HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

JAB: Uhuru wa Vyombo vya Habari Upo, Lakini Lazima Uendane na Maadili

March 17, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesisitiza kuwa uhuru wa vyombo vya habari nchini upo, unalindwa kisheria na unatambuliwa katika Katiba pamoja na Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, huku ikitoa wito kwa wanahabari kuzingatia maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kauli hiyo ya JAB imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo, Wakili Patrick Kipangula, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha moja kwa moja cha Hatua za Ushindi kinachorushwa na Kituo cha Televisheni cha Hope Channel Tanzania, leo Machi 17, 2026 jijini Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa kifungu cha 7 cha Sheria ya Huduma za Habari kinaweka bayana haki na uhuru wa vyombo vya habari, ikiwa ni pamoja na haki ya mwandishi wa habari kutafuta, kuchakata na kusambaza taarifa, huku wananchi wakiwa na haki ya kupata taarifa sahihi kuhusu maendeleo yanayowazunguka.

“Uhuru wa vyombo vya habari upo na unalindwa kisheria. Mwandishi ana haki ya kutafuta na kusambaza taarifa, na mwananchi ana haki ya kupata taarifa. Huu ndio msingi wa uwazi na uwajibikaji katika jamii,” amesema Wakili Kipangula.

Hata hivyo, amesisitiza kuwa uhuru huo unaambatana na wajibu wa kuzingatia maadili ya taaluma, akibainisha kuwa dhana ya uwajibikaji haipaswi kuchanganywa na kile kinachoitwa ukandamizaji wa vyombo vya habari.

Amebainisha kuwa baadhi ya malalamiko ya ukandamizaji yanatokana na kutokuzingatia misingi ya kitaaluma, hususan pale ambapo taarifa zinapotolewa bila uthibitisho, uwiano au kwa lugha isiyozingatia maadili.




“Ni muhimu kutofautisha kati ya uwajibikaji na ukandamizaji. Usipozingatia maadili ya taaluma, usiseme unakandamizwa. Uwajibikaji ni sehemu ya taaluma, na haupaswi kutafsiriwa kama kubanwa kwa uhuru wa habari,” amesisitiza Kipangula.

Katika hatua nyingine, Wakili Kipangula ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya sekta ya habari kupitia mageuzi ya kisheria na kisera, ikiwemo kufutwa kwa Sheria ya Magazeti iliyokuwa ikitajwa kuwa kandamizi na kuanzishwa kwa Sheria ya Huduma za Habari inayolenga kuimarisha uhuru, uwajibikaji na weledi katika tasnia hiyo.

Amesema maboresho hayo yameleta mwelekeo mpya unaowezesha vyombo vya habari na wanahabari kufanya kazi zao kwa uhuru zaidi, huku wakizingatia viwango vinavyokubalika kitaaluma na kisheria.

Aidha, ametoa wito kwa wanahabari kuendelea kuilinda taaluma yao kwa kuzingatia ukweli, usahihi na uwiano katika utoaji wa taarifa, sambamba na kuheshimu haki za wananchi za kupata taarifa sahihi na kwa wakati kwa mujibu wa Sheria ya Kupata Taarifa.

Amesisitiza umuhimu kwa waajiri kote nchini kuhakikisha wanapata wataalamu wenye sifa stahiki kuingia katika menejimenti zao, sanjari na kuwatumia waandishi wenye ithibati, katika kazi zote za kihabari ili kulinda na kuipa thamani taaluma ya uandishi wa habari.

TUMEONDOA VAT KATIKA UAGIZAJI WA MITUNGI YA GESI ILI KURAHISISHA UPATIKANAJI WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KWA WANANCHI- MHE. NDEJEMBI

March 17, 2026 Add Comment




Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema kuwa Serikali imeondoa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye uagizaji wa mitungi ya gesi (LPG), mitungi mikubwa ya gesi (LPG bulk facility) pamoja na carbonizers za kutengeneza mkaa mbadala ikiwa ni sehemu ya jitihada zinazofanywa na Serikali kupunguza bei na kurahisisha upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa wananchi.


