HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts

DC NYAMWESE ATAKA MASHAURI YA ARDHI YASIKILIZWE HARAKA KUCHOCHEA MAENDELEO HANDENI
habari
Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Mahakama ya Wilaya ya Handeni leo Februari 2,2026.
Na Augusta Njoji
Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, ametoa rai kwa Mahakama ya Wilaya ya Handeni kutoa kipaumbele katika usikilizwaji wa mashauri yanayohusu ardhi ili yahitimishwe kwa wakati na kuchochea maendeleo ya wananchi.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Sheria yaliyofanyika katika Mahakama ya Wilaya ya Handeni, Mhe. Nyamwese amesema migogoro ya ardhi imekuwa ikichukua muda mrefu kusikilizwa pindi inapofikishwa mahakamani, hali inayosababisha kucheleweshwa kwa utekelezaji wa shughuli za maendeleo.
Amesema ardhi ni rasilimali muhimu katika Wilaya ya Handeni, lakini imeendelea kukumbwa na migogoro mingi, ambayo baadhi yake haina tija kwa maendeleo ya jamii.
Amesisitiza kuwa haki inapocheleweshwa, maendeleo nayo hucheleweshwa, hususan pale wananchi wanapokusudia kutumia ardhi kwa uwekezaji au shughuli za uzalishaji.
“Sisi kama Wilaya tumekuwa na migogoro ya ardhi, lakini inapofika mahakamani mashauri haya huchukua muda mrefu kusikilizwa. Hali hii inawaathiri wananchi na kudumaza maendeleo kwa ujumla,” amesema Mhe. Nyamwese.
Aidha, amepongeza hatua zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha utendaji wa Mahakama, ikiwemo ujenzi wa miundombinu ya mahakama karibu na wananchi pamoja na matumizi ya teknolojia, hatua zinazoongeza imani ya wananchi katika mfumo wa utoaji haki.
Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya ya Handeni, Joseph Waruku, amesema Mahakama imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kuanzisha Mahakama za Mwanzo 12 mwaka 2025 katika maeneo yenye msongamano wa mashauri, ikiwemo Mahakama ya Mwanzo Msomera.
Naye, Mwakilishi wa Mwanasheria wa Halmashauri ya Mji Handeni, Regina Pangah, amesema Mahakama zina mchango mkubwa katika ustawi wa jamii na ukuaji wa uchumi kwa kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati, huku akiahidi kuendeleza ushirikiano katika kutoa elimu ya sheria kwa wananchi.

RC MAKAME AIPONGEZA REA KUWAPELEKEA UMEME WATEJA 6,135 SONGWE
Nishati



WAKANDARASI WA KUSAMBAZA UMEME WATAKIWA KWENDA NA KASI YA SERIKALI
habariMRADI WA KUPELEKA UMEME KWENYE VITONGOJI KUCHOCHEA UCHUMI, VIWANDA NA BIASHARA
habari

KAMPASI MPYA ZA VYUO VIKUU KUFUNGUA MILANGO YA UBIA RASMI NA SEKTA BINAFSI
habari
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi,akizungumza na wadau leo Februari 02, 2026 jijini Dodoma.
....
Serikali imeelekeza wadau kuhakikisha uwekezaji unaofanyika karibu na kampasi mpya 16 za vyuo vikuu unazingatia mpangilio wa miji, usalama na viwango vya kitaifa ili kuzuia ujenzi holela na kuhakikisha huduma zinazotolewa zinakidhi mahitaji ya wanafunzi, watumishi na jamii jirani.
Akizungumza Februari 02, 2026 jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi,amesema kuwa halmashauri na serikali za mitaa zinapaswa kutenga ardhi na kuandaa mpango wa matumizi ya ardhi kwa kushirikiana na vyuo husika.
Prof. Mushi amesisitiza kuwa mipango hiyo lazima izingatie viwango vya kitaifa vya upangaji miji na kuondoa migongano ya matumizi ya ardhi.
Profesa Mushi pia amevielekeza vyuo vikuu kufungua milango ya ushirikiano na sekta binafsi kupitia ubia rasmi (PPP) katika ujenzi wa hosteli, vituo vya biashara na miundombinu maalum.
Amesema mashauriano ya mara kwa mara kati ya vyuo na serikali za mitaa ni muhimu ili kuoanisha mipango ya maendeleo na kuimarisha mazingira rafiki kwa uwekezaji.
Aidha, sekta binafsi imetakiwa kuhakikisha huduma wanazotoa zinajibu mahitaji halisi ya jamii kwa kuzingatia usalama, ubora na uwajibikaji wa kijamii.
Mratibu wa Mradi wa HEET Taifa, Dkt. Kenneth Hosea, amesema kuwa mbali na kutoa mafunzo ya programu za Shahada ya Kwanza na Shahada ya Pili, kampasi mpya pia zitalenga kutoa ujuzi wa vitendo kwa vijana, wanawake na makundi maalum. Hatua hii inalenga kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo ya pembezoni kupitia ujenzi wa miundombinu, upatikanaji wa huduma za msingi pamoja na fursa za ajira.
Aidha, Dkt. Hosea ameongeza kuwa kila kampasi inatarajiwa kudahili zaidi ya wanafunzi 1,000 mwanzoni, na idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka hadi kufikia takribani wanafunzi 7,000 kadri muda unavyosonga.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mkinga, Rashid Karim Gembe, amesema kuwa kuanzishwa kwa kampasi mpya za elimu ya juu katika maeneo ya pembezoni kumeleta manufaa makubwa ya kiuchumi na kijamii
Amesema kuwa kutachochea ujenzi wa miundombinu kama barabara, maji na umeme, kuongeza upatikanaji wa huduma za msingi, pamoja na kutoa fursa za ajira kwa wananchi kupitia mahitaji ya walimu, wanafunzi na sekta binafsi, hivyo kuchangia kwa kiasi kikubwa ustawi wa jamii na maendeleo ya uchumi wa eneo husika.


























