HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

RC SENDIGA, SEKTA BINAFSI WASHIRIKIANA KUWAWEZESHA WAATHIRIKA WA MAJANGA

February 01, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Manyara

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, amekabidhi pikipiki ya umeme ya magurudumu matatu iliyotolewa na Mati Foundation kwa binti mwenye ulemavu, Bertina Francis, aliyepoteza wazazi wake wote wawili kufuatia maporomoko ya tope yaliyotokea Wilaya ya Hanang’ mwezi Desemba 2023.

Bertina Francis, ambaye kwa sasa anaishi katika moja ya nyumba zilizojengwa na Serikali kwa ajili ya waathirika wa maporomoko hayo katika eneo la Waret wilayani Hanang’, ameelezwa kuwa anajishughulisha na biashara ndogo ya uuzaji wa vitafunwa. Kupatikana kwa pikipiki hiyo ya umeme kunatarajiwa kumrahisishia shughuli zake za kiuchumi hususan katika usambazaji wa bidhaa zake na hivyo kuongeza kipato na kujitegemea.
Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Mhe. Sendiga amesema msaada huo ni matokeo ya ushirikiano mzuri uliopo kati ya Serikali na sekta binafsi, akisisitiza kuwa ushirikiano huo una mchango mkubwa katika kugusa maisha ya wananchi wenye uhitaji. Amempongeza mwekezaji David Mulokozi kupitia taasisi yake ya Mati Foundation kwa moyo wa kujitolea na kusaidia makundi maalum katika jamii.

“Serikali inaendelea kuhamasisha wawekezaji na taasisi binafsi kushiriki katika maendeleo ya jamii. Msaada huu ni mfano mzuri wa namna sekta binafsi inavyoweza kushirikiana na Serikali kuwainua wananchi walioko katika mazingira magumu,” amesema RC Sendiga.
Kwa upande wake, Bertina Francis ameishukuru Serikali pamoja na Mati Foundation kwa msaada huo, akieleza kuwa pikipiki hiyo itamfungulia fursa zaidi za kiuchumi na kumpa matumaini mapya ya maisha. Ameiomba taasisi hiyo kuendelea kuwasaidia watu wenye uhitaji ili nao wajisikie kuwa sehemu ya jamii na kuchangia katika maendeleo yao binafsi na ya Taifa.

Pikipiki hiyo ya umeme ni sehemu ya mpango unaoendelea wa kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia taasisi yake ya Mati Foundation wa kugawa pikipiki za magurudumu matatu kwa watu wenye ulemavu zaidi ya 2,000 kote nchini. Mpango huo ulianza rasmi mwezi Septemba 2025 ukiwa na lengo la kuwawezesha watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kijamii.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni mchango muhimu katika juhudi za Serikali za kuhakikisha makundi maalum yanapata fursa sawa za maendeleo na kujitegemea kiuchumi, hususan kwa waathirika wa majanga mbalimbali nchini.
DC NYAMWESE: MADIWANI MSITANGULIZE MASLAHI BINAFSI KWENYE HALMASHAURI

DC NYAMWESE: MADIWANI MSITANGULIZE MASLAHI BINAFSI KWENYE HALMASHAURI

February 01, 2026 Add Comment

MKUU wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese,akizungumza wakati akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni, Halmashauri ya Wilaya ya Handeni na Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi yaliyolenga kuwaimarisha katika masuala ya utawala bora, ufuatiliaji wa mapato na uelewa wa mipaka ya majukumu yao katika uendeshaji wa halmashauri.

Na Augusta Njoji

MKUU wa Wilaya ya Handeni, Mhe. Salum Nyamwese, amewataka madiwani wa Halmashauri ya Mji Handeni, Halmashauri ya Wilaya ya Handeni na Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi kuacha kutanguliza maslahi binafsi au ya kisiasa wanapotekeleza majukumu yao, na badala yake kuweka mbele maslahi ya wananchi na maendeleo ya halmashauri.

