HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts
VIONGOZI WA AFRIKA NA UFARANSA WAJADILI UWEKEZAJI NA MAENDELEO
_▪️Dkt. Mwigulu asisitiza matumizi sahihi ya rasilimali ili kujenga uchumi wa Afrika_
_▪️Rais Macron atangaza uwekezaji wa dola bilioni 27 Barani Afrika_
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 11, 2026 ameshiriki katika ufunguzi wa Mkutano wa Ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) unaofanyika jijini Nairobi, Kenya.
Mkutano huo umewakutanisha Wakuu wa Nchi na Serikali, viongozi wa sekta binafsi, wadau wa maendeleo pamoja na wawekezaji kwa lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.
Akizungumza baada ya mkutano huo, Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba amesema mkutano huo umekuwa wa manufaa kwa Bara la Afrika na Ufaransa kwa pamoja kwani majadiliano yamegusa namna ya kuzifanya pande hizo mbili ziweze kunufaika na ushirikiano huo.
Amesema rasilimali zinazopatikana barani Afrika zinatosheleza ikiwa zitatumika vizuri katika kujenga uchumi wa Afrika.
“Lengo kubwa la jitihada hizi ni kupambana na umasikini lakini pia na kutengeneza ajira kwa makundi makubwa ikiwemo la vijana pamoja na wanawake,” amesema.
Aidha, Waziri Mkuu amesema maeneo mengi yaliyojadiliwa ni maeneo ambayo yamepewa umuhimu katika Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.
“Nguzo zote zilizoongelewa kwenye dira lakini pia na maeneo ya kipaumbele yameguswa katika mijadala ya leo,” amesema.
Akizungumza katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa Dkt. William Samoei Ruto, alizitaka nchi za Afrika kutafakari upya mifumo ya kiuchumi kwa kuimarisha ukusanyaji wa rasilimali za ndani, uwekezaji pamoja na ushirikiano wa kikanda ili kuhakikisha kunakuwa na maendeleo ya muda mrefu.
Aidha, Rais Ruto amesema ni wakati wa Afrika kujiweka kama mdau katika uchumi wa kimataifa badala ya kuwa mnufaika wa misaada ya nje pekee.
“Afrika haiwezi tena kubaki kama mshiriki asiyekuwa na sauti katika mifumo ya kimataifa ambapo baadhi ya maamuzi muhimu hufanywa bila sauti ya usawa,” alisema.
Kwa upande wake, Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron, alisema Bara la Afrika linapiga hatua kubwa za maendeleo na ni bara ambalo halisubiri majawabu ya changamoto bali linatoa majawabu ya changamoto mbalimbali lilazokabiliana nazo.
Katika hatua nyingine, Rais Macron alitangaza uwekezaji wa thamani ya dola za Marekani bilioni 27 barani Afrika katika sekta za nishati, Akili Unde, uchumi wa bahari pamoja na kilimo.
“Mpango huu utasaidia kutengeneza takriban ajira 250,000 barani Afrika na nchini Ufaransa,” alisema.
Aidha, Rais Macron aliwataka wafanyabiashara wa Afrika kuona fursa zilizopo nchini Ufaransa na kwenda kuwekeza.
“Hatuko hapa tu kuja kuwekeza katika Bara la Afrika pamoja nanyi, tunawahitaji viongozi wakubwa wa biashara wa Afrika kuja kuwekeza nchini Ufaransa,” alisema.
Kwa Upande wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres alisema watu wa Bara la Afrika wanapaswa kuwa wa kwanza kunufaika na rasilimali za bara hilo.
“Bara hili limebarikiwa rasilimali nyingi, hapa wenyewe ndio wanapaswa wawe wa kwanza kunufaika,” alisema.
Dkt. Mwigulu amemuwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mkutano
FCC, BRELA WATOA MAFUNZO YA MILIKI UBUNIFU KWA MAJAJI WA MAHAKAMA KUU
habariWAZIRI NDEJEMBI,BALOZI WA SWEDEN NA UJERUMANI WAJADILI FURSA ZA USHIRIKIANO SEKTA YA NISHATI
Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi leo Mei 12, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na Wawakilishi kutoka Ubalozi wa Sweden, Ujerumani na kampuni ya Siemens Energy kwa lengo la kujadili fursa za uwekezaji na ushirikiano katika sekta ya nishati nchini.
