Showing posts with label elimu. Show all posts
Showing posts with label elimu. Show all posts

UTORO NA VIGODORO VYATAJWA KUCHANGIA UFAULU HAFIFU, POLISI KATA YAISHUKURU TANGAYETU

July 12, 2026 Add Comment


Polisi Kata wa Kata ya Nguvumali, Jiji la Tanga, Inspekta Sharifu Kiswamba, amesema utoro wa wanafunzi na tabia ya kukesha kwenye vigodoro ni miongoni mwa sababu zinazochangia kushuka kwa kiwango cha ufaulu katika shule za sekondari.

Inspekta Kiswamba alitoa kauli hiyo wakati wa mafunzo maalumu ya kuwajengea wanafunzi mbinu za kujifunza kwa ufanisi na kujiandaa vizuri kwa mitihani, yanayoendeshwa na Tanzania Centre for Education (TCE) kwa kushirikiana na Botnar Foundation na Inovex kupitia Mradi wa TangaYetu.


Alisema mradi huo unahusisha shule 10 zilizobainika kuwa na changamoto ya matokeo hafifu ya kitaaluma, ukiwa na lengo la kuwajengea wanafunzi uwezo wa kujifunza kwa ufanisi na kuongeza kiwango cha ufaulu.


"Kama Polisi Kata tunaushukuru Mradi wa TangaYetu pamoja na wadau wake kwa kuanzisha mafunzo haya. Tunaamini yatasaidia kubadilisha mtazamo wa wanafunzi, kuongeza nidhamu na hatimaye kuinua ufaulu katika shule zetu," alisema.


Alieleza kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kushirikiana na viongozi wa kata, walimu na jamii kuhakikisha wanafunzi wanaotoroka masomo wanafuatiliwa na kurejeshwa shuleni ili wasikose haki yao ya elimu.


"Tunatoa onyo kwa wanafunzi wanaotoroka masomo. Tutakaowakuta wakizurura wakati wa vipindi vya masomo watachukuliwa hatua kwa mujibu wa taratibu, ikiwemo kupelekwa ofisini kwa hatua zaidi za kinidhamu," alisema.


Inspekta Kiswamba alisema pia tabia ya wanafunzi kushinda vijiweni na kukesha kwenye vigodoro imeendelea kuwa changamoto inayochangia kuporomoka kwa nidhamu na kuathiri maendeleo yao kitaaluma.


"Hatutavumilia tabia hii. Tutaendelea kufanya doria na kushirikiana na viongozi wa mitaa pamoja na wazazi kuhakikisha wanafunzi wanazingatia masomo na kujiepusha na mazingira yanayoharibu mustakabali wao," alisisitiza.


Aidha, aliwataka wazazi na walezi kutekeleza wajibu wao wa kufuatilia maendeleo ya watoto wao kwa kuhakikisha wanahudhuria masomo, wanapata muda wa kujisomea na kuepuka vitendo vinavyoweza kuhatarisha elimu yao.


Alisema mafanikio ya sekta ya elimu yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya wazazi, walimu, viongozi wa serikali za mitaa, Jeshi la Polisi na wadau wa maendeleo, akieleza kuwa jitihada zinazofanywa na Mradi wa TangaYetu ni sehemu ya suluhisho la changamoto zinazolikabili eneo hilo.


Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Mradi wa TangaYetu za kuboresha matokeo ya kitaaluma katika shule zenye changamoto kwa kuwajengea wanafunzi stadi za kujifunza, nidhamu na maandalizi bora ya mitihani.









MBINU MPYA KUIBUA MATUMAINI YA KUINUA UFAULU WA WANAFUNZI TANGA

July 11, 2026 Add Comment


Wataalamu waanza kuwanoa wanafunzi, walimu na maafisa elimu kukabiliana na matokeo duni ya mitihani


Na Oscar Assenga, Tanga

MATOKEO duni ya mitihani ya Taifa katika baadhi ya shule za sekondari za Serikali jijini Tanga yameibua hatua mpya za kuwanufaisha wanafunzi kupitia mafunzo maalumu yanayolenga kuongeza ufaulu kwa kuwajengea uwezo wa kujifunza kwa ufanisi na kujiandaa vizuri kwa mitihani.

Mafunzo hayo yanatekelezwa na Taasisi ya Tanzania Centre for Education (TCE) kwa kushirikiana na Taasisi ya Botnar foundation na Inovex kupitia mradi wa Tanga Yetu, unaohusisha shule 10 zilizobainika kuwa na changamoto ya matokeo hafifu kwa wanafunzi.

