HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

REA YANADI MAFANIKIO YA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA KUSAMBAZA NISHATI VIJIJINI

April 02, 2026 Add Comment


Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeshiriki katika mahojiano maalum kujadili mafanikio na hatua za ujenzi wa Miradi ya Kusambaza Nishati maeneo ya Vijijini yaliyorushwa Mubashara kupitia Luninga ya ITV.


Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mha. Jones Olotu na Mkurugenzi wa Teknolojia za Nishati Jadidifu na Mbadala, Mha. Advera Mwijage wameshiriki katika mahojiano hayo Machi 2, 2026 Jijini Dar es Salaam ambapo walieleza bayana mafanikio na hatua mbalimbali zilizofikiwa za ujenzi wa Miradi ya Kusambaza Nishati Vijijini.

Awali akizungumza katika mahojiano hayo, Mha. Olotu amesema baada ya kuridhishwa na mafanikio ya REA, Serikali iliiongeza fedha na hivyo kuiwezesha kutanua wigo wa Miradi.


"Hadi sasa tumekamilisha Usambazaji umeme kwenye vijiji na tunaendelea na vitongoji. Tulianza na vijiji 506 na tukianza na maeneo ya kipaumbele ya Serikali ambayo yanatoa huduma ya moja kwa moja kwa wananchi ikiwemo makao makuu ya Wilaya, shule, vituo vya afya, visima vya maji," amesema Mha. Olotu.

Kwa upande wake Mha. Advera alisema REA inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ya Nishati Safi ya Kupikia ili kutimiza dhamira ya Serikali ya asilimia 80 ya wananchi wawe wanaotumia Nishati Safi ya Kupikia ifikapo Mwaka 2034. 

Mha. Advera alizungumzia namna ambavyo REA inawezesha miradi mbalimbali ikiwemo ya kuzalisha umeme kwa Nishati ya maji na jua.

"Kwa sasa hivi tunayo miradi mingi inayoendelea kwenye upande wa ujenzi wa gridi ndogo, tumekwishajenga zaidi ya gridi ndogo 70. Zinatumia Nishati ya maji na Nishati ya jua," amesema. 

Amesema kuwa REA vilevile inawezesha wananchi maeneo ya visiwani kupata Nishati ya Umeme kwa lengo la kujiletea maendeleo.

"Tunao Mradi mkubwa ambao unatekelezwa katika visiwa na tunafunga mifumo 20,000 ya Umeme jua kwa hatua za awali kwa bei ya ruzuku: tumemjali Kila mwananchi kupata Nishati hiyo kulingana na kipato chake," amesema Mha. Advera.

Mahojiano hayo yalitoa fursa kwa Jukwaa la Wahariri (TEF) na wananchi kuuliza maswali, kutoa maono na kupongeza hatua zilizofikiwa.



NISHATI SAFI YA FUNGUA MILANGO YA FURSA KWA WATENGENEZA MAUDHUI

April 02, 2026 Add Comment

 



Na Mwandishi Wetu, Mwanza


Watengeneza maudhui nchini wamehamasishwa kutumia ubunifu wao kujipatia kipato kupitia fursa zitokanazo na nishati safi ya kupikia, kwa kuelimisha jamii kupitia kazi zao zikiwemo video za elimu, vichekesho, hadithi na kampeni mbalimbali zitakazowafikia wananchi kwa urahisi.


Wito huo umetolewa Aprili 1, 2026 jijini Mwanza na Mhandisi Nishati kutoka Wizara ya Nishati, Benezeth Kabunduguru, wakati akizungumza katika mafunzo kwa watengeneza maudhui (content creators).


 Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, huku Wizara ya Nishati ikiwa miongoni mwa wawezeshaji wakuu.

Amesema mafunzo hayo yamelenga kuwasaidia watengeneza maudhui kuboresha kazi zao kwa kuzingatia mbinu za kubiasharisha maudhui mtandaoni, kujenga chapa binafsi pamoja na kuzingatia masuala ya hakimiliki.

Kabunduguru ameeleza kuwa watengeneza maudhui wana nafasi kubwa ya kubadilisha mtazamo wa jamii kupitia ubunifu wao, akisisitiza kuwa maudhui yenye ubora na mvuto yanaweza kununuliwa na kuwapatia kipato waandaaji wake, sambamba na kusambaza ujumbe muhimu kwa jamii.

