HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

TPDC YAJIKITA KUTOA ELIMU ULINZI MIUNDOMBINU YA TAIFA

May 28, 2026 Add Comment

 Na Mwandishi Wetu


WAKATI vitendo vya uharibifu wa miundombinu katika miradi mbalimbali ya kimkakati ikiripotiwa kuendelea hapa nchini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania, (TPDC) limeimarisha ushirikiano na jamii kwa kutoa elimu kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhakikisha usalama wa miundombinu ya bomba la gesi asilia unakuwepo.

Katika Programu ya elimu kwa umma inayolenga kuongeza uelewa wa wananchi wanaoishi karibu na maeneo yanayopitiwa na bomba la gesi asilia iliyofanyika hivi karibuni kwenye vijiji vya Mkwalia Kitumbo na Sunguvuni, wilayani Mkuranga mkoani Pwani, maofisa wa shirika hilo wamesema lengo la elimu hiyo ni kuwafanya wananchi wawe sehemu ya mfumo wa ulinzi wa miundombinu hiyo muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Ofisa Mwandamizi wa Maendeleo ya Jamii wa TPDC, Bw. Oscar Mwakasege alisema mpango huo ni sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa shirika wa kushirikisha wananchi katika kulinda rasilimali za taifa pamoja na kuhakikisha jamii inakuwa na uelewa sahihi kuhusu matumizi salama ya maeneo yanayozunguka bomba la gesi.

Alisema TPDC imeona umuhimu wa kuwafikia wananchi moja kwa moja katika vijiji vyao ili kuwajengea uwezo wa kutambua viashiria vinavyoweza kuhatarisha usalama wa bomba la gesi na namna ya kuchukua hatua mapema.

“Lengo letu ni kuhakikisha wananchi wanaelewa umuhimu wa bomba la gesi asilia, namna ya kulilinda na kutoa taarifa mapema wanapoona viashiria vya uharibifu au shughuli zisizo salama karibu na miundombinu hiyo. Tunataka wananchi wawe walinzi wa kwanza wa rasilimali hii muhimu ya taifa,” alisema Bw. Mwakasege.

Aliongeza kuwa baadhi ya shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wa bomba la gesi ni pamoja na uchimbaji holela karibu na njia ya bomba, ujenzi usioruhusiwa, uchomaji moto ovyo pamoja na vitendo vya uharibifu wa alama za tahadhari zilizowekwa na mamlaka husika.

Kwa mujibu wa Bw. Mwakasege, usalama wa miundombinu ya gesi asilia una mchango mkubwa katika kuhakikisha huduma mbalimbali muhimu zinaendelea kutolewa nchini, ikiwemo uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi asilia, shughuli za viwandani na maendeleo ya sekta nyingine za uchumi.

Aidha alisema ushirikiano kati ya TPDC na wananchi umeendelea kuleta mafanikio katika maeneo mengi yanayopitiwa na bomba hilo, kwani wananchi wengi wamekuwa wakitoa taarifa mapema kuhusu shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wa miundombinu hiyo.

Katika mikutano hiyo ya elimu, wananchi walipata nafasi ya kuuliza maswali mbalimbali kuhusu usalama wa bomba la gesi, matumizi ya ardhi karibu na miundombinu hiyo pamoja na hatua zinazopaswa kuchukuliwa endapo kutatokea hali yoyote ya hatari.

Wananchi walioshiriki katika mikutano hiyo wameipongeza TPDC kwa kuwafikia moja kwa moja vijijini na kutoa elimu inayosaidia kulinda rasilimali za taifa huku ikijenga uelewa wa pamoja kuhusu masuala ya usalama.

Baadhi yao walisema hapo awali kulikuwa na uelewa mdogo kuhusu umuhimu wa bomba la gesi asilia na madhara yanayoweza kujitokeza endapo miundombinu hiyo itaharibiwa, lakini elimu inayotolewa sasa imewasaidia kuelewa wajibu wao kama sehemu ya jamii inayozunguka mradi huo.

Mwananchi mmoja kutoka kijiji cha Sunguvuni alisema elimu hiyo imewapa mwanga mpya kuhusu umuhimu wa kushirikiana na mamlaka katika kulinda rasilimali za taifa.

