HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

MRADI WA EACOP UMETOA ZAIDI YA AJIRA 3,000 MKOANI SINGIDA-MHE.SALOME

June 13, 2026 Add Comment




Iramba, Singida


Zaidi ya ajira 3,000 zimetolewa mkoani Singida kupitia utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), huku wananchi wakinufaika pia kwa kutoa huduma mbalimbali ikiwemo kuuza vyakula, kukodisha vyombo vya usafiri na kutoa huduma nyingine zinazohitajika wakati wa utekelezaji wa mradi huo, hatua inayochangia kuongeza kipato kwa jamii zinazouzunguka mradi.


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema hayo leo Juni 13, 2026 wilayani Iramba mkoani Singida wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba.

Amesema dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha kuwa Mradi wa EACOP hauwi tu mradi wa kukuza uchumi wa nchi bali unakuwa chachu ya kubadilisha maisha ya wananchi mmoja mmoja kupitia fursa za ajira na biashara.

Katika hatua nyingine, Mhe, Salome amesema kuwa ifikapo mwaka 2030 vitongoji vyote wilayani Iramba vitakuwa vimefikiwa na umeme ambapo kati ya vitongoji 393 vilivyopo tayari vitongoji 165 vina umeme na kwa sasa wakandarasi wanaendelea na kazi ya kusambaza umeme katika vitongoji 65.

Ameongeza kuwa Serikali  imetoa  shilingi milioni 285 kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wilayani humo ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi, mradi unaotarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu.


Vilevile amesema Serikali imetoa shilingi bilioni 1.085 katika mwaka huu wa fedha unaoisha kwa ajili ya maboresho ya miundombinu ya umeme wilayani Iramba, ikiwemo kupunguza urefu wa laini za umeme na kuongeza transfoma ili kuboresha upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi.


Kuhusu matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, Mhe. Salome  amesema Wilaya ya Iramba imepokea majiko banifu zaidi ya 1,000 na majiko ya gesi zaidi ya 2,000 ikiwa ni hatua za uhamasishaji wa nishati safi ya kupikia, huku akitoa wito kwa wanaume kuwaunga mkono wanawake kwa kununua na kuhamasisha matumizi ya majiko hayo ili kuwawezesha kina mama kupata muda zaidi wa kushiriki katika shughuli za uzalishaji mali na maendeleo ya familia.

ADO AAHIDI UFANISI, UADILIFU NA UMADHUBUTI USIMAMIZI SEKTA ZA FEDHA NA MIPANGO

June 13, 2026 Add Comment




“Nimeupokea kwa unyenyekevu na hamasa uteuzi wa kuwa Msemaji wa Sekta ya Fedha, Mipango na Hifadhi ya Jamii wa Kamati ya Wasemaji wa Kisekta ya ACT Wazalendo. Wajibu wangu ni kuzisimamia Wizara za Fedha chini ya Balozi Hamis Mussa Omar na Wizara ya Mipango na Uwekezaji chini ya Prof. Kitila Mkumbo. 

Wizara hizi zimebeba taasisi nyeti kama vile Benki Kuu ya Tanzania na Sekta ya Benki kwa Ujumla wake, Hazina, TRA, Taasisi ya Manunuzi ya Umma (PPRA), TISEZA na Taasisi nyinginezo katika tasnia ya fedha na mipango.

Ninamshukuru Kiongozi wa Chama Ndugu Dorothy Semu kwa uteuzi huu. Nitatekeleza wajibu wangu kwa ufanisi, uadilifu na umadhubuti”- Ado Shaibu Ado.

OFISI YA WAZIRI MKUU NA OMDTZ ZAIMARISHA UTAYARI WA JAMII KUKABILIANA NA MAFURIKO DAR ES SALAAM

June 13, 2026 Add Comment




Na, mwandishi wetu - Dar es Salaam

Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi OpenMap Development Tanzania (OMDTZ), kupitia mradi wa Ramani Zetu, Sauti Zetu imeendesha warsha ya kupitia na kuthibitisha Mipango ya Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa kwa kata tano za Makurumula, Mabibo, Keko, Ubungo na Tabata jijini Dar es Salaam.


