HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

Kipangula Asisitiza Weledi Katika Uandishi wa Habari

May 29, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM — Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amesema uhuru wa uhariri ni nguzo muhimu katika taaluma ya habari na unapaswa kulindwa ili vyombo vya habari viweze kutekeleza majukumu yake kwa weledi, uwajibikaji na kwa maslahi ya umma.

Akizungumza Mei 26, 2026 katika mahojiano maalum yaliyofanyika katika Ofisi za JAB jijini Dar es Salaam, Wakili Kipangula alisema hakuna mtu anayepaswa kuingilia maamuzi ya uhariri wa chombo cha habari, awe ni chanzo cha taarifa, mmiliki wa chombo, mwanasiasa au mtu mwingine yeyote mwenye maslahi binafsi.

Alisema uhuru huo unapaswa kuendana sambamba na uwajibikaji wa kitaaluma, huku akisisitiza kuwa maadili ya taaluma ya habari yanamtaka mwandishi kufanya kazi kwa uadilifu, bila upendeleo na kuhakikisha taarifa zote zinathibitishwa kabla ya kuchapishwa au kurushwa.

“Ukweli ndio mlinzi wa taaluma ya habari. Mwandishi anatakiwa kutoa taarifa ambazo amezithibitisha na ana uhakika nazo kwa sababu jamii inategemea kupata taarifa sahihi na kwa wakati ili iweze kufanya maamuzi sahihi kuhusu masuala mbalimbali ya maendeleo,” amesema Wakili Kipangula.

Aidha, alisema waandishi wa habari wana nafasi kubwa katika kujenga jamii yenye uelewa, mshikamano na maendeleo, hivyo ni muhimu kutumia uhuru wa habari kwa kuzingatia sheria, maadili ya taaluma pamoja na kuheshimu haki na uhuru wa wengine kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi.

Kwa upande wake, Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Jamhuri, Bw. Deodatus Balile, alisema uhuru wa vyombo vya habari utakuwa na maana halisi pale vyombo hivyo vitakapokuwa na uwezo wa kiuchumi wa kujiendesha bila kutegemea ushawishi wa nje.

“Uhuru wa vyombo vya habari utakuwa uhuru wa kweli pale vyombo vya habari vitakapokuwa na nguvu ya kiuchumi,” amesema Balile.

TBS YAFUNGUA MILANGO YA MASOKO KWA VIJANA WABUNIFU

May 29, 2026 Add Comment

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kuonesha nafasi yake katika kuchochea maendeleo ya viwanda na kukuza ubunifu wa vijana kwa kutoa elimu ya viwango na ubora wa bidhaa katika Maonesho ya Fursa za Kazi na Ubunifu kwa Vijana (Career Fair 2026), hatua inayolenga kuwajengea vijana uwezo wa kuzalisha bidhaa zenye ushindani katika soko la ndani na kimataifa.

KABUDI AIPONGEZA MAMLAKA YA KUDHIBITI DAWA ZA KULEVYA KWA MAFANIKIO YA 2025

May 29, 2026 Add Comment
WAZIRI wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu(Sera,Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu) Profesa Palamagamba Kabudi ameta taarifa ya hali ya dawa za kulevya kwa mwaka 2025 ambapo inaonesha namna Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ilivyowekeza na kuweka nguvu kubwa katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya.

