HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

NLD WAMSIMAMISHA MHAGAMA KUWANIA UBUNGE JIMBO LA PERAMIHO

January 29, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu ,RUVUMA.


 


CHAMA cha National League For Democracy (NLD) kimempitisha Mhagama Hamisi Yusufu kuwania Ubunge Jimbo la Peramiho Mkoani Ruvuma ambayo ataipeperusha Bendera ya chama hicho katika uchaguzi wa mdogo kufuatia Kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo Jenista Mhagama.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa,Katibu wa NLD Doyo Hassan Doyo ambapo aliwaambia kwamba siku hiyo ni muhimu kwa wananchi wa Jimbo la Peramiho kufanya maamuzi ya kiongozi wanayemtaka .

Alisema kwamba kiongozi ambaye anaweza kuwaletea maendeleo wananchi wa Jimbo hilo ni mgombea wao kutokana na uongozi uliopita kwa miaka mingi umeshindwa kuwapa maendeleo na mabadiliko katika Jimbo hilo.


Katibu huyo aliwataka wananchi hao kutokufanya makosa katika uchaguzi huo wa marudio kutokana na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo kufariki dunia hivyo aliwataka kumchagua mgombea anayetokana na NLD ili aweze kuwapa maendeleo makubwa.

Katika uchaguzi huo Mhagama Hamis Yusuf wa NLD atachuana na wagombea wengine akiwemo Yusuf Rashid Rai wa Chama cha AAFP,Abdallah Boniface Ngonyani wa Chama cha Makini,Hanifa Sembe Mohamed wa Chama cha UMD,Beatrice Omari Muya wa UPDP,Mapunda wa Chama cha DP,Dastan Frolian Pili wa CCK,Morice Thomas Nkongo wa TLP na Mtemi Pachoto wa UDP.


 


Mwisho.

TANZANIA NA SERBIA ZAJADILI USHIRIKIANO WA AJIRA NA MAENDELEO YA RASILIMALI WATU

TANZANIA NA SERBIA ZAJADILI USHIRIKIANO WA AJIRA NA MAENDELEO YA RASILIMALI WATU

January 29, 2026 Add Comment

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu akizungumza na Waziri wa Kazi, Ajira na Ustawi wa Jamii wa Serbia, Mhe. Milica Djurdjevic, walipo kutana katika kikao cha pembeni (side meeting) kujadili ushirikiano wa masuala ya Kazi na Ajira, Jijini Riyadh, Saudi Arabia.

.....

Tanzania na Jamhuri ya Serbia zimejadili fursa za kuimarisha ushirikiano wa masuala ya kazi, ajira na maendeleo ya rasilimali watu, hususan katika Sekta ya Ujenzi na maeneo mengine muhimu ya kiuchumi.

Hayo yamebainishwa wakati wa kikao cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu na Waziri wa Kazi, Ajira na Ustawi wa Jamii wa Serbia, Mhe. Milica Djurdjevic Stamenkovski, walipokutana katika Mkutano wa Mawaziri wa Kazi Duniani (Global Labour Market Conference) uliofanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Akizungumza katika kikao hicho, Waziri Sangu amesema Serikali ya Tanzania imeendelea kufanya mageuzi makubwa yanayolenga kukuza ajira zenye staha, kuongeza ujuzi kwa nguvu kazi na kupanua fursa za ajira kwa wananchi.

Vilevile, Mhe. Sangu alitumia fursa hiyo kueleza wataalamu na uwezo wa wafanyakazi katika nyanja mbalimbali zikiwemo uhandisi, afya, elimu, uhasibu, utawala wa biashara, uchumi, sheria, utalii na ukarimu, kilimo, TEHAMA, biashara ya kilimo na usindikaji wa mazao, anga na usafiri, ufundi mitambo, usafirishaji huduma za majumbani pamoja na fani nyingine nyingi, hivyo amesema Watanzania wanatambulika kwa bidii, unyenyekevu, maadili mema ya kazi na mtazamo chanya kazini.

