HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

March 13, 2026 Add Comment

 KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI YAIPONGEZA TANESCO UTEKELEZAJI WA MRADI WA UMEME JUA KISHAPU



📌 Watembelea mradi kuona ufanisi wake

📌 Shilingi bilioni 118 zatumika kutekeleza mradi

📌 Watoa rai awamu ya pili kuanza kwa kasi


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa usimamizi na utekelezaji mzuri wa Mradi wa Uzalishaji Umeme kwa nguvu ya Jua wa Kishapu wenye uwezo wa Megawati 50 unaotekelezwa katika Mkoa wa Shinyanga.


Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgallu, mara baada ya Kamati kutembelea mradi huo tarehe 13 Machi, 2026 kwa lengo la kujionea maendeleo ya utekelezaji wake pamoja na ufanisi wa matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali.



Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mhe. Mgallu alisema mradi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya nishati nchini kutokana na matumizi ya teknolojia ya nishati jadidifu.


“Tumetembelea mradi huu wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia teknolojia ya jua na tunaona ni mapinduzi makubwa katika sekta ya nishati nchini. Hii ni hatua muhimu kwani kwa mara ya kwanza Tanzania inapata Megawati 50 za umeme kutoka kwenye nishati ya jua,” alisema Mhe. Mgallu.



Alisema Kamati imeridhishwa na namna fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo zimetumika ipasavyo na kufanikisha utekelezaji wa mradi huo kwa ufanisi.


“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, tumeridhishwa na matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya mradi huu. Tunaona wazi kuwa fedha hizo zimetumika vizuri katika utekelezaji wa mradi huu wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 118,” alieleza.



Aidha, alisema mradi huo tayari umeanza kuchangia Megawati 50 katika Mfumo wa Gridi ya Taifa, hatua inayochangia kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini pamoja na kuimarisha vyanzo mseto vya nishati.








“Utekelezaji wa mradi huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kunakuwa na vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme. Hii inaongeza uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme nchini,” alisema.


Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema mradi wa Kishapu unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme katika Gridi ya Taifa.






“Mradi huu una awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme kwenye Gridi ya Taifa. Awamu ya pili itahusisha uzalishaji wa Megawati 100 zaidi na kufanya jumla ya Megawati 150 kutoka katika mradi huu,” alisema Mhe. Ndejembi.


Kamati hiyo imetoa Rai kwa Wizara ya Nishati na TANESCO  inaendelea kuendelea na  mikakati ya kuanza utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo ili kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.

Benki ya Absa Tanzania Yalenga Kuwezesha Wasichana 5,000 Kupata Ujuzi wa AI Kupitia Mpango wa ElevateHer

Benki ya Absa Tanzania Yalenga Kuwezesha Wasichana 5,000 Kupata Ujuzi wa AI Kupitia Mpango wa ElevateHer

March 13, 2026 Add Comment
Benki ya Absa Tanzania, kwa ushirikiano na Microsoft na Women in Tech, imezindua rasmi Mpango wa ElevateHer AI nchini Tanzania, ambao unalenga kuwawezesha wasichana 5,000 wa Kitanzania kupata ujuzi na cheti cha Akili Mnemba (AI).

Mpango huu ni sehemu ya juhudi pana za kiafrika zinazolenga kutoa mafunzo kwa wanawake 50,000 barani Afrika ili waweze kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali unaokua kwa kasi.

Kupitia mpango wa ElevateHer, washiriki watapata fursa ya kujifunza mtandaoni kwa njia ya kujitegemea bila malipo, ambapo watapata maarifa ya msingi ya AI, matumizi ya AI katika biashara, na maendeleo ya taaluma katika mazingira ya kazi yanayoendeshwa na teknolojia ya AI. Mpango huu utakuwa wazi kwa mwaka mzima.

Ofisa Mkuu wa Uendeshaji wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Oscar Mwamfwagasi, amesema mpango huu unaakisi dhamira ya benki kuhakikisha wasichana wanapata ujuzi wa kidijitali unaohitajika kwa siku za usoni. “Artificial intelligence inabadilisha jinsi uchumi unavyofanya kazi na jinsi watu wanavyofanya kazi. 

