HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

Wanawake wa TPSC Watoa Misaada Gereza la Segerea Kuelekea Siku ya Wanawake Duniani

March 04, 2026 Add Comment
Wanawake wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dar es Salam  wametembelea Gereza la Segerea na kutoa misaada mbalimbali kwa wafungwa, ikiwa ni sehemu ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa kila mwaka Machi 8.
Ziara hiyo pia imekuwa muendelezo wa maadhimisho ya miaka 25 ya chuo hicho, ambapo taasisi imekuwa ikitekeleza shughuli za kurejesha kwa jamii kupitia matendo ya kijamii na misaada kwa makundi yenye uhitaji.
Akizungumza wakati wa kukabidhi misaada hiyo, Zena Hussein, Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC, aliyemwakilisha Mkuu wa Chuo, amesema wanamshukuru Mkuu wa  chuo kwa kuwawezesha kutekeleza jukumu hilo la kijamii, akieleza kuwa lengo ni kuonyesha upendo na mshikamano kwa wafungwa kama sehemu ya jamii.
Amesema kuwa, kama wanawake wafanyakazi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, wameona umuhimu wa kutambua kundi hilo na kujitoa kwa moyo wa huruma wakiamini kuwa si kila aliyepo gerezani ni mkosaji wa kukusudia, bali baadhi yao wamejikuta katika mazingira magumu yasiyotegemewa. Ameongeza kuwa misingi ya dini, kwa Waislamu na Wakristo, inahimiza kusaidia wahitaji na kuwa watoaji, hivyo wameamua kupeleka kile walichoweza kumudu.
Miongoni mwa misaada iliyotolewa ni sukari, mchele, unga, maharage, maji, dawa za usafi, khanga, mashuka ya watoto, ndala, mifagio, dawa za meno, mafuta ya kupaka, pedi za wanawake, nepi za watoto, maziwa ya watoto, vitabu vya dini ikiwemo Qur’an na Biblia pamoja na nguo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Gereza la Wanawake Segerea, SSP Hamida Mussa Matimba, ameishukuru TPSC kwa msaada huo akisema vitabu vya dini vitakuwa nguzo muhimu katika kuwajenga wafungwa kiimani na kuwasaidia katika mchakato wa mabadiliko chanya.
Alieleza kuwa gereza hilo linaendesha programu mbalimbali za mafunzo ya ufundi stadi ikiwemo ushonaji, upishi, ufyatuaji wa matofali, ujenzi, ufundi magari na umeme, akisisitiza kuwa lengo ni kuhakikisha kila anayeingia gerezani anatoka akiwa na mabadiliko chanya ya kiimani, kimaadili na kiujuzi ili aweze kujitegemea anaporejea uraiani.
Aidha, aliwahimiza wanawake kuwa na moyo wa kusamehe ili kupunguza migogoro inayoweza kuishia kwenye vyombo vya sheria, akitolea mfano wa migogoro ya madeni katika vikundi vya mikopo. Pia alitoa wito kwa wazazi kuwalea vijana, hususan mabinti, katika misingi ya maadili na kuwajenga kuridhika ili kuepuka tamaa zinazoweza kuwaingiza katika matatizo ya kisheria.
Kaulimbiu ya Siku ya Wanawake Duniani mwaka 2026 inasema: “Haki na usawa kwa wanawake na wasichana ni msingi jumuishi kufikia Dira 2050.” Ziara hiyo imeakisi dhamira ya wanawake wa TPSC ya kuadhimisha siku hiyo kwa vitendo vinavyogusa jamii moja kwa moja
Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC,Zena Hussein (kushoto) akikabidhi
Meneja wa Sehemu ya Mafunzo kwa Njia ya Mtandao TPSC,Zena Hussein akizungmza wakati kukabidhi misaada huo.
Mkuu wa Gereza la Wanawake Segerea, SSP Hamida Mussa Matimba akizungumza  wakati wa kukabidhi misaada huo. 
 
