HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WAZIRI MAKONDA AAHIDI BILIONI MOJA KWA WAANDISHI WA MITANDAONI

January 13, 2026 Add Comment

 

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Makonda, ameahidi kuomba Serikali kutenga kiasi cha shilingi bilioni moja hadi bilioni mbili kwa ajili ya kuwawezesha waandishi wa habari za mitandaoni nchini kukopeshwa fedha zitakazowawezesha kununua vifaa vya kisasa vya kufanyia kazi, kwa lengo la kuboresha ubora wa maudhui na kuitangaza Tanzania kimataifa.

Waziri Makonda ametoa ahadi hiyo Januari 13, 2026, wakati akizungumza na watumishi wa Wizara hiyo katika Ofisi za Wizara zilizopo Mji wa Serikali Mtumba, sambamba na hafla ya makabidhiano ya Ofisi kati yake na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo, Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi.

Amesema Serikali inatambua mchango mkubwa wa vijana waliojiajiri kupitia vyombo vya habari vya mtandaoni, hususan televisheni za mtandaoni (Online TV) na mitandao ya kijamii, hivyo kuna haja ya kuwawezesha ili wafanye kazi zao kwa viwango vinavyokubalika kimataifa.

“Mungu akituwezesha, vijana wengi wamejiajiri kwenye habari, hasa kupitia televisheni za mtandaoni na mitandao ya kijamii. Tutaomba mamlaka husika, na mtakumbuka Mheshimiwa Rais anapenda sana mitandao ya kijamii, hata alipoingia madarakani alihakikisha vijana wanapata ajira,” amesema Mhe. Makonda.

Ameongeza kuwa atamwomba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutenga fedha hizo ili ziwe mikopo kwa waandishi wa mitandaoni, akisisitiza kuwa lengo ni kuboresha ubora wa kazi zao.

“Nitaenda kumlilia Dkt. Samia ili atupatie fedha kiasi cha shilingi bilioni moja hadi bilioni mbili ili tuwakopeshe vijana wa mitandaoni wawe na vifaa vyao wenyewe. Lengo ni kuhakikisha hawarekodi kwa simu pekee, bali wanatumia kamera za kisasa, wanakuwa na kompyuta bora na kutengeneza maudhui ambayo dunia itayaona na kuiona Tanzania katika uzuri wake,” ameeleza.

Katika hatua nyingine, Waziri Makonda amesema Wizara hiyo ina mpango wa kuanzisha Kitengo maalum cha Mawasiliano ya Lugha za Kimataifa kitakachohusika na kuandaa na kusambaza habari za matukio muhimu ya kitaifa kwa vyombo vya habari vya kimataifa.


RAIS SAMIA :MAHAKAMA HURU NI NGUZO YA UTAWALA BORA NA MAENDELEO YA TAIFA

January 13, 2026 Add Comment

 


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema hakuna taifa linaloweza kufikia maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi wake bila kuwepo kwa usimamizi mzuri wa haki unaosimamiwa na Mahakama huru, yenye uwezo na uadilifu.

Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jumanne Januari 13, 2025 jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA), unaoongozwa na kauli mbiu “Jukumu la Mahakama Huru Katika Utoaji Haki.”

Dkt. Samia amesema uwepo wa Mahakama huru ni nguzo muhimu ya utawala bora na ni msingi wa upatikanaji wa haki kwa wananchi, akisisitiza kuwa uhuru wa Mahakama lazima uende sambamba na uwajibikaji, uadilifu, nidhamu, utii wa sheria na uzalendo kwa taifa.

“Serikali itaendelea kuulinda na kuheshimu uhuru wa Mahakama, lakini uhuru huo hauna budi kuenda sambamba na uwajibikaji na maadili ya kazi."

Aidha, Rais Samia amesema Dira ya Taifa ya 2025–2050 imejengwa juu ya misingi ya utawala bora, amani, usalama na utulivu, akibainisha kuwa mhimili wa Mahakama una nafasi muhimu katika kujenga taifa lenye haki na ustawi wa kudumu.

Mkutano huo wa TMJA unawakutanisha majaji na mahakimu kutoka maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kujadili masuala ya uboreshaji wa utoaji haki na kuimarisha utendaji wa Mahakama.









RAIS DKT. SAMIA AWAAPISHA VIONGOZI MBALIMBALI ALIOWATEUA IKULU CHAMWINO

RAIS DKT. SAMIA AWAAPISHA VIONGOZI MBALIMBALI ALIOWATEUA IKULU CHAMWINO

January 13, 2026 Add Comment



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Profesa Palamagamba John Adan Kabudi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Ikulu (Kazi Maalum) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Paul Christian Makonda kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Patrobas Paschal Katambi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Dennis Lazaro Londo kuwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Ayoub Mohamed Mahmoud kuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Dkt. Richard Stanslaus Muyungi kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhandisi Zena Ahmed Said kuwa Balozi kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhandisi Cyprian John Luhemeja kuwa Balozi kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Ndugu Waziri Rajab Salum kuwa Balozi kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Meja Jenerali Mbaraka Naziad Mkeremy kuwa Balozi kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.