Warsha hiyo imewakutanisha viongozi wa serikali za mitaa, Kamati za Usimamizi wa Maafa za Kata, wataalamu wa usimamizi wa maafa, waratibu wa maafa wa mkoa na wilaya pamoja na wadau mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha mipango hiyo inakidhi mahitaji halisi ya jamii zinazokabiliwa na hatari ya mafuriko Dar es Salaam.


Akifungua warsha hiyo Mkurugenzi Msaidizi wa Operesheni za Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Kanali Selestine Masalamado amesema kuwa ubora wa mpango wa maafa hupimwa kwa uwezo wake wa kutekelezeka na kuleta matokeo chanya kwa wananchi, huku akisisitiza umuhimu wa mipango hiyo kuzingatia mazingira halisi, rasilimali zilizopo na uwezo wa taasisi husika.


“Mradi huu unaofadhiliwa na Zayed Sustainability Prize kupitia Taasisi ya Open Map Development Tanzania (OMDTZ), kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – Idara ya Usimamizi wa Maafa, umekuja wakati sahihi na tunamatarajio makubwa katika kuleta matokeo chanya kuhakikisha tunaimarisha masuala ya usimamizi wa maafa nchini, ”alisema Kanali Masalamado


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa OMDTZ, Bw. Innocent Maholi, alisema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa kupitia matumizi ya teknolojia, uchoraji ramani shirikishi na uwekezaji katika mifumo ya tahadhari ya mapema katika maeneo hatarishi.


Naye Mratibu wa Maafa wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Gerald Sondo, amepongeza ushirikiano huo akieleza kuwa mipango hiyo itasaidia kuongeza utayari wa jamii, kuboresha uratibu wa mwitikio wa dharura na kupunguza athari za mafuriko katika Jiji la Dar es Salaam.


“Kwa kipindi cha miezi mitatu iliyopita, kamati za usimamizi wa maafa katika kata husika zimefanya tathmini ya vihatarishi, kubainisha njia za uokoaji na maeneo salama, kuandaa mifumo ya mawasiliano na uratibu pamoja na kupendekeza hatua za tahadhari ya mapema zinazoshirikisha jamii,”alisema Bw. Sondo.


Aliongezea kuwa, Mipango iliyothibitishwa itatumika kama mwongozo wa vitendo kwa jamii kabla, wakati na baada ya maafa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usalama wa wananchi na ustahimilivu dhidi ya mafuriko na majanga mengine.




KIMBE YAJIPANGA KUTENGENEZA MADAWATI 500

June 13, 2026 Add Comment

 


Na Amina Omari,Kilindi


Kata ya Kimbe wilayani Kilindi Mkoa wa Tanga imejipanga kutengeneza madawati 500 Ili kumaliza tatizo la upungufu wa madawati katika shule zilizopo kwenye kata hiyo.


Akiongea kuhusu mkakati huo na gazeti hili Diwani wa kata hiyo Mussa Kalamba alisema kuwa Kata hiyo yenye shule tisa za awali na msingi zina upungufu wa jumla ya madawati 825,huku Sekondari ya Kimbe ikikabiliwa na upungufu wa viti na meza 251.

Katika utekelezaji wa awamu ya kwanza, kata inatarajia kutengeneza madawati 500 kwa shule za msingi na viti 150 kwa Sekondari ya Kimbe ili kukabiliana na upungufu uliopo huku uongozi wa kata ukiendelea na mipango ya kuhakikisha wanaweka mipango ya kumaliza changamoto hiyo.


Kalamba alisema kuwa mpango huo uliokubaliwa katika vikao vya Kamati ya Maendeleo ya Kata (WDC), uongozi umeweka utaratibu wa kufuatilia upungufu wa madawati kila muhula wa masomo na kila mwaka wakati wa uandikishaji wa wanafunzi wapya.



"Lengo letu si tu kuziba pengo lililopo, bali tunataka kuhakikisha tuna ziada ya madawati katika shule zetu. Kwa kutumia idadi ya wanafunzi wanaoongezeka kila mwaka, tutakuwa na uwezo wa kubaini mapema upungufu na kuutatua kwa haraka kabla hali haijawa mbaya," alisema Diwani huyo.


Hata hivyo aliwataka, wananchi wake kuunga mkono juhudi hizi kwa kuchangia nguvu na rasilimali pindi wanaposhirikishwa na viongozi wa serikali za vijiji.


"Tunawaomba wananchi wetu waendelee kuonesha ushirikiano wao. Hii ni ajenda ya pamoja kwa mustakabali wa watoto wetu. Kila mchango wenu ni hatua kuelekea mazingira bora ya kujifunzia," ilisisitiza Kalamba 


Utekelezaji wa mpango huu unatazamwa kama kielelezo cha uwajibikaji wa pamoja, ambapo serikali ya kata imejipanga kusimamia kwa karibu usimamizi wa rasilimali hizo ili kuleta matokeo chanya ya kudumu katika elimu ndani ya Kata ya Kimbe.

WATHIBITI UBORA WA SHULE WAASWA KUSIMAMIA KWA WELEDI MATUMIZI YA NeST

June 13, 2026 Add Comment

Wathibiti Ubora wa Shule nchini wametakiwa kusimamia kwa weledi matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) ili kuhakikisha manunuzi yote ya Serikali yanafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Rai hiyo imetolewa Juni 11, 2026 jijini Arusha na Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Fredrick Salukele, akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, katika ufunguzi wa mafunzo kuhusu matumizi ya Mfumo huo.

Dkt. Salukele amesema mafunzo hayo yatawawezesha washiriki kutumia mfumo huo kwa ufanisi katika usimamizi wa fedha za uchangiaji, ununuzi wa bidhaa na huduma mbalimbali pamoja na malipo ya shughuli za tathmini za shule.

Amewasisitiza washiriki kusimamia kwa ufanisi rasilimali zilizopo, ikiwemo rasilimali watu na miundombinu, sambamba na kuimarisha huduma bora za elimu.

Aidha, Dkt. Salukele amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri na Wathibiti Ubora wa Shule kuhakikisha taasisi za elimu zinazingatia taratibu zote za uendeshaji ikiwemo masuala ya malazi, chakula na usalama wa wanafunzi.

Naye, Miurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule kutoka Wizara hiyo Dkt. Ephrahim Simbeye amesisitiza uzingatiaji wa miongozo ya elimu, akitaka kukomeshwa kwa adhabu zisizokubalika na kuhakikisha kuna mazingira bora ya ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi.

Wakizungumza kuhusu mafunzo hayo, Bi. Lilian Kasenga Mthibiti Ubora kutoka Manispaa ya Temeke pamoja na Emmanuel Hangaya kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema, wametaja mbinu wanazotumia kufikia malengo huku wakisema mafunzo hayo yatakwenda kuwaongezea ufanisi kazini.









TANZANIA YAUNGA MKONO MKATABA MPYA WA KIMATAIFA WA KULINDA WAFANYAKAZI WA MTANDAONI

June 12, 2026 Add Comment
Na: OWM (KAM) – Geneva, Uswisi

Ujumbe wa Tanzania umeunga mkono Mkataba mpya wa Kimataifa unaolenga kulinda haki, usalama na ustawi wa Wafanyakazi wa Mtandaoni ikiwa ni dhamira ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuhakikisha maendeleo ya teknolojia na majukwaa ya kidijitali yanakwenda sambamba na ulinzi wa utu wa mfanyakazi, usawa na haki za msingi za kazi.

DCEA YAZINDUA FILAMU YA ‘KIFURUSHI’ KUIMARISHA ELIMU DHIDI YA USAFIRISHAJI WA DAWA ZA KULEVYA

June 12, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Tume ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imezindua filamu ya “Kifurushi” itakayooneshwa katika mabasi yanayosafiri mikoa mbalimbali nchini kwa lengo la kuongeza uelewa wa jamii kuhusu mbinu zinazotumiwa kusafirisha dawa za kulevya na madhara yatokanayo na vitendo hivyo.

NAIBU KATIBU MKUU UVUVI ATOA WITO KWA WATAALAM KUWA NA MBINU BORA ZA UTEKELEZAJI KATIKA PROGRAMU YA AFDP

June 12, 2026 Add Comment




Na; Mwandishi Wetu - Chato

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Profesa Mohammed Ali Sheikh, Ametoa wito kwa wataalam kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu kuwa na mbinu bora za kiutendaji zitakazowezesha programu hiyo kutekelezeka kwa kasi zaidi.

Ameyasema hayo Wilayani Chato Mkoani Geita Tarehe 12 Juni 2026 alipozungumza na wataalam wa programu wanaofanya kazi ya utekelezaji ya mapitio ya programu mara baada ya ziara yake maalum ya kutembelea kituo cha kuendeleza Ukuzaji viumbemaji cha Rubambagwe kilichopo Wilayani chato.

“Niwapongeze sana kwa kuchukua hatua za haraka baada na maagizo ya kikao cha Mawaziri kukaa pamoja kama wataaalamu na kuyafanyia kazi maagizo yale. Hii ni hatua muhimu sana inayoonesha ni kwa namna gani mnaweza kuwajibika kiutaalamu, mnapewa maelekezo na mnayatekeleza” Alisema.

Naibu Katibu Mkuu Sheikh alibainisha kuwa, kukutana kwa wataalamu hao ni hatua muhimu sana ya kukaa pamoja na kujaribu kujitathmini kuona kila kinachofanyika kinakwenda sawa ama vinginevyo, ‘’Niipongeze sana timu ya Uratibu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kuitisha kikao kazi hiki “Mnapoona kitu hakiendi hebu muitane muone namna ya kukifanyia kazi sisi kama watekelezaji wa Programu hii ni familia moja, Serikali ni moja na tunachotaka ni kufikia malengo na kumsaidia mtanzania katika kilimo na uvuvi kwa ukubwa wake” Alisisitiza

Alibainisha kuwa, kwa kufanya tathmini kunasaidia kujua wapi ulikwama na wapi pa kuboresha. Zaidi aliendelea alisema kuwa, kukua na kubadilika kwa teknolojia kufanya tathmini kunaweza kusaidia  kwenda mbele zaidi, “lazima tusaidianae tuje na mbinu bora za utekelezaji katika utendaji wa mradi msione aibu kushauri na kutoa mapendekezo ya kiutendaji kuhusiana na Programu.” Alisema


Akizungumza katika kikao kazi hicho, Mhandisi Enock Nyanda, Mkurugenzi msaidizi sehemu ya Sekta za Uchumi na Uzalishaji Idara ya Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) alisema lengo mahususi ya wataalam kukutana katika kikao kazi hicho ni kuongeza kasi ya utekelezaji wa Programu ili kufikia malengo.




ZFCT YARIDHISHWA NA MAFUNZO YA FCC KUHUSU USIMAMIZI WA MASHAURI YA USHINDANI

ZFCT YARIDHISHWA NA MAFUNZO YA FCC KUHUSU USIMAMIZI WA MASHAURI YA USHINDANI

June 12, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu

Baraza la Ushindani Halali Zanzibar (ZFCT) limefanya ziara ya mafunzo katika Tume ya Ushindani ya Haki (FCC) kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu katika masuala ya ushindani wa biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na usimamizi wa mashauri yanayohusiana na ushindani.

Ziara hiyo iliyofanyika katika ofisi za FCC Juni 10, 2026 Jijini Dar es Salaam, imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa ya haki kwa wadau wote.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa alisema kuwa kubadilishana uzoefu na taasisi za ndani ya nchi ni muhimu katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa ushindani na kulinda maslahi ya watumiaji dhidi ya vitendo vinavyokiuka sheria za ushindani na biashara.

Alisema ujumbe wa ZFCT unapata fursa ya kujifunza namna FCC inavyotekeleza majukumu yake ya kudhibiti vitendo vya ushindani usio wa haki, kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia pamoja na mifumo ya uchunguzi na uendeshaji wa mashauri mbalimbali yanayofikishwa mbele ya taasisi hiyo.

Kwa upande wake, ujumbe wa ZFCT ukiongozwa na Msajili wa Baraza, Bi. Fatma Yahya alieleza kuridhishwa na mafunzo na uzoefu uliopatikana katika ziara hiyo, ukibainisha kuwa utaisaidia taasisi hiyo kuimarisha utendaji wake katika kushughulikia rufaa na mashauri yanayohusiana na ushindani wa biashara Zanzibar.

ZFCT ni chombo kinachoshughulikia mashauri na rufaa zinazotokana na maamuzi ya mamlaka za ushindani, ambapo wadau wasiokubaliana na maamuzi yaliyotolewa huwasilisha kesi zao kwa ajili ya kusikilizwa na kutolewa uamuzi.

