HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

MTAALAMU SAYANSI,USALAMA WA MTANDAO ATINGA TUME

March 02, 2026 Add Comment




*DAR ES SAALAM:* TUME ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani yaliyojitokeza wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, leo Machi 2, 2026 imekutana na Mtaalamu wa Uchunguzi wa Kisayansi na Usalama wa Mtandao, Yusuph Kileo.


Mkutano huo wa Tume na Mchunguzi huyo umefanyika katika ukumbi wa Tanganyika uliopo jengo la Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mkoani hapa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tume kukusanya taarifa, maoni na ushauri kutoka kwa watu mbalimbali wakiwemo wataalamu, watu wa kawaida, viongozi wa sasa na wastaafu.

Katika mkutano huo hoja zilizojadiliwa zilihusu maeneo ya tathmini ya athari za matukio hayo ndani ya nchi na kimataifa na ushauri wa hatua za kijamii na kisheria zinazochukuliwa ili kuimarisha amani, mshikamano wa kitaifa.

Hivi karibuni Mamlaka ya Uteuzi imeiongezea Tume muda wa siku arobaini na mbili (42) kuanzia tarehe 20 Februari, 2026 ili Tume iweze kukamilisha uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 29 Oktoba, 2025 na kuitaka ikamilishe kazi na kuwasilisha Taarifa yake kabla au ifikapo tarehe 3 Aprili, 2026. 



Tume inaendelea na mahojiano na waathirika wa Matukio hayo kwa ajili ya hatua zaidi kama Taifa ili Matukio kama hayo yasijirudie tena.

ASILIMIA 28 TU YA WANAWAKE WAMILIKI ARDHI NCHINI

ASILIMIA 28 TU YA WANAWAKE WAMILIKI ARDHI NCHINI

March 02, 2026 Add Comment

Na.Alex Sonna-Dodoma

WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha  kliniki maalum iitwayo Samia Ardhi Kliniki nchi nzima kwa lengo la kuongeza idadi ya wanawake wanaomiliki ardhi, ambapo kwa sasa ni asilimia 28 tu.

Hatua hiyo inalenga kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, katika kuhakikisha huduma za ardhi zinatolewa kwa wananchi kwa kuzingatia misingi ya usawa wa kijinsia.

Akizungumza leo Machi 2,2026 jijini Dodoma wakati wa uzinduzi wa kliniki hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo,Mhandisi Anthony Sanga, amesema mpango huo utaendeshwa nchi nzima na unatarajiwa kuhitimishwa Machi 7 mwaka huu, kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani.

Mhandisi Sanga amesema kuwa  lengo kuu la Samia Ardhi Kliniki ni kuongeza asilimia ya umiliki wa ardhi kwa wanawake nchini kupitia utoaji wa elimu, hati za umiliki na utatuzi wa migogoro ya ardhi.

 "Takwimu zinaonesha kuwa ni takriban asilimia 28 pekee ya wanawake nchini wanamiliki ardhi, jambo linaloonesha umuhimu wa kuendelea kutoa elimu na kuhamasisha ushiriki wao katika masuala ya umilikishaji."amesema Mhandisi Sanga

Mhandisi Sanga amefafanua kuwa Sera ya Taifa ya Ardhi ya mwaka 1995 iliweka msingi wa usawa wa kijinsia katika umiliki wa ardhi kati ya wanaume na wanawake. Hata hivyo, amesema changamoto zilijitokeza katika utekelezaji, hasa kwenye masuala ya mirathi na urithi ambapo mila na desturi zilichangia kuwabagua wanawake.

“Tamko la sera ya mwaka 1995 lilielekeza kuzingatia mila na desturi, lakini katika sera mpya iliyozinduliwa mwaka 2025 na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, haki ya umiliki wa ardhi kwa wote—wanaume na wanawake imewekewa usawa bayana,” amesema Mhandisi Sanga

Aidha amesisitiza kuwa katika sera hiyo mpya, masuala ya urithi na mirathi yameainishwa kwa kuzingatia usawa wa kijinsia, hivyo kuweka mazingira rafiki kwa wanawake kumiliki na kurithi ardhi bila ubaguzi.

