Showing posts with label elimu. Show all posts
Showing posts with label elimu. Show all posts

MAKAMU WA RAIS AFUNGUA KONGAMANO LA KIMATAIFA LA ELIMU

March 25, 2026 Add Comment

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala linahitaji ushirikiano wa hali ya juu miongoni mwa wadau wote wa elimu, taasisi za serikali na zile zisizo za serikali, wazazi na jamii yote kwa ujumla


Makamu wa Rais amesema hayo, wakati akifungua Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya sera ya elimu na mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam. Ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Taasisi za elimu, hususan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuendelea kufanya ufuatiliaji na tafiti ili kubaini dosari zozote zinazoweza kukwamisha utekelezaji wa suala hilo ili kubaini na kuibua maeneo yanayohitaji maboresho zaidi kiutendaji.

Makamu wa Rais, amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera yetu ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala kuanzia Elimu ya Awali, Msingi, Sekondari hadi Elimu ya Juu. linataka Watanzania wote kutafsiri vema maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan juu ya mfumo wa elimu unaozingatia kutoa ujuzi na maarifa ili kumwezesha mhitimu kumudu mazingira yake, na kumudu ushindani kwenye ulimwengu wa kazi.

Aidha, Makamu wa Rais amesema suala la elimu jumuishi inayozingatia usawa ni miongoni mwa vipaumbele, ambapo Serikali imeweka msisitizo katika uwepo wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na miundombinu rafiki kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum. Amesema suala hilo linakwenda sambamba na uandaaji wa walimu wenye ujuzi wa elimu maalum ili kufundisha wanafunzi hao.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda amesema kongamano hilo la kimataifa kuhusu maboresho ya sera na elimu na mitaala ni fursa nzuri ya ushirikishwaji wa watalaam na wachambuzi kuangalia jinsi ambavyo utekelezaji huo unaendelea.

Amesema kongamano hilo litaangazia zaidi namna bora na ufanisi ya kutekeleza mageuzi ya elimu nchini.

Awali akitoa Taarifa kuhusu Kongamano hilo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. William Anangisye amesema malengo ya kongamano hilo ni kutafakari na kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa wadau mbalimbali kuhusu sera ya sasa ya elimu na mafunzo na marekebisho ya mitaala na athari zake kwa maendeleo endelevu.

Pia, amesema lengo lingine ni kuibua mijadala ya kitaaluma kuhusu mitaala ya elimu ya msingi, sekondari na elimu ya juu, kutafakari juu ya maendeleo ya kitaaluma na nafasi ya elimu ya ualimu kulingana na maboresho ya sera ya elimu na mafunzo, kubadilishana uzoefu wa kimataifa na kikanda jinsi maboresho ya elimu yanavyoweza kuchangia ukuaji jumuishi na mustakbali wa maendeleo endelevu.

Maboresho yaliyofanywa na serikali kwenye baadhi ya maeneo ya Sera ya Elimu na Mafunzo, yamefanyika ili kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili elimu ya Tanzania, zikiwemo, kujikita zaidi kwenye elimu ya nadharia badala ya vitendo na pia, kutokuwepo kwa fursa za elimu na mafunzo zinazozingatia mahitaji ya soko la ajira. Vilevile, mapungufu katika njia za ujifunzaji ambazo hazikukidhi hali halisi ya mazingira na maadili ya Kitanzania.







KONGOLE NECTA KWA MPANGO WA KUPANDA MITI 150,000 KUTUNZA MAZINGIRA

March 25, 2026 Add Comment

 


Na: Dk. Reubeni Lumbagala

Utunzaji wa Mazingira ni jukumu letu sote. Uwe mtoto, kijana, mtu mzima au mzee. Uwe mwanamke au mwanamme, uwe msomi au usiwe msomi, suala la utunzaji mazingira linakuhusu. Faida za utunzaji mazingira zinatunufaisha sote. Madhara ya uharibifu mazingira yanatuathiri sote. Hakuna aliye salama mazingira yakiharibika. Ndiyo maana ni vyema mikakati ya utunzaji mazingira ikafanyika mapema.