Mazungumzo hayo yalihusisha pia Taasisi ya kifedha ya KfW IPEX ya Ujerumani na EKN ya Sweden ambazo zimekuwa zikishiriki katika kufadhili miradi mbalimbali ya maendeleo ya nishati.
Katika kikao hicho, ujumbe kutoka Siemens Energy uliwasilisha maeneo mbalimbali ambayo wameonesha nia ya kuwekeza ikiwemo uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi asilia, ufadhili na usambazaji wa mitambo ya kuzalisha umeme ambapo ilieleza uzoefu na uwezo wa kampuni hiyo katika teknolojia za mitambo ya kuzalisha umeme.
Katika kikao hicho Waziri Deogratius Ndejembi alieleza kufurahishwa kwake na ujio wa ujumbe huo katika wakati ambao Serikali inaendelea kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati ya nishati nchini.
Aidha, aliipongeza kampuni ya Siemens Energy kwa kupata kandarasi ya kusambaza mitambo ya kuzalisha umeme katika mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia wa Mkuranga wenye uwezo wa kuzalisha megawati 177, akisema hatua hiyo inaonesha imani waliyonayo wawekezaji wa kimataifa kwa Tanzania.
Sambamba na hilo, Mhe. Deogratius Ndejembi alizihimiza kampuni hizo kuangalia fursa za kuwekeza katika vyanzo vingine vya uzalishaji umeme ikiwemo umeme wa jua, upepo na jotoardhi ili kuunga mkono jitihada za Serikali za kufikia lengo la kuzalisha megawati 8,000 ifikapo mwaka 2030.
Nao Wawakilishi wa mabalozi pamoja na kampuni hizo waliishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuamini teknolojia ya Siemens Energy na ushirikiano wa kifedha kutoka katika nchi zao huku wakiahidi kuendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha upatikanaji wa mitambo na fedha za utekelezaji wa miradi hiyo kwa wakati.
Kikao hicho kilihudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, Kamishna Msaidizi wa Umeme Mha. Styden Rwebangira, Kaimu Kamishna wa Petroli, Mha. Petro Marwa pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Nishati.
MDEMU AWATAKA WANAWAKE KUJIKWAMUA KIUCHUMI NA KUDUMISHA MALEZI BORA
habari
Na Saidi Saidi, WMJJWM – Iringa
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum, Felister Mdemu, amewataka wanawake kushirikiana katika kujikwamua kiuchumi huku wakiendelea kuthamini familia, malezi bora, kuwaheshimu waume zao na kuhakikisha watoto wanapata malezi yenye maadili mema.
Mdemu amesema hayo mkoani Iringa, wakati wa mafunzo ya mwongozo wa uanzishwaji na uwezeshaji wa majukwaa ya wanawake kiuchumi yaliyofanyika katika Kijiji cha Kipaduka, Kata ya Uhambingeto, wilayani Kilolo. Mafunzo hayo yalihusisha madiwani pamoja na viongozi wa majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi kutoka kata mbalimbali za mkoa huo.

Akizungumzia umuhimu wa majukwaa hayo, Mdemu amesema ni maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye lengo la kuwainua wanawake kiuchumi kupitia elimu ya fedha, ujasiriamali, matumizi ya teknolojia pamoja na upatikanaji wa mikopo na masoko.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa wanawake kupata taarifa sahihi, kuunganishwa katika vikundi na kushiriki kikamilifu katika majukwaa hayo ili wasiachwe nyuma kutokana na ukosefu wa taarifa au usimamizi hafifu. Pia amewataka madiwani kushirikiana na taasisi za fedha, sekta binafsi pamoja na wataalam ili kuongeza fursa za kiuchumi kwa wanawake katika maeneo yao.

