Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts

MRADI WA UMEME KISHAPU KIELELEZO CHA ONGEZEKO LA UZALISHAJI UMEME NCHINI- DC KISHAPU

November 29, 2025 Add Comment


📌Mradi wa umeme wa jua wafikia asilimia 84 ya utekelezaji


📌MD Twange aagiza ukamilishwe ifikapo Januari 15, 2026


Mkuu wa Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Mhe. Peter Masindi, amesema mradi wa umeme unaozalishwa kwa nguvu ya jua ni kielelezo cha ongezeko la uzalishaji wa umeme nchini  ikiwa ni dhamira ya Serikali ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ya kutaka kuongeza uzalishaji umeme hadi kufikia jumla ya megawati 8000 ifikapo mwaka 2030.

Mhe. Masindi aliyasema hayo Novemba 28, 2025, alipoambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, kukagua maendeleo ya Mradi wa kuzalisha umeme wa jua unaotekelezwa wilayani humo.

Amesema mradi huo sio tu utakuwa na faida kwa wananchi wa Mkoa wa Sinyanga pekee bali hadi katika mikoa ya Jirani ambapo pia amesema zaidi ya wananchi 1,200 waliokuwa wakiendesha shughuli zao katika eneo la Mradi tayari  wamelipwa fidia na kwamba jamii imeupokea mradi kwa mtazamo chanya na imekuwa mstari wa mbele kulinda miundombinu.


“Mradi huu ni tegemeo kwa wananchi  wa Kishapu wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha miundombinu inalindwa. Wameuelewa Mradi na wanaufurahia," alisema Mhe. Masindi.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, ameeleza kuwa mradi huo ni miongoni mwa miradi ya kielelezo inayotakiwa kukamilika ndani ya siku 100 tangu kuapishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameelekeza kiasi cha shilingi bilioni 118 kwa ajili ya utekelezaji wake.


Vilevile, alimuagiza mkandarasi anayetekeleza mradi kuhakikisha unakamilika  ifikapo Januari 15, 2026, akibainisha kuwa haitatolewa nyongeza ya muda na kwamba kinyume chake hatua za kisheria zitachukuliwa.

“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupatia takribani shilingi bilioni 118 kutekeleza mradi huu. Wajibu wetu ni kuhakikisha unakamilika kwa wakati. Watanzania waelewe kuwa dhamira ya Mheshimiwa Rais ni kuongeza uzalishaji wa umeme. Kwa sasa tunazalisha zaidi ya megawati 4,000, na kadri tunavyoongeza vituo vya kuzalisha  umeme ndivyo usambazaji unavyokuwa rahisi kwa wananchi,” alisisitiza Bw. Twange.


Ziara ya Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO imelenga kukagua maendeleo ya miradi ya umeme katika mikoa ya  kanda ya ziwa ukiwemo Mkoa wa Shinyanga, Mara, Geita na Kagera ambapo kwa sasa Mradi wa Kishapu umefikia asilimia 84 ya utekelezaji wake.

MKAKATI WA MAWASILIANO WA NISHATI YA KUPIKIA KICHOCHEO CHA MATUMIZI YA NISHATI SAFI-MBUJA

November 27, 2025 Add Comment


📌 Unalenga kuongeza  uelewa wa Watanzania juu  Matumizi ya Nishati safi ya Kupikia


📌 waambatana na Kauli mbiu isemayo Nishati safi ya kupikia okoa maisha na mazingira


📌Mwitikio wa wananchi  maeneo ya vijijini waongezeka kwa kasi


Imeelezwa kuwa Mkakati wa Taifa  wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia ni nyenzo  muhimu ya kufanikisha malengo ya Taifa ya kuhakikisha wananchi wanapika kwa  kutumia nishati safi, salama na rafiki wa mazingira.


Hayo yamebainishwa leo Novemba 27, 2025 Jijini Dar es Salaam na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano  Serikalini Wizara ya Nishati Bi. Neema Chalila Mbuja,wakati akizungumza  katika Kipindi cha Joto la Asubuhi kinachorishwa na Efm.