"Kupitia Ardhi kliniki hiyo maalum, wanawake watapatiwa hati za umiliki wa ardhi, kusaidiwa kutatua migogoro ya ardhi pamoja na kupewa elimu kuhusu haki na taratibu za umiliki wa ardhi."amesema

Amesema mpango huo unalenga kuhakikisha changamoto zinazowakabili wanawake katika sekta ya ardhi zinatatuliwa kwa wakati, huku ukichochea ushiriki wao katika shughuli za kiuchumi na maendeleo ya familia na taifa kwa ujumla.

Hata hivyo amewataka kuwa watulivu wakati zoezi hilo likiendelea ili waweze kuhudumiwa kikamilivu na kwa weledi.

Kwa upande wake, Mthamini Mkuu wa Serikali wa Wizara hiyo, Bi. Evelyn Baruti Mugasha, amesema hadi majira ya mchana wanawake zaidi ya 160 walikuwa wamejitokeza kupata hati, huku wengine wakiendelea kujitokeza.

Bi. Mugasha amewataka wanawake wa Mkoa wa Dodoma kutumia fursa ya kliniki hiyo kupata elimu, ushauri na huduma mbalimbali, huku akitoa wito kwa wanaume kutoa ushirikiano ili kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu.

“Kumwezesha mwanamke kumiliki ardhi ni hatua muhimu katika kuimarisha uchumi wa familia na taifa kwa ujumla,” amesema Bi. Mugasha.

Nao, wanachi wa Mkoa wa Dodoma wamempongeza Rais Samia  kwa kuwapa kipaumbele wanawake katika suala la hati ili kuhakikisha hawabaki nyuma.

Naye mkazi wa Chidachi, Bi. Veronica Hamisi, amesema amefurahi kupata hati aliyokuwa akiifuatilia kwa takribani miaka mitatu ndani ya siku moja.

Kwa upande wake, mkazi wa Miyuji, Getruda Mathias, amesema amehangaika kwa miaka mitano kupata hati, lakini anamshukuru Rais kwa kutoa kipaumbele kwa wanawake kilichomwezesha kupata hati ndani ya saa moja bila usumbufu.

“Nawasihi wanawake wenzangu tujitokeze kwa wingi kuchangamkia fursa hii ambayo itahitimishwa Machi 7 mwaka huu,” amesema.

Mkazi wa Ilazo, Zena Hamis, pia amemshukuru Rais kwa kuwapa kipaumbele wanawake na kuwasihi wale ambao bado hawajajitokeza kufanya hivyo ili kunufaika na huduma hiyo.

TANZANIA NA GHANA KUIMARISHA USHIRIKIANO KIUCHUMI, AJIRA KWA VIJANA

March 02, 2026 Add Comment


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Dramani Mahama mara baada ya kuwasili katika Ikulu Ndogo ya Arusha tarehe 02 Machi, 2025. Rais wa Ghana Mhe. Mahama amewasili Mkoani Arusha kwa ajili ya Ziara ya Kikazi, ambapo anatarajiwa kuwa mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Mwaka mpya wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, na Sherehe za kumbukizi ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Mahakama hiyo mwaka 2006.

…………….

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amefanya mazungumzo ya pande mbili na Rais wa Jamhuri ya Ghana, Mheshimiwa John Dramani Mahama, yaliyofanyika Ikulu jijini Arusha, yakilenga kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika masuala ya uchumi, ajira kwa vijana na maendeleo ya uchumi wa kidijitali.

Akizungumza kuhusu mazungumzo hayo, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Bakari S. Machumu, amesema viongozi hao wamejadili kwa kina namna ya kuongeza thamani ya rasilimali za ndani ili kukuza uchumi wa mataifa yao badala ya kuendelea kuuza malighafi.

