Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts

MKANDARASI AKAMILISHA AWAMU YA KWANZA UVUTAJI NYAYA MRADI WA CHALINZE–DODOMA

August 05, 2026 Add Comment





➡️ TANESCO yawashukuru wateja kwa uvumilivu na kutangaza awamu ya pili kuanza Agosti 11–14 katika maeneo ya Kikombo na Mkonze - Dodoma

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limesema Mkandarasi amekamilisha kwa mafanikio awamu ya kwanza ya kazi za uvutaji wa nyaya katika eneo la Mkambarani, Mkoa wa Morogoro, ikiwa ni sehemu ya hatua za mwisho za utekelezaji wa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma.

Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 5, 2026 katika eneo la Mkambarani, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja, Bi. Irene Gowelle, amesema zoezi hilo, ambalo lilipangwa kufanyika ndani ya siku sita, limekamilika kwa mafanikio na kwa wakati uliopangwa, hatua ambayo imewezesha kurejea kwa huduma ya umeme katika mikoa yote iliyokuwa imeathiriwa na kazi hiyo na kufanya shughuli kuendelea kama kawaida.

Bi. Gowelle amesema kukamilika kwa mradi huo kutaimarisha na kuongeza uwezo wa Gridi ya Taifa, hatua itakayowezesha usafirishaji wa umeme kwa uhakika zaidi katika maeneo mbalimbali nchini na hivyo kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla

Aidha amewashukuruwananchi na wateja wa TANESCO kwa uvumilivu, ushirikiano waliouonesha katika kipindi chote cha utekelezaji wa kazi hizo.


Ameongeza kuwa TANESCO itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya umeme kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa huduma hiyo nchini.

“Kazi hii imefanyika kwa mafanikio makubwa na kwa wakati uliopangwa. Tunawashukuru sana wateja wetu kwa uvumilivu wao. Kwa sasa huduma ya umeme imerejea kama kawaida. Hata hivyo, napenda kuwakumbusha kuwa zoezi hili litaendelea kwa awamu ya pili katika maeneo ya Mkonze na Kikombo kuanzia Agosti 11 hadi 14. Tutawatangazia ratiba mapema ili muweze kupanga shughuli zenu kulingana na ratiba ya upatikanaji wa umeme,” alisema Bi. Gowelle.






Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Chalinze–Dodoma, Mhandisi Newton Mwakifwamba, amesema awamu ya kwanza ya uvutaji wa nyaya ilitekelezwa katika eneo la Mkambarani, ikihusisha uvutaji wa nyaya juu ya reli ya SGR, juu ya njia za umeme za Msongo wa Kilovolti 220 za Morogoro I na Morogoro II, pamoja na njia ya Msongo wa Kilovolti 132, na kwamba kazi zote zimefanyika kwa ufanisi mkubwa.

Ameeleza kuwa awamu ya pili ya uvutaji wa nyaya itafanyika katika maeneo ya Kikombo na Mkonze Dodoma kuanzia Agosti 11 hadi 14, ambapo shughuli hizo zitafanyika kwa wakati mmoja. Kutokana na hali hiyo, kutakuwa na katizo la umeme kwa muda katika baadhi ya maeneo ili kutoa nafasi ya utekelezaji salama wa kazi hizo.




“Umuhimu wa mradi huu ni mkubwa kwa kuwa utaongeza uwezo wa njia zilizopo za kusafirisha umeme. Mradi huu wa Msongo wa Kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma utaimarisha uwezo wa Gridi ya Taifa na kuongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme nchini"alisisitiza Mha. Mwakifwamba

Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma umefikia asilimia 94 ya utekelezaji na unatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026. Kukamilika kwake kutaongeza uwezo wa mfumo wa usafirishaji wa umeme nchini na kuimarisha upatikanaji wa huduma ya umeme yenye ubora na uhakika kwa wananchi.

WIZARA YA NISHATI YAENDELEA KUHUDUMIA WANANCHI.

August 04, 2026 Add Comment

 

Wataalam wa Wizara ya Nishati wakiwa katika picha ya pamoja kwenye Banda la Wizara ya Nishati katika Maonesho ya NaneNane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.

