HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

DC NYAMWESE: RAIS SAMIA ANAWATUA NDOO KICHWANI WANAWAKE WA HANDENI

DC NYAMWESE: RAIS SAMIA ANAWATUA NDOO KICHWANI WANAWAKE WA HANDENI

March 08, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu

MKUU wa Wilaya ya Handeni, Salum Nyamwese, amesema Rais Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuwatua ndoo kichwani wanawake wa Handeni kupitia utekelezaji wa mradi wa maji wa miji 28 ambao umefikia zaidi ya asilimia 75 ya utekelezaji.

Mradi huo unaogharimu Dola za Marekani 81,142,931 unatekelezwa na mkandarasi M/s Jwil Infra Limited kutoka India na unatarajiwa kuhudumia zaidi ya wakazi 870,629 kutoka vijiji 161 vya wilaya za Handeni, Korogwe, Muheza na Pangani.

Nyamwese ametoa kauli hiyo wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika katika Halmashauri ya Mji Handeni chini ya kaulimbiu isemayo “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Amesema mradi huo utakuwa mkombozi kwa wanawake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakitumia muda mwingi kutafuta maji.

“Niwahakikishie msikae kinyonge mkajiona nyie ni dhaifu. Serikali imewasikia na tatizo hili la maji litatatuliwa hivi karibuni… hata yale mnayosema kina mama wanashindwa kusuka nywele vizuri kwa sababu ya maji, watasuka na tutawaona,” amesema.

Nyamwese amesema serikali chini ya uongozi wa Rais Samia imeendelea kuweka mazingira rafiki ya kumuwezesha mwanamke kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo kupitia sera, sheria na mipango mbalimbali.

Amebainisha kuwa Rais Samia pia alitoa maelekezo ya kuboreshwa kwa utoaji wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu baada ya kubaini awali kulikuwa na changamoto katika utoaji wake.

“Mheshimiwa Rais alielekeza halmashauri kuweka utaratibu mzuri wa utoaji wa mikopo hii ili kuhakikisha makundi haya yanapata fursa ya kujikwamua kiuchumi,” amesema.

Ameongeza kuwa Wilaya ya Handeni imeendelea kushuhudia maendeleo ya wanawake katika shughuli za kiuchumi zikiwamo ujasiriamali, kilimo na ufugaji.

Kuhusu kupambana na ukatili wa kijinsia, Nyamwese amesema serikali inaendelea kutoa elimu kwa jamii ili kuheshimu utu wa mwanamke na kumpa mtoto wa kike nafasi sawa katika fursa mbalimbali.

“Changamoto ya ndoa za utotoni, mimba za utotoni na mila potofu zinazokwamisha maendeleo ya mwanamke, ikiwamo umiliki wa ardhi, serikali imeendelea kuzishughulikia,” amesema.

Amewataka viongozi wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi la Halmashauri ya Mji Handeni kuandaa mpango maalum wa kutoa elimu kwa wanawake ili kuwajengea uwezo wa kutumia fursa zilizopo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Handeni, Maryam Ukwaju, amesema halmashauri imejipanga kuhakikisha wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi ili kufikia malengo ya Dira 2050.

Amesema hadi mwisho wa Machi 2026 halmashauri inalenga kusajili angalau vikundi 50 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika mfumo wa NEST ili vinufaike na miradi inayotekelezwa katika eneo hilo.

Awali akisoma risala ya wanawake wa halmashauri hiyo, Carin Umwambe, amesema ukosefu wa maji umekuwa ukisababisha wanawake kutumia muda mwingi kutafuta maji badala ya kujishughulisha na shughuli za maendeleo na kuiomba serikali kuharakisha upatikanaji wa huduma hiyo.

WAZAZI NA WALIMU WATAKIWA KUSHIRIKIANA KUJENGA TAIFA LENYE MAADILI

March 07, 2026 Add Comment

Afisa Utamaduni wa Manispaa ya Kahama, Martha Kapela akizungumza na wanawake juu ya majukumu ya wanawake katika malezi, elimu ya maadili, na utunzaji wa familia huku akiwahimiza walimu kushirikiana katika malezi ya watoto shuleni.