Dunia kwa sasa inakabiliwa na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi. Kutokana na changamoto hiyo, mikakati inawekwa ya namna bora ya kukabiliana na changamoto hiyo ili kuifanya dunia kuwa mahali salama pa kuishi na kufurahia maisha. Tanzania kwa kuwa si kisiwa, tumeathirika pia na mabadiliko ya tabianchi kama zilivyo nchi nyingine. Serikali imechukua hatua kadhaa ikiwemo suala la kuhamasisha watu binafsi, taasisi, makampuni na wizara kupanda miti ili kupunguza athari.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amekuwa mfano mzuri wa kuigwa kuanzia kuhamasisha watu kupanda miti hadi kufanya kwa vitendo yeye mwenyewe kupanda miti. Tangu akiwa Makamu wa Rais, Dk. Samia kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira hadi sasa amekuwa Rais kamili, anaendelea kuhimiza sana utunzaji mazingira na kupanda miti kwa maendeleo. 

Hata katika kuadhimisha Siku yake ya kuzaliwa (Birthday) Januari 27, 2026, Rais Samia aliitumia siku hiyo kupanda miti. "Sisi tulirithi uoto wa asili mwingi sana, tulirithi nchi yetu ambayo haikuwa imeharibika kiasi hiki. 

Tulirithi miti mingi ya matunda iliyopandwa shambani na mingine kujiotea. Lakini leo mtoto wetu akitaka kula pera lazima akalinunue sokoni. Sisi tulikuwa tunapita msituni na kula mapera ya aina yoyote tunayotaka," amesema Rais Dk. Samia.

Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) kama taasisi ya elimu iliyo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, nayo imeunga mkono juhudi za kutunza mazingira kwa kuweka mpango wa kupanda miti ipatayo 150,000 katika taasisi mbalimbali za elimu kama shule za msingi, sekondari na vyuo vya ualimu nchi nzima. 

Machi 18, 2026, Katibu Mtendaji wa NECTA, Prof. Said Mohamed, alizindua zoezi la kitaifa la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Makutupora ya Jijini Dodoma ambapo katika shule hiyo, miti 600 imepandwa kufuatia agizo ya Rais Dk.Samia kwa NECTA katika maadhimisho ya miaka 50 ya NECTA. Prof Said amesema "Desemba 16, 2023, Rais Dk. Samia alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka miaka 50 ya NECTA alitupa maagizo ya kupanda miti kwa sababu sisi ni watumiaji wa karatasi ambazo zinazalishwa na miti, hivyo tunapanda miti kuunga mkono jitihada za utunzaji mazingira."

Mkakati wa NECTA wa kupanda miti 150,000 katika taasisi mbalimbali za elimu utachangia kwa kiasi kikubwa jitihada za kuiokoa nchi yetu na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Lakini pia miti hiyo itasaidia kupendezesha mandhari za shule na vyuo na kufanya sehemu hizo kuwa vutivu kwa ufundishaji na ujifunzaji wa maarifa, stadi na ujuzi. 

Hakika nawapa kongole NECTA kwa kuratibu mkakati huu mzuri wa kupanda miti katika taasisi za elimu. Kwa mwaka 2023/2024, NECTA walipanda miti 82,676, mwaka 2024/2025 walipanda miti 110,400 na kwa mwaka 2025/2026, lengo ni kupanda miti 150,000. Muhimu ni wanufaika wa shule zitakazopata miche ya miti, kuitunza kikamilifu miti hiyo kwa manufaa endelevu.

Maoni 0620 800 462.