Mhe. Ndejembi ameyasema hayo tarehe 17 Machi 2026 wilayani Morogoro, Mkoa wa Morogoro wakati akifungua Kongamano la Nishati Safi ya Kupikia lililoandaliwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Taasisi ya Uongozi likihusisha Wizara na Taasisi mbalimbali kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, Taasisi za kifedha, Asasi za kiraia pamoja na wazalishaji, wasambazaji na watumiaji wa nishati safi ya kupikia.


“Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan ameweka kipaumbele katika kuhakikisha nishati safi ya kupikia inapatikana kwa wananchi kupitia upatikanaji wa mitungi ya gesi, majiko banifu, gesi vunde na kupitia usambazaji wa umeme hadi ngazi ya vitongoji ambao unawezesha matumizi ya nishati ya umeme katika kupikia. Mpaka sasa TANESCO kupitia kampuni ya MECS imewezesha wateja 480 kupata majiko ya kupikia kwa umeme kwa kulipia kidogokidogo kupitia bili za umeme.” Amesema Mhe.Ndejembi


Ameeleza kuwa, mikakati ya Serikali ya kufikia asilimia 80 ya Watanzania wanaotumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034 na asilimia 75 ifikapo 2030 itawezekana endapo wadau wote watashirikiana, akisema kuwa tayari mwanga wa kufikia malengo hayo umeanza kuonekana kwani wakati Mkakati wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia unazinduliwa mwaka 2024, ni asilimia 6 tu ya Watanzania walikuwa wakitumia nishati safi ya kupikia na sasa hatua imepigwa hadi kufikia asilimia 23.2.


Katika kongamano hilo, Waziri Ndejembi amewasisitiza wadau wote kuweka nguvu katika kutoa elimu kwa wananchi ili kuongeza uelewa kuhusu nishati safi ya kupikia na hivyo kuleta mabadiliko ya tabia na mitazamo hasi juu ya nishati hiyo.


Pia amewataka kuongeza ubunifu na upanuzi wa miundombinu ya usambazaji wa nishati safi ya kupikia akieleza kuwa matumizi ya kuni na mkaa bado yanachangia zaidi ya asilimia 50 ya nishati ya kupikia kwenye kaya nyingi nchini.

Vilevile, ametaka Kongamano hilo la nishati safi ya kupikia litumike kama jukwaa la kuimarisha ushirikiano baina ya Serikali, Sekta binafsi na asasi za kiraia ili kutanua wigo wa upatikanaji wa suluhisho la nishati safi ya kupikia kwa kuwa nishati hiyo ni muhimu kiafya, kimazingira, kiuchumi na katika usawa wa kijinsia.




kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima amesema ajenda ya nishati safi ya kupikia ni kwa ajili ya maendeleo endelevu ya wananchi hivyo amemshukuru Rais, Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuifanya ajenda hiyo kuwa ni ya kitaifa huku akiwaasa wananchi wote kuiunga mkono.


Aidha, ameishauri Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na wadau wengine ikiwemo taasisi za fedha kuwawezesha wajasiriamali mkoani Morogoro kutumia fursa ya upatikanaji wa pumba zinazotokana na mpunga mkoani humo kutengenezea mkaa mbadala kutokana na wingi wa upatikanaji wake.


Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Bw. Nolasco Mlay amesema kongamano hilo linatoa fursa ya kipekee kwa wadau kutoka sekta za umma, binafsi, asasi za kiraia, pamoja na washirika wa maendeleo wa kimataifa kushirikiana, kubadilishana uzoefu, na kujadili mikakati ya kuendeleza ajenda ya nishati safi ya kupikia nchini Tanzania.


Awali, Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo alisema dhumuni la kufanyika kwa kongamano la nishati safi ya kupikia mkoani Morogoro ni pamoja na kukuza uelewa wa manufaa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kiafya, kimazingira na kiuchumi pamoja na kuhamasisha mashirikiano baina ya Serikali, Sekta binafsi na asasi za kiraia.


Aliongeza kuwa, kongamano hilo pia limelenga kuainisha changamoto, utatuzi pamoja na fursa katika matumizi ya nishati safi ya kupikia.



