HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

DMG YATUNUKIWA TUZO KWA MAGEUZI YA SEKTA YA MELI

June 30, 2026 Add Comment

    

By Staff Writer

Morogoro, Tanzania – June 27, 2026_ — Dar es Salaam Merchant Group (DMG) has clinched the coveted _Best Maritime Technology Company of the Year_ award at the 2026 Morogoro Business Awards, cementing its position as a leader in Tanzania’s technological transformation of the blue economy.

NAIBU WAZIRI OFISI YA WAZIRI MKUU KAZI,AJIRA NA MAHUSIANO DKT EVELINE MUNISI AKIPATA MAELEKEZO KWA VIJANA WANAOPATA MAFUNZO YA UANAGENZI

June 30, 2026 Add Comment


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Dkt. Eveline Munisi akipata maelezo kutoka kwa  vijana wanaopata mafunzo ya Uanagenzi awamu ya 8 ya mwaka 2025/2026 katika ziara yake ya kikazi katika  ufatiliaji wa maendeleo ya Mafunzo ya Uanagenzi Chuo cha Maendeleo ya Vijana Sengerema (FDC) Juni 29, 2026 Wilaya ya Sengerema, Mkoani Mwanza.




DKT. KIJAJI AELEKEZA MAAFISA UHIFADHI KUHAKIKISHA MAENEO YA HIFADHI YANALINDWA NA KUHIFADHIWA

June 30, 2026 Add Comment



Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) amewaelekeza maafisa uhifadhi nchini kuhakikisha maeneo yote ya hifadhi yanalindwa na kuhifadhiwa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.


Dkt. Kijaji ametoa maelekezo hayo leo jijini Dodoma wakati wa kikao kilichowakutanisha Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Paul Chacha, Wakuu wa Wilaya wa mkoa huo, watumishi wa Wizara ya Maliasili na Utalii ikiwemo viongozi kutoka  Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA).

 Kikao hicho kilijadili ongezeko la uvamizi na uharibifu wa misitu unaofanywa na watu mbalimbali katika maeneo ya hifadhi, hali inayohatarisha rasilimali za misitu na wanyamapori pamoja na juhudi za Serikali katika usimamizi endelevu wa maliasili.

Katika kikao hicho, Dkt. Kijaji amesisitiza kuwa maazimio yote yaliyofikiwa katika kikao hicho yanapaswa kutekelezwa kikamilifu na kwa wakati, akieleza kuwa hakuna nafasi ya uzembe katika kulinda maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uhifadhi.

Sambamba na hilo, amewataka watendaji wote wenye dhamana ya usimamizi wa maeneo ya hifadhi kutekeleza majukumu yao kwa weledi na uwajibikaji wa hali ya juu, akionya kuwa watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo watachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria.

Aidha, Dkt. Kijaji ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuimarisha sekta ya uhifadhi kupitia utoaji wa ajira kwa wahifadhi pamoja na kuongeza bajeti ya sekta hiyo, hatua zinazochangia kuimarisha ulinzi na usimamizi wa maeneo ya hifadhi nchini.

Amesema pia ni wajibu wa viongozi wa Wizara na wa Mkoa kuhakikisha sheria zinasimamiwa kikamilifu ili kulinda rasilimali za taifa zilizopo katika maeneo ya hifadhi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Paulo Chacha, amesema kikao hicho kimekuwa na manufaa makubwa katika kuweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na uvamizi wa maeneo ya hifadhi na kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara na viongozi wa mkoa.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Misitu kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Daniel Pancras, amesema watahakikisha maeneo yote ya misitu yanalindwa na kuhifadhiwa ipasavyo, huku akiahidi kuwa maazimio na maelekezo yote yaliyotolewa katika kikao hicho yatafanyiwa kazi kwa ufanisi.

Aidha, Dkt. Kijaji amesisitiza kuwa maelekezo yaliyotolewa na Mawaziri wanane wa kisekta kuhusu ulinzi wa maeneo ya hifadhi yatekelezwe kikamilifu katika mikoa yote nchini ili kuimarisha uhifadhi wa rasilimali za taifa na kuhakikisha sheria zinafuatwa bila upendeleo.






