HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WAKULIMA WA PAMBA IGUNGA WAJITOKEZA KWA WINGI KUFUNGUA AKAUNTI

WAKULIMA WA PAMBA IGUNGA WAJITOKEZA KWA WINGI KUFUNGUA AKAUNTI

June 12, 2026 Add Comment

Wakulima wa zao la pamba kutoka vijiji vya Mbutu, Iyogelo, Ilambakuki, Imalanguzu na Mwamakoma vilivyopo katika Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora, wamehamasika kufungua akaunti za benki na kusajili laini za simu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea malipo ya mazao yao kwa njia ya kidijitali. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi, usalama na uharaka wa malipo kwa wakulima.

Wakulima hao wamefungua akaunti kupitia Benki ya NMB pamoja na kusajili laini kupitia mtandao wa simu wa Mixx by Yas, hatua itakayowawezesha kupokea fedha zao kwa urahisi kupitia mifumo ya benki na huduma za kifedha za simu za mkononi.

Zoezi hilo limefanyika kwa kushirikiana na AMCOS za Ngw'ajojabi, Ngw'asabi na Mwamakoma AMCOS, likitekelezwa kufuatia waraka wa Mrajis wa Vyama vya Ushirika unaoelekeza malipo ya wakulima wa pamba kufanyika kupitia akaunti za benki na huduma za fedha kwa njia ya simu badala ya kutegemea fedha taslimu. Lengo ni kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati, kwa uwazi na kwa usalama zaidi.

Mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka siku hadi siku kufuatia juhudi za uhamasishaji zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali. Hadi kufikia Juni 10, 2026, jumla ya wakulima 506 wamejitokeza na kufungua akaunti pamoja na kujiunga na huduma za kifedha za simu, hatua inayoonesha uelewa na utayari mkubwa wa wakulima kupokea mabadiliko ya mfumo wa malipo ya kidijitali.

Aidha, uhamasishaji wa zoezi hilo umefanywa na Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Tabora, Peja Mhoja pamoja na Mrajis Msaidizi (Uhamasishaji), Ibrahim Kadudu, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wakulima kujiunga na mifumo rasmi ya kifedha ili kunufaika na malipo ya kisasa, salama na yenye tija.

TANESCO YAFUNGUA UKURASA MPYA WA MATUMIZI YA UMEME NCHINI

June 12, 2026 Add Comment










📍Yazindua vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme

📍Wananchi kunufaika na mpango wa ukopeshaji wa majiko ya umeme kupitia LUKU




Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limezindua mradi wa vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme pamoja na Mpango wa Ukopeshaji wa Majiko ya Umeme kwa Wateja (On-Bill Financing – OBF), hatua inayofungua ukurasa mpya wa matumizi ya umeme nchini na kuharakisha utekelezaji wa ajenda ya nishati safi.

Akizindua miradi hiyo jijini Dodoma, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb) leo tarehe 11 Juni, 2026 alisema hatua hiyo inaonesha dhamira ya Tanzania kushiriki kikamilifu katika mageuzi ya matumizi ya nishati safi duniani huku ikilenga kuboresha maisha ya wananchi na kukuza uchumi.

“Hatua hii inapanua matumizi ya umeme kutoka kupikia hadi usafiri, kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi, kupunguza gharama za maisha na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa,” alisema Mhe. Ndejembi.

Alisema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya nishati, hali iliyowezesha uzalishaji wa umeme nchini kufikia zaidi ya megawati 4,000 na kuweka msingi wa matumizi mapana ya umeme katika sekta mbalimbali za uchumi.

Katika kuimarisha matumizi ya vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme, TANESCO kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) imepokea mashine 50 za kisasa za kuchajia vyombo hivyo kutoka kampuni ya AUTEL ya China. Mashine hizo zitafungwa katika maeneo mbalimbali ya kimkakati nchini ili kurahisisha huduma za uchaji.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, alisema Shirika limejipanga kuongoza mageuzi ya matumizi ya umeme nchini kwa kutumia fursa ya upatikanaji wa umeme wa kutosha.

