HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts

DKT. AKWILAPO: MSITOE MAAMUZI YA KUWAFURAHISHA WATU
habari
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuapishwa kwa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.
Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akimuapisha mmoja wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026Na Munir Shemweta, WANMM MTWARA
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo ameshuhudia uapisho wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya na kuwataka wajumbe hao kutenda haki kuacha kutoa maamuzi ya kuwafurahisha watu wakati wa kusikiliza mashauri ya ardhi.
Uapisho huo umeongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Donald Wilson Msengi, na kufanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.
Akizungumza mara baada ya kushuhudia uapisho huo, Dkt. Akwilapo aliwaasa wajumbe wa mabaraza hayo kuepuka kutoa maamuzi kwa lengo la kuwafurahisha watu au makundi fulani, badala yake wafanye maamuzi yanayozingatia haki na sheria ili kupunguza migogoro ya ardhi katika jamii.
Alisema wajumbe wanapaswa kutambua kuwa nafasi waliyopewa ni dhamana kubwa kutoka kwa Mungu na Serikali, hivyo wanatakiwa kuitumia kwa uadilifu, uaminifu na kwa kuzingatia misingi ya haki.
“Napenda mtambue kuwa nafasi mlizopewa ni kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, hivyo mheshimu Mungu kwa kufanya maamuzi yanayoendana na haki na uadilifu,” alisema Dkt. Akwilapo.
Aliongeza kuwa, kazi ya kushughulikia mashauri ya ardhi si rahisi, kwani mara nyingi huwa na pande mbili zinazopingana, lakini wajumbe wanapaswa kufanya maamuzi kwa kuzingatia ushahidi na sheria ili haki ipatikane kwa anayestahili.
“Sina wasiwasi na ninyi, ingawa kazi ni ngumu, lakini mfanye maamuzi kwa kuzingatia haki na siyo kumfurahisha mtu,” alisisitiza.
Dkt. Akwilapo pia alisema uimarishaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa kusogeza huduma hizo karibu zaidi na wananchi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Msengi aliwapongeza wajumbe hao kwa kuaminiwa kushika nafasi hizo na kuwataka kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viapo walivyokula na kufanya kazi kwa weledi.
Amesema, wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni kiungo muhimu katika mfumo wa utatuzi wa migogoro ya ardhi, hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa uadilifu ili kujenga imani kwa wananchi.
“Uwepo wa wajumbe wa mabaraza ya ardhi katika wilaya zenu sasa utawezesha wananchi kupata huduma karibu zaidi badala ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo,” alisema.
Ameongeza kuwa, hatua hiyo itasaidia kupunguza gharama na muda ambao wananchi walikuwa wakitumia kufuata huduma za utatuzi wa migogoro ya ardhi katika maeneo ya mbali.
Wajumbe walioapishwa wanatoka katika wilaya za Mtwara, Tandahimba, Newala pamoja na wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara.
Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuimarisha Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya ili kuongeza ufanisi katika kusikiliza na kutatua migogoro ya ardhi kwa wakati, jambo litakalosaidia kuimarisha usalama wa milki na kuleta utulivu katika jamii.

WAZIRI NDEJEMBI ATOA SIKU 14 KWA MKANDARASI KUREJEA MRADI WA UMEME SONGEA-MAHUMBIKA
Na Mwandishi Wetu, Tunduru
Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amempa siku 14 mkandarasi anayetekeleza mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Mahumbika kupitia Tunduru na Masasi kurejea eneo la mradi na kuendelea na kazi mara moja.
Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya Kalpataru Projects International Limited, ambayo ina jukumu la kujenga vituo vya kupoza umeme katika wilaya za Tunduru, Masasi na Mahumbika.
Akitoa agizo hilo Machi 7, 2026 wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, Ndejembi amesema mkandarasi huyo hapaswi kupewa kazi nyingine yoyote ya serikali hadi atakapokamilisha mradi huo ambao utekelezaji wake umechelewa kinyume na masharti ya mkataba.
Aidha, Waziri huyo amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati kumuandikia barua ya onyo mkandarasi huyo, akieleza kuwa tayari walikutana na uongozi wa kampuni hiyo jijini Dodoma na kukubaliana kuwa wangeanza kazi ndani ya siku 25 baada ya kulipwa fedha walizokuwa wanadai tangu Desemba 2025.
Hata hivyo, amesema hadi sasa mkandarasi huyo hajarejea katika eneo la mradi wala kuanza kazi.
“Huyu mkandarasi anafanya kazi kwa kusuasua sana. Walilipwa fedha mwezi Desemba na tukakubaliana ndani ya siku 25 wawe wamerudi site na kazi ianze, lakini muda wote umeisha na hakuna kinachoendelea,” amesema Ndejembi.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, mradi huo ulipaswa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili na kukabidhiwa mwishoni mwa mwaka huu, lakini hadi sasa utekelezaji umefikia takribani asilimia 50 pekee.
Amesema mradi huo ni sehemu ya mpango wa serikali wa kuunganisha mikoa ya kanda ya kusini ambayo ni Ruvuma, Lindi na Mtwara kwenye gridi ya taifa ili kuboresha upatikanaji wa umeme wa uhakika.
“Wananchi wa Kusini wanahitaji umeme wa uhakika na serikali imeweka kipaumbele katika kutatua changamoto hiyo kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi huu. Haiwezekani mkandarasi akachelewesha kazi hii,” amesema.
Ameongeza: “Baada ya onyo tutakalompa, endapo ataendelea kusuasua tutachukua hatua zaidi.”
&&&
WANANCHI ZAIDI YA 13,000 WANUFAIKA NA SAMIA ARDHI KLINIKI NCHINI
MTWARA
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amesema jumla ya wananchi 13,550 wamejitokeza kupata huduma mbalimbali za sekta ya ardhi kupitia Samia Ardhi Kliniki iliyofanyika katika mikoa yote 26 nchini.
Dkt. Akwilapo amesema hayo wakati akifunga rasmi Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026, akisema kliniki hiyo imekuwa jukwaa muhimu la kusogeza huduma za ardhi karibu na wananchi hususan wanawake.
Amesema, kati ya wananchi waliojitokeza katika kliniki hizo, wanawake walikuwa 8,725 sawa na asilimia 64.4 huku wanaume wakiwa 3,892 sawa na asilimia 35.7, jambo linaloonesha mwitikio mkubwa wa wanawake katika kutumia fursa zinazotolewa na Serikali.
Aidha, Waziri Akwilapo amesema, jumla ya hatimiliki 3,131 zimetolewa kwa wananchi waliokamilisha taratibu za umilikishwaji wa ardhi ambapo hatimiliki 2,081 sawa na asilimia 57.4 zimetolewa kwa wanawake na hatimiliki 1,543 sawa na asilimia 43.6 zimetolewa kwa wanaume.
Amefafanua kuwa, hatua hiyo imeongeza usalama wa milki kwa wananchi pamoja na kuimarisha uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.
“Ardhi ni msingi wa uchumi wa mwananchi na Taifa. Mwanamke anapomiliki ardhi kisheria anapata uwezo mkubwa wa kuwekeza, kufanya shughuli za uzalishaji na hata kupata mikopo katika taasisi za fedha,” alisema.
Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi amesema, Samia Ardhi Kliniki imenufaisha wanawake kwa kuwaelimisha jambo alilolieza kuwa limelenga kuwawezesha na kulinda haki na kutatua changamoto zao.
‘’Kupitia Kliniki hiyo wanawake walipewa huduma mbalimbali ambazo ni elimu ya kumiliki ardhi, ushauri wa kitaalamu kuhusu masuala ya ardhi pamoja na utoaji hati’’ amesema Kanali Msengi.

RAIS SAMIA ASHIRIKI MKUTANO WA 25 WA WAKUU WA NCHI WA EAC ARUSHA
habari
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiteta jambo na Marais mbalimbali wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) aliposhiriki Mkutano wa 25 wa Kawaida wa Wakuu wa Jumuiya hiyo uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) Leo Machi 07,2026.


RAIS WA BURUNDI MHE. ÉVARISTE NDAYISHIMIYE AWASILI KIA KUSHIRIKI MKUTANO WA 25 WA WAKUU WA NCHI WA EAC
habari
Rais wa Jumhuri ya Burundi Mheshimiwa Évariste Ndayishimiye amewasili katika Uwanja wa Ndega wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) Mkoani Kilimanjaro, kushiriki katika Mkutano wa 25 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) unaofanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika Makao Makuu ya Jumuiya jijini Arusha.
Akiwasili Mkoani humo amepokelewa na Mhe. Mahmoud Thabit Kombo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiambatana Viongozi Waandamizi mbalimbali wa Serikali.

MHE.SALOME AIBANA KAMPUNI YA DONGFANG KWA KASI ISIYORIDHISHA MRADI WA UMEME MALAGARASI
📌*Atoa maelekezo mahsusi kwa Mkandarasi na Wasimamizi wa mradi*
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba leo amekagua utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa Malagarasi (MW 49.5) unaotekelezwa katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma ambapo ameeleza kutoridhishwa kwake na kasi ya utekelezaji.
Akiwa katika Kijiji cha Mazungwe wilayani Uvinza Mhe Salome amekagua sehemu mbalimbali za mradi ikiwemo ujenzi wa tuta na uchepushaji mto, ujenzi wa jengo la kuendeshea mitambo na kambi za wafanyakazi ambapo hakukuta wafanyakazi wa kutosha kama ambavyo mkataba unaelekeza.
Kutokana na hilo, Naibu Waziri wa Nishati amemuagiza mkandarasi kampuni ya Dongfang ya China kuhakikisha kuwa anaongeza wafanyakazi, vifaa vya kazi na ndani ya mwezi mmoia awe amejenga kambi ya wafanyakazi.
Aidha, amemtaka Mkandarasi kuwasilisha ratiba mpya ya utekelezaji wa kazi.
Vilevile, ameagiza wasimamizi wa mradi wa Malagarasi kutoka Kampuni ya Mkandarasi Mshaurii na TANESCO kuhamia katika eneo la mradi ndani ya mwezi mmoja ili kuweza kuusimamia mradi huo kwa ukaribu.
"Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza Wizara ya Nishati kuzalisha megawati 8000 za umeme ifikapo 2030, hatutakubali mtu atukwamishe katika kufikia malengo haya. Mkandarasi hakikisha unakamilisha kazi ifikapo Oktoba 2027 kama mkataba unavyoelekeza." Amesisitiza Mhe.Salome
Aidha, amemtaka Mkandarasi Mshauri kampuni ya Multiconsult Norge AS ya Norway na Norplan kutoka Tanzania kuhakikisha kuwa wanamsimamia mkandarasi ipasavyo ili mradi ukamilike kwa wakati na kwa viwango stahiki.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Dinah Mathamani ameeleza kuwa uongozi wa wilaya hiyo utasimamia kwa karibu maelekezo yanayotolewa na Wizara ili mkandarasi atekeleze kazi kulingana na.mkataba.
Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Mhandisi Edson Ngabo amesema utekelezaji wa mradi wa Malagarasi kwa saaa ulipaswa kuwa kwenye asilimia 28 ila umefikia asilimia 23.
Amesema Wizara ya Nishati itaendelea kumsimamia kwa karibu mkandarasi ili amalize kazi kwa wakati.
Sehemu nyingne zinazohusisha mradi wa Malagarasi ni upelekaji umeme katika vijiji saba vyenye vitongoji 18 ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100.
Pia ujenzi wa njia ya msongo wa kV 132 kutoka eneo la mradi hadi Kidahwe ambao umekamilika kwa asilimia 100.






























