Showing posts with label elimu. Show all posts
Showing posts with label elimu. Show all posts

RAIS SAMIA: MAGEUZI YA ELIMU NA SAYANSI KUJENGA UCHUMI ENDELEVU

January 09, 2026 Add Comment


NA EMMANUEL MBATILO, ZANZIBAR

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali imedhamiria kufanya mageuzi makubwa katika sekta za elimu, sayansi, utafiti na ubunifu ili kujenga uchumi imara, shindani na endelevu.

Mhe. Rais ameyasema hayo Januari 8, 2026, Buyu visiwani Zanzibarbaada ya kuzindua Jengo la Taaluma na Utawala la Taasisi ya Sayansi za Bahari Zanzibar (UDSM–IMS), akisisitiza kuwa taasisi hiyo ni mdau muhimu wa Serikali katika kukuza uchumi shirikishi, hususan uchumi wa buluu.

Amesema uwepo wa taasisi hiyo ya kimkakati utaimarisha uvuvi endelevu, utalii wa baharini pamoja na ulinzi na matumizi bora ya rasilimali za bahari.

Mhe. Samia ameipongeza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kusimamia kwa ufanisi Mradi wa HEET, ambao umeleta matokeo chanya katika miundombinu na ubora wa elimu ya juu, huku akiwahimiza vijana kutumia fursa hiyo kusoma na kupata elimu pamoja na ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.

MAHAFALI YA 6 YA LAVENDER DAY CARE CENTER YAFANA KITUNDA MASAI

December 24, 2025 Add Comment

 


Na. Mwandishi Wetu, Dar

Mahafali ya sita (6) kwa Watoto wa darasa la Awali ya Kituo cha Lavender Day Care Center kilichopo Kitunda Masai, yameweza kukonga nyoyo Wazazi na viongozi waliofika kushuhudia tukio hilo la kipekee katika kuhitimisha Wanafunzi hao.




Katika mahafali hayo yaliyofanyika hivi karibuni Disemba 2025, Wahitimu hao wa darasa la awali wameweza kuonesha uwezo wao mkubwa wa yale waliofundishwa darasani kama masomo na michezo mbali mbali.




Awali mgeni rasmi katika mahafali hayo, Mdau wa Elimu Bi. Elly Kitaly ambaye ni Mkurugenzi wa taasisi ya Chadron's Hope Foundation amepongeza uongozi wa shule, Walimu pamoja kwa namna ya kipekee katika kumsaidia Mtoto kitaaluma sambamba na wazazi kwa kuichagua Lavender Day Care tawi la Kitunda Masai.




Amesema uwezo wa watoto hao ni mkubwa hivyo wanatakiwa kuendelea kusimamiwa katika malezi sahihi ya kielimu na kuendelea kujengwa katika mambo mema katika hatua ya Elimu ya Msingi.

Bi.Elly Kitaly amesema kuwa, Elimu ni muhimu lakini pia vitu vingine vya Msingi kabisa vinapaswa kufundishwa Watoto ilikuwajenga zaidi.

"Nimeona kuna watu wana elimu kubwa lakini hawafanyi mambo makubwa.Elimu ni pamoja na mambo ya msingi ni kwa kujifunza Hutu, kujifunza kuwa mkweli na kujifunza kusimama kwenye haki." Amesema Bi. Elly Kitaly.

Aidha, katika risala ya Kituo hicho, juu ya kuongeza majengo mengine, Bi. Elly Kitaly amesema kuwa anaamini Wazazi wanaweza kuchangia chochote ilikufanikisha ujenzi huo kwani itasaidia maendeleo ya watoto wengi.

"Nimesikia tunataka kujenga majengo mengine, moja ya changamoto ya kuendeshea shughuli kama hizi za taasisi za shule ni suala la kifedha, na nafahamu pesa ni changamoto hivyo tuungane kusaidia kituo cha Levender ili kiendelee kusaidia watoto wetu, Mimi na wewe tuungane tukatoa kilichopo mifuko ya cement, au matofali au hata kuchangia elfu moja (Tsh 1,000) inaweza kubadilisha mazingira ya Lavender.