“Mtazamo wa awali kwamba umeme ni ghali na matumizi yake yanaishia kwenye mwanga pekee umebadilika kwa kiasi kikubwa. Leo, wananchi wengi wanatumia umeme katika kupikia na shughuli mbalimbali za kiuchumi, huku hatua ya kuzindua vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme ikifungua ukurasa mpya wa matumizi ya nishati safi nchini,” alisema Bw. Twange.

Kwa upande wa nishati safi ya kupikia, TANESCO imeanza kutekeleza Mpango wa On-Bill Financing (OBF) utakaowezesha wateja kupata majiko ya umeme kwa mkopo na kufanya marejesho kupitia manunuzi yao ya kawaida ya umeme wa LUKU.


Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, ameipongeza TANESCO kwa hatua hiyo na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini.

“Nawapongeza TANESCO kwa hatua hii ya kimkakati inayofungua fursa mpya za matumizi ya nishati safi nchini. Ni muhimu kuendelea kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi katika usafiri na kupikia ili kuharakisha maendeleo na kuhifadhi mazingira,” alisema Senyamule.

Uzinduzi wa miradi hiyo unaashiria hatua mpya ya kupanua matumizi ya umeme nchini kutoka matumizi ya kawaida ya majumbani hadi sekta za usafiri, kupikia na shughuli za uzalishaji mali, sambamba na juhudi za Taifa kuelekea uchumi wa kijani na maendeleo endelevu.






TPSC YASIFIWA KUPUNGUZA WATUMISHI WASIO NA MAADILI, KUONGEZA TIJA SERIKALINI

Kajunason June 11, 2026 Add Comment

 

MTWARA – Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeipongeza Taasisi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa mchango wake mkubwa wa kupunguza watumishi wasio na maadili na kuongeza tija serikalini. Pongezi hizo zimetolewa leo, Juni 11, 2026, mkoani Mtwara na Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Xavier Mrope Daudi, wakati akifungua rasmi Baraza la Sita la Wafanyakazi wa chuo hicho.Akizungumza katika ufunguzi huo, Bw. Daudi alisema kuwa Serikali inatambua na kuthamini juhudi kubwa zinazofanywa na chuo hicho katika kuandaa watumishi wa umma kupitia mafunzo mbalimbali. Aliongeza kuwa matunda ya kazi nzuri ya chuo hicho yameleta matokeo chanya kwa kiasi kikubwa katika kuboresha utendaji kazi na nidhamu maeneo ya kazi, jambo linalochangia kuwepo kwa watumishi wenye tija na uadilifu mkubwa.


Aidha, Naibu Katibu Mkuu alisisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora na kutumia lugha yenye staha kwa wateja, akibainisha kuwa chuo hicho ndicho jiko linalopika watumishi wa umma tangu wanapoingia hadi wanapotoka kazini, hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa. Alitoa rai pia kwa uongozi wa chuo kuendelea kubuni mifumo mipya ya TEHAMA kwa kushirikiana na mamlaka husika ili kurahisisha utoaji wa mafunzo kwa watumishi na jamii kwa ujumla, hasa kwa kuwa chuo hicho tayari kiko mstari wa mbele katika matumizi ya teknolojia.

Kuhusu baraza hilo la wafanyakazi, Bw. Daudi alieleza kuwa ni chombo muhimu kinachotoa fursa ya kujadiliana masuala ya tija, ufanisi, na maslahi ya watumishi. Alihimiza uwepo wa maelewano, ushirikiano, na nidhamu kazini ili kuleta mshikamano utakaosaidia chuo kupiga hatua zaidi katika nyanja za mafunzo, tafiti, na ushauri wa kitaaluma, huku akitaka majadiliano ya baraza hilo yatawaliwe na hekima, busara, na uwazi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa TPSC, Dkt. Ernest Mabonesho, ameishukuru serikali kwa kukipatia chuo hicho jumla ya Shilingi bilioni 8.4 katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka wa fedha 2024/25 hadi 2026/27. Fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Kampasi ya Tanga, ambapo ujenzi wake unaendelea vizuri baada ya kupokea bilioni 1.5 katika awamu ya kwanza, bilioni 2.6 awamu ya pili, na bilioni 4.3 zilizotengwa kwa ajili ya mwaka mpya wa fedha unaoanza Julai 2026.