WANANCHI MKINGA WANUFAIKA NA UWEKEZAJI KATIKA KILIMO CHA MWANI

March 17, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu, Tanga.


Wananchi wa Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga wanatarajiwa kunufaika zaidi kiuchumi kupitia uwekezaji wa Serikali katika sekta ya kilimo cha mwani, hatua inayolenga kuongeza thamani ya mazao ya bahari na kuboresha maisha ya jamii za pwani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kaushio jipya na mashine mbili za kisasa za kusaga mwani uliofanyika tarehe 16 Machi 2026 katika Kijiji cha Kichaka Miba, Wilaya ya Mkinga, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Ummy H. Nderiananga, amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali kuimarisha uchumi wa wananchi wa maeneo ya pwani.

Mradi wa Kuimarisha Usalama wa Bahari unaratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Idara ya Menejimenti ya Maafa kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), na unatekelezwa na Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Tawi la Mwanza kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga ambapo Lengo lake ni kuimarisha ufuatiliaji na ulinzi wa bahari pamoja na kuongeza thamani ya rasilimali za baharini kwa manufaa ya jamii.

Mhe. Nderiananga amesema kupitia mradi huo, Serikali imenunua boti mbili za doria, kujenga kaushio la kisasa la mwani, kusimika mashine za kusaga mwani na kutoa mafunzo kwa vikundi vya wakulima. Ameongeza kuwa hatua hizo zitaboresha ubora wa mwani, kupanua masoko, kuongeza kipato cha wakulima na kusaidia kuzuia vitendo vya kihalifu baharini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP), Dkt. Guvenail Mkonoko, amesema kabla ya utekelezaji wa mradi huo wataalamu walifanya tathmini iliyobaini changamoto za mbinu duni za kilimo, ukaushaji usio salama na ukosefu wa miundombinu ya kisasa ya uchakataji. 





Naye mwakilishi wa wakulima wa mwani, Bi. Mwamvua Bwebwe, Ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwawezesha kuongeza uzalishaji, kupunguza upotevu wa mazao na kuboresha kipato chao.


=MWISHO=

EWURA, WRBWB NA TFS WAPANDA MITI 5,000 KUADHIMISHA WIKI YA MAJI DUNIANI MOROGORO

EWURA, WRBWB NA TFS WAPANDA MITI 5,000 KUADHIMISHA WIKI YA MAJI DUNIANI MOROGORO

March 17, 2026 Add Comment

Morogoro:

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo imeongoza kampeni ya kupanda miti mkoani Morogoro ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani, inayofikia kilele chake kila mwaka tarehe 22 Machi, kwa lengo la kulinda vyanzo vya maji na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza wakati zoezi hilo, Wilfred Mwakalosi, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, alisema taasisi hiyo kwa kushirikiana na Ofisi ya Bonde la Maji la Wami Ruvu na Wakala wa Huduma za Misitu ( TFS) wamefanikiwa kupanda miti zaidi ya 5,000 katika eneo linalozunguka mto Lukulunge, Kata ya Mzumbe, mkoani Morogoro.

Mwakalosi alibainisha kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuhifadhi mazingira, vyanzo vya maji na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa maji kqtika maeneo mbalimbali nchini. “Morogoro ni miongoni mwa maeneo yaliyokuwa na vyanzo vingi vya maji hapo awali, lakini kwa sasa hali imebadilika kwa kiasi kikubwa kutokana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, hivyo kutishia upatikanaji wa maji kwa wakazi wake” alieleza.

Mhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) wa Wilaya ya Morogoro, Stanley Kweka, alisema uharibifu wa misitu umechangia kupungua kwa kina cha maji katika Bwawa la Mindu, huku mmomonyoko wa udongo ukiendelea kuwa tatizo kubwa hivyo upandaji wa miti ni suluhisho muhimu katika kulinda kingo za mito na kuhakikisha vyanzo vya maji vinabaki salama kwa matumizi ya sasa na baadaye.

