

HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI


Na Oscar Assenga, Lushoto
Kampuni ya Taifa Gesi imeendelea kujipambanua kama kinara wa usambazaji wa gesi nchini Tanzania, ikiwa na takribani asilimia 51 ya ujazo wa gesi yote inayopatikana nchini.
Akizungumza kuhusu mafanikio hayo wilayani hapa wakati wa Tamasha la NMB Kijiji Day, Meneja wa Masoko wa kampuni hiyo, Oscar Shelukindo, amesema kuwa mafanikio hayo yanatokana na uwekezaji mkubwa katika miundombinu ya kuhifadhi na kusambaza gesi, pamoja na dhamira ya dhati ya kuwahudumia Watanzania.
Ameeleza kuwa lengo kuu la kampuni hiyo ni kusaidia juhudi za taifa za kuhamasisha matumizi ya nishati safi, kwa kuwahamasisha wananchi kuachana na matumizi ya kuni na mkaa, ambayo yamekuwa na athari kubwa kwa afya na mazingira.
Kwa mujibu wa takwimu, zaidi ya Watanzania 33,000 hufariki kila mwaka kutokana na magonjwa yanayosababishwa na matumizi ya nishati zisizo safi. Hali hiyo imeifanya Taifa Gesi kuongeza juhudi za kuhakikisha gesi inapatikana kwa urahisi na kwa gharama nafuu.
Katika hatua hiyo, kampuni hiyo inatoa mitungi ya gesi ya kilogramu 6 na 15 kwa bei nafuu, pamoja na huduma ya kujaza mitungi kwa wateja waliokwisha kuwa nayo, hatua inayolenga kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Aidha, Taifa Gesi kwa kushirikiana na NMB Bank wanatarajiwa kushiriki katika Tamasha la Kijiji Day, ambapo watatoa huduma mbalimbali pamoja na elimu kwa wananchi kuhusu matumizi sahihi ya nishati safi.
Juhudi hizi zinatajwa kuwa chachu ya mabadiliko chanya, zikilenga kuboresha afya za Watanzania na kulinda mazingira kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
Na, Mwandishi Wetu - Korogwe, Tanga
Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Afya Moja kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Salum Manyatta, amesema kuwa Mpango Mkakati wa Afya Moja umejikita kuhakikisha wananchi wananufaika kuanzia ngazi ya Kaya hadi Taifa kupitia utekelezaji shirikishi wa sekta mbalimbali nchini ili kuhakikisha malengo yake yanafikiwa na kuwa na tija kwa jamii kwa ujumla.
Dkt. Manyatta ameyasema hayo Aprili 13, 2026 mkoani Tanga wakati wa kikao kazi cha wataalam cha kuandaa Mpango wa Mkoa wa Afya Moja kilichoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sehemu ya Afya Moja kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania kupitia Mradi wa Usalama wa Afya Duniani.
Amesema kuwa lengo kuu la kikao hicho ni kuwajengea uwezo Watalamu ngazi ya mkoa kuhusu utekelezaji wa Dhana ya Afya Moja na kuwawezesha kutengeneza Mpango wa Utekelezaji wa Afya Moja wa Mkoa ambacho kitafanyika kwa siku tano kuanzia tarehe 13 hadi 17 Aprili 2026 katika Halmashauri ya Mji wa Korongwe, Mkoani Tanga.
Dkt. Manyatta ameeleza kuwa, lengo la dhana ya Afya Moja ni kupanua na kuimarisha ushirikiano baina ya sekta/taaluma mbalimbali katika hatua zote za kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na milipuko ya magonjwa na hatari nyingine za afya zinazohitaji ushiriki wa sekta zaidi ya moja na taaluma mbalimbali.
“Ushirikiano huu pamoja na wadau wengine ikiwemo jamii, kimsingi unaongozwa na sekta/wizara za msingi (lead Ministries) ambazo ni Afya ya Binadamu, Wanyama (Mifugo na Wanyama Pori), Mazingira na Kilimo katika ngazi zote,” alifafanua Dkt. Manyatta.
Alifafanua kuwa, uwepo wa Mpango Mkakati ni muhimu kwani unatarajiwa kuweza kujibu na kutatua changamoto zilizopo katika Mkoa wa Tanga, hivyo utumike kama fursa ya kuhakikisha mkoa unakuwa na uelewa wa pamoja wa masuala ya Afya Moja kwa kuunganisha nguvu ya pamoja na kuweza kufanya kazi pamoja kwani hii ndiyo maana halisi ya dhana ya Afya Moja.
