HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

NGORONGORO NGOMA INOGILE

NGORONGORO NGOMA INOGILE

May 05, 2026 Add Comment





Kutoka Pemba, Unguja, Mji mkongwe, Bagamoyo, Kondoa, Magofu ya kilwa, paa la mlima kilimanjaro na maeneo mengine ya Tanzania, wadau wa urithi wa dunia wamekutana katika Makumbusho ya Urithi Geopark Karatu Mkoani Arusha yanayosimamiwa na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa lengo la kuadhimisha Urithi wa Dunia Afrika yaliyoanza leo tarehe 04/05/2026 hadi tarehe 05/05/2026.

Wakiwa katika jengo la makumbusho ya Urithi Geopark Wadau hao wameelezwa jinsi Ngorongoro ilivyo ni utajiri wa urithi wa dunia kutokana na uumbwaji wake uliotokana na mlipuko wa volcano zaidi ya miaka milioni mbili iliyopita na kutengeneza kasoko iliyokusanya asili, uhai wa binadamu, mifumo ya ikolojia, na ustawi wa viumbe mbalimbali.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru amewashukuru wadau wote hasa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kwa kuipa fursa Ngorongoro kuandaa na kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo kwa mwaka huu.

Wadau wa urithi wa duania wakiwa katika Makumbusho ya Urithi Geopark walipata fursa ya kuelezewa kuhusu uthibitisho wa wasomi unaoeleza wazi historia ya chimbuko la binadamu wa kale aliyepatikana katika bonde la olduvai takribani milioni 2 iliyopita na ushahidi wa Nyanyo za binadamu wa kale katika eneo la Laetoli takribani miaka 3.6 iliyopiTa ambapo binadamu hao walitembea kwa miguu miwili.

Taasisi zinazoshiriki maadhimisho hayo ambazo zinasimamia maeneo ya urithi wa dunia ni pamoja na Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro (NCAA), Shirika la hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) Mamlaka ya Uzimamizi wa Wanyamapori (TAWA), Wakala wa Huduma za misitu Tanzania (TFS), pamoja na wawakilishi wa maeneo ya urithi wa dunia kutoka Zanzibar.


TANZANIA NA KENYA ZASAINI MAKUBALIANO YA USHIRIKIANO SEKTA YA NISHATI

May 05, 2026 Add Comment


 📌*Ni kupitia mauziano ya umeme na upembuzi yakinifu mradi wa Bomba la Gesi Dar-es-Salaam- Mombasa*


Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi na Waziri wa Nishati na Petroli wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Opiyo Wandayi wamesaini makubaliano ya ushirikiano ya kuanza mauziano ya umeme baina ya Tanzania na Kenya pamoja na upembuzi yakinifu wa mradi wa ujenzi wa bomba la gesi asilia kutoka Dar es Salaam hadi Mombasa.

Makubaliano hayo yamefanyika Mei 04, 2026 Ikulu jijini Dar es Salaam mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Dkt. William Samoei Ruto ambaye yuko nchini kwa ziara yake ya kitaifa.

TUME HURU YA TAIFA YA UCHAGUZI YAMKABIDHI RASMI MGOMBEA UBUNGE WA CCM JIMBO LA ISIMANI FOMU ZA KUGOMBEA UBUNGE

May 05, 2026 Add Comment

 

TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imemkabidhi rasmi fomu za kugombea ubunge wa jimbo la Isimani kwa Emanuela Mtatifikolo Kaganda, kwa ajili ya Uchaguzi Mdogo unaotarajiwa kufanyika Juni 1 mwaka huu.


Zoezi hilo limefanyika katika ofisi za tume zilizopo Ihemi chini ya usimamizi wa Mkurugenzi wa Uchaguzi jimbo la Isimani, Caroline Ang’weni Otieno.

Emanuela alikabidhiwa fomu hizo akisindikizwa na viongozi mbalimbali wa wilaya akiwemo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Iringa Vijijini, Costantino Kihwele ambapo baada ya kupokea fomu, Emanuela aliwashukuru viongozi na wanachama wote kwa kujitokeza, akisisitiza kuwa ana dhamira ya kutoa mchango chanya kwa maendeleo ya jimbo la Isimani.

Katika hotuba yake, aliwatambua viongozi wa jumuiya zote za chama ikiwemo jumuiya ya wazazi, vijana na UWT, pamoja na madiwani na viongozi wa ngazi mbalimbali.

Aliweka wazi kuwa, licha ya jimbo hilo kupitia kipindi kigumu kutokana na msiba wa aliyekuwa mbunge, wananchi wamethibitisha umoja na mshikamano mkubwa.