Kupitia Mpango wa ElevateHer AI, Benki ya Absa Tanzania inalenga kuhakikisha wasichana wa Kitanzania wanapata ujuzi na kujiamini kushiriki kikamilifu katika uchumi wa kidijitali na kuchangia ubunifu na ukuaji.”

Juhudi hii inaendeleza michango ya Absa Tanzania ya kukuza ushiriki wa wanawake katika teknolojia, ikiwa ni pamoja na GirlCode Hackathon ya mwaka jana, ambapo wasichana wabunifu walikusanyika ili kutengeneza suluhisho za kiteknolojia.

Mpango wa ElevateHer unatoa njia tatu za kujifunza: AI kwa Wote, AI kwa Biashara, na AI kwa Ukuaji wa Kitaaluma, na kutoa fursa kwa washiriki kujenga maarifa ya vitendo na kutumia zana za AI katika safari zao za kitaaluma au za ujasiriamali.

Bi. Tiara Pathon, Mkurugenzi wa Ujuzi wa AI katika Microsoft Elevate, Microsoft Afrika Kusini, amesema upatikanaji wa ujuzi wa kidijitali kwa kila mmoja ni muhimu kwa ushiriki wa Afrika katika uchumi wa AI duniani. “Ukuaji wa uchumi jumuishi katika zama za AI unahitaji kujenga ujuzi kwa wingi katika masoko yanayokua. Kwa Afrika, hii inamaanisha kuwekeza kwa makusudi katika ujuzi wa kidijitali na AI kwa wanawake. Kupitia ushirikiano wetu na Absa na Women in Tech, mpango wa ElevateHer unawawezesha wanawake barani kote kupata ujuzi wa vitendo unaohitajika kazini na kuimarisha nafasi ya Afrika katika ajira za baadaye.”

Mpango huu pia unasaidiwa na Women in Tech Global, shirika linalojitolea kuwawezesha wanawake na wasichana milioni tano katika Sayansi, Teknolojia, Uhandisi, na Hisabati (STEM) kufikia mwaka 2030.

Wanawake wanaopenda kushiriki wanaweza kujisajili mtandaoni kupitia: https://elevateher-in-africa.org/⁠ 

UJUMBE WA KATIBU MKUU WA TRAMEPRO KATIKA KUADHIMISHA SIKU YA KIMATAIFA YA FIGO – 12 MACHI 2026

UJUMBE WA KATIBU MKUU WA TRAMEPRO KATIKA KUADHIMISHA SIKU YA KIMATAIFA YA FIGO – 12 MACHI 2026

March 13, 2026 Add Comment
Kwa niaba ya Shirika la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira (TRAMEPRO), napenda kuungana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na jumuiya ya kimataifa katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Figo. Siku hii ni muhimu katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa kulinda na kutunza afya ya figo.

Takwimu za kimataifa zinaonesha kuwa zaidi ya watu milioni 850 duniani wanaishi na aina fulani ya ugonjwa wa figo, huku takribani asilimia 10 ya watu wazima duniani wakiwa na dalili za ugonjwa huo. Aidha, mamilioni ya watu hulazimika kutegemea matibabu ya gharama kubwa kama dialysis au upandikizaji wa figo (kidney transplant) ili kuendelea kuishi.

Barani Afrika, tafiti zinaonesha kuwa kati ya asilimia 13 hadi 15 ya watu wazima wanaweza kuwa na dalili za ugonjwa wa figo. Nchini Tanzania, tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa takribani asilimia 10 hadi 12 ya watu wazima wanaweza kuwa katika hatari au tayari wana dalili za ugonjwa wa figo, huku wengi wakigundulika katika hatua za mwisho za ugonjwa.

Gharama za matibabu ya magonjwa ya figo ni kubwa sana. Mgonjwa anayehitaji dialysis hulazimika kufanya matibabu hayo mara mbili hadi tatu kwa wiki, ambapo gharama ya kikao kimoja inaweza kufikia wastani wa dola za Marekani 80 hadi 200. Hii ina maana kuwa kwa mwaka mmoja, gharama za matibabu zinaweza kufikia dola 10,000 hadi 25,000 au zaidi kwa mgonjwa mmoja.