Wizara inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masuala ya umeme, mafuta, gesi asilia, nishati safi ya kupikia pamoja na fursa mbalimbali zinazopatikana katika sekta ya nishati.


Unapotembelea Maonesho ya NaneNane, karibu utembelee Banda la Wizara ya Nishati na taasisi zake lililopo Government Pavilion Na. 2.




ELIMU YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA YAWAFIKIA MADIWANI WA BARIADI, SIMIYU

August 04, 2026 Add Comment

Wizara ya Nishati  inaendelea kuimarisha mnyororo wa thamani wa matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini ambapo imeanza kuwajengea uwezo Madiwani wa halmashauri mbalimbali nchini.

Wanufaika wa awali wa mpango huu ni  Madiwani wa Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu ambao baada ya elimu hii watakuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo yao.

Akizungumza wakati wa semina hiyo, Bw. Ngeleja Mgejwa amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia yana manufaa kwa jamii  ikiwa ni pamoja na kuhifadhi mazingira, kulinda afya, kupunguza gharama za maisha na kuongeza muda kwa wanafamilia kushiriki katika shughuli za maendeleo.

Amesema ajenda ya nishati safi ya kupikia ni ajenda ya kitaifa inahutaji ushiriki wa wadau wote, kuanzia ngazi ya wananchi hadi viongozi, ili kufanikisha azma ya Serikali ya kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.


Bw. Mgejwa amewasihi  madiwani kutumia nafasi zao kuifikisha ajenda hiyo kwa wananchi kutokana na ukaribu wao na jamii.

Kwa upande wake, Mhandisi Benezeth Kabunduguru kutoka Wizara ya Nishati, amesema Bariadi ni miongoni mwa maeneo yanayofikiwa na Serikali katika utekelezaji wa kampeni ya utoaji wa elimu kwa viongozi wa serikali za mitaa ili kuharakisha mabadiliko ya tabia kuelekea matumizi ya nishati safi ya kupikia.



Amesema madiwani wanapaswa kutumia nafasi yao ya uongozi kuwa mabalozi wa nishati safi ya kupikia kwa kuelimisha wananchi kuhusu faida zake na kuhamasisha matumizi ya teknolojia mbalimbali za nishati safi zinazopatikana nchini.


Naye Mkurugenzi wa Mji wa Bariadi, Bw. Idd Ndabhona, ameipongeza Wizara ya Nishati kwa kuendelea kuwajengea uwezo viongozi wa ngazi ya halmashauri, akisema hatua hiyo imeongeza uelewa wao kuhusu wajibu wa kusukuma mbele ajenda ya nishati safi ya kupikia.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi, Bw. Nkenyenge Chales Nkenyenge, ameishukuru Wizara ya Nishati kwa kutoa mafunzo hayo, akisema yamewaongezea viongozi uelewa na kuwapa uwezo wa kutekeleza jukumu lao la kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia katika maeneo yao.

DKT.BITEKO AMPONGEZA WAZIRI WA NISHATI KWA UONGOZI MAHIRI,AZINDUA JENGO JIPYA LA TANESCO BUKOMBE

August 03, 2026 Add Comment




Bukombe, Geita


Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, amempongeza Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, kwa uongozi wake mahiri na usimamizi mzuri wa sekta ya nishati, akisema utekelezaji wa miradi unaonyesha dhamira ya Serikali ya kutekeleza kwa vitendo maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.


Dkt. Biteko ametoa pongezi hizo leo Agosti 3, 2026 wakati wa uzinduzi rasmi wa jengo jipya la Ofisi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Bukombe.

“Kwa kweli nampongeza sana Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Deogratias Ndejembi, pamoja na wasaidizi wake kwa jinsi wanavyofanya kazi kwa weledi na kujituma katika kutekeleza maono ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesema Dkt. Biteko.

Aidha, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za maendeleo zinazowezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kuboresha huduma kwa wananchi nchini.


Amesema ujenzi wa jengo hilo ni ushahidi wa mafanikio ya Serikali katika kuimarisha utoaji wa huduma za umma na kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wa TANESCO, jambo litakaloongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi wa Bukombe na maeneo jirani.