“Mkakati wa Mawasiliano wa nishati safi ya kupikia ni daraja muhimu linalounganisha wananchi, wadau wa maendeleo, na Serikali katika juhudi za kuongeza uelewa wa matumizi ya nishati rafiki kwa mazingira kwani kupitia mkakati huu, taarifa sahihi na za wazi zinawafikika wananchi kwa urahisi ili kusaidia jamii kuelewa faida za kutumia nishati safi lakini pia Mawasiliano madhubuti ili kuchochea mabadiliko ya tabia kwa kuwapa watumiaji taarifa zinazohitajika nakufanya maamuzi sahihi kuhusu matumizi ya nishati”.Amehimiza Bi. Mbuja.

Aidha Bi. Mbuja ameendelea kusisitiza kuwa utekelezaji wa mkakati wa Taifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia unatekeleza pia makubaliano ya kimataifa yanayolenga kupambana na mabadiliko ya tabianchi kwa kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa pamoja na kupunguza athari za kimazingira ili kutimiza malengo ya Serikali ya kuhakikisha  asilimia 80 ya wananchi watumie nishati safi ya kupikia ifikapo 2034.

Ameongeza kuwa katika kutoa elimu ya nishati safi ya kupikia Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Nishati kinaenda na Kauli mbiu isemayo Nishati safi ya kupikia okoa maisha na mazingira,kwani kauli mbiu hii inalenga kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi, kulinda afya za wananchi, kupunguza gharama za maisha, na kuimarisha uchumi kwa kuhakikisha kila mwananchi anafikiwa na huduma,elimu na miundombinu muhimu ya kutumia nishati safi ya kupikia.

 Kwa upande wake Mhandisi  Mwandamizi Utafiti  Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Bi. Catherine  Mwegoha ameeleza kuwa Mkakati wa Taifa wa Nishati safi ya kupikia ni dhana muhimu ya kufanikisha malengo ya Taifa ya kuhakikisha usalama, uendelevu na urahisi wa upatikanaji wa nishati  safi ya kupikia huku akieleza kuwa TANESCO imeendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia lengo likiwa ni kuhakikisha usalama, uendelevu na urahisi wa upatikanaji wa nishati hizo Kuokoa muda jikoni, Kupunguza gharama za matumizi pamoja na kupunguza athari za kimazingira na afya kwa watumiaji.


Naye Mhandisi Miradi kutoka Wakala wa Nishati vijiijini(REA) Bi. Raya Majallah amethibitisha kuwa mwitikio wa wananchi juu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa vijijini umeongezeka kwani wameendelea kutoa majiko kwa bei ya ruzuku. na kupitia ruzuku hiyo wananchi wameendelea kununua majiko kwa wingi hivyo jitihada hizo zinaonyesha hadi kufikia 2034 asilimia 80%  ya wananchi watakua wamehamia kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia.

TUTAENDELEA KUUNGA MKONO AJENDA YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KWA VITENDO

November 25, 2025 Add Comment




Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Nishati, Bi. Neema Mbuja amesema kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa vitendo ili kufikia malengo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha ifikapo mwaka 2034, asilimia 80% ya wananchi wanatumia nishati safi katika shughuli za upishi.

Akizungumza leo Novemba 25, 2024 katika kipindi cha Jambo Tanzania cha TBC1, katika kipengele cha Jikoni na Chigo, Bi. Mbuja amesema kuwa mahojiano hayo ni sehemu ya muendelezo wa ziara ya Wizara ya Nishati katika vyombo mbalimbali vya habari kwa lengo la kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu faida na umuhimu wa kutumia nishati safi ya kupikia.
Aidha, amesisitiza kuwa Wizara ya Nishati itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali pamoja na jamii katika kuhakikisha elimu kuhusu matumizi ya nishati safi inawafikia wananchi wengi zaidi, hivyo kuchochea utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa kuimarisha afya, mazingira na ustawi wa jamii kupitia matumizi ya nishati rafiki.

TANESCO MMEFANYA MABORESHO YA KIWANGO CHA JUU KATIKA KUWAHUDUMIA WATEJA – DC MPOGOLO

November 20, 2025 Add Comment

📌Apongeza jitihada za kuendelea kusogeza huduma karibu na wananchi


📌Awataka Wenyeviti wa Serikali za Mitaa kushirikiana na TANESCO kulinda miundombinu ya umeme 


Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Mhe. Edward Mpogolo, amelipongeza Shirika la umeme Tanzania (TANESCO) kwa kufanya maboresho makubwa ya kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika na kuendelea kusogeza huduma zake karibu wananchi.