Akizungumza wakati wa kuanza kwa mafunzo hayo katika Shule ya Sekondari Nguvumali, Mkurugenzi Mtendaji wa TCE, Yusuf Ogutu, alisema kuboresha ufaulu ni hatua muhimu ya kuinua ubora wa elimu na kuwawezesha wanafunzi kufikia ndoto zao za kitaaluma na maisha ya baadae.

Alisema wanafunzi wengi hufanya mitihani bila kuelewa kwa kina mfumo wa maswali ya umahiri, uzito wa mada na mbinu sahihi za kujibu, hali inayochangia kushuka kwa matokeo licha ya kufundishwa darasani.

"Ndiyo maana tumeamua kuja na mafunzo haya ili kuwasaidia wanafunzi kujifunza kwa kuelewa, badala ya kukariri. Tunawafundisha namna ya kuchambua muhtasari wa masomo, kutambua mada zinazotiliwa mkazo katika mitihani na kuelewa matumizi ya vitenzi vinavyotumika katika maswali," alisema.

Aliongeza kuwa wanafunzi pia wanapatiwa mbinu za kupanga muda wa kujisomea, namna ya kujiandaa kabla,wakati na baada ya mtihani, jinsi ya kujibu maswali kwa ufanisi na namna ya kujitathmini baada ya kufanya mtihani.

Ogutu alisema mafanikio ya wanafunzi hayawezi kupatikana kwa juhudi za mwanafunzi pekee, bali yanahitaji ushirikiano wa walimu, wazazi, viongozi wa elimu na wadau wa maendeleo.

"Tunataka kujenga utamaduni wa ufaulu. Mwanafunzi akielewa namna ya kujifunza na mwalimu akapata mbinu bora za kumwelekeza, matokeo mazuri yatapatikana," alisema.

Mbali na mafunzo hayo, alisema taasisi hiyo imeanza kufanya utafiti katika shule zote 27 za sekondari za Serikali za Jiji la Tanga ili kubaini sababu zinazochangia kushuka kwa ufaulu katika mitihani ya Kidato cha Pili na Kidato cha Nne.

Alisema matokeo ya utafiti huo yatawezesha wadau wa elimu kuweka mikakati ya muda mrefu ya kuboresha ubora wa elimu na kuongeza kiwango cha ufaulu katika shule za Serikali.

Kwa upande wake, Mratibu wa Elimu Kata ya Nguvumali, Lilian Shetua, alisema mafunzo hayo yanawasaidia wanafunzi kuendana na mahitaji ya mtaala ulioboreshwa unaowataka kuwa wabunifu, wachambuzi na wenye uwezo wa kutumia maarifa katika kutatua changamoto.

Alisema wanafunzi wengi wamekuwa wakifanya mitihani bila kuelewa muundo wake, lakini kupitia mafunzo hayo wanapata uelewa wa namna ya kujiandaa na kujibu maswali kwa kuzingatia matakwa ya Baraza la Mitihani.

"Ni matarajio yetu kwamba elimu hii itabadilisha mtazamo wa wanafunzi na kuongeza kiwango cha ufaulu katika shule yetu na nyingine zinazoshiriki mradi huu," alisema.

Naye Inspekta wa Polisi wa Kata ya Nguvumali, Sharifu Kiswamba, alisema pamoja na jitihada za kuboresha elimu, bado utoro wa wanafunzi na tabia ya kuzurura mitaani wakati wa masomo vinaendelea kuwa kikwazo kikubwa.

Aliwataka wazazi kuongeza usimamizi wa watoto wao na kushirikiana na walimu pamoja na viongozi wa kata ili kuhakikisha wanafunzi wanahudhuria masomo na kutumia muda wao kujifunza.

Kwa upande wake, mwalimu wa Shule ya Sekondari Nguvumali, Venosa Massawe, alisema mafunzo hayo yamekuja wakati mwafaka kwani yanawasaidia walimu na wanafunzi kutafsiri kwa usahihi matakwa ya mtaala ulioboreshwa.

Hata hivyo, alisema mazingira magumu ya maisha ya baadhi ya wanafunzi, ikiwamo umaskini, malezi yasiyo ya karibu na changamoto za lishe, bado ni miongoni mwa sababu zinazochangia kushuka kwa kiwango cha ufaulu.

