
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI


MKUU wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni, Halmashauri ya Wilaya ya Handeni na Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi yaliyolenga kuwaimarisha katika masuala ya utawala bora, ufuatiliaji wa mapato na uelewa wa mipaka ya majukumu yao katika uendeshaji wa halmashauri.
Na Augusta Njoji
MKUU wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni, Halmashauri ya Wilaya ya Handeni na Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi kuacha kutanguliza maslahi binafsi au ya kisiasa wanapotekeleza majukumu yao, na badala yake kuweka mbele maslahi ya wananchi na maendeleo ya halmashauri.
Nyamwese ametoa wito huo mjini Handeni wakati akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani, yaliyolenga kuwaimarisha katika masuala ya utawala bora, ufuatiliaji wa mapato na uelewa wa mipaka ya majukumu yao katika uendeshaji wa halmashauri.
Amesisitiza kuwa serikali haitavumilia uzembe, hujuma wala vitendo vyovyote vinavyozorotesha maendeleo ya halmashauri, akiwataka madiwani kuwa macho na kutoa taarifa kwa wakati pindi wanapobaini mianya ya upotevu wa mapato.
“Tunaomba mkawe wabunifu na mzishauri halmashauri namna bora ya kuboresha na kusimamia vyanzo vya mapato. Nyie ndio mnaoishi na wananchi; mnapobaini kapu linavuja, tuambieni linavuja wapi na nani analivujisha ili hatua stahiki zichukuliwe,” amesema Nyamwese.
Ameongeza kuwa madiwani ni macho na masikio ya serikali katika maeneo yao, hivyo wanapaswa kusimamia nidhamu ya watumishi, kuacha kufanya kazi kwa mazoea na kuchochea ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Handeni, Margareth Killo, amesema mafunzo hayo yataongeza ufanisi na uwajibikaji wa madiwani katika kuwahudumia wananchi.
Naye, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko, pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi, Michael Chabai, wamesema mafunzo hayo yamewawezesha madiwani kufahamu vyema wajibu na mipaka yao, hali itakayopunguza migongano na kuongeza tija katika utendaji wa halmashauri.


Waziri wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Mtumba, Antony Mavunde, amekabidhi jumla ya majiko 1,000 ya gesi kwa mama lishe na baba lishe wa Jimbo la Mtumba, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali katika kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mavunde amesema mpango huo unalenga kuboresha afya za mama na baba lishe, kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku pamoja na kulinda mazingira kwa kupunguza matumizi ya mkaa na kuni.
Amesema kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wajasiriamali wadogo ambapo ameahidi kuanzisha klabu za mama lishe katika kila kata za Jimbo la Mtumba zitakazosaidia kuwaunganisha mama lishe na kuwapatia elimu ya ujasiriamali, usimamizi wa fedha pamoja na kuwawezesha kupata mikopo kwa urahisi ili waondokane na mikopo kandamizi maarufu kama kausha damu.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Mafunzo kutoka kampuni ya Oryx Gas, Peter Ndomba, amewataka mama lishe na baba lishe kuacha kabisa matumizi ya mkaa na kuni akisema nishati hizo zimekuwa zikisababisha madhara makubwa ya kiafya ikiwemo magonjwa ya mfumo wa hewa, macho na moyo kutokana na moshi unaotokana na matumizi yake.
Kwa upande wao, mama lishe na baba lishe waliopokea majiko hayo wameishukuru Mbunge wao Antony Mavunde pamoja kwa msaada huo wakisema utawapunguzia adha ya kuni na mkaa, kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku.

