Showing posts with label michezo. Show all posts
Showing posts with label michezo. Show all posts
TCDC YAICHALAZA KILIMO KWA BAO 2 – 1

TCDC YAICHALAZA KILIMO KWA BAO 2 – 1

April 17, 2026 Add Comment

Timu ya Mpira wa miguu ya TCDC Sports Club imechukua alama tatu (3) baada cha kuifunga Timu ya Mpira wa miguu ya Wizara ya Kilimo goli mbili (2) kwa moja (1) katika mechi iliyochezwa leo Aprili 17, 2026 saa 2:30 3:45 katika viwanja vya Venite mkoani Njombe.

Timu hizo zimekutana katika mashindano ya Michezo ya Wafanyakazi (Meimosi) yanayoyafanyika kitaifa mkoani Njombe.

Hapo Kesho Aprili 18, 2026 Timu ya Mpira wa miguu TCDC Sport Club inatarajia kukutana na Timu ya Mpira wa miguu ya TAMISEMI saa10:15 jioni katika viwanja vya Kibena mkoani humo.

TCDC YAKABIDHI VIFAA VYA MICHEZO KWA WACHEZAJI

TCDC YAKABIDHI VIFAA VYA MICHEZO KWA WACHEZAJI

April 14, 2026 Add Comment

Mrajis na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) Dkt. Benson Ndiege kushirikiana na Uongozi wa TCDC Sports Club wanunua vifaa vya michezo kwa wachezaji 42 kuelekea mashindano ya Michezo ya Meimosi mjini Njombe.

Vifaa hivyo vimekabidhiwa leo Aprili 14, 2026 jijini Dodoma wakati wa kuwaaga wanamichezo wakielekea mjini Njombe.

Vifaa vilivyonunuliwa ni jezi za mprira wa miguu, viatu, mipira na vifaa vingine vya michezo.

MWENYEKITI WA CCM MKOA TANGA AINGILIA KATI KUINUSURU KLABU YA AFRICAN SPORTS ISISHUKE DARAJA

April 12, 2026 Add Comment

 

Na Oscar Assenga,Tanga

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman  ameanza jitihada za kuinusuru Klabu ya African Sports ambayo ipo hatarini kushuka daraja kufuatia matokeo mabaya katika Ligi ya Championship.

Rajab aliyasema hayo baada ya kukutana na wachezaji pamoja na viongozi wa klabu hiyo, ambapo alieleza kuwa hali ya timu si ya kuridhisha, akifananisha na mgonjwa aliye katika chumba cha mahututi.

Alibainisha kuwa kwa sasa African Sports inashika nafasi ya 15 kati ya timu 16, hali inayoiweka katika hatari kubwa ya kushuka daraja endapo haitafanya vizuri katika mechi zilizobaki.

Akizungumzia historia ya klabu hiyo, alisema ni moja ya timu zenye heshima kubwa nchini na mshindani wa jadi wa Coastal Union, hivyo ni muhimu kurejesha ushindani wa soka la Tanga.

Katika hatua ya kuokoa timu hiyo, Mwenyekiti huyo  alitangaza kuchangia Shilingi milioni 20 ambazo tayari alikwisha kuziweka kwenye akauti, huku Mbunge wa Jimbo la Tanga akiahidi kutoa milioni tano na mdau mwingine kuahidi milioni 20, ikiwa ni sehemu ya kufikia lengo la kukusanya milioni 45 zinazohitajika kuiwezesha timu kumaliza msimu salama.

Alisema atahakikisha fedha hizo zinapatikana ili kutatua changamoto zinazoikabili klabu hiyo na kuwawezesha wachezaji kucheza kwa utulivu.

Aidha, aliwataka wachezaji kujituma katika mechi zilizobaki ili kuinusuru timu, akisisitiza kuwa wana dhamana ya kulinda heshima ya klabu hiyo.

Kwa upande mwingine, aliwashauri viongozi wa klabu kuweka mikakati ya muda mfupi na mrefu, ikiwemo kutovunja kambi mara baada ya msimu kumalizika ili kuboresha maandalizi ya msimu ujao.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya mara kwa mara ya kikosi na maandalizi hafifu yamekuwa yakichangia kushuka kwa kiwango cha timu, na kusisitiza kuwa kwa mipango madhubuti wanaweza kurejea Ligi Kuu katika msimu ujao.