ORXY YAFUNGUA FURSA MPYA ZA KIUCHUMI KARATU

May 29, 2026 Add Comment
UWEKEZAJI wa ndani umeendelea kupewa msukumo nchini kufuatia juhudi za Serikali za kuboresha mazingira ya biashara, huku uzinduzi wa kituo cha mafuta cha Orxy Karatu ukitajwa kuwa sehemu ya utekelezaji wa maono ya kukuza uchumi jumuishi chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

RAIS SAMIA APOKEA TAARIFA YA SENSA YA WANYAMAPORI ILIYOFANYIKA NCHI NZIMA MWAKA 2024 – 2025

May 29, 2026 Add Comment

 




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati wa kikao cha kupokea Taarifa ya Sensa ya Wanyamapori iliyofanyika nchi nzima mwaka 2024 – 2025 iliyowasilishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji, tarehe 29 Mei, 2026 Ikulu Dar es Salaam.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye kikao cha kupokea Taarifa ya Sensa ya Wanyamapori iliyofanyika nchi nzima mwaka 2024 – 2025 iliyowasilishwa na Waziri ya Maliasili na Utalii Dkt. Ashatu Kijaji kupitia Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), tarehe 29 Mei, 2026 Ikulu Dar es Salaam.




CAREER FAIR 2026 YATUMIKA KUWAKUTANISHA VIJANA NA FURSA ZA AJIRA NA BIASHARA

May 29, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SERIKALI imewataka vijana nchini kutumia ubunifu, ujuzi na teknolojia kama nyenzo muhimu za kuchochea ukuaji wa biashara, viwanda na ajira, ikisisitiza kuwa maendeleo ya uchumi wa taifa yanategemea uwekezaji katika rasilimali watu wenye maarifa ya vitendo na uwezo wa kuzalisha thamani.
MAKAMU WA RAIS AONGOZA WAOMBOLEZAJI MAZISHI YA MAREHEMU BI SUZANA MAGUFULI

MAKAMU WA RAIS AONGOZA WAOMBOLEZAJI MAZISHI YA MAREHEMU BI SUZANA MAGUFULI

May 29, 2026 Add Comment




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amemwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mazishi ya Marehemu Bi. Suzana Ngolo Magufuli, ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, yaliyofanyika Kilimani, Chato mkoani Geita.

Akitoa salamu za rambirambi mara baada ya kumalizika kwa Ibada ya kumuombea Marehemu Bi. Suzana Ngolo Magufuli, Makamu wa Rais amesema Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameguswa na msiba huo na anatoa salamu za pole kwa familia, ndugu jamaa na marafiki na wote walioguswa na msiba huo.

Makamu wa Rais amewasihi Watanzania kumtumia marehemu Bi. Suzana Ngolo Magufuli kama kielelezo cha malezi ya watoto, malezi ya maadili na uzalendo kwa kuwafanya watoto kutanguliza maslahi ya Taifa mbele na kuwa tayari kutumikia Taifa kwa nafasi yeyote wanayopewa. Ameongeza kwamba namna bora ya kumuenzi marehemu Bi. Suzana Ngolo Magufuli ni kuiga mfano wa malezi bora na mema ya watoto.

Amesema msiba wa Bi. Suzana Ngolo Magufuli unafundisha kuwa alikuwa sehemu kuu ya malezi ya Hayati Rais Dkt. John Magufuli ambaye alitoa mchango mkubwa katika utumishi wa nchi yetu. Amesema kitendo cha wananchi wengi kutoa salamu za rambirambi kupitia mitandao ya kijamii ni ishara ya Watanzania kuguswa na Maisha ya Hayati Magufuli ambaye alitumikia nchi kwa uzalendo wa hali ya juu.

Halikadhilika, Makamu wa Rais amemuelezea hayati Dkt. John Pombe Magufuli, kama kiongozi aliyejitoa kutetea nchi pamoja na kuwa na utashi wa kujua wajibu wa kulea watu wengine na kuwafanya kuwa Viongozi wa Taifa baadaye. Ameongeza kwamba kujitoa na kufanya matendo mema kwaajili ya wengine ni matunda ya baadaye kwa mtu na familia yake.

Akitoa salamu za shukrani kwa niaba ya familia Bw. Simon Nyahinga amesema familia hiyo inamshukuru kwa dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa upendo mkubwa, huruma, faraja na mchango wake mkubwa aliyouonesha wakati wa kuugua kwa Bi Suzana Magufuli. Amesema tangu kufariki kwa Hayati Dkt. John Magufuli, Rais Samia ameendelea kusimama pamoja na familia katika kipindi chote cha matibabu.

Aidha, amewashukuru Viongozi wakuu wa Kitaifa na Viongozi wakuu wastaafu kwa msaada waliyotoa na kuifariji familia wakati wa matibabu ya Bi Suzana Magufuli pamoja na wakati wa msiba. Pia ameishukuru Serikali kwa kubeba jukumu ya kugharamia shughuli zote za msiba huo.

Ibada ya kumuaga na kumuombea Marehemu Bi. Suzana Magufuli imeongozwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Katoliki Mwanza Mhashamu Renatus Nkwande na kuhudhuriwa na Maaskofu mbalimbali, Mapadre, Viongozi mbalimbali, Viongozi Wakuu wastaafu, pamoja na wananchi mbalimbali.

Bi Suzana Magufuli amezikwa katika makaburi ya familia ya Magufuli , Kilimani Wilayani Chato.





TBS YATAKIWA KUSHIRIKIANA NA TRA KUONDOA KERO ZA MIFUMO YA VIBALI KWA SHEHENA ZINAZOINGIA NCHINI

TBS YATAKIWA KUSHIRIKIANA NA TRA KUONDOA KERO ZA MIFUMO YA VIBALI KWA SHEHENA ZINAZOINGIA NCHINI

May 29, 2026 Add Comment

Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith  Kapinga (Mb), ameliagiza Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kushirikiana kikamilifu na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na Taasisi nyingine husika katika kushughulikia na kuondoa kero zote zinazosababishwa na mifumo ya utoaji vibali kwa shehena zinazoingia nchini.

Waziri Kapinga ametoa agizo hilo akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Waziri Salum alipokutana na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Ashura Katunzi na ujumbe wake Mei 29, 2026 katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, kufuatia kuibuka kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa kuunganisha mfumo wa TANeSW wa TRA na mfumo wa OAS wa TBS na kusababisha usumbufu kwa baadhi ya wafanyabiashara.

Aidha, Waziri Kapinga amepongeza jitihada zinazoendelea kuchukuliwa baina ya TBS pamoja na TRA katika kuunganisha mifumo ya kielektroniki ili kurahisisha taratibu na kuongeza ufanisi wa utoaji wa vibali kwa shehena za mizigo inayoingia nchini.

DKT. MWIGULU AIPONGEZA TADB KWA KUINUA WAKULIMA, WAFUGAJI NA WAVUVI

May 28, 2026 Add Comment
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba ameipongeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa mchango wake katika kuwawezesha wakulima, wafugaji na wavuvi kupitia utoaji na usimamizi wa mikopo, hatua aliyoeleza kuwa inaendelea kuchochea maendeleo ya sekta za uzalishaji na ukuaji endelevu wa uchumi wa Taifa.
 MAKAMU WA RAIS AWASILI CHATO – KUMWAKILISHA RAIS MAZISHI YA BI SUZANA MAGUFULI

MAKAMU WA RAIS AWASILI CHATO – KUMWAKILISHA RAIS MAZISHI YA BI SUZANA MAGUFULI

May 28, 2026 Add Comment




Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akisaini kitabu cha maombolezo kufuatia kifo cha Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, wakati alipowasili Kilimani Wilayani Chato leo tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwafariji wa watoto wa marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, wakati alipowasili Kilimani Wilayani Chato leo tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimfariji Mama Janeth Magufuli, kufuatia kifo cha marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, wakati alipowasili Kilimani Wilayani Chato leo tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akizungumza na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Kassim Majaliwa, wakati alipowasili Kilimani Wilayani Chato, katika msiba wa marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwasili katika Uwanja wa Ndege wa Geita, Wilayani Chato leo tarehe 28 Mei 2026. Makamu wa Rais anatarajiwa kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Mazishi ya Marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, yatakayofanyika tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.