Nyamwese ametoa wito huo mjini Handeni wakati akifunga mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani, yaliyolenga kuwaimarisha katika masuala ya utawala bora, ufuatiliaji wa mapato na uelewa wa mipaka ya majukumu yao katika uendeshaji wa halmashauri.

Amesisitiza kuwa serikali haitavumilia uzembe, hujuma wala vitendo vyovyote vinavyozorotesha maendeleo ya halmashauri, akiwataka madiwani kuwa macho na kutoa taarifa kwa wakati pindi wanapobaini mianya ya upotevu wa mapato.

“Tunaomba mkawe wabunifu na mzishauri halmashauri namna bora ya kuboresha na kusimamia vyanzo vya mapato. Nyie ndio mnaoishi na wananchi; mnapobaini kapu linavuja, tuambieni linavuja wapi na nani analivujisha ili hatua stahiki zichukuliwe,” amesema Nyamwese.

Ameongeza kuwa madiwani ni macho na masikio ya serikali katika maeneo yao, hivyo wanapaswa kusimamia nidhamu ya watumishi, kuacha kufanya kazi kwa mazoea na kuchochea ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo.

Kwa upande wake, Katibu Tawala wa Wilaya ya Handeni, Margareth Killo, amesema mafunzo hayo yataongeza ufanisi na uwajibikaji wa madiwani katika kuwahudumia wananchi.

Naye, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Handeni, Amiri Mwaliko, pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi, Michael Chabai, wamesema mafunzo hayo yamewawezesha madiwani kufahamu vyema wajibu na mipaka yao, hali itakayopunguza migongano na kuongeza tija katika utendaji wa halmashauri.

TISEZA YATOA VIVUTIO KWA UPANUZI WA MRADI WA HOSPITALI MWANZA

January 31, 2026 Add Comment
Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) imetembelea mradi wa Hospitali ya Kamanga Medics (Kamanga Medics Hospital) iliyopo eneo la Nyegezi jijini Mwanza, ambao kwa sasa uko katika hatua ya upanuzi.

REA YAMTAKA MKANDARASI CCC INTERNATIONAL MKOANI RUVUMA KUONGEZA KASI YA UJENZI WA MRADI

January 31, 2026 Add Comment
Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umemtaka Mkandarasi Kampuni ya CCC International Engineering Nigeria Ltd anayetekeleza Mradi wa Kusambaza umeme katika Vitongoji 135 vya Majimbo 9 ya uchaguzi Mkoani Ruvuma kuongeza kasi ya ujenzi ili kukamilisha Mradi huo kwa wakati.
WAZIRI MAVUNDE AKABIDHI MAJIKO YA GESI 1,000 KWA MAMA NA BABA LISHE DODOMA

WAZIRI MAVUNDE AKABIDHI MAJIKO YA GESI 1,000 KWA MAMA NA BABA LISHE DODOMA

January 31, 2026 Add Comment

Waziri wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Mtumba, Antony Mavunde, amekabidhi jumla ya majiko 1,000 ya gesi kwa mama lishe na baba lishe wa Jimbo la Mtumba, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali katika kukuza matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Mavunde amesema mpango huo unalenga kuboresha afya za mama na baba lishe, kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku pamoja na kulinda mazingira kwa kupunguza matumizi ya mkaa na kuni.

Amesema kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wajasiriamali wadogo ambapo ameahidi kuanzisha klabu za mama lishe katika kila kata za Jimbo la Mtumba zitakazosaidia kuwaunganisha mama lishe na kuwapatia elimu ya ujasiriamali, usimamizi wa fedha pamoja na kuwawezesha kupata mikopo kwa urahisi ili waondokane na mikopo kandamizi maarufu kama kausha damu.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Mafunzo kutoka kampuni ya Oryx Gas, Peter Ndomba, amewataka mama lishe na baba lishe kuacha kabisa matumizi ya mkaa na kuni akisema nishati hizo zimekuwa zikisababisha madhara makubwa ya kiafya ikiwemo magonjwa ya mfumo wa hewa, macho na moyo kutokana na moshi unaotokana na matumizi yake.