 

DKT MUNISI: PROGRAMU YA TAIFA YA UKUZAJI UJUZI YAENDELEA KUWAJENGA VIJANA

June 30, 2026 Add Comment


✅VIJANA 5,746 WANUFAIKA NCHINI

Na: Mwandishi Wetu - Mwanza

Serikali imeendelea kudhihirisha dhamira thabiti ya kuwawezesha vijana kiujuzi kupitia Programu ya Taifa ya Ukuzaji Ujuzi.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Dkt. Evaline Munisi amesema hayo leo Juni 29, 2026 Mwanza alipotembelea Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Sengerema FDC kwa lengo la kukagua maendeleo ya mafunzo ya Uanagenzi yanayotolewa kupitia programu hiyo.

Amesema, Serikali inalenga kujenga nguvukazi yenye ujuzi, maarifa na ubunifu ili kukidhi mahitaji ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kuongeza ushindani katika soko la ajira la ndani na nje ya nchi.

Dkt. Munisi alisema Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano inaendelea kutekeleza Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi kwa kushirikiana na sekta binafsi kupitia mfumo wa ubia (PPP), huku mafunzo ya uanagenzi yakichukua nafasi muhimu katika kuziba pengo la ujuzi kwa vijana. 

Vile vile, amesema kuwa mfumo huo unamwezesha mwanagenzi kutumia asilimia 40 ya muda kujifunza nadharia darasani na zaidi ya asilimia 60 kupata uzoefu wa vitendo sehemu za kazi, huku Serikali ikigharamia ada zote za mafunzo hayo kwa asilimia 100.

Kadhalika, Mhe. Munisi alisema katika awamu ya nane ya programu hiyo, Serikali imeboresha mazingira ya mafunzo kwa kuwapatia wanagenzi 5,746 bima ya afya pamoja na posho ya usafiri ya shilingi 100,000 kwa mwezi kwa kipindi cha miezi miwili watakapokuwa kwenye mafunzo ya vitendo. Aliwataka viongozi wa vyuo kuendelea kuwajengea vijana kimaadili, nidhamu, uzalendo na uwajibikaji pamoja na kuimarisha ushauri nasaha na ushirikiano na waajiri ili kuhakikisha wanagenzi wanapata mafunzo yenye tija.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Ajira na Ukuzaji Ujuzi, Bi. Alana Nchimbi, alisema Programu ya Taifa ya Kukuza Ujuzi ilianzishwa mwaka 2016/17 ikiwa na lengo la kuongeza ujuzi wa nguvukazi na kukuza ajira nchini. Alibainisha kuwa hadi sasa jumla ya Watanzania 168,657 wamenufaika na programu hiyo kupitia maeneo manne ya utekelezaji ambayo ni mafunzo ya uanagenzi, uzoefu wa kazi kwa wahitimu, urasimishaji wa ujuzi uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa elimu na kuongeza ujuzi kwa wafanyakazi.

Bi. Nchimbi alisema katika mwaka wa fedha 2025/26, mafunzo ya uanagenzi yanatekelezwa katika vyuo na taasisi 46 zilizopo katika mikoa 25 ya Tanzania Bara, yakihusisha vijana 5,746 katika fani mbalimbali. Mkoa wa Mwanza unashiriki kupitia vyuo vitatu ambavyo ni Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Sengerema, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Malya na Pine College, vyenye jumla ya wanagenzi 339.

Mmoja wa Wanagenzi  alimshkuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano kwa kuwezesha mafunzo hayo kwa kugharamia ada kwa asilimia 100 na kuwapatia bima ya afya. 

Walisema tangu kuanza kwa mafunzo Januari 2026 wamepata ujuzi wa kitaaluma, uwezo wa kujitegemea, kujenga mahusiano ya kikazi na mbinu za kupata wateja, huku baadhi yao tayari wakianza kujipatia kipato kupitia ujuzi walioupata.

Hata hivyo, wanagenzi hao waliiomba Serikali kuendelea kushirikiana na waajiri ili kuongeza nafasi za mafunzo kwa vitendo, wakieleza kuwa baadhi ya taasisi na waajiri bado wanatoza fedha ili kutoa nafasi za mafunzo. Walisisitiza kuwa mafunzo ya uanagenzi yamewapa msingi imara wa kujiajiri na kuajiriwa, na kuahidi kutumia ujuzi walioupata kuchangia maendeleo ya Taifa kupitia uzalishaji, ubunifu na utoaji wa huduma bora.


Aidha, amesema Programu hiyo inalenga kuwajengea vijana stadi zinazokidhi mahitaji ya soko la ajira, kuongeza fursa za kujiajiri na kuimarisha mchango wao katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

MWISHO




 

MANISPAA YA MOSHI YAKANUSHA KUBADILI MATUMIZI YA ENEO LA UHURU PARK..

