Kazuramimba, Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma, ambacho ni miongoni mwa vitongoji 18 vilivyowashiwa umeme kupitia mradi huo.


Akizungumza na wananchi mara baada ya kuzindua huduma hiyo ya umeme, Mhe. Salome amesema utekelezaji wa mradi huo ni maagizo ya Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ameielekeza Wizara ya Nishati kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2030 vitongoji vyote viwe vimesambaziwa umeme.




Kutokana na hilo, Mhe. Salome amewataka wananchi kutunza miundombinu ya umeme ili kuunga mkono lengo la Rais Samia la kuifanya Kigoma kuwa kitovu cha umeme, hasa baada ya kukamilika kwa kituo kikubwa cha kupoza umeme cha Kidahwe kitakachokuwa na uwezo wa megawati 192, ambacho kitakuwa ngome ya kusambaza umeme katika mikoa ya Magharibi.


Katika hatua nyingine, Mhe. Salome amesema gharama ya kuunganishiwa umeme vitongojini ni shilingi 27,000 tu ambapo amesisitiza kuwa hata kama mwananchi ametandaza nyaya za umeme katika sehemu ya nyumba yake, bado anastahili kuunganishiwa huduma hiyo.


Kuhusu nishati safi ya kupikia, Mhe. Salome amewaasa wananchi kutumia majiko ya umeme, majiko banifu na mitungi ya gesi kwa ajili ya kupikia. Pia ameutaka Wakala wa Nishati Vijijini (REA) pamoja na TANESCO kuhakikisha wanatoa elimu ya matumizi ya nishati hiyo kwa wananchi hadi ngazi ya vitongoji.


Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Dinah Mathamani, kwa upande wake amemshukuru Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuukumbuka Mkoa wa Kigoma katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ya nishati.


Amesema hapo awali hali ya upatikanaji wa umeme ilikuwa haitabiriki, lakini sasa huduma hiyo imeimarika na kuwa ya uhakika, hali inayowawezesha wananchi kufanya shughuli za biashara, kupata mwanga pamoja na kutumia umeme kwa kupikia na hivyo kusaidia kuhifadhi mazingira.


Kwa upande wake, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amesema mradi wa Malagarasi unahusisha sehemu tatu ambazo ni ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme, njia ya kusafirisha umeme msongo wa kv 132 na upelekaji wa umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 pamoja na utekelezaji wa miundombinu mingine ikiwemo ujenzi wa barabara ya lami, hospitali na shule.


Ameongeza kuwa mradi huo tayari umeshaunganisha umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 kwa gharama ya shilingi bilioni 6.8.






MAGARI YA UMEME NAFUU KWA ASILIMIA 85 UKILINGANISHWA NA MAFUTA

March 06, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba amesema utafiti unaonesha kuwa kuendesha gari la umeme nchini ni nafuu kwa takribani asilimia 85 kwa kila kilomita ikilinganishwa na gari linalotumia petroli au dizeli.

Mramba ameyasema hayo Machi 6, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi rasmi wa matumizi ya magari ya umeme nchini kupitia kampuni ya DOW ELEF AUTO EV (ZERA) Limited.

Amesema kwa wastani gari linalotumia mafuta linaweza kugharimu takribani Sh.200 kwa kilomita moja, wakati gari la umeme linatumia karibu Sh.25 pekee kwa kilomita.

“Gharama hii inaonesha wazi kuwa teknolojia ya magari ya umeme ni nafuu zaidi na inaweza kusaidia wananchi kupunguza matumizi katika sekta ya usafiri,” amesema Mramba.

Ameeleza kuwa uzinduzi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya usafiri nchini na unaendana na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan za kukuza uwekezaji na kuhamasisha matumizi ya teknolojia safi ya nishati.

Mramba amesema Serikali tayari imeweka mazingira wezeshi kwa maendeleo ya teknolojia hiyo kwa kupitisha Mfumo wa Kitaifa wa Sera ya Magari ya Umeme (National Electric Vehicles Policy Framework) Desemba 2024.


Amesema sera hiyo inalenga kuhamasisha uzalishaji wa magari ya umeme nchini, kuongeza matumizi yake, kuunganisha sekta hiyo na nishati jadidifu pamoja na kujenga miundombinu ya vituo vya kuchaji magari hayo.