Na Neema Nkumbi, Kahama

Afisa Utamaduni wa Manispaa ya Kahama, Martha Kapela, amesema mwanamke ndiye chanzo cha maadili katika jamii, huku akieleza kwamba yeye ndiye mlezi na msimamizi wa kwanza wa maadili nyumbani.
DKT. AKWILAPO: MSITOE MAAMUZI YA KUWAFURAHISHA WATU

DKT. AKWILAPO: MSITOE MAAMUZI YA KUWAFURAHISHA WATU

March 07, 2026 Add Comment



Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt Leonard Akwilapo akizungumza wakati wa kuapishwa kwa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026.Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi akimuapisha mmoja wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026

Na Munir Shemweta, WANMM MTWARA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Leonard Akwilapo ameshuhudia uapisho wa wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya na kuwataka wajumbe hao kutenda haki kuacha kutoa maamuzi ya kuwafurahisha watu wakati wa kusikiliza mashauri ya ardhi.

Uapisho huo umeongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Donald Wilson Msengi, na kufanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.

Akizungumza mara baada ya kushuhudia uapisho huo, Dkt. Akwilapo aliwaasa wajumbe wa mabaraza hayo kuepuka kutoa maamuzi kwa lengo la kuwafurahisha watu au makundi fulani, badala yake wafanye maamuzi yanayozingatia haki na sheria ili kupunguza migogoro ya ardhi katika jamii.

Alisema wajumbe wanapaswa kutambua kuwa nafasi waliyopewa ni dhamana kubwa kutoka kwa Mungu na Serikali, hivyo wanatakiwa kuitumia kwa uadilifu, uaminifu na kwa kuzingatia misingi ya haki.

“Napenda mtambue kuwa nafasi mlizopewa ni kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu, hivyo mheshimu Mungu kwa kufanya maamuzi yanayoendana na haki na uadilifu,” alisema Dkt. Akwilapo.

Aliongeza kuwa, kazi ya kushughulikia mashauri ya ardhi si rahisi, kwani mara nyingi huwa na pande mbili zinazopingana, lakini wajumbe wanapaswa kufanya maamuzi kwa kuzingatia ushahidi na sheria ili haki ipatikane kwa anayestahili.

“Sina wasiwasi na ninyi, ingawa kazi ni ngumu, lakini mfanye maamuzi kwa kuzingatia haki na siyo kumfurahisha mtu,” alisisitiza.

Dkt. Akwilapo pia alisema uimarishaji wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi kwa kusogeza huduma hizo karibu zaidi na wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Msengi aliwapongeza wajumbe hao kwa kuaminiwa kushika nafasi hizo na kuwataka kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia viapo walivyokula na kufanya kazi kwa weledi.

Amesema, wajumbe wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya ni kiungo muhimu katika mfumo wa utatuzi wa migogoro ya ardhi, hivyo wanapaswa kufanya kazi kwa uadilifu ili kujenga imani kwa wananchi.

“Uwepo wa wajumbe wa mabaraza ya ardhi katika wilaya zenu sasa utawezesha wananchi kupata huduma karibu zaidi badala ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hizo,” alisema.

Ameongeza kuwa, hatua hiyo itasaidia kupunguza gharama na muda ambao wananchi walikuwa wakitumia kufuata huduma za utatuzi wa migogoro ya ardhi katika maeneo ya mbali.

Wajumbe walioapishwa wanatoka katika wilaya za Mtwara, Tandahimba, Newala pamoja na wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara.

Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeendelea kuimarisha Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya wilaya ili kuongeza ufanisi katika kusikiliza na kutatua migogoro ya ardhi kwa wakati, jambo litakalosaidia kuimarisha usalama wa milki na kuleta utulivu katika jamii.

WAZIRI NDEJEMBI ATOA SIKU 14 KWA MKANDARASI KUREJEA MRADI WA UMEME SONGEA-MAHUMBIKA

March 07, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu, Tunduru


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amempa siku 14 mkandarasi anayetekeleza mradi wa kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Mahumbika kupitia Tunduru na Masasi kurejea eneo la mradi na kuendelea na kazi mara moja.

Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi huo unaotekelezwa na kampuni ya Kalpataru Projects International Limited, ambayo ina jukumu la kujenga vituo vya kupoza umeme katika wilaya za Tunduru, Masasi na Mahumbika.

Akitoa agizo hilo Machi 7, 2026 wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, Ndejembi amesema mkandarasi huyo hapaswi kupewa kazi nyingine yoyote ya serikali hadi atakapokamilisha mradi huo ambao utekelezaji wake umechelewa kinyume na masharti ya mkataba.

Aidha, Waziri huyo amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati kumuandikia barua ya onyo mkandarasi huyo, akieleza kuwa tayari walikutana na uongozi wa kampuni hiyo jijini Dodoma na kukubaliana kuwa wangeanza kazi ndani ya siku 25 baada ya kulipwa fedha walizokuwa wanadai tangu Desemba 2025.

Hata hivyo, amesema hadi sasa mkandarasi huyo hajarejea katika eneo la mradi wala kuanza kazi.


“Huyu mkandarasi anafanya kazi kwa kusuasua sana. Walilipwa fedha mwezi Desemba na tukakubaliana ndani ya siku 25 wawe wamerudi site na kazi ianze, lakini muda wote umeisha na hakuna kinachoendelea,” amesema Ndejembi.

Kwa mujibu wa Waziri huyo, mradi huo ulipaswa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili na kukabidhiwa mwishoni mwa mwaka huu, lakini hadi sasa utekelezaji umefikia takribani asilimia 50 pekee.


Amesema mradi huo ni sehemu ya mpango wa serikali wa kuunganisha mikoa ya kanda ya kusini ambayo ni Ruvuma, Lindi na Mtwara kwenye gridi ya taifa ili kuboresha upatikanaji wa umeme wa uhakika.

“Wananchi wa Kusini wanahitaji umeme wa uhakika na serikali imeweka kipaumbele katika kutatua changamoto hiyo kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi huu. Haiwezekani mkandarasi akachelewesha kazi hii,” amesema.

Ameongeza: “Baada ya onyo tutakalompa, endapo ataendelea kusuasua tutachukua hatua zaidi.”



&&&

WANANCHI ZAIDI YA 13,000 WANUFAIKA NA SAMIA ARDHI KLINIKI NCHINI

March 07, 2026 Add Comment



MTWARA

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo amesema jumla ya wananchi 13,550 wamejitokeza kupata huduma mbalimbali za sekta ya ardhi kupitia Samia Ardhi Kliniki iliyofanyika katika mikoa yote 26 nchini.



Dkt. Akwilapo amesema hayo wakati akifunga rasmi Samia Ardhi Kliniki katika viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara tarehe 7 Machi 2026, akisema kliniki hiyo imekuwa jukwaa muhimu la kusogeza huduma za ardhi karibu na wananchi hususan wanawake.



Amesema, kati ya wananchi waliojitokeza katika kliniki hizo, wanawake walikuwa 8,725 sawa na asilimia 64.4 huku wanaume wakiwa 3,892 sawa na asilimia 35.7, jambo linaloonesha mwitikio mkubwa wa wanawake katika kutumia fursa zinazotolewa na Serikali.


Aidha, Waziri Akwilapo amesema, jumla ya hatimiliki 3,131 zimetolewa kwa wananchi waliokamilisha taratibu za umilikishwaji wa ardhi ambapo hatimiliki 2,081 sawa na asilimia 57.4 zimetolewa kwa wanawake na hatimiliki 1,543 sawa na asilimia 43.6 zimetolewa kwa wanaume.


Amefafanua kuwa, hatua hiyo imeongeza usalama wa milki kwa wananchi pamoja na kuimarisha uchumi wa familia na Taifa kwa ujumla.


“Ardhi ni msingi wa uchumi wa mwananchi na Taifa. Mwanamke anapomiliki ardhi kisheria anapata uwezo mkubwa wa kuwekeza, kufanya shughuli za uzalishaji na hata kupata mikopo katika taasisi za fedha,” alisema.


Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Donald Msengi amesema, Samia Ardhi Kliniki imenufaisha wanawake kwa kuwaelimisha jambo alilolieza kuwa limelenga kuwawezesha na kulinda haki na kutatua changamoto zao.


‘’Kupitia Kliniki hiyo wanawake walipewa huduma mbalimbali ambazo ni elimu ya kumiliki ardhi, ushauri wa kitaalamu kuhusu masuala ya ardhi pamoja na utoaji hati’’ amesema Kanali Msengi.

RAIS WA BURUNDI MHE. ÉVARISTE NDAYISHIMIYE AWASILI KIA KUSHIRIKI MKUTANO WA 25 WA WAKUU WA NCHI WA EAC

RAIS WA BURUNDI MHE. ÉVARISTE NDAYISHIMIYE AWASILI KIA KUSHIRIKI MKUTANO WA 25 WA WAKUU WA NCHI WA EAC

March 07, 2026 Add Comment




Rais wa Jumhuri ya Burundi Mheshimiwa Évariste Ndayishimiye amewasili katika Uwanja wa Ndega wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) Mkoani Kilimanjaro, kushiriki katika Mkutano wa 25 wa Kawaida wa Wakuu wa Nchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) unaofanyika leo tarehe 7 Machi 2026 katika Makao Makuu ya Jumuiya jijini Arusha.

Akiwasili Mkoani humo amepokelewa na Mhe. Mahmoud Thabit Kombo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki akiambatana Viongozi Waandamizi mbalimbali wa Serikali.