Naye Mwakilishi wa Katibu Tawala, ambaye ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt. Japhet Simeo amepongeza uratibu wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa namna inavyoendelea kutoa elimu ya masuala ya Afya Moja, na kueleza kuwa mkoa wa Tanga utanufaika kwa uwepo wa Mpango Mkakati wa Afya Moja na kusisitiza kuwa Tanga itautekeleza kwa vitendo na kufanya mkoa huo kuwa wa mfano
“....Ifike mahali tutoke katika mambo ya concept to Action, yaani kuwa na mipango na mikakati ya namna hii na kuitekeleza na hiyo ndiyo umuhimu wa dhana Afya Moja,” alisisitiza Dkt. Simeo
Kwa upande wake, Msimamizi wa Afya Moja na Mratibu wa Mradi wa Usalama wa Afya Duniani unaotekelezwa na Shirika lisilo la Serikali la CIHEB Tanzania Dkt. Irene Massawe amesema kuwa, ushirikiano uliopo utasaidia kufanikisha malengo yaliyopo kwa nguvu ya pamoja na kuhakikisha matarajio ya uwepo wa mpango huo yanafika hadi ngazi za chini.
Aliongezea kuwa, sekta husika zikiungana kwa pamoja katika kutekeleza dhana ya Afya Moja itasaidia kudhibiti vihatarishi vya afya ikiwemo magonjwa ya mlipuko hasa yale yanayoweza kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu, yakiwemo ya kimeta, kichaa cha mbwa kwani itarahisisha na kuleta ufanisi katika kukabiliana na changamoto hizo.
“Tunaamini kuwepo kwetu ndani ya siku tano hizi Korogwe kutazaa matunda kwa washiriki wote kisha kuyaleta haya katika utekelezaji wa kila siku na kuhakikisha tunaleta matokeo chanya ya mipango hii,” alisema Dkt. Irene.
AWALI
Afya Moja ni Dhana ya Kimataifa iliyoridhiwa na Shirika la Afya Duniani (WHO), shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama (OIE), Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Programu ya Kimataifa ya Mazingira (UNEP) kupitia “Global Health Security Agenda” (GHSA) na wadau wengine wa Afya duniani kote. Shirika la Afya Duniani (WHO), Shirika linaloshughulika na Afya ya Wanyama (OIE) na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) yamekuwa yakishirikiana duniani kote na kutoa wito kwa wataalamu wa sekta za Afya ya Binadamu, Wanyama na Mazingira kuongeza na kuimarisha ushirikiano na mawasiliano ili kuboresha ufanisi katika kukabiliana na tishio la magonjwa ya kuambukiza yanayoenea kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu na yanayovuka mipaka; tatizo la usugu wa vimelea vya magonjwa na changamoto zingine zinazokabili afya ya jamii zinazohitaji nguvu ya pamoja.
=MWISHO=

▪︎ Asisitiza Vijana kuomba udahili na ufadhili*
▪︎ Asisitiza Uwazi na Ushindani*
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ametangaza rasmi kutolewa kwa ufadhili kupitia Samia Scholarship Exender AI/DS wa masomo ya Uzamili (Masters) katika Sayansi ya Data, Akili Unde na fani zinazohusiana.
Akizungumza Aprili 13, 2026 jijini Dar es Salaam amesema kuwa Serikali inaendelea kuwekeza katika kuandaa rasilimali watu wenye uwezo wa kushindana kimataifa katika sayansi na teknolojia na kuwashawishi vijana wenye vigezo kuomba udahili na ufadhili.
Prof. Mkenda ameeleza kuwa Samia Scholarship extended DS/AI+ ilianza kufadhili wanafunzi wa shahada ya kwanza waliobobea katika sayansi, uhandisi, tiba na hisabati, ambapo tayari wanafunzi 16 wamepelekwa nchini Afrika Kusini na wengine 34 watakwenda nchini Ireland.
Ameongeza kuwa ufadhili wa sasa unalenga kuongeza idadi ya vijana wa kitanzania wenye ujuzi na taaluma katika maeneo hayo.
