HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts
ADEM YAHITIMISHA MAFUNZO KWA MAAFISA ELIMU WA MIKOA 26 TANZANIA BARA
habariKAMATI YA KUDUMU YA BUNGE NISHATI NA MADINI YARIDHISHWA NA MAENDELEO YA KIWANDA CHA NGUZO ZA ZEGE
📌Ni mradi wa kihistoria kutekelezwa chini ya Serikali ya awamu ya Sita
📌 Yaipongeza TANESCO kwa usimamizi wa Ujenzi wa Kiwanda hiko
📌 Shilingi Bilioni 8 zawekezwa ujenzi wa Kiwanda hiko
Na Mwandishi wetu, Tabora
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na Ujenzi wa Kiwanda cha Zege kinachomilikiwa na kampuni tanzu ya TANESCO ya kuzalisha nguzo za zege kilichopo katika Mkoa wa Tabora wakati wa ziara yao ya kikazi Mkoani humo tarehe 12 Machi, 2026.
Akizungumza baada ya ziara hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu ameeleza kuridhishwa na hatua ya kukamilika kwa Kiwanda hicho kilichoanza uzalishaji na kuwaelekeza Wizara ya Nishati na TANESCO kukisimamia kiwanda hiko kiendelee kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuzalisha faida.
"Kwa niaba ya Kamati tumeridhika na kazi kubwa iliyofanyika katika kiwanda hiki ambacho kimekamilika na uzalishaji umeanza, tunatoa rai kwa Wizara na TANESCO kuendelea kusimamia kiwanda hiki ili kiendelee kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi", alieleza Mhe. Mgallu
Alieleza kuwa uelekeo wa sasa ni kusambaza nguzo za zege hasa kwa maeneo yenye unyevu sambamba na maeneo yaliyo karibu na misitu pamoja na mikondo ya mito ya maji ambayo nguzo za miti huathirika kwa kiasi kikubwa haswa kwenye msimu wa mvua hivyo nguzo za zege zitakuwa msaada mkubwa katika mazingira kama hayo na kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme.
“Kama mnavyofayahamu kwa sasa uelekeo ni kusambaza nguzo za zege badala ya nguzo za miti hasa katika maeneo ambayo yana asili ya unyevu, maeneo karibu na mito ya maji ama visiwa ambapo nguzo za miti huathiriwa na mazingira hayo”, aliongeza.
Naye Mhe. Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hiko umekamilika mwaka huu na kuanza uzalishaji wake rasmi Februari, 2026 ambapo mpaka sasa wastani wa nguzo zinazozalishwa ni 80 hadi 120 kwa siku ambapo mpaka sasa gharama ya shilingi bilioni 6.4 imeshatumika katika hatua zote hadi uzalishaji ulipoanza ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.4 bado hazijalipwa kwa mkandarasi ambaye bado yupo kwenye kipindi cha uangalizi.
“Kiwanda hiki kilianza uzalishaji rasmi mwezi Februari mwaka huu ambapo kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha nguzo 80 hadi 120, mpaka sasa ujenzi wa kiwanda hiki hadi uzalishaji ulipoanza imetumia gharama ya shilingi bilioni 6.4 ambapo bado kuna billioni 1.6 bado haijalipwa kwa mkandarasi kwa kuwa yupo kwenye kipindi cha uangalizi”, aliongeza Mhe. Ndejembi.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kuwa kukamilika kwa kiwanda hiko kunaenda kuleta mageuzi makubwa kwani nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo Shirika bado linaendelea kuikuza sekta na kuwa na utoshelevu wa nguzo zenyewe kwa matumizi ya wananchi.
“Baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda na kuanza uzalishaji ambapo kwa hali ilivyo ya matumizi ya nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo kama Shirika tutahakikisha tunaisimamia sekta hii ili kuendelea kuwapatia wateja wetu huduma ya umeme wa uhakika”, alisema Bw. Twange.
Ziara hiyo ya kamati ya kudumu ya bunge ya nishati na madini inalenga kufanya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Shirika katika maeneo mbalimbali nchini ili kujionea ufanisi wake.

