HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

DC KILOSA AONGOZA UKAGUZI MAENEO YALIYOATHIRIWA NA MVUA

December 31, 2025 Add Comment

 

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka, akikagua miundombinu ya barabra iliyoharibiwa na mvua kubwa iliyonyesha wilayani humo.

.....................................

Na Dotto Mwaibale

Uongozi ni dhamana aliyopewa kiongozi husika kwa ajili ya kusimamia shughuli za maendeleo pamoja na  changamoto mbalimbali za wananchi zinapo jitokeza na siyo kukaa ofisini na kuwatuma au kuwaagiza wakuu wa idara kwenda kuzishughulikia.

Disemba 26 2025  mvua kubwa zilinyesha katika Tarafa ya Kidete wilayani Kilosa mkoani Morogoro na kuharibu baadhi ya miundombinu ya barabara na mashamba na kuwaacha wananchi wasijue la kufanya.

Kutokana na wilaya hiyo kuwa na kiongozi bora na mchapakazi  ambaye anaguswa na changamoto za wananchi Desemba 30, 2025 Mkuu wa wilaya hiyo Shaka Hamdu Shaka akimbatana na kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya bila ya kuchelewa walienda kukagua maeneo yote yaliyoathirika na mvua hiyo ili kuona ukubwa wa changamoto hiyo ili Serikali iifanyie kazi na maisha ya wananchi yaendelee kama kawaida baada ya miundombinu iliyoharibiwa na mvua hiyo kurekebishwa.

Mvua hiyo iliyoambatana na upepo imesababisha athari kwa wakazi wa kata mbili za Dumila na Magole ikiwa ni pamoja na nyumba za makazi na biashara kuathiriwa  pamoja na baadhi ya miundombinu ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na baadhi ya taa za barabarani.

Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka aliyetembelea maeneo yalioathirika na mvua hizo alisema  serikali inafanya tathmini ya haraka ili kujua  athari zilizojitokeza.

DC Shaka alisema kuwa zaidi ya nyumba 120 zikiwemo za makazi pamoja na maghala  mawili ya kuhifadhia nafaka yamekumbwa na maafa hayo.

Aidha amesema kuwa mpaka sasa hakuna athari ya kibinadamu iliyojitokeza kutokana na upepo huo huku akitoa wito kwa wananchi wote wa kilosa kuchukua taadhari kipindi hiki cha mvua.

Ukaguzi wa maeneo yaliyoathiriwa na mvua hizo ukiendelea.

Mkuu wa wilaya hiyo  Shaka Hamdu Shaka pamoja na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wakikagua maeneo yaliyoathiriwa na mvua hizo.
Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka, akikagua maeneo hayo.
ukaguzi ukiendelea
Kazi ya ukaguzi ikiendelea
Kazi ikiendelea.

 

ASANTE EWURA KWA ELIMU YA UDHIBITI WA HUDUMA

ASANTE EWURA KWA ELIMU YA UDHIBITI WA HUDUMA

December 31, 2025 Add Comment

Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari mkoani Dodoma (DPC) Bw.Musa Yusuf,akitoa neno la shukrani kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) mara baada ya waandishi wa klabu hiyo kupatiwa mafunzo kuhusu udhibiti wa huduma za nishati na maji yaliyofanyika leo Disemba 31,2025 jijini Dodoma.

Na.Mwandishi Wetu-Dodoma

Wanachama wa Klabu ya Waandishi wa Habari mkoani Dodoma, leo 31 Desemba 2025, wameishukuru Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa kuwapa mafunzo kuhusu udhibiti wa huduma za nishati na maji.

Mwenyekiti wa klabu hiyo, Musa Yusuf, ameipongeza EWURA kwa hatua ya kutoa mafunzo hayo, akibainisha umuhimu wa mkataba wa huduma kwa wateja, uvunaji wa maji ya mvua, na utekelezaji wa mkakati wa kitaifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Amesisitiza kuwa elimu waliyoipata wataitumia kwa kuelimisha umma.

