HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

KAMATI YA BUNGE YAITAKA WMA KUHAKIKI MITA ZA UMEME KWA MUJIBU WA SHERIA

KAMATI YA BUNGE YAITAKA WMA KUHAKIKI MITA ZA UMEME KWA MUJIBU WA SHERIA

March 15, 2026 Add Comment

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeiagiza Wakala wa Vipimo (WMA) kuhakikisha mita za umeme zinahakikiwa kikamilifu kabla ya kufungwa kwa ajili ya matumizi, kwa kuzingatia sheria zilizopo ili kulinda haki za watumiaji.

Aidha, Kamati hiyo imeipongeza WMA kwa jitihada za uhakiki na ukaguzi wa vipimo mbalimbali, ikiwemo mita za maji, huku ikiitaka Wakala hiyo kuendelea kusimamia kwa ukaribu vipimo katika sekta ya ujenzi ili kupunguza malalamiko ya wananchi yanayotokana na bidhaa hizo.

Hayo yameelezwa leo Machi 14, 2026, na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Deodatus Mwanyika, wakati wa ziara ya kikazi katika Kituo cha WMA cha Uhakiki wa Vipimo Misugusugu mkoani Pwani kwa lengo la kukagua miradi ya maendeleo na kujionea shughuli za uhakiki wa vipimo zinavyotekelezwa kituoni hapo.

Akizungumza katika ziara hiyo, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, aliihakikishia Kamati kuwa wizara itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa.

Alisisitiza kuwa azma ya Serikali ni kuhakikisha WMA inasimamia matumizi ya vipimo sahihi katika uzalishaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali, pamoja na Uhakiki wa mita za umeme na maji, ili kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson Simon, akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, alibainisha kuwa uhakiki wa vipimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa mkoa huo. Alieleza kuwa kwa sasa Mkoa wa Pwani una jumla ya viwanda 1,688, vikiwemo viwanda vikubwa 199 na vidogo sana 1,017, hivyo uhakiki wa usahihi wa Vipimo ni nyenzo muhimu katika kuvutia uwekezaji zaidi.

Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Bw. Alban Kihulla, alisema kuwa ukaguzi na uhakiki wa vipimo una nafasi kubwa katika kuhakikisha haki na usawa baina ya pande mbili zinazofanya biashara.

Pia, aliwahimiza wananchi kuhakikisha wanatumia vipimo vilivyohakikiwa, huku akiwasihi watoa huduma kuzingatia uadilifu kwa kutoa huduma kupitia vipimo sahihi ili kuleta usawa na kuhakikisha bidhaa zinazonunuliwa zinaendana na thamani halisi ya fedha.

MTENDAJI MKUU ADEM AFUNGUA KIKAO KAZI CHA CHAMA CHA KUTETEA HAKI ZA WALIMU

March 14, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefungua kikao kazi cha Chama cha Kulinda na Kutetea Haki za Walimu (CHAKUHAWATA) kinachofanyika jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wadau mbalimbali wa sekta ya elimu ili kuimarisha uongozi, utawala bora na udhibiti wa ubora wa elimu nchini.

KAMATI YA BUNGE YAKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA KAMPASI YA CHUO KIKUU MZUMBE TANGA

March 14, 2026 Add Comment
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Mhe. Husna Juma Sekiboko (Mb) akiongoza Wajumbe wa Kamati hiyo kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi ya Tanga, unaotekelezwa kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET).

GRIDI YA TAIFA YA MAJI ITACHOCHEA MAENDELEO KWA KASI

March 14, 2026 Add Comment




Na: Dk. Reubeni Lumbagala, Tanga


Maji ni kimiminika muhimu kwa maisha na uhai wa viumbei. Maji hutumika kuanzia asubuhi, mchana, jioni hadi usiku. Hutumika kwa matumizi ya nyumbani kama kupikia, kufulia na kuogea. Hutumika katika shughuli za kiuchumi kama viwandani, mashambani, migodini, masokoni kutaja kwa uchache. Maji hayana mbadala, panapohitajika maji, hakuna namna nyingine bali kuyatafuta na kukidhi haja yake. Hakuna siku inaweka kupitia bila kutumia maji. Maji ni uhai na maji ni maisha. Binadamu anahitaji maji kila siku. 