“Marais wamekubaliana kuwa wakati umefika kwa nchi za Afrika kuwekeza zaidi katika uchakataji na kuongeza thamani ya mazao na rasilimali zao, hatua itakayoongeza mapato ya ndani na kuzalisha ajira kwa vijana,” amesema Machumu.

Kwa mujibu wa Machumu, Rais wa Ghana, John Dramani Mahama, ameeleza uzoefu wa nchi yake katika kuimarisha usimamizi wa sekta ya madini na kakao, akisisitiza umuhimu wa sera madhubuti za ndani zinazolenga kukuza uchakataji wa bidhaa hizo kabla ya kuzipeleka katika masoko ya kimataifa.

Kwa upande wake, Rais Samia Suluhu Hassan amesema Tanzania inaendelea kuharakisha mkakati wa uchumi wa viwanda, ikiwemo kuongeza thamani ya mazao ya kimkakati kama pamba na kuimarisha uchakataji wa madini, huku akibainisha kuwa uzoefu wa Ghana ni muhimu katika safari hiyo.

Machumu amesema suala la ajira kwa vijana limepewa kipaumbele katika mazungumzo hayo, ambapo viongozi hao wamekubaliana kuongeza ushirikiano katika maendeleo ya ujuzi, ubunifu na ujasiriamali ili kuweka mazingira bora ya uwekezaji yatakayozalisha ajira endelevu kwa vijana.

Katika eneo la uchumi wa kidijitali, Rais Dkt. Samia amesisitiza dhamira ya Tanzania ya kuimarisha mifumo ya fedha za kidijitali na usalama wa mitandao kama sehemu ya mkakati wa kujenga uchumi shindani na jumuishi. Ameeleza kuwa Tanzania inaendelea kuwekeza katika miundombinu ya TEHAMA na kukuza ubunifu wa vijana, huku akitaja sekta ya teknolojia ya fedha ya Ghana kama eneo muhimu la kujifunza na kushirikiana.

Aidha, viongozi hao wamepongeza hatua ya kuimarishwa kwa safari za Shirika la Ndege la Air Tanzania Company Limited> (ATCL) kati ya Tanzania na Ghana, wakisema hatua hiyo itarahisisha biashara, utalii na mwingiliano wa watu, na kuchochea biashara ndani ya Bara la Afrika.

Rais wa Ghana yupo nchini kwa ziara ya kikazi ya siku moja. Leo, tarehe 02 Machi, 2026, anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Mwaka wa Mahakama na Maadhimisho ya Miaka 20 ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu yenye makao makuu jijini Arusha.



R

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Dramani Mahama, katika Ikulu Ndogo ya Arusha tarehe 02 Machi, 2025. Rais wa Ghana Mhe. Mahama amewasili Mkoani Arusha kwa ajili ya Ziara ya Kikazi, ambapo anatarajiwa kuwa mgeni Rasmi katika Ufunguzi wa Mwaka mpya wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, na Sherehe za kumbukizi ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Mahakama hiyo mwaka 2006.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa na Rais wa Jamhuri ya Ghana Mhe. John Dramani Mahama mara baada ya mazungumzo yao katika Ikulu Ndogo ya Arusha, tarehe 02 Machi, 2025.

NYUMBU NA MSEMO WA "TAHADHARI NA ADUI KIUMBE

March 02, 2026 Add Comment


 


Msanii kutoka Zanzibar Bi Fatma Issa aliimba tahadhari na adui kiumbe, daima asikusibu na Mungu akuepushie.


Nyumbu wakiwa wanazaliwa katika eneo la Ndutu huomba sana Mungu awaepushie adui kiumbe kama Fisi, Simba, chui na mbweha ambao nao msimu huo huhamia katika eneo la Ndutu hifadhi ya Ngorongoro ili kuwavizia Nyumbu na watoto wao.