UJUMBE RASMI WA MAADHIMISHO YA SIKU YA KIMATAIFA YA WANYAMAPORI – 2026

UJUMBE RASMI WA MAADHIMISHO YA SIKU YA KIMATAIFA YA WANYAMAPORI – 2026

March 04, 2026 Add Comment
 

Kauli Mbiu ya Mwaka 2026:

“Medicinal and Aromatic Plants and Their Contribution to Human Welfare: The Way Forward for Sustainable Use”

(“Mimea ya Dawa na Harufu na Mchango Wake kwa Ustawi wa Binadamu: Njia ya Mbele ya Matumizi Endelevu”)

Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), tunaungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Tanzania Wildlife Management Authority (TAWA), pamoja na wadau wote wa uhifadhi wa mazingira, vyombo vya habari, na watabibu asili nchini kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanyamapori tarehe 03 Machi 2026. Aidha, tunaungana na mataifa mengine duniani kusherehekea siku hii muhimu inayotukumbusha wajibu wetu wa kulinda urithi wa asili kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Maadhimisho ya mwaka huu yanatukumbusha umuhimu wa kulinda na kutumia kwa busara rasilimali za asili, hususan mimea ya dawa na harufu, ambayo imekuwa nguzo muhimu katika afya ya jamii, ukuaji wa uchumi wa taifa, na ustawi wa binadamu kwa ujumla. Mimea hii si tu hazina ya tiba asilia bali pia ni rasilimali yenye mchango mkubwa katika tafiti za kisayansi, viwanda vya dawa, na maendeleo ya kijamii.

Tanzania imebarikiwa kuwa na bioanuwai adhimu ya wanyamapori, misitu, na vyanzo vya maji. Rasilimali hizi ni urithi wa taifa letu na msingi wa maendeleo endelevu. Hivyo basi, tunapaswa kushirikiana kwa dhati katika:

• Kulinda wanyamapori dhidi ya ujangili na uharibifu wa makazi yao.

• Kuhifadhi mimea ya tiba kwa matumizi endelevu yasiyoharibu mazingira.

• Kulinda vyanzo vya maji na mifumo ya ikolojia kwa manufaa ya sasa na vizazi vijavyo.

• Kuwezesha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi na kunufaika nazo kiuchumi.

Tukiongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025–2050 inayolenga kujenga taifa lenye uchumi imara, amani, utulivu na maendeleo endelevu ya watu wake, tunasisitiza kuwa:

“Uhifadhi wa rasilimali za asili ni msingi wa ustawi wa taifa na kizazi kijacho.”

Kwa pamoja, tushikamane kulinda urithi wetu wa asili, kuenzi thamani ya mimea ya dawa, na kuhakikisha matumizi yake yanafanyika kwa njia endelevu kwa manufaa ya binadamu na mazingira.

TUSHIRIKIANE KWA UHIFADHI, USTAWI NA MAENDELEO ENDELEVU 

Imetolewa na: Boniventura Mwalongo

Katibu Mkuu Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO)

BRELA KUIMARISHA URASIMISHAJI NA MIFUMO YA KIDIJITALI

BRELA KUIMARISHA URASIMISHAJI NA MIFUMO YA KIDIJITALI

March 04, 2026 Add Comment

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), yatakiwa kuongeza kasi ya urasimishaji wa biashara na kuimarisha mifumo ya kidijitali ili kuchochea ufanisi na ukuaji wa uchumi kwani BRELA ni lango kuu la uwekezaji nchini.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Judith Kapinga (Mb), Machi 04, 2026, wakati akifungua Baraza la wafanyakazi la BRELA na kuhimiza uwekezaji kwenye rasilimali watu, akitaka watumishi wapewe mafunzo na stahiki zao kwani ustawi wa wafanyakazi ndio siri ya mafanikio ya taasisi, na kuwataka watumishi kufanya kazi kwa uadilifu, weledi, na uzalendo.