Tanzania imebarikiwa kuwa na vyanzo vingi vya maji. Mathalani; bahari, maziwa, mito, mabonde. Vyanzo hivi husaidia kupata maji kwa matumizi mbalimbali. Kutokana na ongezeko kubwa la watu nchini na shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, mahitaji ya huduma ya maji pia yameongezeka sana. Wizara ya Maji yenye dhamana ya usambazaji wa huduma ya maji katika maneno mbalimbali nchini ina wajibu mkubwa wa kuhakikisha maji yanawafikia wahitaji ili kuchochea shughuli mbalimbali za kimaendeleo nchini.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ni mdau mkubwa wa sekta ya maji. Anatambua umuhimu wa maji kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Kutokana na hilo, amekuwa akiongeza fedha katika bajeti ya Wizara ya Maji kila mwaka, jambo linalosaidia utekelezaji wa miradi ya maji ambayo inakwenda kutatua changamoto za maji katika maeneo mbalimbali nchini na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwani maji ni kiungo muhimu sana. Mathalani kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Bajeti ya Wizara ya Maji ilikuwa Sh. 1.01 trilioni ambapo katika fedha hizo, Sh. 943.22 bilioni zilikuwa ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Hii inaonyesha namna Wizara ya Maji ilivyojizatiti kutatua kero za wananchi kwa kupeleka fedha nyingi kwenda kwenye miradi ya maji.

Rais Dk. Samia pia ameelekeza Wizara ya Maji kufanikisha mradi kabambe wa Gridi ya Taifa ya Maji kama ilivyo Gridi ya Taifa ya Umeme inayosimamiwa na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha nchi inakuwa na uhakika wa maji kwa shughuli mbalimbali za maendeleo. Kwa nchi yetu yenye utajiri wa vyanzo vya maji, mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji ni suala muhimu hasa kipindi hiki ambacho dunia inapitia changamoto ya mabadiliko ya tabia ya nchi. 

Gridi ya Taifa ya Maji itakusanya maji kutoka vyanzo mbalimbali vya maji nchini kwa matumizi ya kimaendeleo. Kilimo ambacho ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu kinahitaji sana raslimalimaji kwa ajili ya umwagiliaji. Kilimo cha kutegemea maji ya mvua pekee hakitoi uhakika kwa kupata mavuno kwani endapo kutatokea ukame au uhaba wa mvua, mazao yatanyauka na kufa kabisa. Uwepo wa maji ya kutosha unatoa uhakika wa kuvuna, kupata chakula na fedha baada ya kuuza mazao ndani na nje ya nchi. Maji yanawezesha pia uzalishaji wa umeme wa nguvu za maji (Hydo-Electric Power - HEP).

Maji ya uhakika yanatoa uhakika wa uendelevu wa shughuli za ufugaji. Wanyama na ndege watapata maji ya kunywa na majosho ya kuogeshea wanyama. Uvuvi unategemea uwepo wa maji, ukosefu wa maji unarudisha nyuma shughuli za uvuvi ambazo ni muhimu kwa uchumi wetu. Maeneo ya biashara kama masokoni vilevile wanahitaji maji kwa ufanisi wa shughuli zao. Wachimbaji wa madini na wahandisi wa ujenzi nao wanahitaji maji katika shughuli zao. Maeneo ya taasisi kama shule na hospitali, nao bila maji maisha hayaendi.


Katika kufanyia kazi maelekezo ya Rais Dk. Samia kuhusiana na mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji, hivi karibuni Waziri wa Maji Jumaa Aweso, Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Mwajuma Waziri pamoja na watendaji wa sekta ya Maji walifanya ziara katika Jimbo la Shan Dong Kaskazini mwa China kuona na kujifunza namna walivyofanikiwa kuviunganisha vyanzo vya mito na maziwa katika Gridi ya Taifa ya Maji kutoka Kaskazini hadi Kusini mwa China.


Kimsingi, mpango uliopo nchini ni kuviunganisha vyanzo mbalimbali vya maji nchini kama vile Maziwa ya Viktoria, Tanganyika na Nyasa pamoja na mito ya Rufiji, Kagera, Kiwira, Wami, Pangani, Ruvu na Ruvuma na vyanzo vingine ili kuwa na uhakika wa maji kwa maendeleo ya sekta mbalimbali. Katika kutekelekeza miradi huu, ni vyema wananchi tukawa mabalozi wazuri wa kutunza vyanzo vya maji vilivyopo na kutunza mazingira kwa ujumla. Tukumbuke maji hayana mbadala, kila mtu anahitaji maji. Kwa hakika, mafanikio ya kuwa na Gridi ya Taifa ya Maji ni uhakika wa kupata maendeleo endelevu. Tuunge mkono mradi huu muhimu kwa manufaa ya kizazi cha leo na kijacho. Tafakari.


