Showing posts with label elimu. Show all posts
Showing posts with label elimu. Show all posts

MAENDELEO YA ELIMU NI MKOMBOZI WA TAIFA LOLOTE DUNIANI -MAJALIWA

August 06, 2025 Add Comment


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa maendeleo katika sekta ya elimu ndio mkombozi na mafanikio ya Taifa lolote duniani.

 

Amesema kwa kutambua hilo, uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan uliamua kuwekeza katika sekta hiyo ili kuhakikisha watoto wa kitanzania wanapata elimu bora katika ngazi zote.

 


Amesema hayo wakati alipozungumza na wanafunzi na walimu wa shule ya sekondari ya Wasichana ya Lucas Malia iliyopo Ruangwa mkoani Lindi, wakati wa hafla ya kuwapongeza wanafunzi wa kidato cha sita waliofanya vizuri katika mitihani ya kitaifa iliyofanyika mwaka 2025.

 

“Mliopo shuleni na mnaokuja, tambueni kuwa tuna maeneo muhimu ya kuwaelimisha, mtapata elimu iliyobora na imara itakayowapa maarufa na ujuzi ili muweze kukabiliana na changamoto mbalimbali za kijamii na kiuchumi”

 


Amesema kuwa Serikali ya awamu ya sita imefanya maboresho ya mitaala kwa lengo la kukabiliana na mabadiliko ya kiuchumi yaliyopo duniani ikiwemo mahitaji makubwa ya ajira kwa vijana.

 

“Mabadiliko haya yameifanya mitaala yetu itakayofundishwa shuleni kila mwanafunzi akimaliza ana uwezo wa kutumia mazingira alimo na taaluma aliyonayo kuyabadilisha kuwa uchumi”

 

Akisoma matokeo ya kidato cha sita kwa mwaka 2025, Makamu Mkuu wa Shule Amon Chalamila hiyo amesema kuwa shule hiyo ilisajili wanafunzi 188 ambapo wote walifanya mitihani na wanafunzi 90 walipata daraja la kwanza, wanafunzi 95 walipata daraja la pili, wanafunzi watatu walipata daraja la tatu na hakuna mwanafunzi aliyepata daraja na nne na sifuri. “Ufaulu huu ni sawa na GPA ya 2.34”.

BI.SAKINA MWINYIMKUU: JENGENI UTAMADUNI WA UTENDAJI UNAOTEGEMEA MATOKEO

July 25, 2025 Add Comment


*Dodoma, Julai 25, 2025*  

Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Bi. Sakina Mwinyimkuu, amewataka watumishi wa umma kutumia maarifa waliyopata katika mafunzo ya ufuatiliaji na tathmini ili kuongeza uwajibikaji na ufanisi katika kazi zao.

Akifunga rasmi mafunzo hayo ya siku tano yaliyofanyika jijini Dodoma, Bi. Sakina amesisitiza umuhimu wa kujenga utamaduni wa kazi bora unaozingatia matokeo (results-based performance), kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

> “Mafunzo haya si kwa manufaa yenu binafsi pekee, bali yatumike kama nyenzo ya kuleta mabadiliko chanya katika taasisi zenu, sambamba na kuendeleza maadili ya uwajibikaji,” amesema Bi. Sakina.

Ametoa rai kwa washiriki kuwa mabalozi wa kueneza uelewa huo kwa wengine katika maeneo yao ya kazi, ili kuimarisha utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia viwango vya kitaifa vya ufuatiliaji na tathmini ya maendeleo.





KAMPENI YA "TUWAAMBIE KABLA HAWAJAHARIBIWA" YAENDELEA SEKONDARI ROBANDA ,SERENGETI

July 16, 2025 Add Comment

Katika mwendelezo wa kampeni ya kitaifa ya TUWAAMBIE KABLA HAWAJAHARIBIWA, Sajenti Emmanuel kutoka Jeshi la Polisi, kitengo cha Dawati la Jinsia na Watoto, ametembelea Shule ya Sekondari Robanda iliyopo Kijiji cha Robanda, Kata ya Ikoma, Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, na kufanya mazungumzo ya moja kwa moja na wanafunzi wa kidato cha tano.


Akiwa shuleni hapo, Sajenti Emmanuel amewahimiza wanafunzi hao kujitambua na kuelekeza nguvu zao katika masomo ili kufikia malengo yao ya kitaaluma na maisha kwa ujumla, amesisitiza umuhimu wa kuepuka mahusiano ya kimapenzi wakiwa bado shuleni, akieleza kuwa vitendo hivyo vimekuwa chanzo kikuu cha kukatisha ndoto za wanafunzi wengi nchini.

Aidha, amewataka wanafunzi kuwa mstari wa mbele katika kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa kutoa taarifa mapema kwa mamlaka husika, amebainisha kuwa taarifa zinaweza kutolewa katika ofisi ya Dawati la Jinsia na Watoto iliyo katika kituo cha polisi, kwa Afisa wa Ustawi wa Jamii, au kwa viongozi wa serikali ya kijiji na kata.

Kampeni hiyo inalenga kuwafikia vijana walioko mashuleni na katika jamii kwa ujumla, ikiwa ni jitihada za pamoja kati ya serikali, vyombo vya dola, na wadau wa maendeleo katika kutokomeza matukio ya ukatili wa kijinsia na kusaidia vijana kufikia ndoto zao kwa usalama.

KIKWETE NA MALALA WAONYA: BAJETI ZA ELIMU ZISIPUUZWE WAKATI WA MISUKOSUKO YA KIUCHUMI NA KISIASA DUNIANI

July 15, 2025 Add Comment

 Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai, wameonya juu ya mwenendo hatarishi duniani wa kupunguza au kupuuza bajeti za elimu hasa wakati wa misukosuko ya kiuchumi na kisiasa.


Wakizungumza kwenye mjdala kuhusu elimu uliofanyika Jumapoili usiku katika hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam, viongozi hao wawili waliwataka viongozi wa serikali, wafadhili na washirika wa maendeleo kulinda na kuendeleza uwekezaji kwenye elimu, wakisisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa maendeleo ya kudumu.


“Elimu haipaswi kuwa mhanga wa kwanza wakati wa janga. Si anasa—ni uhai wa maendeleo,” alisema Dkt. Kikwete. “Tukiacha kuwekeza katika elimu leo, tunajitengenezea matatizo makubwa kesho.”


Malala aliongeza kuwa madhara ya kupunguzwa kwa bajeti ya elimu huathiri zaidi wasichana. “Kila matatizo yanapotokea, wasichana ndiyo huathirika kwanza—hutolewa shule, ndoto zao hukatizwa. Hili si tu dhuluma, bali ni upumbavu wa kisera,” alisema.


Katika ziara yao katika Shule ya Sekondari Kibasila siku ya Jumatatu, Dkt. Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya GPE, alitangaza kuwa Tanzania itapokea msaada wa dola milioni 88 za Kimarekani kuanzia mwakani. 


Dkt. Kikwete alisema tangu kujiunga na GPE mwaka 2013, Tanzania imepokea zaidi ya dola milioni 344 zilizowezesha ujenzi wa zaidi ya madarasa 3,000, vyoo 7,600, nyumba za walimu 64, shule mpya 18, vituo vya walimu 252, na usambazaji wa vitabu milioni 36.


Kwa upande wake, Malala alitangaza msaada wa dola milioni 3 kutoka kwenye Malala Fund kusaidia wasichana waliokatishwa masomo kutokana na ujauzito au sababu nyingine za kijamii.


Malala pia alipongeza hatua ya serikali ya Tanzania ya mwaka 2021 ya kuruhusu wasichana waliopata ujauzito kurejea shule. 


“Uamuzi huu ulikuwa wa kishujaa na wa kibinadamu,” alisema. “Wasichana sasa wanaweza kurudi shule ndani ya miaka miwili au kujiunga na vituo vya elimu mbadala.”


Hata hivyo, wote walikiri changamoto bado zipo, na kwamba chini ya asilimia 50 ya wasichana wanaokamilisha shule ya msingi, na ni asilimia 16 pekee wanaoendelea hadi sekondari ya juu, sababu kubwa  zikiwa ni umaskini, mila kandamizi, na uhaba wa miundombinu.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary Kipanga, alieleza kuwa kupitia Mpango wa Samia Scholarship ulioanzishwa 2023, wasichana 1,320 tayari wamenufaika kwa kusomea kozi za sayansi vyuo vikuu.