Naye Diwani wa Viti Maalum kutoka Tarafa ya Kilolo, Mheshimiwa Julieth Mkolongo, akizungumza kwa niaba ya madiwani na viongozi wa majukwaa hayo, amesema wako tayari kutekeleza maelekezo yaliyotolewa ili kuhakikisha wanawake wanapata fursa za kiuchumi kwa maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wao, baadhi ya wanawake walioshiriki mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata itawasaidia kuendesha vikundi vyao kwa ufanisi, kuongeza kipato pamoja na kuimarisha ustawi wa familia zao.
RAIS DKT SAMIA AWASILI NCHINI UGANDA KWA AJILI YA KUHUDHURIA SHEREHE ZA UAPISHO WA RAIS MTEULE WA NCHI HIYO YOWERI MUSEVENI
habariRAIS SAMIA AONDOKA NCHINI KUELEKEA UGANDA KUHUDHURIA SHEREHE ZA UAPISHO WA RAIS MUSEVENI
habariGPE, EP4R WARIDHISHWA NA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA ELIMU BUSWELU
habari
Ujumbe wa wadau wa maendeleo ya elimu ukiwemo Global Partnership for Education (GPE) pamoja na Education Program for Results (EP4R) ukiongozwa na Morten Sigsgaard Mratibu wa Ushirika wa Nchi (GPE) umeridhishwa na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya elimu inayotekelezwa katika Shule ya Msingi na Sekondari Buswelu, Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza.

Akizungumza wakati wa ziara ya ukaguzi wa miradi hiyo Mei 11, 2026, Morten amesema miradi hiyo imeendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, hususan kwa wanafunzi wa elimu jumuishi.
Katika Shule ya Msingi Buswelu, inayohudumia wanafunzi 1,211 wakiwemo 176 wenye mahitaji maalumu, imefanikiwa kujenga bweni la wasichana wenye mahitaji maalumu kupitia ufadhili wa Serikali na GPE-LANES II.
Mradi huo9 umewezesha wanafunzi 80 kupata makazi salama ya bweni, huku huduma za bweni zikianza rasmi Mei 8, 2026 baada ya Serikali kuanza kutoa fedha za chakula.
Aidha, walimu na wanafunzi wameeleza mabadiliko chanya yaliyotokana na miradi hiyo, wakisema awali wanafunzi walikuwa wakisoma katika mazingira ya msongamano wa madarasa, lakini sasa wanapata nafasi ya kusoma katika mazingira bora na yenye nafasi ya kutosha, jambo lililoongeza umakini na ushiriki darasani.
Katika Shule ya Sekondari Buswelu, kupitia Programu ya EP4R, shule imepokea Shilingi milioni 50 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa vyenye viti na meza 100, mradi ambao tayari umekamilika na unatumika.
Baadhi ya wanafunzi wa shule hiyo wanasema awali walikuwa wakisoma wakiwa wamebanana kutokana na upungufu wa madarasa, hali iliyokuwa ikichangia usumbufu wakati wa masomo, lakini kwa sasa wanafurahia kusoma katika madarasa mapya yenye nafasi kubwa na mazingira rafiki ya kujifunzia.
Uongozi wa shule ulieleza kuwa miradi hiyo imechangia kuboresha ufaulu pamoja na kuongeza hamasa ya kujifunza.
Wadua wa maendeleo walitoa pongezi kwa Serikali kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya elimu na kuahidi kuendelea kushirikiana katika kuboresha mazingira ya kujifunzia nchini.











TANZANIA KUENDELEA KUTUMIA AKILI UNDE KATIKA KUKABILIANA NA MAAFA
Na Mwandishi Wetu, Masvingo - Zimbabwe
TANZANIA imesema itaendelea kutumia teknolojia ya Akili Unde (AI) katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa tahadhari za mapema na kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali.
Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, wakati wa mkutano wa maandalizi ya Mkutano wa Sita wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika Mei 11, 2026 mjini Masvingo, Zimbabwe.
Alisema matumizi ya AI yatasaidia uchakataji na ufuatiliaji wa taarifa mbalimbali zinazoripotiwa kuhusu masuala ya maafa nchini, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa Serikali katika kufanya maamuzi ya haraka wakati wa majanga.