June 29, 2026 Add Comment

Moshi.

Halmashauri ya Manispaa ya Moshi imesema haijabadilisha matumizi ya eneo lolote la wazi, ikieleza kuwa kinachoendelea katika eneo la Uhuru Park ni utekelezaji wa mpango wa muda mrefu wa kuboresha eneo hilo bila kuathiri matumizi yake ya awali.

Hayo yamebainishwa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, Mwajuma Nasombe, alipozunguma kuhusiana na tetesi za kubadilishwa kwa matumizi ya eneo hilo.

Alisema kuwa, ofisi yake haijabadilisha matumizi ya ardhi katika eneo lolote na kudai  baada ya Waziri Mkuu kuagiza Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kufuatilia suala hilo, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa ilitembelea eneo husika na taarifa ya uchunguzi itawasilishwa serikalini.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Mipango Miji ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, Francis Shio, alisema eneo la Uhuru Park lina hati miliki ya halmashauri na tangu awali lilipangwa kutumika kama eneo la wananchi kupumzika na kufanyia shughuli mbalimbali za kijamii.

Alisema ujenzi unaoendelea wa vibanda vinavyozunguka eneo hilo ni sehemu ya mpango wa kulijengea uzio, kuweka mageti ya kuingilia na kutokea pamoja na kuimarisha usalama na mazingira ya bustani hiyo.

"Mpango huu si wa leo, miaka ya nyuma tayari halmashauri ilijenga vibanda takribani 39 katika eneo hilo. Sasa tunaendelea na hatua nyingine za utekelezaji wa mpango huo," alisema Shio.

Alieleza kuwa baada ya kukamilika kwa uzio, eneo hilo litaboreshwa kwa ndani kwa kuweka sehemu za watoto kuchezea, maeneo ya mapumziko na huduma nyingine zitakazowezesha wananchi kulitumia kwa usalama zaidi.

"Lengo letu si kubadilisha matumizi ya eneo hili, bali kulifanya liwe salama na lenye huduma bora. Mzazi atakapomleta mtoto wake atakuwa na uhakika wa usalama kutokana na uwepo wa uzio," alifafanua.




 

THBUB YAWAFIKIA ZAIDI YA WANANCHI 89,000 KUPITIA ELIMU YA HAKI ZA BINADAMU

June 29, 2026 Add Comment

 


Na Mwandishi Wetu- Dar es Salaam


Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imeendelea kuimarisha uelewa wa wananchi kuhusu haki za binadamu na misingi ya utawala bora kwa kuwafikia zaidi ya wananchi 89,000 kupitia njia mbalimbali za utoaji elimu katika mwaka wa fedha 2025/2026.


Elimu hiyo ilitolewa kupitia mafunzo kwa makundi mbalimbali ya jamii, vipindi vya redio na televisheni, mitandao ya kijamii, huduma ya ujumbe mfupi wa simu (Bulk SMS) pamoja na usambazaji wa vipeperushi na machapisho ya elimu.


Taarifa hiyo imetolewa na Msemaji wa Tume hiyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Elimu kwa Umma, Mawasiliano,Utafiti na Nyaraka wakati akiongea na vyombo vya habari katika viwanja vya Maonesho ya Kimataifa ya Biashara saba saba leo Juni 29,2029


Bi. Mnanka amesema katika kipindi hicho, wananchi zaidi ya 80,000 walifikishiwa ujumbe wa elimu kupitia simu za mkononi, huku vipeperushi 39,129 na vitabu 200 vya elimu vikisambazwa kwa wananchi ili kuongeza uelewa kuhusu haki za binadamu, utawala bora na namna ya kuwasilisha malalamiko THBUB.


Aidha, Tume ilirusha vipindi 79 vya elimu kupitia redio na televisheni, hatua iliyochangia kuwafikia wananchi wengi zaidi nchini.


THBUB imesema itaendelea kutumia teknolojia na majukwaa mbalimbali kuhakikisha elimu ya haki za binadamu inawafikia Watanzania wengi zaidi.


Pia, Bi. Mnanka amesema THBUB imeendelea kuwekeza katika elimu ya haki za binadamu kwa kutoa mafunzo kwa zaidi ya washiriki 9,300 kutoka makundi mbalimbali ya jamii nchini katika mwaka wa fedha 2025/2026.