Kadhalika, Waziri Sangu amemwalika Waziri wa Kazi, Ajira na Ustawi wa Jamii wa Serbia, Mhe. Milica Djurdjevic Stamenkovski kutembelea Tanzania ili kujionea mikakati inayotekelezwa na Serikali katika kuimarisha soko la ajira pamoja na sera za ajira. Pia, amemkaribisha kutembelea vivutio vya utalii nchi ya Tanzania.

Kwa upande wake, Waziri wa Kazi, Ajira na Ustawi wa Jamii wa Serbia, Mhe. Milica Djurdjevic Stamenkovski, amesema nchi ya Serbia ipo katika mchakato wa kufungua ubalozi nchini Tanzania ili kuendelea kukuza ushirikiano kati ya mataifa hayo. Pia alimwalika Waziri Sangu kutembelea nchi ya Serbia ili kujadili kuhusu masuala ya kazi na ajira ikiwemo fursa za ajira zilizopo nchini humo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu akisalimiana na Waziri wa Kazi, Ajira na Ustawi wa Jamii wa Serbia, Mhe. Milica Djurdjevic, walipo kutana katika kikao cha pembeni (side meeting) kujadili ushirikiano wa masuala ya Kazi na Ajira, Jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu akizungumza na Waziri wa Kazi, Ajira na Ustawi wa Jamii wa Serbia, Mhe. Milica Djurdjevic, walipo kutana katika kikao cha pembeni (side meeting) kujadili ushirikiano wa masuala ya Kazi na Ajira, Jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Baadhi ya Wajumbe kutoka Tanzania wakifuatilia maelezo ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu alipokutana na kuzungumza na Waziri wa Kazi, Ajira na Ustawi wa Jamii wa Serbia, Mhe. Milica Djurdjevic, katika kikao cha pembeni (side meeting) kujadili ushirikiano wa masuala ya Kazi na Ajira, Jijini Riyadh, Saudi Arabia.

TADB yaadhimisha miaka 10 kwa mafanikio makubwa ya kifedha

January 29, 2026 Add Comment
Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imeendelea kuimarisha uwezo wake wa kifedha baada ya mali zake kuongezeka na kufikia shilingi trilioni 1.3, hatua inayotokana na mafanikio ya utoaji mikopo katika mnyororo wa thamani wa sekta ya kilimo.
DK.JAFO AIBANA WIZARA YA UJENZI KUTENGA BAJETI YA BARABARA YA LAMI MLANDIZI-MZENGA-BOGA

DK.JAFO AIBANA WIZARA YA UJENZI KUTENGA BAJETI YA BARABARA YA LAMI MLANDIZI-MZENGA-BOGA

January 29, 2026 Add Comment

Mbunge wa Jimbo la  Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akiuliza swali la nyongeza leo Januari 29,2026 bungeni jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna, Dodoma

Mbunge wa Jimbo la  Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo, amehoji mpango wa Serikali wa kutenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Mlandizi–Mzenga–Maneromango kwa kiwango cha lami, akisisitiza kuwa ni barabara muhimu kwa shughuli za kiuchumi na kijamii.

Akiuliza swali la nyongeza Bungeni, Dkt. Jafo amesema barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 70.2 inaanzia Mlandizi kupitia Mzenga hadi Maneromango, na kwamba tayari upembuzi yakinifu umekamilika.

Ameeleza kuwa kwa sasa mkandarasi ameanza kazi katika kipande cha Mzenga chenye urefu wa mita 300, hali iliyomfanya kuihoji Serikali kuhusu mpango wake wa kuongeza fedha katika bajeti ya mwaka huu ili kufungua kipande cha Mlandizi hadi Mzenga.

“Nini mpango wa Serikali katika bajeti ya mwaka huu kuongeza fedha ili kuhakikisha barabara hii muhimu inaanza kujengwa kuanzia Mlandizi hadi Mzenga?” amehoji Dkt. Jafo.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, amesema Serikali tayari imeonesha nia ya dhati ya kuijenga barabara hiyo, akibainisha kuwa kutokana na ukubwa na umuhimu wake, lazima ijengwe kwa kiwango cha lami.