Alisema ushirikiano wa Serikali, wazazi, walimu na wadau wa maendeleo utaendelea kuwa nguzo muhimu katika kujenga mazingira bora ya kujifunza na kuongeza idadi ya wanafunzi wanaofaulu kwa viwango vya juu katika mitihani ya taifa.


TIRDO YAWAWEZESHA WAJASIRIAMALI KWA TEKNOLOJIA YA KUCHAKATA NGOZI

July 07, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Matumizi ya kemikali katika uchakataji wa ngozi yanatarajiwa kupungua kufuatia ubunifu wa Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) wa kubuni dawa ya asili inayotokana na mimea, teknolojia inayolenga kulinda mazingira, afya za watumiaji na kuongeza ushindani wa bidhaa za ngozi za Tanzania katika masoko ya ndani na kimataifa.

MAKAMU WA RAIS AFUNGUA KONGAMANO LA KIMATAIFA LA ELIMU

March 25, 2026 Add Comment

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala linahitaji ushirikiano wa hali ya juu miongoni mwa wadau wote wa elimu, taasisi za serikali na zile zisizo za serikali, wazazi na jamii yote kwa ujumla


Makamu wa Rais amesema hayo, wakati akifungua Kongamano la Kimataifa kuhusu maboresho ya sera ya elimu na mitaala nchini, linalofanyika katika Ukumbi wa Maktaba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Jijini Dar es Salaam. Ameitaka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kushirikiana na Taasisi za elimu, hususan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuendelea kufanya ufuatiliaji na tafiti ili kubaini dosari zozote zinazoweza kukwamisha utekelezaji wa suala hilo ili kubaini na kuibua maeneo yanayohitaji maboresho zaidi kiutendaji.

Makamu wa Rais, amesema suala la utekelezaji wa mabadiliko na maboresho yaliyofanyika kwenye Sera yetu ya Elimu na Mafunzo, na Mitaala kuanzia Elimu ya Awali, Msingi, Sekondari hadi Elimu ya Juu. linataka Watanzania wote kutafsiri vema maono ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan juu ya mfumo wa elimu unaozingatia kutoa ujuzi na maarifa ili kumwezesha mhitimu kumudu mazingira yake, na kumudu ushindani kwenye ulimwengu wa kazi.

Aidha, Makamu wa Rais amesema suala la elimu jumuishi inayozingatia usawa ni miongoni mwa vipaumbele, ambapo Serikali imeweka msisitizo katika uwepo wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia pamoja na miundombinu rafiki kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum. Amesema suala hilo linakwenda sambamba na uandaaji wa walimu wenye ujuzi wa elimu maalum ili kufundisha wanafunzi hao.

Kwa upande wake Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda amesema kongamano hilo la kimataifa kuhusu maboresho ya sera na elimu na mitaala ni fursa nzuri ya ushirikishwaji wa watalaam na wachambuzi kuangalia jinsi ambavyo utekelezaji huo unaendelea.

Amesema kongamano hilo litaangazia zaidi namna bora na ufanisi ya kutekeleza mageuzi ya elimu nchini.

Awali akitoa Taarifa kuhusu Kongamano hilo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. William Anangisye amesema malengo ya kongamano hilo ni kutafakari na kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa wadau mbalimbali kuhusu sera ya sasa ya elimu na mafunzo na marekebisho ya mitaala na athari zake kwa maendeleo endelevu.

Pia, amesema lengo lingine ni kuibua mijadala ya kitaaluma kuhusu mitaala ya elimu ya msingi, sekondari na elimu ya juu, kutafakari juu ya maendeleo ya kitaaluma na nafasi ya elimu ya ualimu kulingana na maboresho ya sera ya elimu na mafunzo, kubadilishana uzoefu wa kimataifa na kikanda jinsi maboresho ya elimu yanavyoweza kuchangia ukuaji jumuishi na mustakbali wa maendeleo endelevu.

Maboresho yaliyofanywa na serikali kwenye baadhi ya maeneo ya Sera ya Elimu na Mafunzo, yamefanyika ili kuondoa changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili elimu ya Tanzania, zikiwemo, kujikita zaidi kwenye elimu ya nadharia badala ya vitendo na pia, kutokuwepo kwa fursa za elimu na mafunzo zinazozingatia mahitaji ya soko la ajira. Vilevile, mapungufu katika njia za ujifunzaji ambazo hazikukidhi hali halisi ya mazingira na maadili ya Kitanzania.







