HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WIZARA YA NISHATI YAPOKEA TRIL.1 ZA MIRADI YA MAENDELEO

March 10, 2026 Add Comment




 ðŸ“ŒNi asilimia 61 ya bajeti ya 2025/26


Na Mwandishi Wetu, Dodoma


WIZARA ya Nishati imepokea Sh. trilioni 1.150 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika kipindi cha Julai 2025 hadi Februari 2026, sawa na asilimia 61 ya bajeti ya maendeleo iliyoidhinishwa kwa mwaka wa fedha 2025/26.


Taarifa hiyo imetolewa Machi 10, 2026 na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, wakati akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi ya sekta ya nishati kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini inayoongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Subira Mgalu, katika Ukumbi wa Bunge jijini Dodoma.

Mhe.Ndejembi amesema katika mwaka wa fedha 2025/26 wizara imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo inayolenga kuimarisha uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini.

Amesema katika fedha zilizopokelewa hadi sasa, Sh. bilioni 410.04 ni fedha za ndani na Sh. bilioni 740.30 ni fedha za nje ambazo zimeendelea kusaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya sekta ya nishati.

Ameongeza kuwa miradi hiyo inajumuisha upelekaji wa umeme vijijini na vitongojini, utafutaji na uendelezaji wa mafuta na gesi asilia, ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji na uhifadhi wa bidhaa za mafuta ya petroli pamoja na kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Kwa mujibu wa Ndejembi, katika mwaka wa fedha 2025/26 Wizara ya Nishati iliidhinishiwa kutumia jumla ya Sh trilioni 1.965, ambapo Sh trilioni 1.886 sawa na asilimia 95.97 zilitengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo huku Sh bilioni 79.23 sawa na asilimia 4.03 zikiwa kwa matumizi ya kawaida.

Amefafanua kuwa kati ya fedha za maendeleo zilizoidhinishwa, Sh trilioni 1.466 ni fedha za ndani na Sh bilioni 420.49 ni fedha za nje.

Ndejembi ameishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa miongozo na maelekezo ambayo imekuwa ikitoa na kuchangia mafanikio katika utekelezaji wa miradi hiyo.

Amesisitiza kuwa wizara itaendelea kupokea ushauri na maoni ya kamati hiyo pamoja na kutoa ushirikiano unaostahili ili kuimarisha maendeleo ya sekta ya nishati nchini.