Naye  Meneja wa Uratibu wa Mazingira na Jumuiya za Watumia Maji kutoka Bodi ya Bonde la ya Maji la Wami/Ruvu Janeth Kisoma,alisema mto Lukulunge ni chanzo muhimu kinachochangia maji katika Bwawa la Mindu, ambalo linahudumia zaidi ya asilimia 75 ya wakazi wa Manispaa ya Morogoro, hivyo uhifadhi wake unahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali.

SERIKALI KUIFANYA TANZANIA KITOVU CHA BIASHARA -DKT.YONAZI

March 17, 2026 Add Comment



Na. MWANDISHI WETU - DAR ES SALAAM


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge,Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi amesema Serikali imefanya juhudi mbalimbali za Kisera, Sheria na Kimkakati ili kuhakikisha Tanzania inakuwa kitovu cha biashara Afrika Mashariki na Kati.

 

Dkt. Yonazi aliyasema hayo katika kikao  cha Kikundi Kazi cha Mazingira ya Biashara cha Baraza la Taifa la Biashara TNBC kilichofanyika jijini Dar es salaam.

 


Alisema Serikali imefanya jitihada za kukuza biashara nchini huku akizitaka sekta binafsi kuendelea kushirikiana na serikali.

 

“Serikali imefanya juhudi mbalimbali katika uwekezaji nchini ikiwemo mazingira ya ufanyaji wa biashara ya kisera, kisheria na lengo ni kuhakikisha Tanzania inakuwa kitovu cha biashara Afrika mashariki na kati.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) Dkt. Godwill Wanga  alisema kikao hicho kimefanyika ili kujadili maendeleo ya biashara nchini.


Alisema kikao hicho kimejadili vivutio  ambavyo serikali inaweza kufanya uwekezaji zaidi katika sekta ya afya  ili bima ya afya kwa wote itakapoanza iweze kuwa na faida kwa Watanzania.

“Kikao hichi ni muendelezo wa vikao ambavyo tumekuwa tukifanya mara kwa mara katika kujadili maendeleo ya biashara ambapo katika kikao hiki kimejadili kuhusu miundombinu ya mtandao katika  katika nchi yetu.


Aliongeza kuwa :”Tumekubaliana kufanya utafiti kuhusu madhara ya vita katika mashariki ya kati katika uchumi wetu.


=MWISHO=

SHINCHEONJI YAADHIMISHA MIAKA 42: "KUTOKA KWENYE HANDAKI HADI KUWA DHEHEBU LINALOONGEZEKA KWA MAKUMI MAELFU KILA MWAKA"

March 17, 2026 Add Comment

 


Mwenyekiti Lee Man-hee akitoa ujumbe katika Ibada ya Kuadhimisha Miaka 42 ya Kuanzishwa kwa Shincheonji Kanisa la Yesu, iliyofanyika katika Kanisa la Cheongju, Shincheonji Kanisa la Yesu tarehe 15. 

****

- Ibada ya Ukumbusho Iliyofanyika katika Kanisa la Cheongju, Shincheonji Kanisa la Yesu tarehe 15

- Siri ya Ukuaji wa Haraka wa Vizazi Vingi: Mafundisho ya Kipekee

Kujitolea kwa waumini wa mwanzoni walioanza katika ghorofa ya chini ya nyumba miaka 42 iliyopita kukawa mbegu ya uamsho ambao leo unawavutia maelfu ya waaminifu kutoka kote ulimwenguni kila mwaka. Katikati ya ukuaji huo kuna kanuni thabiti ya imani iliyojikita katika Neno — kiini hasa cha imani ya kweli.

MAONESHO KATIKA KONGAMANO LA NISHATI SAFI YA KUPIKIA MOROGORO

March 17, 2026 Add Comment

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius  Ndejembi akizungumza na wazalishaji,  wasambazaji na watumiaji wa nishati safi ya kupikia katika maonesho yanayoenda sambamba na Kongamano la Nishati Safi ya Kupikia linalofanyika leo mkoani Morogoro.

Kongamano hilo limehusisha Wizara na Taasisi mbalimbali za Umma kutoka Tanzania Bara na Zanzibar pamoja na wadau mbalimbali zikiwemo taasisi za fedha pamoja na wazalishaji, wasambazaji na watumiaji wa nishati safi ya kupikia.