Maoni: 0620 800462.

MZIKI WA DKT.AGNES GIDNA WAIKUNA KAMATI YA BUNGE

March 14, 2026 Add Comment




Kamati ya kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imempongeza Afisa Uhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Dkt. Agnes Gidna kutokana na umahiri, umakini, kujiamini na uchambuzi wake mkubwa wa masuala ya mambo kale na jiolojia.


Wakiongozwa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Timotheo Mnzava wabunge hao wametoa pongezi hizo baada ya kukagua na kupata maelezo ya mradi wa makumbusho ya _Urithi Geopark Museum._ 


Wabunge wamepongeza kazi kubwa iliyofanywa na serikali ya Tanzania na China ambapo hawakusita kuelezea hisia zao kutokana na mtaalam huyo  alivyowakonga nyoyo kwa kuelezea historia kuhusa kutokea kwa kreta ya Ngorongoro, milpuko ya volkano, maumbile ya dunia, chanzo cha binadamu wa kale na masuala mengine.


Kamati ya Bunge imeielekeza wizara ya Maliasili na Utalii kuitumia makumbusho hiyo kama bidhaa ya utalii na kitovu cha elimu kwa vijana wa kitanzania na kimataifa.


Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt.Ashatu Kijaji aliwashukuru wabunge kwa pongezi hizo na kuwahakikishia kuwa wizara yake itasimamia kwa karibu maendeleo ya Urithi Geopark Museum.


Dkt.Agnes Gidna, mtaalam wa makumbusho, mambo kale na urithi wa utamaduni amekuwa kiungo muhimu  katika makumbusho hayo kutokana na umahiri wake wa kitaaluma na kitaalam kuihadithia yaliyopo kwenye makumbusho hiyo.

MIRADI SEKTA YA MAFUTA NA GESI ASILIA IKAMILIKE KWA WAKATI-DKT.MATARAGIO

March 14, 2026 Add Comment


📌*Asisitiza kuhusu uwekezaji wa vitalu vipya vya Mafuta na Gesi Asilia*


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, ameitaka Menejimenti ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuhakikisha kuwa miradi ya mafuta na gesi asilia inayoendelea nchini inatekelezwa na kukamilika kwa wakati ili iweze kuendelea kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Dkt. Mataragio ametoa maelekezo hayo leo wakati alipokutana na menejimenti ya TPDC  kwa lengo la kujadili fursa zilizopo katika sekta ya Mafuta  na Gesi Asilia, changamoto pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha sekta.

Aidha, Dkt. Mataragio ameiagiza TPDC, kuongeza vitalu vipya vya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia.


“Ni muhimu TPDC ikaendelea kupanua maeneo ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia kama mnavyofahamu rasilimali hii ni muhimu katika kutoa uhakika wa nishati nchini mfano kwenye  uzalishaji wa umeme na kukuza uchumi wa viwanda." Amesisitiza Dkt.Mataragio


Kwa upande wake, Kamishna wa Petroli, Goodluck Shirima, amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia ili kuongeza matumizi yake katika sekta mbalimbali ikiwemo majumbani, viwandani na katika uzalishaji wa umeme.



Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutenga na kuandaa maeneo kwa ajili ya ushiriki wa sekta binafsi kwenye miradi ya usambazaji wa gesi, akibainisha kuwa miradi hiyo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati (flagship projects) inayolenga kuongeza matumizi ya gesi asilia.


Naye,  Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame amesema Shirika hilo litaendelea kutekeleza maagizo  yanayotolewa na viongozi wa Wizara kwa lengo la kuzidi kuiimarisha sekta ya Mafuta na Gesi Asilia.


“TPDC itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha miradi ya gesi asilia na mafuta inatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya Watanzania wote."  Amesema Makame


Ziara ya Dkt. Mataragio TPDC ni muendelezo wa ziara zake katika Taasisi zinazosimamia Sekta ya Mafuta na Gesi Asilia ikiwa ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Nishati kuimarisha usimamizi wa taasisi zake ili ziendelee kutekeleza majukumu kwa ufanisi lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wananufaika  na rasilimali zilizopo nchini.

