HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

DKT. AKWILAPO: MSITOE MAAMUZI YA KUWAFURAHISHA WATU

DKT. AKWILAPO: MSITOE MAAMUZI YA KUWAFURAHISHA WATU

March 07, 2026 Add Comment



Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuapishwa kwa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akimuapisha mmoja wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026

Na Munir Shemweta, WANMM MTWARA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo ameshuhudia uapisho wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya na kuwataka wajumbe hao kutenda haki kuacha kutoa maamuzi ya kuwafurahisha watu wakati wa kusikiliza mashauri ya ardhi.

Uapisho huo umeongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Donald Wilson Msengi, na kufanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Akizungumza mara baada ya kushuhudia uapisho huo, Dkt. Akwilapo aliwaasa wajumbe wa mabaraza hayo kuepuka kutoa maamuzi kwa lengo la kuwafurahisha watu au makundi fulani, badala yake wafanye maamuzi yanayozingatia haki na sheria ili kupunguza migogoro ya ardhi katika jamii.

Alisema wajumbe wanapaswa kutambua kuwa nafasi waliyopewa ni dhamana kubwa kutoka kwa Mungu na Serikali, hivyo wanatakiwa kuitumia kwa uadilifu, uaminifu na kwa kuzingatia misingi ya haki.

“Napenda mtambue kuwa nafasi mlizopewa ni kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, hivyo mheshimu Mungu kwa kufanya maamuzi yanayoendana na haki na uadilifu,” alisema Dkt. Akwilapo.

Aliongeza kuwa, kazi ya kushughulikia mashauri ya ardhi si rahisi, kwani mara nyingi huwa na pande mbili zinazopingana, lakini wajumbe wanapaswa kufanya maamuzi kwa kuzingatia ushahidi na sheria ili haki ipatikane kwa anayestahili.

“Sina wasiwasi na ninyi, ingawa kazi ni ngumu, lakini mfanye maamuzi kwa kuzingatia haki na siyo kumfurahisha mtu,” alisisitiza.

Dkt. Akwilapo pia alisema uimarishaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa kusogeza huduma hizo karibu zaidi na wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Msengi aliwapongeza wajumbe hao kwa kuaminiwa kushika nafasi hizo na kuwataka kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viapo walivyokula na kufanya kazi kwa weledi.

Amesema, wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni kiungo muhimu katika mfumo wa utatuzi wa migogoro ya ardhi, hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa uadilifu ili kujenga imani kwa wananchi.

“Uwepo wa wajumbe wa mabaraza ya ardhi katika wilaya zenu sasa utawezesha wananchi kupata huduma karibu zaidi badala ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo,” alisema.

Ameongeza kuwa, hatua hiyo itasaidia kupunguza gharama na muda ambao wananchi walikuwa wakitumia kufuata huduma za utatuzi wa migogoro ya ardhi katika maeneo ya mbali.

Wajumbe walioapishwa wanatoka katika wilaya za Mtwara, Tandahimba, Newala pamoja na wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara.

Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuimarisha Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya ili kuongeza ufanisi katika kusikiliza na kutatua migogoro ya ardhi kwa wakati, jambo litakalosaidia kuimarisha usalama wa milki na kuleta utulivu katika jamii.

WAZIRI NDEJEMBI ATOA SIKU 14 KWA MKANDARASI KUREJEA MRADI WA UMEME SONGEA-MAHUMBIKA

March 07, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu, Tunduru


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amempa siku 14 mkandarasi anayetekeleza mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Mahumbika kupitia Tunduru na Masasi kurejea eneo la mradi na kuendelea na kazi mara moja.

Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya Kalpataru Projects International Limited, ambayo ina jukumu la kujenga vituo vya kupoza umeme katika wilaya za Tunduru, Masasi na Mahumbika.

Akitoa agizo hilo Machi 7, 2026 wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, Ndejembi amesema mkandarasi huyo hapaswi kupewa kazi nyingine yoyote ya serikali hadi atakapokamilisha mradi huo ambao utekelezaji wake umechelewa kinyume na masharti ya mkataba.