Kongamano limeandaliwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Taasisi ya Uongozi likiwa na kaulimbiu ya Kuimarisha Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa Maendeleo Endelelevu.

Kutoka Wizara ya Nishati, Mhe. Ndejembi ameongozana na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Bw.Nolasco Mlay.



WAZIRI NDEJEMBI AWASILI MOROGORO KUSHIRIKI KONGAMANO LA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

March 17, 2026 Add Comment


Waziri wa Nishati, Mhe.Deogratius Ndejembi akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Adam Malima mara baada ya kuwasili mkoani Morogoro kushiriki Kongamano la Nishati Safi ya Kupikia.

Kongamano hilo limehusisha Wizara na Taasisi mbalimbali za Umma kutoka Tanzania Bara na Zanzibar pamoja na wadau mbalimbali zikiwemo taasisi za fedha pamoja na wazalishaji, wasambazaji na watumiaji wa nishati safi ya kupikia.

Kongamano limeandaliwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Taasisi ya Uongozi likiwa na kaulimbiu ya Kuimarisha Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa Maendeleo Endelelevu

Kutoka Wizara ya Nishati, Mhe. Ndejembi ameongozana na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Bw.Nolasco Mlay.


JAHAZI LAZAMA PANGANI: WAWILI WAFARIKI DUNIA, WATATU HAWAJULIKANI WALIPO

March 17, 2026 Add Comment




Na Oscar Assenga, Pangani

Jahazi la MV Tarawanda lililokuwa likitoka Wilaya ya Pangani mkoani Tanga likielekea Mkokotoni, Zanzibar, likiwa limebeba tani 20 za mizigo mbalimbali ikiwemo mihogo, ndizi, machungwa na nazi, limezama katika eneo la Nungwi kutokana na hali mbaya ya hewa pamoja na giza.

Jahazi hilo lilikuwa na watu sita wakiwemo nahodha na wafanyakazi wa chombo hicho.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na Jeshi la KMKM Zanzibar kwa viongozi wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) jijini Dar es Salaam, ambao waliwasiliana na Kituo cha Utafutaji na Uokozi Baharini (MRCC) Dar es Salaam, chombo hicho kilipopata ajali kilikutwa na watu wapatao 12.

Kati ya hao, watu saba waliokolewa na boti za uokozi kutoka Mkokotoni, Nungwi na Ushongo na kupelekwa katika Hospitali ya Kivunge, Kaskazini Unguja.

Katika ajali hiyo, watu watatu bado hawajapatikana huku miili ya watu wawili ikiwa imeokotwa katika eneo la Nungwi na kupelekwa Bandari ya Mkokotoni Zanzibar.

Akizungumza mara baada ya kufika Wilaya ya Pangani, Kaimu Afisa Mfawidhi wa TASAC Mkoa wa Tanga, Mhandisi Christopher Mlewa, alisema chombo hicho kilitoka Pangani kikielekea Mkokotoni lakini kilipata ajali katika eneo la Nungwi baada ya kupoteza mwelekeo kutokana na upepo mkali pamoja na giza.

Alisema nahodha wa chombo hicho hawakuzingatia utabiri wa hali ya hewa ambao wamekuwa wakikumbushwa mara kwa mara kuufuata kabla ya kuanza safari.

Awali, Afisa Mwandamizi wa Meli kutoka TASAC, Selemani Puzzy, alisema shirika hilo limepokea kwa masikitiko taarifa za ajali hiyo na kusisitiza umuhimu wa kuchukua tahadhari ili kupunguza madhara ya ajali kama hizo.

Alisema kwa mujibu wa sheria za Tanzania hakuna chombo cha mizigo kinachoruhusiwa kusafirisha abiria kwenda Unguja, isipokuwa vyombo vinavyotoka Bandari ya Tanga pekee. Alieleza kuwa vyombo vinavyotoka Bandari za Kigombe, Pangani na maeneo ya Mkwaja vina leseni za kusafirisha mizigo na wanyama tu, si abiria.