“Sasa tunajua kuwa bomba hili lina umuhimu mkubwa kwa taifa na hata kwa maendeleo ya wananchi wenyewe. Tuko tayari kushirikiana na TPDC kuhakikisha miundombinu hii inalindwa wakati wote,” alisema.

Kwa upande wake, uongozi wa vijiji vya Mkwalia Kitumbo na Sunguvuni umeeleza kuwa utaendelea kushirikiana na TPDC katika kutoa elimu kwa wananchi na kuhamasisha jamii kuwa sehemu ya ulinzi wa bomba la gesi.

Utoaji wa elimu kwa umma uaendelea kutekelezwa katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Pwani ikiwa ni sehemu ya juhudi za TPDC za kuimarisha usalama wa miundombinu ya gesi asilia na kujenga mahusiano mazuri kati ya shirika hilo na jamii inayozunguka mradi wa gesi asilia.

TPDC imesisitiza kuwa ushirikiano wa wananchi ni nguzo muhimu katika kuhakikisha miundombinu ya gesi asilia inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho pamoja na kuendelea kuchochea maendeleo ya uchumi wa taifa.
Ofisa Mwandamizi wa Maendeleo ya jamii kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC)Oscar Mwakasege akizungumza na wananchi wa vijiji vya wilaya ya Mkuranga hivi karibuni kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu ya Taifa.

WAZIRI MKUU MGENI RASMI KONGAMANO LA WADAU WA MAZINGIRA, MIAKA 40 YA NEMC

May 28, 2026 Add Comment



WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba leo Mei 28, 2026 amewasili kuwa Mgeni Rasmi katika Kongamano la Kitaifa la Wadau wa Mazingira pamoja na maadhimisho ya miaka 40 ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) yanayofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.

Katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu ametembelea mabanda mbalimbali ya maonesho ya wadau wa mazingira na kupata fursa ya kujionea shughuli na teknolojia zinazotumika katika uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini.


SERIKALI KUJENGA VITUO 10 VYA GESI YA CNG NCHINI: SALOME

May 28, 2026 Add Comment




📌 Vituo vitano vya CNG vinavyohamishika kununuliwa.


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), kwa kushirikiana na sekta binafsi, inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa vituo 10 vya CNG (Gesi Asilia Iliyobanwa) nchini katika mikoa ya Dar es Salaam vituo nane, Mtwara kituo kimoja na Morogoro kituo kimoja.


Salome ameeleza hayo leo Mei 28, 2026, Bungeni jijini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mhe. Arif Suleman Premji, Mbunge wa Mtwara Vijijini, aliyetaka kujua mkakati wa Serikali wa kuwekeza kwenye vituo vya CNG baada ya kuondoa ushuru wa shilingi 382 kwa kilo ya gesi ili kuhimiza matumizi ya CNG kwenye vyombo vya moto.

Salome amesema Serikali kupitia TPDC inakamilisha taratibu za ununuzi wa vituo vitano vya CNG vinavyohamishika (CNG Mobile Stations), kati ya hivyo vituo viwili vitawekwa Mkoa wa Dar es Salaam, kituo kimoja Mkoa wa Morogoro katika eneo la Chuo cha Ardhi, na vituo viwili Mkoa wa Dodoma katika maeneo ya Mji wa Serikali - Mtumba na Chako ni Chako.


Amesema Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi inaendelea na ujenzi wa vituo vya CNG katika maeneo mbalimbali nchini, Kwa sasa kuna vituo 18 vya CNG vinavyofanya kazi katika mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara na Pwani.

Aidha, Salome amefafanua kuwa Serikali inaendelea na majadiliano na kampuni binafsi sita kwa ajili ya kuendeleza miradi midogo ya kubadili gesi asilia kuwa kimiminika (Mini-LNG) na kusafirishwa kwa magari maalum kwenda mikoa mbalimbali nchini ambayo haijafikiwa na miundombinu ya mabomba ya gesi asilia.



Amesema kwa mikoa iliyopitiwa na bomba la gesi, ikiwemo Mtwara, Serikali imejielekeza zaidi katika kusambaza gesi majumbani na kwenye taasisi kupitia mabomba ili kuhakikisha wananchi wa maeneo hayo wananufaika na rasilimali hiyo.

TPA -TOZO MPYA YA MIUNDOMBINU KUONGEZA UFANISI WA BANDARI.