Aidha, matibabu ya upandikizaji wa figo (kidney transplant) yanaweza kugharimu kati ya dola 15,000 hadi 30,000, bila kujumuisha gharama za dawa za kudhibiti kinga ya mwili ambazo mgonjwa hulazimika kutumia maisha yote.

Kutokana na hali hii, ni wazi kuwa kinga ni bora zaidi kuliko tiba, na jamii inapaswa kuhamasishwa kuchukua hatua za kulinda afya ya figo mapema.

Katika muktadha huu, tiba asilia ina nafasi muhimu katika kusaidia kuimarisha kinga ya mwili na afya kwa ujumla. Hata hivyo, bado kuna changamoto ya uhaba wa ushahidi wa kisayansi unaothibitisha kwa kina baadhi ya dawa na mbinu za tiba asilia. Kwa sababu hiyo, TRAMEPRO inaendelea kusisitiza umuhimu wa tafiti za kisayansi, uthibitishaji wa dawa za asili, na ushirikiano kati ya wataalamu wa afya na taasisi za utafiti.

Kwa sasa, nikiwa katika ziara ya kitaaluma mjini New Delhi, India, ninapata uzoefu na kujifunza kuhusu matibabu mtambuka (Integrative Medicine) katika taasisi mbalimbali ikiwemo Max Super Speciality Hospital pamoja na taasisi za tiba asilia chini ya mfumo wa AYUSH. Uzoefu huu unalenga kuimarisha uelewa na ushirikiano katika kuunganisha tiba asilia na tiba za kisasa kwa manufaa ya afya ya jamii.

TRAMEPRO itaendelea kushirikiana na taasisi za utafiti, hospitali, na wataalamu wa magonjwa ya figo ili kuendeleza tafiti, kutoa elimu kwa jamii, na kuhakikisha matumizi salama na yenye tija ya tiba asilia.

Katika maadhimisho haya, ninatoa wito kwa:

Watabibu wa tiba asilia kuzingatia viwango vya usalama, maadili ya kitaaluma na uthibitisho wa kisayansi katika huduma wanazotoa.

Wananchi kuchukua hatua za kinga dhidi ya magonjwa ya figo ikiwa ni pamoja na kudhibiti shinikizo la damu na kisukari, kunywa maji ya kutosha, kutumia dawa kwa usahihi, na kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara.

Serikali na taasisi za utafiti kuendelea kuwekeza katika tafiti za dawa za asili na kuimarisha mfumo wa huduma za afya jumuishi.

Kwa pamoja tunaweza kujenga mfumo wa afya unaounganisha hekima ya tiba asilia na sayansi ya tiba ya kisasa kwa manufaa ya binadamu na mazingira yetu.

Mungu aibariki Tanzania na awajalie wananchi wake afya njema.

Boniventura Mwalongo Katibu Mkuu – TRAMEPRONew Delhi, India 12 Machi 2026

TRA NA TAFFA ZAIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA USIMAMIZI WA MAADILI YA WATUMISHI

TRA NA TAFFA ZAIMARISHA USHIRIKIANO KATIKA USIMAMIZI WA MAADILI YA WATUMISHI

March 13, 2026 Add Comment

Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Ndani ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Shaibu Mmari, amesema ushirikiano kati ya TRA na mawakala wa forodha ni nguzo muhimu katika kuimarisha usimamizi wa maadili na uwajibikaji kwa watumishi wa Mamlaka.

Bw. Mmari amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa kikao cha mazungumzo kati ya TRA na viongozi wa Chama cha Waondoshaji na Wapelekaji Shehena Bandarini na Mipakani Tanzania (TAFFA), kilicholenga kuimarisha mahusiano ya kikazi na kubadilishana taarifa kuhusu uvunjifu wa maadili unaoweza kujitokeza katika shughuli za forodha.

Amesema kuwa ushirikiano wa karibu kati ya TRA na wadau wa sekta ya forodha ni muhimu katika kusaidia kubaini na kudhibiti vitendo vinavyokiuka maadili, pamoja na kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma.

