
MTANDAO WATWAA ASILIMIA 44 YA MAWASILISHO YA SAMIA KALAMU
habari
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi,akitoa taarifa kwa umma kuelekea kuhitimisha maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake Juni 19,2026 jijini Dodoma.
...
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) linatarajia kuandika historia mpya Juni 19, 2026 kwa kuhitimisha maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, huku likitarajia kuzindua kitabu maalumu kitakachobeba historia, mafanikio na mchango wake katika maendeleo ya viwanda, biashara na ustawi wa Watanzania.
Akizungumza jijini Dodoma kuhusu maandalizi ya kilele cha maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Ashura Katunzi, amesema hafla hiyo itafanyika katika ofisi za shirika hilo na inatarajiwa kuhudhuriwa na wadau mbalimbali kutoka sekta za umma na binafsi.
Dkt. Katunzi amesema mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho hayo anatarajiwa kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Salvio Kapinga (Mb), ambaye ataungana na viongozi, wadau na wananchi kusherehekea mafanikio ya nusu karne ya taasisi hiyo muhimu nchini.
Amesema sambamba na sherehe hizo, TBS itazindua kitabu maalumu cha miaka 50 kitakachoelezea safari ya shirika hilo tangu kuanzishwa kwake, hatua mbalimbali za maendeleo iliyopitia pamoja na mchango wake katika kuhakikisha bidhaa na huduma zinazotolewa nchini zinazingatia viwango vinavyotakiwa.
“Kitabu hiki kitakuwa sehemu ya kumbukumbu muhimu ya taifa. Kitaelezea historia ya TBS, mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 50 na kitakuwa rejea kwa vizazi vya sasa na vijavyo ili kuelewa mchango wa shirika katika maendeleo ya nchi,” amesema Dkt. Katunzi.
Ameeleza kuwa kwa kipindi cha miaka 50, TBS imeendelea kuwa mhimili muhimu katika kulinda afya na usalama wa watumiaji wa bidhaa mbalimbali, huku ikichochea ukuaji wa viwanda kwa kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa nchini zinakuwa bora na zenye ushindani katika masoko ya ndani na nje ya nchi.
Kwa mujibu wa Dkt. Katunzi, mafanikio yaliyofikiwa na TBS katika kipindi hicho si ya shirika pekee bali ni matokeo ya ushirikiano mkubwa kati ya taasisi hiyo, wadau wa maendeleo, sekta binafsi na wananchi kwa ujumla.
“Miaka 50 ya TBS ni mafanikio ya wadau wetu na jamii kwa ujumla. Tunawakaribisha wananchi na wadau wote kushiriki katika kilele cha maadhimisho haya ili kwa pamoja tuadhimishe safari hii ya mafanikio,” amesema.
Maadhimisho hayo yanatarajiwa kuwa fursa ya kutafakari mchango wa TBS katika maendeleo ya taifa, huku yakitoa mwanga wa matarajio na mwelekeo wa shirika hilo katika kuendelea kuimarisha ubora wa bidhaa na huduma kwa manufaa ya Watanzania na uchumi wa nchi.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amelitaka Shirika la umeme Tanzania ( TANESCO) kuongeza vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia nishati ya umeme ili kuongeza wigo wa utoaji huduma hiyo ambayo imeonekana kuleta mageuzi katika matumizi ya nishati safi.
Mhe. Ridhiwani ameyasema hayo Juni 17, 2026 alipotembelea Banda la TANESCO katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea kufanyika katika Viwanja vya Chinangali Mkoani Dodoma.
Waziri huyo mwenye dhamana ya Utumishi ametumia nafasi hiyo kuipongeza TANESCO kwa kuendelea kuhamasisha matumizi ya Nishati safi kwa ajili ya kupikia na katika vyombo vya usafiri.
‘’ TANESCO mnafanya kazi kubwa nawapongeza kwa mageuzi ya matumizi ya nishati ya umeme katika vyombo vya usafiri, natoa rai muongeze Vituo vya kuchajia vyombo hivyo ili kuongeza wigo wa utoaji huduma,’’ alisisitiza Mhe. Ridhiwani
Naye Meneja Masoko Bw. Fredrick Kalinga amesema TANESCO inashiriki katika Maonesho hayo ili kutoa elimu kwa wananchi juu ya huduma na bidhaa zinazotolewa na Shirika ikiwemo maendeleo ya miradi ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji umeme, maboresho makubwa yaliyofanywa na Shirika kwenye mifumo ya kidigitali ya utoaji huduma kwa wateja pamoja na kuhamasisha jamii kutumia nishati safi ya umeme kupikia na katika vyombo vya usafiri kama magari, bajaji, guta, na pikipiki.
Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwa mwaka 2026 yenye kauli mbiu isemayo ‘’Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa huduma Endelevu’’ yameanza rasmi Juni 16, 2026 na yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)

.jpeg)



.jpeg)
*📌Asema REA Digital Platform ni mfumo wa kisasa kueleza miradi*
📍Chinangali Park - Dodoma
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete, amevutiwa na mfumo wa Kupanga na Kusimamia miradi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
Mhe. Kikwete ameipongeza REA kwa kuja na mfumo huo mara baada ya kutembelea banda hilo kwenye ufunguzi wa Maadhimiaho ya Wiki ya Utumishi kwa Umma 2026 yanayofanyika katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma.
Mfumo huo (*REA DIGITAL PLATFORM*) unaonyesha miradi yote inayotekelezwa na REA na kuweza kuisimamia kidijitali na kuwapa taarifa wadau popote walipo duniani kuhusiana na miradi ya Nishati vijijini.
Akimueleza Mhe. Kikwete, Afisa Upimaji Mwandamizi wa REA, Bw. Hussein Shamdas ameeleza kuwa kupitia mfumo huo mwananchi anaweza kujua mipango ya Wakala kwenye eneo lake na kufuatilia miradi inayotekelezwa na Wakala katika eneo husika.
Mwisho
Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwan Kikwete ameipongeza Wizara ya Nishati na Taasisi zake kwa kuendelea kuhamasisha Matumizi ya Nishati Safi kwa Wananchi pamoja na kuimarika kwa upatikanaji wa huduma za nishati nchini.
Kikwete amesema hayo Juni 17, 2026 alipotembelea Banda la Wizara ya Nishati na Taasisi zake wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika Katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Aidha, amesisitiza Wizara pamoja na Taasisi zake kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu Matumizi ya Nishati Safi ili Kila mmoja aifahamu kwa kina kwa manufaa ya kulinda Afya na mazingira.
" Hongerani Sana Nishati kwa kuendelea kuwasha Umeme na kuangaza Maisha ya Wananchi, tunaona Umeme upo wa kutosha" Alisema Kikwete
Sambamba na hilo amesisitiza kuendelea kutangaza fursa zilizopo katika Sekta ya Nishati nchini kwa wananchi.
Ametembelea Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati ambazo ni TANESCO, REA, TPDC, EWURA, PURA,PBPA na EWURA CCC ambapo alipata fursa ya kujionea huduma zinazotolewa na taasisi hizo pamoja na mafanikio ya miradi mbalimbali inayotekelezwa.
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limesisitiza ushirikiano wa wadau wote wakiwemo Serikali, Sekta binafsi, taasisi za umma, jamii na wananchi katika kusimamia na kuhifadhi mazingira kwa maendeleo endelevu.
Akizungumza na waandishi wa habari tarehe 17 Juni, 2026 katika ukumbi wa mikutano wa NEMC Jijini Dar es salaam, Kaimu Meneja Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma NEMC, Bi. Martha Kawishe, amesema mazingira ni suala mtambuka linalohitaji kila mdau kutimiza wajibu wake kwa kuzingatia Sheria na Miongozo ya Mazingira iliyowekwa.
Ameeleza kuwa NEMC inaendelea kusimamia utekelezaji wa Sheria kupitia ukaguzi wa miradi, utoaji wa elimu kwa umma katika masuala mazima ya udhibiti wa kelele chafuzi za mazingira, uharibifu wa vyanzo vya maji, utupaji holela wa taka, kutiririsha maji taka msimu wa mvua, ukataji hovyo wa miti na kuhakikisha miradi yote inazingatia Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) kabla ya kuanza.
Aidha, amewataka wananchi kuwa makini na watu wanaojifanya maafisa wa NEMC kwa lengo la udanganyifu, akisisitiza kuwa malipo yote hufanyika kwa utaratibu wa kiserakili na ukaguzi hufanywa na maafisa kisheria wakiwa na vithibitsho vifuatavyo: vitambulisho vya ukaguzi, vitambulisho vya kazi pamoja na nyaraka zinazompa mamlaka kisheria ya kufanya ukaguzi, na hasa ikizingatiwa ukaguzi hufanywa kidigitali ambapo mteja hupokea ujumbe mara baada ya ukaguzi.
