Showing posts with label biashara. Show all posts
Showing posts with label biashara. Show all posts

MH. LUSWETULA: TRA IHARAKISHE TATHMINI YA MAHITAJI YA VITUO VYA FORODHA.

April 08, 2026 Add Comment


Na. Saidina Msangi, WF, Dodoma.

Serikali imesema kuwa kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inaendelea kufanya tathmini ya mahitaji ya ujenzi wa Kituo cha Forodha katika Jimbo la Momba, ikiwemo upembuzi yakinifu, upatikanaji na utambuzi wa eneo, gharama za mradi na utayari wa nchi jirani.

Hayo yalisemwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Momba, Mhe. Condester Michael Sichalwe, aliyetaka kujua wakati ambao Serikali itajenga kituo cha forodha katika Jimbo la Momba mkoa wa Songwe.

Alisema eneo hilo linaangaliwa kwa kuzingatia ongezeko la shughuli za biashara na umuhimu wake katika kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato na udhibiti wa biashara mipakani.

’’Ujenzi wa vituo vya forodha, ikiwemo katika Jimbo la Momba, hufanyika kwa kuzingatia vipaumbele vya Serikali, ukamilifu wa taratibu na kanuni za kiforodha, utayari wa nchi jirani tunazopakana nazo, masuala ya kiusalama, upatikanaji wa rasilimali fedha, pamoja na tathmini ya umuhimu wa eneo husika katika shughuli za biashara za mipakani,’’ alifafanua Mhe. Luswetula.

Aliongeza kuwa ujenzi wa kituo hicho utaanza mara baada ya kukamilika kwa maandalizi yote muhimu, ikiwa ni pamoja na kupatikana kwa fedha za utekelezaji wa mradi katika bajeti ya Serikali na kutangazwa kwenye Gazeti la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aidha, Mhe. Luswetula alieleza kuwa TRA inaendelea na maandalizi na itatoa taarifa rasmi pindi ratiba ya utekelezaji wa ujenzi itakapokamilika na kuielekeza TRA kuharakisha tathmini hiyo ambayo iko katika hatua za mwisho.

TANZANIA YANG’ARA KIMATAIFA KWA USIMAMIZI BORA WA DENI LA SERIKALI

March 28, 2026 Add Comment

  Na Joseph Mahumi, WF


Serikali ya Tanzania imeendelea kung’ara katika jukwaa la kimataifa baada ya kuibuka mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.

Ushindi huo mkubwa unatokana na juhudi za Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa deni la umma, ikiwemo kuunganisha vyema mifumo ya kifedha ya Serikali na kuboresha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya maendeleo, ambapo Jopo huru la wataalamu lililochambua mawasilisho kutoka nchi mbalimbali za Jumuiya ya Madola lilizingatia vigezo vya ubunifu, uimara na uendelevu katika kutoa tuzo hizo.

Akifungua hafla ya utoaji tuzo hizo, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal, alisisitiza umuhimu wa nchi wanachama kuendelea kubuni mbinu madhubuti za kusimamia deni la umma ili kulinda uchumi dhidi ya misukosuko ya kifedha duniani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola, Bi. Ruth Kattumuri, aliipongeza Tanzania kwa mageuzi makubwa iliyoyafanya katika kuimarisha usimamizi wa deni la umma.

Alieleza kuwa mafanikio hayo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya nchi katika kujenga uchumi imara na unaostahimili mishtuko ya kiuchumi.

Aidha, Bi. Kattumuri, alisema kuwa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola itaendelea kuisaidia Tanzania katika juhudi zake za kuboresha sera na mifumo ya usimamizi wa deni, sambamba na utekelezaji wa maazimio ya Kikao cha 72 cha Kundi la Mawaziri wa Jumuiya ya Madola.

Mkutano huo wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola uliofanyika kwa muda wa wiki moja uliwakutanisha wataalamu wa usimamizi wa deni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kujifunza na kujadili mbinu bora za kukopa, kusimamia na kulipa deni la umma, na umeandaliwa ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Jumuiya ya Madola wa Deni Imara, Bunifu na Endelevu, ambapo Tanzania imejitokeza kama kinara na mfano wa kuigwa barani Afrika na katika Jumuiya nzima ya Madola.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) akiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal (kushoto) na  Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya hiyo, Bi. Ruth Kattumuri.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama, akionesha tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) Aakiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni washindi wenngine wa tuzo hizo kutoka nchi ya Barbados ambayo iliibuka mshindi wa Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Caribbean na Sri Lanka Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Asia.