"Ufadhali huu ni kwa waombaji watakaosoma shahada ya Uzamili katika Taasisi ya Indian Institute of Technology (IIT) Madras – Kampasi ya Zanzibar," amesisitiza Prof. Mkenda
Waziri Mkenda amesema kuwa masharti ni ya wazi ambapo mwombaji awe Mtanzania, mwenye umri usiozidi miaka 35, awe na daraja la kwanza katika masomo ya sayansi ya kidato cha sita, GPA ya angalau 3.8 katika shahada ya kwanza, na awe amepata udahili katika IIT Madras, Zanzibar.Amesisitiza kuwa hatua ya kwanza ni kuomba udahili chuoni kabla ya Aprili 15, kisha kuwasilisha maombi ya ufadhili kuanzia Juni 1 hadi Juni 30 na kwamba Kamati huru itapitia maombi kwa uwazi na ushindani, kuhakikisha wanafunzi bora zaidi wanapata nafasi.
Mhe. Salome ametoa kauli hiyo leo Aprili 13, 2026 wakati akijibu swali la Mbunge wa Ndanda, Mhe. Faraji Buriani Nandala aliyehoji ni lini Wananchi wa Kata za Chikukwe, Chigugu, Chigundi, Mwena, Ndanda na Nanganga ambao wamepitiwa na Mradi wa Grid ya Taifa watalipwa fidia.
Na Oscar Assenga,Tanga
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman ameanza jitihada za kuinusuru Klabu ya African Sports ambayo ipo hatarini kushuka daraja kufuatia matokeo mabaya katika Ligi ya Championship.
Rajab aliyasema hayo baada ya kukutana na wachezaji pamoja na viongozi wa klabu hiyo, ambapo alieleza kuwa hali ya timu si ya kuridhisha, akifananisha na mgonjwa aliye katika chumba cha mahututi.
Alibainisha kuwa kwa sasa African Sports inashika nafasi ya 15 kati ya timu 16, hali inayoiweka katika hatari kubwa ya kushuka daraja endapo haitafanya vizuri katika mechi zilizobaki.
Akizungumzia historia ya klabu hiyo, alisema ni moja ya timu zenye heshima kubwa nchini na mshindani wa jadi wa Coastal Union, hivyo ni muhimu kurejesha ushindani wa soka la Tanga.
Katika hatua ya kuokoa timu hiyo, Mwenyekiti huyo alitangaza kuchangia Shilingi milioni 20 ambazo tayari alikwisha kuziweka kwenye akauti, huku Mbunge wa Jimbo la Tanga akiahidi kutoa milioni tano na mdau mwingine kuahidi milioni 20, ikiwa ni sehemu ya kufikia lengo la kukusanya milioni 45 zinazohitajika kuiwezesha timu kumaliza msimu salama.
Alisema atahakikisha fedha hizo zinapatikana ili kutatua changamoto zinazoikabili klabu hiyo na kuwawezesha wachezaji kucheza kwa utulivu.
Aidha, aliwataka wachezaji kujituma katika mechi zilizobaki ili kuinusuru timu, akisisitiza kuwa wana dhamana ya kulinda heshima ya klabu hiyo.
Kwa upande mwingine, aliwashauri viongozi wa klabu kuweka mikakati ya muda mfupi na mrefu, ikiwemo kutovunja kambi mara baada ya msimu kumalizika ili kuboresha maandalizi ya msimu ujao.
Aliongeza kuwa mabadiliko ya mara kwa mara ya kikosi na maandalizi hafifu yamekuwa yakichangia kushuka kwa kiwango cha timu, na kusisitiza kuwa kwa mipango madhubuti wanaweza kurejea Ligi Kuu katika msimu ujao.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu), Dkt. James Henry Kilabuko (wapili kulia) akishiriki kuimba Wimbo wa Wafanyakazi wakati wa ufunguzi wa Barala la Wafanyakazi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi lililokutana leo Aprili 11, 2026 mkoani Morogoro. Wengine pichani ni Mwenyekiti wa Baraza hilo na Mkurugenzi wa Uchaguzi wa INEC, Ramadhani Kailima (wapili kushoto), Katibu wa Baraza, Livini Avith (kulia) na Kulia ni mtumishi wa Tume, Rose Tengu. (Picha na INEC).