Aidha, amesema Tanzania imeendelea kupiga hatua katika uzalishaji wa umeme ambapo uwezo umeongezeka hadi zaidi ya megawati 4,500, huku upatikanaji wa umeme ukifikia asilimia 85.5 mwaka 2025.

Kwa mujibu wa Mramba, hatua hiyo inalenga kuimarisha sekta mbalimbali za kiuchumi ikiwamo usafiri wa kisasa wenye gharama nafuu na rafiki kwa mazingira.

Kwa sasa Afrika ina zaidi ya magari ya umeme 30,000, huku Afrika Mashariki ikijitokeza kuwa kitovu cha ubunifu katika sekta hiyo.

Nchini Tanzania, inakadiriwa kuwa tayari kuna zaidi ya magari ya umeme 10,000 yakiwemo pikipiki pamoja na vyombo vingine vya usafiri vya magurudumu mawili na matatu.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kampuni ya DOW ELEF AUTO EV (ZERA) Limited, Emmanuel Kazimoto, amesema kampuni hiyo imeanza na mpango wa kuagiza magari kamili ya umeme, kabla ya kuanza kuleta magari ya kuunganishwa hapa nchini.

Ameongeza kuwa lengo la baadaye ni kuanzisha kiwanda cha kuunganisha magari ya umeme nchini, hatua itakayochochea ajira na kuwajengea vijana wa Kitanzania ujuzi katika teknolojia ya kisasa.

MATUMIZI YA NISHATI SAFI YAPUNGUZA UKATAJI WA MITI MVOMERO

March 05, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu,


Wananchi wa Mvomero wamesema kuwa utekelezaji wa agizo la Serikali la kuhamasisha matumizi ya nishati safi umeanza kuleta matokeo chanya, ikiwemo kupungua kwa ukataji wa miti na uchomaji wa mkaa katika baadhi ya maeneo.


Hayo yameelezwa na baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Mvomero wakati wa ziara ya timu kutoka Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF), iliyofika wilayani humo kutoa elimu kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. 

Kampeni hiyo imefanyika katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Morogoro kwa lengo la kuhamasisha matumizi ya nishati salama.

Wameeleza kuwa wananchi wengi sasa wameanza kuhamia katika matumizi ya gesi na umeme kwa ajili ya kupikia, jambo linalowasaidia kuokoa muda katika shughuli zao za kila siku pamoja na kujikinga na madhara ya kiafya yanayotokana na moshi wa kuni na mkaa.

Katika kampeni hiyo, wananchi wamepata fursa ya kushuhudia maonesho ya matumizi ya majiko ya gesi na umeme, ambapo walioneshwa jinsi yanavyoweza kupika chakula kwa haraka, kwa gharama nafuu na kuhifadhi ubora pamoja na ladha ya chakula. Hali hiyo imeongeza mwitikio wa wananchi wengi kuanza kutumia nishati safi ya kupikia.



KIHONGOSI AIPONGEZA WIZARA YA NISHATI KWA MRADI WA UMEME JUA KAYENZE

March 05, 2026 Add Comment






📌Umegharimu bilioni 11 na kuingiza umeme gridi ya Taifa.

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Kenan Kihongosi ameipongeza Wizara ya Nishati kwa utekelezaji wa mradi wa umeme jua wenye thamani ya shilingi bilioni 11 unaoingiza megawati tano (5) katika Gridi ya Taifa.

Kihongosi ametoa pongezi hizo mara baada ya kutembelea mradi huo uliopo katika Kijiji cha Kayenze, Jimbo la Ushetu wilayani Kahama, akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Shinyanga.



“Naipongeza Wizara ya Nishati kwa mradi huu wenye tija ambao ni sehemu ya vielelezo vya utekelezaji wa miradi ya nishati safi kwa ajili ya wananchi. Kupitia mradi huu tunaendelea kuona dhamira ya Serikali ya kupeleka maendeleo katika maeneo mbalimbali nchini,” amesema Kihongosi

Aidha, amemshukuru na kumpongeza Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono yake yaliyowezesha kukamilika kwa miradi mbalimbali ya kimkakati ikiwemo mradi wa Julius Nyerere unaozalisha megawati 2,115 pamoja na mradi wa umeme jua wa Kishapu ambapo awamu ya kwanza imekamilika na kuanza kuzalisha megawati 50.