Ameongeza "Utakuja hapa utakuta mazingira safi yame boreshwa, madarasa yame ongezeka, sehemu ya michezo ya watoto imeboreshwa hata utakuta na eneo la kuogelea (swimming pool) ya watoto.

Aidha amesema kuwa, 

Elimu ni muhimu, lakini pia lazima tujifunze mengine kama fani ya muziki, kuogelea na mengine katika vipaji ili kukabiliana na soko la ajira.

"Nimeona watoto wamefanya mambo makubwa hapa, niwapongeze Uongozi wa Lavender, na Walimu kwa kuwalea vyema watoto hawa, na wakawe mfano huko katika ngazi inayofuata.

Nae Mkurugenzi wa kituo cha Lavender Day Care, Bi.Vida Andrew Ngowi amewashukuru Wazazi na Walezi kwa kuendelea kuwaunga mkono na kwa sasa wanaendelea kuongeza majengo mengine ya Kituo hicho cha eneo la Kitunda Masai.

Aidha, kupitia risala ya msimamizi wa kituo hicho, amesema Lavender Day Care Center kilichopo Kitunda Masai ilianzishwa mwaka 2019 kwa lengo la kutoa huduma bora ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya watoto. 

"Kituo kilianza na watoto wachache mwaka 2019 na hadi kufikia sasa tuna watoto wengi, tuna washukuru Wazazi na Walezi kutukimbilia Lavender kwa hapa eneo la Kitunda Masai, kwani kituo chetu "Mtoto ndiye kiini cha ujifunzaji ", lakini pia falsafa yetu kuu inasema"Tunajifunza kupitia michezo".

Kituo cha Lavender pia kina tawi katika eneo la Bunju A ambacho nacho kinafanya vizuri sana ikiwemo watoto wanajifunza kifaransa, kuogolea na muziki kama chaguo kwa wale wanaopenda. 












MUONEKANO WA MAJENGO YA KAMPASI YA LINDI YA UDSM AMBAYO WAZIRI MKUU DKT MWIGULU ALIWEKA JIWE LA MSINGI JUMAMOSI DISEMBA 20, 2025

December 22, 2025 Add Comment




Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kampasi ya Lindi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), katika hafla iliyofanyika eneo la Ngongo, Manispaa ya Lindi.

Ujenzi wa kampasi hiyo, ambayo majengo yake ni hayo pichani, unatekelezwa kwa mkopo wa masharti nafuu kutoka Benki ya Dunia kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), ukiwa na lengo la kusogeza elimu ya juu karibu na wananchi na kuimarisha mchango wa elimu katika maendeleo ya taifa.

Kwa mujibu wa UDSM, bajeti ya mradi ni Shilingi bilioni 14.8, ikihusisha ujenzi wa jengo la utawala na taaluma lenye madarasa sita yatakayohudumia wanafunzi 360, karakana ya kilimo, maabara yenye uwezo wa wanafunzi 125, mabweni mawili kwa wanafunzi 200, pamoja na Kituo cha Utafiti cha Ruangwa chenye uwezo wa kuhudumia wanafunzi 50.

Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi Shandong Hi-Speed Dejian Group Ltd chini ya usimamizi wa Geometry Consultants Limited, ambapo utekelezaji umefikia asilimia 60.

Kampasi ya Lindi inatarajiwa kutoa programu za uzamili, shahada, stashahada na vyeti, hususan katika sekta za kilimo, ufugaji, ufugaji wa nyuki na teknolojia ya chakula, na kuchochea ajira, tafiti bunifu na maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Ukanda wa Kusini.







DKT. MWIGULU AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA KAMPASI YA LINDI YA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM

December 21, 2025 Add Comment

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba akiweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kampasi ya Lindi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika eneo la Ngongo mkoani Lindi na kusema kwamba huo ni uthibitisho wa dhamira ya Serikali ya kupanua fursa za elimu ya juu nchini. Pamoja naye ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wa UDSM

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba akipata maelezo baada ya kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kampasi ya Lindi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika eneo la Ngongo mkoani Lindi na kusema kwamba huo ni uthibitisho wa dhamira ya Serikali ya kupanua fursa za elimu ya juu nchini. Pamoja naye ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam Rais Mstaafu Dkt Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wa UDSM


WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Kampasi ya Lindi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika eneo la Ngongo mkoani Lindi na kusema kwamba huo ni uthibitisho wa dhamira ya Serikali ya kupanua fursa za elimu ya juu nchini.