Kwa upande wao, mama lishe na baba lishe waliopokea majiko hayo wameishukuru Mbunge wao Antony Mavunde pamoja kwa msaada huo wakisema utawapunguzia adha ya kuni na mkaa, kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza ufanisi katika shughuli zao za kila siku.

VITONGOJI VYOTE MKOA WA KILIMANJARO SASA KUWA NA UMEME

January 31, 2026 Add Comment

 📌 Wananchi wahamasishwa kuanza kufanya wiring kupokea mradi wa vitongojini

📌 Wananchi watakiwa kulinda miundombinu ya umeme

📌 Bilioni 33.5 kupeleka umeme vitongoji 186 Kilimanjaro


Wananchi katika vitongoji 186 ambavyo vinatarajiwa kupelekewa umeme Mkoani Kilimanjaro wamehamasishwa kuanza kufanya maandalizi ya kuupokea mradi huo kwa kuanza kutandaza nyaya ndani ya nyumba zao (wiring).

Rai hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Mkoa wa Kilimnajrao, Mhe. Nurdin Babu wakati wa kikao cha kumtambulisha mkandarasi, Derm Group (T) Limited alieshinda zabuni ya kupeleka umeme kwenye vitongoji 186 vya Mkoa huo katika kipindi cha miaka mitatu.

Mradi huo wa kupeleka umeme katika vitongoji unatekelezwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) utagharimu zaidi ya shilingi bilioni 33.5.

Kuanza kwa mradi huo wa kupeleka umeme katika vitongoji 186, kutaufanya Mkoa wa Kilimanjaro kuwa na umeme katika vitongoji vyake vyote 2,258.

“Tunamshkuru sana Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake njema ya kutaka kuhakikisha kwamba wananchi wa Tanzania wote wanapata nishati ya umeme mpaka kwenye ngazi ya kitongoji.

Mkoa wa Kilimanjaro tunaenda kuandika historia kuwa miongoni mwa mikoa 3 inayokwenda kufikisha umeme katika vitongoji vyake vyote. Hii ni heshima kubwa sana. Nitumie fursa hii kuwahamasisha wananchi kuanza kufanya maandalizi ya kupokea umeme pindi mkandarasi atakapoanza kazi rasmi kwa kufanya wiring kwenye nyumba zao,” amesema Mhe. Babu.

Mkuu huyo wa Mkoa pia ametoa rai kwa wananchi kuchangamkia fursa ya uwepo wa umeme kwa kuanzisha biashara mbalimbali ili lengo la serikali la kuboresha maisha ya wananchi wa vijijini kupitia upatikanaji wa nishati ya umeme liweze kutimia.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA ambaye pia ni Mkurugenzi wa Fedha, CPA. Daniel Mungure ametoa wito kwa wananchi kumpa ushirikiano mkandarasi pindi atakapoanza kutekeleza mradi lakini pia kulinda miundombinu ya umeme ambayo imejengwa kwa gharama kubwa.

Kwa upande wake Meneja wa kampuni ya Derm Group, Mhandisi Musa Abdallah ameahidi kukamilisha mradi huo ndani ya muda uliopangwa kimkataba na kwamba atashirikiana karibu na viongozi na wananchi wa maeneo ya mradi.



MBEYA WAPOKEA BILIONI 42.6, KUPELEKA UMEME VITONGOJI 318

January 31, 2026 Add Comment




*📌Idadi ya vitongoji vyenye umeme Mbeya ni 1,970 sawa na asilimia 67%*


*📌Mkandarasi atakiwa kutekeleza mradi huo kulingana Taratibu zilizowekwa*


📍Mbeya


Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Beno Malisa ameishukuru Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kwa kupeleka kiasi cha shilingi bilioni 42.6 mkoani Mbeya ili kupeleka umeme kwenye vitongoji 316 kupitia mradi wa HEP 2B unaotekelezwa mkoani humo ili wananchi wanufaike na nishati hiyo. 