May 28, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga, Tanga

MAMLAKA ya Bandari Tanzania (TPA) imesema kuanzishwa kwa tozo mpya ya maendeleo ya miundombinu ya bandari kutasaidia kuongeza uwezo wa bandari nchini kuhudumia shehena, kupunguza gharama kwa wafanyabiashara na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Akizungumza jijini Tanga juzi katika mkutano wa wadau wa watumiaji wa Bandari ya Tanga kuhusu ada ya maendeleo ya miundombinu ya bandari, Meneja wa Bandari ya Tanga, Salehe Mbega, alisema tozo hiyo inayojulikana kama Port Infrastructure Development Levy (PID) ilitarajiwa kuanza kutumika Machi mwaka huu, lakini imeahirishwa hadi Julai Mosi kufuatia maoni ya wadau mbalimbali.

Mkutano huo ulihudhuriwa na wadau mbalimbali, wakiwemo wanachama wa Chama cha Mawakala wa Forodha Tanzania (TACAS), ambao waliunga mkono tozo hiyo wakisema italeta mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma bandarini nchini.

Mbega alisema lengo la tozo hiyo ni kuboresha miundombinu ya bandari ambayo imeanza kuelemewa kutokana na ongezeko kubwa la shehena katika bandari za Tanga, Dar es Salaam na Mtwara.

“Bandari ya Tanga kwa sasa inahudumia takribani tani milioni mbili za shehena kwa mwaka, wakati uwezo wa miundombinu iliyopo unatarajiwa kufikia tani milioni tatu ifikapo mwaka 2030. Hata hivyo, kutokana na kasi ya ukuaji wa shehena, kiwango hicho kinaweza kufikiwa mapema mwaka 2027 au 2028,” alisema Mbega.

Alisema Serikali kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya usafirishaji imeona umuhimu wa kuwekeza zaidi katika miundombinu ili bandari ziweze kuhimili ongezeko la mizigo.

Mbega alisema fedha zitakazokusanywa kupitia tozo hiyo zitatumika kujenga na kuboresha miundombinu mbalimbali, ikiwemo kuongeza gati jipya katika Bandari ya Tanga.

“Kwa sasa tuna magati mawili, lakini tuna mpango wa kuongeza gati la tatu lenye urefu wa mita 900. Pia eneo la Mwambani lina nafasi kubwa ya kujengwa bandari mpya yenye zaidi ya magati 10 katika eneo la ekari 174,” alisema.

Aliongeza kuwa maboresho hayo yataongeza uwezo wa nchi kuhudumia shehena nyingi zaidi na kuifanya Tanzania kuwa kitovu muhimu cha biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Kwa mujibu wa Mbega, tozo hiyo pia itasaidia kupunguza gharama wanazopata wafanyabiashara kutokana na ucheleweshaji wa huduma bandarini.

Alisema baadhi ya meli hulazimika kusubiri nje ya bandari kwa muda wa wiki tatu hadi mwezi mmoja kabla ya kuhudumiwa, hali inayosababisha hasara kubwa kwa wafanyabiashara.

“Meli inapokaa nje ya bandari hulipiwa hadi dola za Marekani 20,000 kwa siku. Ukihesabu kwa mwezi mzima ni gharama kubwa sana kwa wafanyabiashara. Tozo hii itasaidia kuongeza ufanisi na kupunguza mzigo huo,” alisema.

Aidha, Mbega alisema maboresho yaliyofanywa kwenye reli ya Tanga kwa gharama ya Sh bilioni 429.1 yameongeza usafirishaji wa mizigo kwenda Rwanda na Burundi.

Alisema reli hiyo ambayo kwa muda mrefu ilikuwa haitumiki sasa imefunguliwa na kuanza kupokea shehena nyingi kutoka bandarini kwenda Isaka kabla ya kusafirishwa kwenda nchi hizo jirani.

Hata hivyo, alisema ongezeko la mahitaji ya usafirishaji kwa njia ya reli limezidi uwezo wa mabehewa yaliyopo.


“Wateja wanaopendelea kutumia reli wameongezeka zaidi kuliko uwezo wa mabehewa yaliyopo. Huu ni wakati sahihi kwa sekta ya reli kuongeza mabehewa ili kukidhi mahitaji ya soko,” alisema.

Awali akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa TACAS, Ephraim Mwankusye, alisema pendekezo la ada ya asilimia 4.5 ya maendeleo ya miundombinu ya bandari lina lengo la kusaidia maboresho makubwa ya bandari nchini ili kuongeza ufanisi wa huduma za usafirishaji wa mizigo.

Alisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kuendeleza Bandari za Dar es Salaam, Tanga, Mtwara pamoja na Bandari ya Bagamoyo na ujenzi wa miundombinu ya mafuta katika bandari mbalimbali nchini.

Mwankusye alisema lengo kubwa ni kuhakikisha bandari za Tanzania zinakuwa za kisasa, zenye uwezo mkubwa wa kuhudumia mizigo mingi kwa haraka na kwa ufanisi zaidi.

Kwa mujibu wa pendekezo hilo, asilimia 4.5 ya tozo ya PID itaelekezwa katika miradi ya kuboresha bandari, magati, reli, matenki ya mafuta pamoja na barabara zinazosaidia usafirishaji wa mizigo.

TANESCO YATAMBULIWA KAMA SEKTA WEZESHI NA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM (UDSM)

May 27, 2026 Add Comment


📍Yapokea cheti cha pongezi kwa mchango wake katika kuendeleza elimu jumuishi

📍Utambuzi watolewa katika hafla maalum ya kuwapongeza wadau wa maendeleo wa UDSM


Na Mwandishi Wetu


Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limetambuliwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kama miongoni mwa sekta wezeshi zinazochangia maendeleo ya elimu jumuishi na ustawi wa wanafunzi chuoni hapo.


Utambuzi huo umetolewa Mei 26, 2026, wakati wa hafla maalum ya kuwatambua na kuwapongeza wadau wa maendeleo wa chuo hicho iliyofanyika katika Ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.


Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe.Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete, amesema mchango wa wadau mbalimbali wakiwemo TANESCO una mchango mkubwa katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na maendeleo ya kitaaluma kwa wanafunzi.

“Tunapowasaidia wanafunzi hawa, hatuwafanyii fadhila. Tunathibitisha uwezo wao, utu wao na nafasi yao halali katika elimu ya juu,” amesema Dkt. Kikwete.


Aidha, ameshukuru wadau wote wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na chuo hicho katika kuhakikisha upatikanaji wa elimu jumuishi kwa wanafunzi wote, wakiwemo wenye mahitaji maalum.

Kwa upande wa TANESCO, cheti hicho cha utambuzi na pongezi kilipokelewa na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja, Irene Gowelle, kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji Lazaro Twange. 


Utambuzi huo umetolewa ikiwa ni ishara ya kuthamini mchango wa TANESCO katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na kujisomea kwa wanafunzi pamoja na wakufunzi wenye changamoto mbalimbali za ulemavu na mahitaji maalumu chuoni hapo.


Hafla hiyo ilibebwa na kaulimbiu isemayo “Kujenga Mazingira Jumuishi ya Kujifunzia kupitia Ushirikiano wa Kimkakati”, ikiwa na lengo la kuhamasisha ushirikiano kati ya taasisi, wadau wa maendeleo na jamii katika kuendeleza elimu jumuishi nchini.



Katika hafla hiyo pia, Dkt. Kikwete alizindua rasmi mbio za “UDSM Marathon 2026” zitakazofanyika Desemba 5, 2026, zikiwa na lengo la kukusanya rasilimali kwa ajili ya kusaidia elimu jumuishi, ustawi wa wanafunzi na programu za kuwasaidia wanafunzi wenye mahitaji maalum.

BARRICK NORTH MARA YAZINDUA KLINIKI AWAMU YA PILI YA UTATUZI WA MIGOGORO VIJIJI 11 VINAVYOZUNGUKA MGODI

May 27, 2026 Add Comment

 

Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele, akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kliniki ya kusikiliza na kushughulikia malalamiko ya wananchi dhidi ya Mgodi wa Barrick North Mara.
Meneja wa Idara ya Mahusiano ya Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara, Francis Uhadi, akizungumza wakati wa uzinduzi wa kliniki hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele na viongozi wa Barrick wakiwa katika picha ya pamoja na wadau wengine baada ya uzinduzi wa awamu ya pili ya Kiliniki ya Kusikiliza na Kushughulikia Malalamiko ya Wananchi.

BUNGE LAPITISHA BAJETI YA WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI

May 27, 2026 Add Comment
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepitisha bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa mwaka wa fedha 2026/2027 baada ya kujadili na kuidhinisha makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara hiyo.