“TRA ina jukumu la kukusanya mapato ya Serikali, kusimamia shughuli za forodha, na kuhakikisha sheria na taratibu za ushuru zinafuatwa ipasavyo. Ushirikiano na wadau kama TAFFA unatusaidia kuimarisha uadilifu na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu haya,” amesema Bw. Mmari.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa wadau kuendelea kushirikiana na TRA katika kutoa taarifa pale wanapoona dalili za uvunjifu wa maadili au vitendo vinavyoweza kuathiri uadilifu wa huduma za forodha.

Kwa upande wake, Mhasibu Mkuu wa TAFFA, Bw. Anthony Mukyamuzi, ameipongeza TRA kwa juhudi inazoendelea kufanya katika kuboresha mifumo ya forodha na utoaji wa huduma kwa wadau.

Amesema maboresho hayo yameongeza ufanisi katika shughuli za uondoshaji na uingizaji wa mizigo bandarini na mipakani, na kuimarisha mazingira ya biashara kwa wadau wa sekta ya usafirishaji na uondoshaji shehena.

Mwisho, pande hizo mbili zimeahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano katika kubadilishana taarifa, kuhamasisha maadili mema kwa watumishi, na kujenga mfumo wa uwajibikaji utakaosaidia kulinda uadilifu wa shughuli za forodha nchini.

 

RAMADHAN CHARITY PROGRAM 2026 YATOA SADAKA YA IFTAR GEREZA LA SINGIDA (M)

March 13, 2026 Add Comment
Ofisi ya BAKWATA Mkoa wa Singida, kupitia Sheikh wa Mkoa huo Issa Bin Nassoro, imezipongeza taasisi za Ramadhan Charity Programme2026, inayoongozwa na Ndugu Ahmed Misanga pamoja na Taasisi ya JAI Tanzania kwa kutoa sadaka katika Gereza la Manispaa ya Singida, misikiti pamoja na vituo vya watoto yatima.
Sheikh Issa amesema hayo leo wakati wa ziara yake ya kutembelea wafungwa katika Gereza la Manispaa ya Singida, ambapo pia walitoa sadaka ya Iftar kwa wafungwa ili waweze kupata futari pamoja na daku katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani. Sadaka hizo zimetolewa na taasisi za Ramadhan Charity Programme 2026 pamoja na JAI Tanzania.
Katika hotuba yake, Sheikh Issa aliwaomba watu mbalimbali katika jamii kuwajali watu wenye mahitaji na masikini, akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni jambo linalompendeza Mungu. Aliongeza kuwa hata mitume waliwahudumia na kuwasaidia watu masikini na wenye uhitaji.
Aidha, Sheikh wa Mkoa alitoa salamu kutoka kwa Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Dkt. Abubakar Zubeir bin Ally, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kuwajali watu wenye mahitaji maalum, wakiwemo wafungwa na makundi mengine yenye uhitaji katika jamii.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Ramadhan Charity Programme 2026, Ndugu Ahmed Misanga, amesema kuwa utoaji wa sadaka ya Iftar kwa watu wenye mahitaji ni utaratibu wao wa kila mwaka, hususan katika magereza na makundi mengine ya jamii. Amesema kuwa wamekuwa wakifanya shughuli hiyo kwa zaidi ya miaka mitano sasa.
Misanga alisisitiza kuwa watu waliopo magerezani wanahitaji huruma na faraja kutoka kwa jamii ili kuwapa moyo na kuwasaidia kumkaribia Mungu, ili wanaporudi uraiani wawe watu wema wenye hofu ya Mungu na mchango chanya kwa jamii.
Katika msaada huo, Ramadhan Charity Programme 2026 kwa kushirikiana na JAI Tanzania walitoa sadaka ya Iftar iliyojumuisha boksi la tende, sukari, tambi, mchele, ngano, juisi pamoja na taulo za kike kwa ajili ya wafungwa wanawake katika gereza hilo.
Naye Kaimu Mkuu wa Gereza la Wilaya ya Singida, Ndugu Amini Mjenza, amesema amefurahishwa na taasisi ya Ramadhan Charity chini ya uongozi wa Ahmed Misanga kwa kuwapatia sadaka ya Iftar, akieleza kuwa msaada huo utawasaidia sana wafungwa waliopo gerezani.
“Tutaitumia sadaka hii ya Iftar kama mlivyokusudia, na tunamuomba Mungu awalipie pale mlipotoa kwa ajili ya wafungwa wote, wanawake na wanaume,” amesema.
Katika tukio hilo, washiriki pia walipata nafasi ya kuliombea Taifa pamoja na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Taasisi ya Ramadhan Charity Programme 2026 imewataka Watanzania kutumia mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kuwa wamoja, kusaidiana na kufanya kazi kwa pamoja katika kuwasaidia wenye mahitaji katika jamii.
 