Ziara hiyo pia ilitoa nafasi kwa wataalamu kutoka pande zote mbili kujadiliana changamoto na fursa zilizopo katika usimamizi wa ushindani wa biashara, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana katika kujenga uwezo wa kitaasisi na kuimarisha utekelezaji wa sheria zinazolinda ushindani wa haki katika soko.

USHIRIKIANO WA WADAU NI MUHIMU KUFIKIA LENGO LA NISHATI SAFI YA KUPIKIA LA 2034"- MHE. SALOME

June 12, 2026 Add Comment



Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Tanzania imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa agenda ya nishati safi ya kupikia, ambapo upatikanaji wa huduma hiyo umeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025.


Amesema mafanikio hayo yametokana na uongozi thabiti wa Serikali, ushirikiano wa wadau wa maendeleo, sekta binafsi na kuongezeka kwa uelewa wa jamii kuhusu matumizi ya nishati safi.


Akifungua rasmi Mkutano wa Wadau wa Nishati Safi ya Kupikia 2026 uliofanyika Arusha leo Juni 10,2026 Mhe. Salome amesema Serikali imejipanga kufikia lengo la asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034 kupitia utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024–2034.


‘Miradi mbalimbali imechangia mafanikio hayo ikiwemo usambazaji wa mitungi 452,445 ya LPG, majiko banifu 200,000, pamoja na utekelezaji wa mradi wa CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya kupitia UNCDF, ambao umewezesha kaya zaidi ya 634,000 kupata huduma za nishati safi ya kupikia katika mikoa mbalimbali nchini’.


Pia amewataka wadau wote kuendelea kushirikiana ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata nishati safi, salama na nafuu ya kupikia, huku akisisitiza kuwa agenda hiyo ni muhimu kwa afya, mazingira, uchumi wa kaya na maendeleo endelevu ya Taifa.


Mkutano huo ulioandaliwa na UNCDF ukiwa na kwa lengo la kujadili maendeleo, fursa na mikakati ya kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini Tanzania.





WAKULIMA WA PAMBA IGUNGA WAJITOKEZA KWA WINGI KUFUNGUA AKAUNTI

WAKULIMA WA PAMBA IGUNGA WAJITOKEZA KWA WINGI KUFUNGUA AKAUNTI

June 12, 2026 Add Comment

Wakulima wa zao la pamba kutoka vijiji vya Mbutu, Iyogelo, Ilambakuki, Imalanguzu na Mwamakoma vilivyopo katika Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora, wamehamasika kufungua akaunti za benki na kusajili laini za simu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea malipo ya mazao yao kwa njia ya kidijitali. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi, usalama na uharaka wa malipo kwa wakulima.

Wakulima hao wamefungua akaunti kupitia Benki ya NMB pamoja na kusajili laini kupitia mtandao wa simu wa Mixx by Yas, hatua itakayowawezesha kupokea fedha zao kwa urahisi kupitia mifumo ya benki na huduma za kifedha za simu za mkononi.

Zoezi hilo limefanyika kwa kushirikiana na AMCOS za Ngw'ajojabi, Ngw'asabi na Mwamakoma AMCOS, likitekelezwa kufuatia waraka wa Mrajis wa Vyama vya Ushirika unaoelekeza malipo ya wakulima wa pamba kufanyika kupitia akaunti za benki na huduma za fedha kwa njia ya simu badala ya kutegemea fedha taslimu. Lengo ni kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati, kwa uwazi na kwa usalama zaidi.

Mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka siku hadi siku kufuatia juhudi za uhamasishaji zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali. Hadi kufikia Juni 10, 2026, jumla ya wakulima 506 wamejitokeza na kufungua akaunti pamoja na kujiunga na huduma za kifedha za simu, hatua inayoonesha uelewa na utayari mkubwa wa wakulima kupokea mabadiliko ya mfumo wa malipo ya kidijitali.

Aidha, uhamasishaji wa zoezi hilo umefanywa na Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Tabora, Peja Mhoja pamoja na Mrajis Msaidizi (Uhamasishaji), Ibrahim Kadudu, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wakulima kujiunga na mifumo rasmi ya kifedha ili kunufaika na malipo ya kisasa, salama na yenye tija.