WALAJI KUNUFAIKA NA UFUATILIAJI WA FCC KWENYE MIKATABA YA UPANDE MMOJA

March 10, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu
Dar es Salaam, Machi 10, 2026. Tume ya Ushindani (FCC) imesema itaendelea kusimamia kwa karibu haki za walaji kwa taasisi na kampuni zinazotumia mikataba iliyoandaliwa kwa upande mmoja, ili kuhakikisha watumiaji wa huduma na bidhaa hawapati hasara kutokana na mikataba hiyo.
Kauli hiyo imetolewa leo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Khadija Ngasongwa, alipokuwa akizungumza katika semina ya wadau kutoka taasisi na kampuni zinazotumia mikataba ya upande mmoja, iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Ngasongwa alisema FCC inaendelea kufuatilia kwa karibu mikataba ya aina hiyo ili kuhakikisha haikiuki haki za walaji katika soko. Alifafanua kuwa mikataba ya upande mmoja hutumiwa sana na taasisi mbalimbali kwa lengo la kurahisisha utoaji wa huduma kwa wakati, lakini ni muhimu iwe chini ya uangalizi ili kuepuka matumizi yanayoweza kuwa kinyume na sheria za ushindani na ulinzi wa mlaji.
Alisema semina hiyo ni sehemu ya mwendelezo wa utoaji wa elimu kwa wadau kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani, yanayolenga kuongeza uelewa kuhusu haki na wajibu wa walaji pamoja na watoa huduma.
“Ninatambua kuwa mikataba inayoandaliwa kwa upande mmoja ina faida katika kurahisisha utoaji wa huduma kwa wakati. Hata hivyo, FCC ina jukumu la kuifuatilia kwa karibu, kwani bila uangalizi kunaweza kuwa na mambo yanayofanyika kinyume na maslahi ya walaji katika soko,” alisema Ngasongwa.
Aliongeza kuwa hata pale taasisi zinapotaka kuunganisha huduma au mikataba yao, ni muhimu kufanya tathmini ya kina ili kubaini kama kuna vipengele vinavyoweza kukiuka masharti ya ushindani au kuathiri ubora wa huduma kwa walaji.
Ngasongwa alisisitiza kuwa kila mtu ni mlaji kwa namna moja au nyingine, hivyo ni muhimu kuhakikisha thamani ya fedha inayotolewa na mteja inaendana na ubora wa huduma au bidhaa anayopata. Alisema hali hiyo pia husaidia kujenga uaminifu kati ya watoa huduma na walaji.
Aidha, alisema FCC itaendelea kukutana na makundi mbalimbali ya wadau kwa lengo la kuwapa uelewa mpana kuhusu majukumu ya taasisi hiyo na umuhimu wa kuzingatia sheria za ushindani na ulinzi wa mlaji.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA), Tusekelege Mwaikasu, alisema semina hiyo ni muhimu kwa taasisi za kifedha kwani itawasaidia kuboresha utoaji wa huduma kwa walaji kwa kuzingatia viwango vinavyokubalika.
Alisema benki, kupitia umoja wao, zimekuwa zikitekeleza kampeni ya “Niko Fiti”, inayolenga kuhakikisha huduma za kifedha zinatolewa kwa ubora na kwa kuzingatia mahitaji ya walaji.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindqni Ushindani Ushindani (FCC), Bi. Khadija Ngasongwa akizungumza wakati akifungua Semina kwa Taasisi na Kampuni zenye mikataba iliyoandaliwa upande mmoja jijini Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani FCC, Bi.Magdalena Utouh  akizunguza wakati wa kuhitimisha semina ya wadau wa Taasisi na Kampuni zenye mikataba iliyoandaliwa na upande mmoja jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa FCC,Bi. Roberta Feruzi akitoa maelezo kuhusiana na Semina ya wadau wa Taasisi na Kampuni zenye mikataba iliyoandaliwa upande mmoja jijini Dar es Salaam. Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA ) Bi.Tusekelege Mwaikasu akitoa neno kwa niaba ya wadau katika mkutano na FCC ,jijini Dar es Salaam. Mkutano ukiendelea Kaimu Mkurugenzi Mkurugenzi Mkuu wa FCC Khadija Ngasongwa akiwa katika matukio picha za za pamoja makundi mbalimbali.

SHULE 13 TEMEKE KUANZA KUPIKA KWA UMEME

March 10, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu


GHARAMA za kupika chakula cha wanafunzi katika shule 13 za msingi Wilaya ya Temeke, mkoani Dar es Salaam, zinatarajiwa kupungua kwa kiasi kikubwa kufuatia shule hizo kuanza kutumia nishati ya umeme kupikia badala ya kuni.


Hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa majiko ya umeme katika taasisi za elimu ya msingi unaosimamiwa kwa ushirikiano wa Wizara ya Nishati, Idara ya Elimu ya Awali na Msingi ya Wilaya ya Temeke pamoja na Shirika la Chakula Duniani (WFP).

Akizungumza wakati wa ziara ya kukagua utekelezaji wa mradi huo katika Shule ya Msingi Kibasila, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Halima Rukumbwe, amesema awali walikuwa wanatumia kati ya Sh.20,000 hadi Sh.25,000 kwa siku kupika chakula cha wanafunzi 450, ikiwemo uji na chai ya asubuhi pamoja na chakula cha mchana cha wali na maharagwe.

