Na Amina Omari,Kilindi
Kata ya Kimbe wilayani Kilindi Mkoa wa Tanga imejipanga kutengeneza madawati 500 Ili kumaliza tatizo la upungufu wa madawati katika shule zilizopo kwenye kata hiyo.
Akiongea kuhusu mkakati huo na gazeti hili Diwani wa kata hiyo Mussa Kalamba alisema kuwa Kata hiyo yenye shule tisa za awali na msingi zina upungufu wa jumla ya madawati 825,huku Sekondari ya Kimbe ikikabiliwa na upungufu wa viti na meza 251.
Katika utekelezaji wa awamu ya kwanza, kata inatarajia kutengeneza madawati 500 kwa shule za msingi na viti 150 kwa Sekondari ya Kimbe ili kukabiliana na upungufu uliopo huku uongozi wa kata ukiendelea na mipango ya kuhakikisha wanaweka mipango ya kumaliza changamoto hiyo.
Kalamba alisema kuwa mpango huo uliokubaliwa katika vikao vya Kamati ya Maendeleo ya Kata (WDC), uongozi umeweka utaratibu wa kufuatilia upungufu wa madawati kila muhula wa masomo na kila mwaka wakati wa uandikishaji wa wanafunzi wapya.
"Lengo letu si tu kuziba pengo lililopo, bali tunataka kuhakikisha tuna ziada ya madawati katika shule zetu. Kwa kutumia idadi ya wanafunzi wanaoongezeka kila mwaka, tutakuwa na uwezo wa kubaini mapema upungufu na kuutatua kwa haraka kabla hali haijawa mbaya," alisema Diwani huyo.
Hata hivyo aliwataka, wananchi wake kuunga mkono juhudi hizi kwa kuchangia nguvu na rasilimali pindi wanaposhirikishwa na viongozi wa serikali za vijiji.
"Tunawaomba wananchi wetu waendelee kuonesha ushirikiano wao. Hii ni ajenda ya pamoja kwa mustakabali wa watoto wetu. Kila mchango wenu ni hatua kuelekea mazingira bora ya kujifunzia," ilisisitiza Kalamba
Utekelezaji wa mpango huu unatazamwa kama kielelezo cha uwajibikaji wa pamoja, ambapo serikali ya kata imejipanga kusimamia kwa karibu usimamizi wa rasilimali hizo ili kuleta matokeo chanya ya kudumu katika elimu ndani ya Kata ya Kimbe.





