…………

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amewasili Chato Mkoani Geita, ambapo anatarajiwa kumwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mazishi ya Marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, yatakayofanyika tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.

Makamu wa Rais amepokelewa katika Uwanja wa Ndege Geita, Wilayani Chato, Mapokezi yaliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Martin Shigela, Viongozi wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi pamoja na Viongozi mbalimbali Waandamizi.

Pia Makamu wa Rais, amefika nyumbani kwa marehemu, Kilimani Chato kusaini kitabu cha maombolezo pamoja na kuwafariji wafiwa kufuatia msiba huo.

Imetolewa na
Ofisi ya Makamu wa Rais
28 Mei 2026
Chato, Geita.

JAJI MWAMBEGELE AWAPA NENO MAKARANI WA UCHAGUZI ISIMANI

May 28, 2026 Add Comment



Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe.Jacobs Mwambegele akizungumza wakati alipotembelea mafunzo ya siku moja kwa Makarani waogozaji Wapiga Kura katika Jimbo la Isimani yaliyofanyika katika Shule Sekondari Ufundi Ifunda mkoani Iringa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi huo utakaofanyika Jumatatu ya Juni 1, 2026.





Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe.Jacobs Mwambegele akizungumza wakati alipotembelea mafunzo ya siku moja kwa Makarani waogozaji Wapiga Kura katika Jimbo la Isimani yaliyofanyika katika Shule Sekondari Ufundi Ifunda mkoani Iringa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi huo utakaofanyika Jumatatu ya Juni 1, 2026.


Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa Mhe.Jacobs Mwambegele amewataka watendaji wa uchaguzi ambao ni Makarani waongozaji Wapiga kura kufanya kazi yao kwa kufuata Sheria, Kanuni na utaratibu wakati wa uchaguzi Mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Isimani Mkoani Iringa na Kata 12 za Tanzania Bara.

Jaji Mwambegele ameyasema hayo wakati akitembelea mafunzo ya siku moja kwa Makarani hao waogozaji katika Jimbo la Isimani yaliyofanyika katika Shule Sekondari Ufundi Ifunda mkoani Iringa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya Uchaguzi huo utakaofanyika Jumatatu ya Juni 1, 2026.

Jaji Mwambegele pia amewasisistiza watendaji hao kuishi kwenye viapo vyao wakati wa utekelezaji majukumu yao ya Uchaguzi ili kujiepusha na upendeleo wa aina yoyote.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Mafunzo hayo ya Makarani Waongozaji Wapiga Kura Vituoni Bw. Baraka Matonya amemuhakikishia Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kwamba watafuata sheria, kanuni, miongozo na maelekezo ya Tume wakati wote wa Utekelezaji wa majukumu yao ya Uchaguzi .

Naye Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Isimani,Bi. Caroline Otieno amesema maandalizi ya uchaguzi huo Mdogo wa Jimbo hilo, yamekamilika kwa asilimia 100 ambapo vifaa vyote vimepokelewa.

Uchaguzi huo utafanyika sambamba na uchaguzi mdogo katika kata 12 za Tanzania Bara ambazo ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.

Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.





Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume.

Mratibu wa Uchaguzi Mkoa wa Iringa Bi. Nuru Sovella akizungumza wakati wa mafunzo hayo.
Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume.

Sehemu ya washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza Mwenyekiti wa Tume.

Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Isimani,Bi. Caroline Otieno akizungumza na kusema kua maandalizi ya uchaguzi huo Mdogo wa Jimbo hilo, yamekamilika kwa asilimia 100 ambapo vifaa vyote vimepokelewa.

