Mbunge wa Jimbo jipya la Itwangi Mhe. Azza Hillal Hamad akikagua ujenzi wa shule ya Sekondari Nhumbili katika kata ya Tinde Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI
Mbunge wa Jimbo jipya la Itwangi Mhe. Azza Hillal Hamad akikagua ujenzi wa shule ya Sekondari Nhumbili katika kata ya Tinde Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.


Katibu Tawala wa Wilaya ya Temeke Bw. Kimeta Mpui amezindua Ofisi mpya ya Wilaya ya KITANESCO Mikwambe ikiwa ni mkakati wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wa kuendelea kuwahudumia na kusogeza huduma mbalimbali zinazotolewa na TANESCO karibu na wananchi.
Akizungumza Mei 16, 2026 wakati wa zoezi hilo amesema uzinduzi wa ofisi hiyo umelenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kutokana na mahitaji ya msingi ya Nishati ya umeme kwa wananchi yanavyozidi kuongezeka kila kukicha.
Ameeleza kuwa hatua hiyo inaakisi maboresho ya kiutendaji yanayolenga kuongeza ufanisi na kupunguza changamoto ya umbali kwa wananchi ambao hapo awali walilazimika kufuata huduma katika ofisi za Mkoa wa KITANESCO Kigamboni.
Amesema TANESCO imefanya mabadiliko makubwa ili kuendana na ongezeko la mahitaji ya huduma ya umeme kutoka kwa wananchi hivyo ameipongeza TANESCO kwa kuanzisha ofisi hiyo nakuwataka wafanyakazi kuendelea kuimarisha utoaji wa huduma bora zaidi kwa wananchi.
“Napenda kuupongeza uongozi wa TANESCO kwa kuanzisha ofisi hii kwani ni kielelezo cha maboresho ya kiutendaji inayolenga kuongeza ufanisi na kupunguza kero na kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa wakati”
Akizungumza Kaimu Meneja Huduma kwa Wateja, Bw. Shamu Lameck, amesema TANESCO imejipanga kikamilifu na inaendelea kuimarisha na kusogeza huduma zake kwa wateja ili kuwarahisishia wananchi kupata huduma za umeme.
“Hii ni sehemu mhimu sana, ni ishara kwamba TANESCO tumedhamilia kwamba hali ya upatiakanaji wa umeme Kigamboni unaimarika na huduma yenyewe pia,tumejipanga kuhakikisha kwamba wananchi na wateja wetu tunawahudumia kwa ukaribu na ubora zaidi.
Kwa upande wake, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Kigamboni Mhandisi Paschal Luhavi amesema kuwepo kwa ofisi hiyo ya TANESCO Wilaya ya Mikwambe kunakwenda kusogeza huduma zaidi kwa wananchi ndani ya wilaya hiyo hasa maeneo ya kata za Kimbiji, Somangila, Pemba Mnazi na Kisarawe II na maeneo jirani.




Na Mwandishi wetu- MBEYA
Serikali imeendelea kuimarisha uwezo wa Kitaifa wa Kuzuia, Kujiandaa, Kukabiliana na Kurejesha hali baada ya maafa ili kuhakikisha wananchi wanaishi katika mazingira salama ya kuepuka madhara makubwa yatokanayo na maafa.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu Ofisi ya Mkoa wa Mbeya, Dkt. Noah Sikwese wakati akifunga mafunzo kwa Wajumbe Wateule wa Timu ya Kukabiliana na Dharura (RERT), Waatalamu wa Unendeshaji wa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura (REOCC) katika Mkoa huo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa.
Dkt. Sikwese, amesema timu za kukabiliana na dharura zimejengewa msingi muhimu wa utendaji utakaowezesha Mkoa kuwa na uwezo wa kujiandaa na kukabiliana na matukio ya dharura kwa haraka na ufanisi mkubwa .
“Timu hizi zitahusika katika kufanya tathmini za awali na za kina wakati wa maafa kubaini mahitaji halisi ya waathirika, pamoja na kuratibu upatikanaji wa rasilimali muhimu kwa ajili ya kukabiliana na athari za maafa,” alisema Dkt. Sikwese.
Pia, aliongeza kwamba mafunzo yamekuwa nyenzo muhimu katika kujenga na kuimarisha uwezo wa kitaalamu na kiutendaji kwa watumishi wanaohusika katika Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya dharura.
