HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

RC MTWARA AELEZA MANUFAA YA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA KWA UCHUMI WA WAKULIMA

RC MTWARA AELEZA MANUFAA YA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA KWA UCHUMI WA WAKULIMA

May 14, 2026 Add Comment

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mhe. Kanal Donald Msengi, amewashauri Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwahimiza wakulima kutumia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala ili kuleta mabadiliko chanya kiuchumi na kuongeza tija katika uzalishaji wa mazao.

Akizungumza  wakati wa Mafunzo ya Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa Viongozi wa Chama na Serikali kutoka mkoa wa Dodoma yaliyofanyika mkoani Mtwara, Kanal Msengi amesema mfumo huo umeleta mafanikio makubwa kwa vyama vya ushirika mkoani humo kwa kuviwezesha kuwa imara kiuchumi. Ameeleza kuwa kupitia mfumo huo, vyama vimefanikiwa kufanya uwekezaji mbalimbali ikiwemo ujenzi wa maghala, ununuzi wa magari, uanzishaji wa viwanda pamoja na kuchangia huduma za kijamii kama elimu, afya na maji.

“Ni muhimu viongozi mkatumia nafasi zenu kuwahamasisha wakulima na wanaushirika kutumia mfumo huu, kwani umeleta manufaa makubwa na una uwezo wa kuleta mageuzi chanya kwa sekta ya kilimo,” amesema Kanal Msengi.

Naye Kaimu Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Mtwara, Robert Nzunza, amebainisha hatua muhimu za mchakato wa stakabadhi za ghala kuwa ni pamoja na maandalizi ya msimu wa mauzo, ukusanyaji wa mazao ghalani, usafirishaji wa mazao kwenda ghala kuu, mapokezi ya mazao, mauzo kupitia minada ya mtandao, malipo ya fedha kupitia vyama vikuu (Unions), malipo kwa wakulima na wadau, pamoja na utoaji wa mizigo ghalani.

Kwa upande wake Mkuu wa msafara huo ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kutoka mkoa wa Dodoma, Donald Mejetii, amesema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia kuwajengea uwezo viongozi hao ili waweze kuwahamasisha wakulima wa Dodoma kutumia mfumo huo kwa tija zaidi.

Viongozi wa Chama na Serikali kutoka mkoa wa Dodoma wapo mkoani Mtwara kwa ziara ya kujifunza Mfumo wa Stakabadhi za Ghala katika vyama vya ushirika na namna unavyoweza kuinua kipato cha mkulima. Katika ziara hiyo pia wametembelea Chama Kikuu cha Ushirika cha MAMCU LTD pamoja na Chama cha Msingi Mayanga AMCOS.

TANZANIA NA KENYA KUHARAKISHA UTEKELEZAJI MIRADI YA KUUNGANISHA NJIA ZA UMEME

May 14, 2026 Add Comment


Tanzania na Kenya zimekubaliana kuharakisha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya njia za umeme zinazounganisha gridi za nchi hizo mbili pamoja na kuboresha mifumo ya usafirishaji wa umeme ili kuimarisha usalama wa nishati, kuongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme na kukuza biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki.


Makubaliano hayo yamefikiwa baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta wa Kenya, Bw. Alex Wachira, jijini Nairobi, Kenya.

Mazungumzo hayo yalijikita katika kuimarisha ushirikiano katika sekta ndogo ya umeme na nishati jadidifu, hususan biashara ya umeme, utekelezaji wa miradi ya uunganishaji wa gridi za umeme pamoja na maboresho ya mifumo ya usafirishaji na usambazaji wa umeme kati ya Tanzania na Kenya.


Viongozi hao pia walijadili hatua mbalimbali za kuimarisha biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki kupitia Umoja wa Soko la pamoja la Kuuziana Umeme na Kuimarisha Mifumo ya Gridi-Eastern Africa Power Pool (EAPP).


Sambamba na hilo, Makatibu Wakuu hao walisisitiza umuhimu wa kuongeza wigo wa njia za usafirishaji umeme zitakazounganisha nchi hizo mbili kupitia maeneo ya Namanga, Lungalunga, Loitoktok na Isibania/Sirari.


Aidha, kikao hicho kilijadili pendekezo la kuanzishwa kwa mfumo wa Ring Circuit utakaojumuisha njia za Ibadakuli – Masaka, Ibadakuli – Kilgoris na Kilgoris – Masaka kwa lengo la kuongeza uthabiti wa gridi za umeme na kuimarisha biashara ya umeme kati ya Tanzania na Kenya.

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mafuta wa Kenya, Bw. Alex Wachira alieleza kuwa nchi hiyo imejipanga pia katika uwekezaji wa miundombinu ya gesi asilia kwa lengo la kuimarisha upatikanaji wa nishati hiyo nchini humo, pia kuongeza ushirikiano wa kikanda katika sekta ya nishati.



Aidha, Kenya ilieleza uzoefu wake katika biashara ya umeme wa kikanda, ikibainisha kuwa inaendelea kupokea umeme kutoka Ethiopia kupitia mikataba ya biashara ya umeme ya kikanda, ambapo kiwango cha umeme hupungua na kuongezeka kulingana na mahitaji, huku kikifikia takriban megawati 100 katika vipindi vya kawaida.


Hatua hiyo imeelezwa kusaidia kuimarisha uthabiti wa mfumo wa umeme nchini Kenya.


Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi na wataalam mbalimbali kutoka Wizara za Nishati za Tanzania na Kenya pamoja na taasisi za sekta ya umeme zikiwemo TANESCO, KETRACO na KPLC.


