Showing posts with label afya. Show all posts
Showing posts with label afya. Show all posts

DKT.MAGEMBE ATAKA KILA MWAJIRI AHAKIKISHE MTUMISHI WAKE ANAKUWA NA UHAKIKA WA MATIBABU KUELEKEA BIMA YA AFYA KWA WOTE

March 10, 2026 Add Comment




Na Hassan Kimweri, WAF - Dar es Salaam


Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amewataka waajiri kuhakikisha kila muajiriwa anakuwa na uhakika wa matibabu kuelekea utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050. 


Dkt. Magembe amesema hayo leo Machi 10, 2026 baada ya wasilisho la maandalizi ya Bima ya Afya kwa Wote kwenye mkutano na Wakurugenzi Wakuu wa Makampuni ya Tanzania (CEO Roundtable of Tanzania – CEOrt) uliofanyika jijini Dar es Salaam na kuwakutanisha viongozi kutoka serikalini, sekta binafsi na washirika wa maendeleo. 



"Serikali inaendelea kuimarisha utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kuwa na ubunifu wa vyanzo vya fedha pamoja na kuanzisha kitita muhimu kitakachohakikisha kila mwananchi anapata huduma muhimu za afya katika vituo vyote vya kutolea huduma nchini," amesema Dkt. Magembe

Aidha, Dkt. Magembe amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ambapo utekelezaji wake unafanyika kwa awamu, awamu ya kwanza ilianza Januari 6, 2025 kwa kuwatambua zaidi ya familia milioni 3.6 kidijitali kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa," amesema Dkt. Magembe

Katika hatua nyingine, Dkt. Magembe amesema Serikali imeanzisha Mfuko wa kugharamia huduma za Afya (Health Equity Fund) utakaosaidia kugharamia huduma za afya kwa wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za matibabu kupitia vyanzo mbalimbali.

Pia, amesema Serikali imeanza kuchukua hatua za kupunguza utegemezi wa misaada ya wahisani katika sekta ya afya kwa kuimarisha zaidi vyanzo vya ndani vya fedha na kutafuta mbinu mpya za ubunifu zitakazochangia kugharamia huduma za afya nchini.

Hata hivyo, ameeleza dhamira ya Serikali kuimarisha viwanda vya ndani vya dawa na bidhaa za afya ili kuhakikisha upatikanaji wa dawa unakuwa wa uhakika, kuongeza ajira na kukuza sekta binafsi kuelekea utekelezaji wa bima ya afya kwa wote. 

Mwisho, Serikali imewahimiza wawekezaji kutumia fursa zilizopo katika sekta hiyo, huku ikiendelea kukuza ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi katika uzalishaji wa dawa na vifaa tiba nchini. 



SERIKALI, SEKTA BINAFSI KUIMARISHA HUDUMA ZA DHARURA KUCHOCHEA AJIRA NCHINI

SERIKALI, SEKTA BINAFSI KUIMARISHA HUDUMA ZA DHARURA KUCHOCHEA AJIRA NCHINI

March 05, 2026 Add Comment






Na Abduly Iddy, Dar es Salaam

Serikali imesema ushirikiano kati yake na Sekta binafsi utaendelea kuwa chachu muhimu ya kuimarisha huduma za afya nchini, hususan katika kuboresha huduma za dharura kupitia mpango wa kuanzisha uzalishaji wa magari ya wagonjwa (ambulance) mkoani Tanga.

Akizungumza Machi 5, 2026 jijini Dar es Salaam katika kikao cha maandalizi ya kuanzisha uzalishaji wa magari hayo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe.Batilda Burian, amesema Serikali inakaribisha uwekezaji huo unaofanywa kwa kushirikiana na SO Company Limited kwani utaimarisha upatikanaji wa huduma za dharura za afya nchini hususan magari ya wagonjwa.

Amesema uzalishaji wa ambulance ndani ya nchi utaongeza upatikanaji wa magari ya kisasa ya kuwahudumia wagonjwa na kupunguza muda wa kuwafikia wananchi wanaohitaji msaada wa haraka wa kitabibu, hatua itakayosaidia kuokoa maisha ya watu.

“Mradi huu ni hatua muhimu tunapoimarisha mfumo wetu wa huduma za afya. Kupatikana kwa ambulance zinazozalishwa hapa nchini kutarahisisha usambazaji wake katika maeneo mbalimbali, hususan ya pembezoni,” amesema, RC Batlida.

Aidha, amesema mradi huo pia utaleta manufaa ya kiuchumi kwa kufungua fursa za ajira kwa vijana, kukuza wazalishaji wa ndani wa vipuri na kuchochea maendeleo ya sekta zinazohusiana na uzalishaji wa vifaa vya magari na huduma za afya.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Dharura na Maafa kutoka Wizara ya Afya, Dkt. Erasto Sylvanus, amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji ili kuhakikisha mradi huo unatekelezwa kwa ufanisi na kuchangia maendeleo ya sekta ya afya pamoja na uchumi wa taifa.

Mradi huo unatarajiwa kuimarisha huduma za dharura za afya huku ukifungua fursa mpya za ajira na maendeleo ya kiuchumi nchini.

RAS TANGA- MIKAKATI ENDELEVU SULUHISHO KUKABILI DHARURA ZA KIAFYA

RAS TANGA- MIKAKATI ENDELEVU SULUHISHO KUKABILI DHARURA ZA KIAFYA

March 05, 2026 Add Comment








Na Andrea Kadege, WAF-Korogwe

Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Mchatta ameagiza kuwekwa kwa mikakati endelevu itakayoiwezesha jamii kukabiliana na majanga ya dharura yanayopelekea athari kiafya, kwa ufanisi zaidi.

Bw. Mchatta ameyasema hayo leo Machi 05, 2026 wakati akifunga kikao kazi cha tathmini ya matukio na athari za kiafya mkoani Tanga, kilichoandaliwa na Wizara ya Afya Idara ya Dharura na Maafa kwa kushirikiana na Mradi wa Usalama wa Afya Duniani unaotekelezwa na asasi zisizo za kiserikali za PATH na CIHEB Tanzania, kilichofanyika Wilayani Korogwe.

“Maazimio yote yaliyojadiliwa yawekwe katika mpango kazi wenye malengo yanayopimika, muda wa utekelezaji na mgawanyo wa majukumu kwa kila sekta” amesema Bw. Mchatta

Aidha, amesema kwa kuwa idadi kubwa ya washiriki katika kikao kazi hicho ni wajumbe wa kamati ya maafa ya mkoa hivyo, amesisitiza kuwekwa kwa mikakati endelevu na ya muda mrefu kuhakikisha kuwa majanga ya dharura yanakabiliwa ili kulinda afya ya jamii.

Katika hatua nyingine ameishukuru na kuipongeza Wizara ya Afya kwa kuandaa kikao kazi hicho, huku akitambua mchango wa ushirikiano baina ya serikali na wadau wa maendeleo, mashirika yasiyo ya kiserikali (PATH na CIHEB Tanzania) pamoja na sekta binafsi katika kuimarisha utayari wa kukabiliana na dharura.

Naye Mratibu-Udhibiti Maafa na Dharura kutoka Wizara ya Afya Dkt. Saumu Nungu amesema kwa ngazi ya mikoa, Tanga umekuwa mkoa wa nne kufanyiwa tathmini ya matukio na athari za kiafya, huku akieleza kuwa kupitia mpango kazi utakaoandaliwa, Mkoa wa Tanga utakuwa na uwezo wa mapema wa kukabiliana na dharura za kiafya pindi zitakapotokea.

Amebainisha kuwa baada ya mpango huo kuandaliwa, utawasilishwa Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa kwa ajili ya mapitio kisha kusainiwa na kuidhinishwa ili utekelezaji wake uwe wa lazima na unaosimamiwa kikamilifu ili uweze kuwa wenye tija.

Kwa upande wake Mratibu wa Vituo vya Operesheni za Dharura za Afya ya Jamii kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI, Idara ya Afya Dkt. Ernest Kyungu ameeleza kuwa mafanikio katika kukabiliana na majanga ya kiafya yanetokana na maandalizi ya mapema, uratibu wa sekta mtambuka na uwekezaji katika elimu ya kinga kwa jamii.

Amesitiza kuwa Tanga inapaswa kujenga mfumo madhubuti unaojumuisha hatua za kabla ya janga, wakati wa janga na baada ya janga ili kupunguza madhara kwa wananchi kwa kuzingatia jiografia yake hususani mipaka ya bahari na bandari pamoja na mpaka wa nchi jirani ya Kenya.

Naye kiongozi wa Ufuatiliaji wa Magonjwa ya Mlipuko na yaliyopewa kipaumbele kutoka Mradi wa Usalama wa Afya Duniani unaotekelezwa na asasi zisizo za kiserikali za PATH na CIHEB Tanzania Dkt. Said Sheuya, ameeleza kuwa kupitia ushirikiano uliopo baina ya Wizara ya Afya na wadau mbalimbali , wamefanikiwa kuendesha mafunzo kwa wataalam, kuimarisha mifumo ya taarifa na kuongeza upatikanaji wa rasilimali muhimu za kukabiliana na majanga.

Kwa ujumla, kikao hicho kimeweka msingi wa maboresho ya kimkakati katika sekta ya afya mkoani Tanga, huku utekelezaji wa mpango kazi utakaoidhinishwa ukitarajiwa kuwa dira ya kuhakikisha ulinzi wa afya ya jamii unaimarika na athari za majanga zinapunguzwa kwa kiwango kikubwa.

WAZIRI MCHENGERWA -HAKUNA MGONJWA WA UVIKO-19 ,MAFUA MAKALI NA KIPINDUPINDU TANZANIA

February 27, 2026 Add Comment


Na Mwandishi  wetu– WAF, Dar es Salaam.