Hata hivyo kwa kuwa  Mungu ni wa wote, huwaepusha nyumbu na adui hao kwa kuwa katika  safari ya nyumbu, kuanzia wanapozaliwa Ndutu na kuanza mzunguko wa kuhama kila mwaka kuelekea  Kenya, hukabiliana na changamoto nyingi za kuliwa na wanyama wala nyama lakini wengi husalimika.


Kila nyumbu mzima (adult) ni ushahidi wa ustahimilivu mkubwa kwamba alinusurika hatari wakati wa kuzaliwa, akapita salama katika mito yenye mamba na wanyama wanaokula Nyama (Predators) katika maisha ya kila siku. Kuishi hadi utu uzima kwa nyumbu ni matokeo ya ushindi dhidi ya vikwazo vingi vya asili vilivyojaa taabu, chuki, hila na madhila.

WAJUMBE WA KAMATI YA JPCDS WAJIONEA MAAJABU YA HIFADHI YA NGORONGORO

March 02, 2026 Add Comment




Wajumbe wa Kamati ya Wataalamu wa Kamisheni ya Kudumu ya Pamoja ya Ulinzi na Usalama (Joint Permanent Commission of Defense and Security – JPCDS) kutoka Tanzania na Zambia, wakiongozwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Patrobas Katambi pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani na Usalama wa Jamhuri ya Zambia Mhe. Jacob Jack Mwiimbu Februari 26, 2026 walipata fursa ya kutembelea na kujionea maajabu ya Hifadhi ya Ngorongoro wakati wakishiriki kikao cha siku tano Jijini Arusha kilicholenga kuimarisha ushirikiano katika kukabiliana na uhalifu unaovuka mipaka na matishio yanayoibukia.


Ziara hiyo ilikuwa sehemu ya kuimarisha uelewa wa pamoja kuhusu umuhimu wa kulinda rasilimali za asili kama sehemu ya ajenda ya usalama wa kikanda.


Kote duniani inafahamika kuwa, Ngorongoro ni hifadhi ya kipekee duniani, iliyotokana na kaldera bonde kubwa la volkano lililosababishwa na mlipuko na kuporomoka kwa volkano kubwa takribani miaka milioni 2 hadi 3 iliyopita.


Ambapo unapoteremka ndani ya kreta yake, unashuka hadi kina cha takribani mita 600 na kujikuta katika eneo lenye ukubwa wa zaidi ya kilomita za mraba 260, likiwa limezungukwa na kuta za asili zinazovutia na kuhifadhi mfumo wake wa ikolojia.


Aidha, wakiwa ndani ya kreta hiyo, wajumbe hao waliona mandhari ya kuvutia ya nyanda pana za majani, misitu midogo na mabwawa ya maji, likiwemo bwawa la chumvi maarufu kama Lake Magadi.


Upekee wa eneo hili unalifanya kuwa kreta kamili na kubwa zaidi duniani isiyojaa maji wala kuvujisha maji, huku ikiwa na mkusanyiko mkubwa wa wanyamapori wanaoishi kwa kudumu ndani yake.


Maajabu ya Ngorongoro hayaishii kwenye mandhari na wanyamapori pekee. Eneo hili ni miongoni mwa hifadhi chache duniani ambapo binadamu, hususani jamii ya Wamasai wanaishi kisheria na kuchunga mifugo yao sambamba na wanyamapori.


Itakumbukwa kuwa, Mwaka 1959 eneo hilo lilitengwa rasmi kama hifadhi mchanganyiko ya wanyamapori na makazi ya watu na mwaka 1979 likatangazwa kuwa Urithi wa Dunia na UNESCO kutokana na thamani yake ya kipekee ya asili na kihistoria.


Vilevile, hifadhi ya Ngorongoro iko karibu na Olduvai Gorge, eneo maarufu kama chimbuko la binadamu, lililotoa ushahidi muhimu wa kale kuhusu historia ya mwanadamu. Hivyo, pamoja na kuwa kivutio cha utalii, pia ni hazina ya tafiti za kisayansi na urithi wa kihistoria wa dunia.