Waziri Kapinga amebainisha kuwa kwa mujibu wa tafiti mbalimbali za wadau, zaidi ya 80% ya biashara nchini zipo sekta isiyo rasmi, hivyo BRELA lazima iwe kinara wa kuzirasimisha, hatua ambayo itawawezesha Wajasiriamali wadogo kupata mikopo, masoko, na ulinzi wa kisheria.

Aidha, ameagiza kuhuisha mifumo ya TEHAMA ili iwe rafiki itakayopunguza gharama pamoja na muda wa mteja kupata huduma na kusisitiza kuwa mifumo hiyo lazima iwe na usalama wa taarifa wa hali ya juu na itumike kupata mrejesho wa haraka kutoka kwa wateja ili kuboresha utendaji.

Aidha, ameipongeza BRELA kwa ongezeko la usajili na makusanyo, akisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyakazi na kuitaka taasisi hiyo kugeukia mfumo wa uwezeshaji badala ya udhibiti pekee ili kukuza sekta binafsi nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa BRELA Bw. Godfrey Nyaisa amebainisha kuwa BRELA imevuka lengo la mapato kwa asilimia 105 na kutekeleza malengo kwa asilimia 78 katika nusu mwaka wa 2025/26, ambapo taasisi hiyo imewasilisha Shilingi bilioni 3.1 kwa Msajili wa Hazina, na kusema mafanikio hayo yanayotokana na mshikamano, kujituma na bidii ya watumishi.

Vilevile, amewasilisha Mpango Mkakati wa 2026–2031 unaolenga kuboresha za usajili na miundombinu, ikiwemo ujenzi wa ofisi za Dodoma na Kinondoni na kubainisha kuwa uongozi unaendelea kuimarisha maslahi ya watumishi kupitia muundo mpya wa mishahara na motisha ili kutatua changamoto za uhaba wa wafanyakazi na kuongeza tija.

 

OPERESHENI KALI: DCEA YAKAMATA TANI 9.93 ZA DAWA ZA KULEVYA

March 04, 2026 Add Comment

  


Mwezi Januari na Februari 2026, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya imekamata tani 9.93 za dawa za kulevya aina mbalimbali, chupa 1,795 za dawa tiba zenye asili ya kulevya na kuteketeza ekari 87.5 za mashamba ya bangi.  Magari 6 na pikipiki 29 vilikamatwa katika operesheni hizo huku watuhumiwa 151 wakikamatwa kuhusika na uhalifu huo. 

RC MARA ATEMBELEA UJENZI WA MAKAZI MAPYA YA WANANCHI WANAOPISHA UPANUZI WA MGODI WA BARRICK NORTH MARA

March 04, 2026 Add Comment

 


Mkuu wa Mkoa wa Mara,Kanali Evans Mtambi akitembelea moja ya sehemu inapojengwa nyumba ya mwananchi ambaye amepatiwa fidia kupisha upanuzi wa mgodi wa Barrick North Mara,aliongozana na viongozi mbalimbali wa Serikali mkoani humo na maofisa waandamizi wa mgodi.
Mkuu wa Mkoa wa Mara,Kanali Evans Mtambi akitembelea moja ya sehemu inapojengwa nyumba ya mwananchi ambaye amepatiwa fidia kupisha upanuzi wa mgodi wa Barrick North Mara,aliongozana na viongozi mbalimbali wa Serikali mkoani humo na maofisa waandamizi wa mgodi.
Mkuu wa Mkoa wa Mara,Kanali Evans Mtambi akitembelea moja ya sehemu inapojengwa nyumba ya mwananchi ambaye amepatiwa fidia kupisha upanuzi wa mgodi wa Barrick North Mara,aliongozana na viongozi mbalimbali wa Serikali mkoani humo na maofisa waandamizi wa mgodi.