“Uwekezaji huu ni utekelezaji wa vitendo wa nguzo ya pili ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 katika kujenga uwezo wa watu kifikra, kiubunifu, kufanya uchambuzi, kutatua changamoto, pamoja na kuwa na utaalamu na umahiri katika nyanja mbalimbali za maisha,” amesema.

Akizungumza na viongozi na mamia ya wananchi wa mkoa wa Lindi waliofika kushuhudia uzinduzi huo leo (Jumamosi, Desemba 20, 2025), Waziri Mkuu amewapongeza viongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kuamua kutekeleza maono ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kupanua huduma za elimu ya juu katika maeneo ya kimkakati kama vile Mkoa wa Lindi.

“Maono haya ni ya kwake mwenyewe Mheshimiwa Rais. Zilipotolewa fedha za mradi huu kwa vyuo vikuu kama vya Dar es Salaam na Mzumbe, alisema ujenzi uelekezwe katika kupeleka kampasi za vyuo vikuu kwenye mikoa yote ambayo haikuwa na vyuo vikuu.”

Amesema Mkoa wa Lindi, kama ilivyo kwa mikoa mingine ya Kusini mwa Tanzania una ardhi yenye rutuba, rasilimali watu na mazingira rafiki kwa kilimo cha kisasa na biashara ya mazao.

“Kampasi hii ya kilimo itasogeza huduma ya elimu karibu na wananchi wa Kanda ya Kusini na kuendeleza utafiti na ubunifu katika sekta ya kilimo ambayo ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wa Taifa letu. Uwekezaji huu utachangia kwa kiasi kikubwa katika kuimarisha sekta ya kilimo kupitia maarifa, teknolojia na tafiti za kisasa zitakazojibu changamoto halisi za wakulima wetu,” amesisitiza.

Dkt. Mwigulu amesema ujenzi wa Kampasi ya Kilimo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mkoani Lindi ni ushahidi mwingine wa dhamira ya dhati ya Serikali ya kuifanya elimu ya juu kuwa chombo cha mageuzi ya kiuchumi na kijamii. “Kupitia Kampasi hii, Serikali inalenga kuandaa wataalamu wabobezi wa kilimo, utafiti na biashara ya kilimo watakaosaidia kuongeza uzalishaji, thamani ya mazao, ajira kwa vijana na mapato ya wakulima.”

Sambamba na ujenzi wa chuo hicho, Waziri Mkuu amesema katika kipindi cha miaka mitano ijayo ya utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2025, Serikali itahakikisha inafanya ukarabati wa barabara katika maeneo ya Nane Nane (Ngongo), ujenzi wa barabara zenye urefu wa km. sita kwa kiwango cha lami katika Kampasi za Chuo Kikuu (Ngongo na Ruangwa); ujenzi wa barabara za lami za Kilambo (km 1.5); Mtange – Kinengene - Kibaoni na barabara ya Mahakama – Mitwero (km 1.2).

Mapema, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Rais mstaafu, Dkt. Jakaya Kikwete alimpongeza Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba kwa sababu yeye ni zao la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. “Shahada zako zote tatu umezipatia pale chuo kikuu. Tunajivunia kwani wewe ni miongoni mwa mabalozi wema wa chuo chetu,” alisema.

Akielezea uwekaji wa jiwe la msingi la Kampasi ya Lindi, Dkt. Kikwete alisema anaamini iko siku kampasi ya Lindi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nayo pia itakuwa chuo kikuu kamili.

Alisema chuo hicho kinatarajiwa kuanza kupokea wanafunzi wa kwanza ifikapo Oktoba, mwakani. “Mwaka ujao wa masomo utakaoanza Oktoba, 2026 Chuo Kikuu cha Dar es Salaam - Kampasi ya Lindi kitapokea wanafunzi wa kwanza; vivyo hivyo kwa kampasi za Bukoba na kule Zanzibar,” alisema.

