HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts
TANZANIA,BURUNDI ZAZINDUA UJENZI WA RELI YA SGR UVINZA- MUSONGATI
habari*_Kugharimu dola za Marekani bilioni 2.154_*
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa leo (Jumamosi, Agosti 16, 2025) ameshiriki uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa reli ya kisasa ya kutoka Uvinza hadi Musongati na kuwahahikishia Watanzania na WanaBurundi kwamba ujenzi huo utaanza katika muda uliopangwa.
Waziri Mkuu ambaye ameshiriki hafla hiyo kwa niaba ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema reli hiyo itakayokuwa na urefu wa km.240 pindi ikikamilika, itakuwa ndiyo reli ya kwanza inayounganisha nchi na nchi katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika eneo la Musongati, Burundi, Waziri Mkuu amesema kukamilika kwa ujenzi wa reli hiyo kutasaidia kuunganisha masoko na kuendeleza biashara baina ya Tanzania na Burundi.
"Reli ikikamilika itafungua fursa kwa wananchi wetu ambao wataweza kutoka hapa hadi Dar es Salaam ndani ya siku moja. Hata kwenye usafirishaji wa mizigo, hivi sasa, lori linatumia saa 96 kutoka Dar hadi Bujumbura lakini baada ya kukamilisha ujenzi, usafirishaji wa mizigo kwa kutumia treni utatumia saa 20 tu."
"Mradi wa reli ya kisasa siyo tu kwamba utarahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo, bali pia utafungua milango ya fursa mpya za uwekezaji na biashara kati ya Tanzania na Burundi."
Akielezea kuhusu mradi huo, Waziri Mkuu amesema ujenzi wa reli hiyo utagharimu dola za Marekani bilioni 2.154 na unatarajiwa kukamilika ndani ya miaka mitano na kwamba mwaka mmoja baada ya ujenzi utakuwa ni wa matazamio.
Kwa upande wake, Rais wa Burundi, Meja Jenerali Evarist Ndayishimiye alisema kuanza kwa ujenzi wa reli hiyo kutatibu shauku ya muda mrefu ya nchi hiyo kuwa na usafiri wa reli.
"Leo ni siku ya furaha sana kwetu. Tumepata jawabu la tangu enzi na enzi. Mwaka 1921, mradi huu ulianzishwa na Wabelgiji kisha wakaja Wajerumani lakini wakashindwa. Leo hii Tanzania na Burundi tumeweza," alisema.
Alisema nchi yake imebarikiwa kuwa madini mengi na kuna wakati aliitisha kikao cha wawekezaji kutoka nchi kadhaa. "Wengi walivutiwa na wakataka kuwekeza mara moja, lakini wakaniuliza, tukianza kuchimba madini ya Nickel, tutayasafirishaje?"
"Hiyo changamoto ilitufanya tubungue bongo zetu na kutafuta suluhisho. Tunaishukuru sana Serikali ya Tanzania kwa kukubali kuungana nasi ili tuanze mradi huu muhimu. Tukitoka hapa, tunataka reli iunganishe hadi Kindu, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC). Na baada ya hapo, tunataka reli yetu ifike Afrika Magharibi kwenye ufukwe wa bahari ya Atlantiki kwani tunaamini njia hiyo itaharakisha kuleta maendeleo."
Rais Ndayishimiye alimpongeza Rais Dkt. Samia kwa kufikia hatua kubwa za maendeleo. "Ukirudi nyumbani mwambie Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan kwamba tunampongeza sana kwa kuleta maendeleo ya haraka nchini Tanzania."
"Nimekaa Tanzania kwa muda mrefu lakini kwa sasa nikija naweza kupotea. Magomeni napajua, Tabata na Vingunguti napajua, Mwenge napajua, na Kinondoni nilishakaa; lakini kwa sababu ya maendeleo yaliyopatikana, naweza kupotea. Tunamshukuru kwa uongozi wake imara,"
Rais huyo alizungumza kwa Kiswahili na kuamsha shangwe miongoni mwa wananchi waliohudhuria tukio hilo.
