Showing posts with label elimu. Show all posts
Showing posts with label elimu. Show all posts
SERIKALI YAPANIA KUANDAA WALIMU USHIRIKIANO WA ATE NA WIZARA WAZAA MATUNDA KWA WATAFUTA AJIRA

SERIKALI YAPANIA KUANDAA WALIMU USHIRIKIANO WA ATE NA WIZARA WAZAA MATUNDA KWA WATAFUTA AJIRA

September 25, 2025 Add Comment

 

KATIKA  kuhakikisha mafunzo ya darasani yanaendana na mahitaji halisi ya soko la ajira, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Carolyne Nombo, amekutana na Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Bi. Suzzane Ndomba, kwa mazungumzo ya namna ya kuwawezesha vijana wahitimu kupata mafunzo ya vitendo sehemu za kazi.

Mkutano huo umefanyika  katika ofisi za ATE jijini Dar es Salaam, ambapo Prof. Nombo alisema Serikali imefanya mapitio ya Sera ya Elimu na kuboresha mitaala ya ngazi zote ili vijana wapate ujuzi unaowawezesha kujiajiri au kuajiriwa.

Aidha, Prof. Nombo alisisitiza kuwa Serikali inaendelea kutoa mafunzo kwa walimu walioko kazini ili kuboresha mbinu za ufundishaji, akieleza kuwa ufundishaji bora ndio msingi wa kuwajengea wanafunzi ujuzi wa maisha na ajira.

“Lengo la ziara hii ni kujadiliana na ATE kuhusu njia bora za kuwashirikisha waajiri katika kusaidia vijana waliopo vyuoni au waliomaliza masomo kupata mafunzo ya vitendo sehemu za kazi,” alisema Prof. Nombo.

Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Bi. Suzzane Ndomba, alisema ATE imekuwa ikisaidia wanafunzi kupata mafunzo kwa vitendo kupitia wanachama wake, wakiwemo viwanda na makampuni. Alitolea mfano wa Mradi wa Kukuza Ujuzi wa Vijana unaotekelezwa na ATE, uliowawezesha zaidi ya vijana 1,000 waliomaliza kidato cha nne kupata mafunzo ya miezi sita katika vyuo vya ufundi kabla ya kupelekwa makampuni kwa mafunzo ya vitendo, ambapo baadhi yao walipata ajira.

Aidha, alitoa wito kwa Watanzania kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kujifunza ujuzi kwa gharama nafuu bila kujali kiwango cha elimu rasmi walichonacho.

Mazungumzo hayo yameonesha dhamira ya pamoja ya Serikali na sekta binafsi katika kuimarisha ujuzi wa vijana na kuandaa nguvu kazi yenye mchango katika maendeleo ya taifa.

TUME YA HAKI ZA BINADAMU YAENDESHA MAFUNZO YA HAKI ZA BINADAMU NA WAJIBU WA ASKARI WAKATI WA UCHAGUZI MKUU

September 19, 2025 Add Comment



Tume ya Haki za Binadamu imeendesha mafunzo ya haki ya binadamu na wajibu wa Askari Polisi wakati wa uchaguzi kwa askari Polisi ngazi ya kata wilaya ya Tanga. 

Mafunzo hayo  yamefanyika katika Ukumbi wa mikutano wa jiji la Tanga leo Septemba19, 2025 ikiwa ni sehemu ya kuwakumbusha  askari hao  kuhusu umuhimu wa kufuata sheria, kanuni na misingi ya haki za binadamu katika utekelezaji wa majukumu yao, hususan kuelekea kipindi cha Uchaguzi Mkuu.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufungua mkutano wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Idara ya Elimu kwa Umma, Mawasiliano, Utafiti na Nyaraka wa Tume ya Haki za Binadamu, Bi Monica Mnanka, kwa niaba ya Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu,.

Amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwakumbusha  Askari Polisi umuhimu wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia haki za binadamu ili kutoa fursa kwa wananchi kutumia haki yao ya kikatiba kuchagua viongozi wanaowataka.

Nao baadhi ya askari wa Jeshi la Polisi mkoani Tanga waliopata nafasi ya kuhudhuria mafunzo hayo wamesema mafunzo hayo  yatakuwa msaada mkubwa kwao katika kutoa elimu kwa wananchi kuelekea kipindi hiki cha uchaguzi.