NEMC YATAKIWA KUONGEZA ELIMU YA UHIFADHI WA MAZINGIRA NCHINI

May 28, 2026 Add Comment
- Ataka kila mmoja mmoja aone ni suala lake

MBUNGE MWAKIOJA ASHIRIKI DALUNI MARATHON 2026

May 28, 2026 Add Comment



‎MKINGA,TANGA,TANZANIA-Katika mwendelezo wa kuwa karibu na wananchi wenzake wa Mkinga,Mbunge wa Jimbo la Mkinga,Mheshimiwa Mwakioja,leo asubuhi ameshiriki katika mbio za DALUNI MARATHON 2026 akiwa kama Mgeni Rasmi.

‎Katika mwendelezo wa kuwa karibu na wananchi wenzake wa Mkinga,pia alipata nafasi ya kukimbia mbio za kilometa moja na kuibuka mshindi wa mbio hizo.

‎Imetolewa na:

‎🏢 Kitengo cha Mawasiliano,

‎📍 Ofisi ya Mbunge,Jimbo la Mkinga.

‎#Mkinga.#DaluniMarathon2026. #MabadilikoKwaMaendeleo.#Mwakioja.

WASOMI WATAKA AFRIKA KUWA NA SAUTI IMARA KATIKA SIASA ZA DUNIA

May 28, 2026 Add Comment

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Mkutano wa kimataifa wa siku tatu wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere umezinduliwa rasmi jijini Dar es Salaam, ukiwa na lengo la kujadili masuala ya siasa za kimataifa (geopolitics), maendeleo na mwelekeo mpya wa Afrika katika mazingira ya dunia yanayobadilika kwa kasi.

PROF NOMBO AFUNGUA RASMI MAFUNZO YA KITAIFA KWA WAKUU WA SHULE ZA SEKONDARI NCHINI

May 28, 2026 Add Comment
SERIKALI imezindua rasmi Mpango wa Mafunzo ya Uongozi na Usimamizi wa Elimu kwa Wakuu wa Shule za Sekondari na Maafisa Elimu Kata nchini, hatua inayolenga kuimarisha ufanisi wa uongozi wa shule, usimamizi wa ufundishaji na ujifunzaji pamoja na kuimarisha ubora wa elimu nchini.

TPDC YAJIKITA KUTOA ELIMU ULINZI MIUNDOMBINU YA TAIFA

May 28, 2026 Add Comment

 Na Mwandishi Wetu


WAKATI vitendo vya uharibifu wa miundombinu katika miradi mbalimbali ya kimkakati ikiripotiwa kuendelea hapa nchini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania, (TPDC) limeimarisha ushirikiano na jamii kwa kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhakikisha usalama wa miundombinu ya bomba la gesi asilia unakuwepo.

Katika Programu ya elimu kwa umma inayolenga kuongeza uelewa wa wananchi wanaoishi karibu na maeneo yanayopitiwa na bomba la gesi asilia iliyofanyika hivi karibuni kwenye vijiji vya Mkwalia Kitumbo na Sunguvuni, wilayani Mkuranga mkoani Pwani, maofisa wa shirika hilo wamesema lengo la elimu hiyo ni kuwafanya wananchi wawe sehemu ya mfumo wa ulinzi wa miundombinu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Ofisa Mwandamizi wa Maendeleo ya Jamii wa TPDC, Bw. Oscar Mwakasege alisema mpango huo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa shirika wa kushirikisha wananchi katika kulinda rasilimali za taifa pamoja na kuhakikisha jamii inakuwa na uelewa sahihi kuhusu matumizi salama ya maeneo yanayozunguka bomba la gesi.

Alisema TPDC imeona umuhimu wa kuwafikia wananchi moja kwa moja katika vijiji vyao ili kuwajengea uwezo wa kutambua viashiria vinavyoweza kuhatarisha usalama wa bomba la gesi na namna ya kuchukua hatua mapema.

“Lengo letu ni kuhakikisha wananchi wanaelewa umuhimu wa bomba la gesi asilia, namna ya kulilinda na kutoa taarifa mapema wanapoona viashiria vya uharibifu au shughuli zisizo salama karibu na miundombinu hiyo. Tunataka wananchi wawe walinzi wa kwanza wa rasilimali hii muhimu ya taifa,” alisema Bw. Mwakasege.