Amesema baada ya kuanza kutumia majiko ya umeme, gharama hizo zimepungua na kufikia kati ya Sh.8,000 hadi Sh.10,000 kwa siku, huku kiasi hicho kikijumuisha pia matumizi ya mota ya kupandisha maji kwa shughuli mbalimbali za shule.

“Mbali na kupunguza gharama, wapishi sasa wanapika chakula kwa muda mfupi zaidi na katika mazingira safi,” amesema Rukumbwe.


Ameongeza kuwa matumizi ya nishati hiyo yamechangia pia kupungua kwa utoro wa wanafunzi, kwani chakula kinapatikana kwa wakati na hivyo kuwahamasisha wanafunzi kuhudhuria masomo.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia wa Wizara ya Nishati, Omar Khalifa amesema mradi huo katika awamu ya kwanza unatekelezwa katika mikoa minne ambayo ni Dar es Salaam (Wilaya ya Temeke), Dodoma (Wilaya ya Dodoma Mjini), Tabora (Wilaya ya Tabora Mjini) na Kigoma.

Naye, Mshauri wa Chakula kutoka Shirika la Chakula Duniani (WFP), Dkt. Geoffrey Ngegwa amesema katika Mkoa wa Dar es Salaam mradi huo unatekelezwa katika shule 13 za Wilaya ya Temeke.

Amesema mbali na Shule ya Msingi Kibasila ambayo tayari imeanza kutumia mfumo huo, shule nyingine zinazoendelea kukamilishiwa miundombinu ni Likwati, Madenge, Umoja, Alhasan Mwinyi, Unubini, Lioness Miburani, Nzasa, Ponde, Wailes, Chemchem na Charambe.

Ameongeza kuwa miundombinu katika shule hizo tayari imekamilika na kinachosubiriwa kwa sasa ni ufungaji wa masufuria ya kisasa ya kupikia (pressure cooker) unaotarajiwa kukamilika mwishoni mwa Machi 2026.


&&&

KIKOSI CHA DHARURA NA UOKOAJI CHA BARRICK NORTH MARA CHAOKOA WANANCHI WALIOZINGIRWA NA MAJI TARIME

March 10, 2026 Add Comment

Shughuli za uokoaji wakulima waliozingirwa na mafuriko katika eneo la mashambani kijijini Matongo wilayani Tarime
Shughuli za uokoaji wakulima waliozingirwa na mafuriko katika eneo la mashambani kijijini Matongo wilayani Tarime
Faida za kuwepo mwekezaji mwenye uwezo, teknolojia za kisasa na mahusiano mazuri na jamii umedhihirika kutokana na Kikosi cha Dharura na Uokoaji (ERT) kutoka Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara ambacho kimesaidia kuokoa watu 22 wakiwemo watoto - waliokuwa wamezingirwa na mafuriko na kukwama kwa siku mbili katika kijiji cha Matongo, wilayani Tarime.

MAAFISA ELIMU MIKOA 26 WAPATIWA MAFUNZO ARUSHA

March 10, 2026 Add Comment
Mafunzo ya siku tano kwa Maafisa Elimu kutoka mikoa 26 ya Tanzania Bara yameanza rasmi jijini Arusha, yakilenga kuwajengea uwezo viongozi hao katika utekelezaji wa majukumu yao ya kiutendaji.

TANZANIA YASHIKA NAFASI YA NNE KWA UWEKEZAJI SEKTA YA MADINI AFRIKA

March 10, 2026 Add Comment

 

▪️Ni ya 4 barani Afrika, nyuma ya Botswana, Morocco na Zambia

▪️Alama ya Tanzania yapanda hadi 68.04 mwaka 2025 kutoka 62.75 (2024) na 46.38 (2023)

▪️Tanzania yaorodheshwa nafasi ya 15 duniani kwenye Best Practices Mineral Potential Index kwa alama 75.00

▪️Utafiti uliwahusisha wataalam na viongozi 2,304 wa kampuni za utafiti na uchimbaji.