Tume ya Haki za Binadamu inaendelea na zoezi la kutoa mafunzo hayo kwa makundi mbalimbali, yakiwemo Jeshi la Polisi,pamoja na waandishi wa habari, Tanzania Bara na  Zanzibar.



UNESCO Yaunga Mkono Juhudi za Serikali Kuboresha Mfumo wa Usimamizi wa Mafunzo Endelevu ya Walimu (MEWAKA)

September 11, 2025 Add Comment


Picture1

Picture2

Picture3

Picture4

Picture5

Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeonyesha dhamira ya dhati Kufanya kazi bega kwa bega na wadau wa maendeleo kuhakikisha uboreshaji wa mfumo wa usimamizi wa mafunzo endelevu wa walimu kazini yaani MEWAKA unaboreshwa na kukamilika kwa wakati na kwa ufanisi ili kuwezesha mahitaji ya walimu wa Sekondari.


Akizungumza wakati wa kuhitimisha warsha  iliyofanyika kwa muda ya siku mbili ya tarehe 28 na 29 Agosti 2025, ya mapitio ya mfumo wa MEWAKA ulioboreshwa Mratibu wa Mradi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Bi. Lina Rujweka, alitoa shukrani kwa juhudi na muda uliowekezwa na wadau wote, ikitambua mchango wao muhimu unaotarajiwa kuleta mafanikio makubwa katika utekelezaji wa mradi huu hasa UNESCO na Jamhuri ya Korea kupitia mradi wa ‘’KFIT III wa Transforming Education through ICT in Africa’’ kwa kuendelea kutoa msaada wa kifedha.


Shirika la UNESCO Dar es Salaam, kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), inaendelea na juhudi za uboreshaji mfumo wa MEWAKA ili kuzingatia mahitaji ya walimu wa shule za sekondari.

Ushirikiano huu ulitokana na tathmini ya mahitaji iliyoonyesha kuwa mfumo wa sasa ulikuwa umeundwa mahsusi kwa ajili ya kuwa jukwaa la mafunzo ya maendeleo ya kitaaluma kwa walimu wa shule za msingi.

Hivyo, wadau walikutanishwa ili kupitia toleo la awali la mfumo wa MEWAKA kwa lengo la kuhakikisha umuhimu, ubora, na uendelevu wa muda mrefu wa jukwaa hilo.


Wadau hao walikuwa kutoka  wizara ya elimu, sayansi na Teknolojia , Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Taasisi ya Elimu Tanzania, Tume ya Kitaifa ya UNESCO na baadhi ya walimu wa shule za sekondari.


Katika hotuba yake ya ufunguzi, mwakilishi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ally Mape alisema majukwaa ya kidijitali ni nyenzo yenye nguvu ya maendeleo ya kitaaluma, yanayochangia kwa kiasi kikubwa kuwawezesha walimu kupata ujuzi na kujiamini ili kufanikisha kazi zao katika Dunia ya sasa.


Kwa upande wake mkuu wa Sekta ya Elimu kutoka Ofisi ya UNESCO Dar es Salaam, Dkt. Faith Shayo, ameeleza kuwa lengo kuu ni kupanua upatikanaji wa mafunzo endelevu ya kitaaluma kupitia majukwaa ya kidijitali, hivyo itasaidia kuboresha matokeo ya ufundishaji na ujifunzaji kote nchini.


Hata hivyo Dkt. Shayo aliwahimiza wadau kutoa maoni na mitazamo yao kusaidia kuhakikisha toleo la mwisho la mfumo huu sio tu kuwa la kisasa bali pia rahisi kutumia na lenye matokeo chanya.

Mpango huu unalingana na juhudi za Serikali za kuunganisha TEHAMA katika elimu, kama inavyoonekana katika sera na mikakati muhimu ya kitaifa ikiwemo Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023, Mkakati wa Kitaifa wa Elimu ya Kidijitali 2025 – 2030, Dira ya Maendeleo ya 2050, Mitaala ya Elimu ya Msingi na ya Ualimu, pamoja na mipango ya kimataifa kama vile Malengo ya Maendeleo Endelevu hasa lengo namba nne.