KONGOLE NECTA KWA MPANGO WA KUPANDA MITI 150,000 KUTUNZA MAZINGIRA

March 25, 2026 Add Comment

 


Na: Dk. Reubeni Lumbagala

Utunzaji wa Mazingira ni jukumu letu sote. Uwe mtoto, kijana, mtu mzima au mzee. Uwe mwanamke au mwanamme, uwe msomi au usiwe msomi, suala la utunzaji mazingira linakuhusu. Faida za utunzaji mazingira zinatunufaisha sote. Madhara ya uharibifu mazingira yanatuathiri sote. Hakuna aliye salama mazingira yakiharibika. Ndiyo maana ni vyema mikakati ya utunzaji mazingira ikafanyika mapema.

Dunia kwa sasa inakabiliwa na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi. Kutokana na changamoto hiyo, mikakati inawekwa ya namna bora ya kukabiliana na changamoto hiyo ili kuifanya dunia kuwa mahali salama pa kuishi na kufurahia maisha. Tanzania kwa kuwa si kisiwa, tumeathirika pia na mabadiliko ya tabianchi kama zilivyo nchi nyingine. Serikali imechukua hatua kadhaa ikiwemo suala la kuhamasisha watu binafsi, taasisi, makampuni na wizara kupanda miti ili kupunguza athari.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan amekuwa mfano mzuri wa kuigwa kuanzia kuhamasisha watu kupanda miti hadi kufanya kwa vitendo yeye mwenyewe kupanda miti. Tangu akiwa Makamu wa Rais, Dk. Samia kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira hadi sasa amekuwa Rais kamili, anaendelea kuhimiza sana utunzaji mazingira na kupanda miti kwa maendeleo. 

Hata katika kuadhimisha Siku yake ya kuzaliwa (Birthday) Januari 27, 2026, Rais Samia aliitumia siku hiyo kupanda miti. "Sisi tulirithi uoto wa asili mwingi sana, tulirithi nchi yetu ambayo haikuwa imeharibika kiasi hiki. 

Tulirithi miti mingi ya matunda iliyopandwa shambani na mingine kujiotea. Lakini leo mtoto wetu akitaka kula pera lazima akalinunue sokoni. Sisi tulikuwa tunapita msituni na kula mapera ya aina yoyote tunayotaka," amesema Rais Dk. Samia.

Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) kama taasisi ya elimu iliyo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, nayo imeunga mkono juhudi za kutunza mazingira kwa kuweka mpango wa kupanda miti ipatayo 150,000 katika taasisi mbalimbali za elimu kama shule za msingi, sekondari na vyuo vya ualimu nchi nzima. 

Machi 18, 2026, Katibu Mtendaji wa NECTA, Prof. Said Mohamed, alizindua zoezi la kitaifa la upandaji miti katika Shule ya Sekondari Makutupora ya Jijini Dodoma ambapo katika shule hiyo, miti 600 imepandwa kufuatia agizo ya Rais Dk.Samia kwa NECTA katika maadhimisho ya miaka 50 ya NECTA. Prof Said amesema "Desemba 16, 2023, Rais Dk. Samia alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka miaka 50 ya NECTA alitupa maagizo ya kupanda miti kwa sababu sisi ni watumiaji wa karatasi ambazo zinazalishwa na miti, hivyo tunapanda miti kuunga mkono jitihada za utunzaji mazingira."

Mkakati wa NECTA wa kupanda miti 150,000 katika taasisi mbalimbali za elimu utachangia kwa kiasi kikubwa jitihada za kuiokoa nchi yetu na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Lakini pia miti hiyo itasaidia kupendezesha mandhari za shule na vyuo na kufanya sehemu hizo kuwa vutivu kwa ufundishaji na ujifunzaji wa maarifa, stadi na ujuzi. 

Hakika nawapa kongole NECTA kwa kuratibu mkakati huu mzuri wa kupanda miti katika taasisi za elimu. Kwa mwaka 2023/2024, NECTA walipanda miti 82,676, mwaka 2024/2025 walipanda miti 110,400 na kwa mwaka 2025/2026, lengo ni kupanda miti 150,000. Muhimu ni wanufaika wa shule zitakazopata miche ya miti, kuitunza kikamilifu miti hiyo kwa manufaa endelevu.

Maoni 0620 800 462.