“Mpango huu pamoja na sera ya re-entry ni silaha muhimu kuhakikisha wasichana hawapotei kwenye mfumo wa elimu,” alisema.


Dkt. Neema Mwakalinga, mchambuzi wa elimu, alisema ushirikiano na GPE na Malala Fund umeinua hadhi ya Tanzania kimataifa. “Sio tu fedha—ni pia ushauri wa kitaalamu, uraghibishaji, na dhamira ya kisiasa ya kweli.”

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary  Kipanga, walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai akivishwa skafu alipowasili kutembelea  shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika moja ya madarasa walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika moja ya madarasa walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai  akiwa na baadhi ya wanafunzi wanamichezo alipotembelea  shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaamsiku ya Jumatatu. 

  

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakimwagilia mti baada ya Malala Kuupanda, walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. Kushoto  ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary Kipanga

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati yeye na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

 Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika mazungumzo ofisini kwa Rais Mstaafu siku ya Jumatatu

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai baada ya mazungumzo ofisini kwa Rais Mstaafu siku ya Jumatatu
Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akimpa zawadi ya kitabu cha  Global Partnership for Education (GPE)  mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai baada ya mazungumzo ofisini kwa Rais Mstaafu siku ya Jumatatu
 

NISHATI SAFI YA KUPIKIA NI AGENDA YA DUNIA,WIZARA INAITEKEKEZA KWA VITENDO - DKT.KAZUNGU

July 04, 2025 Add Comment


*📌Apokea Magari Mawili kutoka Umoja wa Ulaya kwa ajili ya kuanza kampeni ya kutoa elimu ya uhamasishaji wa nishati safi ya kupikia nchi nzima*


*📌 Amshukuru Dkt Samia kwa kuwa kinara wa nishati safi na kuibeba ajenda hiyo*


*📌 Umoja wa Ulaya waridhishwa na jitihada za Tanzania kwenye kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia*


*📌UNCDF yaahidi kushirikiana na Wizara kuhakikisha watanzania wanafikiwa na elimu ya nishati safi*


Naibu katibu Mkuu Wizara ya Nishati anayeshughulikia umeme na nishati Jadidifu, Dkt Khatibu Kazungu leo 04 Julai, 2025 amepokea magari mawili yatakayotumika kwa ajili ya kampeni ya kuhamasisha na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia chini ya kampeni ya nishati safi ya kupikia Okoa Maisha na Mazingira itakayoendeshwa nchi nzima na Wizara ya nishati kwa kushirikiana na UNCDF.

‘’ Ajenda ya Nishati safi ya kupikia ni ajenda ya Dunia na sisi Wizara ya Nishati tuko tayari kwa utekelezaji ili kumuunga mkono Mhe. Rais Samia’’ Amesema Dkt. Kazungu

Aidha, ameishukuru Umoja wa Ulaya, na UNCDF kwa kutekeleza mradi wa nishati safi ya kupikia chini ya mfuko wa Cook fund kwa kuwa umesaidia kubadili maisha na mitazamo ya wananchi kuhusu  utekelezaji wa miradi ya Nishati safi.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo,  Balozi wa Umoja wa Ulaya Mhe. Balozi Christine Grau amesema umoja wa Ulaya uko tayari kuendelea kuisaidia Tanzania kwenye utekelezaji wa Nishati safi ya kupikia na tayari EU imetoa kiasi cha Euro Milioni 19.4 sawa na shilingi Bilioni 59 kutekeleza miradi ya nishati safi ya kupikia kwa mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Pwani, Morogoro  na Mwanza. 

Kuhusu magari amesema magari hayo mawili yana thamani ya Euro 130,000 na amewataka wizara ya Nishati kuhakikisha wananchi wa vijijini wanafikiwa na nishati safi ya kupikia

Tanzania inajipanga kutekeleza kwa vitendo mkakati wa Taifa wa Nishati safi ya kupikia chini ya mkakati wa Mawasiliano wa Taifa ili kutoa elimu kwa wananchi na kufikia lengo la Serikali la asilimia 80 ya watanzania kuanza kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.