Kutokana na wingi na utofauti wa wanyamapori, wataalamu hao wa sekta ya ulinzi na usalama walipata fursa ya kuona wanyama mbalimbali wakiwemo, tembo, simba, nyati, nyumbu, viboko, pundamilia, swala, digidigi, ngiri, mbweha, fisi na ndege wa aina mbalimbali. Uwepo wa wanyamapori hao kwa wingi ndani ya kreta moja ni kielelezo cha mafanikio ya juhudi za uhifadhi zinazoendelea kufanywa na mamlaka husika.


Ziara hiyo imeongeza hamasa kwa wajumbe hao kuimarisha ushirikiano katika kupambana na uhalifu unaovuka mipaka, hususan uhalifu dhidi ya maliasili. Wametambua kuwa kulinda urithi wa kipekee tuliyo rithishwa katika mataifa yetu ni jukumu la pamoja kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho, wakienzi maono ya waasisi wa mataifa yao, Julius Kambarage Nyerere na Kenneth Kaunda, waliothamini mshikamano wa kikanda na uhifadhi wa rasilimali za taifa.

DED MANISPAA YA SHINYANGA ATUNIKIWA SHAHADA YA HESHIMA YA UDAKTARI,ATEULIWA BALOZI WA AMANI DUNIANI

March 02, 2026 Add Comment


Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said 'kushoto', akimkabidhi cheti Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kaganze, alipotunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara kutoka Christian Ministerial Training University (CMTU) ya nchini Zambia katika hafla iliyofanyika Februari 28, 2026 Mkoa wa Shinyanga. Kulia ni Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe.

...................................

Na Dotto Mwaibale, Shinyanga

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Alexius Revocatus Kaganze, ametunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara kutoka Christian Ministerial Training University (CMTU) ya nchini Zambia.

Mbali na tuzo hiyo, pia ameteuliwa kuwa Balozi wa Amani Duniani (Peace Ambassador – AMB) na Greenling Peace Foundation kwa kutambua mchango wake katika kuhimiza amani, mshikamano na maendeleo ya kijamii.

Tuzo hizo zilitolewa Februari 27, 2026, mkoani Shinyanga katika maadhimisho ya Siku ya Amani na Upendo Duniani yaliyofanyika kitaifa, yakihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wanaharakati wa amani na wageni kutoka ndani na nje ya nchi. Maadhimisho hayo yaliandaliwa na Umoja wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO).

Mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said, ambaye alisema amani ni nguzo kuu ya maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kiutamaduni.

Alieleza kuwa UNESCO ilianzishwa baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia kwa lengo la kujenga utamaduni wa amani kupitia elimu, sayansi na utamaduni, ili kuzuia migogoro na kuhakikisha dunia inabaki katika mshikamano wa kudumu.

“Tunampongeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga kwa uteuzi wake wa kuwa Balozi wa Amani. Hii ni ishara kuwa viongozi wa ngazi zote wana wajibu wa kueneza ujumbe wa amani, uvumilivu na mshikamano wa kitaifa,” alisema Dkt. Said.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe, alisema wakati dunia ikiadhimisha siku ya amani, Mwalimu Kaganze ametambuliwa kwa juhudi zake za kuunganisha jamii kupitia haki na umoja.

Alisema shirika hilo linafanya kazi katika zaidi ya mataifa 30 likilenga kuinua kizazi cha viongozi wenye maono ya kuleta amani endelevu.

Naye Profesa Stephano Nzowa wa African Graduate University alisema Tanzania imejijengea sifa ya kuwa “Kisiwa cha Amani,” hivyo ni wajibu wa kila Mtanzania kuilinda na kuienzi amani hiyo kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Safari ya Utumishi wa Miaka 15

Mwl. Alexius Kaganze alizaliwa Machi 3, 1986, na kwa zaidi ya miaka 15 amelihudumia Taifa katika nyadhifa mbalimbali serikalini, zikiwemo:

Mwalimu

Afisa Elimu Mkuu, Ofisi ya Rais – TAMISEMI

Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga (kuanzia 2021)

Mchango Wake Katika Sekta Mbalimbali

1. Elimu:

Amehimiza ubora wa elimu, akisisitiza walimu kuwa nguzo ya maarifa, maadili na ujenzi wa amani. Amesimamia ujenzi wa madarasa, mabweni na miundombinu ya shule za msingi na sekondari, pamoja na kuhakikisha utekelezaji sahihi wa sera ya elimu bila malipo.

 

2. Ajira na Uwezeshaji Vijana:

Amekuwa mstari wa mbele kuhimiza nidhamu ya kazi, maadili na kujiajiri kwa vijana, huku akisimamia miradi ya miundombinu inayochochea uchumi wa manispaa.

3. Biashara:

Amehamasisha utoaji wa mitaji kwa wafanyabiashara wadogo na kukutana na wadau wa sekta ya nyumba za kulala wageni ili kuboresha huduma na kukuza uchumi wa eneo hilo.

5. Michezo:

Ameunga mkono michezo kama chachu ya kukuza vipaji, afya na nidhamu kwa vijana.

6. Miundombinu:

Amesimamia miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa barabara za lami zenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 1.6, kituo kipya cha mabasi Katunda, pamoja na miradi ya elimu na afya yenye thamani ya mabilioni ya shilingi.

Katibu Mkuu wa TAMUFO, Stella Joel ndiye aliyemuibua Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga baada ya kupewa taarifa kuhusu anavyojitoa kwa jamii kuwatumikia baada ya hapo ulianza mchakato wa kujua jinsi anavyofanya kazi na hatimaye kutambulika na kutunukiwa shahada hiyo ya udaktari wa heshima.

“Tuzo ambazo amepata nataka kuwahakikishiaWanashinyanga na Watanzania kwa ujumla wao kuwa tumepata mtu ambaye atalisaidia taifa hivyo tumuombee kwani watu wa namna yake ni wachache,” alisema Joel.

Mkazi wa Shinyanga kwa zaidi ya miaka 20, Charles Luchagula, alisema mkurugenzi huyo amekuwa karibu na jamii kwa kusaidia mikopo kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu, pamoja na kuchangia maendeleo ya shule na michezo.

Kwa upande wake, Daud Moses, mmiliki wa Hope Conscious Pre and Primary School, alisema alipata msaada wa haraka katika mchakato wa usajili wa shule yake baada ya kuwasiliana na ofisi ya mkurugenzi huyo.

Akizungumza baada ya kutunukiwa tuzo hiyo, Dkt. Kaganze alishukuru CMTU kwa kutambua mchango wake akiwa hai, akisema tuzo hiyo itamhamasisha kuongeza bidii katika kuwatumikia wananchi.

“Tuzo hii inanipa nguvu mpya ya kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu na kujituma zaidi kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Shinyanga na Taifa kwa ujumla,” alisema.

Kwa ujumla, tuzo hiyo ni uthibitisho wa mchango wake katika kuimarisha utawala bora, kuhamasisha amani na kusimamia maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika Manispaa ya Shinyanga.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kaganze, akionesha cheti baada ya kutunukiwa tuzo hizo.

Profesa Stephano Nzowa wa African Graduate University, akimvika kofia ikiwa ni ishara ya kumtunuku Mwalimu Dkt. Alexius Revocatus Kaganze, alipotunukiwa Shahada ya Heshima ya Udaktari (Honoris Causa) katika Ustawi wa Jamii na Uongozi wa Biashara. 

Mwenyekiti Mwanzilishi wa Greeling Global Peace Organization na mmiliki wa CMTU, Profesa Askofu Kennedy Songwe, akimpongeza Mwalimu Dkt. Kaganze.