Akitoa takwimu ya walionufaika na mafunzo hayo, Bi. Mnanka ametaja makundi hayo kuwa ni pamoja na askari wa Jeshi la Polisi 827, waandishi wa habari 324, madiwani 60, wanafunzi zaidi ya 8,000 na walimu 121 kutoka vyuo vikuu tisa pamoja na taasisi nyingine za elimu.


Mafunzo hayo yalilenga kuongeza uelewa kuhusu haki za binadamu, misingi ya utawala bora na wajibu wa kila mmoja katika kulinda na kuheshimu haki hizo.


“…..kuwajengea uwezo makundi mbalimbali katika jamii ni hatua muhimu ya kuimarisha utamaduni wa kuheshimu haki za binadamu na kuzuia vitendo vya uvunjifu wa haki na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora…..” amesema Bi.Mnanka.

IRELAND YAHAKIKISHA KUENDELEA KUFADHILI MIRADI YA USAWA WA KIJINSIA VYUONI

June 29, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Serikali ya Ireland imesisitiza kuendelea kuunga mkono juhudi za kukuza usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake katika taasisi za elimu ya juu nchini Tanzania, ikieleza kuwa elimu jumuishi ni msingi wa maendeleo endelevu na jamii yenye usawa.

WAZIRI NDEJEMBI -MRADI WA EACOP WAELEKEA UKINGONI MELI YA KWANZA KUBEBA MAFUTA JANUARI 2027

June 29, 2026 Add Comment




Na Oscar Assenga, Tanga

WAZIRI wa Nishati, Dkt. Deogratius Ndejembi, amesema ujenzi wa Mradi wa Bomba la Kusafirisha Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) umefikia asilimia  86, huku mafuta ya kwanza yakitarajiwa kupokelewa katika Kituo cha Chongoleani, Tanga, na kusafirishwa Januari mwaka 2027.

Dkt. Ndejembi alisema hayo leo baada ya kutembelea eneo la mradi Chongoleani, mkoani Tanga, kujionea maendeleo ya utekelezaji wake, ambapo alieleza kuwa matarajio ni kukamilisha ujenzi huo ifikapo mwisho wa Agosti mwaka huu.

Alisema kazi nyingi muhimu zimekamilika na kilichobaki ni hatua za mwisho ikiwemo kukamilisha miundombinu ya umeme ili kuwezesha mitambo ya kusukuma mafuta kufanya kazi.

"Nimefurahishwa na maendeleo ya mradi. Kazi kubwa imefanyika na tunaamini ifikapo mwisho wa Agosti ujenzi utakuwa umekamilika. Ratiba inaonyesha kuwa meli ya kwanza itachukua mafuta ghafi kutoka Chongoleani mwezi Januari, 2027," alisema.

Hata hivyo, alisema changamoto iliyobaki ni kukamilika kwa njia ya umeme kutoka Majani Mapana kuelekea eneo la mradi, huku akiutaka mkandarasi anayetekeleza kazi hiyo chini ya Tanesco kuhakikisha anakamilisha mradi huo kwa wakati.

Alionya kuwa mkandarasi atakayeshindwa kutekeleza kazi hiyo ndani ya muda uliopangwa atachukuliwa hatua, ikiwemo kuondolewa katika orodha ya wakandarasi wanaofanya kazi na Tanesco.

Dkt. Ndejembi alisema EACOP ni mradi wa kimkakati kwa Tanzania, Uganda na ukanda mzima wa Afrika Mashariki, akibainisha kuwa bomba hilo lenye urefu wa zaidi ya kilomita 1,400 ni la kwanza duniani lenye mfumo wa kupashwa joto katika urefu wake wote.

Alisema Serikali ya Tanzania imewekeza zaidi ya Sh bilioni 973 kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), ambalo linamiliki asilimia 15 ya hisa za mradi huo kwa kushirikiana na kampuni za UNOC, TotalEnergies na CNOOC.

Aidha, aliwataka Watanzania kuendelea kutumia fursa zinazotokana na mradi huo, akieleza kuwa zaidi ya Watanzania 3,000 wamepata ajira za moja kwa moja, huku vijana wengine zaidi ya 100 wakipelekwa Madimba kwa mafunzo ya kuongeza ujuzi kabla ya kuajiriwa.