Akizungumza Novemba 20 wakati akifungua kikao kazi kati ya TANESCO, madiwani na wenyeviti wa Serikali za mitaa kutoka Halmashauri za Manispaa ya Ilala, Temeke na Kigamboni, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Mpogolo amebainisha kuwa viongozi hao ni nguzo muhimu katika kufikisha taarifa, kero na changamoto za wananchi kwa Taasisi husika.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa viongozi hao katika kusimamia ulinzi wa Miundombinu ya Umeme, kwani Serikali imewekeza fedha nyingi katika utekelezaji wa miradi ya umeme ambayo inapaswa kuendelea kuwanufaisha wananchi kijamii na kiuchumi.

“Kikao kazi hiki kinawapa nafasi Wenyeviti wa Serikali za Mitaa pamoja na Madiwani kutambua kazi kubwa inayofanywa na TANESCO kwa nchi yetu, ikiwa ni pamoja na kuwaweka karibu viongozi hao na TANESCO katika kushirikiana na wananchi katika suala zima la utumiaji wa huduma za umeme na ulinzi wa miundombinu ya umeme.

"Nachukua nafasi hii kumpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO pamoja na Serikali kwa ujumla kwa uwekezaji mkubwa katika miradi ya umeme ambayo imekuwa na manufaa chanya kwa wananchi kiuchumi na kijamii,” alisisitiza Mhe. Mpogolo.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja akimuwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bi. Irene Gowelle, amesema TANESCO inaendeleza mkakati wa kufanya kazi kwa karibu zaidi na Viongozi wa Serikali za mitaa ili kuwafahamisha kuhusu maboresho yanayoendelea kufanyika pamoja na maendeleo ya miradi ya umeme katika maeneo yao. Pia kuwaweka karibu viongozi hao kuwafanya kuwa kiungo muhimu katika kupeleka taarifa kwa wananchi.

“Serikali sasa imeelekeza kuongeza nguvu katika kuwahudumia wananchi hivyo Ushirikiano na viongozi hawa ni muhimu kwa kuwa wao daraja kati yetu na wananchi kwenye maeneo yao na tukifanya nao kazi kwa ukaribu, tutawafikia wananchi kwa haraka na kwa uhakika zaidi,” alisema Bi. Gowelle.


Naye Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa Mkoa wa Dar es Salaam, Juma Abbas Mwegamno, ameishukuru TANESCO kwa kutoa nafasi kwa viongozi hao kushiriki katika kikao kazi hicho na kuwapa elimu kuhusu miradi ya umeme. Amesema hatua hiyo inawajengea uwezo wa kurudisha taarifa  kwa wananchi, kama inavyoelekezwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu wajibu wa mamlaka za umma.


Miongoni mwa elimu waliyopewa viongozi wa Serikali za mitaa na madiwani ni pamoja na maendeleo ya miradi mbalimbali ya umeme katika maeneo yao, elimu kuhusu Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa Umeme, pamoja na maboresho yanayoendelea katika eneo la huduma kwa mteja

MKAKATI WA TAIFA UMELENGA KUFIKIA 80% YA WATANZANIA KUTUMIA NISHATI SAFI IFIKAPO 2034

November 17, 2025 Add Comment


*📌Kutoa uelewa kwa Watanzania kuhusu Matumizi ya Nishati safi ya Kupikia*


*📌Kuwashirikisha Wadau mbalimbali ili kuhakikisha upatikanaji wa vifaa kwa bei nafuuu hususani maeneo ya Vijijini*


Dar es salaam


Imeelezwa Kuwa, Mkakati wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia ni Dira muhimu ya kufanikisha malengo ya Taifa ya kuhakikisha wananchi wanatumia nishati safi na salama, rafiki wa mazingira na yenye gharama nafuu hadi kufikia mwaka 2034 ambapo asilimia 80% ya Watanzania wawe wanatumia  nishati safi ya kupikia.


Hayo yamebainishwa leo novemba 17, 2025 na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano  Serikalini Wizara ya Nishati Bi. Neema Mbuja wakati akizungumza  na wananchi katika kipindi cha Crown Sport Jijini Dar es Salaam, ambapo ameeleza kuwa Mkakati wa Nishati safi ya kupikia ni nyenzo muhimu katika kutekeleza makubaliano ya kitaifa na kimataifa yanayolenga kupambana na mabadiliko ya tabia ya nchi na kupunguza uzalishaji wa gesi joto.   

“Kupitia Mkakati wa Taifa wa miaka kumi, Serikali inalenga kufikisha asilimia 80 ya kaya za Tanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034. Mkakati huu unajikita katika kupunguza magonjwa ya kupumua yanayotokana na moshi, kulinda misitu, na kuongeza fursa za kiuchumi kupitia uwekezaji katika teknolojia na vifaa safi vya kupikia pia Serikali imesisitiza kuwa utekelezaji wa mkakati huo utahusisha sekta binafsi, taasisi za maendeleo, na jamii kwa ujumla zinazolisha watu zaidi ya 100 kama Shule na Magereza”. Ameeleza Bi. Mbuja.



Amefafanua kuwa, Mkakati wa Taifa wa Nishati safi ya kupikia unakwenda sambamba na Mkakati wa mawasiliano kwani umelenga kuamsha uelewa wa watanzania  kupata taaarifa juu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia siliano kwani kupitia kampeni za kitaifa zitakazohusisha redio, televisheni, mitandao ya kijamii, maonyesho ya wazi, pamoja na mafunzo maalum kwa viongozi wa jamii, waandishi wa habari na washawishi wa mitandaoni  Watanzania wanapata ujumbe mahususi na uelewa  kuhusu nishati safi ya kupikia.



Kwa upande wake, Mhandisi wa Utafiti Shirika la Umeme Tanzania(TANESCO) Samwel Kessy ameeleza kuwa Mkakati wa Taifa wa Nishati safi ya kupikia ni dhana muhimu ya kufanikisha malengo ya Taifa ya kuhakikisha usalama, uendelevu na urahisi wa upatikanaji wa nishati  safi ya kupikia, kuokoa muda, pamoja na kupunguza gharama za matumizi, athari za kimazingira na kiafya kwa watumiaji.


Ameongeza kuwa, Serikali  ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imejikita kutoa elimu kwa wananchi ili kuhakikisha kila Mwananchi anapata uelewa juu ya faida za matumizi ya  nishati safi ya kupikia pamoja na kuhakikisha wadau mbalimbali wanashirikishwa ili kuhakikisha upatikanaji wa vifaa na nishati kwa bei nafuu, hususan imaeneo ya vijijini.


“Sisi kama TANESCO tumehakikisha umeme umewafikia wateja kwa kiasi kikubwa na unapatikana kwa uharaka lakini pia kwa kushirikiana na sekta binafsi tumehakikisha wananchi wanapata vifaa bora vya kupikia na vyenye gharama nafuu ili waweze kuhamia kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia. Amesisitiza Mhandisi. Kessy.

ELIMU YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA YAWAFIKIA MAAFISA DAWATI NGAZI YA MIKOA NA HALMASHAURI

October 27, 2025 Add Comment


📌 *Lengo ni  kuwa na uelewa wa pamoja katika utekelezaji  wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia.*


📌 *Mafunzo kuhusisha mikoa 26 na Halmashauri zake.*


Wizara ya Nishati imeanza kutoa elimu kuhusu Nishati Safi ya Kupikia  kwa  Maafisa Dawati wa Nishati Safi ya Kupikia ngazi ya mikoa na halmashauri  kwa lengo la kuwa na uelewa wa pamoja katika utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia pamoja na  kuwawezesha Maafisa Dawati kutambua majukumu yao katika utekelezaji wa mkakati..

Akifungua  mafunzo hayo, wilayani Kibaha mkoani Pwani,  Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa  Pwani, Bi. Hadija Mruma ameipongeza Wizara ya Nishati kwa jitihada mbalimbali inazochukua kwa vitendo katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini mojawapo ikiwa ni kuhakikisha elimu na vifaa vya nishati safi ya kupikia vinafika hadi ngazi za Mikoa, Halmashauri na Vijiji.

Ameeleza kuwa Mkoa wa Pwani unachukua hatua mbalimbali kuhakikisha kuwa wanachi wanatumia nishati safi ya kupikia katika ngazi ya taasisi, kaya n.k akitoa mfano kuwa asilimia 76 ya taasisi zinazolisha watu zaidi ya 100 mkoani humo zimeshahamia kwenye nishati safi ya kupikia.