“Kuanzishwa kwa Kituo cha Operesheni na Mawasiliano ya Dharura Mkoa wa Mbeya ni hatua muhimu katika kuimarisha uratibu wa shughuli za usimamizi wa maafa. Kituo hiki kitawezesha ufuatiliaji wa matukio kwa ukaribu, ukusanyaji na uchambuzi wa taarifa kwa wakati, pamoja na kuimarisha mawasiliano miongoni mwa wadau,” alieleza.
Sambamba na hilo Dkt. Sikwese alifafanua kuwa, utekelezaji wa mafunzo hayo ulianza katika Mikoa a Mwanza, Arusha, Dodoma, ambapo hatua za kuanzisha Vituo vya Operesheni na Mawasiliano ya Dharura pamoja na kuimarisha Timu za kukabiliana na maafa zilianza kutekelezwa.
“Ni matarajio yangu mafunzo haya yataongeza ufanisi, uwajibikaji, ustahimilivu dhidi ya majanga katika Mkoa wetu wa Mbeya,”aliongeza.
Aidha, alitoa wito kwa wataalamu wote waliopatiwa mafunzo kuendelea kuyafanyia kazi maarifa na stadi, kudumisha nidhamu ya kazi na kujenga utamaduani wa ushirikiano wa kitaalamu huku akiwasisitiza kuendelea kufanya mazoezi ya mara kwa mara ya uokoaji na utoaji wa huduma ya kwanza kwa majeruhi au waliofikwa na maafa.
“Usimamizi wa maafa ni jukumu letu sote, kila mmoja ashiriki sasa na kuchukua hatua katika eneo lake ili kuokoa na kulinda maisha, mali na mazingira,” alisisitiza Dkt. Sikwese.
Ikumbukwe kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Usimamizi wa Maafa yam waka 2004 (Toleo la 2025) pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya mwaka 202 imeipa jukumu la kuratibu masuala yote ya usimamizi wa maafa nchini.
MWISHO
Mbunge wa Jimbo la Itwangi mkoani Shinyanga, Mhe. Azza Hilal Hamad akiwashukuru wananchi wa Kijiji cha Igalamya, Kata ya Usule kwa imani yao ya kumchagua yeye kuwa Mbunge, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Rais pamoja na madiwani wao katika uchaguzi mkuu. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
*📌Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa aridhishwa na miradi ya REA*
📍Nyasa - Ruvuma
Wananchi wa Kitongoji cha Ndecha Wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma wameanza kushuhudia mwanga wa matumaini baada ya kuzinduliwa rasmi kwa mradi wa REA kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 4.17 wa kusambaza umeme unaotekelezwa kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), mradi ambao unatarajiwa kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa eneo hilo.
Mradi huo umezinduliwa leo tarehe 16 Mei, 2026 na Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ndugu Wazo Michael Mwang’onda, ambaye amesema kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma bora za nishati ili kuboresha maisha yao na kuchochea maendeleo ya Taifa.
Halikadhalika Bw. Mwang'onda amewataka wananchi kutumia nafasi hiyo ya mradi kulipa shilingi 27,000 tu ili waweze kuwekewa umeme huo.
“Tunataka kuona wananchi wanalipia 27,000 ili wawekewe umeme hata ukiuza kuku mmoja 27,000 unaenda kuweka umeme kwenye nyumba yako sio 300,000 kama ilivyokuwa hapo zamani'' amesema Kiongozi wa Mwenge kitaifa.
Kwa upande wake, Msimamizi wa Miradi ya REA Mkoa wa Ruvuma, Mha. Hamisi Mrope, amesema mradi wa kusambaza umeme vijijini (REDP2C) katika Wilaya ya Nyasa unalenga kufikisha huduma ya umeme katika vitongoji vyote ili kuinua maisha ya wananchi na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Aidha, Mha. Mrope amesema mradi huo ulianza rasmi tarehe 16 Novemba 2023 na unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Oktoba, 2026, huku ukihusisha vitongoji 30, mashine umba 30 pamoja na wateja 1,247 kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 4.17.
Katika Kitongoji cha Ndecha pekee, mradi umehusisha ujenzi wa kilomita 8.43 za njia ya umeme, ufungaji wa mashine umba mbili pamoja na kuunganisha wateja 94 kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 307.6. Hadi sasa, miundombinu imekamilika kwa asilimia 100 huku wananchi 56 tayari wakiwa wameunganishiwa huduma ya umeme kwa gharama nafuu ya shilingi 27,000 kwa kila mteja.
Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi mzawa MF Electrical Engineering Ltd chini ya usimamizi wa TANESCO.
