HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

RAIS DKT SAMIA AWASILI NCHINI UGANDA KWA AJILI YA KUHUDHURIA SHEREHE ZA UAPISHO WA RAIS MTEULE WA NCHI HIYO YOWERI MUSEVENI

May 12, 2026 Add Comment
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Naibu Waziri Mkuu wa Tatu wa Uganda Mhe. Rukia Isaya Nakadama mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe nchini humo tarehe 12 Mei, 2026. Rais Dkt. Samia amewasili nchini Uganda kwa ajili ya kuhudhuria Sherehe za Uapisho wa Rais Mteule nchi hiyo, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni, zitakazofanyika katika Viwanja vya Kololo Jijini Kampala nchini humo.


RAIS SAMIA AONDOKA NCHINI KUELEKEA UGANDA KUHUDHURIA SHEREHE ZA UAPISHO WA RAIS MUSEVENI

May 12, 2026 Add Comment
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Uganda kuhudhuria Sherehe za Uapisho wa Rais wa nchi hiyo Mhe. Yoweri Kaguta Museveni tarehe 12 Mei, 2026. 













GPE, EP4R WARIDHISHWA NA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA ELIMU BUSWELU

May 12, 2026 Add Comment

Ujumbe wa wadau wa maendeleo ya elimu ukiwemo Global Partnership for Education (GPE) pamoja na Education Program for Results (EP4R) ukiongozwa na Morten Sigsgaard Mratibu wa Ushirika wa Nchi (GPE) umeridhishwa na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya elimu inayotekelezwa katika Shule ya Msingi na Sekondari Buswelu, Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza.

Akizungumza wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi hiyo Mei 11, 2026, Morten amesema miradi hiyo imeendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, hususan kwa wanafunzi wa elimu jumuishi.

Katika Shule ya Msingi Buswelu, inayohudumia wanafunzi 1,211 wakiwemo 176 wenye mahitaji maalumu, imefanikiwa kujenga bweni la wasichana wenye mahitaji maalumu kupitia ufadhili wa Serikali na GPE-LANES II.

Mradi huo9 umewezesha wanafunzi 80 kupata makazi salama ya bweni, huku huduma za bweni zikianza rasmi Mei 8, 2026 baada ya Serikali kuanza kutoa fedha za chakula.

Aidha, walimu na wanafunzi wameeleza mabadiliko chanya yaliyotokana na miradi hiyo, wakisema awali wanafunzi walikuwa wakisoma katika mazingira ya msongamano wa madarasa, lakini sasa wanapata nafasi ya kusoma katika mazingira bora na yenye nafasi ya kutosha, jambo lililoongeza umakini na ushiriki darasani.

Katika Shule ya Sekondari Buswelu, kupitia Programu ya EP4R, shule imepokea Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa vyenye viti na meza 100, mradi ambao tayari umekamilika na unatumika.

Baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wanasema awali walikuwa wakisoma wakiwa wamebanana kutokana na upungufu wa madarasa, hali iliyokuwa ikichangia usumbufu wakati wa masomo, lakini kwa sasa wanafurahia kusoma katika madarasa mapya yenye nafasi kubwa na mazingira rafiki ya kujifunzia.

Uongozi wa shule ulieleza kuwa miradi hiyo imechangia kuboresha ufaulu pamoja na kuongeza hamasa ya kujifunza.

Wadua wa maendeleo walitoa pongezi kwa Serikali kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu na kuahidi kuendelea kushirikiana katika kuboresha mazingira ya kujifunzia nchini.










TANZANIA KUENDELEA KUTUMIA AKILI UNDE KATIKA KUKABILIANA NA MAAFA

May 11, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu, Masvingo - Zimbabwe

TANZANIA imesema itaendelea kutumia teknolojia ya Akili Unde (AI) katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa tahadhari za mapema na kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali.


Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, wakati wa mkutano wa maandalizi ya Mkutano wa Sita wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika Mei 11, 2026 mjini Masvingo, Zimbabwe.

Alisema matumizi ya AI yatasaidia uchakataji na ufuatiliaji wa taarifa mbalimbali zinazoripotiwa kuhusu masuala ya maafa nchini, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa Serikali katika kufanya maamuzi ya haraka wakati wa majanga.


“Matumizi ya teknolojia ya Akili Unde yatawezesha uchambuzi wa taarifa kwa haraka, kutabiri hatari zinazoweza kujitokeza na kusaidia hatua za mapema za kukabiliana na maafa,” alisema Dkt. Yonazi.


Dkt. Yonazi alisema Serikali inaendelea kuweka mkazo katika maeneo muhimu yatakayosaidia kuwa na usimamizi wenye tija wa maafa ikiwemo utafiti wa kisayansi, matumizi sahihi ya Akili Unde, ushirikiano katika uhifadhi wa taarifa za matukio pamoja na matumizi ya menejimenti ya maarifa.

Aidha alisema Tanzania imeendelea kuwa mfano katika ukanda wa Kusini mwa Afrika kutokana na uwezo wake wa kuratibu na kusimamia maafa kwa mafanikio huku ikiendelea kuzuia, kupunguza madhara, kujiandaa na kurejesha hali pindi majanga yanapotokea.

Alifafanua kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na uwepo wa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema ambacho hufanya kazi saa 24 kupokea, kufuatilia na kuchambua taarifa za majanga kwa wakati halisi.