Kihongosi pia amempongeza Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba pamoja na viongozi wengine kwa usimamizi madhubuti unaoifanya sekta ya nishati kuwa imara na yenye utulivu, huku akisisitiza kasi ya utekelezaji wa miradi kuendelea.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati na Mbunge wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Salome Makamba amesema umeme unaozalishwa katika mradi huo unaingizwa kwenye Gridi ya Taifa kupitia njia ya msongo wa kilovolti 33 (33kV). Ameongeza kuwa mradi huo ulikamilika mwezi Mei 2025 na kuanza kufanya kazi mara moja.

Ameeleza pia kuwa pamoja na kusaidia kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme, mradi huo umechangia maendeleo ya jamii kwa kujenga jengo la zahanati katika Kijiji cha Kayenze kwa gharama ya shilingi milioni 130.

Kuhusu usambazaji wa umeme katika Jimbo la Ushetu, Mhe. Salome amesema Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha kwa ajili ya kusambaza umeme katika vitongoji 136 jimboni humo, huku vitongoji takriban 100 vilivyosalia vitakuwa vimefikiwa na huduma hiyo ifikapo mwaka 2030.


































WAZIRI NDEJEMBI AITAKA TPDC KUONGEZA KASI YA UPATIKANAJI WA MAENEO YA UCHIMBAJI WA GESI

March 01, 2026 Add Comment


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amelitaka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuongeza kasi katika utafiti wa upatikanaji wa maeneo mapya ya uchimbaji wa visima vipya vya gesi asilia ili kuongeza upatikanaji wa gesi kwa matumizi mbalimbali pamoja na kufanikisha agenda ya matumizi ya nishati safi nchini.

Ndejembi ameeleza hayo tarehe 27 Februari 2026 mkoani Mtwara wakati akizindua mradi wa uchimbaji wa visima vitatu ambapo viwili ni kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa gesi asilia katika Kitalu cha Mnazi Bay na kimoja kwa ajili ya utafutaji huku utekelezaji umefikia asilimia 58.

“Rai yangu kwenu TPDC ni kuongeza kasi ya uchimbaji wa gesi katika maeneo mengine na kuhakikisha mashapo yaliyopo yanaanza kuzalisha tunapozindua kitalu hiki hapa mipango ya kuanza kuchimba sehemu nyingine ianze mara moja” amesisitiza Ndejembi.

Ndejembi ameeleza kuwa Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan iliamua kuwekeza fedha kupitia TPDC kwani mahitaji ya gesi yanaongezeka kutokana na nchi inavyoendelea kukua na kusababisha mahitaji ya gesi kuongezeka kwa ajili ya uzalishaji wa umeme matumizi ya viwandani na taasisi nishati kwenye vyombo vya usafiri pamoja na matumizi ya majumbani.

Ndejembi ameipongeza TPDC kwa kushirikiana na Kampuni ya Maurel & Prom katika kutekeleza mradi wa uchimbaji wa visima hivyo ambavyo vitaongeza uzalishaji wa gesi na kuchochea kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi.

Kadhalika Ndejembi ameitaka TPDC kuendelea kuyawezesha makampuni na wataalamu wazawa ikiwa ni pamoja na kuweka mpango wa kuendelea kuwajengea uwezo wataalamu waliopo katika maeneo ya utekelezaji wa miradi ili nao wanufaike na kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi yao.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Dkt James Mataragio ameeleza kuwa Serikali imewekeza fedha nyingi katika nishati ya gesi ambapo katika mradi huo pekee itatumika zaidi ya shilingi bilioni 235.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC Mussa Makame amesema Serikali kupitia TPDC inamiliki Kitalu cha Mnazi Bay kwa asilimia 40 na Kampuni ya Maurel & Prom inamiliki asilimia 60 na kubainisha kuwa uzalishaji umeendelea kuongezeka ambapo kwa sasa uzalishaji katika kitalu hicho umefikia futi za ujazo milioni 100 kwa siku.

Mwisho.