Aliongeza kuwa zaidi ya vijana 400 kutoka Chongoleani wamepatiwa mafunzo na kuajiriwa katika maeneo mbalimbali ya mradi huo, huku fursa nyingine nyingi zikiendelea kujitokeza.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, alisema mradi huo umeendelea kuleta manufaa makubwa kwa mkoa huo kupitia ongezeko la shughuli za Bandari ya Tanga, mapato ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na fursa za ajira kwa wananchi.

Alisema vifaa vingi vya mradi vimepitia Bandari ya Tanga kabla ya kusafirishwa katika maeneo mbalimbali ya utekelezaji wa bomba hilo, jambo lililochochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi.

Balozi Burian alisema pia mradi huo umezingatia viwango vya kimataifa vya utunzaji wa mazingira, akieleza kuwa shughuli za uvuvi zinaendelea kama kawaida na hakuna viumbe hai walioathirika kutokana na ujenzi wa gati na miundombinu mingine.

Aliongeza kuwa kupitia mradi huo, Halmashauri na jamii zinazozunguka eneo la mradi zimenufaika na miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo ujenzi wa uwanja wa mpira unaotumiwa na klabu ya Coastal Union.

Naye Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Huduma za Mradi wa EACOP, Jofrey Mponda, ambaye pia alizungumza kwa niaba ya uongozi wa EACOP Tanzania, alisema mradi umefikia hatua za mwisho za utekelezaji, huku zaidi ya asilimia 90 ya kazi ikiwa imekamilika.

Alisema mradi huo unaounganisha mikoa 18 ya Tanzania na wilaya 27 umeingia katika hatua ya ukaguzi na makabidhiano ya mifumo mbalimbali, ikiwemo vituo vya kusukuma mafuta, matenki ya kuhifadhi mafuta na miundombinu mingine muhimu.

Mponda alisema pampu sita za kusukuma mafuta zimejengwa, mbili zikiwa nchini Uganda na nne nchini Tanzania, huku pampu mbili za kupunguza shinikizo la mafuta zikiwa Chongoleani.

Alibainisha kuwa matenki manne ya kupokelea mafuta tayari yamekamilika, huku kazi iliyobaki ikiwa ni kuunganisha mfumo wa umeme ili kuwezesha mitambo yote kuanza kufanya kazi kwa wakati.

Alisema EACOP inaendelea kushirikiana kwa karibu na Tanesco kuhakikisha miundombinu ya umeme inakamilika ifikapo Septemba mwaka huu, hatua itakayowezesha maandalizi ya kupokea mafuta ya kwanza mwezi Januari, 2027.


TAMISEMI YAWAKARIBISHA WANANCHI KUTEMBELEA BANDA LAKE SABASABA

June 29, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) imewahimiza wananchi na wadau wa maendeleo kutembelea banda lake katika Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) ili kupata huduma mbalimbali na elimu kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wizara pamoja na taasisi zilizo chini yake.

GEL yataka wanafunzi warejee na maarifa ya kulijenga taifa

June 29, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu

NDOTO za vijana wa Tanzania wanaotarajia kujiunga na vyuo vikuu mbalimbali nje ya nchi kwa mwaka wa masomo 2026/2027 zimeingia hatua muhimu baada ya Global Education Link kuwakutanisha wanafunzi hao pamoja na wazazi na walezi wao kwa ajili ya kuhakiki nyaraka na kukamilisha maandalizi ya safari.

MWENGE WA UHURU WARIDHISHWA NA MIRADI YA BILIONI 2.159 SAME

June 29, 2026 Add Comment


Na Ashrack Miraji 

SAME, Kilimanjaro,  Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ndugu Wazo Mwang'onda, ameridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo yenye thamani ya Shilingi bilioni 2.159 iliyotembelewa katika Wilaya ya Same, mkoani Kilimanjaro, wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru 2026.

Mwenge wa Uhuru uliwasili mkoani Kilimanjaro  ukitokea Mkoa wa Tanga na kupokewa katika Kata ya Hedaru, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Nurdin Babu, alimkabidhi Mwenge huo Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Same, Mhe. Godfrey Mzava, kwa ajili ya kuendelea na mbio zake ndani ya wilaya hiyo.

Akizungumza wakati wa mapokezi hayo, Mhe. Godfrey Mzava alisema Mwenge wa Uhuru utakimbizwa umbali wa kilomita 76 katika Wilaya ya Same na utapitia miradi mitano ya maendeleo yenye thamani ya jumla ya Shilingi bilioni 2.159 kwa ajili ya kukaguliwa, kuwekwa mawe ya msingi, kuzinduliwa na kutembelewa.