“Kituo cha Operesheni ya Maafa kimekuwa msaada mkubwa kwani kimerahisisha upatikanaji wa taarifa za mapema, uchambuzi wa takwimu za wakati halisi na upangaji wa mikakati ya kurejesha hali pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu namna ya kujiandaa na kukabiliana na maafa,” alisisitiza.


=MWISHO=

MENEJIMENTI YA WIZARA YA NISHATI YATEMBELEA MRADI WA EACOP TANGA, WAFIKIA 85% YA UTEKELEZAJI.

May 11, 2026 Add Comment

Menejimenti ya Wizara ya Nishati imetembelea mradi wa kimkakati wa kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani mkoani Tanga nchini Tanzania wa EACOP (East African Crude Oil Pipeline) katika leo tarehe 11 Mei 2026.

Menejimenti hiyo ikiongozwa na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga imepokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo pamoja na kujionea ujenzi wa kituo cha kupokea, kuchakata na ujenzi wa gati la kupakia mafuta.

Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amesema Wizara ya Nishati imejionea kazi nzuri inayoendelea kufanyika ambapo mradi huo unatekelezwa kwa wakati na umefikia asilimia 85 ya utekelezaji.

“Tumeridhishwa na utekelezaji wa mradi huu. Umezalisha ajira kwa Watanzania katika fani mbalimbali, pia umefungua fursa nyingi kwa wananchi wa Mkoa wa Tanga moja kwa moja na Taifa kwa ujumla, ikiwa ni pamoja na ushiriki wa wazawa. vile vile mradi huu umesaidia jamii kupitia ukarabati wa barabara, miradi ya maji na miradi mingine ya kijamii,” amesema Kamishna Luoga.

Akitoa maelezo ya mradi huo, Mhandisi wa Mradi wa Kituo cha Kuhifadhi Mafuta, Mhandisi Musa Msafiri amesema utekelezaji wa upande wa matenki ya kuhifadhi mafuta umefikia asilimia 94, ambao ni ujenzi wa matenki manne yenye uwezo wa kubeba mapipa 2,000,000.

Kwa upande mwingine, Mhandisi wa Ujenzi wa gati, Fred Mahenge amesema utekelezaji wa mradi wa upande wa kituo cha kupakia na kusafirisha mafuta baharini (Jet) ni zaidi ya asilimia 90.

Mradi huu umezalisha jumla ya ajira 1,834, ambapo Watanzania wamepata asilimia 84 ya nafasi zote za ajira.

Aidha mradi huu unahusisha ujenzi wa bomba la mafuta lenye urefu wa kilomita 1,443 kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani mkoani Tanga, ambapo mafuta yatapakiwa na kusafirishwa kwenda soko la dunia.







BALOZI MTEULE TANZANIA NCHINI KOREA AANZA RASMI MAJUKUMU

May 11, 2026 Add Comment
Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Jamhuri ya Korea Mheshimiwa Noel Kaganda amepokelewa rasmi katika Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Seoul kuanza rasmi majukumu yake ya uwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Jamhuri ya Korea.

KAMISHNA KUJI AZINDUA MRADI WA KUSAFIRISHA NA KUSAMBAZA UMEME KATIKA HIFADHI YA TAIFA MIKUMI

May 11, 2026 Add Comment


Na. Philipo Hassan - Mikumi

Mwisho mwa wiki ikiyopita, Kamishna wa Uhifadhi TANAPA CPA Musa Nassoro Kuji alizindua rasmi mradi wa kusafirisha na kusambaza umeme wa TANESCO ndani Hifadhi ya Taifa Mikumi. Mradi huo unaolenga kuboresha utoaji wa huduma ndani ya hifadhi, kuimarisha shughuli za uhifadhi na utalii, kuboresha matumizi ya nishati ya umeme kwa watumishi wa hifadhi na kuongeza fursa za uwekezaji katika sekta ya utalii.

Usambazaji wa umeme wa TANESCO ndani ya hifadhi utaboresha na kuleta mapinduzi makubwa kwenye upatikanaji wa nishati hiyo kwa watumishi, watalii, wawekezaji waliopo ndani ya hifadhi hiyo pamoja na wananchi ambao nao wamefaidika na umeme huo ambao pia umepita kwenye maeneo yao wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Menenejimenti ya hifadhi, Maafisa na Askari wa uhifadhi wakiongozwa na Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Augustine Masesa ambaye ndiye Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Mikumi, Meneja wa TANESCO Morogoro Kusini Mhandisi Lugata Masingija pamoja na wananchi wa maeneo jirani na hifadhi hiyo.

Kamishna Kuji aliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuidhinisha bajeti ya mradi huo pia Bodi ya Wadhamini ya TANAPA kwa usimamizi wa karibu wa shughuli za Shirika ikiwemo utekelezaji wa mradi huo.

Aidha, Kamishna Kuii aliupongeza uongozi wa TANESCO kwa utekelezaji wa mradi huo ambapo mbali na kuunga mkono jitihada za Serikali za uwepo wa nishati safi utaongeza kasi ya maendeleo kwa wananchi wa vijiji jirani vilivyonufaika na mradi huu,” alisema Kamishna Kuji.

Mradi huo unaweka historia mpya katika Hifadhi ya Taifa Mikumi kwa kuimarisha matumizi ya nishati safi na uhakika, hatua inayotarajiwa kuongeza ubora wa huduma, kuchochea uwekezaji wa utalii na kuendelea kufungua fursa za maendeleo kwa jamii zinazozunguka hifadhi hiyo.