Aliongeza kuwa baadhi ya shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wa bomba la gesi ni pamoja na uchimbaji holela karibu na njia ya bomba, ujenzi usioruhusiwa, uchomaji moto ovyo pamoja na vitendo vya uharibifu wa alama za tahadhari zilizowekwa na mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Bw. Mwakasege, usalama wa miundombinu ya gesi asilia una mchango mkubwa katika kuhakikisha huduma mbalimbali muhimu zinaendelea kutolewa nchini, ikiwemo uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi asilia, shughuli za viwandani na maendeleo ya sekta nyingine za uchumi.

Aidha alisema ushirikiano kati ya TPDC na wananchi umeendelea kuleta mafanikio katika maeneo mengi yanayopitiwa na bomba hilo, kwani wananchi wengi wamekuwa wakitoa taarifa mapema kuhusu shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wa miundombinu hiyo.

Katika mikutano hiyo ya elimu, wananchi walipata nafasi ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusu usalama wa bomba la gesi, matumizi ya ardhi karibu na miundombinu hiyo pamoja na hatua zinazopaswa kuchukuliwa endapo kutatokea hali yoyote ya hatari.

Wananchi walioshiriki katika mikutano hiyo wameipongeza TPDC kwa kuwafikia moja kwa moja vijijini na kutoa elimu inayosaidia kulinda rasilimali za taifa huku ikijenga uelewa wa pamoja kuhusu masuala ya usalama.

Baadhi yao walisema hapo awali kulikuwa na uelewa mdogo kuhusu umuhimu wa bomba la gesi asilia na madhara yanayoweza kujitokeza endapo miundombinu hiyo itaharibiwa, lakini elimu inayotolewa sasa imewasaidia kuelewa wajibu wao kama sehemu ya jamii inayozunguka mradi huo.

Mwananchi mmoja kutoka kijiji cha Sunguvuni alisema elimu hiyo imewapa mwanga mpya kuhusu umuhimu wa kushirikiana na mamlaka katika kulinda rasilimali za taifa.

“Sasa tunajua kuwa bomba hili lina umuhimu mkubwa kwa taifa na hata kwa maendeleo ya wananchi wenyewe. Tuko tayari kushirikiana na TPDC kuhakikisha miundombinu hii inalindwa wakati wote,” alisema.

Kwa upande wake, uongozi wa vijiji vya Mkwalia Kitumbo na Sunguvuni umeeleza kuwa utaendelea kushirikiana na TPDC katika kutoa elimu kwa wananchi na kuhamasisha jamii kuwa sehemu ya ulinzi wa bomba la gesi.

Utoaji wa elimu kwa umma uaendelea kutekelezwa katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Pwani ikiwa ni sehemu ya juhudi za TPDC za kuimarisha usalama wa miundombinu ya gesi asilia na kujenga mahusiano mazuri kati ya shirika hilo na jamii inayozunguka mradi wa gesi asilia.

TPDC imesisitiza kuwa ushirikiano wa wananchi ni nguzo muhimu katika kuhakikisha miundombinu ya gesi asilia inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho pamoja na kuendelea kuchochea maendeleo ya uchumi wa taifa.
Ofisa Mwandamizi wa Maendeleo ya jamii kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC)Oscar Mwakasege akizungumza na wananchi wa vijiji vya wilaya ya Mkuranga hivi karibuni kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu ya Taifa.

WAZIRI MKUU MGENI RASMI KONGAMANO LA WADAU WA MAZINGIRA, MIAKA 40 YA NEMC

May 28, 2026 Add Comment



WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Mei 28, 2026 amewasili kuwa Mgeni Rasmi katika Kongamano la Kitaifa la Wadau wa Mazingira pamoja na maadhimisho ya miaka 40 ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) yanayofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.

Katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu ametembelea mabanda mbalimbali ya maonesho ya wadau wa mazingira na kupata fursa ya kujionea shughuli na teknolojia zinazotumika katika uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini.


SERIKALI KUJENGA VITUO 10 VYA GESI YA CNG NCHINI: SALOME

May 28, 2026 Add Comment




📌 Vituo vitano vya CNG vinavyohamishika kununuliwa.


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), kwa kushirikiana na sekta binafsi, inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa vituo 10 vya CNG (Gesi Asilia Iliyobanwa) nchini katika mikoa ya Dar es Salaam vituo nane, Mtwara kituo kimoja na Morogoro kituo kimoja.


Salome ameeleza hayo leo Mei 28, 2026, Bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mhe. Arif Suleman Premji, Mbunge wa Mtwara Vijijini, aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuwekeza kwenye vituo vya CNG baada ya kuondoa ushuru wa shilingi 382 kwa kilo ya gesi ili kuhimiza matumizi ya CNG kwenye vyombo vya moto.

Salome amesema Serikali kupitia TPDC inakamilisha taratibu za ununuzi wa vituo vitano vya CNG vinavyohamishika (CNG Mobile Stations), kati ya hivyo vituo viwili vitawekwa Mkoa wa Dar es Salaam, kituo kimoja Mkoa wa Morogoro katika eneo la Chuo cha Ardhi, na vituo viwili Mkoa wa Dodoma katika maeneo ya Mji wa Serikali - Mtumba na Chako ni Chako.


Amesema Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi inaendelea na ujenzi wa vituo vya CNG katika maeneo mbalimbali nchini, Kwa sasa kuna vituo 18 vya CNG vinavyofanya kazi katika mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara na Pwani.

Aidha, Salome amefafanua kuwa Serikali inaendelea na majadiliano na kampuni binafsi sita kwa ajili ya kuendeleza miradi midogo ya kubadili gesi asilia kuwa kimiminika (Mini-LNG) na kusafirishwa kwa magari maalum kwenda mikoa mbalimbali nchini ambayo haijafikiwa na miundombinu ya mabomba ya gesi asilia.



Amesema kwa mikoa iliyopitiwa na bomba la gesi, ikiwemo Mtwara, Serikali imejielekeza zaidi katika kusambaza gesi majumbani na kwenye taasisi kupitia mabomba ili kuhakikisha wananchi wa maeneo hayo wananufaika na rasilimali hiyo.

TPA -TOZO MPYA YA MIUNDOMBINU KUONGEZA UFANISI WA BANDARI.

May 28, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga, Tanga

MAMLAKA ya Bandari Tanzania (TPA) imesema kuanzishwa kwa tozo mpya ya maendeleo ya miundombinu ya bandari kutasaidia kuongeza uwezo wa bandari nchini kuhudumia shehena, kupunguza gharama kwa wafanyabiashara na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Akizungumza jijini Tanga juzi katika mkutano wa wadau wa watumiaji wa Bandari ya Tanga kuhusu ada ya maendeleo ya miundombinu ya bandari, Meneja wa Bandari ya Tanga, Salehe Mbega, alisema tozo hiyo inayojulikana kama Port Infrastructure Development Levy (PID) ilitarajiwa kuanza kutumika Machi mwaka huu, lakini imeahirishwa hadi Julai Mosi kufuatia maoni ya wadau mbalimbali.

Mkutano huo ulihudhuriwa na wadau mbalimbali, wakiwemo wanachama wa Chama cha Mawakala wa Forodha Tanzania (TACAS), ambao waliunga mkono tozo hiyo wakisema italeta mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma bandarini nchini.

Mbega alisema lengo la tozo hiyo ni kuboresha miundombinu ya bandari ambayo imeanza kuelemewa kutokana na ongezeko kubwa la shehena katika bandari za Tanga, Dar es Salaam na Mtwara.

