
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kuonesha nafasi yake katika kuchochea maendeleo ya viwanda na kukuza ubunifu wa vijana kwa kutoa elimu ya viwango na ubora wa bidhaa katika Maonesho ya Fursa za Kazi na Ubunifu kwa Vijana (Career Fair 2026), hatua inayolenga kuwajengea vijana uwezo wa kuzalisha bidhaa zenye ushindani katika soko la ndani na kimataifa.





Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), ameliagiza Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kushirikiana kikamilifu na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) pamoja na Taasisi nyingine husika katika kushughulikia na kuondoa kero zote zinazosababishwa na mifumo ya utoaji vibali kwa shehena zinazoingia nchini.
Waziri Kapinga ametoa agizo hilo akiwa ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Balozi Waziri Salum alipokutana na Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Dkt. Ashura Katunzi na ujumbe wake Mei 29, 2026 katika ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam, kufuatia kuibuka kwa changamoto zilizojitokeza wakati wa kuunganisha mfumo wa TANeSW wa TRA na mfumo wa OAS wa TBS na kusababisha usumbufu kwa baadhi ya wafanyabiashara.
Aidha, Waziri Kapinga amepongeza jitihada zinazoendelea kuchukuliwa baina ya TBS pamoja na TRA katika kuunganisha mifumo ya kielektroniki ili kurahisisha taratibu na kuongeza ufanisi wa utoaji wa vibali kwa shehena za mizigo inayoingia nchini.



Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akiwafariji wa watoto wa marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, wakati alipowasili Kilimani Wilayani Chato leo tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi akimfariji Mama Janeth Magufuli, kufuatia kifo cha marehemu Bi. Suzana Magufuli ambaye ni Mama wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, wakati alipowasili Kilimani Wilayani Chato leo tarehe 29 Mei 2026 Wilayani Chato.