📌 Wananchi wahamasishwa kuanza kufanya wiring kupokea mradi wa vitongojini
📌 Wananchi watakiwa kulinda miundombinu ya umeme
📌 Bilioni 33.5 kupeleka umeme vitongoji 186 Kilimanjaro
Wananchi katika vitongoji 186 ambavyo vinatarajiwa kupelekewa umeme Mkoani Kilimanjaro wamehamasishwa kuanza kufanya maandalizi ya kuupokea mradi huo kwa kuanza kutandaza nyaya ndani ya nyumba zao (wiring).
Rai hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Mkoa wa Kilimnajrao, Mhe. Nurdin Babu wakati wa kikao cha kumtambulisha mkandarasi, Derm Group (T) Limited alieshinda zabuni ya kupeleka umeme kwenye vitongoji 186 vya Mkoa huo katika kipindi cha miaka mitatu.
Mradi huo wa kupeleka umeme katika vitongoji unatekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 33.5.
Kuanza kwa mradi huo wa kupeleka umeme katika vitongoji 186, kutaufanya Mkoa wa Kilimanjaro kuwa na umeme katika vitongoji vyake vyote 2,258.
“Tunamshkuru sana Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake njema ya kutaka kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wote wanapata nishati ya umeme mpaka kwenye ngazi ya kitongoji.
Mkoa wa Kilimanjaro tunaenda kuandika historia kuwa miongoni mwa mikoa 3 inayokwenda kufikisha umeme katika vitongoji vyake vyote. Hii ni heshima kubwa sana. Nitumie fursa hii kuwahamasisha wananchi kuanza kufanya maandalizi ya kupokea umeme pindi mkandarasi atakapoanza kazi rasmi kwa kufanya wiring kwenye nyumba zao,” amesema Mhe. Babu.
Mkuu huyo wa Mkoa pia ametoa rai kwa wananchi kuchangamkia fursa ya uwepo wa umeme kwa kuanzisha biashara mbalimbali ili lengo la serikali la kuboresha maisha ya wananchi wa vijijini kupitia upatikanaji wa nishati ya umeme liweze kutimia.
Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA ambaye pia ni Mkurugenzi wa Fedha, CPA. Daniel Mungure ametoa wito kwa wananchi kumpa ushirikiano mkandarasi pindi atakapoanza kutekeleza mradi lakini pia kulinda miundombinu ya umeme ambayo imejengwa kwa gharama kubwa.
Kwa upande wake Meneja wa kampuni ya Derm Group, Mhandisi Musa Abdallah ameahidi kukamilisha mradi huo ndani ya muda uliopangwa kimkataba na kwamba atashirikiana karibu na viongozi na wananchi wa maeneo ya mradi.
*📌Idadi ya vitongoji vyenye umeme Mbeya ni 1,970 sawa na asilimia 67%*
*📌Mkandarasi atakiwa kutekeleza mradi huo kulingana Taratibu zilizowekwa*
📍Mbeya
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa ameishukuru Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kwa kupeleka kiasi cha shilingi bilioni 42.6 mkoani Mbeya ili kupeleka umeme kwenye vitongoji 316 kupitia mradi wa HEP 2B unaotekelezwa mkoani humo ili wananchi wanufaike na nishati hiyo.
RC Malisa amesema mradi huo unakwenda kuleta tija na kuchochea maendeleo ya wananchi wa mkoa huo ambao wataunganishiwa umeme huo kuwawezesha kuendesha shughuli zao za kiuchumi.
"Gharama ya kuunganisha umeme ni shilingi 27,000 tu. Nawaomba wananchi wa mkoa huu mtumie fursa hii ya kuunganisha umeme iliyoletwa na Serikali kupitia REA.," Amesema RC Malisa.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, Bw. Frank Mugogo amesema jumla ya Vitongoji mkoa wa Mbeya ni 2,951 ambapo vitongoji vyenye umeme ni 1,970 sawa na asilimia 67%.
Ameongeza kuwa vitongoji ambavyo havina umeme ni 1,981 na vitongoji vilivyopo kwenye mradi huo wa HEP 2B uliotambulishwa mkoani Mbeya ni 316 na vitongoji vitakavyosalia ni 665.
Kwa upande wake, Meneja wa Miradi kutoka kampuni ya White City International Contractors Ltd, Mha.Baraka Mungai ambaye atatekelesa mradi huo ameishukuru Serikali kupitia REA kwa kupewa fursa ya kutekeleza mradi huo. Ameuhakikishia uongozi wa mkoa wa Mbeya kuwa mradi huo utakamilika kwa wakati ili uweze kuleta tija kwa wananchi wa mkoa huo.
Na Kassim Nyaki, Amboni Tanga.
Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro imeshiriki na kudhamini mbio za AmbonI Adventure run zilizofanyika leo tarehe 31 Januari 2026 jijini Tanga kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii hususan mapango ya Amboni yanayosimamiwa na Mamlaka yah ifadhi ya Ngorongoro
Mbio hizo za umbali wa kimomita 6, 10 na 20 ambazo zimehudhuriwa na wakimbiaji zaidi ya 500 kutoka maeneo mbalimbali nchini zimeanzia katika viwanja vya Shule ya Sekondari Galanos hadi Mapango ya amboni ambapo washiriki wa mbio hizo wamepata fursa ya kufanya utalii wa ndani katika mapango hayo.
Kaimu meneja uhusiano wa Ngorongoro Hamis Dambaya ambaye ameshiriki mbio hizo kwa kukimbia kilomita 10 ameeleza kuwa Ngorongoro imeamua kuungana na wadau mbalimbali kuendelea kutangaza vivutio vilivyoko katika mapango ya Amboni ili yaendelee kujulikana kitaifa na kimataifa na kuvutia wageni wengi kutembelea na kuona vivutio vinavyopatikana katika mapango hayo na kupataa taarifa mbalimbali ikiwemo historia ya wapigania uhuru.
Msimamizi wa Mapango ya Amboni Afisa Uhifadhi Daraja la kwanza Ramadhan Rashid ameeleza kuwa baadhi ya vivutio vinavyopatikana katika Mapango ya Amboni ni pamoja na maumbo ya asili ya kijiolojia, vivutio vilivyochongwa na maji kama meli, mlima Kilimanjaro, kanisa, msikiti, shughuli za kimila na mataambiko, ndege ndani ya mapango, pango la jinsia, Pango la fatuma ambalo watu hulitumia kuomba mchumba wa kuoa, mimea ya aina mbalimbali, mto pamoja na mazingira asilia yanayopaambwa naa upepo mwanana wa bahari ya hindi.
Mkuugenzi wa Kale Amboni Caves Sophia Mulamula ameeleza kuwa Mbio za Amboni Adventure Run ambazo zimefanyika kwa msimu wa tatu na kuhudhuriwa na wakimbiaji takriban 500 zinatendelea kuboreshwa ili kuvutia wakimbiaji wengi zaidi mwaka ujao 2027
“Tumefanya tathmini kwa miaka hii miwili tumeona mbio hizi zinavutia watu wengi, tunaamini mwakani tunaboresha vitu vingi zaidi ili tupate wakimbiaji wengi kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii, kutangaza nchi yetu lakini kuendelea kuhamasisha utalii wa michezo” alilisitiza Mulamula.
Diamond amekiri kuwa kuanzishwa kwa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari kumeleta nidhamu na uwajibikaji mkubwa katika taaluma ya habari, akisisitiza kuwa Wasafi Media inaunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha weledi, maadili na heshima ya taaluma hiyo inalindwa.