JESCA SIMUCHILE FT EV. DANIEL SAFARI WAACHIA VIDEO MPYA YA INJILI “TUIMBE TUMEPONA”

May 26, 2026 Add Comment

 




Muimbaji wa muziki wa injili Jesca Simuchile kwa kushirikiana na Ev. Daniel Safari wameachia rasmi video mpya ya wimbo wao unaoitwa “Tuimbe Tumepona”, kazi yenye ujumbe wa matumaini, ushuhuda na kumshukuru Mungu kwa wema wake.

PAULINA GEKUL AMBURUZA MTOTO KORTINI, MAHAKAMA YASIMAMISHA KESI

May 26, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu


BABATI — Mahakama ya Mwanzo Wilaya ya Babati mkoani Manyara imesitisha kusikiliza kesi ya jinai namba 291 ya mwaka 2026 iliyofunguliwa na aliyekuwa Mbunge wa Babati Mjini, Paulina Gekul, inayomkabili Brayton Lucas (17), baada ya kujiridhisha kuwa mshtakiwa huyo ni mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 18 na hivyo shauri hilo linapaswa kusikilizwa katika Mahakama ya Watoto kwa mujibu wa sheria.

Uamuzi huo ulitolewa baada ya Wakili wa upande wa utetezi, Thadei Lister, kuiomba mahakama kujiridhisha kuhusu umri wa mshtakiwa kwa kuwasilisha nyaraka mbalimbali ikiwemo cheti cha kuzaliwa kilichoonesha kuwa Brayton alizaliwa Novemba 12, 2008 na kwa sasa ana umri wa miaka 17 na miezi sita, tofauti na taarifa zilizokuwa katika hati ya mashtaka zilizomtaja kuwa na miaka 19.




Katika shauri hilo, Paulina Gekul alidai kuwa Brayton Lucas, ambaye alikuwa akichunga mifugo yake, alihusika katika wizi wa mbuzi 15 wenye thamani ya shilingi milioni tatu, kosa linalodaiwa kufanyika chini ya kifungu cha 268 cha sheria ya wizi wa mifugo. Kesi hiyo ilikuwa na jumla ya watuhumiwa watatu.

Mahakama pia ilielezwa kuwa mtoto huyo alikuwa amechanganywa katika shauri moja na watuhumiwa watu wazima, jambo ambalo upande wa utetezi ulidai ni kinyume na sheria zinazolinda haki za mtoto.




Baada ya kupitia nyaraka zilizowasilishwa, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Babati, Ahmed Mgodo, alisema mahakama imejiridhisha kuwa Brayton Lucas ni mtoto na hivyo haina mamlaka ya kuendelea kusikiliza kesi hiyo. Kutokana na uamuzi huo, mahakama ilisimamisha shauri hilo dhidi ya mshtakiwa huyo na kuagiza polisi kuandaa hati mpya ya mashtaka kwa mujibu wa sheria zinazohusu watoto.

Brayton Lucas alipatiwa dhamana huku washtakiwa wawili wengine wakiendelea kushikiliwa. Wakili Thadei Lister amesema wako tayari kuendelea kumtetea mtoto huyo iwapo atafikishwa katika Mahakama ya Watoto.

Akizungumza nje ya mahakama, Wakili Thadei alisema Brayton ni mwanafunzi wa kidato cha nne ambaye alitoweka akiwa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha na wazazi wake walikuwa wakimtafuta kwa kipindi cha miezi mitatu kabla ya kupata taarifa kuwa amekamatwa Babati kwa tuhuma za wizi.

Mama mzazi wa Brayton alisema mtoto wake alitakiwa kuwa shuleni baada ya kumaliza kidato cha nne na tayari alikuwa amepangiwa shule, lakini aliondoka nyumbani bila kutoa taarifa na baada ya juhudi za muda mrefu za kumtafuta walipata taarifa kuwa alikuwa Babati akifanya kazi.


Wakati huo huo, Diwani wa Kata ya Maruvango Wilaya ya Arumeru Mashariki, Digna Nassari, amesema taarifa za kupotea kwa mtoto huyo zilikuwa zimetolewa polisi miezi mitatu kabla ya kufunguliwa kesi dhidi yake na Paulina Gekul.