 

ADEM NA WADAU WA ELIMU WAAZIMIA KUIMARISHA UONGOZI WA SHULE NCHINI

March 12, 2026 Add Comment
Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) leo imepokea ujumbe wa wadau wa maendeleo kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Mastercard Foundation, Education for Sub-Saharan Africa (ESSA), Tanzania Education Network (TEN/MET), African Centre for School Leadership (ACSL), Teach United na Educate kwa ajili ya kujadili ushirikiano wa kuimarisha uongozi wa shule za sekondari nchini.

ADEM YAHITIMISHA MAFUNZO KWA MAAFISA ELIMU WA MIKOA 26 TANZANIA BARA

March 12, 2026 Add Comment
Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu - ADEM umeendesha mafunzo maalumu ya siku tano kwa Maafisa Elimu wa Mikoa 26 kutoka Tanzania Bara kuanzia tarehe 8-12 Machi, 2026 jijini Arusha.

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE NISHATI NA MADINI YARIDHISHWA NA MAENDELEO YA KIWANDA CHA NGUZO ZA ZEGE

March 12, 2026 Add Comment


📌Ni mradi wa kihistoria kutekelezwa chini ya Serikali ya awamu ya Sita 


📌 Yaipongeza TANESCO kwa usimamizi wa Ujenzi wa Kiwanda hiko


📌 Shilingi Bilioni 8 zawekezwa ujenzi wa Kiwanda hiko 


Na Mwandishi wetu, Tabora


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeridhishwa na Ujenzi wa Kiwanda cha Zege kinachomilikiwa na kampuni tanzu ya TANESCO ya  kuzalisha nguzo za zege  kilichopo katika Mkoa wa Tabora wakati wa ziara yao ya kikazi Mkoani humo tarehe 12 Machi, 2026.

Akizungumza baada ya ziara hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu ameeleza kuridhishwa na   hatua ya kukamilika kwa Kiwanda hicho kilichoanza uzalishaji  na kuwaelekeza Wizara ya Nishati  na TANESCO kukisimamia kiwanda hiko kiendelee kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kuzalisha faida.

"Kwa niaba ya Kamati tumeridhika na kazi kubwa iliyofanyika katika kiwanda hiki ambacho kimekamilika na uzalishaji umeanza, tunatoa rai kwa Wizara na TANESCO kuendelea kusimamia kiwanda hiki ili kiendelee kufanya kazi yake kwa ufanisi zaidi", alieleza Mhe. Mgallu

Alieleza kuwa uelekeo wa sasa ni kusambaza nguzo za zege hasa kwa maeneo yenye unyevu sambamba na maeneo yaliyo karibu na misitu pamoja na mikondo ya mito ya maji ambayo nguzo za miti huathirika kwa kiasi kikubwa haswa kwenye msimu wa mvua hivyo nguzo za zege zitakuwa msaada mkubwa katika mazingira kama hayo na  kuboresha upatikanaji wa huduma ya umeme.

“Kama mnavyofayahamu kwa sasa uelekeo ni kusambaza nguzo za zege badala ya nguzo za miti hasa katika maeneo ambayo yana asili ya unyevu, maeneo karibu na mito ya maji ama visiwa ambapo nguzo za miti huathiriwa na mazingira hayo”, aliongeza. 