“Asanteni sana EWURA kwa elimu hii, hakika imetufungua macho. Wenzangu wote ni mashahidi. Tunaomba mafunzo kama haya yaendelee,” amesema Bw. Yusuf.

Kwa upande wake Kaimu Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kuelewa masuala yanayodhibitiwa na EWURA, kwani yanagusa huduma ambazo kila mwananchi kwa namna moja au nyingine anazitumia.

“Ninyi waandishi wa habari ni daraja kati ya EWURA na wananchi, tuendelee kushirikiana katika kuelimisha umma ili kila mtumiaji wa huduma tunazodhibiti ajue haki na wajibu wake”. Amesisitiza Mwakalosi.

 

   

RC TANGA AWATAKA WALIOPANGA KUCHOMA MATAIRI MKESHA WA MWAKA MPYA WASITHUBUTU

December 31, 2025 Add Comment




Na Oscar Assenga, TANGA


MKUU wa Mkoa wa Tanga Balozi,Dkt Batilda Burian amewataka wananchi wa mkoa wa Tanga ambao wamepanga kutumia matairi kuchoma moto barabarani kama njia ya kusheherekea sikuuu ya mwaka mpya wasithubutu kufanya hivyo.

Dkt Batilda aliyasema hayo leo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelekea mkesha wa mwaka mpya ambao unatarajiwa kufanyika kwenye viwanja vya Urithi Jijini Tanga ambapo alisema kutokana huo ni uharibifu wa miundombinu ya barabara na hatari kwa Taifa.

Alisema kwamba ndio maana Ofisi ya Mkoa huo kwa kushirikiana na Uongozi wa Halmashauri ya Jiji la Tanga na Mbunge wa Jimbo la Tanga wameamua kufanya shughuli ya wana Tanga kwenye uwanja wa Burudani wa Uhuru Park.

Alisema kwamba kutakuwa na sanaa mbalimbali taarabu na miziki mbalimbali ikiwemo mashindano ya kupika maandazi ,vitumbua na watakaokuwa mabingwa wa kupika sambusa lakini watachoma samaki na mbuzi watu watakula bila gharama yoyote ili kuendeleza umoja,amani na ukarimu wa wana Tanga.

Aidha alisema kwamba baada ya hapo usiku watawasha mafataki watakayowashwa na wataalamu maalumu ya viwango maalumu hivyo kuliko kuchoma matairi waje kwenye uwanja wa uhuru ili kuona burudani mbalimbali ikiwemo mafataki.

Mkuu huyo wa mkoa aliwataka wana Tanga kwenda uwanja wa Urithi ili kuweza kuomba dua kumshukuru Mungu kuuona mwaka na baada ya hapo mtu kurudi nyumbani ni eneo ambalo litakuwa salama.

.



RAIS SAMIA ATOA ZAWADI ZA MWAKA MPYA KWA WENYE UHITAJI, NAIBU WAZIRI UMMY AMUWAKILISHA

December 31, 2025 Add Comment


Na Mwandishi wetu- KILIMANJARO

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Watu wenye Ulemavu Mhe. Ummy Nderiananga ametoa wito kwa jamii kuwapenda, kuwajali na kuwahudumia makundi ya wenye mahitaji maalumu ili kukuza umoja na mshikamano katika Jamii.


Mhe. Nderiananga alisema hayo leo Disemba 31, 2025  akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa utaratibu wa utoaji zawadi za sikukuu mbalimbali kuelekea Sikukuu ya Mwaka Mpya wa 2026, zawadi hizo  zimeenda kwa watoto 190 wakiwemo wenye ulemavu na wasio na ulemavu wanaolelewa na Shirika la The Creator Share Foundation lililopo Kata ya Kirua, Wilaya ya Moshi Vijijini mkoani  Kilimanjaro.