Katika ziara hiyo, Mwenge wa Uhuru ulikagua miradi ya afya, miundombinu, miradi ya kijamii, vikundi vya wajasiriamali pamoja na kuzindua jukwaa (platform) la vijana la Wilaya ya Same, hatua inayolenga kuimarisha ushiriki wa vijana katika shughuli za maendeleo na kujenga uchumi wa wilaya hiyo.

Miongoni mwa miradi iliyopongezwa ni ujenzi wa wodi mbili za wagonjwa, za wanawake na wanaume, pamoja na jengo la  kuhifadhia miili katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Same, ambapo Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa aliweka jiwe la msingi na kupongeza hatua iliyofikiwa katika utekelezaji wake.

Ndugu Wazo Mwang'onda alisema ameridhishwa na ubora wa miradi hiyo na kusisitiza kuwa inakwenda kuongeza thamani ya huduma kwa wananchi. Aidha, aliwataka wakandarasi kuhakikisha wanakamilisha kazi zilizobaki kwa kuzingatia viwango vya ubora, muda wa mkataba na matumizi sahihi ya fedha za umma.

Alisema Serikali inaendelea kuwekeza katika miradi ya maendeleo ili kuboresha maisha ya wananchi, hivyo ni wajibu wa viongozi, wataalamu na wananchi kulinda na kuitunza miradi hiyo ili iweze kutoa huduma kwa muda mrefu.

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Same, Mhe. Godfrey Mzava, alimshukuru Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kwa kuridhishwa na utekelezaji wa miradi hiyo, akisema maoni na ushauri uliotolewa utakuwa chachu ya kuongeza ufanisi katika usimamizi wa miradi ya maendeleo wilayani humo.

Mhe. Mzava alisisitiza kuwa uongozi wa Wilaya ya Same utaendelea kusimamia kwa karibu utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zinazokusudiwa na Serikali, huku akiahidi kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuharakisha maendeleo ya wilaya hiyo.

Baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Same walieleza kufurahishwa na kukamilika kwa baadhi ya miradi hiyo, wakisema itaongeza upatikanaji wa huduma muhimu hususan katika sekta ya afya. Mkazi wa Same, Hawa Said, alisema ujenzi wa wodi mpya na majengo ya kuhifadhia miili utasaidia kuboresha huduma hospitalini na kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika kutokana na changamoto za miundombinu.

Baada ya kukamilisha mbio zake ndani ya Wilaya ya Same, Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kukabidhiwa  kwenye wilaya inayofuata kwa mujibu wa ratiba ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2026, huku viongozi wakitoa wito kwa wananchi kuendelea kushiriki kikamilifu katika kulinda amani, kuchochea maendeleo na kuunga mkono miradi inayotekelezwa na Serikali.

Kauli mbiu ya Mwenge wa Uhuru 2026 Tanzania ni Yetu Sote tushikamane Kwa pamoja kuleta Maendeleo



 

MALIKALE, HAZINA INAYOPASWA KUENZIWA KWA VIZAZI VIJAVYO

June 28, 2026 Add Comment

    

📌Wizara ya Maliasili na Utalii yajipanga kunadi Malikale kama fursa ujio wa  AFCON

📌Maboresho maeneo ya Malikale kuvutia utalii wa ndani na nje ya nchi

📌Menejimenti ya Wizara na taasisi zake yahitimisha ziara maeneo ya Kaole, Ngome Kongwe na Caravan Serai 

Na Neema Chalila Mbuja, Bagamoyo

IMEELEZWA  kuwa ni muhimu kwa maeneo yenye Malikale kuenziwa na kutangazwa ili  historia yake irithishwe kwa vizazi vijavyo.

Hayo yamesemwa leo Juni 28, 2026 mjini Bagamoyo na Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Kale, Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Cristowaja Ntandu wakati wa kuhitimisha ziara ya Menejimenti ya wizara hiyo na taasisi zake waliokuwa wakitembelea maeneo ya Malikale na namna watakavyotumia fursa ya ujio wa Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON -2027) kunadi Malikale kuvutia watalii.

TRA YAKABIDHI VIFAA TIBA VYA SH. MILIONI 162 HOSPITALI YA RUFAA YA MWANANYAMALA

June 28, 2026 Add Comment
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imekabidhi vifaa tiba mbalimbali vyenye thamani ya Sh. Milioni 162 katika Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 ya TRA na utoaji wa Tuzo za Rais kwa Mlipakodi Bora zinazotarajiwa kutolewa Julai Mosi mwaka huu Mlimani City Jijini Dar es Salaam. 