Aidha, amewapongeza Watendaji wa Wakala wa Nishati Vijijini ( REA)  ambao wanashirikiana na Mkoa wa Pwani kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwemo utoaji mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku.


Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Ngereja Mgejwa ameeleza kuwa mafunzo kuhusu Nishati Safi ya Kupikia yameanza kutolewa wilayani Kibaha, mkoani Pwani kwa kuhusisha Mikoa ya Pwani, Morogoro, Dar es Salaam, Mtwara, Lindi na Tanga.

Ameongeza kuwa, elimu ya nishati safi ya kupikia itaendelea kutolewa kwa Maafisa Dawati wa Nishati Safi ya Kupikia katika mikoa mingine iliyosalia kwani lengo ni kutoa elimu husika katika  Mikoa yote 26 pamoja na Halmashauri zake.


Amesema kuwa suala la matumizi ya nishati safi ya kupikia ni kipaumbele cha nchi na dunia kwa ujumla ili kuondokana na athari zake katika  mazingira, afya na kiuchumi.


Naye, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kutoka Wizara ya Nishati, Bi. Neema Mbuja ameeleza kuwa mafunzo yanayotolewa kwa maafisa dawati hao yanahusisha pia masuala ya Mkakati wa Taifa wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia.


Ameeleza kuwa ili kufikisha elimu kwa wananchi kuhusu nishati safi ya kupikia ni muhimu maafisa dawati hao wakafahamu njia za mawasiliano zitakazowasadia kufikisha elimu  na  jumbe zitakazotumika kuendana na maeneo wanayoyasimamia.


Ameongeza kuwa uwepo wa Mkakati wa Taifa wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia  (National Clean Cooking Communication Strategy) unatoa mwongozo wa namna wadau watakavyoshirikiana kutoa elimu kwa umma ili kuondoa dhana potoshajii (misconception) kuhusu nishati safi ya kupikia na kubadili mitazamo hasi kuwa chanya kwa lengo la kuleta mabadiliko katika utekelezaji wa ajenda ya kitaifa ya nishati safi ya kupikia.

TANESCO YAOKOA UPOTEVU WA MAPATO WA SHILINGI BILIONI 1.7 KUPITIA ZOEZI LA UKAGUZI WA MITA NCHINI

October 25, 2025 Add Comment


📌 Jumla ya wateja 1,700 wamebainika kutumia umeme kinyume na taratibu.


📌 Yatoa  onyo kali kwa wateja wanaofanya udanganyifu kurejesha umeme kwa kutumia vishoka baada ya kusitishiwa huduma 


Na. Agnes Njaala, Dar es Salaam


Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limefanikiwa kuokoa upotevu wa mapato unaokadiriwa kufikia shilingi bilioni 1.7, kufuatia utekelezaji wa zoezi la ukaguzi wa miundombinu ya umeme linaloendelea kote nchini.


Akitoa tathmini ya utekelezaji wa zoezi hilo mapema wiki hii , Meneja Msimamizi wa mfumo wa Mita, Mhandisi Nyanda Mlagwa, alisema ukaguzi huo ulianza mwezi Julai 2025 ukilenga kubaini matumizi yasiyo halali ya umeme na kudhibiti vitendo vya wizi unaosababisha hasara kwa Shirika na Serikali.

“ Napenda kuutarifu umma kuwa hadi sasa, ukaguzi uliofanyika umebaini upotevu wa takribani shilingi bilioni 4, ambapo zaidi ya bilioni 1 zimeshalipwa na wateja waliobainika kuwa na makosa, huku wengine wakiendelea kulipa madeni yao,” alibainisha Mhandisi Mlagwa.

Ameongeza kuwa mapato yanayopatikana yataelekezwa katika kuboresha huduma kwa wateja na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme nchini. Aidha, amesema baadhi ya makosa yaliyobainika ni pamoja na uunganishaji wa umeme kinyume na taratibu, uchepushaji wa nyaya kabla ya mita (bypass), uhamishaji holela wa mita, na kuchezea kufuli za mita (seal).