NEMC pia imehimiza wananchi kutumia huduma rasmi ya kituo cha huduma kwa mteja kwa kupiga namba ya bure 0800110115 na kutumia mfumo wa e-mrejesho kwa kufuata menyu ya *152*00# na kufuata maelekezo ili kutoa ushauri, taarifa au changamoto za kimazingira.


DAR ES SALAAM:
Mabadiliko yanayoendelea kufanyika katika mpango wa Marekani wa Food for Peace yameibua mjadala muhimu ambao Afrika haiwezi tena kuupuuza: utegemezi wa muda mrefu wa misaada ya chakula kutoka nje ya bara.
Kwa zaidi ya miongo saba, mpango huo umekuwa miongoni mwa vyanzo vikubwa vya msaada wa chakula kwa mataifa yanayokabiliwa na njaa, migogoro na majanga ya kibinadamu. Hata hivyo, taarifa za hivi karibuni zinaonyesha kuwa mwelekeo wa mpango huo unabadilika, huku ukihusishwa zaidi na maslahi ya kilimo na biashara ya Marekani kuliko malengo ya kibinadamu pekee.
Kwa Afrika, suala hili linapaswa kutazamwa kama tahadhari badala ya mgogoro. Linaonesha jinsi usalama wa chakula wa bara unavyoweza kuathiriwa na maamuzi yanayofanyika nje ya mipaka yake.
Kwa miaka mingi, mataifa mengi ya Afrika yamekuwa yakitegemea misaada ya chakula wakati wa ukame, migogoro au misukosuko ya kiuchumi. Ingawa misaada hiyo imeokoa maisha ya mamilioni ya watu, imeacha swali muhimu: Je, usalama wa chakula wa Afrika unaweza kuendelea kutegemea sera zinazobadilika kulingana na vipaumbele vya mataifa wafadhili?
Jibu linaonekana kuwa hapana.
Hoja hii inaendana na mjadala mpana unaoendelea kuhusu uhuru wa kiuchumi wa Afrika. Wanasiasa, wachambuzi na wanazuoni wengi wa Kiafrika wamekuwa wakisisitiza kuwa uhuru wa kisiasa hauwezi kuwa kamili bila uwezo wa bara kujitegemea kiuchumi.
Mgombea urais wa Tanzania kupitia chama cha ADC, Doyo Hassan Doyo, hivi karibuni alieleza kuwa Afrika inapaswa kuimarisha mifumo yake ya ndani badala ya kutegemea sana taasisi za kimataifa. Akizungumzia nafasi ya bara katika mfumo wa dunia, alisema lengo si kujitenga na mataifa mengine bali kuhakikisha usawa katika mahusiano ya kimataifa.
“Lengo si kujitenga, bali ni kuwa na uwiano,” alisema.
Kauli hiyo inaweza kutumika pia katika mjadala wa usalama wa chakula. Kadri nchi za wafadhili zinavyobadilisha sera zao kulingana na mahitaji ya ndani, ndivyo hatari ya Afrika kubaki katika mazingira ya kutegemea maamuzi ya wengine inavyoongezeka.
Wakati huo huo, Afrika ina rasilimali nyingi zinazoweza kuiwezesha kujitosheleza kwa chakula. Bara lina sehemu kubwa ya ardhi inayofaa kwa kilimo ambayo bado haijatumika kikamilifu, vyanzo vikubwa vya maji pamoja na nguvu kazi inayoongezeka kwa kasi.
Hata hivyo, changamoto zinaendelea kujitokeza katika maeneo ya umwagiliaji, uhifadhi wa mazao, usafirishaji na uchakataji wa bidhaa za kilimo. Kiasi kikubwa cha mazao hupotea baada ya kuvunwa huku baadhi ya nchi zikiendelea kuagiza chakula kutoka nje.
Hali hii inaonesha kuwa tatizo si ukosefu wa rasilimali, bali ni namna ya kuzitumia kwa ufanisi.
Eneo la Biashara Huria la Afrika (AfCFTA) linaweza kuwa sehemu ya suluhisho. Kupitia ushirikiano wa kikanda, nchi za Afrika zinaweza kurahisisha biashara ya mazao ya kilimo na kuhakikisha maeneo yenye ziada ya chakula yanasaidia yale yanayokabiliwa na upungufu.