Mapema, Waziri wa Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa alisema utekelezaji wa mradi huo unaenda sambamba na Ajenda 63 ya Umoja wa Afrika ambayo inataka bara la Afrika liunganishwe kwa mtandao wa reli ya kisasa.
Alisema mbali na kuziunganisha nchi hizo mbili, kukamilika kwa ujenzi wa reli hiyo, kutarahisisha kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo. "Hivi sasa, kontena moja la futi 20 linasafirishwa kwa gharama ya dola za Marekani 3,800 lakini reli ikikamilika, gharama itashuka hadi dola za Marekani 2,000.
Alisema faida nyingine itakayopatikana baada ya mradi huo kukamilika ni kuwezesha kusafirisha mizigo mingi kwa wakati mmoja. "Hivi sasa, mzigo unaosafirishwa kwa lori moja ni tani 30, lakini reli ikianza kazi, tutaweza kusafirisha tani 3,000 kwa wakati mmoja," alisema Waziri Mbarawa.
(Mwisho)
Imetolewa na
Ofisi ya Waziri Mkuu,
Jumamosi, Agosti 16, 2025
WAANDISHI WA HABARI DODOMA WAPATIWA MAFUNZO YA USALAMA NA ULINZI
habariBaadhi ya waandishi wa habari kutoka Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dodoma (Dodoma Press Club) wamepatiwa mafunzo ya usalama wa kimwili, kidijitali na afya ya akili, kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kujilinda binafsi katika mazingira ya kazi.
Mafunzo hayo yalifanyika Agosti 16, 2025, yakiongozwa na Mkufunzi wa Usalama na Ulinzi, Okuly Julius, ambaye pia ni mwandishi wa habari. Okuly alipata mafunzo hayo kupitia Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na kisha kupewa jukumu la kuwajengea uwezo waandishi wenzake katika mikoa.
Akizungumza kwenye mafunzo hayo, Okuly amesema waandishi wa habari wanapaswa kuwa makini na kuchukua tahadhari muda wote kwani usalama huanzia kwa mwandishi mwenyewe.
“Ni muhimu kuchukua tahadhari kubwa dhidi ya mashambulizi ya kimtandao kwa kuhakikisha viunganishi vinavyopokelewa vinathibitishwa kabla ya kubofya, kutumia nywila imara na kuweka uthibitishaji wa hatua mbili. Waandishi wanapaswa kuwa makini zaidi hasa kuelekea uchaguzi mkuu wa Oktoba 2025, kipindi ambacho mara nyingi huambatana na vitisho, ukatili na hata kukamatwa kiholela,” alisema Okuly.
Ameongeza kuwa ni vyema waandishi kutoa taarifa kwa watu wa karibu au wenzao wanapokwenda kwenye kazi, ili kuepuka hatari zinazoweza kutokea endapo watapatwa na matatizo wakiwa peke yao.
Kwa upande wao, baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo akiwemo Bahati Msanjila (Crown Media), Saida Issa (Gazeti la Zanzibar Leo), Rhoda Simba (Channel Ten), Gideon Gregory (Jambo FM) na Joyce Kasiki (Gazeti la Majira), walisema yamewajengea uwezo mkubwa na sasa wanafahamu mbinu bora za kufanya kazi kwa usalama.
Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa “Empowering Journalists for Informed Community” (Kuwawezesha Waandishi wa Habari ili Jamii Iweze Kupata Taarifa Sahihi) unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) na Shirika la Maendeleo la Uswisi (SDC). Mradi huu unatekelezwa kwa ushirikiano wa International Media Support (IMS), Union of Tanzania Press Clubs (UTPC) na JamiiAfrica.
TUKITUMIA NISHATI SAFI YA KUPITIKIA TUTAOKOA HEKTA 400,000 ZA MISITU ZINAZOTEKETEA KWA MWAKA -MJIOLOJIA NSAJIGWA
habari📌 *Awanoa Wanawawake na Wajasiriamali Songwe kuhusu Nishati Safi ya Kupikia*
📌 *Atoa wito kwa Wadau kushirikiana na Wizara ya Nishati kutoa elimu ya Nishati Safi ya Kupikia*
Songwe
Imeelezwa kuwa matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia si tu yanahatarisha afya bali pia yanachochea uharibifu wa mazingira ambapo takribani hekta 400,000 za misitu hupotea kila mwaka nchini kutokana na ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa, jambo linalochangia kuongezeka kwa ukame na mabadiliko ya tabianchi.