“Imekuwa ni kawaida kwa baadhi ya vyombo kuondoka na watu zaidi ya wanaoruhusiwa. Unakuta chombo kina wafanyakazi sita lakini ajali ikitokea ndani wanapatikana watu hadi 12, jambo ambalo si sahihi,” alisema.

Aliongeza kuwa baadhi ya manahodha wamekuwa wakipakia abiria kinyume cha sheria kwa siri, hali inayoweza kusababisha vifo bila hata kujulikana taarifa sahihi za waathirika.

“Ni muhimu kujenga utamaduni wa kusajili watu wote wanaosafiri. Kubeba abiria kwenye vyombo vya mizigo ni kosa na kunaweza kusababisha vifo. Hata mfanyabiashara aliyekuwa akisafirisha mbao alipanda kwenye jahazi hilo, jambo ambalo si sahihi,” alisisitiza.

Puzzy pia alitoa wito kwa wamiliki wa vyombo na wasafiri kufuatilia utabiri wa hali ya hewa kabla ya safari, kuhakikisha vyombo vina vifaa vya uokoaji na kutumia vyombo vilivyoruhusiwa kisheria kwa usafiri wa abiria.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Pangani, Adv. Agape Fue, alilishukuru Shirika la TASAC kwa kutoa elimu kwa wadau wa usafiri wa majini ili kuwakumbusha umuhimu wa kufuata sheria na kanuni za usalama baharini.

Alisema usalama ni msingi muhimu wa maendeleo ya uchumi na kuwataka wamiliki wa vyombo kusajili vyombo vyao pamoja na kuvitumia kwa shughuli zilizoidhinishwa tu.

Naye mmiliki wa Jahazi la Salamati kutoka Pangani, Mngwali Haji Ussi, alisema miongoni mwa waliofariki katika ajali hiyo ni mtoto wa dada yake.

Alisema kabla ya tukio hilo alimwonya kijana huyo asiichezee bahari kutokana na hatari zake, lakini alimjibu kuwa amepitwa na wakati.

“Serikali inapaswa kuwachunguza na kuwahakiki manahodha wote wanaoendesha vyombo vya baharini ili kuhakikisha wana leseni halali,” alisema.

Akizungumzia tukio hilo, alisema siku ya ajali alimtafuta mjomba wake kwa simu ili kumueleza kuhusu hali mbaya ya bahari na kumshauri asiende safari, lakini hakupatikana.

“Hapa kwetu mara nyingi tunatazama nyota kabla ya kuanza safari. Kama hakuna nyota baharini huwa hawatoki kwa sababu wanajua bahari si shwari. Mpaka sasa mjomba wangu bado sijamuona,” alisema.

Kwa upande wake, Katibu wa Makuli Wilaya ya Pangani, Waziri Hamisi, aliiomba Serikali kuangalia uwezekano wa kuwepo kwa boti ya uokozi katika maeneo hayo ili kusaidia wakati majanga kama hayo yanapotokea.




NGORONGORO NI KAPU LILILOBEBA MATUNDA MATAMU,SASA TUNAYAUZA

March 17, 2026 Add Comment


Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii Tanzania Ephraim Balozi Mafuru kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii ameongoza timu ya wizara hiyo kwenye kikao cha mkakati na viongozi wa wizara ya Utalii kutoka Jamhuri ya Zambia huku Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ikijinasibu kwa upekee  wa vivutio vilivyomo ndani ya hifadhi hiyo ambayo asili, urithi na maajabu yanakutana eneo moja.


Mkurugenzi Mafuru ameeleza ujumbe huo kuimarika kwa ushirikiano kati ya Tanzania na Zambia kutokana na juhudi kubwa zilizofanywa na Waasisi wa Tanzania na Zambia kuunganisha mshikamano wa kiuchumi na kijamii.


Mafuru amesema Tanzania inasonga mbele katika sekta ya utalii kutokana na kuimarisha  uhifadhi,miundombinu ya utalii pamoja na utafutaji wa masoko ya kimkakati ndani na nje ya nchi.