Ameongeza kuwa Serikali itaendelea kutenga na kuongeza fedha kadri zinavyopatikana, ili kuhakikisha ujenzi wa barabara hiyo unaendelea hadi kukamilika kwa kiwango kilichokusudiwa.

BILIONI 151 RUWASA MWANZA KUNG’ARISHA HUDUMA YA MAJI VIJIJINI

January 29, 2026 Add Comment


Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) mkoa wa Mwanza unaendelea na utekelezaji wa miradi 71 inayoendelea kujengwa katika wilaya mbalimbali ambapo ikikamilika inatarajiwa kupandisha wastani wa huduma ya maji vijijini mkoani humo kutoka wastani wa asilimia 73 ya sasa hadi kufikia asilimia 88 hivyo kuendelea kuimarisha uchumi wa mtu mmoja na jamii kwa ujumla.

Miradi hiyo inatekelezwa kwa gharama ya shilingi bilioni 151 kutoka vyanzo mbalimbali vya fedha ikiwemo Serikali Kuu, Programu ya lipa kwa matokeo (PforR) na Mfuko wa Taifa wa Maji.

Hayo yameelezwa na Meneja wa RUWASA mkoa wa Mwanza Mha. Godfrey Sanga wakati wa ziara ya timu ya Menejimenti ya taasisi hiyo kutoka Makao Makuu inayofanya tathimini ya uendeshaji wa huduma ya maji vijijini inayotolewa na Vyombo vya Utoaji Huduma ya Maji Ngazi ya Jamii (CBWSOs) kote nchini.

Mha. Sanga alisema miradi hiyo ipo katika hatua tofauti za ujenzi ikiwemo mradi wa maji wa Ukiriguru wenye vijiji 19, na Ilujamahate-Buhingo utakaohudumia vijiji 16, na kwamba itakapokamilika itainua huduma kufikia vijiji vingi zaidi mkoani humo na kuendelea kukamilisha dhamira ya serikali ya kumtua mama wa kijijini ndoo kichwani.
Katika siku ya kwanza mkoani Mwanza, timu ya Menejimenti ya ukaguzi na tathimini ya kazi za CBWSO ilitembelea Chombo cha Nyamwaki kilichopo wilayani Magu na Miswaso kilichopo wilaya ya Kwimba ambapo zoezi hilo litaendelea katika wilaya za Misungwi na Segerema.





RC IRINGA ASISITIZA WANANCHI KUWALINDA WAKANDARASI NA VIFAA VYA UJENZI

January 29, 2026 Add Comment


*📌Mradi wa bilioni 32.3 kusambaza umeme kwenye vitongoji 214 vya mkoa wa Iringa*


*📌Mkandarasi M/s Silo Power atakiwa kumaliza kazi kwa wakati*


*📌Wateja 7,500 wataunganishiwa huduma ya umeme*


*📌Asema umeme ni maendeleo, uchumi, huduma na biashara*


📍Iringa


Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe. Kheri James, amewataka wananchi wa Mkoa huo kutoa ushirikiano kwa Wakandarasi wa miradi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), ikiwemo kulinda miundombinu na vifaa vya ujenzi ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati na iweze kuleta tija na kuchochea maendeleo nchini. 

RC James amebainisha hayo leo Januari 29, 2026 wakati Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ikimtambulisha rasmi mkandarasi; kampuni ya M/s Silo Power itakayotekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme kwenye vitongoji 214 vya mkoa wa Iringa  ambapo mradi huo unatarajiwa kutekelezwa katika kipindi cha miaka mitatu, kuanzia sasa.

Vile vile, RC James amesema mkoa wa Iringa unamahitaji makubwa ya umeme kutokana na kuongezeka kwa viwanda vidogo na vya kati na kwamba hiyo ni fursa kwa Wananchi kukuza uchumi na maendeleo kwa ujumla.


“Namshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wanna Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa kipaumbele kwenye Sekta ya Nishati hususan katika Sekta ya nishati; nikitoa mfano kwenye usambazaji wa umeme kwenye vijiji, Iringa vijiji vyote 360 vilishaunganishwa na huduma ya umeme na sasa tunapokea Mradi wenye thamani ya shilingi bilioni 32.3 na  wananchi zaidi ya 7,500 watanufaika”. Amesema RC James. 

Katika hatua nyingine, RC James amemtaka na kumsisitiza mkandarasi wa mradi huo kuhakikisha anatoa kipaumbele cha ajira kwa wazawa wanaozunguka eneo la mradi ili wananchi hao pia waweze kunufaika na miradi hiyo na kuchochea shughuli za kijamii na kiuchumi mkoani Iringa. 

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, Bw. Frank Mugogo amesema kuwa vitongoji 1,458 tayari vimefikiwa na huduma ya umeme mkoani Iringa na ambavyo havina umeme ni vitongoji 382. Ameongeza kuwa REA itaendelea kusimamia miradi yote inayotekelezwa nchini kwa weledi ili iweze kukamilika kwa wakati na kuwaomba vingozi wa Serikali ya kijiji na wananchi walioshiriki katika kikao hicho kutoa ushirikiano kwa wakandarasi ili miradi hiyo ikamilike kwa wakati. 

Kwa upande wake,  Mha. Mmbalo Msuya kutoka kampuni ya M/s Silo Power amesema kampuni yao, imejipanga ili kukamilisha Mradi wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 214 vya mkoa wa Iringa kwa wakati na kuongeza kuwa maelekezo ya RC James ya kutoa ajira kwa wazawa yatapewa kipaumbele ili wananchi wanaozunguka miradi hiyo waweze kunufaika. 


Mwisho

REA WAMTAMBULISHA MKANDARASI ATAKAYEFIKISHA UMEME VITONGOJI 175 MTWARW

January 29, 2026 Add Comment


Katika kutekeleza kauli mbiu ya “Vitongojini kama Mjini”, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wamefika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mtwara kumtambulisha mkandarasi wa atakaesambaza umeme kwenye vitongoji 175 mkoa wa Mtwara.


Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Kanali Patrick Sawala amewataka REA kumsimamia vema mkandarasi ili aweze kukamilisha kwa wakati huku akiwahakikishia ushirikiano.

“Nahitaji Ofisi ya Mkoa ipatiwe mpango kazi wa mkandarasi ili tuweze kufuatilia mwenendo wa utekezwaji wa mradi. Kwa ile miradi iliyokamilika, REA toeni taarifa ili izinduliwe wananchi waweze kuanza kuitumia. Umeme ni uchumi, unachochea ajira na uwekezaji.” Alieleza Kanali Sawala

Meneja Usimamizi  wa miradi REA, Mha. Deogratius Nagu ameeleza kuwa mradi huo wa kusambaza umeme kwa ngazi ya vitongoji kwa Mkoa wa Mtwara itatekelezwa kwa miaka mitatu kuanzia Januari 2026 mpaka Januari 2029 ukitarajiwa kunufaisha wananchi 5,646

Kwa upande wake Meneja wa kampuni ya Dieynem inayotekeleza mradi huo, Mha. Novatus Lyimo ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwapa kipaumbele wakandarasi wazawa huku akiahidi kutekeleza maradi ndani ya kipindi tarajiwa.



TANZANIA NA OMAN KUIMARISHA USHIRIKIANO MASUALA YA KAZI NA AJIRA

TANZANIA NA OMAN KUIMARISHA USHIRIKIANO MASUALA YA KAZI NA AJIRA

January 28, 2026 Add Comment

Tanzania na Oman zimeendelea kuonyesha dhamira ya kuendelea kuimarisha ushirikiano katika masuala ya kazi na ajira ili kuongeza ajira zenye staha, kulinda haki za wafanyakazi na kukuza uchumi wa mataifa yote mawili.

