HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

VITONGOJI VYOTE MKOA WA KILIMANJARO SASA KUWA NA UMEME

January 31, 2026 Add Comment

 📌 Wananchi wahamasishwa kuanza kufanya wiring kupokea mradi wa vitongojini

📌 Wananchi watakiwa kulinda miundombinu ya umeme

📌 Bilioni 33.5 kupeleka umeme vitongoji 186 Kilimanjaro


Wananchi katika vitongoji 186 ambavyo vinatarajiwa kupelekewa umeme Mkoani Kilimanjaro wamehamasishwa kuanza kufanya maandalizi ya kuupokea mradi huo kwa kuanza kutandaza nyaya ndani ya nyumba zao (wiring).

Rai hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Mkoa wa Kilimnajrao, Mhe. Nurdin Babu wakati wa kikao cha kumtambulisha mkandarasi, Derm Group (T) Limited alieshinda zabuni ya kupeleka umeme kwenye vitongoji 186 vya Mkoa huo katika kipindi cha miaka mitatu.

Mradi huo wa kupeleka umeme katika vitongoji unatekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 33.5.

Kuanza kwa mradi huo wa kupeleka umeme katika vitongoji 186, kutaufanya Mkoa wa Kilimanjaro kuwa na umeme katika vitongoji vyake vyote 2,258.

“Tunamshkuru sana Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake njema ya kutaka kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wote wanapata nishati ya umeme mpaka kwenye ngazi ya kitongoji.

Mkoa wa Kilimanjaro tunaenda kuandika historia kuwa miongoni mwa mikoa 3 inayokwenda kufikisha umeme katika vitongoji vyake vyote. Hii ni heshima kubwa sana. Nitumie fursa hii kuwahamasisha wananchi kuanza kufanya maandalizi ya kupokea umeme pindi mkandarasi atakapoanza kazi rasmi kwa kufanya wiring kwenye nyumba zao,” amesema Mhe. Babu.

Mkuu huyo wa Mkoa pia ametoa rai kwa wananchi kuchangamkia fursa ya uwepo wa umeme kwa kuanzisha biashara mbalimbali ili lengo la serikali la kuboresha maisha ya wananchi wa vijijini kupitia upatikanaji wa nishati ya umeme liweze kutimia.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA ambaye pia ni Mkurugenzi wa Fedha, CPA. Daniel Mungure ametoa wito kwa wananchi kumpa ushirikiano mkandarasi pindi atakapoanza kutekeleza mradi lakini pia kulinda miundombinu ya umeme ambayo imejengwa kwa gharama kubwa.

Kwa upande wake Meneja wa kampuni ya Derm Group, Mhandisi Musa Abdallah ameahidi kukamilisha mradi huo ndani ya muda uliopangwa kimkataba na kwamba atashirikiana karibu na viongozi na wananchi wa maeneo ya mradi.



MBEYA WAPOKEA BILIONI 42.6, KUPELEKA UMEME VITONGOJI 318

January 31, 2026 Add Comment




*📌Idadi ya vitongoji vyenye umeme Mbeya ni 1,970 sawa na asilimia 67%*


*📌Mkandarasi atakiwa kutekeleza mradi huo kulingana Taratibu zilizowekwa*


📍Mbeya


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa ameishukuru Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kwa kupeleka kiasi cha shilingi bilioni 42.6 mkoani Mbeya ili kupeleka umeme kwenye vitongoji 316 kupitia mradi wa HEP 2B unaotekelezwa mkoani humo ili wananchi wanufaike na nishati hiyo. 


RC Malisa amesema mradi huo unakwenda kuleta tija na kuchochea maendeleo ya wananchi wa mkoa huo ambao wataunganishiwa umeme huo kuwawezesha kuendesha shughuli zao za kiuchumi. 

"Gharama ya kuunganisha umeme ni shilingi 27,000 tu. Nawaomba wananchi wa mkoa huu mtumie fursa hii ya kuunganisha umeme iliyoletwa na Serikali kupitia REA.," Amesema RC Malisa. 


Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, Bw. Frank Mugogo amesema jumla ya Vitongoji mkoa wa Mbeya ni 2,951 ambapo vitongoji vyenye umeme ni 1,970 sawa na asilimia 67%. 

Ameongeza kuwa vitongoji ambavyo havina umeme ni 1,981 na vitongoji vilivyopo kwenye mradi huo wa HEP 2B uliotambulishwa mkoani Mbeya ni 316 na vitongoji vitakavyosalia ni 665.