AIRTEL TANZANIA YAZINDUA MADUKA 17 YA SMART SHOPS DAR ES SALAM ,KUKUZA HUDUMA ZA KIDIJITALI

March 25, 2026 Add Comment

  Airtel Tanzania, kampuni inayoongoza huduma za mawasiliano nchini, imezindua maduka mapya 17 ya Airtel Smart Shops jijini Dar es Salaam. Maduka haya ni sehemu ya mtandao wa maduka 31 nchini kote, ukiwa na lengo la kupanua huduma za kidijitali na kuongeza ujumuishaji wa kifedha kwa wananchi.


Uzinduzi huo uliofanyika Machi 12, 2026, ulihudhuriwa na Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, pamoja na viongozi wa serikali, wajasiriamali, na vyombo vya habari.

Waziri Kairuki alieleza kuwa uwekezaji huu ni ishara ya nia ya dhati kwa Airtel kuleta mapinduzi makubwa katika sekta ya mawasiliano na kuonyesha imani yake katika mazingira ya biashara Tanzania chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Maduka haya mapya yanaonyesha dhati ya Airtel katika kuleta huduma karibu na wananchi huku yakiboresha uzoefu wa wateja. Pia unaashiria imani thabiti katika mazingira ya biashara Tanzania,” alisema Waziri Kairuki.


Kwa upande wake, Charles Kamoto, Mkurugenzi Mtendaji wa Airtel Tanzania, alisema maduka haya hayako tu kama maduka ya rejareja. Yameundwa kama vituo vya kisasa vya huduma za kidijitali, vinavyotoa usajili wa SIM, intaneti ya kasi, huduma za kifedha kupitia Airtel Money, mauzo ya simu, na suluhisho za kibiashara kwa SMEs.


Maduka haya yamewekwa katika maeneo yenye shughuli nyingi jijini Dar es Salaam, ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wakazi na wajasiriamali. Uzinduzi huu ni sehemu ya mpango wa kitaifa wa “Airtel Kila Kona”, unaolenga kufanikisha upatikanaji wa huduma za mawasiliano hata katika maeneo ya vijijini.

Kampuni pia imewekeza katika kupanua mtandao wake wa 4G, kuanzisha teknolojia ya 5G, na kuongeza uunganishaji wa kimataifa kupitia mfumo wa nyaya za chini ya bahari wa 2Africa Submarine Cable System.



Adriana Lyamba, Mkurugenzi wa Uzoefu wa Wateja Airtel Tanzania, alisema maduka haya yameundwa kutoa huduma haraka, bila karatasi, na kwa ufanisi. Maduka haya yanatarajiwa pia kuunda ajira na kusaidia SMEs na wajasiriamali wa ndani kwa kuwapatia zana za kifedha za kidijitali na huduma za mawasiliano za kisasa.

WAZIRI NANAUKA -SERIKALI ITAENDELEA KUVIPA KIPAUMBELE VIKUNDI VINAVYOREJESHA MIKOPO

March 15, 2026 Add Comment

 

















Na Oscar Assenga,Muheza, Tanga

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka amesema serikali itaendelea kuvipa kipaumbele vikundi vya vijana vinavyoonyesha uwajibikaji kwa kurejesha mikopo wanayopewa ili viweze kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Nanauka aliyasema hayo leo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyotembelea kikundi cha Vijana cha Mali Hai kilichopo wilayani Muheza mkoani Tanga kwa lengo la kukagua shughuli zao za uzalishaji pamoja na miradi iliyopata fedha kupitia mikopo ya halmashauri.

Akiwa kwenye kikundi hicho alionyesha kuridhishwa na juhudi na nidhamu ya kikundio hicho kurejesha mikopo baada ya kufanikiwa kukuza mtaji wake kutoka shilingi milioni 20 hadi kufikia zaidi ya shilingi milioni 50, hatua inayotajwa kuwa mfano bora kwa vikundi vingine vya vijana nchini.