Aidha, Digna amesema Brayton ni miongoni mwa watoto 16 kutoka kata hiyo waliotoroka shule, huku akisisitiza umuhimu wa jamii kushirikiana kuhakikisha watoto wanarudi katika mfumo wa elimu na kupata ulinzi unaostahili

TBS YASISITIZA USALAMA WA CHAKULA KATIKA BIASHARA ZA UOKAJI (BAKERY)

May 26, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limetoa mafunzo maalumu kwa wafanyabiashara wa bidhaa za uokaji (bakary) Mkoa wa  Dar es Salaam ili kuongeza uelewa kuhusu masuala ya viwango, kuboresha usalama wa chakula na kuimarisha ushindani wa biashara zao sambamba na kulinda afya za watumiaji.

JAB YAWATAKA WAANDISHI KUTAFAKARI MWELEKEZO WA TASNIA

May 26, 2026 Add Comment

 



Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Bw. Tido Mhando, amewataka Waandishi wa Habari nchini kutafakari upya wajibu wao katika kuijenga jamii kupitia maudhui yenye tija, akieleza kuwa ipo haja ya kurejesha hadhi na nguvu ya taaluma hiyo katika kujenga fikra na maendeleo ya taifa.


Akizungumza jijini Dar es Salaam, Bw. Mhando amesema pamoja na JAB kusimamia utoaji wa ithibati kwa kuzingatia vigezo vya elimu na sheria, bado kuna umuhimu wa Waandishi wa Habari kuendelea kujengewa uwezo kupitia mafunzo ya kitaaluma.

“Tukitazama baadhi ya vyombo vyetu vya habari, iwe ni magazeti, redio au televisheni, mambo ya kufikirisha kwa kiasi kikubwa yamepungua. Waandishi wa Habari wanapaswa kutafakari kama hiyo ndiyo taswira wanayotaka kuiacha katika jamii ya Watanzania,” amesema.

Amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa ya kuunda mtazamo wa jamii, hivyo kuna wajibu wa kuhakikisha maudhui yanayotolewa yanajenga uelewa, yanakuza maendeleo na yanalinda maslahi ya taifa.

“Tunachosimamia ni kuhakikisha Mwandishi wa Habari anayepata ithibati anakuwa na kiwango cha elimu kisichopungua Diploma, lakini tunataka pia Waandishi wa Habari waendelee kupata mafunzo ili waweze kuimarika zaidi kitaaluma,” amesema.

WAZIRI SANGU AZINDUA BODI YA SABA YA USHAURI YA OSHA.

May 26, 2026 Add Comment
-Asisitiza Utekelezaji wa Viwango vya Kimataifa vya Usalama na Afya katika Maeneo ya Kazi
NAIBU WAZIRI KWAGILWA AHIMIZA USHIRIKIANO USAFI WA MAZINGIRA

NAIBU WAZIRI KWAGILWA AHIMIZA USHIRIKIANO USAFI WA MAZINGIRA

May 26, 2026 Add Comment




Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa leo Mei 25, 2026 akiongoza zoezi la usafi wa mazingira lililohusisha uokotaji wa taka na kusafisha mifereji ya maji machafu katika eneo la Taifa Road ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.



Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa lei Mei 25, 2026 akipanda mti aina ya mwembe katika eneo la Shule ya Sekondari ya Ndaoya, Mtaa wa Chongoleani jijini Tanga ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.



Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa leo Mei 25, 2026 akizungumza na wananchi katika uwanja wa Tangamaano jijini Tanga mara baada ya zoezi la usafi wa mazingira lililohusisha uokotaji wa taka na kusafisha mifereji ya maji machafu katika eneo la Taifa Road ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa leo Mei 25, 2026 akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian alipowasili katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa kabla ya zoezi la upandaji miti na usafi wa mazingira ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.

TPDC YAHIMIZA WANANCHI KULINDA MIUNDOMBINU YA BOMBA LA GESI ASILIA

May 25, 2026 Add Comment


Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeendelea kuwashirikisha  wananchi katika kulinda miundombinu ya bomba la gesi asilia, likieleza kuwa usalama wa miundombinu hiyo unategemea kwa kiasi kikubwa ushirikiano wa jamii nzima.

Katika kuimarisha ulinzi huo, TPDC inaendelea kutekeleza programu ya utoaji elimu kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yanayopitiwa na bomba la gesi asilia mkoani Pwani, hususan katika wilaya za Rufiji, Kibiti na Mkuranga.