Hivyo, Watanzania wameaswa kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuachana na matumizi ya nishati isiyo safi kama kuni na mkaa kutokana na athari zake kwa binadamu na mazingira.
Wito huo umetolewa leo Agosti 16, 2025, na Mjiolojia kutoka Wizara ya Nishati, Nsajigwa Maclean, wakati akitoa elimu ya Nishati Safi ya Kupikia kwa Wajasiriamali mkoani Songwe.
Amesema kwa mujibu wa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, ni asilimia 16 tu ya Watanzania ndio wanaotumia nishati safi ya kupikia, hivyo bado kuna magonjwa yanayotokana na moshi wa kuni na mkaa, ambayo yanasababisha vifo vya zaidi ya watu 33,000 kwa mwaka nchini.
Katika ngazi ya kimataifa, amesema watu bilioni 2.1 hawana upatikanaji wa nishati safi ya kupikia, huku zaidi ya watu milioni 3 wakifariki dunia kila mwaka kutokana na madhara ya kiafya yanayotokana na nishati isiyo safi ya kupikia ambapo Kusini mwa Jangwa la Sahara zaidi ya watu milioni 960 hawana nishati hiyo.
Aidha amebainisha kuwa kuna dhana potofu miongoni mwa jamii kuwa chakula kinachopikwa kwa kutumia gesi au umeme hakiwi na ladha nzuri, jambo ambalo amesema halina msingi wa kisayansi na linaendelea kuwazuia wananchi wengi kufanya mabadiliko kuelekea matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Ameeleza kuwa Wizara ya Nishati imeweka mkakati wa kitaifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ili kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2034 asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia, huku mkakati huo ukiangazia mafanikio kutoka nchi nyingine kama India na Ghana, ambazo zimepiga hatua katika kuhimiza matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Imeelezwa pia kuwa changamoto kubwa kwa wananchi si kutotaka kutumia nishati safi ya kupikia bali wanahitaji elimu pia kuhusu matumizi ya nishati hiyo hivyo ametoa wito kwa Wadau kushirikiana na Serikali katika kutekeleza Mkakati wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia.
Katika semina hiyo wanawake na wajasiriamali walihimizwa kuwa mabalozi wa mabadiliko kwa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia si kwa ajili ya afya pekee, bali pia kwa ajili ya kulinda mazingira na kizazi kijacho.
“SERIKALI IMEENDELEA KUBORESHA MAZINGIRA YA KUJIFUNZIA NA KUFUNDISHIA” MWAMBENE
habariTANZANIA YAPONGEZWA KUONGOZA JUHUDI ZA KUTAFUTA AMANI, SADC
habariSERIKALI YAFUNGUA MILANGO YA FURSA KWA WAKULIMA WA MWANI
habariNA. MWANDISHI WETU – TANGA
SERIKALI imewataka wakulima wa mwani nchini kutumia mbinu bora na za kisasa za kilimo ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo na kuongeza ushindani katika masoko ya ndani na nje ya nchi.
Hayo, yamebainishwa na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Bunge na Uratibu, Dkt. James Kilabuko wakati akifunga mafunzo ya kujenga uwezo kwa vikundi vinavyojihusisha na kilimo cha mwani yaliyofanyika Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga kwa muda wa siku kumi na mbili kuanzia tarehe 04 hadi 15 Agosti,2025.
“Mafunzo mliyojifunza ya kilimo bora cha mwani yatawasaidia kuongeza kiwango cha uzalishaji na ubora wa mwani katika soko la ndani na nje ya nchi,” alisema na kuongeza kuwa, “Mafunzo ya uongezaji thamani, matumizi bora ya kemikali mnazotumia kutengeneza bidhaa mbalimbali zitokanazo na mwani, vifungashio vya bidhaa, zitazoweza kuwatambulisha na kuzitangaza bidhaa zenu ndani na hata nje ya nchi, upatikanaji wa masoko ya mwani” Alisema Dkt. Kilabuko.