RC TANGA AIPONGEZA NHC KWA UJENZI WA JENGO LA KITEGA UCHUMI MKWAKWANI PLAZA

March 04, 2026 Add Comment

 












Na Oscar Assenga, Tanga

MKUU wa Mkoa wa Tanga Balozi Batilda Burian amefanya ziara ya kutembelea Jengo la Kitega Uchumi la Shirika la Taifa la  Nyumba (NHC) “Mkwakwani Plaza” ambalo litagharimu kiasi cha Bilioni 8.6 huku akiwapongeza  kwa  usimamizi imara na ubora mkubwa.

Akizungumza akiwa katika eneo la mradi huo RC Batilda alisema kwamba ubunifu ambao wameutumia shirika hilo kuanzia hatua ya ujenzi mpaka usimamizi wanafanya wenyewe kupitia wataalamu wao jambo ambalo litawezesha kuwepo kwa ubora.

Alisema kwamba kutokana na uwepo wa fursa hiyo watu wa Tanga wanapaswa kuichangamkia sasa na wasisubiri bali waanze sasa kujiitokeza kuchukua nyumba katika Jengo hilo la kitega Uchumi la NHC

“Nitumie fursa hii kuwahimiza wananchi kuchangamkia fursa zilizopo katika Jengo hili wale ambao wana fedha za mitaji waweze kuzungumza na Meneja wa NHC na leo tumekuja kwenye ziara hapa na kamati ya usalama ya mkoa kukagua ujenzi wa jengo hilo niendelee kuwapongeza NHC kazi inaendelea vizuri na ya viwango vya hali ya juu hongereni sana”Alisema  

Aidha alimpongeza Rais Dkt Samia Suluhu kwa kuendelea kusukuma mbela maendeleo katika sekta mbalimbali ikiwemo miundombinu na makazi

Awali akizungumza Menej awa Shirika la Taifa la Nyumba (NHC) Mhandisi Mussa Kamendu alisema kwamba Jengo hilo litakuwa na maeneo ya maduka ,ofisi za kupangisha katika sehemu ya Biashara huku likiwa na Gorofa nne za makazi.

Alisema kwamba katika Jengo hilo eneo la makazi nyumba ya vyuma viwili itakuwa inauzwa kwa kiasi cha Milioni 178 na za vyumba vitatu zitauzwa kwa shilingi Milioni 240 bei zote zikijumuisha VAT.

Aidha alisema kwamba wanawakaribisha wananchi kuchangia fursa ya kuweza kununua vyumba hizo huku akiwashukuru ambao wamekwisha kujitokeza na wapangaji wamepata wengi.

Naye kwa upande wake Mhandisi wa Ujenzi huo Mhandisi Ephahim Fanuel Msigwa alisema kwamva  jengo hilo lilianza mwaka 2025 na kwa mujibu wa  mkataba wanatakiwa kumaliza  mwezi Juni 2027.

Mhandisi Ephahim aliongeza kwamba kupitia mradi huo wametengeneza ajira za kazi 189 na wanawashukuru watu wa Tanga wamejitokeza kwa asilimia kubwa .

Mradi wa jengo hilo la Mkwakwani Plaza ni mradi wa Kisasa ambalo linajumisha sehemu za biashara na makazi na kwamba utajkapokamilika utaongeza thamani ya mji wa Tanga na kutoa fursa zaidi ya ajira na uwekezaji kwa wananchi.

PCOI LOHI ZAKARIA, JIKE LA MBEGU LILILOKABILIANA USO KWA USO NA FARU HIFADHI YA NGORONGORO

March 04, 2026 Add Comment




Anajulikana kwa jina la Utani Profesa kutokana na uwezo mkubwa wa kujua vitu vingi katika hifadhi ya Ngorongoro katika utumishi wake wa miaka 34, ni mwanamke shupavu kuelekea siku ya wanawake tarehe 8 Machi, 2026


Tukio la kusisimua na hatari katika maisha yake ni tarehe 6 Machi 2020 Kreta ya Ngorongoro kwenye utekelezaji wa majukumu yake, ghafla Faru akamkimbiza bila yeye kujua ambapo alijaribu kutumia mbinu za medani alizofundishwa jeshini kujinasua lakini bahati mbaya alishambuliwa ingawa baadaye aliweza kuokolewa na kukimbizwa hospitali kwa matibabu.


