Showing posts with label michezo. Show all posts
Showing posts with label michezo. Show all posts

DKT.BITEKO AHIMIZA WANAMICHEZO KUCHUNGUZA AFYA ZAO

September 08, 2025 Add Comment


📌 Tasnia ya Burudani na Michezo kwa mwaka 2024/2025 imekuwa kwa asilimia 18


📌 Watumishi  3,353 washiriki SHIMIWI mwaka 2025


📌 Awahimiza washiriki SHIMIWI kusikiliza kampeni za wagombea na kupiga kura Oktoba 29


📌 Serikali kujenga Kituo cha Kulea Vipaji Mwanza


Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ametoa rai kwa wanamichezo kufanya uchunguzi wa afya zao kwa kuhusisha vipimo vyote muhimu ikiwemo vya moyo, damu na viungo vyote vya mwili ili kuhakikisha usalama wa Afya zao.

 


Ameliomba Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali Tanzania (SHIMIWI) kuendelea kushirikiana na Taasisi za Afya nchini na kuweka mfumo sahihi wa upimaji wa afya kwa wanamichezo.


Dkt. Biteko ametoa rai hiyo Septemba 7, 2025 katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wakati akifungua rasmi mashindano ya 39 ya SHIMIWI yaliyotanguliwa na maandamano ya watumishi wa umma.


Ametaja masuala mengine muhimu ya kuzingatiwa kwa wanamichezo “ Mazoezi ya awali na mbinu nyingine mbalimbali kwa kujenga uimara wa mwili kupitia mazoezi kama vile kukimbia, mazoezi ya nguvu na mazoezi mfano wa hayo. Pia, kuiandaa akili ili kuikabili michezo na mashindano kwa ujumla, wataalamu husema mafanikio huanza katika fikra,” amesema Dkt. Biteko.

 Ameongeza kwa kusema Nimejulishwa kwamba, katika michezo ya mwaka wa jana mlisajili watumishi 2,995. Na mwaka huu 2025 mmesajili watumishi 3,353 kushiriki michezo hii ambapo ni sawa na ongezeko la asilimia 12 hongereni sana,” 


Pia, ameipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na viongozi wa SHIMIWI kwa kazi kubwa ya kuratibu, kusimamia na kuendeleza michezo nchini.

Dkt. Biteko pia amewataka waajiri kutekeleza maagizo ya Rais Samia ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya watumishi wanaoshiriki SHIMIWI huku akiwaeleza watumishi kuwa Rais Samia anawatakia kila la heri katika michezo yao na kuwa yuko tayari kuendelea kushirikiana nao ili kupata mahitaji yao.


Amesema takwimu zinaonesha kuwa, Tasnia ya Burudani Tanzania ambayo michezo ipo ndani yake imeendelea kukua kwa kasi na kuchangia sehemu muhimu katika Pato la Taifa na kuongeza ajira nchini.

 


Ametolea mfano kwa mwaka 2022/2023 sekta hiyo imekua kwa asilimia 15 na mwaka 2023/24 kwa asilimia 18. Aidha, uwepo wa watumishi wanaoshiriki SHIMIWU zaidi ya 3,000 Jijini Mwanza umesaidia kutengeneza ajira na kuchangia mzunguko wa fedha. 


“Nawaomba  viongozi muweke mikakati ya kuhakikisha manufaa haya yanawagusa Watanzania wa maeneo yote nchini kwa maslahi mapana ya Taifa kwa ujumla,” amesisitiza Dkt. Biteko.



Halikadhalika amewaasa wachezaji wote kujenga fikra ya kupendana na si kuchukiana baina yao pamoja na kufuata na kuzingatia taratibu zote za michezo.


Fauka ya hayo, Dkt. Biteko amewasihi wanamichezo hao kuhimizana kushiriki kwa amani katika zoezi la kusikiliza kampeni za wagombe na kukumbushana umuhimu wa kupiga kura.


Naye Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Said Mtanda ameishukuru Serikali ya Rais Samia kwa  kuendelea kuwekeza katika michezo ambapo inajenga Kituo cha Kulea Vipaji katika Chuo cha Michezo Malya.