MAHAFALI YA 11 NELSON MANDELA: WAHITIMU WAPEWA WITO WA KUBUNI, KUBIASHARISHA NA KUITUMIKIA JAMII

MAHAFALI YA 11 NELSON MANDELA: WAHITIMU WAPEWA WITO WA KUBUNI, KUBIASHARISHA NA KUITUMIKIA JAMII

August 29, 2025 Add Comment

 

Wahitimu wa Mahafali ya 11 ya Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) wakiwa tayari kwa ajili ya kutunukiwa shahada zao na Mkuu wa Taasisi, Mhe. Omari Issa (hayupo katika picha).

......

TAASISI  ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) imejivunia kutimiza malengo matano ya msingi iliyojiwekea, likiwemo eneo la utafiti na ubunifu, pamoja na usimamizi madhubuti wa programu za uatamizi wa teknolojia.

Akizungumza Agosti 28, 2025 jijini Arusha wakati wa Mahafali ya 11 ya taasisi hiyo, Makamu Mkuu wa Taasisi, Prof. Maulilio Kipanyula, alisema taasisi hiyo imepanua wigo wake wa kitaaluma kwa kutoa Shahada ya Umahiri katika Ubunifu na Usimamizi wa Ujasiriamali kupitia Shule Kuu ya Mafunzo ya Biashara na Sayansi za Jamii (BuSH), ambapo wahitimu wa kwanza kutoka shule hiyo walitunukiwa shahada kwa mara ya kwanza.

Jumla ya wahitimu 111 walitunukiwa shahada katika mahafali hayo, ambapo 71 walitunukiwa Shahada ya Umahiri na 40 walitunukiwa Shahada ya Uzamivu.

Prof. Kipanyula alieleza kuwa dhana ya kubiasharisha bunifu na teknolojia inayoendelezwa na NM-AIST inalenga kusaidia Serikali katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hususan katika kukuza viwanda na uchumi wa nchi kwa ujumla.

“Tunawataka wahitimu wetu kuwa na mtazamo wa soko katika kila bunifu wanayoanzisha. Hadi sasa, zaidi ya bunifu 35 zimepata hatimiliki. Hatua inayofuata ni kuhakikisha zinabiasharishwa kwa tija na kuwa chanzo cha mapato kwa taasisi na taifa,” alisema Prof. Kipanyula.

Aliongeza kuwa usimamizi wa uatamizi, uhaulishaji wa teknolojia na ubia kati ya watafiti na sekta binafsi ni nguzo muhimu ya kuimarisha uchumi kupitia maarifa yanayotolewa na taasisi hiyo. Hata hivyo, alisisitiza kuwa mafanikio hayo hayawezi kufikiwa bila kushirikisha jamii.

Katika mwaka wa kwanza wa masomo, Prof. Kipanyula alisema NM-AIST imefanikiwa kudahili wanafunzi 250 wa shahada za umahiri na uzamivu, ambapo wengi wao walinufaika na ufadhili wa Samia Scholarship. Kupitia ufadhili huo, wanafunzi 50 wamepata mafunzo katika maeneo ya akili bandia (Artificial Intelligence) na Sayansi ya Takwimu (Data Science).

Aidha, alieleza kuwa taasisi hiyo imenunua vifaa vya kisasa vya maabara na imepata ithibati ya kimataifa, hatua inayowezesha utafiti wa kiwango cha juu kinachokubalika kitaifa na kimataifa, hususan kwa kushirikiana na viwanda.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Taasisi, Balozi Maimuna Tarish, aliwahimiza wahitimu kutumia ujuzi walioupata kutatua changamoto za jamii, kuanzisha ajira na kushiriki kikamilifu katika mageuzi ya kiuchumi.

“Maarifa, ujuzi na ubobezi mlioupata lazima uwe chachu ya mabadiliko chanya kwa taifa. Muwe na moyo wa kujituma, mzingatie uadilifu, na mwe mfano wa kuigwa katika jamii,” alisema Balozi Tarish.

Wakati huo huo, mmoja wa wahitimu hao, Isaac Mengele, alishukuru kukamilisha masomo yake katika taasisi hiyo huku akieleza kuwa tafiti yake ilihusu kuenea kwa vinasaba vya kinga kwa ng’ombe wa maziwa dhidi ya ugonjwa wa maziwa, kwenye mashamba madogo ya ufugaji.

“Nitahakikisha matokeo ya tafiti yangu yanawasaidia wafugaji wa ng’ombe wa maziwa kufuga kisasa zaidi, kupunguza magonjwa, na kuongeza tija,” alisema Mengele.

Mlau wa Mahafali ya 11 ya Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Prof. Gabriel Shirima, akiongoza maandamano ya wanataaluma kuelekea sherehe za Mahafali, Agosti 28, 2025, katika kampasi ya Tengeru, Arusha. Jumla ya wahitimu 111 walitunukiwa shahada mbalimbali za Umahiri na Uzamivu.

Makamu Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Prof. Maulilio Kipanyula, akisoma hotuba wakati wa Mahafali ya 11 yaliyofanyika Agosti 28, 2025, ambapo jumla ya wahitimu 111 walitunukiwa shahada mbalimbali za Umahiri na Uzamivu.

Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, Mhe. Omari Issa (kulia), akimtunuku mmoja wa wahitimu (kushoto) wa Shahada ya Uzamivu wakati wa Mahafali ya 11 ya taasisi hiyo, Agosti 28, 2025. Jumla ya wahitimu 111 walitunukiwa shahada mbalimbali za Umahiri na Uzamivu.

Wahitimu wa Mahafali ya 11 ya Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) wakiwa tayari kwa ajili ya kutunukiwa shahada zao na Mkuu wa Taasisi, Mhe. Omari Issa (hayupo katika picha).

 
UDOM YAKUTANA NA WADAU KUCHAMBUA NAFASI YA AKILI UNDE KATIKA UTAWALA BORA

UDOM YAKUTANA NA WADAU KUCHAMBUA NAFASI YA AKILI UNDE KATIKA UTAWALA BORA

August 26, 2025 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), kwa kushirikiana na wadau wa teknolojia na wataalamu wa utawala wamekutana leo Jijini Dodoma chuoni hapo kwenye warsha maalumu inayolenga kuchambua nafasi ya akili unde katika kuimarisha misingi ya utawala bora nchini.

Akizungumza mara baada ya kufungua warsha hiyo leo Agosti 25,2025 Naibu Makamu Mkuu Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) - Taaluma, Utafiti na Ushauri Elekezi Prof. Razack Lokina amesema wananangazia kuhusu matumizi ya akili Hunde na namna ya kuimarisha utawala bora na kuongeza ufanisi katika utendaji wa Serikali

"Suala kubwa ni katika kungalia matumizi bora ya akili hunde namna ambavyo inaweza kusaidia katika sekta ya Afya na kilimo pamoja na kujadili changamoto zake endapo itatumika vibaya ni wapi inaweza kuharibu lakini ikitumika vizuri inaweza kuongeza ufanisi katika utendaji wa Serikali, "amesema.

Amesema suala hilo kwa wao kama wana taaluma ni muhimu kuliongelea kwasababu tayari lipo duniani na hawawezi kulikwepa kwani changamoto mbalimbali wameanza kuzuiona kutokana na baadhi kuitumia vibaya japo inaweza kuwa vizuri katika kuboresha maisha ya binadamu na kizazi kijacho.

"Huu ni wakati mwafaka wa kuweza kulijadili kwa uwazi na kuweza kuchanganua kila eneo ambalo namna gani akili Hunde inaweza ikatumika kwa ubora zaidi kuliko ambao watu wanaweza kuichukua labda wakatimia vibaya.

Kwa upande wake Msimamizi wa mradi wa Africa Artificial Intelligence Lab (AfriAI Lab), UDOM Dkt. Mohamed Mjahid amesema mradi huo ulianza mwaka 2021, ambapo katika warsha hiyo watajadili namna bora ya uwazi katika mifumo ya Serikali na sekta binafsi.

"Pia kupitia warsha hii tunajidiliana kuhusu matumizi ya akili unde ili kuweza kutoa uaminifu kwa wananchi na wadau wengine kiamini mifumo ya Serikali katika namna nyingine ya matumizi, "amesema.

Sanjari na hilo Dkt. Mjahid amesema akili unde isipotumika vizuri inaweza kuharibu mifumo mbalimbali ikiweno kudharirisha watu vitu ambavyo sio sahihi pamoja na utoaji wa taarifa zisizo sahihi.