Showing posts with label burudani. Show all posts
Showing posts with label burudani. Show all posts

SERIKALI KUTOA MIRAHABA YA BILIONI 1 KWA WASANII MWAKANI

December 19, 2025 Add Comment


NA MASHAKA MHANDO


WIZARA ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, kupitia Taasisi ya Hakimiliki nchini (COSOTA), inatarajia kuweka historia mpya kwa kugawa zaidi ya shilingi bilioni moja kama mirabaha kwa wasanii wa makundi mbalimbali nchini ifikapo Januari 23, 2026.


Hatua hiyo inakuja baada ya majadiliano ya kimkakati kati ya Naibu Waziri wa sekta hiyo, Mhe. Hamis Mwinjuma (MwanaFA), na uongozi wa COSOTA, yaliyolenga kujibu kiu ya muda mrefu ya wasanii kuhusu malipo ya haki zao.


Akizungumza katika mahojiano maalum, MwanaFA alisema kuwa Serikali imejipanga kufanya ugawaji huo kuwa shughuli kubwa na ya kihistoria kutokana na kiwango kikubwa cha fedha kilichokusanywa.


"Kama msanii na kama Naibu Waziri, nimekuwa nikipokea maswali mengi kutoka kwa wasanii wenzangu wakitaka kujua hatma ya mirabaha yao. Nimefanya majadiliano (discussion) nzuri na COSOTA na tumekubaliana kuwa Januari 23 mwakani, tunakwenda kutoa zaidi ya shilingi bilioni moja na ushee. Hiki ni kiwango kikubwa ambacho hakijawahi kutokea nchini," alisema MwanaFA.

MwanaFA alibainisha kuwa mafanikio hayo yametokana na hatua ya Bunge kubadilisha sheria inayoruhusu kuanzishwa kwa Taasisi za Pamoja za Kusimamia Hakimiliki (Collective Management Organizations - CMOs). 

Alieleza kuwa hadi sasa, leseni mbili zimetolewa kwa kampuni za CMO ambazo zimeshirikiana na taasisi za kimataifa, ikiwemo Taasisi ya Afrika Kusini inayosimamia mirabaha ya kidijitali (CAPASSO) kupata fedha hizo zinazokwenda kutolewa Januari.


Aidha, alitaja kuwa miongoni mwa vyanzo vikuu vya fedha hizo ni pamoja na kodi ya vifaa vinavyobeba kazi za sanaa na ada zinazotokana na Vibali vya Jumla vya kupiga nyimbo kwenye Redio na Televisheni (Blanket License).


"Tumepata zaidi ya shilingi bilioni moja kupitia mfumo wa Blanket License. Fedha hizi zitawanufaisha wasanii, huku sehemu ikiongoza Mfuko wa Utamaduni na Sanaa, COSOTA, pamoja na kodi ya Serikali," aliongeza.


Alifafanua kuwa tofauti na zamani, safari hii wigo umepanuliwa ambapo wanufaika watatoka katika makundi ya Muziki, Filamu, Sanaa za Maonyesho, Sanaa za Ufundi, pamoja na Waandishi wa Vitabu.


Hata hivyo, MwanaFA alitoa rai kwa wasanii wote: "ili unufaike na fedha hizi, ni lazima usajili kazi zako COSOTA. Usajili ndio utambulisho pekee utakaorahisisha utaratibu wa wewe kupata mirabaha yako pindi kazi zako zinapotumika au kuchezwa."

Mwisho

🔴🔴 WALIMBWENDE WA MISS GRAND TANZANIA WAFANYA ZIARA YA MAFUNZO HIFADHI YA PANDE

August 14, 2025 Add Comment




Na Beatus Maganja,

Dar es Salaam

Walimbwende 24 wanaoshiriki mashindano ya Miss Grand Tanzania 2025 kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara, wamefanya ziara ya siku moja katika Hifadhi ya Pande iliyopo jijini Dar es Salaam tarehe 13 Agosti 2025 kwa lengo la kujifunza masuala ya uhifadhi na utalii wa ndani.

Ziara hiyo iliandaliwa kwa ushirikiano kati ya waandaaji wa Miss Grand Tanzania na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), ikiwa ni sehemu ya kuwawezesha walimbwende hao kujifunza masuala ya uhifadhi na utalii na kuwa mabalozi wa vivutio vya utalii wa ndani, hususan Hifadhi ya Pande.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Kamanda wa Hifadhi ya Pande, PC Suleiman Keraryo, alisema hifadhi hiyo ni kivutio cha kipekee kilichopo katikati ya Jiji la Dar es Salaam, ambapo wageni hupata fursa ya kutalii na kujionea vivutio mbalimbali  ikiwa ni pamoja na kujifunza kuhusu historia ya hifadhi hiyo, bioanuwai na mchango wake katika uhifadhi wa mazingira na viumbe hai.

“Karibuni sana katika Hifadhi yetu ya Pande, hifadhi iliyo katikati ya Jiji la Dar es Salaam, ikiwa na wanyamapori wa aina mbalimbali na vivutio vingine lukuki. Hapa ni mahali sahihi kwenu kujifunza na kujionea rasilimali za nchi yenu,” alisema Keraryo.

Aidha, alibainisha kuwa mshindi wa Miss Grand Tanzania 2025 atateuliwa kuwa Balozi wa Hifadhi ya Pande, ambapo atashirikiana na TAWA katika juhudi za kuitangaza hifadhi hiyo pamoja na kuchochea utalii wa ndani, sambamba na kuunga mkono juhudi za Serikali katika sekta ya maliasili na utalii.


Mashindano ya fainali ya Miss Grand Tanzania yanatarajiwa kufanyika tarehe 16 Agosti 2025 katika Ukumbi wa Superdome, Masaki – Dar es Salaam.

Uongozi wa Hifadhi ya Pande pia umeeleza dhamira yake ya kuendeleza ushirikiano na waandaaji wa Miss Grand Tanzania kwa kuhakikisha kuwa walimbwende wanapata fursa ya kulala ndani ya hifadhi hiyo na kufanya mazoezi katika mazingira ya asili, ili kuongeza uelewa wao kuhusu uhifadhi wa mazingira.

Kwa upande wao, walimbwende wameeleza kufurahishwa na ziara hiyo, hususan kupata fursa ya kuona kwa ukaribu aina mbalimbali za wanyamapori waliopo hifadhini humo, sambamba na mapokezi mazuri kutoka kwa maofisa wa TAWA. Pia waliahidi kuwa mabalozi wa kuitangaza hifadhi hiyo kwa jamii.

Ziara hiyo imeelezwa kuwa ni mwanzo wa ushirikiano endelevu kati ya TAWA na taasisi za kijamii, hususan zinazowalenga vijana, kwa lengo la kuongeza uelewa juu ya umuhimu wa kulinda mazingira na kuendeleza utalii wa ndani kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho