
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI

O
Tanzania inaendelea kuimarisha na kuongeza matumizi ya gesi asilia katika uzalishaji wa nishati ya umeme nchini, hatua inayolenga kuiwezesha kufikia lengo la kuzalisha megawati 8,000 za umeme ifikapo mwaka 2030. Katika mpango huo, gesi asilia ni miongoni mwa vyanzo muhimu vitakavyotumika kuimarisha uzalishaji wa umeme wa uhakika na wa kutosha nchini.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratus Ndejembi, katika Mikutano ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa (World Bank – IMF Spring Meetings 2026) inayoendelea jijini Washington D.C, nchini Marekani.
Akizungumza katika mjadala kuhusu uzalishaji wa umeme kupitia gesi asilia uliofanyika chini ya mada isemayo “Gas in Sub-Saharan Africa’s Energy Sector”, Waziri Ndejembi amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizoweka kipaumbele kikubwa katika kutumia gesi asilia kama chanzo cha kuzalisha umeme.
Ameeleza kuwa hadi sasa, Tanzania inazalisha zaidi ya megawati 1,200 za umeme kupitia gesi asilia, ambazo tayari zimeunganishwa katika Gridi ya Taifa, hatua inayochangia kuimarika kwa upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.
Aidha, Waziri Ndejembi amebainisha kuwa serikali inaendelea kuimarisha uzalishaji wa gesi asilia, ambapo kazi ya uchimbaji wa visima vipya vitatu katika Kitalu cha Mnazi Bay mkoani Mtwara inaendelea. Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza upatikanaji wa gesi na hivyo kuimarisha zaidi uzalishaji wa nishati nchini.
Pia, amesisitiza kuwa Tanzania inaendelea kuwakaribisha wawekezaji katika sekta ya nishati, hususani katika eneo la matumizi ya gesi asilia, ambalo lina fursa kubwa za kiuchumi na maendeleo ya taifa.
Katika mkutano huo, Benki ya Dunia imezitaka nchi za Afrika kuendelea kuongeza uzalishaji wa umeme kwa kutumia gesi asilia, huku Tanzania ikitajwa kuwa miongoni mwa nchi zilizopiga hatua muhimu katika matumizi ya nishati hiyo.
Katika Mkutano huo, Waziri Ndejembi ameambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio pamoja na wataalam kutoka taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati.











📌Ni katika Kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa umeme
📌Waishukuru TANESCO kwa zawadi hiyo, wapongeza kazi kubwa inayofanywa na Shirika
📌Waahidi kwenda kuwa mabalozi wazuri wa Nishati Safi ya Kupikia kwa Umeme
Na. Mwandishi Wetu, Manyara
Katika Kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa umeme hapa nchini Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Bw. Lazaro Twange ametoa Majiko zaidi ya 30 kwa Walimu wa Shule ya Wasichana Mkoa wa Manyara ili kuwapa hamasa kwa kazi wanayoifanya.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga, Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro Mhe. Fakii Lulandala amempongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Bw. Lazaro Twange kwa kutoa majiko hayo kwa walimu yanayolenga kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa umeme.
Amesema Bw. Twange anaunga mkono kwa vitendo ajenda ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kutokana na jitihada kubwa zinazofanywa na TANESCO katika maeneo mbalimbali hapa nchini.
Amesema majiko hayo yanakwenda kutoa motisha kubwa kwa walimu wa shule hiyo na kuchochea ari ya ufundishaji kwa wanafunzi kwani sasa watatumia muda mchache wakati wa kupika hali ambayo itasaidia kuongeza ufaulu zaidi kwa wanafunzi hao.
Amesema licha ya kutoa Majiko hayo Bw. Lazaro Twange anamchango Mkubwa katika ujenzi wa Shule hiyo ya Wasichana kwani alihakikisha anaisimamia kikamilifu wakati akiwa Mkuu wa Wilaya ya Babati na kufanikisha ujenzi wake kutokana na kujitoa kwakwe usiku na mchana ili kuhakikisha ujenzi wa shule hiyo unakamilika.
“Bw. Lazaro Twange ndiye kinara wa ujenzi wa Shule hii na leo ametoa majiko ya kisasa yanayotumia umeme kidogo sana kwa ajili ya kuwagawia walimu, na hii inakwenda kuwa motisha kubwa kwa walimu wa shule hii hasa katika matumizi ya Nishati Safi ya umeme “
Kwa upande wake, Meneja wa TANESCO Mkoa wa Manyara Mhandisi Regina Mvungi amesema kwa Niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Bw. Lazaro Twange wamekabidhi majiko 30 kwa walimu wa shule hiyo kama zawadi kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO.
Amesema majiko hayo yamekabidhiwa kwa walimu wote wa Shule hiyo na sasa wanakwenda kuwa mabalozi wa kuhamasisha matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa umeme kwa vitendo kwa jamii inayowazunguka wakiwemo wanafunzi wao na wananchi kwa ujumla.
“Kupitia Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Bw. Lazaro Twange tumetoa zawadi ya majiko 30 kwa walimu wa shule hii ili wakawe mabalozi wa kupikia kwa umeme kuanzia shuleni na jamii zinazowazunguka”
Naye Mkuu wa Shule hiyo ya Sekondari ya Wasichana Mkoa wa Manyara Mwl. Gisela Msoffe amelishukuru Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO wakati akiwa Mkuu wa Wilaya ya Babati hasa kwa usimamizi uliotukuka wa ujenzi wa shule hiyo pamoja na kuwezesha kufikishiwa kwa huduma ya umeme katika majengo yote ya shule hiyo.
Zaidi ameshukuru kwa zawadi ya majiko ya kisasa ya umeme waliyopatiwa walimu kwani yanakwenda kuwa msaada mkubwa hasa katika kuokoa muda wakati wa kupika ili kuwawezesha kuwa na muda wa kutosha kufundisha wanafunzi.
“Nimshukuru kwa dhati Bw. Lazaro Twange watumishi wote wa shule hii hasa Walimu tumepewa majiko ya kisasa ya umeme yatatusaidia kuokoa muda wakati wa kupika na tutapata Muda mwingi wa kufundisha Wanafunzi” ameongeza Mwl. Gisela
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali imetenga kiasi cha Sh Bilioni 3.2 kupitia kwa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa ajili ya kusambaza umeme katika vitongoji vilivyopo ndani ya vijiji Tisa vya Kitewele, Kimata, Ndoa, Chanjale, Nkanda, Lumbila, Nsele na Kilondo vilivyopo wilayani Ludewa mkoani Njombe ambapo mradi huo unatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba 2026.
Mhe. Salome ameyasema hayo leo Aprili 17, 2026 Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Ludewa, Mhe. Joseph Kamonga aliyehoji ni lini Vijiji hivyo vitawashiwa umeme.
" Kwa kutambua changamoto ya Jiografia na ugumu wa kufikisha vifaa katika maeneo hayo, tumempatia kazi hiyo Mkandarasi M/s SUMA JKT Electric Co. Ltd ambaye tumemuelekeza kufanya kazi kama Jeshi na kuhakikisha kuwa azma ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kufungamanisha nishati na maendeleo ya kiuchumi inatimia," Amesema Mhe. Salome.
Aidha Mhe. Salome ameiagiza REA kumsimamia Mkandarasi huyo ili aweze kutimiza majukumu yake ili kuhakikisha wananchi wa Ludewa wananufaika na uwepo wa nishati imara na uhakika.

Timu ya Mpira wa miguu ya TCDC Sports Club imechukua alama tatu (3) baada cha kuifunga Timu ya Mpira wa miguu ya Wizara ya Kilimo goli mbili (2) kwa moja (1) katika mechi iliyochezwa leo Aprili 17, 2026 saa 2:30 3:45 katika viwanja vya Venite mkoani Njombe.
Timu hizo zimekutana katika mashindano ya Michezo ya Wafanyakazi (Meimosi) yanayoyafanyika kitaifa mkoani Njombe.
Hapo Kesho Aprili 18, 2026 Timu ya Mpira wa miguu TCDC Sport Club inatarajia kukutana na Timu ya Mpira wa miguu ya TAMISEMI saa10:15 jioni katika viwanja vya Kibena mkoani humo.