Alisema, ndani ya siku 100 za uongozi wake ameendelea kuleta faraja, upendo, tumaini na umoja kwa watanzania huku akisema kuwa kitendo hicho ni ishara ya upendo mkubwa kwa wananchi bila kujali hali zao.


“Naomba nitumie fursa hii kuwatakia kheri ya sikukuu ya mwaka mpya  wa  2026 twende tukasherehekee kwa amani  na tukiwa na faraja kwa sababu Mhe. Rais ametukumbuka sisi ni watoto wake hivyo tudumishe upendo huu miongoni mwetu kila mmoja amuone mwenzake ni wa muhimu katika jamii,” alisema Mhe. Nderiananga.

Akitaja vitu alivyovikabidhi kwa watoto hao alisema, ni pamoja na Mchele kilo 100, Ngano kilo 50, Mbuzi wawili, sabuni, mafuta ya kupikia, madaftari, sukari kilo 25 na vinywaji



" Nitoe wito kwa jamii kuwa, kila mmoja ana wajibu wa kuwahudumia watoto na watu wenye mahitaji maalum, siyo tu kwa siku za sikukuu, bali kwa muda wote ili kuwapa faraja na huo ndio upendo tunaotakiwa kuwaonesha," aliongeza.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Moshi Bw. Godfrey Mnzava  alibainisha kuwa,  ili kuwa na ustawi wa maisha ya kijamii ni lazima kuwajali watu wenye uhitaji  ili waweze kukidhi mahitaji muhimu ya kila siku.


Naye,Diwani wa Viti Maalum Tarafa ya Vunjo Magharaibi ambaye pia ana mtoto mwenye ulemavu anayelelewa katika Shirika hilo Bi. Pamela Chuwa alipongea hatua hiyo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwafikia watu wenye ulemavu hatua inayowaganya kujisikia kuwa ni sehemu ya jamii.



“Mimi kama mama mwenye mtoto wa mahitaji maalum nimejisikia furaha kwa kupewa kipaumbele na tumefurahi sana Naibu Waziri Ummy kutufikia ukizingatia baadhi yetu tumefukuzwa katika familia  tukionekana kama kuzaa watoto wenye ulemavu ni mkosi na laana katika familia,” alipongeza Bi. Diwani huyo.



Vilevile Afisa Rasilimali Watu katika Shirika hilo Bi. Judith Shio mara  baada ya kupokea zawadi hizo alimshukuru Mhe. Rais Dkt.  Samia  Suluhu Hassan kwa moyo wa upendo na kuwajali watu wenye mahitaji Maalum huku akitoa wito kwa wadau mbalimbali kujitolea ili kuendelezwa moyo wa upendo na faraja kwa makundi hayo.



“Kwa niaba ya Shirika tunatanguliza shukrani zetu za dhati kwa upendo huu na mwaka huu tunauanza kipekee sana na watoto wamefurahi hivyo kwetu imekuwa faraja kubwa na imegusa jamii,” alishukuru Bi. Judith.


 Nao baadhi ya watoto wanaolelewa katika Shirika hilo wameishukuru Serikali kwa kuwakumbuka wakisema ujio huo kwao umekuwa ni historia na furaha kubwa ya kuuanza mwaka mpya kwa matumaini huku wakimshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa upendo huo wa the kuwashika mkono watoto wenye mahitaji maalum.


MWISHO

RUNALI YATATUA CHANGAMOTO YA MAJI KITUO CHA AFYA MARAMBO

December 31, 2025 Add Comment

 

Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Hassan Ngoma aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea katika hafla ya kukabidhi kisima cha maji kilichojengwa na RUNALI katika kituo cha afya Marambo kwa uongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Hassan Ngoma aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea katika hafla ya kukabidhi kisima cha maji kilichojengwa na RUNALI katika kituo cha afya Marambo kwa uongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Hassan Ngoma aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea akifungua maji wakati hafla ya kukabidhi kisima cha maji kilichojengwa na RUNALI katika kituo cha afya Marambo kwa uongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Nachingwea 


Na Fredy Mgunda, Nachingwea 

Chama Kikuu cha Ushirika RUNALI kimetatua changamoto ya upatikanaji wa maji katika Kituo cha Afya Marambo, changamoto iliyodumu kwa miaka mingi na kusababisha baadhi ya huduma kushindwa kutolewa ipasavyo katika kituo hicho.


Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kisima hicho cha maji, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika RUNALI, Odas Mpunga, alisema kuwa lengo kuu la mradi huo ni kusogeza huduma muhimu kwa jamii inayohudumiwa na Kituo cha Afya Marambo.


Mpunga alisema chama hicho kilipokea maombi ya kusaidia kutatua changamoto ya maji katika kituo hicho cha afya, hali iliyopelekea RUNALI kuchukua jukumu hilo kwa dhamira ya kuisaidia jamii.


Aliongeza kuwa kisima hicho kimekamilika na kuanza kutoa huduma, hivyo ni jukumu la wananchi pamoja na viongozi wa eneo hilo kuhakikisha wanakitunza ili kiwe mradi endelevu wenye manufaa ya muda mrefu.


Kwa upande wake, Meneja wa RUNALI, Jahida Hassan, alisema kuwa utekelezaji wa mradi huo ni sehemu ya kutimiza msingi wa saba (7) wa vyama vya ushirika, unaohimiza vyama hivyo kurudisha mchango kwa jamii inayowazunguka.


Jahida aliongeza kuwa kisima hicho ni kirefu na kina maji ya kutosha, hivyo kinapaswa kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa, hususan kuhudumia Kituo cha Afya Marambo.


Alisema kuwa RUNALI imetumia zaidi ya shilingi milioni 15 kuchimba kisima hicho hadi kukamilika kwake na kuanza kutoa huduma za maji katika kituo hicho cha afya.


Naye mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Hassan Ngoma, aliwataka wananchi na viongozi wa eneo hilo kuhakikisha wanauhudumia na kuutunza mradi huo ili uwe na manufaa ya kudumu kwa jamii na serikali kwa ujumla.


Ngoma alisema kuwa fedha nyingi zimewekezwa katika mradi huo wa kisima cha maji kwa lengo la kutatua kero ya maji kwa wagonjwa, wahudumu wa afya pamoja na wananchi wanaohudumiwa na kituo hicho, hivyo ni muhimu kulinda na kuutunza uwekezaji huo.


Aidha, aliwahimiza wananchi na wakulima ambao bado hawajajiunga na vyama vya ushirika kufanya hivyo kwa ajili ya maendeleo yao binafsi na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

SALAMU ZA MWAKA MPYA 2026 KUTOKA KWA MWENYEKITI WA TANZANIA BLOGGERS NETWORK (TBN)

December 31, 2025 Add Comment




Ndugu Wasomaji na Watumiaji wa Blogu Tanzania.


Tunapouaga mwaka 2025, nachukua fursa hii, kwa niaba ya wanachama wote wa Tanzania Bloggers Network (TBN), kuwapongeza Watanzania wenzangu kwa kumaliza mwaka huu "kibabe". 


Tumekuwa na mwaka wenye matukio mengi ya kihistoria, na ninyi wasomaji wetu mmekuwa wadau muhimu kwa kufuatilia habari, uchambuzi, na taarifa mbalimbali kupitia majukwaa yetu ya kidijitali.


Kuelekea Mwaka 2026: Makubwa Zaidi Yanakuja! Mwaka 2026 unakwenda kuwa mwaka wa mageuzi makubwa kwa TBN. Tunatarajia kuleta maudhui yenye ubunifu wa hali ya juu, habari za kina, na teknolojia ya kisasa zaidi katika kuhabarisha umma. Wanachama wetu wamejipanga kuwa daraja imara zaidi kati ya serikali na wananchi, tukihakikisha kila Mtanzania anapata habari sahihi na kwa wakati.


Ombi Langu kwa Watanzania: Tunapoingia 2026, rai yangu ni kuendelea kudumisha amani na utulivu. Tuepuke vurugu na migawanyiko, badala yake tujikite katika umoja wetu kama Taifa. Huu ni wakati wa kuungana kwa nguvu moja kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (Vision 2050). Lengo letu ni moja: kuhakikisha kila Mtanzania, kuanzia mjini hadi vijijini, anafaidi "keki ya taifa" na kupata maendeleo ya kweli.


Mwaka 2026 uwe mwaka wa neema, baraka, na mafanikio tele katika kazi na shughuli zenu za kila siku.


Heri ya Mwaka Mpya 2026!


Beda Msimbe

Mwenyekiti, Tanzania Bloggers Network (TBN).

MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA YAFUNGUA FURSA MPYA ZA AJIRA KWA WATANZANIA

December 31, 2025 Add Comment




Imeelezwa kuwa matumizi ya nishati safi ya kupikia yameendelea kufungua fursa nyingi za ajira kwa Watanzania, hususani katika uzalishaji wa mkaa mbadala na utengenezaji wa mashine za kuzalishia mkaa huo.

Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Nolasco Mlay amesema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea Taasisi ya Wazalendo Movement inayojishughulisha na utengenezaji wa mashine za kuzalisha mkaa mbadala pamoja na uzalishaji wa mkaa huo wilayani Mkuranga mkoani Pwani.

Bw. Mlay amesema kuwa taasisi nyingi zinazohudumia watu kuanzia 100 na kuendelea zimeanza kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia, jambo linaloongeza kwa kiasi kikubwa mahitaji ya mkaa mbadala na hivyo kuhitaji uzalishaji wa kasi zaidi.

“Niwapongeze kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kuzalisha mkaa mbadala pamoja na mitambo ya kutengenezea mkaa huo. Hii ni fursa kubwa kwa Watanzania kwani mahitaji ni makubwa, lakini ni muhimu kuhakikisha mkaa huu unaozalishwa ni wa ubora wa hali ya juu na unaodumu hata ukisafirishwa kwa umbali mrefu,” amesisitiza Bw. Mlay

Kwa upande wake, Mhandisi Mwandamizi kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Deusdedit Malulu amesisitiza umuhimu wa kushirikisha Shirika la Viwango Tanzania (TBS) katika utengenezaji wa mkaa mbadala ili kuhakikisha bidhaa zinakidhi viwango vinavyotakiwa.

Aidha, amewahimiza wazalishaji kujisajili kwenye mfumo wa NEST ili kupata fursa mbalimbali na kubainisha kuwa REA ina mpango wa kutoa fursa kwa wananchi katika utengenezaji wa mashine kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa vifaa vya kuzalisha mkaa mbadala.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Wazalendo Movement,Bw. Saidi Malema amesema kuwa taasisi hiyo, katika kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, imeanzisha kikundi cha nishati safi ya kupikia kinachojihusisha na uzalishaji wa mkaa mbadala unaotengenezwa kutokana na magunzi ya mahindi na nyasi kavu.

Amesema taasisi hiyo hutengeneza mashine za kuzalishia mkaa zinazotumia umeme na zisizotumia umeme.

Ameongeza kuwa taasisi hiyo pia imeanzisha kikundi cha Nishati Safi Sanaa Group, kinacholenga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia kupitia sanaa ya maigizo na nyimbo.

Amesema Taasisi ya Wazalendo Movement imefanikiwa kuuza mashine zake kwa wadau katika mikoa ya Tabora, Singida na Pwani. Aidha, imekuwa ikigawa mashine ndogondogo kwa wananchi wa vijiji vya Wilaya ya Mkuranga ambako umeme bado haujafika ili kuwahamasisha kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Katika ziara hiyo, Bw. Nolasco Mlay pia alitembelea kampuni ya Matima Investment inayojishughulisha na utengenezaji wa majiko ya kuchomea nyama yanayotumia gesi, kwa lengo la kujionea namna majiko hayo yanavyosaidia kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.






MABORESHO MAKUBWA HOSPITALI YA MJI HANDENI, SERIKALI YATOA BIL.1.2 KUWEKA VIFAA TIBA VYA KISASA

MABORESHO MAKUBWA HOSPITALI YA MJI HANDENI, SERIKALI YATOA BIL.1.2 KUWEKA VIFAA TIBA VYA KISASA

December 31, 2025 Add Comment

Na Mwandishi Wetu

Maboresho ya huduma za afya katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji Handeni yameanza kuleta matokeo chanya baada ya idadi ya wagonjwa wanaohudumiwa kwa siku kuongezeka kutoka wagonjwa 100 hadi kufikia 175.

Akizungumza kuhusu maboresho hayo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mji Handeni, Dkt.Hudi Muradi, amesema ongezeko hilo limetokana na kuboreshwa kwa miundombinu ya hospitali, upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa pamoja na kuimarika kwa utoaji wa huduma za uchunguzi na matibabu.

Ameeleza kuwa kwa sasa huduma zote muhimu za uchunguzi wa magonjwa zinapatikana hospitalini hapo, huku huduma za kibingwa zikiendelea kutolewa muda wote, hatua inayowapunguzia wananchi gharama na usumbufu wa kufuata huduma hizo nje ya halmashauri.

Aidha, amesema Serikali imetoa zaidi ya shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa, jambo lililochangia kwa kiasi kikubwa kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma na kuimarisha imani ya wananchi kwa hospitali hiyo.

Mganga Mkuu huyo ameongeza kuwa dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma bora na za uhakika kupitia utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, ambao unalenga kuweka usawa katika upatikanaji wa huduma za afya kati ya wananchi wenye kipato kikubwa na wale wa kipato cha chini.

Amesisitiza kuwa hospitali itaendelea kuboresha huduma ili kukidhi mahitaji ya wananchi na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha sekta ya afya nchini.

KUELEKEA MWAKA MPYA 2026,REA YAWASHIKA MKONO WAHITAJI

December 30, 2025 Add Comment




📍Hombolo - Dodoma


Kuelekea Mwaka Mpya 2026, Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imewagusa Watanzania wenye mahitaji mbalimbali kwa kutoa mkono wa faraja na kuwatakia heri ya mwaka Mpya ujao.


Zoezi la kuwapatia mahitaji walemavu limeongozwa na Bi. Judith Abdalah kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA mha. Hassan Saidy ambapo REA imetoa mahitaji mbalimbali kwa Kikundi cha Walemavu wa Ukoma waliopo Kata ya Hombolo jijini Dodoma. 

Akiwasilisha salamu za REA, Bi. Abdalah amewataka walemavu wa Ukoma kuishi kwa upendo na amani na kusisitiza kuwa, REA itaendelea kuwashika mkono kwa kuwapatia mahitaji mbalimbali ili wakue kiuchumi na kijamii. 


Halikadhalika, Swalehe Kibwana Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi Tawi la REA (TUGHE), amesema zoezi hilo la kuwafikia na kuwasaidia wahitaji mbalimbali ni endelevu na REA itaendelea kutoa mahitaji kwao hususan kwa walemavu wa ukoma waliopo Hombolo. 

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kikundi cha Wanawake na Samia mkoa wa Dodoma Bi. Fatuma Madudu ameishukuru REA kwa kufika Hombolo na kuwasaidia walemavu wa ukoma katika sehemu hiyokwa kuwapatia mahitaji mbalimbali. 

Naye, Katibu wa Walemavu Hombolo ametoa rai kwa wadau mbalimbali kujitokeza kuwashika mkono Walemavu wa ukoma na kuwapatia mahitaji mbalimbali ikiwemo chakula ili nao waweze kufurahia sikukuu ya kuukaribisha Mwaka Mpya wa 2026


Mwisho.i