Pia, amesema shughuli za kampeni mkoani humo zinaendelea vizuri na Oktoba 29, 2025 wananchi watajitokeza kwa wingi kupiga kura.


Kwa upande wake, Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amemshukuru Rais Samia kwa kuendelea kuruhusu kufanyika kwa  mashindano ya SHIMIWI kwa watumishi wa umma kwa miaka mitano mfululizo kwa kuwa yameendelea kuwa na faida kubwa.


“ Wizara yetu itaendelea kuhakikisha michezo hii inafanyika kwa haki, sisi kama Wizara tunamshukuru Mhe. Rais kwa maelekezo yake na kutoa raslimali fedha ili kukuza sekta ya michezo nchini,” amesema Msigwa.


Ametaja jitihada za Serikali katika kuimarisha sekta ya michezo ni pamoja na kukamilisha viwanja na shule za michezo katika maeneo mbalimbali nchini.


Ameongeza kuwa Tanzania imeendelea kufanya vizuri katika michezo kimataifa  katika ngazi mbalimbali.


Katika salamu zake za utangulizi, Mwenyekiti wa SHIMIWI, Daniel Mwalusamba amesema Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Baraza la Michezo la Taifa imefanya shughuli zake kwa ufanisi mkubwa na hivyo kuleta matokeo chanya.


Awali,  Dkt. Biteko ametembelea banda la Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) ambapo ameelezwa majukumu na huduma zinazotolewa kwa wananchi.


Mashindano ya Michezo ya 39 ya SHIMIWI kwa mwaka 2025 yanayoongozwa na kaulimbiu “ Michezo kwa Watumishi Huongeza Tija Kazini, Jitokeze Kushiriki Uchaguzi Mkuu 29 Oktoba 2025 kwa Amani na Utulivu  Kazi Iendelee.”yatafikia tamati Septemba 16, 2025. 


Mwisho

TIMU YA NETIBOLI NISHATI YATINGA KUMI NA SITA BORA MASHINDANO YA SHIMIWI

September 05, 2025 Add Comment


📌 *Yawa kinara katika kundi C*


Wakati mashindano yaliyoandaliwa na Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali  (SHIMIWI) yakishika kasi jijini Mwanza  kwa hatua za awali, Wizara ya Nishati imetinga  katika hatua ya 16 bora  katika mchezo wa Netiboli kwa kuwa na jumla  ya alama tisa (9). 

Wizara ya Nishati ipo  katika kundi C ambapo kundi hilo linaundwa na Timu ya RAS Singida, RAS Shinyanga, Wizara ya Kilimo, pamoja na  Hazina.

Awali,  Wizara ya Nishati ilitupa karata yake ya kwanza dhidi ya  RAS Singida na kuibuka na ushindi wa magoli 40 kwa 0 (sifuri), Mchezo wa Pili Nishati ilicheza na Wizara ya Kilimo na kushinda kwa magoli  34 kwa 22, mchezo wa tatu Nishati ilipoteza  dhidi ya timu ya Hazina kwa magoli 36 kwa 21, huku katika mchezo wa nne Nishati ikicheza na Timu ya RAS Shinyanga na kuibuka na ushindi wa magoli 27 kwa 19 na hivyo  kuwa kinara katika kundi C ikiwa na jumla ya magoli 122.

Aidha, Timu ya Wizara kwa sasa inasubiri  taratibu za upangaji  wa makundi ambayo yanatarajiwa kupangwa mwisho wa juma hili ambayo ni tarehe 6-7 Septemba, 2025.


Michezo  ya SHIMIWI ilianza Septemba Mosi 2025  ambapo ufunguzi utafanyika Septemba 07, 2025 na mashindano yatamalizika Septemba  16, 2025.

Katika michezo hiyo, Wizara ya Nishati imepeleka timu mbalimbali ikiwemo  timu ya mpira wa miguu,riadha,karata,draft,mchezo wa Vishale, mchezo wa bao na baiskeli.



Mashindano ya SHIMIWI yamebeba na kauli mbiu isemayo  "Michezo kwa Watumishi Huongeza Tija Kazini, Jitokeze Kushiriki Uchaguzi Mkuu 2025,kwa Amani na Utulivu".

MALIASILI YAZIDI KUNG'ARA MWANZA YAITANDIKA TIMU YA NETBALL YA KATIBA NA SHERIA 38-8 SHIMIWI 2025

September 03, 2025 Add Comment


Na John Bera – Mwanza


Timu ya netiboli ya Wizara ya Maliasili na Utalii imeendelea kuonesha ubabe kwenye Mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) kwa kuichapa kwa kishindo Wizara ya Katiba na Sheria kwa mabao 38–8, katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza.

Timu hiyo ilianza kwa kasi na kutawala mchezo kutoka mwanzo hadi dakika ya mwisho, ikionesha uelewano mzuri, umakini mkubwa na nidhamu ya hali ya juu uwanjani. Ushindi huo umeiweka Maliasili katika nafasi nzuri ya kusonga mbele kwenye hatua za mtoano.

Kocha wa timu hiyo, Bi. Rehema Kapela, amesema ushindi huo si wa bahati nasibu, bali ni matokeo ya maandalizi ya muda mrefu na ari ya wachezaji wake waliodhamiria kuweka historia mwaka huu.

“Tumekuwa tukifanya mazoezi kwa bidii na leo tumeona matokeo. Wachezaji wameonesha kujituma, umoja na uthabiti. Tuna malengo makubwa, na huu ni mwanzo mzuri kwetu,” alisema Kocha Kapela.

Mchezaji wa timu hiyo, Julia Kepha, ambaye aling’ara katika mchezo huo kwa kucheza kwa kiwango cha juu katika safu ya ulinzi, amesema walijiandaa kisaikolojia na kimwili kuhakikisha wanapata ushindi.

“Ushindi huu umetokana na kazi ya pamoja. Kila mmoja alitimiza majukumu yake. Tuliingia uwanjani tukiwa na malengo, na tulihakikisha tunayatimiza kwa vitendo,” alisema Julia.

Kwa upande wake, Kaimu  Mratibu wa Timu ya Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. George Rwezaura, amechukua fursa hiyo kuipongeza timu kwa ushindi huo wa kuvutia na kuahidi kuwa wataendelea kushirikiana na benchi la ufundi kuhakikisha timu inasonga mbele zaidi.

“Leo tumeandika historia dhidi ya timu ngumu. Ushindi huu umetupa hamasa kubwa na tunawaahidi watumishi wenzetu kwamba tutapambana hadi mwisho. Hakuna majeruhi, morali ni kubwa, na tumejiandaa vyema kwa mechi zijazo,” alisema George.

Katika michezo mingine ya leo, timu ya wanaume ya Maliasili iliibuka na ushindi wa bao 2–0 dhidi ya Tume ya Haki za Binadamu kwenye mchezo wa kuvuta kamba, huku timu ya wanawake ikipoteza kwa bao 1–0 dhidi ya timu ya Mkoa wa Geita (RAS Geita).


Kesho michezo hiyo itaendelea kwa timu Kamba ME kukutana na RAS Pwani na Kamba KE kukutana Maji wakati Netball watacheza na TAMISEMI

SHIMIWI NI MAHALA PA KAZI- BI ZIANA MLAWA

August 31, 2025 Add Comment


📌 *Asema Wizara ya Nishati ipambane irudi na ushindi*


📌 *Asema Wizara ya Nishati iwe mfano kwa Wizara zingine*


Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Wizara ya Nishati, Bi. Ziana Mlawa leo amesema kushiriki michezo mbali mbali inasaidia katika kujenga afya ya mwili na akili hivyo mtumishi anapopata nafasi ya kushiriki michezo yeyote aitumie ipasavyo pia husaidia hali itakayowajengea uwezo kujiamini zaidi ikiwemo katika maeneo ya kazi.

Bi. Mlawa ameyasema hayo alipokuwa akiwaaga watumishi wa Wizara ya Nishati watakao shiriki michezo ya SHIMIWI itakayofanyika jijini Mwanza kwanzia tarehe 1 Septemba 2025


" Pamoja na kushiriki michezo ambapo ni mbali na eneo la kazi mkumbuke mkiwa huko ni eneo la kazi nidhamu na uadilifu uwe kipau mbele mdaa wote muwapo kwenye michezo  hiyo." Amesisitiza Bi. Mlawa


Ameongeza kuwa watumishi hao wajitahidi wapate ushindi ambapo kwa ushindi huo Wizara itapata heshima njee na ndani ya Wizara

DED MUHEZA ATOA AHADI NONO KWA WACHEZAJI WA TIMU YA HALMASHAURI HIYO

August 25, 2025 Add Comment

 


Na Oscar Assenga,TANGA

MKURUGENZI wa Halmashauri ya wilaya ya Muheza Mkoani Tanga Dkt. Juma Mhina ametoa ahaidi ya kununua kila goli litakalofungwa na timu ya mpira wa Miguu ya Halmashauri hiyo wa kiasi cha 20,000 ikiwa ni kutoa motisha kwa wachezaji wa Halmahauri hiyo wanaoshiriki katika Michuano ya Shimisemita inayoendelea Jijini Tanga.

Aliyasema hayo leo mara baada ya kutembelea timu hiyo kabla ya kuanza mchezo wa mpira wa miguu dhidi yao na Halmasahauri ya Mpimbwe ikiwa ni michuano ya Shimisemita inayoendelea kwenye viwanja v ya Shule ya Sekondari Ufundi Mkoani Tanga

Alisema kwamba anaridhishwa na kiwango na mwenendo wa timu hiyo katika mashindano hayo hivyo akaendelea kutoa hamasa kwao kuhakikisha wanaendelea kufanya vizuri na kuibuka na ubingwa.

“Hongereni sana mmefanya kazi kubwa sana kwa kuendelea kufanya vizuri naomba tuendelea kuwa na nidhamu msichoke tupo pamoja na tutaendelea kuwasapoti “Alisema Mkurugenzi huyo

Hata hivyo aliwataka kuendelea kuhakikisha wanaendelea kupambana ili kuweza kusonga hatua nyengine kwenye mashindano hayo huku akisisitiza nidhamu na kujituma

MUHEZA YAIGARAGAZA BUMBULI MAGOLI 3-2 MICHEZO SHIMISEMITA

August 24, 2025 Add Comment







Na Oscar Assenga,TANGA

TIMU ya Mpira wa Miguu ya Halmashauri  ya Wilaya ya Muheza imebamiza Halmashauri ya wilaya ya Bumbuli mabao 3-2 katika michuano ya Shirikisho la Michezo la Mamlaka za Serikali za Mitaa kaika mchezo uliochezwa kwenye viwanja vya Shule ya Ufundi Tanga.

Shirikisho hili la Michezo linahusisha watumishi waliopo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ( Halmashauri) waliopo kwenye idara na vitengo mbalimbali.

Katika mchezo huo ambao ulikuwa na upinzani mkubwa kutokana na kila timu kutaka kupata ushindi lakini Halmashauri ya wilaya ya Muheza iliweza kuhimili na kuutawala vyema mchezo huo na hatimaye kuweza kuibuka na kidedea
Mashindano ya Shirikisho la Serikali za Mitaa Tanzania ( SHIMISEMITA) yalianza rasmi Agosti 15, 2025 na yanatarajiwa kukamilika Agosti 29, 2025 huku yakilenga kuwakutanisha watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, kushirikiana pamoja, kufahamiana, kubadilishana mawazo, kujenga Afya za watumishi ili kuepukana na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo kisukari na shinikizo la damu.
Michezo hii inaendelea katika Viwanja mbalimbali vya Michezo vilivyopo Jijini Tanga huku yakiwa yamebeba Kauli mbiu ya SHIMISEMITA 2025  " Jitokeze kupiga Kura kwa maendeleo ya Michezo".