Alitumia fursa hiyo kumshukuru Waziri Mkuu mstaafu, Kassim Majaliwa kwa kusaidia upatikanaji wa ardhi wilayani Ruangwa ambako Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kimejenga tayari kituo cha utafiti wa kilimo.

Naye, Naibu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam anayesimamia Fedha, Utawala na Mipango, Prof. Bernadeta Killian alisema ujenzi wa chuo hicho unafuata masterplan ya miaka 20 (2025-2045) kutegemea na uwezo wa Serikali na uwepo wa bajeti. “Mradi wote utagharimu sh. bilioni 14.8 na kati ya hizo, sh. bilioni 13.7 ni za mkandarasi ambaye tayari amelipwa sh. bilioni 5.9. Shilingi bilioni moja ni za kumlipa mshauri mwelekezi.”

Akitoa maelezo ya ujenzi huo mbele ya Waziri Mkuu, Prof. Killian ambaye pia ni msimamizi wa mradi wa kuendeleza elimu ya juu kwa mageuzi ya kiuchumi (HEET) alisema majengo mengi yanaendelea yakiwemo ya utawala, vyumba vya mikutano, madarasa sita yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 60 kila moja, karakana ya mafunzo na maabara yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 125 kwa wakati mmoja.

Alisema kampasi hiyo pia ina mabweni mawili yenye uwezo wa kuchukua wanafunzi 200 lakini kuna nafasi ya kuongeza ghorofa tatu kila moja na hivyo kuweza kuchukua wanafunzi 800.

NAIBU WAZIRI WANU ATAKA KASI IONGEZWE UJENZI WA MRADI WA EASTRIP DIT MWANZA

NAIBU WAZIRI WANU ATAKA KASI IONGEZWE UJENZI WA MRADI WA EASTRIP DIT MWANZA

December 15, 2025 Add Comment

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Hafidh Ameir, amemtaka Mkandarasi wa COMFIX & ENGINEERING kuongeza kasi ya ujenzi wa miundombinu ya Mradi wa Kujenga Ujuzi na Ushirikiano Afika Mashariki (EASTRIP ) katika Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) Kampasi ya Mwanza, ili ikamilike kwa wakati kulingana na maktaba.

Naibu Waziri huyo, ametoa maagizo hayo jijini Mwanza wakati akikagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo. Pia amewataka wazabuni wote kuhakikisha vifaa na mitambo vinawasili na kufungwa kwa wakati ili kuwezesha utoaji wa mafunzo kwa wakati.

Mhe. Wanu Ameir amesema ucheleweshaji wa ujenzi unaweza kuathiri malengo ya Serikali ya kuhakikisha vijana wanapata ujuzi na umahiri unaohitajika katika soko la ajira la ndani na kimataifa, kama alivyoelekeza Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Ameir amewahakikishia wananchi na uongozi wa DIT kuwa Serikali itaendelea kuimarisha uwezo wa kampasi hiyo, ikiwemo kuongeza udahili wa wanafunzi kutoka 358 wa sasa hadi 2,000

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, amesema kuwa katika Kampasi ya DIT Mwanza kinajengwa Kituo cha Kikanda cha Umahiri cha uchakataji na utengenezaji wa bidhaa za Ngozi ambacho kinatekelezwa kupitia Mradi wa EASTRIP. Amesema kuwa ujenzi huo unahusisha majengo matano ambayo ni jengo la kufundishia, jengo la taaluma, hosteli mbili na karakana ya kisasa kwa ajili ya mafunzo ya utengenezaji wa bidhaa za ngozi.

Prof. Mushi ameongeza kuwa ujenzi wa majengo hayo unatekelezwa na Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia ambayo imetoa mkopo wa riba nafuu kufanikisha mradi huo. Ambapo gharama za utekelezaji wa mradi DIT Mwanza ni shilingi bilioni 37.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Teknolojia ya Dar Es Salaam (DIT) Kampasi ya MWANZA Dkt. John Msumba amesema kuwa Kampasi hiyo imefufua Sekta ambayo ilikuwa imekufa nchini kutokana na kukosekana Kwa wataalamu na kwamba Viwanda Kwa sasa vinapata wataalamu tofauti na awali ambapo walikuwa wakilazimika kuwatoa nje ya nchi.