Kamanda huyu wa Uhifadhi anaadhimisha siku ya wanawake duniani akiendelea kuchapa kazi na mara nyingi utamkuta kreta akifanya shughuli za uhifadhi, utafiti, sensa za wanyamapori na kupambana na mimea vamizi bila woga.


Ngorongoro tunampa maua yake kwa kuwa uzoefu ni mama wa Maarifa hivyo yeye kama Chanda chema tunamvika Pete anapotimiza miaka 6 ya tukio la Faru.

MHE. MCHENGERWA ; USHIRIKIANO IMARA WA MFUKO WA PAMOJA WA AFYA NI NGUZO YA MAGEUZI YA SEKTA YA AFYA NCHINI

March 04, 2026 Add Comment

Na John Mapepele

Waziri wa Afya, Mohammed Mchengerwa, amesema kuwa ushirikiano madhubuti kati ya Serikali na Washirika wa Mfuko wa Pamoja wa Afya (Health Basket Fund) umeendelea kuwa chachu ya maboresho makubwa katika utoaji wa huduma za afya nchini.
JUKWAA LA UWEZESHAJI WANAWAKE HANDENI MJI KUZINDULIWA MACHI 5

JUKWAA LA UWEZESHAJI WANAWAKE HANDENI MJI KUZINDULIWA MACHI 5

March 04, 2026 Add Comment
 

Na Mwandishi Wetu

KATIKA kuelekea kilele cha maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, Halmashauri ya Mji Handeni imejipanga kutekeleza shughuli mbalimbali ikiwamo uzinduzi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi.

Akizungumza kuhusu maandalizi ya maadhimisho hayo, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema halmashauri hiyo inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa wanawake katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Amesema Machi 5, 2026 kutafanyika kongamano la wanawake litakaloenda sambamba na uzinduzi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi la Halmashauri ya Mji Handeni, linalolenga kuwaunganisha wanawake ili kubadilishana uzoefu, kupata taarifa za fursa za kiuchumi na kuimarisha shughuli zao za ujasiriamali.

Ukwaju amesema kongamano hilo pia litaambatana na maonesho ya bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na wanawake wajasiriamali, hatua inayolenga kuonesha ubunifu wao pamoja na juhudi wanazofanya katika kujikwamua kiuchumi.

Ameongeza kuwa katika kongamano hilo litakalofanyika katika ukumbi wa CCM Wilaya ya Handeni, washiriki watapatiwa elimu mbalimbali ikiwemo masuala ya umiliki wa ardhi na mirathi, malezi na makuzi ya watoto, ujasiriamali na biashara, elimu ya ushirika na SACCOS pamoja na kilimo bora na ufugaji wa kisasa.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, Machi 6, 2026 halmashauri itatoa msaada kwa baadhi ya kaya zinazoishi katika mazingira hatarishi ikiwa ni sehemu ya kuonesha mshikamano na kusaidia jamii zenye uhitaji.

Kadhalika amesema kilele cha maadhimisho hayo kwa ngazi ya Halmashauri kitafanyika Machi 7, 2026 katika viwanja vya Shule ya Msingi Kwenjugo, ambapo kutafanyika ugawaji wa taulo za kike kwa wanafunzi wa kike pamoja na utoaji wa vyeti kwa vikundi vinne vya wanawake vilivyotekeleza miradi yao kwa mafanikio na kurejesha mikopo ya asilimia 10 kwa wakati. Amesema mgeni rasmi katika shughuli hizo anatarajiwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese.

Ukwaju amesema maadhimisho hayo yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050,” huku halmashauri ikiendelea kuhamasisha wananchi wote kushiriki kikamilifu katika kuimarisha usawa wa kijinsia na kuchochea maendeleo jumuishi kwa wanawake na wasichana.