Emanuela alitoa shukurani za pekee kwa uongozi wa chama kuanzia ngazi ya shina hadi taifa, kwa kusimamia mchakato wa uteuzi kwa haki na uwazi na alipongeza pia wagombea wenzake walioshiriki mchakato huo na kuonyesha umoja baada ya kukamilika kwa uteuzi.

Aidha, alisisitiza kuwa jimbo la Isimani tangu kuanzishwa kwake limeongozwa na kiongozi mmoja, marehemu William Vangimembe Lukuvi, ambaye alifanya kazi kubwa ya kuliletea maendeleo.

Aliahidi kuendeleza misingi ya maendeleo iliyoachwa na kiongozi huyo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Iringa Vijijini, Costantino Kihwele, alimpongeza Emanuela kwa kuteuliwa na kamati kuu kuiwakilisha CCM kwenye uchaguzi huo mdogo.

Aliwahimiza wanachama kuendelea na umoja na maandalizi ya kampeni, akieleza kuwa chama kitafanya kampeni za kidiplomasia na za ushahidi wa kazi zilizofanyika.

Kihwele pia aliwapongeza wagombea wengine waliokuwa kwenye mchakato wa awali kwa kuonyesha uzalendo na kukubali matokeo, akiahidi kuwa watashirikishwa kikamilifu katika kampeni zitakapoanza rasmi.

Viongozi na washiriki wa mkutano huo walionyesha hamasa ya pamoja, huku wakiahidi kumpa mgombea wao ushindi wa kishindo katika uchaguzi wa Juni 1.






MBUNGE MWAKIOJA ATANGAZA NEEMA YA SOKA WILAYA MKINGA,AGAWA VIFAA VYA MICHEZO KWA TIMU ZINAZOSHIRIKI LIGI YA WILAYA

May 04, 2026 Add Comment


>Agawa vifaa vya michezo kwa timu zote zinazoshiriki Ligi ya wilaya ya Mkinga

Na Oscar Assenga, MKINGA

Mbunge wa Jimbo la Mkinga mkoani Tanga (CCM), Twaha Mwakioja, ameahidi kushirikiana na wadau mbalimbali wa michezo kuinua kiwango cha soka wilayani humo kwa kuwekeza katika elimu na maendeleo ya waamuzi pamoja na makocha.

Akizungumza wakati wa mchezo wa Ngao ya Jamii uliokwenda sambamba na uzinduzi wa Ligi ya Wilaya ya Mkinga, uliofanyika katika Uwanja wa Chamazi, Kata ya Matamba, Mwakioja alisema lengo lao ni kuwekeza katika michezo kwa vijana ili kuwapatia ajira, kuboresha afya zao, pamoja na kuimarisha amani, mahusiano mema na ushirikiano miongoni mwao.

Alieleza kuwa dhamira yao ni kuwashika mkono vijana ili waweze kupiga hatua kutoka ngazi ya wilaya, kwenda mkoa, kanda na hatimaye ligi za juu, huku yeye akiwa bega kwa bega nao kuhakikisha wanafikia malengo yao.

Mbunge huyo alibainisha kuwa wamepata taarifa ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali, ikiwemo uhaba wa makocha na waamuzi wenye sifa. Hivyo, wamejipanga kuwekeza katika mafunzo ya makocha ili kila kata iwe na angalau kocha mmoja mwenye ujuzi na mafunzo rasmi, pamoja na kuandaa waamuzi wenye vyeti ili kuboresha usimamizi wa michezo.

Alisisitiza kuwa uwekezaji huo utaenda sambamba na ushirikiano na Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga katika kukuza na kuendeleza vipaji vya vijana.

Aidha, alisema mpango wao ni kuhakikisha kila kata na kijiji kinakuwa na timu ya mpira wa miguu inayoshiriki ligi ya wilaya. Aliongeza kuwa watawekeza zaidi ili kuibua timu imara zitakazoweza kushiriki ligi za ngazi ya mkoa, kanda na hatimaye Ligi Kuu, hatua itakayosaidia kuitangaza Mkinga katika ramani ya soka nchini.

Katika kuonyesha dhamira hiyo, Mwakioja alikabidhi jezi na mipira kwa timu zinazoshiriki ligi hiyo, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha na kusaidia maendeleo ya michezo wilayani humo.

Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Fadhili Habibu, alisema ratiba ya ligi hiyo imeanza Mei 4 katika kituo cha Mkinga, huku kituo cha Maramba kikitarajiwa kuanza Mei 6 (Jumatano), ambapo kutakuwa na vituo vinne vitakavyochezwa katika Kijiji cha Maramba, ikiwa ni pamoja na mechi kati ya Viva Dynamo na Maramba FC.

Habibu alisema lengo la ligi hiyo ni kusimamia na kuibua vipaji vya vijana, pamoja na kuwapa mwelekeo wa maendeleo yao kisoka. Alimshukuru mbunge kwa kujitoa na kushirikiana nao katika kufanikisha malengo hayo.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Hassan Zumo, alimpongeza mbunge kwa juhudi zake za kuendeleza michezo wilayani humo, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza hamasa na matarajio ya ushindani mkubwa katika ligi hiyo, hasa baada ya timu kukabidhiwa vifaa.

Zumo aliongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 2008, wamekuwa wakipeleka vilabu katika mashindano ya ngazi ya mkoa lakini wamekuwa wakikwama kutokana na changamoto za kifedha. Hata hivyo, alisema kupitia uongozi wa Mbunge Mwakioja, wana matumaini ya kupata timu itakayoweza kufika hadi Ligi Kuu.

Aidha, timu zinazoshiriki mashindano hayo zimeahidi kujituma na kupambana kwa juhudi zote ili kuhakikisha ligi hiyo inaleta mafanikio na tija kwa vijana wa Wilaya ya Mkinga.




WANANCHI WA DODOMA WAPONGEZA JUHUDI ZA SERIKALI MKAKATI WA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

May 04, 2026 Add Comment

 



Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Wananchi wa Dodoma wamepongeza juhudi za Serikali kupitia mkakati wa kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, wakieleza kuwa mkakati huo unasaidia kuboresha afya, kuokoa muda na kulinda mazingira.
Hayo yamejiri leo tarehe 4 Mei 2026 katika Soko la Mavunde, Chang’ombe, ambapo wananchi wamepata elimu ya nishati safi ya kupikia kwa nadharia na vitendo, ikiwemo mafunzo ya jinsi ya kutumia nishati hizo kwa usahihi na kwa ufanisi zaidi katika shughuli za upishi wa kila siku.
Baadhi ya wananchi waliohudhuria wamesema kuwa elimu hiyo ya vitendo imewasaidia kuelewa kwa urahisi faida za nishati safi, hususan kupunguza moshi majumbani unaochangia magonjwa ya njia ya hewa na kurahisisha shughuli za upishi.
Aisha Ramadhani, mmoja wa wananchi waliohudhuria na ni mkazi wa Kata ya Chang’ombe, amesema amefurahishwa na kampeni hiyo inayoendelea jijini Dodoma, akibainisha kuwa elimu aliyoipata imemsaidia kubadili mtazamo wake kuhusu matumizi ya nishati, na sasa anaelewa vizuri faida za kutumia nishati safi kama vile kupunguza matumizi ya kuni na mkaa, kuokoa muda pamoja na kuboresha afya ya familia.
Akizungumza katika eneo hilo, mtaalamu kutoka Wizara ya Nishati, Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia, Nsajigwa Maclean, amesema Serikali inaendelea kutekeleza mkakati kwa kuhakikisha nishati safi ya kupikia inapatikana kwa urahisi, kwa gharama nafuu na kuwafikia wananchi wa makundi yote bila kujali kipato au eneo wanaloishi.
Aidha, amefafanua kuwa serikali imeweka juhudi katika kutoa elimu endelevu kwa jamii kupitia mafunzo ya vitendo, ili kuhakikisha wananchi wanapata uelewa wa kina kuhusu matumizi salama ya nishati safi, pamoja na kuhimiza mabadiliko ya tabia kutoka matumizi ya kuni na mkaa kwenda nishati mbadala inayolinda afya na mazingira.
Wananchi waliohudhuria wameeleza kuridhishwa na juhudi hizo za Serikali na kuahidi kuendelea kuhamasishana juu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo yao wanayoishi.

KAMISHNA LUOGA NA MAKAMU BALOZI WA NEW ZEALAND WAJADILI MAENDELEO YA MRADI WA JOTOARDHI

May 04, 2026 Add Comment


Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mha. Innocent Luoga amekutana na Naibu Balozi wa New Zealand nchini, Nicholas Meehan ambapo wamejadiliana kuhusu ushirikiano katika miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia rasilimali ya jotoardhi.

Kikao hicho kimefanyika leo, tarehe 4 Mei 2026, katika Ofisi za Wizara ya Nishati Mtumba jijini Dodoma.

Akizungumza katika kikao hicho, Kamishna Luoga ameishukuru Serikali ya New Zealand kwa mchango wake katika miradi ya jotoardhi nchini kupitia programu ya Africa Geothermal Facility (AGF1) awamu ya kwanza iliyowezesha watumishi wa Kampuni ya Uendelezaji wa Jotoardhi Tanzania (TGDC) kujengewa uwezo wa kiufundi na kitaasisi, jambo lililowaongezea ujuzi wa kuendeleza kazi zao kwa weledi zaidi.

Anesisitiza kuwa mradi wa AGF1 awamu ya kwanza umefika tamati lakini Tanzania inahitaji ushirikiano huo uendelee ili kuendeleza rasilimali ya jotoardhi ambapo Tanzania inalenga kuzalisha takribani MW 130 kutokana na nishati hiyoi ifikapo 2030.

Amefafanua kuwa, Wizara kupitia TGDC imepanga miradi miwili ya kimkakati itakayoweza kufanikisha lengo hilo ambayo ni mradi wa Ngozi utakaozalisha megawati 60 pamoja na Kiejo-Mbaka utakaozalisha megawati 70.

Aidha, ameiomba New Zealand kuangalia uwezekano wa kufadhili miradi hiyo ya kimkakati, pia kusaidia kutafuta ufadhili wa miradi hiyo.

Kwa upande wake, Balozi Meehan ameeleza kuwa New Zealand inatambua ushirikiano mkubwa uliopo kati ya nchi hizo mbili hususan katika miradi ya jotoardhi huku akiahidi kuendeleza ushirikiano kupitia awamu ya pili ya programu ya Africa Geothermal Facility, pamoja na kutafuta nafasi za ufadhili katika masuala ya jotoardhi ili kuwawezesha wataalam wa Tanzania kuongeza weledi na ujuzi.

Kikao hicho kimehudhuriwa na wataalam kutoka Wizara ya Nishati, TGDC, pamoja na wawakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.





TUME YA TAIFA YA MIPANGO KUJENGA MIFUMO IMARA YA UFUATILIAJI NA TATHMINI UTEKELEZAJI WA DIRA 2050

May 04, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu, Kibaha-Pwani.


Imeelezwa kuwa Tume ya Taifa ya Mipango imekamilisha nyenzo zote za utekelezaji wa Dira 2050 ambazo ni Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/2027–2050/2051 (LTPP 2050), Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 (FYDP IV) na Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2026/2027 kuelekea Julai 1, 2026 ambapo utekelezaji wa Dira hiyo utaanza rasmi.

Hayo yameelezwa leo Mei 4, 2026 na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alipofungua mafunzo kwa Wakurugenzi wa Sera na Mipango, Wakurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini, na Wakuu wa Idara na Vitengo vya Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali yanayofanyika katika Chuo cha Uongozi Mwalimu Julius Nyerere, Kibaha - Pwani.

Dkt. Kida amewaambia washiriki wa mafunzo hayo kuwa, baada ya kukamilisha Dira 2050 na nyenzo zake, mafunzo hayo ni utekelezaji wa mkakati mahususi wa Serikali wa kujipanga kufanya utekelezaji wa Dira hiyo kwa kuhakikisha kunakuwepo na uelewa wa pamoja na utekelezaji unaolingana katika ngazi zote za Wizara, Taasisi za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa katika kuhakikisha mipango ya Kitaifa inatekelezwa kwa tija.

“ Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango inakamilisha Miongozo ya Upangaji (NPGs), Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Programu na mirado ya Maendeleo (NF-MEDeP) na Mfumo wa Kidigitali uitwao E-Delivery. Mfumo huu na miongozo hiyo italetwa kwenu na mafunzo stahiki yanaandaliwa kwa ajili yenu” Amesisitiza Dkt. Kida.

Aidha, Dkt. Kida amesema kupitia mafunzo hayo, washiriki watapata fursa ya kujifunza kwa vitendo (i.e. case studies), kubadilishana uzoefu, na kujenga uwezo katika hatua zote za mzunguko wa miradi ya maendeleo kuanzia uibuaji, upangaji, uchambuzi, uidhinishaji hadi utekelezaji na ufuatiliaji.






CBE YASISITIZA MCHANGO WA ALUMNI KATIKA KUENDELEZA VIJANA

May 04, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAHITIMU wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) (alumni) wametakiwa kutumia nafasi zao kuchangia maendeleo ya taifa kupitia taaluma, uzoefu na rasilimali walizonazo.

SAMIA ATOA BILIONI 20, CONTENT CREATORS WANUFAIKA NA BILIONI 2

May 04, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda amesema Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, zitahakikisha zinawawezesha vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari kwa kuwapa mitaji ya kukuza, kuendeleza na kuzalisha kazi zao katika ubora unaokidhi mahitaji ya soko kupitia mikopo yenye masharti nafuu.

Akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/2027, Mhe. Makonda amesema katika kutekeleza hilo, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa Shilingi bilioni 20 kwa ajili ya Mfuko wa Utamaduni na Sanaa, ambapo kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 2 tayari zimetolewa kwa ajili ya mikopo kwa Watengeneza Maudhui Mtandaoni (content creators).

Amesema fedha hizo zinalenga kuwasaidia Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi na kuongeza uzalishaji wa kazi zao.

Hatua hiyo inatajwa kuwa mkombozi kwa vijana wanaojiajiri katika sekta ya habari na ubunifu, kwani inafungua fursa mpya za upatikanaji wa mitaji, vifaa vya kisasa na kuongeza uzalishaji wa maudhui yenye ubora unaokidhi mahitaji ya soko la ndani na kimataifa.

“Fedha hizi zinalenga kuwawezesha Watengeneza Maudhui kupata vitendea kazi, kuboresha ubora wa kazi zao na kuongeza ushindani katika soko la kidijitali,” alisema Mhe. Makonda.

Alisema hatua hiyo inaashiria mabadiliko ya kifikra katika namna Serikali inavyotambua na kuwekeza katika kundi la vijana wabunifu, ambalo kwa muda mrefu limekuwa likikua kwa kasi bila mifumo madhubuti ya kulisimamia na kulikuza.

“Huu ni uwekezaji wa moja kwa moja katika ubunifu wa vijana na uchumi wa kidijitali, unaolenga kuongeza ajira na kipato kwa Watanzania,” aliongeza.

Kwa mujibu wa wadau wa sekta hiyo, upatikanaji wa mitaji ni changamoto kubwa inayokwamisha ukuaji wa maudhui ya kidijitali, hivyo hatua hiyo ya Serikali inatarajiwa kuongeza uzalishaji wa kazi bora, kukuza vipato na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha ubunifu wa maudhui katika ukanda wa Afrika Mashariki.



JAB YAPOKEA MAOMBI 4,139, WENGI WAPATA ITHIBATI

May 04, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

SERIKALI imeanza kuvuna matokeo ya mageuzi ya kidijitali katika sekta ya habari baada ya Waandishi wa Habari 3,357 kuthibitishwa na kupatiwa ithibati ndani ya kipindi cha chini ya mwaka mmoja kupitia mfumo wa kisasa wa TAI HABARI.

Mafanikio hayo ni hatua kubwa katika kuimarisha weledi, uwajibikaji na usimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, kwa kuwa kwa mara ya kwanza sekta hiyo imeanza kuwa na mfumo rasmi, wa kidijitali na unaowezesha kuchakata maombi na kuhakiki waandishi wanaokidhi vigezo kwa mujibu wa sheria ya Huduma za Habari.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma, Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Paul Christian Makonda, alisema kuanzia Julai 2025 hadi Aprili 2026, Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imepokea na kushughulikia jumla ya maombi 4,139 ya usajili kupitia mfumo huo wa TAI HABARI.

Kati ya maombi hayo, Waandishi wa Habari 3,357 waliokidhi vigezo vilivyoainishwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, wamepatiwa ithibati.
Katika hatua nyingine, Waziri Makonda alisema JAB imeshughulikia malalamiko 14 ya uvunjifu wa maadili ya taaluma ya habari, jambo linaloonesha kuanza kuimarika kwa mfumo wa uwajibikaji katika sekta hiyo.

Aidha, Mheshimiwa Makonda alisema Serikali kupitia JAB imeandaa mwongozo maalumu wa kisheria utakaowawezesha Waandishi wa Habari wakongwe walioathiriwa na mfumo wa ithibati kureiea katika mfumo rasmi, kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 ambayo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari.
Alisema kuwa sheria hiyo ilitungwa kwa ajili ya kukuza taaluma ya uandishi wa habari kwa kuweka mfumo wa kitaasis utakaosimamia sekta ya habari. 

“Mwongozo huu unaweka utaratibu wa kisheria wa kutambua na kuthibitisha umahiri wao kupitia tathmini maalumu ya uzoefu, weledi na maadili ya taaluma, na kuwawezesha kupata ithibati kwa mujibu wa sheria.” Alisema Mhe. Makonda

Hatua hii inalenga kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuhakikisha hata waandishi wa habari wenye uzoefu mkubwa wanapata nafasi ya kuingia katika mfumo rasmi unaotambuliwa kisheria.