Aidha, Waziri huyo amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati kumuandikia barua ya onyo mkandarasi huyo, akieleza kuwa tayari walikutana na uongozi wa kampuni hiyo jijini Dodoma na kukubaliana kuwa wangeanza kazi ndani ya siku 25 baada ya kulipwa fedha walizokuwa wanadai tangu Desemba 2025.

Hata hivyo, amesema hadi sasa mkandarasi huyo hajarejea katika eneo la mradi wala kuanza kazi.


“Huyu mkandarasi anafanya kazi kwa kusuasua sana. Walilipwa fedha mwezi Desemba na tukakubaliana ndani ya siku 25 wawe wamerudi site na kazi ianze, lakini muda wote umeisha na hakuna kinachoendelea,” amesema Ndejembi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, mradi huo ulipaswa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili na kukabidhiwa mwishoni mwa mwaka huu, lakini hadi sasa utekelezaji umefikia takribani asilimia 50 pekee.


Amesema mradi huo ni sehemu ya mpango wa serikali wa kuunganisha mikoa ya kanda ya kusini ambayo ni Ruvuma, Lindi na Mtwara kwenye gridi ya taifa ili kuboresha upatikanaji wa umeme wa uhakika.

“Wananchi wa Kusini wanahitaji umeme wa uhakika na serikali imeweka kipaumbele katika kutatua changamoto hiyo kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi huu. Haiwezekani mkandarasi akachelewesha kazi hii,” amesema.

Ameongeza: “Baada ya onyo tutakalompa, endapo ataendelea kusuasua tutachukua hatua zaidi.”



&&&

WANANCHI ZAIDI YA 13,000 WANUFAIKA NA SAMIA ARDHI KLINIKI NCHINI

March 07, 2026 Add Comment



MTWARA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amesema jumla ya wananchi 13,550 wamejitokeza kupata huduma mbalimbali za sekta ya ardhi kupitia Samia Ardhi Kliniki iliyofanyika katika mikoa yote 26 nchini.



Dkt. Akwilapo amesema hayo wakati akifunga rasmi Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026, akisema kliniki hiyo imekuwa jukwaa muhimu la kusogeza huduma za ardhi karibu na wananchi hususan wanawake.



Amesema, kati ya wananchi waliojitokeza katika kliniki hizo, wanawake walikuwa 8,725 sawa na asilimia 64.4 huku wanaume wakiwa 3,892 sawa na asilimia 35.7, jambo linaloonesha mwitikio mkubwa wa wanawake katika kutumia fursa zinazotolewa na Serikali.


Aidha, Waziri Akwilapo amesema, jumla ya hatimiliki 3,131 zimetolewa kwa wananchi waliokamilisha taratibu za umilikishwaji wa ardhi ambapo hatimiliki 2,081 sawa na asilimia 57.4 zimetolewa kwa wanawake na hatimiliki 1,543 sawa na asilimia 43.6 zimetolewa kwa wanaume.


Amefafanua kuwa, hatua hiyo imeongeza usalama wa milki kwa wananchi pamoja na kuimarisha uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.


“Ardhi ni msingi wa uchumi wa mwananchi na Taifa. Mwanamke anapomiliki ardhi kisheria anapata uwezo mkubwa wa kuwekeza, kufanya shughuli za uzalishaji na hata kupata mikopo katika taasisi za fedha,” alisema.


Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi amesema, Samia Ardhi Kliniki imenufaisha wanawake kwa kuwaelimisha jambo alilolieza kuwa limelenga kuwawezesha na kulinda haki na kutatua changamoto zao.


‘’Kupitia Kliniki hiyo wanawake walipewa huduma mbalimbali ambazo ni elimu ya kumiliki ardhi, ushauri wa kitaalamu kuhusu masuala ya ardhi pamoja na utoaji hati’’ amesema Kanali Msengi.

RAIS WA BURUNDI MHE. ÉVARISTE NDAYISHIMIYE AWASILI KIA KUSHIRIKI MKUTANO WA 25 WA WAKUU WA NCHI WA EAC

RAIS WA BURUNDI MHE. ÉVARISTE NDAYISHIMIYE AWASILI KIA KUSHIRIKI MKUTANO WA 25 WA WAKUU WA NCHI WA EAC

March 07, 2026 Add Comment




Rais wa Jumhuri ya Burundi Mheshimiwa Évariste Ndayishimiye amewasili katika Uwanja wa Ndega wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) Mkoani Kilimanjaro, kushiriki katika Mkutano wa 25 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) unaofanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika Makao Makuu ya Jumuiya jijini Arusha.