Dkt. Mabonesho alibainisha kuwa baraza hilo la sita linajumuisha wajumbe 64 kutoka kampasi zote sita za chuo hicho, wakiwemo wawakilishi wa menejimenti, wafanyakazi, na viongozi wa chama cha wafanyakazi (TUGHE). Katika kikao hicho cha Mtwara, wajumbe watapitia na kujadili Mpango Mkakati wa Miaka Mitano (2026/27 - 2030/31), Mpango wa Bajeti ya mwaka ujao wa fedha, pamoja na tathmini ya utekelezaji wa bajeti ya kipindi kilichopita ili kuweka vipaumbele thabiti.

Alihitimisha kwa kusisitiza kuwa wafanyakazi wote wa TPSC wamejipanga kufanya kazi kwa weledi, uadilifu, na bidii ili kutekeleza kwa ufanisi malengo ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, yenye kusudi la kuleta maendeleo na kuondoa umaskini nchini.





















SERIKALI YASISITIZA NAFASI YA UTAFITI KATIKA KUJENGA UCHUMI WA MAARIFA

June 11, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Serikali imesisitiza umuhimu wa kuimarisha elimu, utafiti na ubunifu kama nguzo muhimu za kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi wa kisasa unaotegemea maarifa, teknolojia na ushindani wa kimataifa.

TUCTA-MWRC KUWAPA MWONGOZO WAFANYAKAZI WANAOTAFUTA AJIRA NJE YA NCHI

June 11, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) kwa kushirikiana na Shirika la Kazi la Umoja wa Mataifa (ILO) limezindua Kituo cha Msaada kwa Wafanyakazi Wahamiaji Tanzania (TUCTA-MWRC) kwa lengo la kuwapatia taarifa, ushauri na msaada wafanyakazi wanaotafuta ajira ndani na nje ya nchi.

WAZIRI PROF,MKUMBO ATAJA MAENEO MATANO YA KIPAUMBELE MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA WA MWAKA 2026/27

June 11, 2026 Add Comment

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amewasilisha Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2026/27 akisisitiza vipaumbele vitano vya utekelezaji wake.

Akitaja vipaumbele hivyo, amesema mosi ni kuimarisha utawala bora, demokrasia, amani, na utulivu na pili ni kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani na kipaumbele cha tatu ni, kuimarisha uwezo wa watu na maendeleo ya jamii.

Akiendelea kufafanua vipambele hivyo, Mhe. Waziri amesema kipaumbele cha nne ni kuimarisha uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu kwa mabadiliko ya tabianchi na cha tano kikiwa kusimamia utekelezaji wa vichocheo vya mageuzi ambavyo ni pamoja na nishati, miundombinu ya usafiri na usafirishaji, utafiti na maendeleo, na mageuzi ya kidigitali.

Prof Kitila amesesema utekelezaji wa vipaumbele hivyo ni hatua za kuyatekeleza malengo makuu ya Dira 2050, na vimezingatia Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 wenye dhima ya “Mageuzi kwa ajili ya Ukuaji Jumuishi wa Uchumi na Uzalishaji Ajira” ambao ni wa kwanza katika utekelezaji wa Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/27 – 2050/51.

Aidha katika kutekeleza maeneo ya vipaumbele hivyo, Serikali imepanga kuanza kutekeleza programu na miradi mbalimbali ikiwemo miradi shikizi 38 kati ya 51 iliyopo katika programu saba (7) za kielelezo zilizoainishwa katika Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano.