Na Oscar Assenga,Tanga
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman ameanza jitihada za kuinusuru Klabu ya African Sports ambayo ipo hatarini kushuka daraja kufuatia matokeo mabaya katika Ligi ya Championship.
Rajab aliyasema hayo baada ya kukutana na wachezaji pamoja na viongozi wa klabu hiyo, ambapo alieleza kuwa hali ya timu si ya kuridhisha, akifananisha na mgonjwa aliye katika chumba cha mahututi.
Alibainisha kuwa kwa sasa African Sports inashika nafasi ya 15 kati ya timu 16, hali inayoiweka katika hatari kubwa ya kushuka daraja endapo haitafanya vizuri katika mechi zilizobaki.
Akizungumzia historia ya klabu hiyo, alisema ni moja ya timu zenye heshima kubwa nchini na mshindani wa jadi wa Coastal Union, hivyo ni muhimu kurejesha ushindani wa soka la Tanga.
Katika hatua ya kuokoa timu hiyo, Mwenyekiti huyo alitangaza kuchangia Shilingi milioni 20 ambazo tayari alikwisha kuziweka kwenye akauti, huku Mbunge wa Jimbo la Tanga akiahidi kutoa milioni tano na mdau mwingine kuahidi milioni 20, ikiwa ni sehemu ya kufikia lengo la kukusanya milioni 45 zinazohitajika kuiwezesha timu kumaliza msimu salama.
Alisema atahakikisha fedha hizo zinapatikana ili kutatua changamoto zinazoikabili klabu hiyo na kuwawezesha wachezaji kucheza kwa utulivu.
Aidha, aliwataka wachezaji kujituma katika mechi zilizobaki ili kuinusuru timu, akisisitiza kuwa wana dhamana ya kulinda heshima ya klabu hiyo.
Kwa upande mwingine, aliwashauri viongozi wa klabu kuweka mikakati ya muda mfupi na mrefu, ikiwemo kutovunja kambi mara baada ya msimu kumalizika ili kuboresha maandalizi ya msimu ujao.
Aliongeza kuwa mabadiliko ya mara kwa mara ya kikosi na maandalizi hafifu yamekuwa yakichangia kushuka kwa kiwango cha timu, na kusisitiza kuwa kwa mipango madhubuti wanaweza kurejea Ligi Kuu katika msimu ujao.































.jpeg)
.jpeg)