Lakini mafanikio hayo hayawezi kupatikana bila taasisi imara za ndani.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Lupa Ramadhani, anaamini kuwa uimara wa mifumo ya utawala ni msingi muhimu wa kujenga uhuru wa kweli wa Afrika.
“Kushindwa kuchukua hatua ndani ya nchi kunakaribisha uangalizi kutoka nje,” amesema.
Kauli hiyo inaakisi hali ilivyo katika sekta ya chakula. Pale ambapo sera za kilimo hazitekelezwi ipasavyo, uwekezaji ni mdogo au taasisi zinashindwa kutimiza wajibu wake, utegemezi wa misaada kutoka nje huongezeka.
Katika kipindi ambacho dunia inashuhudia mabadiliko ya kisiasa na kiuchumi, pamoja na kuongezeka kwa ushindani wa kijiografia kati ya mataifa makubwa, Afrika inalazimika kufikiria upya mkakati wake wa maendeleo.
Hii haimaanishi kukataa ushirikiano wa kimataifa. Misaada ya kibinadamu itaendelea kuwa muhimu wakati wa majanga na dharura. Hata hivyo, ushirikiano huo unapaswa kuimarisha vipaumbele vya Afrika badala ya kuvibadilisha.
Mustakabali wa usalama wa chakula wa bara hautaamuliwa Washington, Brussels au katika miji mingine ya dunia. Utaamuliwa na maamuzi yatakayofanywa katika miji mikuu ya Afrika kuhusu uwekezaji katika kilimo, miundombinu, biashara ya kikanda na taasisi za umma.
Mjadala kuhusu Food for Peace ni zaidi ya mjadala wa misaada. Ni ukumbusho kwamba uhuru wa kweli unahitaji uwezo wa kulisha wananchi wako mwenyewe. Kwa Afrika, huo si uchaguzi wa kisera pekee, bali ni hitaji la kimkakati kwa mustakabali wa bara.

Mwenza wa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Neema Mwigulu Nchemba, amehimiza Taasisi za umma na binafsi kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za kijamii kupitia utekelezaji wa programu za uwajibikaji kwa jamii (CSR).
Ameyasema hayo, Juni 16, 2026 katika hafla ya kukabidhi vifaa vya hospitali vilivyotolewa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino, Mkoa wa Dodoma, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya Shirika hill.
Aisha, Mama Neema ameishukuru, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya hususani katika ujenzi wa Hospitali, utoaji wa ajira kwa wataalamu wa atya, upatikanaji wa dawa na vifaa tiba pamoja na kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi ziliOrahisisha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini.
Amesema vifaa hivyo vilivyotolewa vinajumuisha vitimwendo 20, vitanda vya kujifungulia vitano, vitanda vya kufanyia uchunguzi vitano, vitanda vitano vya kulaza wagonjwa, machela moja ya kisasa, makabati matatu ya kuhitadhia vitaa tiba pamoja na mabeseni yenye vifaa mbalimbali kwa ajili ya akinamama 30 waliojifungua vitasaidia vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Chamwino na kuongeza ustawi wa mama na mtoto.
Awali, akimkaribisha mgeni rasmi kuzungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Viwanda na Blashara, Judith Kapinga amesema Serikali itaendelea kuhimiza taasisi zake kutekeleza kwa vitendo sera ya uwajibikaji kwa jamii ili kuchangia kuboresha huduma za kijamii na maisha ya wananchi.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, amesema Mkoa wake uko tayari katika kushirikiana na Wizara Pamoja na TBS kwa ujumla katika kuendeleza Sekta ya Viwanda na Biashara na jitihada za uwajibikaji kwa Jamii katika Mkoa wake.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya (TBS) Profesa Othman Chande na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Ashura Katunzi wamesema TBS itaendelea kutekeleza sera yake ya kuwajibika kwa jamii (CSR Policy) ili kuendelea kuwa karibu na jamii katika kuleta tija na maendeleo.