Hayo yamebainishwa wakati wa kikao cha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Clement Sangu na Waziri wa Kazi wa Oman, Dkt. Mahad bin Said bin Ali Baawain walipokutana katika Mkutano wa Mawaziri wa Kazi Duniani (Global Labour Market Conference) uliofanyika Jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Aidha, katika kikao hicho Waziri Sangu alielezea umuhimu wa kukamilishwa na kutiwa saini kwa Hati ya Makubaliano ya Ushirikiano wa masuala ya Kazi na Ajira (MoU) kati ya nchi hizo mbili, ili kuweka mfumo rasmi na endelevu wa usimamizi wa masuala ya ajira, ulinzi wa haki za wafanyakazi na utatuzi wa changamoto za kiutendaji zinazojitokeza.

Vilevile, Waziri Sangu ameishukuru Serikali ya Oman kwa kuendelea kutoa fursa za ajira kwa Watanzania katika sekta mbalimbali. Pia, amesema idadi ya Watanzania wanaofanya kazi nchini Oman imeendelea kuongezeka , jambo linaloonesha kuimarika kwa mahusiano ya ajira kati ya mataifa hayo mawili.

Kwa upande mwingine, nchi hizo zimekubaliana kuendeleza ushirikiano kwa kuendelea kupanua wigo wa ajira zenye staha, kulinda haki za wafanyakazi na kuimarisha mahusiano ya kiuchumi na kijamii kati ya mataifa yetu mawili.

MUCOHAS,WIZARA YA AFYA,MUHAS ZATEKELEZA MRADI WA AFUA JUMUISHI KUBORESHA HUDUMA RAFIKI KWA WAGONJWA WA VVU NA WATUMIAJI DAWA ZA KULEVYA

January 28, 2026 Add Comment


Chuo cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUCOHAS) kwa kushirikiana Wizara ya Afya na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS), zinaendelea kutekeleza mradi wa Afua Jumuishi (Total Facility Approach) unaolenga kuondoa unyanyapaa na ubaguzi miongoni mwa watoa huduma za afya kwa wagonjwa wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (VVU) pamoja na watumiaji wa dawa za kulevya. 

Kikao cha siku tano kinafanyika mkoani Morogoro, kikilenga kuandaa nyenzo za  kufundishia ili kuwajengea uwezo walimu  na wanafunzi wa vyuo vya kati, juu ya unyanyapaa na ubaguzi.

Akizungumza kuhusu utekelezaji wa mradi huo, Mkuu wa Chuo cha MUCOHAS, Dkt. Bonny Betson, amesema mradi huo umejikita katika kuboresha uelewa, mitazamo na ujuzi wa watoa huduma ili kuhakikisha huduma za afya zinazotolewa ni jumuishi, rafiki na zenye kuzingatia utu wa kila mteja.

“Huu ni mwaka wa tatu tangu tulipoanza mradi huu, na kwa sasa tumetekeleza awamu ya kwanza hapa MUCOHAS kwa wanafunzi na walimu, baada ya hapo tunapitia mtaala mdogo tulioutengeneza mahsusi kwa ajili ya kuendesha mafunzo haya,” amesema Dkt. Betson.

Ameongeza kuwa kabla ya kuandaa mtaala huo, utafiti wa awali ulifanyika kwa wanafunzi na walimu waliopata mafunzo ili kubaini mahitaji halisi na changamoto zilizopo katika utoaji wa huduma na matokeo ya utafiti huo yalitumika kutengeneza mtaala unaolenga kutumika pia katika vyuo vingine vya afya nchini, ikiwa ni hatua muhimu ya kupunguza unyanyapaa na ubaguzi miongoni mwa watoa huduma za afya.

Utekelezaji wa mradi wa Afua Jumuishi unaendana na malengo ya Serikali kupitia Wizara ya Afya ya kuboresha huduma za afya kwa wananchi, hususan katika kuondoa unyanyapaa unaodhorotesha upatikanaji  na utumiaji wa huduma kwa watu wanaoishi na VVU Pamoja na watumiaji wa madawa ya kulevya.


Hili litachangia katika mikakati ya Serikali iliyowekwa  ili kutokomeza maambukizi ya VVU ifikapo mwaka 2030, kwa kuimarisha utoaji wa huduma rafiki, jumuishi na zenye usawa kwa wote.