VIJIJI VINNE MBULU VYAANZA KUNUFAIKA NA MRADI WA MAJI WA BILIONI 41

March 13, 2026 Add Comment

Wananchi na wakazi wa Hydom wilayani Mbulu mkoa wa Manyara wamemshukuru Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia Wizara ya Maji kupitia RUWASA kutekeleza mradi mkubwa wa Majisafi ya bomba wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 41 na tayari vijiji vinne vimeshaanza kunufaika na mradi huo.

Wametoa pongezi hizo wakati wa ziara ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira alipotembelea na kukagua mradi huo ikiongozwa na Mwemyekiti wake Mhe. Jackson Kiswaga (Mb) katika eneo la Hydom lilipo tangi kubwa la ujazo wa lita 2,000,000 la mradi huo.

Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA Mha. Wolta Kirita aliieleza Kamati hiyo kuwa tayari wananchi zaidi 800 wameshasajiliwa na kupatiwa kadi za malipo kabla ya matumizi kwani mradi huo unaenda sambamba na ufungaji wa dira za maji za malipo ya kabla, ambapo mwananchi anaweza kuchota maji kwenye kituo muda wowote anapokuwa anahitaji huduma hiyo.

Mkurugenzi Mkuu Kirita alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika Novemba 2027.

Kwa mujibu wa Meneja wa RUWASA mkoa wa Manyara Mha. James Kionaumela alisema mradi huo umeshaanza kutoa huduma katika vijiji vinne na ukikamilika utahudumia zaidi ya wakazi 100,000 wa eneo hilo.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbulu Mhe. Michael Semindu akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga alisema kwa sasa wananchi wa wilaya hiyo wanapata maji kwa saa 12 kwa siku huku akiipongeza RUWASA kwa kazi nzuri katika kutekeleza mradi huo.








KAIMU KAMISHNA WA UHIFADHI TAWA AFUNGUA KIKAO KAZI CHA MAANDALIZI YA BAJETI YA TAWA

KAIMU KAMISHNA WA UHIFADHI TAWA AFUNGUA KIKAO KAZI CHA MAANDALIZI YA BAJETI YA TAWA

March 13, 2026 Add Comment

Na. Joyce Ndunguru, Dodoma.

Kaimu Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Mlage Yussuf Kabange amefungua rasmi kikao kazi cha maandalizi ya bajeti ya TAWA kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi kilichofanyika Machi 13,2026, Jijini Dodoma, Kamishna Kabange amesema Bajeti ya mwaka 2026/27 ni ya kipekee kwa kuzingatia kuwa ni bajeti ya kwanza katika kuchangia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025 pamoja na Dira ya maendeleo ya Taifa 2050.

“Pia bajeti hii imezingatia kutafsiri Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan wakati wa kuzindua Bunge la 13, Mkakati wa kuongeza mapato wa TAWA na ni bajeti ya kwanza tangu Bodi ya Nne ya Wakurugenzi ya TAWA iteuliwe”, amesema Kamishna Kabange.

Kamishna Kabange ameongeza kuwa katika bajeti hii TAWA itajielekeza katika vipaumbele mbalimbali ikiwemo kuimarisha ulinzi na usimamizi wa Rasilimali wanyamapori na malikale.

Pia, Kuimarisha shughuli za utalii pamoja na kuongeza idadi ya watalii kwa kuboresha miundombinu ya utalii pamoja na kuongeza vyanzo vipya vya mapato.

Kadhalika, Utatuzi wa migogoro ya mipaka na udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu pamoja na Kuimarisha mazingira ya utendaji kazi kwa watumishi na uwezo wa Mamlaka katika kutoa huduma.

Vilevile , Kamishna Kabange amewapongeza Makamanda na Askari ambao wamekuwa mstari wa mbele kusimamia utekelezaji wa malengo ya Mamlaka. Aidha, amewaelekeza Makamanda wa vituo kuhakikisha Usimamizi madhubuti wa vitendea kazi yakiwemo magari.

Aidha, Kamishna Kabange amewaelekeza Makamanda kuendelea na utangazaji wa vivutio vya utalii pamoja na kubuni mazao mapya ya utalii.