📌 Itanufaisha wilaya za Kongwa,Gairo, Mpwapwa, na Chamwino
📌 Waziri Ndejembi azindua Kituo cha Kubadilishia Njia za Usambazaji Umeme na Transfoma ya Kudhibiti Umeme
📌 Serikali yawekeza zaidi ya Shilingi Bilioni 10.5 kuimarisha huduma ya umeme
Na Mwandishi Wetu, Kongwa
Wananchi wa Wilaya za Gairo, Mpwapwa, Kongwa, Chamwino na Kiteto wanatarajiwa kunufaika na huduma ya umeme wa uhakika zaidi kufuatia kukamilika kwa miradi ya kuimarisha mfumo wa usambazaji wa umeme iliyotekelezwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa gharama ya zaidi ya Shilingi bilioni 10.5.
Miradi hiyo inahusisha Kituo cha Kubadilishia Njia za Usambazaji Umeme (Switching Station), Transfoma ya Kudhibiti Umeme (Automatic Voltage Regulator – AVR) yenye uwezo wa MVA 20 pamoja na njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Zuzu hadi Mbande yenye urefu wa kilomita 92.
Akizindua miradi hiyo Juni 16, 2026 katika eneo la Mbande, Wilaya ya Kongwa, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema uwekezaji huo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, za kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya umeme wa uhakika kwa ajili ya shughuli za kijamii na kiuchumi.
Alisema miradi hiyo imeleta maboresho makubwa katika mfumo wa usambazaji wa umeme katika ukanda huo, ambapo hapo awali hitilafu zilizokuwa zikitokea katika eneo moja zilisababisha wananchi wa maeneo mengine kukosa huduma ya umeme kwa muda.
“Kituo hiki kimeimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika. Hapo awali changamoto zilikuwa kubwa, hususan wakati wa mvua ambapo hitilafu katika wilaya moja ziliathiri huduma katika wilaya nyingine. Leo tunashuhudia matokeo ya uwekezaji huu kwa manufaa ya wananchi wetu,” alisema Mhe. Ndejembi.
Waziri huyo alibainisha kuwa Serikali itaendelea kuwekeza katika sekta ya nishati kupitia miradi mbalimbali ya kimkakati inayolenga kuimarisha uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini ili kuendana na kasi ya maendeleo ya Taifa na mahitaji ya wananchi.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, alisema utekelezaji wa miradi ya umeme unaendelea kuleta matokeo chanya kwa wananchi na kuchangia kufanikisha agenda ya maendeleo ya Serikali.
“Tunafarijika kuona kazi kubwa inayofanywa na TANESCO kuhakikisha Watanzania wanapata umeme wa uhakika. Hapo nyuma kulikuwa na changamoto za kukatika kwa umeme mara kwa mara katika maeneo haya, lakini Serikali ya Awamu ya Sita imefanya uwekezaji mkubwa kupitia TANESCO na matokeo yake yanaonekana wazi,” alisema Mhe. Mgalu.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Kongwa, Mhe. Mayeka Simon Mayeka, aliwataka wananchi na wawekezaji kutumia fursa ya upatikanaji wa umeme wa uhakika kuanzisha shughuli mbalimbali za uzalishaji mali ikiwemo viwanda vya usindikaji, biashara na shughuli nyingine za kiuchumi zitakazochochea maendeleo ya eneo hilo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, alisema kwa muda mrefu wananchi wa Kongwa na maeneo jirani walitegemea njia moja ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Dodoma Mjini, hali iliyokuwa ikisababisha changamoto za upatikanaji wa umeme wa uhakika kutokana na ongezeko la mahitaji ya huduma hiyo.
Alisema kukamilika kwa miradi hiyo kumeimarisha mfumo wa usambazaji wa umeme katika ukanda huo na kupunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zilizokuwa zikiathiri upatikanaji wa huduma.
“Awali kulikuwa na njia moja ya kusambaza umeme inayopita katika wilaya tano tofauti. Kuongezeka kwa mahitaji ya umeme pamoja na fursa za uwekezaji kulianza kuleta changamoto katika utoaji wa huduma. Tangu miradi hii ilipoanza kufanya kazi, tumeshuhudia maboresho makubwa na changamoto zilizokuwa zikiathiri huduma zimepungua kwa zaidi ya asilimia 90,” alisema Bw. Twange.
Kukamilika kwa miradi hiyo kunatarajiwa kuimarisha zaidi upatikanaji wa huduma ya umeme, kuongeza fursa za uwekezaji, kukuza shughuli za kiuchumi na kuboresha utoaji wa huduma za kijamii katika Wilaya za Gairo, Mpwapwa, Kongwa, Chamwino na Kiteto.