Pia Dkt. Kilabuko alisema lengo la kuandaa mafunzo hayo ni kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wakulima wa mwani ili kuongezea mnyororo wa thamani wa zao hilo nchini.
Vilevile, aliwataka wakulima hao kujipangia utaratibu wa kufikisha maarifa waliyoyapata kwa wanakikundi wengine ambao hawakupata fursa ya kupata mafunzo hayo kwa kufanya mazoezi katika vikundi vyao hususani mafunzo ya wokozi na huduma ya kwanza majini.
“Mazingira ya kazi zenu ni katika maji, hivyo suala mlilojifunza la namna ya kujiokoa shambani ni muhimu sana, elimu hiyo itawasaidia katika kuokoa maisha yako binafsi pamoja na jirani yako pindi anapopata changamoto akiwa katika shughuli za kilimo shambani” Alisema na kuongeza kuwa,” “kile mlichojifunza muwafikishie na wenzenu ili kuwa na uwelewa wa pamoja katika kuboresha maslahi ya pamoja ya vikundi vyenu”.
Awali akitoa neno la utangulizi kuhusu mafunzo haya Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Bunge na Uratibu Kanali Selestine Masalamado amesema Kuwa mafunzo haya yaliyofanyika wilayani Mkinga ni awamu ya pili ya sehemu ya utekelezaji wa mwongozo wa kukabiliana na vitendo vya kihalifu katika bahari na maziwa makuu kwa lengo la kuimarisha ulinzi na usalama katika maeneo hayo uliozinduliwa Februari 2023 na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa.
“sehemu ya kwanza ulitekelezwa katika Wilaya tatu ikiwa ni pamoja na Mafia, Pangani na Bagamoyo ambazo shughuli zake kuu za kiuchumi zinategemea mazao ya bahari kwa kutoa mafunzo kwa vikundi na vyama vya ushirika, ujenzi wa vichanja vya kukaushia dagaa, na ununuzi wa boti moja ya kisasa kwa ajili ya doria baharini,”. Alisema Kanali Masalamado.
Aliongezea kuwa Kutokana na Mafanikio Makubwa wa awamu ya kwanza wa mradi wa kuimarisha ulinzi na usalama , Serikali ya Japan na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) wameendelea kuunga mkono juhudi za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuimarisha usalama majini kwa kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa boti mbili za doria, ujenzi wa makaushio ya mwani na mashine ya kusaga mwani, pamoja na kutoa mafunzo elekezi kwa vikundi 26 vya wakulima wa mwani katika Wilaya ya Mkinga.
Naye, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga Bw. Rashid Karim Gembe amepongeza uwepo wa mafunzo na kutoa shukrani za dhati kwa wafadhili pamoja na waratibu wa mafunzo hayo yatakayo leta mapinduzi ya mnyororo wa thamani wa zao la mwani na kuwakomboa kiuchumi wakulima wa mwani, hivyo ameahidi kuendelea kuwashika mkono wakulima wa mwani kwa kuwahakikishia ushirikiano utakao wawezesha kuyafikia malengo kupitia zao hilo.
Kwa upande wake Mwakilishi kutoka Shirika la Maendelo la Umoja wa Mataifa (UNDP) Bw. Saimon Nkonoki amesema kuwa, awamu ya pili ya sehemu ya mradi ambao umeanza kwa mafunzo wilayani Mkinga umepokelewa vizuri kwa muitikio na ushirikiano mkubwa ikiwa ni ishara ya utayari wa Serikali katika kuwahudumia wananchi wake.
“Tunaahidi kuendeleza ushirikiano huu kwa wadau mbali mbali wa maendeleo hapa nchini, huku tukitoa rai kwa vikundi vilivyonufaika na mafunzo haya kuyaishi kwa vitendo hasa yale ya vitendo tunaamini yatawasaidia sana”. Alisema Bw. Nkonoki
Kwa upande wao washiriki wa mafunzo haya wameshukuru mafunzo yaliyotolewa kwao huku wakieleza namna yatavyowasaidia wakulima wa zao la mwani kwa ujumla na kueleza yatawafaa wao na jamii nzima.