Naye Mhe. Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hiko umekamilika mwaka huu na kuanza uzalishaji wake rasmi Februari, 2026 ambapo mpaka sasa wastani wa nguzo zinazozalishwa ni 80 hadi 120 kwa siku ambapo mpaka sasa gharama ya shilingi bilioni 6.4 imeshatumika katika hatua zote hadi uzalishaji ulipoanza ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.4 bado hazijalipwa kwa mkandarasi ambaye bado yupo kwenye kipindi cha uangalizi.


“Kiwanda hiki kilianza uzalishaji rasmi mwezi Februari mwaka huu ambapo kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha nguzo 80 hadi 120, mpaka sasa ujenzi wa kiwanda hiki hadi uzalishaji ulipoanza imetumia gharama ya shilingi bilioni 6.4 ambapo bado kuna billioni 1.6 bado haijalipwa kwa mkandarasi kwa kuwa yupo kwenye kipindi cha uangalizi”, aliongeza Mhe. Ndejembi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kuwa kukamilika kwa kiwanda hiko kunaenda kuleta mageuzi makubwa kwani nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo Shirika bado linaendelea kuikuza sekta  na kuwa na utoshelevu wa nguzo zenyewe kwa matumizi ya wananchi. 

“Baada ya kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda na kuanza uzalishaji ambapo kwa hali ilivyo ya matumizi ya nguzo za zege ni teknolojia ambayo bado inakuwa hivyo kama Shirika tutahakikisha tunaisimamia sekta hii ili kuendelea kuwapatia wateja wetu huduma ya umeme wa uhakika”, alisema Bw. Twange. 

Ziara hiyo ya kamati ya kudumu ya bunge ya nishati na madini inalenga kufanya ukaguzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Shirika katika maeneo mbalimbali nchini ili kujionea ufanisi wake.

KAMATI YA BUNGE YARIDHISHWA NA KASI YA UJENZI WA JENGO LA GHOROFA 10 CBE

KAMATI YA BUNGE YARIDHISHWA NA KASI YA UJENZI WA JENGO LA GHOROFA 10 CBE

March 12, 2026 Add Comment

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mhe. Deodatus Mwanyika (Mb), ameeleza kuridhishwa kwake na hatua ya ujenzi wa jengo la kisasa la Vipimo na Viwango katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) jijini Dar es Salaam.

Akizungumza Machi 12, 2026, Mhe. Mwanyika amebainisha kuwa mradi huo wa ghorofa 10 umefikia asilimia 93 ya utekelezaji wake, jambo linaloashiria usimamizi madhubuti na weledi katika ukamilishaji wa Jengo Jengo hilo ili kukidhi ongezeko la wanafunzi wanaodahiliwa kila mwaka.

Vilevile, Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa uongozi wa chuo kuendelea kutoa na kuimarisha elimu ya kati (middle-level education) katika fani za biashara hususani ujasiliamali kwa kuwa ni nyenzo adhimu kwa wahitimu wanaojiandaa kuingia kwenye soko la ajira binafsi na

Kutasaidia kuongeza hadhi ya chuo na kuchochea ari ya wanafunzi wengi zaidi kujiunga na taasisi hiyo.

Amesema kuwa uimara wa chuo unategemea ubora wa mafunzo unayoyatoa na uwezo wake wa kuzalisha wataalamu wenye ushindani katika soko la ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo (Mb), amefafanua kuwa mradi huo unatekelezwa kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2025/26 na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kubeba zaidi ya wanafunzi 4,000 kwa wakati mmoja.

Aidha amebainisha kuwa Jengo hilo la Vipimo na Viwango litakuwa kitovu cha mafunzo ya masoko na nyanja mbalimbali za kibiashara ambazo zinahitajika kwa kiasi kikubwa kulingana na mwelekeo wa sasa wa uchumi wa viwanda.

Naye Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Prof. Edda Lwoga, ameeleza kuwa mradi huo ulioanza Mei 25, 2023, umekuwa mhimili wa mabadiliko makubwa ya kitaaluma chuoni hapo. Alibainisha kuwa kukamilika kwa jengo hilo kutaongeza fursa za udahili kwa wanafunzi wengi wanaohitaji masomo ya biashara na ujasiriamali, ikiwemo kozi fupi ambazo zimekuwa na mahitaji makubwa kwa wadau wa sekta binafsi.