DC SUMAYE - NMB KIJIJI DAY NI HATUA MUHIMU YA KUWAFIKIA WANANCHI WA VIJIJINI KUWAPATIA ELIMU YA FEDHA

April 12, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga, Lushoto

Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Zephania Sumaye, ameishukuru Benki ya NMB Bank Plc kwa kuandaa tukio la kipekee la Kijiji Day, akisema ni hatua muhimu katika kuwafikia wananchi vijijini na kuwapatia elimu ya kifedha.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Lushoto (CCM), alisema kuwa wizara ina malengo mahsusi ya miaka mitano, likiwemo kuhakikisha wananchi wanapata uhuru wa kiuchumi.

Alisisitiza kuwa uhuru huo hauwezi kupatikana bila wananchi kujihusisha na taasisi za kifedha, ikiwemo benki kama NMB.

Alieleza kuwa tukio la Kijiji Day ni sehemu ya utekelezaji wa malengo hayo, kwani linawawezesha wananchi kupata elimu ya kifedha pamoja na huduma mbalimbali za kibenki moja kwa moja walipo.

Tukio hilo lilifanyika katika Kata ya Magamba, ambapo wananchi walipata fursa ya kujifunza na kunufaika na huduma zinazotolewa na benki hiyo.

Aidha, alisema moja ya malengo ya serikali ni kuhakikisha jamii ya Lushoto inaunganishwa na kuwa kitu kimoja.

Alibainisha kuwa njia mojawapo ya kuimarisha mshikamano huo ni kupitia michezo na mabonanza, kama ilivyofanyika katika tukio hilo ambapo NMB ilitumia siku nzima kushirikiana na wananchi wa Kijiji cha Magamba.

Alisisitiza umuhimu wa elimu kwa maendeleo ya mwanadamu, akieleza kuwa hata katika mafundisho ya dini mbalimbali, elimu imepewa kipaumbele kikubwa.

Alifananisha juhudi za NMB na msemo usemao: “Usimpe mtu samaki, mfundishe kuvua.” Akasema benki hiyo inafanya kazi kubwa kwa kuwafundisha wananchi namna ya kutumia huduma za kifedha kwa ufanisi, badala ya kuwapatia msaada wa moja kwa moja bila uelewa.

Aliongeza kuwa kama benki zingetoa mikopo bila elimu ya matumizi sahihi, matokeo yasingekuwa endelevu,Hivyo, matukio kama Kijiji Day yanafungua njia ya kuwafikia wananchi, kuwapa elimu na kuwasogezea huduma za kifedha karibu zaidi.

Aliwahimiza NMB kuendelea na juhudi hizo pamoja na kuandaa mabonanza yatakayoongeza furaha, mshikamano na uelewa wa wananchi kuhusu huduma zao, jambo litakalosaidia kujenga imani na umiliki wa wananchi kwa benki hiyo.

Katika tukio hilo la Kijiji Day lililofanyika Magamba, shughuli mbalimbali zilifanyika ikiwemo mbio za marathon, huduma ya chakula, pamoja na mabonanza mengine. Lengo kuu lilikuwa ni kuwafikia wananchi, kuwapa elimu ya kifedha na kuwajengea uelewa mpana kuhusu huduma za benki.

Awali akizungumza Meneja wa Kanda ya Kaskazini wa NMB Bank Plc, Baraka Ladislaus, amesema benki hiyo inaendelea kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi kupitia matamasha ya Kijiji Day yanayofanyika vijijini.

Alisema lengo la mpango huo ni kuwafikia wananchi walipo, kuwapatia elimu ya kifedha na kuwaunganisha na huduma mbalimbali za kibenki ili kuwawezesha kiuchumi.

Alieleza kuwa pamoja na elimu ya kifedha, tukio hilo linaambatana na shughuli za kijamii ikiwemo upandaji miti kwa kushirikiana na Taifa Gas, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhifadhi mazingira na kuifanya Tanzania kuwa ya kijani.

Aidha, alisema NMB ina mtandao mpana wa mawakala zaidi ya 80,000 nchi nzima wanaotoa huduma karibu asilimia 60 ya mahitaji ya kifedha ya wananchi, sambamba na matumizi ya magari maalum ya kibenki yanayowafikia wananchi vijijini.

Aliongeza kuwa benki hiyo imeboresha huduma zake za kidijitali ikiwemo programu ya NMB Mkononi, inayorahisisha upatikanaji wa huduma kwa wateja popote walipo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto Whitney Mwinzagi aliwataka wananchi kutumia vyema elimu wanayoipata na kuelekeza mikopo wanayoipata kuitumia shughuli za uzalishaji mali badala ya matumizi yasiyo na tija.











NYASI BANDIA SULUHISHO LA KUDUMU UWANJA WA CCM MKWAKWANI

April 11, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga, Tanga

Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimeeleza kuwa suluhisho la kudumu la kuboresha eneo la kuchezea katika Uwanja wa CCM Mkwakwani ni uwekaji wa nyasi bandia, huku wakipanga kushirikiana na wadau wa soka kufanikisha mpango huo.

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua uwanja huo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurahman, alisema uwekaji wa nyasi bandia unakadiriwa kugharimu kati ya shilingi milioni 400 hadi 500.

Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani humo, ikiwemo ile inayotekelezwa kwa fedha zinazotolewa na Serikali chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa lengo la kupunguza kero kwa wananchi.

Abdurahman aliwataka viongozi wa CCM, ambao ni wamiliki wa uwanja huo, kutumia ubunifu na kushirikiana na wadau wa soka ili kuhakikisha wanapata fedha za kuweka nyasi bandia.

“Tutawaomba wadau wa soka nchini watakapohitajika kutusaidia, kwani dhamira yetu ni njema. Kama ambavyo wamekuwa wakitusaidia hapo awali, tunaamini watashiriki nasi kuhakikisha tunakuwa na uwanja wa kisasa zaidi,” alisema.

Alieleza kuwa maboresho ya uwanja huo yatasaidia kuinua uchumi wa Mkoa wa Tanga, kwani utaweza kutumika kwa mashindano ya kitaifa na kimataifa, ikiwemo CECAFA na michuano mingine ya Afrika.

“Tunapokuwa na uwanja mzuri, hata timu za nje zitakuja kucheza hapa Tanga. Hii itaongeza mzunguko wa fedha na kukuza uchumi wa mkoa wetu,” aliongeza.

Aidha, alikumbusha kuwa uwanja huo uliwahi kufungiwa kutokana na kutokidhi vigezo, hasa ubora wa eneo la kuchezea, akisisitiza kuwa hatua zinazochukuliwa sasa zinalenga kuhakikisha viwango vinazingatiwa kwa usalama wa wachezaji na ubora wa mchezo.

“Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linapofungia uwanja si kwa kupenda, bali kuhakikisha viwango vinazingatiwa. Ndiyo maana tumekuwa wepesi kuchukua hatua za maboresho,” alisema.

Katika hatua nyingine, Abdurahman alieleza kuridhishwa na maendeleo ya ufungaji wa viti 6,500 vilivyotolewa na TFF chini ya Rais wake, Wallace Karia, licha ya kuwepo kwa ucheleweshaji mwanzoni.

Amesema tayari ameagiza kazi hiyo ikamilike ndani ya mwezi mmoja, na kwa sasa inaendelea vizuri chini ya usimamizi wa Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa, Nasoro Makau.

Kwa mujibu wa mpango huo, maeneo ya kipaumbele ni jukwaa kuu pamoja na sehemu za mashabiki wa klabu za Coastal Union na African Sports. Pia wameomba viti vingine 2,500 ili kukamilisha uwanja mzima.

Abdurahman aliishukuru Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, inayoongozwa na Waziri Paul Makonda na Naibu wake Hamisi Mwinjuma, pamoja na Rais wa TFF Wallace Karia, kwa ushirikiano wao katika kuboresha uwanja huo.

Alisisitiza kuwa maboresho hayo yanalenga kuhakikisha klabu za Coastal Union na African Sports zinaendelea kucheza mechi zao za nyumbani mkoani Tanga badala ya kuhamishiwa maeneo mengine.

Aidha, aliwataka mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani kuunga mkono timu zao.

“Haileti maana kuwa na uwanja mzuri halafu mashabiki wanabaki nyumbani kuangalia mechi,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani, Nasoro Makau, alisema hadi sasa wamefikia asilimia 40 ya ufungaji wa viti na wana uhakika wa kukamilisha kazi hiyo ndani ya mwezi mmoja.