HESLB INAVYOSHIRIKIANA NA WADAU KUWAWEZESHA WANAFUNZI KUJITEGEMEA KIUCHUMI

February 23, 2026 Add Comment

 Na: Dk. Reubeni Lumbagala, Tanga



Elimu ni haki muhimu ya binadamu. Elimu ni nyenzo muhimu ya kumsaidia binadamu kumudu maisha yake. Kwa kutambua hilo, ndiyo maana wazazi na walezi wanapambana sana kusomesha watoto na vijana wao ili kuwawezesha kupata elimu bora ya kuwasaidia katika maisha yao na kutimiza ndoto zao za kimaendeleo walizonazo.

Kazi kubwa na nzuri zimefanyika nchini katika kuboresha sekta ya elimu katika ngazi zote za elimu kuanzia elimu ya awali, msingi, sekondari, vyuo vya kati na vyuo vikuu Ili watoto na vijana wa Kitanzania waweze kupata elimu bora ya kuwasaidia maishani mwao. Mitaala ya ujifunzaji imeboreshwa ili kuwajengea wanafunzi umahiri wa kujitegemea pindi wanapohitimu ngazi mbalimbali za masomo yao.

Ikumbukwe kuwa mabadiliko haya mazuri ya mitaala yamekuja kipindi hiki ambacho wahitimu wengi wana changamoto ya kukosa stadi na ujuzi stahiki wa kuwawezesha kuajiriwa au kujiajiri katika sekta mbalimbali. Ndiyo maana wengi tunapongeza mabadiliko haya ya mitaala kwa ustawi mwema wa wahitimu. Katika elimu ya juu, serikali kupitia Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) inaratibu zoezi la utoaji mikopo kwa wanafunzi huku wanufaika wa mikopo hiyo wakiwajibika kuirejesha mikopo hiyo baada ya kuhitimu na kuwa na kipato katika sekta rasmi au isiyo rasmi.

Kwa kutambua changamoto iliyopo kwa baadhi ya wahitimu kukosa ujuzi na stadi mbalimbali, HESLB inashirikiana na taasisi mbalimbali zikiwemo taasisi ya kifedha katika kuhakikisha wanawajengea uwezo wahitimu ili waweze kuajiriwa au kujiajiri ambapo kufanikiwa kwao kunaiwezesha HESLB kukusanya fedha kutoka kwa wahitimu hao lakini pia nchi kupata wataalamu kwa maendeleo.

Mathalani, Februari 18, 2026, katika Ofisi za CRDB Makao Makuu Jijini Dar es Salaam, HESLB iliingia makubaliano ya kushirikiana na CRDB Bank Foundation na kampuni ya Basil Link ili kuwawezesha wanafunzi wa vyuo vikuu kupata ujuzi wa kidigitali, elimu ya ujasiriamali na elimu ya fedha.

Kwa hakika makubaliano haya ni mwelekeo mzuri katika kuwaandaa wanafunzi wa vyuo vikuu kujitegemea kutokana na mafunzo muhimu watakayoyapata kupitia uwezeshaji utakaofanywa hasa katika kuwa na jicho la kuona fursa za kiuchumi zilizopo.

Kupitia programu hiyo lijulikanalo kwa jina la "Imbeju - SmartElite," wanafunzi wa vyuo watapata mafunzo ya ujasiriamali ili kuweza kujiajiri wenyewe. Aidha, watapata pia elimu ya fedha ambayo ni muhimu sana katika ulimwengu huu wa sasa. Sanjari na hilo, wanafunzi watapata mikopo nafuu na ushauri elekezi wa namna bora ya kuwekeza mikopo hiyo ili ilete tija kiuchumi.

Katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Foundation, Tully Mwambapa alisema "Tunataka kuona vijana wanachangamkia fursa, wanabuni, wanaanzisha biashara na hata kuajiri wengine. Hii si tu kuwasaidia kumaliza chuo, bali kuwaandaa kuingia katika uchumi wa kidigitali wakiwa tayari na ujuzi pamoja na raslimali."