“Bandari ya Tanga kwa sasa inahudumia takribani tani milioni mbili za shehena kwa mwaka, wakati uwezo wa miundombinu iliyopo unatarajiwa kufikia tani milioni tatu ifikapo mwaka 2030. Hata hivyo, kutokana na kasi ya ukuaji wa shehena, kiwango hicho kinaweza kufikiwa mapema mwaka 2027 au 2028,” alisema Mbega.

Alisema Serikali kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya usafirishaji imeona umuhimu wa kuwekeza zaidi katika miundombinu ili bandari ziweze kuhimili ongezeko la mizigo.

Mbega alisema fedha zitakazokusanywa kupitia tozo hiyo zitatumika kujenga na kuboresha miundombinu mbalimbali, ikiwemo kuongeza gati jipya katika Bandari ya Tanga.

“Kwa sasa tuna magati mawili, lakini tuna mpango wa kuongeza gati la tatu lenye urefu wa mita 900. Pia eneo la Mwambani lina nafasi kubwa ya kujengwa bandari mpya yenye zaidi ya magati 10 katika eneo la ekari 174,” alisema.

Aliongeza kuwa maboresho hayo yataongeza uwezo wa nchi kuhudumia shehena nyingi zaidi na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Kwa mujibu wa Mbega, tozo hiyo pia itasaidia kupunguza gharama wanazopata wafanyabiashara kutokana na ucheleweshaji wa huduma bandarini.

Alisema baadhi ya meli hulazimika kusubiri nje ya bandari kwa muda wa wiki tatu hadi mwezi mmoja kabla ya kuhudumiwa, hali inayosababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara.

“Meli inapokaa nje ya bandari hulipiwa hadi dola za Marekani 20,000 kwa siku. Ukihesabu kwa mwezi mzima ni gharama kubwa sana kwa wafanyabiashara. Tozo hii itasaidia kuongeza ufanisi na kupunguza mzigo huo,” alisema.

Aidha, Mbega alisema maboresho yaliyofanywa kwenye reli ya Tanga kwa gharama ya Sh bilioni 429.1 yameongeza usafirishaji wa mizigo kwenda Rwanda na Burundi.

Alisema reli hiyo ambayo kwa muda mrefu ilikuwa haitumiki sasa imefunguliwa na kuanza kupokea shehena nyingi kutoka bandarini kwenda Isaka kabla ya kusafirishwa kwenda nchi hizo jirani.

Hata hivyo, alisema ongezeko la mahitaji ya usafirishaji kwa njia ya reli limezidi uwezo wa mabehewa yaliyopo.


“Wateja wanaopendelea kutumia reli wameongezeka zaidi kuliko uwezo wa mabehewa yaliyopo. Huu ni wakati sahihi kwa sekta ya reli kuongeza mabehewa ili kukidhi mahitaji ya soko,” alisema.

Awali akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa TACAS, Ephraim Mwankusye, alisema pendekezo la ada ya asilimia 4.5 ya maendeleo ya miundombinu ya bandari lina lengo la kusaidia maboresho makubwa ya bandari nchini ili kuongeza ufanisi wa huduma za usafirishaji wa mizigo.

Alisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kuendeleza Bandari za Dar es Salaam, Tanga, Mtwara pamoja na Bandari ya Bagamoyo na ujenzi wa miundombinu ya mafuta katika bandari mbalimbali nchini.

Mwankusye alisema lengo kubwa ni kuhakikisha bandari za Tanzania zinakuwa za kisasa, zenye uwezo mkubwa wa kuhudumia mizigo mingi kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Kwa mujibu wa pendekezo hilo, asilimia 4.5 ya tozo ya PID itaelekezwa katika miradi ya kuboresha bandari, magati, reli, matenki ya mafuta pamoja na barabara zinazosaidia usafirishaji wa mizigo.