Viongozi Wateule wakiapa Kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emanuel John Nchimbi akiwa pamoja na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba katika hafla ya uapisho wa viongozi mbalimbali, Ikulu Mkoani Dodoma tarehe 13 Januari, 2026

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza mara baada ya kuwaapisha Viongozi mbalimbali, Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 13 Januari,2026.

DKT. MIGIRO: MAENDELEO YA JAMII NA SIASA HAVIWEZI KUTENGANISHWA

January 13, 2026 Add Comment


*Asisitiza mabalozi kupandisha bendera za chama kwenye maeneo yao.


* Asema chama kinawajali na kuwathamini mabalozi.

Mahusiano kati ya maendeleo ya jamii na maendeleo ya kisiasa hayawezi kutenganishwa, kwani maendeleo ya kweli huanzia katika misingi imara ya uongozi wa wananchi wenyewe. 

Kauli hiyo imesisitizwa na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, alipobainisha kuwa injini ya maendeleo ya chama na Taifa kwa ujumla ipo katika mashina ya CCM.

Dkt. Migiro amesema maendeleo ya kweli kwa wananchi huanzia katika mashina ya Chama hicho, akisisitiza kuwa jitihada zote za maendeleo ya kijamii na kiuchumi hupata nguvu kupitia uongozi wa ngazi za chini.

Katibu Mkuu huyo, ambaye ni mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo tangu chama kianzishwe, ameyasema hayo katika mkutano wake na Mabalozi wa Mashina wa CCM Wilaya ya Ilala, ikiwa ni hitimisho la ziara yake katika Mkoa wa Dar es Salaam yenye lengo la kuimarisha uhai wa CCM kuanzia mashinani, kwa kauli mbiu ya “Shina lako linakuita.”

Akizungumza na mabalozi hao, amesema mashina ndiyo ngazi ya kwanza inayowawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika mchakato wa maendeleo, kwa kuwa ndiko wanakotoka wananchi wenyewe na ndiko changamoto zao halisi zinapojadiliwa na kutafutiwa ufumbuzi.

Ameeleza kuwa mashina imara huwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa uwazi, ushirikishwaji na uwajibikaji, jambo linaloongeza imani ya wananchi kwa Chama Cha Mapinduzi na kuimarisha mshikamano wa kisiasa na kijamii.

Ameongeza kuwa viongozi wa mashina wana wajibu mkubwa wa kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo yao, akisisitiza kuwa uangalizi wa karibu wa miradi hiyo ndio msingi wa maendeleo yenye tija na yanayogusa maisha ya wananchi moja kwa moja.

Aidha, Mwanadiplomasia huyo amesema Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongeza kazi kubwa inayofanywa na Mabalozi wa Mashina, huku akibainisha kuwa chama kitaendelea kuwajali, kuwathamini na kuwatambua kama mhimili muhimu wa uhai na ushindi wa CCM kuanzia ngazi ya chini.


TEA YASHIRIKI SIKU MAALUM YA WATAALAMU WA UHASIBU

January 13, 2026 Add Comment
Wadau mbalimbali wakipata Elimu katika banda la Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) wakati wa maonesho kwenye siku maalum ya Wataalamu wa Uhasibu (NBAA Career Day)
MAVUNDE KUANZISHA KIJIJI CHA WANAWAKE DODOMA KUWAKWAMUA KIUCHUMI

MAVUNDE KUANZISHA KIJIJI CHA WANAWAKE DODOMA KUWAKWAMUA KIUCHUMI

January 12, 2026 Add Comment

Waziri wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Mtumba, Anthony Mavunde, amesema ana mpango wa kujenga eneo maalumu litakalofanya kazi kama kijiji cha wanawake kwa ajili ya kuwakutanisha wanawake wafanyabiashara katika sehemu moja ili waweze kuuza bidhaa zao kwa pamoja.

Mavunde ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, Januari 12, 2025 jijini Dodoma wakati akizungumza na wanawake kwenye hafla ya kukabidhi vitendea kazi kwa wanawake waliohitimu mafunzo ya ufundi stadi kupitia Chuo cha Veta, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwawezesha wanawake kiuchumi.

Amesema kijiji hicho kitatoa fursa kwa wanawake kufanya biashara katika mazingira rafiki, kubadilishana uzoefu pamoja na kuongeza thamani ya bidhaa zao, hali itakayosaidia kuongeza kipato na kuchangia maendeleo ya familia na taifa kwa ujumla.

“Lengo letu ni kuwawezesha wanawake kiuchumi kwa vitendo, ndiyo maana tunapanga kuwa na eneo maalumu litakalowaunganisha wanawake wote wanaojishughulisha na biashara mbalimbali,” amesema Mavunde.

Aidha, amewataka wanawake wa Jiji la Dodoma kuchangamkia fursa mbalimbali zinazojitokeza ikiwemo mafunzo ya ufundi, mikopo na miradi ya maendeleo ili kujikwamua kiuchumi na kuboresha maisha yao.