Nanauka alisema kikundi cha Mali Hali ni miongoni mwa vikundi vichache nchini vilivyofanikiwa kurejesha mikopo kwa wakati, jambo ambalo limekifanya kupata nafasi ya kuangaliwa kwa karibu zaidi katika mipango ya kusaidiwa kuongeza mtaji na kupanua shughuli zake.

Alisema katika mchakato unaoendelea wa kusaidia wajasiriamali wadogo na kurasimisha shughuli zao, serikali itaangalia namna ya kukiweka kikundi hicho kwenye orodha ya vikundi vitakavyosaidiwa ili kuimarisha shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, alieleza kuwa serikali inatekeleza maelekezo ya Rais ya kuhakikisha vijana wanaochukua hatua ya kufanya kazi na kuonyesha juhudi wanapatiwa mikopo na serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi na pia kutoa ajira kwa wengine.

“Vijana hawa wameonyesha mfano mzuri kwa watanzania wengine wameanza na mtaji mdogo mwaka 2008,wakapata msaada wa shilingi milioni tano mwaka 2018 na baadaye mkopo wa shilingi milioni 20 mwaka wa fedha 2020/2021. Leo hii wameongeza mtaji wao hadi kufikia zaidi ya milioni 50. Huu ni ushahidi kwamba ndoto kubwa zinaweza kuanza na mwanzo mdogo,” alisema Nanauka.

Aliongeza kuwa serikali itahakikisha vijana wenye juhudi kama hao wanapata fursa zaidi, ikiwemo mikopo mingine, pamoja na kushirikishwa katika zabuni za serikali ili waweze kukuza biashara zao.

Nanauka pia aliwashauri vijana nchini kutokudharau mwanzo mdogo na kuwa na uvumilivu wanapotekeleza ndoto zao za kimaendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Hawa Mchafu, alisema kamati hiyo ipo katika ziara ya kawaida ya kukagua miradi ya maendeleo kabla ya kuanza kwa Bunge la Bajeti, ambapo wamepita katika maeneo mbalimbali kutathmini miradi iliyopata fedha za serikali.

Alisema kamati hiyo imevutiwa na kazi nzuri inayofanywa na kikundi hicho cha vijana, lakini imebaini changamoto ya eneo la uzalishaji kuwa dogo na huenda lisiweze kukidhi mahitaji yao iwapo wataongeza mtaji zaidi.

Kutokana na hali hiyo, kamati imeitaka wizara husika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuhakikisha vijana hao wanapatiwa eneo kubwa zaidi la kufanyia shughuli zao za uzalishaji ili waweze kupanua biashara zao.

“Eneo walilonalo sasa ni dogo ukilinganisha na malengo yao ya kupanua uzalishaji hivyo tunashauri wapatiwe eneo kubwa zaidi na lililopo sasa likibaki kama sehemu ya maonesho ya bidhaa wanazozalisha,” alisema Mchafu.

Pia aliishauri serikali kuangalia uwezekano wa kukipa kikundi hicho mkopo mwingine wa kifedha ili kiweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokikabili, ikiwemo kununua gari kwa ajili ya shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha vijana nchini kutumia fursa zilizotolewa na serikali kupitia mifuko mbalimbali ya maendeleo ya vijana badala ya kujikita kwenye mfuko mmoja pekee.

Mchafu alisema kuwa Rais ametoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vijana kupitia wizara na taasisi mbalimbali, hivyo vijana wanapaswa kuzitumia fursa hizo kujikwamua kiuchumi.

Kamati hiyo pia imeishauri serikali kuhakikisha sheria ya manunuzi ya umma inayotaka asilimia 30 ya zabuni za serikali zitolewe kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu inatekelezwa kikamilifu ili kuwapatia vijana nafasi ya kukua kiuchumi.

Kwa sasa kikundi cha Mali Hali kinadaiwa kuajiri vijana zaidi ya 20 katika shughuli zake za uzalishaji, jambo ambalo limeelezwa kuwa linaunga mkono dhamira ya serikali ya kukuza ajira kwa vijana na kuimarisha uchumi wa wananchi.

Vijana wa kikundi hicho pia wamemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fursa na kuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kufikia ndoto zao za kuanzisha kampuni kubwa inayoweza kutoa ajira kwa vijana wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini.

Mwisho.