Wizara ya Afya imewataka wananchi kuendela kuchukua tahadhari na kufuatilia ushauri wa kitaalam ili kujikinga dhidi ya magonjwa mbalimbali kama ilivyoelezwa katika taarifa kwa umma  ya   Mganga Mkuu wa Serikali hivi karibuni


Hayo yamebainishwa leo Februari 27, 2026 Jijini Dar es salaam na Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa alipofanya ziara ya kimakakati katika hospitali ya Rufaa Mkoa Amana kwa lengo la kukagua utolewaji wa huduma za afya pamoja na maendeleo ya uboreshaji wa miundombinu ya hospitali hiyo

Aidha amesema, Serikali bado inaendelea kufuatilia kwa ukaribu juu ya mienendo  ya  magonjwa mbalimbali kama kipindu pindu, Dengue na UVIKO-19 hususani katika kipindi hiki cha mvua  huku akisistiza kwamba hakuna kisa chochote UVIKO, cha mgonjwa aliyelazwa katika hospitali nchini


“Napenda kuwahakikishia wananchi na Watanzania wote Serikali yenu ipo makini na inaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa maambukizi ya UVIKO-19 nchini na kimataifa, lakini pia tunasisitiza umuhimu wa kila mmoja kuendelea kuchukua tahadhari na kuzingatia ushauri wa kitaalamu unaotolewa na wataalamu wa afya ili kulinda afya binafsi na ya jamii kwa ujumla,” amesema Mhe. Mchengerwa.

Mhe. Mchengerwa amewataka Watanzania kujiandikisha na kulipia bima ya afya kwa wote sababu gharama za matibabu zinaweza kuwa kikwazo kwa wananchi wa hali ya chini hasa wanapohitaji kufanyiwa huduma za kibingwa na kibingwa bobezi


Waziri Mchengerwa amesema kuwepo kwa bima ya afya kwa wote kuendana sanjari na upatikanaji wa dawa katika vituo vya afya na hospitali ili kukamilisha dhamira ya serikali katika kurahisisha huduma za afya kwa wananchi 


Katika ziara hiyo, Mhe. Mchengerwa ameambatana na Katibu Mkuu Dkt. Seif Shekalaghe pamoja na menejimenti ya Wizara ya Afya, ambapo alikagua hali ya upatikanaji wa huduma, kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi na wagonjwa, na kueleza mikakati madhubuti ya serikali katika kuimarisha ubora na ufanisi wa huduma za afya kwa wananchi.

RC SENDIGA AZINDUA NA KUHAMASISHA UTEKELEZAJI WA BIMA YA AFYA KWA WOTE MKOANI MANYARA

December 21, 2025 Add Comment

 

 

Babati, Manyara Desemba 19, 2025: Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, leo Desemba 19, 2025 amezindua rasmi na kuhamasisha utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote (NHIF) katika Mkoa wa Manyara, akisisitiza umuhimu wa kila mwananchi kuwa na bima ya afya ili kupata huduma za matibabu kwa urahisi na kwa gharama nafuu.

Uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) mjini Babati, na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wataalamu wa afya, wawakilishi wa mpango wa kitaifa wa Bima ya Afya kwa Wote pamoja na wananchi mbalimbali.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mhe. Sendiga amesema mpango wa Bima ya Afya kwa Wote ni utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kutimiza ahadi ya siku 100 za kuanzisha mfumo utakaohakikisha kila Mtanzania anakuwa na bima ya afya.
“Mfumo huu unalenga kumwondolea mwananchi mzigo wa gharama kubwa za matibabu na kuhakikisha kila mmoja, bila kujali kipato chake, anapata huduma bora za afya kwa wakati,” amesema Mhe. Sendiga.

Aidha, amewaelekeza Wasimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya mkoani Manyara kuhakikisha mpango wa Bima ya Afya kwa Wote unatekelezwa kwa kuzingatia miongozo, kanuni na taratibu zilizowekwa, ili kufikia malengo yaliyokusudiwa na Serikali.

Sambamba na hilo, Mhe. Sendiga amesisitiza kuwa ni wajibu wa viongozi na watendaji wote kwenda kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kujiunga na mpango huo, ili waweze kunufaika na huduma za afya kwa uhakika.

Kwa upande wake, Bi. Janeth Kibambo, Mwakilishi wa Timu ya Kitaifa ya Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, amesema lengo kuu la mfumo huo ni kuhakikisha wananchi wote wanakuwa na uwezo wa kupata huduma za afya katika vituo vyote vya umma na binafsi vilivyosajiliwa, bila kikwazo cha kifedha.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, ameeleza kuwa mkoa umejipanga kikamilifu kutekeleza mpango huo, akibainisha kuwa changamoto ya wananchi kushindwa kugharamia matibabu imekuwa kubwa, hivyo kuanzishwa kwa Bima ya Afya kwa Wote ni mwarobaini muhimu katika kuboresha sekta ya afya.

Dkt. Method ameongeza kuwa Mkoa wa Manyara uko tayari kuupokea na kuutekeleza mpango huo kikamilifu, kwa kushirikiana na vituo vyote vya afya na wadau mbalimbali, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu.

Uzinduzi wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote mkoani Manyara unatarajiwa kuongeza wigo wa upatikanaji huduma za afya, kupunguza vifo vinavyotokana na ukosefu wa matibabu kwa wakati, na kuboresha ustawi wa jamii kwa ujumla.