Akiongea kwa niaba ya washiriki wenzake Bi. Aisha Jumbe amesema, “tunaamini zao hili tunaenda kulipa heshima kwa kupitia mafunzo haya, ambapo tutakuwa na mbinu mpya za huduma za kifedha, kujua soko na mahitaji ya soko, uandaaji wa fedha na utunzaji wa fedha na hii itatusaidia katika hatua zote za kilimo hadi kufikia matokeo ya mwisho kwa watumiaji wa bidhaa zetu ikiwemo; sabuni za kuogea, kufua, kusafisha maliwato, dawa kwa magonjwa mbalimbali na nyingine nyingi;”.
Mafunzo hayo ya kuvijengea uwezo wa kilimo bora, usimamizi wa vikundi, usimamizi wa fedha,utunzaji kumbukumbu, kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao pamoja na masoko ya zao la mwani kwa vikundi vya wanawake na vijana vya wakulima wa zao la mwani wa Wilaya ya Mkinga, Mkoani Tanga, yameratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini kwa ufadhili wa Serikali ya Japan pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).
=MWISHO=
ELIMU YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA YAWAFIKIA WANAWAKE MKOANI MBEYA
habari📌 *Ni kupitia Kongamano la Wanawake na Fursa za Kiuchumi*
📌 *Wizara ya Nishati yasisitiza matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ili kulinda afya na mazingira*
Mbeya.
Serikali kupitia Wizara ya Nishati imetoa wito kwa wananchi kuachana na matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia na kutumia nishati safi ya kupikia kama vile umeme na gesi ikiwa ni njia pia ya kulinda afya, mazingira na kuimarisha uchumi wa kaya.
Wito huo umetolewa leo na Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka Wizara ya Nishati, Ndg. Deo Alex katika Kongamano la Wanawake na Wajasiriamali kuhusu fursa za kiuchumi lililofanyika mkoani Mbeya.
Ndg. Deo Alex amesema kuwa mwaka 2022 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, alitoa maelekezo ya kuandaliwa kwa Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ikiwa ni mwanzo wa safari ya kuelekea katika matumizi ya nishati iliyosafi ya kupikia.
Ameeleza kuwa kufuatia agizo hilo, Wizara ya Nishati iliandaa mkakati huo na kuuzindua rasmi mwaka 2024 ambapo utekelezaji wake umeanza rasmi.
Ameeleza kuwa, kwa mujibu wa mkakati huo, matumizi ya nishati isiyo safi yameonekana kuwa chanzo kikuu cha athari mbalimbali, ikiwemo uharibifu wa mazingira na matatizo ya kiafya kwa watumiaji, miongoni mwa athari za kiafya zilizobainishwa ni pamoja na saratani, homa za mapafu, ujauzito kuharibika na kujifungua watoto kabla ya muda.
Ameeleza kuwa gharama za kumtibu mtu mwenye saratani ni kubwa ukilinganisha na gharama ya ununuzi wa nishati safi ya kupikia kama vile mtungi wa gesi, hivyo wananchi wanahimizwa kuwekeza katika matumizi ya nishati salama kwa ajili ya afya zao na mazingira,
Ndg. Alex amebainisha kuwa mkakati huo umefungua fursa mbalimbali kwa wajasiriamali, ikiwa ni pamoja na kuwa mawakala wa gesi na nishati nyingine mbadala.
Amezitaja aina za nishati safi zinazopendekezwa kuwa ni pamoja na umeme, gesi na mkaa mbadala.
Wanawake mbalimbali waliohudhuria Kongamano hilo kwa nyakati tofauti wameishukuru Wizara ya Nishati kwa kuwapa elimu hiyo ya Nishati Safi ya Kupikia na kutoa wito kuwa iendelee hadi ngazi ya vijiji.
Kongamano hilo limeandaliwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, likiwa na kauli mbiu isemayo “Changamkia Fursa, Jenga Leo na Kesho Yako.”
MPINA WA ACT WAZALENDO ACHUKUA FOMU ZA UTEUZI INEC KUWANIA KITI CHA RAIS
Wanachama wa chama cha ACT Wazalendo waliohudhurio utoaji fomu wakiwa ukumbini.