TRA YAPANDA MITI 3850 NCHI NZIMA KUELEKEA MAADHIMISHO YA MIAKA 30

June 28, 2026 Add Comment

   Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imepanda  miti 3850 nchi nzima ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 tangu kuanzishwa kwake huku Kamishna Mkuu wa Mamlaka hiyo Bw. Yusuph Juma Mwenda ikiutaka umma kuitunza miti hiyo kwa lengo la kuhifadhi mazingira.

Abdulmalik Mollel awaandaa walimu Dodoma kuiwakilisha Tanzania Korea Kusini

June 28, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu

UJUMBE wa walimu na viongozi wa elimu kutoka Mkoa wa Dodoma wapatao 40 umeondoka kwenda Korea Kusini kujifunza, namna ya kufundisha, kusimamia shule na kutumia teknolojia katika elimu.

MSALABS, BARRICK BULYANHULU WATOA MSAADA KWA MAKUNDI YENYE MAHITAJI MAALUM NYANG'HWALE

June 28, 2026 Add Comment

 

Meneja Mkuu wa MSALABS , Albert Kamwela na Afisa Mahusiano wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu Mary Lupamba wakigawa mitungi ya gesi ya kupikia kwa watu wenye ulemavu katika kata ya Nyang’hwale
Mmoja wa wanufaika akiendesha baiskeli aliyokabidhiwa na Kampuni ya MSALABS kwa kushirikiana na Mgodi wa Barrick Bulyanhulu, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kuwainua wananchi wenye mahitaji maalum.

Wafanyakazi wa Mgodi wa Barrick Bulyanhulu na MSALABS wakifurahi katika picha ya pamoja na watu wenye ulemavu

Afisa wa Kampuni ya MSALABS akikabidhi Baiskeli kwa mama mlemavu katika hafla hiyo , huku mnufaika akiwa mwenye furaha na matumaini


Kampuni ya MSALABS inayotoa huduma ya maabara ya kupima madini katika mgodi wa Barrick Bulyanhulu uliopo katika Halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga imeshirikiana na mgodi huo kukabidhi misaada mbalimbali kwa wananchi wanaoishi kwenye mazingira magumu kwenye kata ya Mwingiro , Wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita.

'RUVUMA NI GHALA LA CHAKULA, SI LA MIFUGO MINGI' – YOGE

June 28, 2026 Add Comment

 

Mkurugenzi Mtendaji wa YOGE, Wakili Philomena Mwalongo

***
Na Mwandishi Wetu, Songea

Serikali mkoani Ruvuma imeshauriwa kuzuia kabisa uingizwaji wa makundi makubwa ya mifugo mkoani humo ili kunusuru nchi dhidi ya janga la njaa, kwa kuzingatia kuwa Ruvuma ni moja ya mikoa muhimu kwa uzalishaji wa chakula nchini.

KAMISHNA MKUU WA TRA AWAPA UBALOZI WASTAAFU WA TAASISI HIYO

June 27, 2026 Add Comment

 

Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Yusuph Juma Mwenda amewataka watumishi wastaafu wa Mamlaka hiyo kuwa Mabalozi wa Kodi ili kuongeza uelewa wa umuhimu wa kulipa kodi kwa jamii na kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari. 

WAZIRI MASAUNI ASITISHA SHUGHULI ZA KIWANDA CHA AFRICAN STEEL KWA UCHAFUZI WA MAZINGIRA

June 27, 2026 Add Comment
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Masauni, amesitisha shughuli za Kiwanda cha African Steel Group Company Limited kilichopo Kijiji cha Mwavi, Kata ya Fukayosi, Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa Pwani, kinachotumia chuma chakavu kuzalisha nondo kwa ukiukwaji wa Sheria na Kanuni za uhifadhi wa mazingira.

*RAIS DKT.SAMIA S. HASSAN KUFUNGUA MKUTANO MKUBWA WA MADINI NOVEMBA 2026*

June 27, 2026 Add Comment



-▪️Ni Mkutano mkubwa wa Madini na Uwekezaji

▪️Washiriki 2000 kutoka mataifa 50 Duniani kushiriki

▪️Kauli Mbiu ya Mkutano inalenga kuongeza thamani madini kwa maendelezo ya Viwanda

▪️Serikali na Sekta Binafsi kushirikiana kuandaa mkutano huo


▪️Waziri Mavunde azindua rasmi maandalizi ya mkutano huo



📍 DAR ES SALAAM. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. Samia S. Hassan anatarajiwa kufungua rasmi Mkutano wa Saba wa Madini na Uwekezaji Tanzania (TMIC 2026) utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Akizungumza leo Juni 27, 2026 wakati wa uzinduzi wa TMIC 2026, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema serikali imeamua kujenga uchumi wa viwanda unaotokana na madini kwa kuwekeza katika uchakataji na uyeyushaji wa madini badala ya kuendelea kuuza malighafi.