Akiwasili Mkoani humo amepokelewa na Mhe. Mahmoud Thabit Kombo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiambatana Viongozi Waandamizi mbalimbali wa Serikali.

MHE.SALOME AIBANA KAMPUNI YA DONGFANG KWA KASI ISIYORIDHISHA MRADI WA UMEME MALAGARASI

March 07, 2026 Add Comment

 



📌*Atoa maelekezo mahsusi kwa Mkandarasi na Wasimamizi wa mradi*


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba leo amekagua utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa Malagarasi (MW 49.5) unaotekelezwa katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ambapo ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji.

Akiwa katika Kijiji cha Mazungwe wilayani Uvinza Mhe Salome amekagua sehemu mbalimbali za mradi ikiwemo ujenzi wa tuta na uchepushaji mto, ujenzi wa jengo la kuendeshea  mitambo na kambi za wafanyakazi ambapo hakukuta wafanyakazi wa kutosha kama ambavyo mkataba unaelekeza.

Kutokana na hilo, Naibu Waziri wa Nishati amemuagiza mkandarasi kampuni ya Dongfang ya China kuhakikisha kuwa anaongeza wafanyakazi,  vifaa vya kazi na ndani ya mwezi mmoia awe amejenga kambi ya wafanyakazi.


Aidha,  amemtaka Mkandarasi kuwasilisha ratiba mpya  ya utekelezaji wa kazi.

Vilevile, ameagiza wasimamizi wa mradi wa Malagarasi kutoka Kampuni ya Mkandarasi  Mshaurii na TANESCO kuhamia katika eneo la mradi ndani ya mwezi  mmoja ili kuweza kuusimamia mradi huo kwa ukaribu.


"Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Nishati kuzalisha megawati 8000 za umeme ifikapo 2030, hatutakubali mtu atukwamishe katika kufikia malengo haya. Mkandarasi hakikisha unakamilisha kazi ifikapo Oktoba 2027 kama mkataba unavyoelekeza." Amesisitiza Mhe.Salome

Aidha, amemtaka Mkandarasi  Mshauri kampuni ya Multiconsult Norge AS ya Norway na Norplan kutoka Tanzania kuhakikisha kuwa wanamsimamia mkandarasi ipasavyo ili mradi ukamilike kwa wakati na kwa viwango stahiki.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Dinah Mathamani ameeleza kuwa uongozi wa wilaya hiyo utasimamia kwa karibu maelekezo yanayotolewa na Wizara ili mkandarasi atekeleze kazi kulingana na.mkataba.

Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amesema utekelezaji wa mradi wa Malagarasi kwa saaa ulipaswa kuwa kwenye asilimia 28 ila  umefikia asilimia 23.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea  kumsimamia kwa karibu mkandarasi  ili amalize kazi kwa wakati.


Sehemu nyingne zinazohusisha mradi wa Malagarasi ni upelekaji umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.

Pia ujenzi wa njia ya msongo wa kV 132 kutoka eneo la mradi hadi Kidahwe ambao umekamilika kwa asilimia 100.






TPA YASHEHEREKEA MAADHIMISHO YA SIKU YA WANAWAKE KWA KUTOA MSAADA WA MASHINE YA KUWASAIDIA WATOTO WACHANGA KUPUMUA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA TANGA-BOMBO

March 07, 2026 Add Comment




Na Oscar Assenga,TANGA


Watumishi Wanawake  Bandari ya Tanga imesheherekea maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani kwa kutoa msaada wa Mashine ya Kuwasaidia watoto wachanga kupumua na Oyxgen Flowmeter  katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga-Bombo vyenye  thamani ya zaidi ya Milioni 5.


Akizungumza wakati akikabidhi msaada huo,Afisa Rasimali Watu wa Bandari ya Tanga  Bi. Sharifa  Konshuma Nuhu  alisema wamekuwa wakitumia siku hiyo kufanya matendo ya huduma kwa jamii zinazowazunguka na mwaka huu wameamua kwenda Bombo Hospitali kwa ajili ya kutoa msaada

Alisema kwamba msaada huo ni kuchangia nguvu zao kwa juhudi za Serikali kuhakikisha wanaboresha afya za watoto na raia wa nchi na wao walichagua kutoa mashine hizo kwa  wodi ya watoto wachanga wanaozaliwa kutokana na changamoto mbalimbali na kutambua umuhimu wa watoto .

