Na: Dk. Reubeni Lumbagala, Tanga
Maji ni kimiminika muhimu kwa maisha na uhai wa viumbei. Maji hutumika kuanzia asubuhi, mchana, jioni hadi usiku. Hutumika kwa matumizi ya nyumbani kama kupikia, kufulia na kuogea. Hutumika katika shughuli za kiuchumi kama viwandani, mashambani, migodini, masokoni kutaja kwa uchache. Maji hayana mbadala, panapohitajika maji, hakuna namna nyingine bali kuyatafuta na kukidhi haja yake. Hakuna siku inaweka kupitia bila kutumia maji. Maji ni uhai na maji ni maisha. Binadamu anahitaji maji kila siku.
Tanzania imebarikiwa kuwa na vyanzo vingi vya maji. Mathalani; bahari, maziwa, mito, mabonde. Vyanzo hivi husaidia kupata maji kwa matumizi mbalimbali. Kutokana na ongezeko kubwa la watu nchini na shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, mahitaji ya huduma ya maji pia yameongezeka sana. Wizara ya Maji yenye dhamana ya usambazaji wa huduma ya maji katika maneno mbalimbali nchini ina wajibu mkubwa wa kuhakikisha maji yanawafikia wahitaji ili kuchochea shughuli mbalimbali za kimaendeleo nchini.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ni mdau mkubwa wa sekta ya maji. Anatambua umuhimu wa maji kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Kutokana na hilo, amekuwa akiongeza fedha katika bajeti ya Wizara ya Maji kila mwaka, jambo linalosaidia utekelezaji wa miradi ya maji ambayo inakwenda kutatua changamoto za maji katika maeneo mbalimbali nchini na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwani maji ni kiungo muhimu sana. Mathalani kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Bajeti ya Wizara ya Maji ilikuwa Sh. 1.01 trilioni ambapo katika fedha hizo, Sh. 943.22 bilioni zilikuwa ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Hii inaonyesha namna Wizara ya Maji ilivyojizatiti kutatua kero za wananchi kwa kupeleka fedha nyingi kwenda kwenye miradi ya maji.

Rais Dk. Samia pia ameelekeza Wizara ya Maji kufanikisha mradi kabambe wa Gridi ya Taifa ya Maji kama ilivyo Gridi ya Taifa ya Umeme inayosimamiwa na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha nchi inakuwa na uhakika wa maji kwa shughuli mbalimbali za maendeleo. Kwa nchi yetu yenye utajiri wa vyanzo vya maji, mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji ni suala muhimu hasa kipindi hiki ambacho dunia inapitia changamoto ya mabadiliko ya tabia ya nchi.

Gridi ya Taifa ya Maji itakusanya maji kutoka vyanzo mbalimbali vya maji nchini kwa matumizi ya kimaendeleo. Kilimo ambacho ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu kinahitaji sana raslimalimaji kwa ajili ya umwagiliaji. Kilimo cha kutegemea maji ya mvua pekee hakitoi uhakika kwa kupata mavuno kwani endapo kutatokea ukame au uhaba wa mvua, mazao yatanyauka na kufa kabisa. Uwepo wa maji ya kutosha unatoa uhakika wa kuvuna, kupata chakula na fedha baada ya kuuza mazao ndani na nje ya nchi. Maji yanawezesha pia uzalishaji wa umeme wa nguvu za maji (Hydo-Electric Power - HEP).

Maji ya uhakika yanatoa uhakika wa uendelevu wa shughuli za ufugaji. Wanyama na ndege watapata maji ya kunywa na majosho ya kuogeshea wanyama. Uvuvi unategemea uwepo wa maji, ukosefu wa maji unarudisha nyuma shughuli za uvuvi ambazo ni muhimu kwa uchumi wetu. Maeneo ya biashara kama masokoni vilevile wanahitaji maji kwa ufanisi wa shughuli zao. Wachimbaji wa madini na wahandisi wa ujenzi nao wanahitaji maji katika shughuli zao. Maeneo ya taasisi kama shule na hospitali, nao bila maji maisha hayaendi.
Katika kufanyia kazi maelekezo ya Rais Dk. Samia kuhusiana na mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji, hivi karibuni Waziri wa Maji Jumaa Aweso, Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Mwajuma Waziri pamoja na watendaji wa sekta ya Maji walifanya ziara katika Jimbo la Shan Dong Kaskazini mwa China kuona na kujifunza namna walivyofanikiwa kuviunganisha vyanzo vya mito na maziwa katika Gridi ya Taifa ya Maji kutoka Kaskazini hadi Kusini mwa China.
Kimsingi, mpango uliopo nchini ni kuviunganisha vyanzo mbalimbali vya maji nchini kama vile Maziwa ya Viktoria, Tanganyika na Nyasa pamoja na mito ya Rufiji, Kagera, Kiwira, Wami, Pangani, Ruvu na Ruvuma na vyanzo vingine ili kuwa na uhakika wa maji kwa maendeleo ya sekta mbalimbali. Katika kutekelekeza miradi huu, ni vyema wananchi tukawa mabalozi wazuri wa kutunza vyanzo vya maji vilivyopo na kutunza mazingira kwa ujumla. Tukumbuke maji hayana mbadala, kila mtu anahitaji maji. Kwa hakika, mafanikio ya kuwa na Gridi ya Taifa ya Maji ni uhakika wa kupata maendeleo endelevu. Tuunge mkono mradi huu muhimu kwa manufaa ya kizazi cha leo na kijacho. Tafakari.
Maoni: 0620 800462.