Dkt. Biteko amesisitiza kuwa pamoja na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika sekta ya nishati na miundombinu ya huduma za umma, ni wajibu wa kila mtumishi kulinda na kutunza mali za umma ili ziendelee kutoa huduma bora kwa vizazi vya sasa na vijavyo.


“Tunzeni jengo letu jipya la TANESCO ili liendelee kutoa huduma bora kwa muda mrefu. Miundombinu hii imejengwa kwa gharama kubwa kwa manufaa ya wananchi, hivyo inahitaji kutunzwa na kulindwa wakati wote,” amesisitiza Dkt. Biteko.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Eng. Paskasi Muragili, amesema Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya nishati ili kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza upatikanaji wa umeme na kuchochea shughuli za kiuchumi pamoja na maendeleo ya jamii.


Naye Meneja wa TANESCO Wilaya ya Bukombe, Eng. Valerian Myula, amesema jengo hilo la kisasa limejengwa kwa fedha za ndani za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa gharama ya shilingi milioni 285, ikiwa ni sehemu ya jitihada za shirika hilo za kuendelea kuboresha huduma za umeme na kuongeza ufanisi wa kuwahudumia wananchi.

WAZIRI NDEJEMBI AONGOZA KIKAO MAALUM KUIMARISHA USALAMA WA UPATIKANAJI WA MAFUTA NCHINI

August 03, 2026 Add Comment



Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, leo Agosti 3, 2026 ameongoza kikao kazi cha pamoja na taasisi zinazoshughulikia sekta ya mafuta na gesi katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Nishati, jijini Dar es Salaam.


Lengo la kikao hicho lilikuwa kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha usalama wa upatikanaji na usambazaji wa mafuta nchini, sambamba na kuendelea kuhakikisha nchi inakuwa na akiba ya kutosha ya mafuta katika kipindi hiki cha mgogoro wa vita ya Mashariki ya kati kuliko pelekea kufungwa kwa mlango bahari wa Hormuz na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika soko la kimataifa.


Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio; Kamishna wa Mafuta, Bw. Godluck Shirima; Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Bw. Salum Mnuna; Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Bw. Mussa Makame; Mkurugenzi Mtendaji wa PBPA, Bw. Erasto Simon; pamoja na wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na taasisi zake.




MAMBAMIAMBA YAINGIA RASMI KATIKA SAFARI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

July 30, 2026 Add Comment

 





Wananchi wa Kata ya Mambamiamba, Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, leo Julai 30, 2026, wamejengewa uelewa kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia wakati wa hafla ya uzinduzi wa tawi la Tanzania Women Empowerment Network (TAWEN).


Hafla hiyo imezikutanisha taasisi mbalimbali za Serikali, wadau wa maendeleo na wananchi, ambapo kila taasisi imepata fursa ya kuwasilisha huduma zake pamoja na kuelezea fursa zinazopatikana katika sekta zake. Wizara ya Nishati ilitumia fursa hiyo kutoa elimu kuhusu faida za matumizi ya nishati safi ya kupikia, ikiwemo kulinda afya, kuhifadhi mazingira na kupunguza gharama za matumizi ya nishati.


Akiwasilisha mada, Mtaalamu kutoka Wizara ya Nishati, Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia, Mha. Benezeth Kabunduguru, amesema Serikali inaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034), unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034, kutoka asilimia 28.6 mwaka 2025.


Amesema lengo hilo litafikiwa kupitia ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo na wananchi katika kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia na kuendelea kutoa elimu kuhusu faida za matumizi yake. Ameongeza kuwa matumizi ya nishati safi ya kupikia yanachangia kulinda afya za wananchi kwa kupunguza athari za moshi unaotokana na matumizi ya kuni na mkaa, kuhifadhi mazingira kwa kupunguza ukataji wa miti, pamoja na kuokoa muda na gharama zinazotumika katika shughuli za kupikia, hususan kwa wanawake na watoto.


Aidha, amewahimiza wananchi wa Kata ya Mambamiamba kuchangamkia matumizi ya teknolojia mbalimbali za nishati safi ya kupikia zinazopatikana nchini ili kuongeza matumizi ya nishati hiyo na kuunga mkono juhudi za Serikali za kufikia malengo ya Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.


Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TAWEN, Balozi Amina Salum Ali, ameipongeza Wizara ya Nishati na taasisi zake kwa kuendelea kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia. Amesema juhudi hizo zinaongeza uelewa wa wananchi na kuwasaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu matumizi ya nishati.


Ameongeza kuwa TAWEN itaendelea kushirikiana na Wizara ya Nishati pamoja na wadau wengine kuhakikisha elimu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia inawafikia wanawake na jamii kwa ujumla ili kuongeza matumizi ya nishati hiyo kwa manufaa ya afya, mazingira na maendeleo ya kiuchumi ya wananchi.


MRADI WA NJIA YA KUSAFIRISHA UMEME WA MSONGO WA KILOVOLTI 400 CHALINZE–DODOMA MBIONI KUKAMILIKA

July 28, 2026 Add Comment



Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limesema Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Msongo wa Kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma uko kwenye hatua za mwisho za utekelezaji wake, huku ujenzi ukiwa umekamilika kwa asilimia 94 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Agosti 21, 2026.


Akizungumza na waandishi wa habari leo Julai 28, 2026, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO, Bi. Irene Gowelle, amesema ili kuwezesha ukamilishaji wa kazi za mradi huo kutakuwepo na katizo la muda la umeme katika baadhi ya maeneo nchini kwa ratiba maalumu kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza itakua Julai 30 hadi Agosti 4 na ya pili itaanza Agosti 11 hadi 17, 2026.


Gowelle amesema hatua hiyo ni sehemu ya maandalizi ya ombi la Mkandarasi anayetekeleza mradi huo kampuni ya TBEA ambayo inalenga kuhakikisha kazi zinafanyika kwa hali ya usalama .


“Mradi huu umefikia hatua muhimu sana ya utekelezaji ambapo kipindi hiki, baadhi ya njia za kusafirisha umeme za kilovolti 220 na 132 zitalazimika kuzimwa kwa muda ili kuruhusu kazi za kuvuta na kuunganisha nyaya mpya kufanyika kwa usalama. Hii ni hatua ya kawaida katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya miundombinu ya kusafirisha umeme na inalenga kukamilisha mradi huu wenye manufaa makubwa kwa Taifa,” amesema Bi. Gowelle.


Amefafanua kuwa baadhi ya maeneo katika mikoa iliyoko Kanda ya Kati, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Magharibi na Kanda ya Kusini Magharibi inaweza kuathiriwa kwa nyakati tofauti kulingana na ratiba za utekelezaji wa kazi hizo.


Bi. Gowelle amesema TANESCO itaendelea kutoa taarifa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na majukwaa mbalimbali ya mawasiliano ili kuwawezesha wateja kupanga matumizi yao ya umeme kwa kuzingatia ratiba zitakazotolewa.


Aidha, amesisitiza kuwa Tanzania ina umeme wa kutosha na kwamba katizo hilo ni la muda, likiwa ni sehemu ya kukamilisha mradi huo wa kimkakati unaolenga kuimarisha uwezo wa usafirishaji wa umeme nchini. Ameongeza kuwa mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Lindi na Mtwara haitahusika katika ratiba hiyo ya katizo.


Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Kilovolti 400 Chalinze–Dodoma, Mhandisi Newton Mwakifwamba, amesema mradi huo wenye urefu wa kilomita 345 na thamani ya takribani shilingi bilioni 514 umefadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.


Amesema mradi unahusisha ujenzi wa njia mpya ya kusafirisha umeme pamoja na upanuzi wa vituo vya kupokea na kusambaza umeme vya Chalinze na Dodoma.


“Katika hatua hizi za mwisho, tutafanya kazi za kuvusha na kuunganisha njia mpya ya umeme katika maeneo ya Mkambarani, Kikombo na Mkonze. Hatua hizi ni muhimu ili kuhakikisha mradi unaanza kufanya kazi kwa ufanisi na usalama,” amesema Mhandisi Mwakifwamba.


Ameongeza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutaimarisha uwezo wa mfumo wa taifa wa usafirishaji umeme na kuwezesha usafirishaji wa umeme unaozalishwa katika Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere kwenda maeneo mbalimbali ya nchi, hatua itakayoimarisha uhakika wa upatikanaji wa umeme na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.