MKINGA,TANGA,TANZANIA-Katika mwendelezo wa kuwa karibu na wananchi wenzake wa Mkinga,Mbunge wa Jimbo la Mkinga,Mheshimiwa Mwakioja,leo asubuhi ameshiriki katika mbio za DALUNI MARATHON 2026 akiwa kama Mgeni Rasmi.
Katika mwendelezo wa kuwa karibu na wananchi wenzake wa Mkinga,pia alipata nafasi ya kukimbia mbio za kilometa moja na kuibuka mshindi wa mbio hizo.
Imetolewa na:
🏢 Kitengo cha Mawasiliano,
📍 Ofisi ya Mbunge,Jimbo la Mkinga.
#Mkinga.#DaluniMarathon2026. #MabadilikoKwaMaendeleo.#Mwakioja.
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM
Mkutano wa kimataifa wa siku tatu wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere umezinduliwa rasmi jijini Dar es Salaam, ukiwa na lengo la kujadili masuala ya siasa za kimataifa (geopolitics), maendeleo na mwelekeo mpya wa Afrika katika mazingira ya dunia yanayobadilika kwa kasi.
Na Mwandishi Wetu
WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Mei 28, 2026 amewasili kuwa Mgeni Rasmi katika Kongamano la Kitaifa la Wadau wa Mazingira pamoja na maadhimisho ya miaka 40 ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) yanayofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.
Katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu ametembelea mabanda mbalimbali ya maonesho ya wadau wa mazingira na kupata fursa ya kujionea shughuli na teknolojia zinazotumika katika uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini.
📌 Vituo vitano vya CNG vinavyohamishika kununuliwa.
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), kwa kushirikiana na sekta binafsi, inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa vituo 10 vya CNG (Gesi Asilia Iliyobanwa) nchini katika mikoa ya Dar es Salaam vituo nane, Mtwara kituo kimoja na Morogoro kituo kimoja.
Salome ameeleza hayo leo Mei 28, 2026, Bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mhe. Arif Suleman Premji, Mbunge wa Mtwara Vijijini, aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuwekeza kwenye vituo vya CNG baada ya kuondoa ushuru wa shilingi 382 kwa kilo ya gesi ili kuhimiza matumizi ya CNG kwenye vyombo vya moto.
Salome amesema Serikali kupitia TPDC inakamilisha taratibu za ununuzi wa vituo vitano vya CNG vinavyohamishika (CNG Mobile Stations), kati ya hivyo vituo viwili vitawekwa Mkoa wa Dar es Salaam, kituo kimoja Mkoa wa Morogoro katika eneo la Chuo cha Ardhi, na vituo viwili Mkoa wa Dodoma katika maeneo ya Mji wa Serikali - Mtumba na Chako ni Chako.
Amesema Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi inaendelea na ujenzi wa vituo vya CNG katika maeneo mbalimbali nchini, Kwa sasa kuna vituo 18 vya CNG vinavyofanya kazi katika mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara na Pwani.
Aidha, Salome amefafanua kuwa Serikali inaendelea na majadiliano na kampuni binafsi sita kwa ajili ya kuendeleza miradi midogo ya kubadili gesi asilia kuwa kimiminika (Mini-LNG) na kusafirishwa kwa magari maalum kwenda mikoa mbalimbali nchini ambayo haijafikiwa na miundombinu ya mabomba ya gesi asilia.
Amesema kwa mikoa iliyopitiwa na bomba la gesi, ikiwemo Mtwara, Serikali imejielekeza zaidi katika kusambaza gesi majumbani na kwenye taasisi kupitia mabomba ili kuhakikisha wananchi wa maeneo hayo wananufaika na rasilimali hiyo.
Na Oscar Assenga, Tanga
MAMLAKA ya Bandari Tanzania (TPA) imesema kuanzishwa kwa tozo mpya ya maendeleo ya miundombinu ya bandari kutasaidia kuongeza uwezo wa bandari nchini kuhudumia shehena, kupunguza gharama kwa wafanyabiashara na kuchochea ukuaji wa uchumi.
Akizungumza jijini Tanga juzi katika mkutano wa wadau wa watumiaji wa Bandari ya Tanga kuhusu ada ya maendeleo ya miundombinu ya bandari, Meneja wa Bandari ya Tanga, Salehe Mbega, alisema tozo hiyo inayojulikana kama Port Infrastructure Development Levy (PID) ilitarajiwa kuanza kutumika Machi mwaka huu, lakini imeahirishwa hadi Julai Mosi kufuatia maoni ya wadau mbalimbali.
Mkutano huo ulihudhuriwa na wadau mbalimbali, wakiwemo wanachama wa Chama cha Mawakala wa Forodha Tanzania (TACAS), ambao waliunga mkono tozo hiyo wakisema italeta mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma bandarini nchini.
Mbega alisema lengo la tozo hiyo ni kuboresha miundombinu ya bandari ambayo imeanza kuelemewa kutokana na ongezeko kubwa la shehena katika bandari za Tanga, Dar es Salaam na Mtwara.
“Bandari ya Tanga kwa sasa inahudumia takribani tani milioni mbili za shehena kwa mwaka, wakati uwezo wa miundombinu iliyopo unatarajiwa kufikia tani milioni tatu ifikapo mwaka 2030. Hata hivyo, kutokana na kasi ya ukuaji wa shehena, kiwango hicho kinaweza kufikiwa mapema mwaka 2027 au 2028,” alisema Mbega.
Alisema Serikali kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya usafirishaji imeona umuhimu wa kuwekeza zaidi katika miundombinu ili bandari ziweze kuhimili ongezeko la mizigo.
Mbega alisema fedha zitakazokusanywa kupitia tozo hiyo zitatumika kujenga na kuboresha miundombinu mbalimbali, ikiwemo kuongeza gati jipya katika Bandari ya Tanga.
“Kwa sasa tuna magati mawili, lakini tuna mpango wa kuongeza gati la tatu lenye urefu wa mita 900. Pia eneo la Mwambani lina nafasi kubwa ya kujengwa bandari mpya yenye zaidi ya magati 10 katika eneo la ekari 174,” alisema.
Aliongeza kuwa maboresho hayo yataongeza uwezo wa nchi kuhudumia shehena nyingi zaidi na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Kwa mujibu wa Mbega, tozo hiyo pia itasaidia kupunguza gharama wanazopata wafanyabiashara kutokana na ucheleweshaji wa huduma bandarini.
Alisema baadhi ya meli hulazimika kusubiri nje ya bandari kwa muda wa wiki tatu hadi mwezi mmoja kabla ya kuhudumiwa, hali inayosababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara.
“Meli inapokaa nje ya bandari hulipiwa hadi dola za Marekani 20,000 kwa siku. Ukihesabu kwa mwezi mzima ni gharama kubwa sana kwa wafanyabiashara. Tozo hii itasaidia kuongeza ufanisi na kupunguza mzigo huo,” alisema.
Aidha, Mbega alisema maboresho yaliyofanywa kwenye reli ya Tanga kwa gharama ya Sh bilioni 429.1 yameongeza usafirishaji wa mizigo kwenda Rwanda na Burundi.
Alisema reli hiyo ambayo kwa muda mrefu ilikuwa haitumiki sasa imefunguliwa na kuanza kupokea shehena nyingi kutoka bandarini kwenda Isaka kabla ya kusafirishwa kwenda nchi hizo jirani.
Hata hivyo, alisema ongezeko la mahitaji ya usafirishaji kwa njia ya reli limezidi uwezo wa mabehewa yaliyopo.
“Wateja wanaopendelea kutumia reli wameongezeka zaidi kuliko uwezo wa mabehewa yaliyopo. Huu ni wakati sahihi kwa sekta ya reli kuongeza mabehewa ili kukidhi mahitaji ya soko,” alisema.
Awali akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa TACAS, Ephraim Mwankusye, alisema pendekezo la ada ya asilimia 4.5 ya maendeleo ya miundombinu ya bandari lina lengo la kusaidia maboresho makubwa ya bandari nchini ili kuongeza ufanisi wa huduma za usafirishaji wa mizigo.
Alisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kuendeleza Bandari za Dar es Salaam, Tanga, Mtwara pamoja na Bandari ya Bagamoyo na ujenzi wa miundombinu ya mafuta katika bandari mbalimbali nchini.
Mwankusye alisema lengo kubwa ni kuhakikisha bandari za Tanzania zinakuwa za kisasa, zenye uwezo mkubwa wa kuhudumia mizigo mingi kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.
Kwa mujibu wa pendekezo hilo, asilimia 4.5 ya tozo ya PID itaelekezwa katika miradi ya kuboresha bandari, magati, reli, matenki ya mafuta pamoja na barabara zinazosaidia usafirishaji wa mizigo.