Kwa upande wa Dk. Peter Mmari ambaye ni Mkurugenzi na Upangaji Mikopo wa HESLB amesema "Kupitia mpango huu, wanafunzi wataongeza uwezo wa kutumia mifumo ya kidijitali na watapata fursa ya kujiajiri wakiwa vyuoni au baada ya kuhitimu. Tunaamini wataweza pia kutoa mchango katika kuwainua Watanzania wengine kielimu na kiuchumi."

Kimsingi, vijana wenye vipaji na mawazo bunifu watanufaika na mpango huu huku wakiwezeshwa mitaji na vitendea kazi kama kompyuta. Kwa hakika programu ya Imbeju - Smart Elite, ni mkombozi kwa vijana hasa katika ulimwengu wa uchumi wa kidijitali na biashara.












MBUNGE MAKUBEL AANZA NA ELIMU AGAWA MADAFTARI SHULE ZA MSINGI KUUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI

February 19, 2026 Add Comment


Na Oscar Assenga, TANGA

MBUNGE wa Jimbo la Tanga (CCM) Kassim Amar Makubel ameanza kugawa madaftari kwa wanafunzi wa shule za Msingi ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuinua sekta ya elimu hapa nchini.

Makubel aliyasema hayo wakati wa halfa ya kuzindua zoezi la kugawa Madaftari kwa wanafunzi wa Shule za Msingi Pongwe kupitia Mpango wa Daftari la Mama Samia kwa kushirikiana na Taasisi ya Watoto Foundation ambapo mpango huo utazifikia shule zote kwenye Jimbo hilo.

Mbunge huyo alisema kwamba mpango huo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali na Rais Dkt Samia Suluhu katika sekta ya elimu kutokana na mabadiliko na mageuzi makubwa yaliyofanyika.

Alisema kwamba wakati alipoingia madarakani alikaa na kubaini vijana wengi wa shule ya msingi wanapitia changamoto nyingi hivyo akaona ni bora kila kila mzazi wa mtoto wa Jimbo hilo anayesoma shule ya msingi walau aguse maisha yake kwa kutoa madaftari matano 5 ili kuwapunguzia makali kwenye baadhi ya mahitaji.


Alieleza madaftari hayo ni sehemu ya mchango wake kurejesha shukrani kwa kumchagua katika uchaguzi mkuu uliopita na wameanza rasmi uzinduzi ambapo wataanza kugawa madaftari hayo Tarafa ya Pongwe na kasha kuelekea kwenye kata nyengine.

Aidha alisema kwamba Tarafa hiyo inayojumuisha Kata za Marungu,Kirare na Pongwe na baadae wataenda kwenye Tarafa nyengine ili kuhakikisha shule zote za misngi zinafikiwa na kuwagusa.



Alisema keamba mabadiliko hayo yaliyofanywa na Rais Dkt Samia Suluhu katika sekta ya elimu wakati alipoingia madarakani ni kuona elimu walionayo haikizi mahitaji ya sasa na wanatakiwa kuendana na mabadiliko kwenye mitaa ya elimu ya sasa na sasa watoto watasoma darasa la kwanza mpaka la sita.



Aidha alisema mabadiliko hayo machache ikiwemo mkondo wa amali ambao ni muhimu kwa ajili ya kuwapatia ujuzi watoto wanapomaliza shule jambo ambalo litasaidia kuongeza wataalamu mbalimbali ambao watakuwa na mchango mkubwa wa kuweza kujiajiri na kuweza kujiendeleza kwenye vyuo vya kati

“Kutokana na mabadiliko hayo makubwa ya kielimu hapa nchi na hakuna malipo hivyo tuwahimize watoto waende shule pamoja na kufuatilia maendeleo yao na tuhudhurie vikao”Alisema .



Awali akizungumza Mwalimu Mkuu Msaidizi wa shule ya Pongwe Mchanganyiko Abubakari Sadik alimshukuru Mbunge huyo kwa kuwapelekea msaada huo madaftari ambayo yamekuja kutatua changamoto ya watoto ambao hawana uwezo wa kununua madaftari kwa wakati .