“Matumizi ya teknolojia ya Akili Unde yatawezesha uchambuzi wa taarifa kwa haraka, kutabiri hatari zinazoweza kujitokeza na kusaidia hatua za mapema za kukabiliana na maafa,” alisema Dkt. Yonazi.
Dkt. Yonazi alisema Serikali inaendelea kuweka mkazo katika maeneo muhimu yatakayosaidia kuwa na usimamizi wenye tija wa maafa ikiwemo utafiti wa kisayansi, matumizi sahihi ya Akili Unde, ushirikiano katika uhifadhi wa taarifa za matukio pamoja na matumizi ya menejimenti ya maarifa.
Aidha alisema Tanzania imeendelea kuwa mfano katika ukanda wa Kusini mwa Afrika kutokana na uwezo wake wa kuratibu na kusimamia maafa kwa mafanikio huku ikiendelea kuzuia, kupunguza madhara, kujiandaa na kurejesha hali pindi majanga yanapotokea.
Alifafanua kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na uwepo wa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema ambacho hufanya kazi saa 24 kupokea, kufuatilia na kuchambua taarifa za majanga kwa wakati halisi.
“Kituo cha Operesheni ya Maafa kimekuwa msaada mkubwa kwani kimerahisisha upatikanaji wa taarifa za mapema, uchambuzi wa takwimu za wakati halisi na upangaji wa mikakati ya kurejesha hali pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu namna ya kujiandaa na kukabiliana na maafa,” alisisitiza.
=MWISHO=
MENEJIMENTI YA WIZARA YA NISHATI YATEMBELEA MRADI WA EACOP TANGA, WAFIKIA 85% YA UTEKELEZAJI.
Nishati
Menejimenti ya Wizara ya Nishati imetembelea mradi wa kimkakati wa kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani mkoani Tanga nchini Tanzania wa EACOP (East African Crude Oil Pipeline) katika leo tarehe 11 Mei 2026.
Menejimenti hiyo ikiongozwa na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga imepokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo pamoja na kujionea ujenzi wa kituo cha kupokea, kuchakata na ujenzi wa gati la kupakia mafuta.
Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amesema Wizara ya Nishati imejionea kazi nzuri inayoendelea kufanyika ambapo mradi huo unatekelezwa kwa wakati na umefikia asilimia 85 ya utekelezaji.
“Tumeridhishwa na utekelezaji wa mradi huu. Umezalisha ajira kwa Watanzania katika fani mbalimbali, pia umefungua fursa nyingi kwa wananchi wa Mkoa wa Tanga moja kwa moja na Taifa kwa ujumla, ikiwa ni pamoja na ushiriki wa wazawa. vile vile mradi huu umesaidia jamii kupitia ukarabati wa barabara, miradi ya maji na miradi mingine ya kijamii,” amesema Kamishna Luoga.
Akitoa maelezo ya mradi huo, Mhandisi wa Mradi wa Kituo cha Kuhifadhi Mafuta, Mhandisi Musa Msafiri amesema utekelezaji wa upande wa matenki ya kuhifadhi mafuta umefikia asilimia 94, ambao ni ujenzi wa matenki manne yenye uwezo wa kubeba mapipa 2,000,000.
Kwa upande mwingine, Mhandisi wa Ujenzi wa gati, Fred Mahenge amesema utekelezaji wa mradi wa upande wa kituo cha kupakia na kusafirisha mafuta baharini (Jet) ni zaidi ya asilimia 90.
Mradi huu umezalisha jumla ya ajira 1,834, ambapo Watanzania wamepata asilimia 84 ya nafasi zote za ajira.
Aidha mradi huu unahusisha ujenzi wa bomba la mafuta lenye urefu wa kilomita 1,443 kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani mkoani Tanga, ambapo mafuta yatapakiwa na kusafirishwa kwenda soko la dunia.




























.jpeg)