Ametoa  wito kwa watanzania kutoa taarifa za wahujumu kupitia mfumo wa TANESCO wa Whistleblower ambao umekuwa ukisisitizwa kuwa ni mfumo bora na salama  ili kusaidia kudhibiti vitendo vya uhujumu. 


Mhandisi Msimamizi  Kitengo cha Uthibiti wa Mapato Makao Makuu , Mposheleye Mwasenga alisema jumla ya wateja 1,700  katika kipindi tajwa wamebainika kutumia umeme kinyume na taratibu akisisitiza kuwa makadirio yote yamefanywa kwa usahihi kulingana na matumizi halisi na wote wameandikiwa madeni na faini kwa mujibu wa sheria na miongozo ya EWURA.

Akitoa onyo kwa wateja wanaofanya udanganyifu wa kurejesha umeme kwa kutumia vishoka, Mhandisi wa Uthibiti wa Mapato wa Mkoa wa Kinondoni Kusini, Salumu Mbepei, amesema kuwa Shirika lipo macho na limeunda timu maalumu ya kufuatilia vitendo hivyo, na kwamba wote watakaobainika watachukuliwa hatua kali zaidi za kisheria.


Naye Bw. Damasi Kimaro, Fundi Mkaguzi, ametaja mojawapo ya changamoto kubwa wanazokutana nazo wakati wa ukaguzi kuwa ni baadhi ya wateja kukaidi kuruhusu ukaguzi, hali inayokwamisha utekelezaji wa operesheni kwa ufanisi. Ameitoa wito kwa wateja kutoa ushirikiano kwa wakaguzi, akisisitiza kuwa zoezi hilo linafanyika kwa mujibu wa sheria na taratibu.


Shirika linaendelea kuufahamisha umma kuwa utekelezaji wa mkakati wa kudhibiti upotevu wa mapato nchini ni endelevu, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuhakikisha matumizi sahihi ya huduma ya umeme na kuimarisha ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

MRADI WA TAZA KUFUNGUA SOKO JIPYA LA BIASHARA YA UMEME AFRIKA

October 23, 2025 Add Comment


📌 *Wafikia asilimia 83*


*📌Dkt. Mataragio akagua mradi na kutoa maelekezo TANESCO*


📌 *TAZA kuunganisha Mkoa wa Rukwa na gridi ya Taifa*


📌 *Kuimarisha upatikanaji umeme Mikoa ya Kusini mwa Tanzania*



Mbeya


Imeelezwa kuwa mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Iringa hadi Zambia kupitia Tunduma (TAZA) umefikia asilimia 83.45 huku ukitarajiwa kukamilika ifikapo Mei 2026 na hivyo  kufungua soko jipya la biashara ya umeme barani Afrika.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua utekelezaji wa mradi huo leo Oktoba 23, 2025 katika eneo la Iganjo, Mbeya, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Dkt. James Mataragio amesema mradi wa TAZA ni muhimu kwa Taifa kwa kuwa utaiunganisha Tanzania na Nchi za ukanda wa Kusini mwa Afrika (Southern Africa Power Pool) na pia kuimarisha muunganiko wa ukanda wa Mashariki mwa Afrika (East Africa Power Pool).

“Nimshukuru na kumpongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya nishati. Kupitia mradi huu tutaimarisha biashara ya kuuza na kununua umeme kati ya nchi za Mashariki mwa Afrika na zile zilizopo Kusini mwa Afrika”. Amesema Dkt. Mataragio

Kuhusu biashara ya umeme ya kikanda, Dkt. Mataragio amesema kuwa tayari Tanzania imeshaunganisha gridi ya umeme na  Nchi za Afrika za Kenya, Rwanda, Burundi na Ethiopia kupitia muunganiko wa East Africa Power Pool.

“Tutaunganisha pia gridi na nchi za Kaskazini na Magharibi mwa Afrika ili Afrika nzima tuweze kuuziana umeme ikiwa ni sehemu pia ya  kutekeleza Mpango wa Nishati unaolenga kuwafikishia umeme waafrika takribani milioni 600 ambao bado hawajafikiwa na nishati ya umeme”. Amesisitiza Dkt. Mataragio.

Kuhusu mradi wa TAZA, ameeleza kuwa unatekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ambao ni Benki ya Dunia, Umoja wa Ulaya na Shirika la Maendeleo la Ufaransa kwa Dola za kimarekani milioni 584.