Naye, Mbunge wa jimbo la Nyasa Mhe. John Nchimbi amesema miradi ya REA imesaidia kwa sasa vijiji vyote 84 vya wilaya Nyasa kupata huduma ya umeme huku Tanzana ikijivunia kuwa ya pili Afrika Mashariki kwa kusambaza umeme.
Kwa upande wake, Mkandarasi wa mradi huo MF Electrical Engineering Ltd mhandisi Mussa David amesema mradi huo kwa kitongoji cha Ndecha 1 wameshafikisha umeme na wameshawasha nyumba 56.
Wananchi wa Ndecha wameeleza furaha yao kutokana na ujio wa umeme ambapo mwenyekiti wa kijiji cha Linda Antony Nkoma amesema sasa wataweza kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa ufanisi zaidi tofauti na zamani walipotegemea taa za vibatari na vyanzo vya nishati visivyo salama.
Uzinduzi wa mradi huo umeonekana kuwa hatua muhimu katika safari ya kuwaletea wananchi maendeleo endelevu huku ukiunga mkono kaulimbiu ya Mwenge wa Uhuru 2026 isemayo:
“Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo.”
Mwisho
Katika jitihada za kuendeleza ustawi wa wananchi na kuchochea uchumi wa maeneo ya vijijni na vitongojini, Serikali inaendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme wilayani Kondoa kupitia mpango wa kusambaza umeme katika vitongoji vyote vya wilaya hiyo.
Mpaka sasa vitongoji 113 vina umeme huku kukiwa na mradi unaoendelea wa kupeleka umeme katika vitongoji 60.
Hayo yameelezwa leo Mei 16, 2026 na Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri Mkuu Mhe. Dkt Mwigulu Nchemba wilayani Kondoa, Dodoma.
Mhe. Salome ameeleza kwamba katika mradi wa umeme unaotekelezwa sasa wa kusambaza umeme katika vitongoji 60 zaidi ya shilingi billion 21 imetengwa kuhakikisha mradi huo unakamilika ambapo kukamilika kwake kutafanya Kondoa kubakiwa na vitongoji 88 tu ambavyo havina umeme vitakavyofikiwa na huduma hiyo ifikapo mwaka 2030.
Pia Mhe Salome ameeleza kwamba Serikali imetenga zaidi ya shilingi milioni 752 kwa ajili ya kuhakikisha wananchi ambao miradi ya umeme inapita karibu na nyumba zao wanafikiwa na huduma ya umeme katika kaya zao.
Ameongeza kuwa katika Wilaya ya Kondoa, Wizara ya Nishati ina mpango wa kubadilisha nguzo zote chakavu na kupeleka nguzo za zege ili kuhakikisha wilaya hiyo inakuwa na nishati ya umeme ya uhakika ili wananchi waendelee kufanya shughuli zao za kiuchumi kama vile uendeshaji wa viwanda vidogo na shughuli za kijamii.
Vilevile amesema Serikali ina mpango mahsusi kujenga laini kubwa ya umeme ili kuimarisha na kutatua changamoto ya nguvu ya umeme (Low Voltage katika Jimbo la Kondoa).
Katika hatua nyingine, Mhe. Salome amewaasa wananchi kuendelea kutumia nishati safi ya kupikia akieleza kuwa pamoja na jitihada zinazofanywa na Wananchi Kondoa kutunza misitu bado wanatakiwa kuilinda kwa kuachana na matumizi ya Kuni na mkaa na kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia kama vile gesi, umeme na mkaa mbadala
“Niwahakikishie wanakondoa sasa hivi Serikali imeweka ruzuku katika mitungi ya gesi, hivyo niwaombee sana tuanze kutumia Nishati safi kwa ajili ya kulinda afya, mazingira na kuokoa muda wa kukaa jikoni ili tuweze kujiendeleza kiuchumi lakini pia tutumie nishati nyingine kama mkaa mbadala usiotoa moshi ambapo utatumia mkaa kidogo kupika chakula kingi na katika hali iliyo bora zaidi." Amesisitiza Mhe Salome.
.jpeg)
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), akizungumza wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, semina inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), ambapo alitoa wito kwa Taasisi za Fedha nchini kupunguza riba na gharama nyingine za mikopo ili kuwawezesha wananchi wakiwemo vijana kupata mitaji ya kuwekeza kwenye shughuli zao za kiuchumi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdulmajid Nsekela, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya “Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa”, uliofunguliwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) (hayupo pichani), uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).