Kwa upande wake, Meneja wa Miradi kutoka kampuni ya White City International Contractors Ltd, Mha.Baraka Mungai ambaye atatekelesa mradi huo ameishukuru Serikali kupitia REA kwa kupewa fursa ya kutekeleza mradi huo. Ameuhakikishia uongozi wa mkoa wa Mbeya kuwa mradi huo utakamilika kwa wakati ili uweze kuleta tija kwa wananchi wa mkoa huo.


AMBONI ADVENTURE RUN, FURSA YA KUTANGAZA MAPANGO YA AMBONI TANGA

January 31, 2026 Add Comment



Na Kassim Nyaki, Amboni Tanga.

Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro imeshiriki na kudhamini mbio za AmbonI Adventure run zilizofanyika leo tarehe 31 Januari 2026 jijini Tanga kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii hususan mapango ya Amboni yanayosimamiwa na Mamlaka yah ifadhi ya Ngorongoro

Mbio hizo za umbali wa kimomita 6, 10 na 20 ambazo zimehudhuriwa na wakimbiaji zaidi ya 500 kutoka maeneo mbalimbali nchini zimeanzia katika viwanja vya Shule ya Sekondari Galanos hadi Mapango ya amboni ambapo washiriki wa mbio hizo wamepata fursa ya kufanya utalii wa ndani katika mapango hayo.

Kaimu meneja uhusiano wa Ngorongoro Hamis Dambaya ambaye ameshiriki mbio hizo kwa kukimbia kilomita 10 ameeleza kuwa Ngorongoro imeamua kuungana na wadau mbalimbali kuendelea kutangaza vivutio vilivyoko katika mapango ya Amboni ili yaendelee kujulikana kitaifa na kimataifa na kuvutia wageni wengi kutembelea na kuona vivutio vinavyopatikana katika mapango hayo na kupataa taarifa mbalimbali ikiwemo historia ya wapigania uhuru. 

Msimamizi wa Mapango ya Amboni Afisa Uhifadhi Daraja la kwanza Ramadhan Rashid ameeleza kuwa baadhi ya vivutio vinavyopatikana katika Mapango ya Amboni  ni pamoja na maumbo ya asili ya kijiolojia, vivutio vilivyochongwa na maji kama meli, mlima Kilimanjaro, kanisa, msikiti, shughuli za kimila na mataambiko, ndege ndani ya mapango, pango la jinsia, Pango la fatuma ambalo watu hulitumia kuomba mchumba wa kuoa, mimea ya aina mbalimbali, mto pamoja na mazingira asilia yanayopaambwa naa upepo mwanana wa bahari ya hindi.

Mkuugenzi wa Kale Amboni Caves Sophia Mulamula ameeleza kuwa Mbio za Amboni Adventure Run ambazo zimefanyika kwa msimu wa tatu na kuhudhuriwa na wakimbiaji takriban 500 zinatendelea kuboreshwa ili kuvutia wakimbiaji wengi zaidi mwaka ujao 2027 


“Tumefanya tathmini kwa miaka hii miwili tumeona mbio hizi zinavutia watu wengi, tunaamini mwakani tunaboresha vitu vingi zaidi ili tupate wakimbiaji wengi kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii, kutangaza nchi yetu lakini kuendelea kuhamasisha utalii wa michezo” alilisitiza Mulamula.






Diamond Akiri Umuhimu wa JAB, Wasafi Media Yakubali Kutii Sheria ya Habari

January 31, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi wa Wasafi Media, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz, ameipongeza Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kwa kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, huku akiahidi kuwa vyombo vyake vya habari viko tayari kufuata kikamilifu matakwa yote ya kisheria yanayoongoza sekta ya habari nchini.

Diamond ametoa kauli hiyo baada ya kufika katika ofisi za Bodi ya Ithibati kwa ajili ya kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari, akisema Wasafi Media haina nia ya kukwepa sheria bali ina dhamira ya kushirikiana kwa karibu na wasimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari.

Amesema licha ya Sheria hiyo kuleta changamoto kwa baadhi ya vyombo vya habari na watumishi wake, bado haiwezi kupingwa kwani ilitoa muda wa kutosha kwa wadau wote kujipanga na kutimiza vigezo vilivyowekwa, ikiwemo sharti la waandishi wa habari kuwa na kiwango cha elimu cha kuanzia Diploma na kuendelea.
Diamond amekiri kuwa kuanzishwa kwa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari kumeleta nidhamu na uwajibikaji mkubwa katika taaluma ya habari, akisisitiza kuwa Wasafi Media inaunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha weledi, maadili na heshima ya taaluma hiyo inalindwa.

“Sisi hatutaki kukwepa utekelezaji wa Sheria. Hakuna namna unaweza kuvunja Sheria na ukabaki salama. Tumehakikisha watumishi wetu wote wanazingatia Sheria na katika hilo sina utani,” amesema Diamond.

Aidha, amesema hapo awali alipata taarifa na tafsiri tofauti kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, hali iliyosababisha sintofahamu kwa baadhi ya wadau, lakini baada ya kufika katika ofisi za Bodi na kupewa ufafanuzi wa kina, ameelewa vyema dhamira ya Serikali ya kuimarisha taaluma ya habari nchini.

Amepongeza pia msimamo wa Waziri mwenye dhamana aliyesisitiza kuwa Bodi ya Ithibati ni mlezi wa waandishi wa habari, akisema baada ya mazungumzo na uongozi wa Bodi, ameridhishwa kuwa taasisi hiyo ipo kwa ajili ya kulinda na kukuza taaluma hiyo, si kuibana.
“Nakiri wazi kuwa Bodi ni mlezi kwa waandishi wa habari. Baada ya kuielewa Sheria vizuri, hakuna sababu ya kupingana nayo. Watu wangu tayari wamechukua hatua stahiki na wamerejea vyuoni kujiendeleza kielimu,” amesema Diamond, akisisitiza umuhimu wa mawasiliano mazuri kati ya wadau wa sekta ya habari na wasimamizi wa Sheria.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, amesema Sheria ya Huduma za Habari ilitungwa mwaka 2016 na Serikali ilitoa kipindi cha mpito cha miaka mitano kwa waandishi na taasisi za habari kutimiza matakwa ya kisheria.

Ameeleza kuwa kipindi hicho kiliongezwa kwa miaka miwili na baadaye miaka mingine mitatu, hivyo kufikisha jumla ya miaka kumi, muda ambao Serikali inaamini ulikuwa wa kutosha kwa wadau wote wa sekta ya habari kujiandaa na kutekeleza Sheria hiyo kikamilifu.

Wakili Kipangula amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unalenga kujenga sekta ya habari yenye weledi, maadili na heshima, sambamba na kulinda maslahi ya waandishi, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla.

MMOMONYOKO WA MAADILI KWA JAMII KWAWAIBUKA TAASISI YA SUBRA NA NUSRA KUJA NA KONGAMANO MAALUMU

January 31, 2026 Add Comment

 


Kutokana na kuporomoka  mmomonyoko wa maadili katika jamii, wanawake wa Kiislamu mkoani Tanga wameanzisha majadiliano na mikakati maalum ya kutafuta suluhisho la changamoto hiyo, sambamba na maandalizi ya kuupokea mwezi mtukufu wa Ramadhani.


Kupitia Taasisi ya Subra na Nusra, wanawake hao wameandaa kongamano maalum litakalofanyika Jumamosi hii katika Ukumbi wa Simba Mtoto, jijini Tanga, likilenga kuwaandaa wanawake kiroho na kijamii ili kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia mafundisho ya Mtume Muhammad (SAW).


Mratibu wa kongamano hilo, Bi Mwanakombo Abdallah Kipanga, alisema lengo kuu ni kutoa elimu kwa jamii, hususan wanawake, kuhusu umuhimu wa maadili mema na maandalizi sahihi ya mwezi wa Ramadhani.



“Huu si mwezi wa kawaida. Tunataka wanawake wapate elimu itakayowasaidia kuimarisha imani, malezi ya watoto na maadili ndani ya familia na jamii kwa ujumla,” alisema.




Alisema Mufti Abubakar Bin Zuberi anatarajiwa kuwa mgeni wa heshima, huku Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk Batilda Burian, akiwa mgeni rasmi. Hili litakuwa kongamano la nne kufanyika chini ya taasisi hiyo.


Bi Kipanga aliongeza kuwa jitihada hizo zimeungwa mkono pia na wanawake wenye asili ya Tanga wanaoishi Dar es Salaam, walioungana kuimarisha maandalizi ya kongamano hilo.




Miongoni mwa mada zitakazojadiliwa ni maandalizi ya wanawake katika mwezi wa Ramadhani, kujenga hofu ya Mungu, malezi bora ya watoto pamoja na umuhimu wa kuzingatia maadili mema katika maisha ya kila siku.


Aliwataka wanawake wa Kiislamu pamoja na wa dini nyingine kujitokeza kwa wingi kushiriki kongamano hilo.
Naye mjumbe wa kamati ya maandalizi, Bi Shamsi Diwani kutoka Dar es Salaam, alisema kuna haja ya dharura kwa wanawake kuungana kupambana na kuporomoka kwa maadili kunakojitokeza katika jamii.


“Ni wakati wa kusaidiana kurejesha maadili mema. Inasikitisha kuona mienendo isiyofaa na burudani zinazokiuka maadili zikizidi kushika kasi katika jamii,” alisema.


Aliongeza kuwa wako tayari kukaa pamoja na wanawake na kujadili kwa kina chanzo cha changamoto hiyo ili kupata suluhisho la kudumu.


Bi Diwani pia alielezea wasiwasi wake juu ya kuongezeka kwa migogoro ya ndoa na kuvunjika kwa familia, akisema si jambo jema kushuhudia baadhi ya wanawake wakisherehekea talaka.
“Hili si jambo la kufurahia. Ingawa talaka inaruhusiwa, si tukio la kushangiliwa,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Bi Kibibi Saidi Kibao aliwahimiza wanawake kuhudhuria ili kunufaika na mafunzo yatakayotolewa na Mashehe maarufu pamoja na mke wa Mufti wa Kwanza, Sheikh Jumaa.
Naye mjumbe mwingine wa kamati, Bi Hawa Mweri, alisisitiza umuhimu wa wanawake wa Kiislamu kudumisha maadili mema wakati wote, si kipindi cha Ramadhani pekee.
MWISHO

UDSM: WANAFUNZI WA UANDISHI WA HABARI WAKUMBUSHWA UMUHIMU WA ITHIBATI NA SHERIA

January 30, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amewahimiza wanafunzi wa uandishi wa habari kusoma, kuielewa na kuizingatia Sheria ya Huduma za Habari ili kujijenga kitaaluma na kuepuka migongano ya kisheria wanapoingia kwenye tasnia ya habari.

Wakili Kipangula ametoa wito huo wakati akitoa mhadhara kwa wanafunzi wa Mwaka wa Pili wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma, uliofanyika Januari 30, 2026, chuoni hapo. Mhadhara huo ulilenga kuwaongezea uelewa wanafunzi kuhusu majukumu ya JAB na misingi ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229.

Katika wasilisho lake, Wakili Kipangula ameeleza kuwa JAB ina jukumu la kusimamia ithibati ya waandishi wa habari nchini, kulinda taaluma ya uandishi wa habari na kuhakikisha maadili na weledi vinazingatiwa. Amesisitiza kuwa wanafunzi na waandishi chipukizi wanapaswa kuifahamu Sheria ya Huduma za Habari kabla ya kuanza kazi rasmi ili kujiepusha na makosa yanayoweza kuathiri taaluma yao.

Ameeleza pia kuwa ithibati na vitambulisho vya uandishi wa habari ni muhimu kwa wanafunzi wanapokuwa kwenye mafunzo kwa vitendo (field), akisisitiza kuwa uwepo wa nyaraka hizo unatoa uhalali wa kisheria katika utekelezaji wa majukumu ya kihabari, hususan wanapokuwa wakikusanya habari katika maeneo mbalimbali.
Akijibu swali kutoka kwa wanafunzi kuhusu mafunzo katika vyombo vya habari vya vyuo, ikiwemo Mlimani Radio na Televisheni pamoja na SAUT, Wakili Kipangula amesema Sheria inatambua uwepo wa wanafunzi katika vituo hivyo kwa kipindi maalumu cha mafunzo. Amesema baada ya kukamilisha muda wa mafunzo kwa vitendo, wanafunzi wanapaswa kurejea katika ratiba yao ya kawaida ya masomo chuoni.

Mhadhara huo umeelezwa kuwa sehemu ya juhudi za JAB katika kujenga uelewa wa kisheria kwa waandishi wa habari chipukizi, hatua inayolenga kuimarisha weledi, uwajibikaji na heshima ya taaluma ya uandishi wa habari nchini.

MATI FOUNDATION YAREJESHA FAIDA KWA JAMII, KAYA 2,000 KUNUFAIKA MANYARA

January 30, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Manyara

Zaidi ya kaya 2,000 zenye uhitaji maalum mkoani Manyara zinatarajiwa kunufaika na msaada wa vyakula unaotolewa na Mati Foundation, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kampuni ya Mati Super Brands Ltd wa kurejesha sehemu ya faida yake kwa jamii inayozunguka maeneo ya uzalishaji na biashara zake.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada wa awamu ya kwanza kwa kaya 37 katika Kata ya Bagara, Wilaya ya Babati, Meneja wa Mradi wa Mati Foundation, Isack Piganio, amesema mpango huo unalenga kusaidia makundi yaliyo katika mazingira magumu, yakiwemo kaya zenye mahitaji maalum, ili kupunguza changamoto za maisha wanazokabiliana nazo kila siku.
Piganio ameeleza kuwa msaada huo wa vyakula ni sehemu ya dhamira ya taasisi hiyo kushiriki kikamilifu katika juhudi za kijamii kwa kushirikiana na Serikali na wadau wengine wa maendeleo, huku akisisitiza kuwa lengo la sasa ni kuongeza wigo wa msaada huo ili kuwafikia walengwa wengi zaidi.

“Lengo letu ni kuhakikisha kaya nyingi zaidi zenye uhitaji zinanufaika. Tunatarajia kufikia takriban kaya 2,000 ifikapo mwisho wa mradi huu wa msaada wa vyakula,” amesema Piganio.

Baadhi ya wanufaika wa msaada huo wameeleza kufurahishwa na hatua hiyo, wakipongeza juhudi zinazofanywa na Mati Super Brands Ltd kupitia taasisi yake ya Mati Foundation kwa kuwakumbuka wananchi wenye uhitaji, hususan wale wanaoishi katika maeneo yanayozunguka kiwanda hicho.

Wanufaika hao wamesema msaada wa vyakula walioupokea utawapunguzia kwa kiasi kikubwa changamoto za kimaisha, hasa katika kipindi cha ugumu wa upatikanaji wa mahitaji ya msingi, na wameishukuru kampuni hiyo kwa moyo wa kujali na kugusa maisha ya wananchi wa kawaida.
Viongozi mbalimbali wa Serikali waliokuwa mashuhuda wa zoezi hilo wameipongeza Mati Foundation kwa moyo wa kujitolea na ushirikiano wake na Serikali katika kutatua changamoto za kijamii, wakisema mchango huo ni mfano mzuri wa sekta binafsi kushiriki katika maendeleo ya jamii.

Viongozi hao wamesisitiza kuwa ushirikiano wa aina hiyo unasaidia kuimarisha ustawi wa jamii na kupunguza mzigo kwa Serikali katika kuwahudumia wananchi wenye uhitaji.
Mati Foundation ni taasisi isiyo ya kiserikali iliyo chini ya kampuni mama Mati Super Brands Ltd, inayojihusisha na uzalishaji na usambazaji wa vinywaji changamshi mbalimbali nchini. Miongoni mwa bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo ni pamoja na Strong Dry Gin, Sed Pineapple Flavoured Gin, Strong Coffee, Tai Original Portable Spirit, Tanzanite Premium Vodka na Tanzanite Royal Gin.

Kupitia Mati Foundation, kampuni hiyo imeendelea kutekeleza programu mbalimbali za kijamii zenye lengo la kuinua ustawi wa jamii na kuchangia maendeleo endelevu katika maeneo inayofanyia shughuli zake.

NGORONGORO SAKO KWA BAKO NA TAASISI ZA ELIMU KUTANGAZA VIVUTIO VYA UTALII NA ELIMU YA UHIFADHI

January 30, 2026 Add Comment


Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro leo tarehe 30 Januari, 2026 imeendelea na kampeni ya kutoa elimu ya vivutio vya utalii vilivyopo Ngorongoro na elimu ya uhifadhi endelevu kwa wanafunzi na walimu wa shule za Sekondari Manyara, Lowasa , Rift valley na Chuo cha Maendeleo ya wananchi FDC Mto wa Mbu ambapo taasisi zote zipo Wilaya ya Monduli Mkoani Arusha.