KAMATI YA BUNGE YARIDHISHWA NA KASI YA UJENZI WA JENGO LA GHOROFA 10 CBE
habari
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), ameeleza kuridhishwa kwake na hatua ya ujenzi wa jengo la kisasa la Vipimo na Viwango katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) jijini Dar es Salaam.
Akizungumza Machi 12, 2026, Mhe. Mwanyika amebainisha kuwa mradi huo wa ghorofa 10 umefikia asilimia 93 ya utekelezaji wake, jambo linaloashiria usimamizi madhubuti na weledi katika ukamilishaji wa Jengo Jengo hilo ili kukidhi ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa kila mwaka.
Vilevile, Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa uongozi wa chuo kuendelea kutoa na kuimarisha elimu ya kati (middle-level education) katika fani za biashara hususani ujasiliamali kwa kuwa ni nyenzo adhimu kwa wahitimu wanaojiandaa kuingia kwenye soko la ajira binafsi na
Kutasaidia kuongeza hadhi ya chuo na kuchochea ari ya wanafunzi wengi zaidi kujiunga na taasisi hiyo.
Amesema kuwa uimara wa chuo unategemea ubora wa mafunzo unayoyatoa na uwezo wake wa kuzalisha wataalamu wenye ushindani katika soko la ndani na nje ya nchi.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb), amefafanua kuwa mradi huo unatekelezwa kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2025/26 na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kubeba zaidi ya wanafunzi 4,000 kwa wakati mmoja.
Aidha amebainisha kuwa Jengo hilo la Vipimo na Viwango litakuwa kitovu cha mafunzo ya masoko na nyanja mbalimbali za kibiashara ambazo zinahitajika kwa kiasi kikubwa kulingana na mwelekeo wa sasa wa uchumi wa viwanda.
Naye Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Edda Lwoga, ameeleza kuwa mradi huo ulioanza Mei 25, 2023, umekuwa mhimili wa mabadiliko makubwa ya kitaaluma chuoni hapo. Alibainisha kuwa kukamilika kwa jengo hilo kutaongeza fursa za udahili kwa wanafunzi wengi wanaohitaji masomo ya biashara na ujasiriamali, ikiwemo kozi fupi ambazo zimekuwa na mahitaji makubwa kwa wadau wa sekta binafsi.

KAMATI YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI YAWASILI KUKAGUA KIWANGA CHA NGUZO ZA ZEGE TCPM-TABORA
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Subira Mgalu (Mb), imewasili katika Kiwanda cha Kutengeneza Nguzo za Zege cha TCPM Tabora kinachomilikiwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kupitia kampuni tanzu ya TCPM mkoani Tabora na kupokelewa na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi.
![]() |
Ziara ya Kamati hiyo imeanza rasmi leo tarehe 12 Machi 2026 na itakuwa na mwendelezo katika mikoa mbalimbali ambapo wajumbe wa Kamati watakagua na kujionea miradi inayotekelezwa na Wizara ya Nishati kupitia taasisi zake katika maeneo tofauti nchini.

BALOZI MASILINGI APONGEZA MCHANGO WA MGODI WA DHAHABU WA GEITA KATIKA MAPATO YA SERIKALI
habari
📍*Geita.*
Mwenyekiti wa Kamati ya TEITI, Balozi Wilson Masilingi, ametembelea Mgodi wa Dhahabu wa Geita Gold Mining Limited akiambatana na Menejimenti ya TEITI, kwa lengo la kujitambulisha na kufanya mazungumzo na menejimenti ya mgodi huo.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Balozi Masilingi alisema ziara hiyo imelenga kujenga na kuimarisha ushirikiano kati ya TEITI na wadau wa sekta ya uziduaji, hususan migodi mikubwa inayochangia maendeleo ya taifa.
Alisema kuwa aliteuliwa kusimamia taasisi hiyo muhimu na Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, mwezi Januari mwaka huu, hivyo anaona ni muhimu kujitambulisha kwa wadau wakuu wa sekta hiyo ili kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya TEITI.
“Utekelezaji wa shughuli za EITI nchini ni wa ushirikiano, hivyo nitashirikiana kikamilifu na wadau wote ili kuendeleza gurudumu la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji,” alisema Balozi Masilingi.
Katika ziara hiyo, menejimenti ya mgodi ilitoa maelezo kuhusu maendeleo yaliyofikiwa tangu kuanzishwa kwa mgodi huo, ikiwemo namna wanavyotekeleza sheria, kanuni na miongozo ya sekta ya madini pamoja na masharti ya leseni ya uchimbaji.
Aidha, ilielezwa kuwa mgodi huo umeendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) katika halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Geita, hatua inayochangia maendeleo ya jamii zinazouzunguka mgodi.
Pia ilibainishwa kuwa kwa sasa mgodi huo unaendeshwa kwa kiasi kikubwa na Watanzania na umeendelea kuongeza ajira kwa wananchi wa ndani ikilinganishwa na miaka ya awali ya uendeshaji wake.
Balozi Masilingi aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa mapokezi mazuri waliompatia pamoja na utayari wao wa kuendeleza ushirikiano kwa manufaa ya sekta ya uziduaji na maendeleo ya taifa.
Kwa upande wake, Katibu Mtendaji wa TEITI, Bi. Mariam Mgaya, aliishukuru menejimenti ya mgodi kwa kuendelea kushirikiana na TEITI katika utekelezaji wa matakwa ya EITI pamoja na Sheria ya TEITA ya mwaka 2015, inayolenga kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji.
Alisisitiza kuwa ushirikiano huo unapaswa kuendelezwa ili kuongeza uwazi na uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za madini, mafuta na gesi asilia nchini.
Naye Meneja wa mgodi huo, Bw. Ashraf Suryaningrat, alisema Geita Gold Mining Limited itaendelea kushirikiana kikamilifu na TEITI katika kufanikisha lengo la uwazi na uwajibikaji katika sekta ya uziduaji, akibainisha kuwa mgodi huo ni miongoni mwa wadau wakubwa wa TEITI nchini.



