Amesema kaulimbiu ya mkutano huo, "Madini Yaliyoongezwa Thamani: Chachu ya Ukuaji wa Viwanda na Uchumi," inaakisi dira ya serikali ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa madini barani Afrika.

Kwa mujibu wa Mhe. Mavunde, amesema Tanzania tayari ina viwanda vinane vya kusafisha dhahabu, huku Mkoa wa Dodoma ukiwa na viwanda tisa vinavyojengwa na vinavyoendelea na uzalishaji pamoja na kiwanda kikubwa cha kuyeyusha madini ya nikeli na shaba.

"Zaidi ya Sh bilioni 600 zinawekezwa katika ujenzi wa kiwanda cha chuma kitakachotumia asilimia 100 ya malighafi za ndani, huku uwekezaji mwingine ukiendelea Kigamboni na Tanga kwa ajili ya uchakataji wa madini ya 'Heavy Mineral Sands' na mradi wa madini ya niobium wa Panda Hill, Mbeya," amesema Mhe. Mavunde

Amesema, katika kuongeza ushiriki wa Watanzania kwenye sekta hiyo,  thamani ya manunuzi kupitia mpango wa 'Local Content' imefikia Sh trilioni 5.1, huku bidhaa 20 zikitakiwa kuzalishwa na wazawa kwa ajili ya kuhudumia migodi mikubwa.

 Amesisitiza wafanyabiashara kuzingatia uaminifu na viwango vya kimataifa ili kunufaika zaidi na fursa hizo.

Amesema sekta ya madini imeendelea kuimarisha mchango wake katika uchumi kwa kuingiza Sh trilioni 1.374 katika Mfuko Mkuu wa Serikali, kiwango kilichovuka lengo la Sh trilioni 1.2 kwa mwaka huu wa fedha.

Mhe. Mavunde, amesema Serikali imeidhinisha asilimia 10 ya mapato yote ya sekta ya madini kuelekezwa kwenye utafiti wa kina wa jiofizikia ili kuongeza maeneo yanayofahamika kuwa na madini kutoka asilimia 16 ya sasa hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, amesema Serikali inaandaa mfuko maalumu wa mikopo kwa wachimbaji wadogo, ambao licha ya changamoto za mitaji na teknolojia, wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato ya sekta ya madini.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaanza operesheni ya kufuta kidijitali leseni zote za madini zisizotumika. Wamiliki watakaoshindwa kuwasilisha taarifa ndani ya muda uliowekwa watapewa notisi ya siku 30 kabla ya leseni hizo kujifuta moja kwa moja.

Nae, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha utajiri wa madini unakuwa chachu ya kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi kupitia uongezaji thamani badala ya kuishia kwenye uchimbaji pekee.

Amesema TMIC 2026 utawakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za fedha, kampuni za madini, wataalamu wa teknolojia, watafiti na wadau wengine kutoka duniani kote kujadili fursa za uwekezaji na maendeleo ya sekta hiyo.

 "Huu ni wakati wa kuingia katika awamu mpya ya uwekezaji, ubunifu na ukuaji wa sekta ya madini nchini," amesema.

Kwa upande wa Katibu Mtendaji wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, amesema mkutano huo unatarajiwa kuwakutanisha washiriki zaidi ya 2,000 na watoa mada zaidi ya 100 kutoka mataifa zaidi ya 50, huku zaidi ya mada 20 zikijadiliwa zikiwemo sera, kodi, uwekezaji, teknolojia, nishati safi, madini ya kimkakati, uongezaji thamani na masuala ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG).

Mchwampaka amesema TMIC 2026 pia utaweka mkazo katika maendeleo ya wachimbaji wadogo pamoja na ushirikishwaji wa wanawake na watu wenye ulemavu katika mnyororo mzima wa uongezaji thamani wa madini. Mkutano huo unatarajiwa kufungwa rasmi na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi.

..........