 Lengo la programu hiyo ni kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu hiyo pamoja na kuwajengea uwezo wa kutambua na kuripoti mapema vitendo au shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wake.


Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Afisa Maendeleo ya Jamii wa TPDC, Bi. Ashura Hoja alisema “Bomba la gesi asilia ni rasilimali ya taifa hivyo  kila mwananchi ana wajibu wa kuwa mlinzi wa miundombinu hii na  kutoa taarifa mapema mnapoona shughuli zisizo za kawaida karibu na bomba la gesi,” alisema Bi. Hoja

Aidha, TPDC imewapongeza wananchi wa maeneo husika kwa mwitikio wao katika kushiriki kulinda miundombinu hiyo, huku ikiwataka kuendelea kuwa makini zaidi kwani uharibifu wowote unaweza kuathiri huduma muhimu pamoja na maendeleo ya taifa kwa ujumla.


Kwa upande wake, mwananchi wa Kijiji cha Jaribu Mpakani, Wilaya ya Kibiti, Bw. Kassimu Iddi alisema elimu inayotolewa na TPDC imeleta mabadiliko makubwa ya mtazamo kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda bomba la gesi.

“Sasa tunaelewa kuwa kulinda bomba la gesi ni kulinda maisha yetu na maendeleo ya taifa letu. Tumeamua kuwa walinzi wa kwanza wa miundombinu hii,” alisema Kassimu

TPDC imeendelea kutoa wito kwa jamii zote zinazoishi karibu na bomba la gesi asilia kushiriki kikamilifu katika mfumo wa ulinzi wa pamoja, ili kuhakikisha miundombinu hiyo inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

TANZANIA KUANDAA MPANGO WA HATUA ZA MAPEMA ZA KUJIANDAA KUKABILIANA NA UKAME - DKT. YONAZI

May 25, 2026 Add Comment


Na Mwandishi wetu - Msumbiji

TANZANIA  inaandaa Mpango wa Kitaifa wa Hatua za Mapema za kujiandaa, kukabiliana na ukame kwa maeneo yanayokabiliwa na janga hilo kwa kushirikiana na Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), ikiwa ni jitihada za kupunguza athari za janga hilo nchini.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya serikali kuachana na utaratibu wa kusubiri madhara yatokee ndipo ichukue hatua, na badala yake kuelekea katika usimamizi wa hatari unaozingatia maandalizi na tahadhari za mapema.


Hayo yameelewa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi, katika ziara ya kubadilishana uzoefu kati ya Tanzania na Msumbiji kuhusu hatua za mapema kabla ya majanga unaoendelea kwa siku tano kuanzia tarehe 25 hadi 29 Mei, 2026 Mjini Maputo Msumbiji.

Alisema ukame una madhara makubwa katika kilimo, mifugo, rasilimali za maji, usalama wa chakula, maisha ya wananchi, maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa ujumla.


“Kwa sasa Tanzania inaendelea kuandaa Mpango wa Kitaifa wa Hatua za Mapema dhidi ya ukame kwa msaada wa WFP, kwa kutambua kuwa bado ni moja ya majanga makubwa yanayoathiri nchi yetu,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa mpango huo utawezesha kuwepo kwa mifumo imara ya tahadhari na utekelezaji wa hatua za mapema kabla ya majanga hayajatokea.

Kuhusu ziara hiyo, Dkt. Yonazi alisema Tanzania imechagua kujifunza kutoka Msumbiji kutokana na mafanikio yake katika kuanzisha na kutekeleza mifumo ya hatua za mapema dhidi ya majanga, hususan ukame, mafuriko na vimbunga.

Alisema kupitia ushirikiano huo, Tanzania itanufaika kwa kubadilishana uzoefu na mbinu bora, kujifunza mifumo ya uratibu wa taasisi, vigezo vya kuanzisha hatua za mapema pamoja na namna ya kugharamia hatua hizo.

Aidha, alieleza kuwa uzoefu huo utasaidia kuunganisha hatua za mapema ndani ya mifumo ya hifadhi ya jamii ili kuongeza ufanisi katika kukabiliana na majanga.

“Ziara hii ni muhimu kwa Tanzania katika kujifunza kwa vitendo na kupata mafunzo kutokana na mafanikio ya Msumbiji katika utekelezaji wa hatua za mapema kabla ya maafa,” alisema.

=MWISHO=