Kwa upande wao, wanufaika wa mafunzo hayo wamesema vitendea kazi walivyokabidhiwa vitawawezesha kuanza na kuendeleza shughuli zao za kiuchumi, huku wakimshukuru Mavunde na Serikali kwa kuwapa mafunzo na msaada unaowawezesha kujitegemea.

“Tunashukuru kwa mafunzo na vitendea kazi hivi, sasa tuna uhakika wa kuanza kujipatia kipato na kusaidia familia zetu,” amesema Boke Ramadhan

Naye Sylvia Mpanda amesema kuwa wangetamani eneo watakalojengewa basi liwe la mjini ili wawapate wateja wengi kutoka maeneo mbalimbali kwani wateja wengi wanapatikana maeneo yenye watu wengi

"Sisi tutafanya kazi kwa kikundi hivyo kwenye hichi kijiji atakachoanzisha Mhe Mavunde kitakuwa na wanawake wengi hivyo niwatake wanawake wengine kuacha kulala majumbani na waje kuchangamkia fursa zinazotolewa na serikali yetu." Amesema Sylvia

TANZANIA INA FURSA KUBWA YA KUENDELEZA NISHATI YA JOTOARDHI; WAZIRI NDEJEMBI ALIELEZA BARAZA LA IRENA

TANZANIA INA FURSA KUBWA YA KUENDELEZA NISHATI YA JOTOARDHI; WAZIRI NDEJEMBI ALIELEZA BARAZA LA IRENA

January 12, 2026 Add Comment
 

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amesema kutokana na uwepo wa vyanzo vingi vya nishati ya jotoardhi, Tanzania inayo fursa ya kuviendeleza vyanzo hivyo ili wananchi wapate nishati ya kutosha, nafuu na endelevu ikiwa pia ni sehemu ya kuunga mkono malengo ya dunia ya kuelekea kwenye uzalishaji wa umeme unaotokana na nishati safi.

Akizungumza kwenye Baraza la Kimataifa la Nishati Jadidifu (IRENA) katika Mkutano wa Mwaka wa Muungano wa Kimataifa wa Jotoardhi (Global Geothermal Alliance – GGA), unaofanyika Jijini Abu Dhabi, Falme za Kiarabu, Waziri Ndejembi amesema Serikali imeweka mipango ya uzalishaji wa umeme wa jotoardhi katika Dira ya Maendeleo 2050, Sera ya Taifa ya Nishati ya mwaka 2015, Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Dunia (SDGs) na Mkataba wa Nchi kuhusu Masuala ya Mabadiliko ya Tabia Nchi (NDCs).

Amesema Tanzania pia kupitia Kampuni ya Uendelezaji wa Jotoardhi (TGDC) inaendeleza maeneo kadhaa ya kipaumbele ya jotoardhi ikiwemo Ngozi (MW 70), Songwe (MW 5–38), Kiejo-Mbaka (MW 60), Natron (MW 60) na Luhoi (MW 5), huku lengo likiwa ni kuwa na mtambo wa kwanza wa kuzalisha umeme wa megawati 130 ifikapo 2030 ambapo mtambo huo utaanza kwa kuzalisha megawati 30.

Katika Mkutano huo, Waziri Ndejembi amealika wawekezaji nchini akieleza kuwa Tanzania inaendelea kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji, kuimarisha mifumo ya kisheria na kanuni ili kutoa uhakika wa uwekezaji, kuboresha michakato ya kupata leseni na vibali pamoja na kuboresha mazingira ya upatikanaji wa data za jotoardhi.

Aidha, ili kuweza kuiendeleza ipasavyo nishati ya jotoardhi Ndejembi amesema bado kunahitajika mikopo ya riba nafuu pamoja na kuwa na ushirikiano na Jumuiya za kimataifa pamoja na Sekta binafsi ili kukabiliana na changamoto ya uendelezaji hasa katika hatua za awali za utafiti ambazo zina gharama kubwa.

Ameongeza kuwa, Tanzania pia inakaribisha mataifa yaliyopiga hatua katika uendelezaji wa jotoardhi kuendeleza Wataalam wazawa katika masuala ya Jotoardhi.

Ndejembi amesema kuwa kutokana na uwepo wa Bonde la Ufa, Tanzania imebarikiwa kuwa na vyanzo vingi vya jotoardhi vinavyoweza kuzalisha megawati 5,000 za umeme. Ametaja kuwa kuna maeneo 52 yenye viashiria vya jotoardhi ndani ya mikoa 16.

Akifungua mkutano huo, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa IRENA, Gauri Singh amesema kuwa nishati ya jotoardhi ni muhimu duniani katika kutoa hakikisho la usalama wa nishati lakini ameeleza kuwa bado mchango wake bado ni mdogo duniani katika kuzalisha umeme hivyo vyanzo zaidi vinapaswa kuendelezwa.

Katika mkutano wa IRENA, Waziri Ndejembi ameambatana na Kaimu Balozi wa Tanzania katika Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Bakari Ameir, Kamishna Msaidizi anayeshughulikia Nishati Jadidifu, Mhandisi Imani Mruma pamoja na wataalamu wengine kutoka Wizara ya Nishati.