Akitoa wasilisho la Mamlaka ya Hifadhi  ya Ngorongoro Afisa Masoko Mwandamizi Selestine Saitabau alisema Ngorongoro ni kama kikapu cha zawadi ambapo kimebeba vivutio vingi kuanzia historia ya chimbuko la binadamu, wanyamapori, mazalia ya Nyumbu, mchanga unaohama, misitu, ndege, hali ya hewa ya kuvutia na uoto wa asili wenye mandhari yanayonawirisha ikolojia ya Ngorongoro, Serengeti hadi Masai Mara.


Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru aliwashukuru wageni hao wakiongozwa na Naibu Katibu Mkuu Kiongozi na katibu Mkuu wa wizara ya Utalii Zambia na kuwaeleza kuwa Ngorongoro ina sifa zote za kuwa Bustani ya Eden na kuwahakikishia wageni hao kuwa wamerudi nyumbani kwenye asili ya Mababu zao wa takriban miaka zaidi ya milioni 3 iliyopita.

NDALA MKONONI, MIKOPO PASUA KICHWA INAYOTESA FAMILIA MKOANI IRINGA

March 16, 2026 Add Comment

 

Na Rose Ngunangwa, Iringa

Wanawake Mkoani Iringa wameaswa kuachana na mikopo almarufu kama Shikilia Dera au Ndala mkononi kwani mikopo hiyo imekuwa ikisababisha mali za familia kuuzwa au kutaifishwa ili kufidia na kuiacha familia ikiingia kwenye lindi la umaskini.

SHULE YA VIZIWI NJOMBE YAHAMIA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

March 16, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu,Njombe

SHULE ya Sekondari ya Viziwi mkoani Njombe imetekeleza agizo la Serikali la kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuepukana na madhara ya kiafya yanayosababishwa na moshi wa nishati chafu.

Akizungumza wakati wa ziara ya timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Nishati iliyotembelea shule hiyo kukagua utekelezaji wa agizo hilo, Mjiolojia kutoka Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia,  Nsajigwa Maclean, amesema shule hiyo imefanikiwa kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya kampeni ya utoaji wa elimu kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Njombe.

 Maclean amefafanua kuwa matumizi ya nishati mbadala kama gesi, majiko banifu na umeme yana mchango mkubwa katika kupunguza uharibifu wa misitu unaotokana na ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa.

Aidha, amesema moshi unaotokana na matumizi ya nishati za jadi umekuwa ukichangia kusababisha magonjwa ya mfumo wa upumuaji kwa wapishi na wanafunzi, hivyo matumizi ya nishati safi yanasaidia kulinda afya pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia shuleni.

Amezipongeza shule ambazo tayari zimeanza kutumia nishati safi ya kupikia, akisema hatua hiyo inaunga mkono juhudi za Serikali za kulinda mazingira na kuboresha afya za watumiaji.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea kutoa elimu na kuhamasisha taasisi mbalimbali, ikiwemo shule, hospitali na magereza, kuachana na matumizi ya kuni na mkaa na badala yake kutumia nishati safi na salama kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.


Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Viziwi,  Rosemary Mbuya, amesema kufuatia agizo la Serikali, shule hiyo iliamua kuachana na matumizi ya kuni na mkaa kutokana na gharama kubwa za upatikanaji wake.

“Gharama ya kununua kuni na mkaa ilikuwa kubwa sana, na mara nyingi tulilazimika kuvifuata mbali. Pia wapishi wetu walikuwa wakikumbwa na changamoto za kiafya mara kwa mara kutokana na moshi,” amesema Mbuya.

Ameongeza kuwa tangu kuanza kutumia nishati safi ya kupikia, kumekuwa na maboresho makubwa katika ufanisi wa shughuli za jikoni pamoja na afya za wapishi.

 Amesema matumizi ya gesi yamepunguza muda wa kupika chakula kwa wanafunzi na kupunguza gharama zilizokuwa zikitumika kununua kuni na mkaa mara kwa mara.

Mwalimu Mbuya pia amebainisha kuwa hatua hiyo imechangia kulinda mazingira kwa kupunguza utegemezi wa ukataji wa miti kwa ajili ya kuni.