UMEME JUA KISHAPU AWAMU YA PILI KUIONGEZEA TANZANIA MEGAWATI 100 ZA NISHATI JADIDIFU

July 27, 2026 Add Comment




Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) imeingia hatua mpya ya kuongeza vyanzo vya uzalishaji umeme baada ya kusaini mkataba wa utekelezaji wa awamu ya pili ya Mradi wa umeme kwa nguvu ya Jua Kishapu utakaozalisha jumla ya megawati 100.



Hatua hiyo imekuja baada ya kukamilika kwa awamu ya kwanza ya mradi huo wenye uwezo wa kuzalisha jumla ya megawati 50 na kuingizwa katika Gridi ya Taifa, jambo lililoongeza uwezo na uthabiti wa gridi hiyo na kuimarisha upatikanaji wa umeme katika maeneo mbalimbali nchini.





Akizungumza katika hafla hiyo Julai 27, 2026, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amesema sekta ya nishati ni mhimili wa maendeleo ya Taifa ambapo Serikali inaendelea kufanya jitihada za kuongeza vyanzo mseto vya uzalishaji wa umeme (Energy Mix) ili kuhakikisha Tanzania haitegemei chanzo kimoja pekee cha uzalishaji wa umeme.

"Wananchi wa maeneo haya walikuwa wanategemea umeme uliokuwa unasafirishwa kutoka umbali mrefu. Kukamilika kwa mradi huu kutaifanya Tanzania kuwa na mfumo salama zaidi wa umeme na kuwa nchi ya mfano katika uzalishaji wa umeme unaostahimili mabadiliko ya tabianchi," amefafanua Mhe. Ndejembi.

Aidha, amelishukuru Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD) kwa kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania kupitia ufadhili wa mkopo wenye masharti nafuu. Amesema ushirikiano huo unaonesha imani kubwa ya washirika wa maendeleo katika usimamizi na utekelezaji wa miradi ya kimkakati nchini.

Pia ameipongeza TANESCO kwa kuendelea kusimamia utekelezaji wa miradi mikubwa ya umeme inayobadili taswira ya sekta ya nishati nchini, huku akiitaka kuhakikisha mradi huo unasimamiwa kwa karibu katika kila hatua ili ukamilike ndani ya muda uliopangwa na kuanza kuwanufaisha wananchi.

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, amesema utekelezaji wa mradi huo unaonesha dhahiri dhamira ya Wizara ya Nishati ya kuelekeza asilimia 97 ya bajeti yake katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

"Hatua hii ya utiaji saini ni matokeo ya diplomasia nzuri ya Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, iliyowafanya washirika wetu wa maendeleo kuendelea kuiamini Tanzania katika utekelezaji wa miradi ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme. Tunaamini Tanzania itaendelea kuwa na umeme wa kutosha," amesisitiza Mhe. Mgalu.

Akizungumza katika hafla hiyo, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO, Mhe. Balozi Zuhura Bundala, amesema Bodi ilisimamia kwa karibu utekelezaji wa awamu ya kwanza ya mradi huo na kuridhishwa na namna ulivyotekelezwa kwa kuzingatia thamani ya fedha iliyowekezwa. Amesema utiaji saini wa awamu ya pili ni hatua nyingine muhimu inayodhihirisha mafanikio ya mradi huo.



Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema gharama za mradi mzima wa Umeme wa Jua wa Kishapu wenye uwezo wa kuzalisha megawati 150 ni takribani Shilingi bilioni 323. Kati ya fedha hizo, awamu ya kwanza yenye uwezo wa kuzalisha megawati 50 imegharimu Shilingi bilioni 118.6, huku awamu ya pili yenye uwezo wa kuzalisha megawati 100 ikitarajiwa kugharimu takribani Shilingi bilioni 204.4.

"Mradi huu utatekelezwa kwa kipindi cha miezi 17 kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia TANESCO na Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD), ambalo limetoa mkopo wenye masharti nafuu," amefafanua Bw. Twange.

Mkataba huo umesainiwa kati ya TANESCO na muungano wa makampuni mbili kutoka Ufaransa na Tunisia, ambayo ni Sagemcom Energy, Telecom SAS na STEG International Services.