Alisema kwamba watoto ni Taifa la kesho ambalo linatakiwa lijengwe  hivyo wanahitaji watoto wenye nguvu,watu wenye nguvu ambao wataleta mchango mkubwa kuhakikisha nchi inasonga mbele.

“Tulifika hapa tukafahamu mahitaji na Mkuu wa Idara ya Watoto wanachangamoto hizo za watoto hivyo tukaona tuwashike mkono bombo kutokana na Hospitali ya Rufaa ya  Bombo ndio hospitali zote wagonjwa wanapewa rufaa kutoka wilayani kufika hapa kwa kiasi kidogo ambacho tumekifanya kitakuwa kimeongeza huduma”Alisema

Hata hivyo alisema kwamba vifaa vyenye thamani ya zaidi ya milioni 5 waliona wachangie ili kuweza kufikisha malengo na wanajisikia furaha na faraja kutokana na furaha ya mama ambao wanapata watoto salama na huzuni kwa wale wanaowazaa wenye changamoto .

Awali akizungumza baada ya kupokea msaada huo ,Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hosptali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga-Bombo Dkt Abdi Msangi aliwashukuru kwa msaada huo ambao wameutoa kutokana na kufika wakati muafaka kutokana na uwepo wa upungufu mkubwa wa vifaa vya kuwahudumia watoto na watoto wachanga wenye matatizo ya upumuaji

Alisema hasa ukizingatia kumekuwa na ongezeko kubwa kwa watoto wanaozaliwa na wanaopewa rufaa kwenda kwenye hospitali hiyo kupata huduma hizo ambao wanakuwa na changamoto za kupumua kwa hiyo wanashukruu kwa msaada huo ambao utaendelea kuboresha huduma wanazotoa kwenye Hospitali hiyo.

Alisema huduma hizo zitaendelea kuboreshwa hasa katika idara ya watoto na watoto wachanga huku akiwahimiza wadau wengine waliopo Tanga na nje kuendelea kuwasapoti kwenye nyanja mbalimbali za utoaji huduma na hiyo itasaidia kuboresha huduma na kukava ile gepu.

Naye kwa upande wake Daktari Bingwa wa Watoto katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tanga-Bombo Dkt Mohamed Salehe alisema kwamba wanawashukuru TPA Tanga kwenda na  kutembelela wodi ya watoto na kuwapelekea zawadi kati yao mashine ya Simpapu kuwawezesha hasa watoto waliozaliwa kabla ya siku zao (watoto  ) kuweza kupumua.

Alisema na  mashine ya  Suction ambayo inasidia kuvuta katika njia ya hewa ikiwa  kuna uchafu kwa mtoto na mashine nyengine ambazo ni msaada mkubwa kwenye wodi yao pamoja na hayo wameweza kutoa zawadi kwa wakina mama na watoto na wamefarijika kwa ujio wao na wameona hispitali yao imeweza kuonwa na uhitaji ni mkubwa.

Aidha alisema kwamba changamoto za hospitali hazikoesekana kutokana na hospitali ya mkoa wanapata watoto wengi wanaolazwa na kupelekea mahitaji waliokuwa nayo yanavuka uwezo hospitali walionao.

Aliongeza kwamba vifaa vimefika wakati muafaka kwa maana idadi ya watoto wanaolazwa inaongezeka kadri siku zinavyokwenda kuonekana umuhimu wa hiyo huduma kutokana nawali walipokuwa wakizaa watoto njiti walikuwa wanaona hawana uwezo  wa kuweza kuishi.

“Lakini baada ya kuona huduma zipo watu wanaona umuhimu wa kuwapeleka Hospitali watoto kupata huduma huku akieleza hizo mashine zitakuwa msaada mkubwa na tunawaomba na wadau wengine waone umuhimu wa kujitokeza kuwasaidia kuokoa maisha na kuwasaidia “Alisema


Mwisho.