▪️Rais Samia apongezwa kwa mazingira mazuri ya Uwekezaji Tanzania

Tanzania imeendelea kuimarisha nafasi yake kama kivutio cha kimataifa cha uwekezaji kwenye sekta ya madini baada ya kuorodheshwa miongoni mwa maeneo yanayoongoza barani Afrika, kwa mujibu wa ripoti ya Fraser Institute, Annual Survey of Mining Companies 2025.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Tanzania imepata nafasi ya 34 kati ya maeneo 68 duniani yaliyotathminiwa katika Investment Attractiveness Index (IAI), kielezo kinachotumiwa na wawekezaji na kampuni za utafiti wa madini kuamua wapi waelekeze mitaji ya utafiti na maendeleo ya miradi.  

Katika muktadha wa Afrika, Tanzania imeendelea kushika nafasi ya juu kwa kuwa ya 4 barani Afrika katika IAI, ikifuata Botswana, Morocco na Zambia, hatua inayothibitisha ushindani wa Tanzania katika kuvutia mitaji ya kimataifa ya utafiti na uwekezaji wa madini.  

Ripoti inaonesha pia mwenendo chanya wa kupanda kwa alama za Tanzania, ambapo alama ya IAI imefikia 68.04 mwaka 2025, ikilinganishwa na 62.75 mwaka 2024 na 46.38 mwaka 2023 mwenendo unaoashiria kuongezeka kwa uaminifu na mvuto wa Tanzania kwa wawekezaji wa sekta ya madini.  

Kwa maelezo ya ripoti, IAI hujengwa kwa kuzingatia vipengele viwili vikuu vinavyoongoza maamuzi ya uwekezaji: uwezo wa kijiolojia wa rasilimali (mineral potential) na mazingira ya jumla ya kufanya biashara kwenye sekta husika. Ripoti hiyo inaeleza kuwa katika hesabu yake, asilimia 60 ya uzito huenda kwenye mineral potential na asilimia 40 huenda kwenye policy framework, ili kutoa taswira ya mvuto wa eneo husika kwa uwekezaji wa utafiti na uchimbaji.  

Katika kipengele cha Best Practices Mineral Potential Index kinachoangalia mvuto wa kijiolojia kama eneo lingekuwa na kanuni bora zaidi duniani Tanzania imeorodheshwa nafasi ya 15 duniani kwa alama 75.00, jambo linaloonesha kwa uwazi ukubwa wa fursa na uwezo wa rasilimali madini zilizopo nchini.  

Utafiti huu wa Fraser Institute ni miongoni mwa rejea muhimu zinazotumiwa kimataifa na sekta binafsi, taasisi za utafiti na wadau mbalimbali kutathmini mwenendo wa masoko ya uwekezaji wa madini. Kwa mujibu wa taarifa ya utafiti, dodoso lilipelekwa kwa viongozi na wataalam 2,304 wa kampuni za utafiti na uchimbaji, na waliotoa majibu waliripoti matumizi ya pamoja ya takribani Dola za Marekani bilioni 4.2 kwenye shughuli za utafiti wa madini mwaka 2025.  

Kwa Tanzania, nafasi hii inaongeza msukumo kwenye jitihada za Serikali za kuendelea kuimarisha sekta ya madini kama nguzo muhimu ya uchumi ikiwemo kuongeza utafiti, kuvutia mitaji mikubwa ya uendelezaji wa miradi, na kukuza ushiriki wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani wa madini.  

Wataalamu wa uchumi na wadau wa sekta ya madini nchini wamempongeza Rais Dkt. Samia S. Hassan kwa kuvutia uwekezaji mkubwa kwenye sekta ya madini nchini Tanzania,huku wengi wakibashiri kuwa sekta ya madini kuwa nguzo kuu ya uchumi wa Tanzania kwa miaka michache ijayo.