Aidha, amesema Serikali imeweka mkakati wa kuhakikisha ifikapo mwaka 2034 angalau asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

 Amebainisha kuwa suluhisho za nishati hiyo tayari zipo na zinaendelea kuwafikia wananchi, huku changamoto kubwa ikiwa ni upatikanaji wa taarifa sahihi kwa watu wengi zaidi.

Kutokana na hali hiyo, amewataka watengeneza maudhui kuchangamkia fursa hiyo kwa kuandaa kazi zitakazolenga kuelimisha kuhusu faida za nishati safi ya kupikia na madhara ya matumizi ya nishati zisizo safi.

Amesisitiza kuwa utoaji wa taarifa sahihi kwa jamii utachochea mabadiliko chanya yatakayoboresha maisha ya wananchi na kulinda afya za Watanzania.


&&&

BoT YASALIA NA RIBA YA MSINGI YA ASILIMIA 5.75 KWA TAHADHARI YA HATARI ZA KIMATAIFA

April 02, 2026 Add Comment

 Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imeamua kuendelea kubakiza kiwango chake cha riba ya msingi ya ukopeshaji (benchmark lending rate) katika asilimia 5.75 kwa robo ya pili ya mwaka huu, ikionesha tahadhari kufuatia kuongezeka kwa sintofahamu katika uchumi wa dunia.


Uamuzi huo ulifikiwa katika kikao cha hivi karibuni cha Kamati ya Sera ya Fedha (MPC), ambapo watunga sera walitathmini hatari zinazotokana na mazingira ya kimataifa dhidi ya uimara wa uchumi wa ndani.

Akizungumza kuhusu uamuzi huo, Naibu Gavana wa BoT, Dkt. Yamungu Kayandabila, alisema hatua hiyo inalenga kusawazisha kati ya kukuza uchumi na kudhibiti mfumuko wa bei.

“Haikuwa uamuzi rahisi,” alisema, akieleza kuwa mvutano wa kisiasa unaoendelea katika Mashariki ya Kati umeanza kuathiri mwenendo wa masoko ya dunia.

Alifafanua kuwa mvutano huo umevuruga minyororo ya usambazaji wa bidhaa na kuchangia kupanda kwa bei, hususan mafuta ambayo sasa yamevuka dola za Marekani 100 kwa pipa, juu ya makadirio ya awali.

Katika hatua nyingine, MPC ilitangaza kupunguza wigo wa riba (interest rate corridor) unaozunguka kiwango cha CBR kutoka pointi 200 hadi 150 za msingi (basis points), hatua inayoweka kiwango cha riba ya siku saba kati ya benki katika viwango vya asilimia 4.25 hadi 7.25.

Kwa mujibu wa Dkt. Kayandabila, hatua hiyo inalenga kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa sera ya fedha, huku ikidumisha uthabiti wa bei na kusaidia ukuaji wa uchumi.

Licha ya changamoto za kimataifa, BoT imeeleza kuwa uchumi wa ndani unaendelea kuonesha uimara.

Katika robo ya kwanza ya mwaka, uchumi ulikua kwa asilimia 6.2 Tanzania Bara na asilimia 6.7 Zanzibar, ukichochewa na sekta za ujenzi, kilimo, utalii na huduma za kifedha.

Kwa robo ya pili, ukuaji unatarajiwa kufikia asilimia 6.1 kwa Tanzania Bara na asilimia 6.6 Zanzibar, ingawa hatari za nje zinaweza kuathiri mwenendo huo endapo zitaongezeka.

Kwa upande wa mfumuko wa bei, umeendelea kubaki ndani ya lengo la BoT la asilimia tatu hadi tano. Kwa wastani, ulikuwa asilimia 3.3 Tanzania Bara na asilimia 4.5 Zanzibar, hali iliyochangiwa na utulivu wa bei za chakula pamoja na kiwango cha ubadilishaji fedha.

Hata hivyo, Benki Kuu imeonya kuwa ongezeko la gharama za nishati na usafirishaji linaweza kuongeza shinikizo la mfumuko wa bei katika miezi ijayo.

Katika sekta ya benki, hali imeendelea kuwa imara ambapo kiwango cha mikopo chechefu kimeshuka hadi asilimia 2.9, chini ya kiwango kinachokubalika kisheria, huku benki zikiendelea kuwa na mtaji wa kutosha na ukwasi wa kuridhisha.

Kwa upande wa sekta ya nje, nakisi ya akaunti ya sasa imepungua hadi asilimia 2.2 ya Pato la Taifa (GDP), ikichangiwa na kuongezeka kwa mauzo ya nje ya dhahabu, mazao ya kilimo na huduma za utalii.

Zanzibar nayo imeendelea kufanya vizuri, ikirekodi ziada ya akaunti ya sasa kutokana na mapato ya utalii.

Aidha, akiba ya fedha za kigeni imefikia zaidi ya dola za Marekani bilioni 6.2, kiwango kinachoweza kugharamia uagizaji wa bidhaa kwa karibu miezi mitano, juu ya viwango vya kikanda.

Kwa upande wa mapato ya serikali, makusanyo ya kodi yamevuka malengo kutokana na kuimarika kwa usimamizi na utii wa walipakodi, huku matumizi ya serikali yakiendelea kubaki ndani ya mipaka ya rasilimali zilizopo.

Hata hivyo, MPC imeonya kuwa bado kuna hatari zinazoikabili uchumi.

“Tishio kubwa kwa matarajio ya uchumi ni mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati. Endapo utaongezeka, unaweza kuongeza mfumuko wa bei na kupunguza kasi ya ukuaji wa uchumi duniani na nchini,” alisisitiza Dkt. Kayandabila. 








BODI MPYA TFS YAANZA KAZI RASMI, YAPOKEA MPANGO WA BIASHARA 2026/2027

April 02, 2026 Add Comment


Morogoro

Bodi ya Tano ya Ushauri ya Wizara kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeanza rasmi majukumu yake kwa kufanya kikao cha 47 cha Bodi, ambacho pia ni kikao cha kwanza cha bodi hiyo mpya.

Kikao hicho kimefunguliwa leo Aprili 2, 2026 mkoani Morogoro na Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Luteni Mstaafu Chiku Abdallah Sumbu Gallawa, katika Ukumbi wa Kituo cha Mbegu Bora za Miche ya Miti cha TFS.

Kabla ya kikao hicho, wajumbe walifanya vikao vya kamati kuanzia Machi 31 hadi Aprili 1, 2026, kujadili masuala mbalimbali ya kiutendaji ya wakala.

Pamoja na mambo mengine, Bodi ilipokea na kujadili Mpango wa Biashara wa TFS kwa mwaka wa fedha 2026/2027, sambamba na taarifa mbalimbali za utekelezaji wa majukumu ya taasisi.

Kuanza kwa kikao hicho kunafuatia uzinduzi wa Bodi hiyo uliofanywa Februari 13, 2026 jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji.











RAIS DKT. MWINYI AZINDUA MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2026, ASISITIZA AMANI, UZALENDO NA UWAJIBIKAJI

April 02, 2026 Add Comment


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewataka Watanzania kulinda, kuimarisha na kudumisha Muungano wa Tanzania, amani, utulivu na umoja wa kitaifa kama msingi wa maendeleo endelevu.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 02 Aprili , 2026 wakati wa uzinduzi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 uliofanyika Uwanja wa Gombani, Pemba.

Aidha, Rais Mwinyi amesema taasisi zote nchini na wananchi kwa ujumla wana wajibu wa kuheshimu utu, haki, usawa na utawala wa sheria ili kuendeleza mshikamano wa Taifa.

Ameeleza kuwa Mwenge wa Uhuru unaendelea kuwa chombo muhimu cha kuhamasisha uzalendo, uwajibikaji na mapambano dhidi ya maadui wa maendeleo wakiwemo umasikini, ujinga na maradhi.

Vilevile, amewahimiza Watanzania kupinga ubaguzi wa aina yoyote na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kupambana na rushwa, dawa za kulevya na magonjwa kama UKIMWI na malaria.

Halikadhalika, Rais Dkt. Mwinyi amebainisha kuwa Serikali inaendelea kuimarisha huduma za afya, kudhibiti matumizi ya dawa za kulevya na kupunguza maambukizi ya malaria, huku akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa wadau wote katika kufanikisha maendeleo ya Taifa.

Mwenge wa Uhuru umeanza mbio zake katika Mkoa wa Kusini Pemba na unatarajiwa kufikia kilele chake Oktoba 14, 2026 mkoani Rukwa, ukiwa na kaulimbiu: “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane.”