Mwalimu Dkt. Kaganze akiwapungia mkono wananchi wa Manispa ya Shinyanga 'hawapo pichani wakati alipokuwa akienda kutunukiwa tuzo hizo'
Mwalimu Dkt. Kaganze akiwa kwenye gari maalumu wakati akielekea ukumbi wa Level One kutunukiwa tuzo hizo.

Picha ya pamoja.

Wapiga matarumbeta wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania 'KKKT' Mkoa wa Shinyanga wakinoesha hafla hiyo.


Ndugu , jamaa na marafiki wa Mwalimu Dkt. Kaganze wakiwa kwenye hafla hiyo.
Mwalimu Mlemwa Msusi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Shinyanga akitafsiri kwa vitendo mambo mbalimbali yaliyokuwa yakiendelea katika hafla hiyo kwa ajili ya wenzetu wenye usikivu hafifu.
Viongozi mbalimbali wakiwa meza kuu.
Wadau wakiwa kwenye hafla hiyo.
Bi. Editha Alex akiwa na mtoto wake, Joleene Joel kwenye hafla hiyo.
Ndugu zake Mwalimu Kaganze wakiwa kwenye hafla hiyo. Kutoka kushoto ni Mwalimu Autalia Sukari, Beatrice George na Linda Joel.
Viongozi wakiwa meza kuu.
Katibu Mkuu wa TAMUFO, Stella Joel akionesha furaha kwenye hafla hiyo. Kushoto ni Mlezi wa TAMUFO, Dkt. Frank Mbuli.. 
Afisa Program wa Tume ya Taifa UNESCO, Edelfrida Tibaija 'kushoto' akiwaelekeza jambo Mlezi wa TAMUFO na Katibu wa TAMUFO, Stella Joel katika hafla hiyo.
Katibu wa TAMUFO, Stella Joel akiteta jambo na Mwenza wake Mwalimu Dkt. Kaganze, Safina Kaganze.
Mmoja wa uratibu wa hafla hiyo, Joel Komba,  akipokea maelekezo ya viongozi katika hafla hiyo
Mwalimu Dkt. Kaganze akiteta jambo na Mwenza wake Safina..
Naibu Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya UNESCO, Dkt. Khamis Said akiwasalimia washiriki wa hafla hiyo.
Mwimbaji wa Nyimbo za Injili, Nesta Sanga, akiwavika Beji maalumu washiriki wa hafla hiyo.
Mwimbaji wa Nyimbo za Injili Nesta Sanga, akimvika beji maalumu Balozi wa Amani, Mess Chengula ambaye pia ni kiongozi wa wchimba madini.
Nesta aakiendelea na kuwavika Beji Maalumu washiriki katika hafla hiyo

Mama mzazi wa Mwalimu Dkt. Kaganze Christina Gafisa akivikwaa beji maalumu
Baba Mzazi wa Mwalimu Dkt. Kaganze Mathias Fungamake, akivikwa Beji.
Mama Mkwe wa Mwalimu Dkt. Kaganze akivikwa Beji.
Afisa Program wa Tume ya Taifa UNESCO, Edelfrida Tibaija akivikwa Beji.
Mkurugenzi wa Maalula TV, Daniesa Malula, akionesha furaha yake wakati wa hafla hiyo.
Mratibu wa hafla hiyo Dkt. Christina Ngereza akizungumza katika hafla hiyo.
Mwalimu Luhunga akizungumzia kazi mbalimbali alizofanya Balozi Dkt. Kaganze
Daud Moses, mmiliki wa Hope Conscious Pre and Primary School, akizungumza.
Katibu wa TAMUFO Stella Joel akizungumza.
Ndugu waa Mwalimu Dkt. Kaganze wakiwa katika foleni ya kwenda kumpongeza ndugu yako kwa kutunukiwa tuzo