“Nitoe rai kwenu kuendelea kuwa wabunifu na kutangaza maeneo mnayoyasimamia,” amesema Kamishna Kabange 

Sambamba na hilo, Kamishna Kabange amewaelekeza Makamanda kuendelea kusimamia askari kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kwa kuzingatia haki, sheria na miongozo iliyowekwa.

Kikao kazi cha maandalizi ya bajeti kimehudhuriwa na viongozi wa TAWA kwa ngazi ya Makao Makuu, Kanda na Vituo.

KAMATI YA BUNGE YARIDHISHWA NA MABORESHO YA BANDARI YA TANGA

March 13, 2026 Add Comment





Na Oscar Assenga,TANGA

Kamati ya kudumu ya Bunge ya miundombinu leo imefanya ziara ya kutembelea Bandari ya Tanga huku ikiridhinshwa na uboreshaji wa miundombinu katika Bandari ya Tanga hatua inayoonesha mabadiliko ya kiutendaji ikiwemo ongezeko la shehena za mizigo.

Hayo yalisemwa leo na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Profesa Joyce Ndalichako wakati wa ziara hiyo katika Bandari ya Tanga ambapo alisema maono ya Serikali yameleta mapinduzi katika Bandari ya Tanga na wao kama wasimamizi wataendelea kuisimamia Serikali katika utekelezaji wa mradi huo



Uboresho huo wa Bandari ya Tanga umepelekea kuvuka lengo la upokeaji wa shehena za mizigo kutoka mataifa mbalimbali kutoka tani 137,000 mwezi Oktoba hadi kufikia tani zaidi ya 200,000 mwezi Novemba mwaka 2025.



Alisema kutokana na maboresho hayo wana kila sababu ya kuipongeza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Raisi Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uboreshaji wa Bandari ya Tanga hatua inayochagiza kuinua uchumi wa mkoa wa Tanga kwa kiasi kikubwa.




Profesa Ndalichako alisema kwamba uwekezaji huo wa shilingi bilioni 429.1 uliofanywa na Serikali katika Bandari ya Tanga umewezesha uchimbwaji wa kina na ujenzi wa gati hatua iliyoiongezea ufanisi wa utendaji na hivyo kuwezesha meli kubwa kutia nanga na kurahisisha shughuli za upakiaji na upakuaji wa mizigo.

Aliongeza Serikali ina maono ya kuunganisha Bandari na reli ambapo mpango uliopo ni kujenga reli ya kisasa ya SGR kutoka Tanga hadi Musoma hatua itakayochochea maendeleo ya mkoa wa Tanga na kuzalisha ajira kwa vijana.



Kamati ya kudumu ya Bunge ya miundombinu imeipongeza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Raisi Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uboreshaji wa Bandari ya Tanga hatua inayochagiza kuinua uchumi wa mkoa wa Tanga kwa kiasi kikubwa.

Uwekezaji wa shilingi bilioni 429.1 uliofanywa na Serikali katika Bandari ya Tanga zimewezesha uchimbwaji wa kina na ujenzi wa gati na hatimaye kuleta ufanisi wa utendaji katika Bandari hiyo hatua inayowezesha Meli kubwa kutia nanga na kurahisusha shughuli za upakiaji na upakuaji wa mizigo.



Aidha katika hatua nyengine Profesa Ndalichako amesema Serikali ina maono ya kuunganisha Bandari na reli ambapo mpango uliopo ni kujenga reli ya kisasa ya SGR kutoka Tanga hadi Musoma hatua itakayochagiza maendeleo ya mkoa wa Tanga hususani kwa vijana kupata ajira.



Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile, alisema Serikali inaendelea na mpango wa kuunganisha bandari hiyo na mtandao wa reli wa kilomita 248 (Tanga–Mruazi–Ruvu) na hatimaye kufika Arusha.



Alisema pamoja na kuwa na reli ya SGR kupitia Minjingu na Engaruka hadi Musoma itakuwa kiunganishi muhimu cha kiuchumi.

Naye kwa upande wake ,Meneja wa Bandari ya Tanga, Salehe Mbega alisema maboresho hayo yameongeza kina cha maji kufikia mita 12 hali inayoruhusu meli kubwa zenye urefu wa hadi mita 200 kutia nanga gatini tofauti na hapo awali.