"Ukosefu wa daftari ni kwamba wanafunzi asipokuwa na madaftari anakosa kumbukumbu ya kusoma kipindi anapofikia kwenye mtihani yake hivyo msaada huu umeenda kutatua changamoto ya kila mmoja kutokana na wazazi wa watoto wengine wako mbali na inakuwa vigumu kuwa na madaftari kila wakati”Alisema

Alisema kwamba shule hiyo imekuwa ikifanya vizuri katika taaluma na wamekuwa na mwendelezo mzuri wa wanafunzi katika madarasa ya mitihani ya darasa la nne.

Aliongeza kwamba changamoto ambazo zinawakabili ni upungufu wa madarasa unaotokana na ongezeo la uandikishaji wanafunzi kila mwaka na wale wanaohamia kutoka maeneo mengine huku akieleza jambo linguine ni bima za afya kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu.

“Tunamshukuru Mhe Mbunge Wetu kwa kutupelekea wadau wenye kuwasaidia madaftar mchango huo umewapa faraja kubwa na matumaini motisha mpya kwa watoto wao kuonyesha dhamira ya kweli kujenga jamii inayojali na kuthamini kila mtoto bila ubaguzi”Alisema

Hata hiyo alitoa shukrani zake kwa Rais Dkt Samia Suluhu katika kukuza na kutoa kipaumbeme kwenye elimu jumuishi na kupitia uongozi wake fursa za elimu zinaendelelea kuimarishwa na kuwafikia hata wenye mahitaji maalumu.

Naye kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya Watoto Foundation Ally Yakub Pingizi alisema taasisi hiyo imezindua mpango unaoitwa Daftari la Mama Soma na Samia ikiwa ni kipaumbele kuhakikisha wanafunzi hawana sababu ya kutoroka shule ikiwa hana vitendea kazi cha shule.

Alisema kwamba wao wamekuja na mpango wa daftari la mama soma na samia ikiwa ni kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais Dkt Samia Suluhu katika kuboresha sekta ta elimu na amefanya maboresho makubwa kwa kujenga miundombinu ya elimu, nyumba za walimu,mabweni na vyoo.


Alisema kwamba taasisi hiyo kupitia mpango huo wameona wao waunge mkono kwa kutoa vifaa hivyo vitendea kazi na kuwatia moyo watoto wa kike waweze kusoma kwa hari na moyo ili kuepuka kujiingiza kwenye vishawishi na watoto wa kike na hivyo kusoma kwa bidii pamoja na kupunguza utoro shuleni hatua itakayochochea ufaulu.
 






WAZIRI MKUU AZINDUA UJENZI WA CHUO KIKUU MZUMBE TANGA

WAZIRI MKUU AZINDUA UJENZI WA CHUO KIKUU MZUMBE TANGA

February 15, 2026 Add Comment


Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, leo tarehe 15 Februari, 2026 akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa miundombinu ya Chuo Kikuu Mzumbe kampasi ya Tanga ambayo hadi kukamilika kwake utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 12. Pembeni yake ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Wanu Hafidh Ameir. PICHA NA OFISI YA WAZIRI MKUU

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, akipanda mti katika eneo la Chuo Kikuu Mzumbe kampasi ya Tanga mara baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Chuo hicho leo tarehe 15 Februari, 2026. PICHA NA OFISI YA WAZIRI MKUU



Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba, akizungumza na wananchi wa Tanga mjini mara baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa miundombinu ya Chuo Kikuu Mzumbe kampasi ya Tanga ambayo hadi kukamilika kwake utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 12 leo tarehe 15 Februari, 2026. PICHA NA OFISI YA WAZIRI MKUU

Muonekano wa Chuo Kikuu Mzumbe kampasi ya Tanga ambayo hadi kukamilika kwake utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 12 ambao umewekwa jiwe la msingi na Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba leo tarehe 15 Februari, 2026.