Amesema kuwa mbali ya mradi wa TAZA kuunganisha gridi za umeme za Nchi za Kusini mwa Afrika, utauunganisha Mkoa wa Rukwa na umeme wa gridi pamoja na kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme katika Mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya na Songwe.

Baada ya kukagua mradi huo, Dkt. Mataragio ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kuhakikisha linamsimamia Mkandarasi kwa karibu hasa katika kipindi hiki cha mvua ili hatua za awali za ujenzi wa misingi (foundation) ziweze kukamilika kwa wakati na kumtaka Mkandarasi kuhakikisha vifaa vyote vipo eneo la Mradi.

Katika hatua nyingine Dkt. Mataragio ameiagiza TANESCO kuhakikisha inapeleka umeme eneo la Ngozi unapotekelezwa mradi wa kuzalisha umeme kwa jotoardhi ambapo kwa hivi sasa mitambo ya uhakiki wa jotoardhi katika eneo hilo inatumia mafuta ya dizeli.

Katika ziara hiyo Naibu Katibu Mkuu aliambatana na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu Mha. Innocent Luoga na watendaji wa Wizara ya Nishati na TANESCO.



TANESCO YAANZA MAJARIBIO YA MTAMBO WA KUZALISHA UMEME MTWARA

October 23, 2025 Add Comment


📍Jumla ya megawati 70 zaongezeka katika mikoa ya Lindi na Mtwara


📍RC Mtwara kuuzindua Mtambo huo tarehe 27/10/2025


Na Charles Kombe, Mtwara.


Kazi ya ufungwaji wa Mtambo wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia katika Kituo cha TANESCO cha Mtwara II umekamilika kwa ufanisi mkubwa, na tayari mashine mpya imeanza kufanyiwa majaribio ya kuanza kuwahudumia wakazi wa mikoa ya Kusini mwa Tanzania ya Mtwara na Lindi.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa maendeleo ya kazi ya ufungwaji wa mtambo huo, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma kwa Wateja, Bi. Irene Gowelle, amesema hatua hiyo ni ushahidi wa utekelezaji wa mipango ya serikali ya awamu ya sita ya kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.

“Kwa mafanikio makubwa, ile kazi ya ufungaji wa mashine ya kuzalisha umeme kwa njia ya gesi asilia ambayo imekuwa ikiendelea katika kituo chetu cha Mtwara II, imekamilika kwa ufanisi mkubwa na kabla ya muda ambao tuliutangaza na hivi sasa uanfanyiwa majaribio kwa ajili ya kuangalia ufanisi na namna itaendelea kuwahudumia wateja wetu,” amesema Bi. Gowelle.

Ameongeza kuwa mashine hiyo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mhe Kanali Patrick Sewala hivi karibuni, na itakuwa ni nyongeza muhimu kwa nguvu ya uzalishaji wa umeme katika mikoa ya Mtwara na Lindi.


“Hizi zote ni jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha kwamba kila Mtanzania anapata huduma ya umeme wa uhakika,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Kaimu Naibu Mkurugenzi wa Uzalishaji Umeme TANESCO, Mhandisi Antony Mbushi, amesema kukamilika kwa mradi huo kunamaanisha ongezeko la uzalishaji wa megawati 20 zaidi kwa kanda ya kusini.


“Awali tulikuwa na uwezo wa megawati 50.5, lakini sasa tutakuwa na jumla ya megawati 70 katika mikoa yetu ya Mtwara na Lindi. Tunaendelea kuwahakikishia wateja wetu kuwa umeme upo wa kutosha na wa uhakika,” amesema Mha. Mbushi.


Naye mtaalamu wa umeme, Bw. Fikiri Khalifa, amesema kazi hiyo imekamilika kwa kasi isiyotarajiwa.


“Tulitarajia mwisho wa mwezi ndio mashine ingeanza kazi, lakini tumekamilisha kabla ya muda huo. Hili ni jambo kubwa katika utekelezaji wa miradi ya kitaifa,” amesema Bw. Khalifa.


Kufungwa kwa mtambo huu ni sehemu ya juhudi za serikali kuongeza upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa Watanzania wote, hasa katika maeneo ambayo yamekuwa yakikumbwa na changamoto za upungufu wa umeme kwa miaka mingi ya Mtwara na Lindi.