RC Malisa amesema mradi huo unakwenda kuleta tija na kuchochea maendeleo ya wananchi wa mkoa huo ambao wataunganishiwa umeme huo kuwawezesha kuendesha shughuli zao za kiuchumi. 

"Gharama ya kuunganisha umeme ni shilingi 27,000 tu. Nawaomba wananchi wa mkoa huu mtumie fursa hii ya kuunganisha umeme iliyoletwa na Serikali kupitia REA.," Amesema RC Malisa. 


Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa REA, Bw. Frank Mugogo amesema jumla ya Vitongoji mkoa wa Mbeya ni 2,951 ambapo vitongoji vyenye umeme ni 1,970 sawa na asilimia 67%. 

Ameongeza kuwa vitongoji ambavyo havina umeme ni 1,981 na vitongoji vilivyopo kwenye mradi huo wa HEP 2B uliotambulishwa mkoani Mbeya ni 316 na vitongoji vitakavyosalia ni 665.

Kwa upande wake, Meneja wa Miradi kutoka kampuni ya White City International Contractors Ltd, Mha.Baraka Mungai ambaye atatekelesa mradi huo ameishukuru Serikali kupitia REA kwa kupewa fursa ya kutekeleza mradi huo. Ameuhakikishia uongozi wa mkoa wa Mbeya kuwa mradi huo utakamilika kwa wakati ili uweze kuleta tija kwa wananchi wa mkoa huo.


AMBONI ADVENTURE RUN, FURSA YA KUTANGAZA MAPANGO YA AMBONI TANGA

January 31, 2026 Add Comment



Na Kassim Nyaki, Amboni Tanga.

Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro imeshiriki na kudhamini mbio za AmbonI Adventure run zilizofanyika leo tarehe 31 Januari 2026 jijini Tanga kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii hususan mapango ya Amboni yanayosimamiwa na Mamlaka yah ifadhi ya Ngorongoro

Mbio hizo za umbali wa kimomita 6, 10 na 20 ambazo zimehudhuriwa na wakimbiaji zaidi ya 500 kutoka maeneo mbalimbali nchini zimeanzia katika viwanja vya Shule ya Sekondari Galanos hadi Mapango ya amboni ambapo washiriki wa mbio hizo wamepata fursa ya kufanya utalii wa ndani katika mapango hayo.

Kaimu meneja uhusiano wa Ngorongoro Hamis Dambaya ambaye ameshiriki mbio hizo kwa kukimbia kilomita 10 ameeleza kuwa Ngorongoro imeamua kuungana na wadau mbalimbali kuendelea kutangaza vivutio vilivyoko katika mapango ya Amboni ili yaendelee kujulikana kitaifa na kimataifa na kuvutia wageni wengi kutembelea na kuona vivutio vinavyopatikana katika mapango hayo na kupataa taarifa mbalimbali ikiwemo historia ya wapigania uhuru. 

Msimamizi wa Mapango ya Amboni Afisa Uhifadhi Daraja la kwanza Ramadhan Rashid ameeleza kuwa baadhi ya vivutio vinavyopatikana katika Mapango ya Amboni  ni pamoja na maumbo ya asili ya kijiolojia, vivutio vilivyochongwa na maji kama meli, mlima Kilimanjaro, kanisa, msikiti, shughuli za kimila na mataambiko, ndege ndani ya mapango, pango la jinsia, Pango la fatuma ambalo watu hulitumia kuomba mchumba wa kuoa, mimea ya aina mbalimbali, mto pamoja na mazingira asilia yanayopaambwa naa upepo mwanana wa bahari ya hindi.

Mkuugenzi wa Kale Amboni Caves Sophia Mulamula ameeleza kuwa Mbio za Amboni Adventure Run ambazo zimefanyika kwa msimu wa tatu na kuhudhuriwa na wakimbiaji takriban 500 zinatendelea kuboreshwa ili kuvutia wakimbiaji wengi zaidi mwaka ujao 2027 


“Tumefanya tathmini kwa miaka hii miwili tumeona mbio hizi zinavutia watu wengi, tunaamini mwakani tunaboresha vitu vingi zaidi ili tupate wakimbiaji wengi kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii, kutangaza nchi yetu lakini kuendelea kuhamasisha utalii wa michezo” alilisitiza Mulamula.






Diamond Akiri Umuhimu wa JAB, Wasafi Media Yakubali Kutii Sheria ya Habari

January 31, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi wa Wasafi Media, Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz, ameipongeza Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) kwa kutekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, huku akiahidi kuwa vyombo vyake vya habari viko tayari kufuata kikamilifu matakwa yote ya kisheria yanayoongoza sekta ya habari nchini.

Diamond ametoa kauli hiyo baada ya kufika katika ofisi za Bodi ya Ithibati kwa ajili ya kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali yanayohusu utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari, akisema Wasafi Media haina nia ya kukwepa sheria bali ina dhamira ya kushirikiana kwa karibu na wasimamizi wa taaluma ya uandishi wa habari.

Amesema licha ya Sheria hiyo kuleta changamoto kwa baadhi ya vyombo vya habari na watumishi wake, bado haiwezi kupingwa kwani ilitoa muda wa kutosha kwa wadau wote kujipanga na kutimiza vigezo vilivyowekwa, ikiwemo sharti la waandishi wa habari kuwa na kiwango cha elimu cha kuanzia Diploma na kuendelea.
Diamond amekiri kuwa kuanzishwa kwa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari kumeleta nidhamu na uwajibikaji mkubwa katika taaluma ya habari, akisisitiza kuwa Wasafi Media inaunga mkono juhudi za Serikali za kuhakikisha weledi, maadili na heshima ya taaluma hiyo inalindwa.

“Sisi hatutaki kukwepa utekelezaji wa Sheria. Hakuna namna unaweza kuvunja Sheria na ukabaki salama. Tumehakikisha watumishi wetu wote wanazingatia Sheria na katika hilo sina utani,” amesema Diamond.

Aidha, amesema hapo awali alipata taarifa na tafsiri tofauti kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, hali iliyosababisha sintofahamu kwa baadhi ya wadau, lakini baada ya kufika katika ofisi za Bodi na kupewa ufafanuzi wa kina, ameelewa vyema dhamira ya Serikali ya kuimarisha taaluma ya habari nchini.

Amepongeza pia msimamo wa Waziri mwenye dhamana aliyesisitiza kuwa Bodi ya Ithibati ni mlezi wa waandishi wa habari, akisema baada ya mazungumzo na uongozi wa Bodi, ameridhishwa kuwa taasisi hiyo ipo kwa ajili ya kulinda na kukuza taaluma hiyo, si kuibana.
“Nakiri wazi kuwa Bodi ni mlezi kwa waandishi wa habari. Baada ya kuielewa Sheria vizuri, hakuna sababu ya kupingana nayo. Watu wangu tayari wamechukua hatua stahiki na wamerejea vyuoni kujiendeleza kielimu,” amesema Diamond, akisisitiza umuhimu wa mawasiliano mazuri kati ya wadau wa sekta ya habari na wasimamizi wa Sheria.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, amesema Sheria ya Huduma za Habari ilitungwa mwaka 2016 na Serikali ilitoa kipindi cha mpito cha miaka mitano kwa waandishi na taasisi za habari kutimiza matakwa ya kisheria.

Ameeleza kuwa kipindi hicho kiliongezwa kwa miaka miwili na baadaye miaka mingine mitatu, hivyo kufikisha jumla ya miaka kumi, muda ambao Serikali inaamini ulikuwa wa kutosha kwa wadau wote wa sekta ya habari kujiandaa na kutekeleza Sheria hiyo kikamilifu.

Wakili Kipangula amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unalenga kujenga sekta ya habari yenye weledi, maadili na heshima, sambamba na kulinda maslahi ya waandishi, vyombo vya habari na jamii kwa ujumla.