KAMATI YA BUNGE:SEKTA YA VIWANDA NA BIASHARA NI MHIMILI WA UCHUMI

KAMATI YA BUNGE:SEKTA YA VIWANDA NA BIASHARA NI MHIMILI WA UCHUMI

May 14, 2026 Add Comment

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeipongeza Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja na taasisi zake kwa utekelezaji mzuri wa majukumu yake, huku ikizitaka kuongeza kasi ya utekelezaji wa mikakati ya kukuza uchumi wa taifa.

Pongezi hizo zimetolewa jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Deodatus Mwanyika (picha ya kwanza), wakati wa kikao cha tathmini ya utekelezaji wa shughuli za wizara kupitia taasisi zake ambazo ni Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Tume ya Ushindani Tanzania (FCC), Wakala wa Vipimo (WMA) na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA). Mwanyika amesema juhudi zinazofanywa na wizara hiyo zimeanza kuleta matokeo chanya katika kuimarisha mazingira ya biashara na uzalishaji nchini. Aidha, ameielekeza wizara kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya bidhaa bandia na hafifu zinazoingia sokoni, akieleza kuwa bidhaa hizo husababisha hasara kwa wazalishaji wa ndani na kuhatarisha afya pamoja na usalama wa watumiaji. Pia ameagiza hatua kali kuchukuliwa dhidi ya matumizi ya vipimo visivyo sahihi katika biashara, hususan lumbesa, ambalo limekuwa likilalamikiwa na wananchi katika maeneo mbalimbali nchini kutokana na matumizi ya vipimo visivyo rasmi. Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Dennis Londo, amesema wizara imepokea maelekezo na ushauri uliotolewa na kamati hiyo na kuahidi kuyafanyia kazi kwa lengo la kuboresha huduma na kuongeza ufanisi katika sekta ya viwanda na biashara nchini. Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Ashura Katunzi, pamoja na viongozi wengine wa taasisi zilizo chini ya wizara hiyo, wamesema wanaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha usimamizi wa bidhaa na huduma nchini. Hatua hizo ni pamoja na kufanya operesheni maalumu za ukaguzi wa bidhaa bandia na kutoa elimu kwa wafanyabiashara kuhusu matumizi sahihi ya vipimo vinavyotambulika kisheria.

MEYA TANGA AKERWA NA MABASI KUZAGAA MJINI ATOA NENO KWA MAMLAKA HUSIKA

May 14, 2026 Add Comment

 

Na Oscar Assenga,TANGA


MSTAHIKI Meya wa Jiji la Tanga, Mustapha Selebosi amechukizwa na kitendo cha mabasi makubwa kuendelea kuzagaa katikati ya mji huku kituo rasmi cha mabasi cha Kange kikishindwa kufanya kazi ipasavyo licha ya Serikali kuwekeza mabilioni ya fedha.

Akizungumza kwenye kikao katika kikao cha Baraza la Madiwani ambapo alisema kuwa tayari walitoa maelekezo mabasi yote makubwa yaanze kutumia kituo hicho rasmi ili kupunguza msongamano wa magari mjini, lakini bado utekelezaji wake umekuwa wa kusuasua.

Meya huyo aliwataka LATRA na TARURA kushirikiana badala ya kuoneshana tofauti katika ukusanyaji wa mapato na usimamizi wa sheria.

“Sote tunajenga nyumba moja. Isiwe kama kuna wivu wa ukusanyaji wa mapato,” alisema Selebosi.

Katika kauli yake iliyobeba hisia kali, Selebosi alikosoa kitendo cha mabasi kupakia abiria katika vituo vya mafuta badala ya kutumia stendi rasmi, akisema hali hiyo ni uvunjifu wa sheria unaofanyika waziwazi huku mamlaka zikiwa kimya.

“Leo kuna watu wana vituo vya mafuta lakini wanapakilia mabasi hapo hapo. Sheria inasemaje kuhusu hilo?” alihoji.

Aidha, Meya huyo alisema hatakuwa tayari kufumbia macho changamoto zinazolinyima Jiji mapato, akisisitiza kuwa nafasi yake amepewa na wananchi na si mtu binafsi.

“Nimepata udiwani na umeya kwa kura za wananchi. Nitabaki na msimamo wangu,” alisema.

Selebosi pia aliibua hoja ya hasara kubwa iliyopatikana katika kituo kikuu cha mabasi cha Tanga ambacho kilijengwa kwa gharama ya zaidi ya Shilingi bilioni 3 tangu mwaka 2008/2009, huku baadaye Serikali ikiendelea kuwekeza zaidi ya bilioni 8 katika maboresho ya mradi huo.

Kwa mujibu wa Meya huyo, kituo hicho kilikuwa mfano wa kuigwa nchini ambapo halmashauri mbalimbali zilifika kujifunza mfumo wa uwekezaji wake, lakini hadi sasa hakitumiki kikamilifu kutokana na uzembe wa utekelezaji.

“Serikali imewekeza zaidi ya bilioni 8 lakini kituo hakifanyi kazi kama ilivyokusudiwa. Hii ni hasara kubwa kwa halmashauri na Serikali,” alisisitiza.


Mwisho, Selebosi aliwataka watendaji wa mamlaka mbalimbali kusimamia sheria bila kumuogopa mtu yeyote na kuhakikisha mabasi yote yanaelekezwa katika kituo rasmi ili kuongeza mapato ya halmashauri na kuondoa msongamano mjini.

Mwisho.

MODERNIZED MV. LIEMBA NEARS COMPLETION, SET FOR JULY 2023

May 14, 2026 Add Comment

       

By Prosper Makene 

Residents of Kigoma, Katavi, and Rukwa regions are set to benefit once the historic MV. Liemba completes rehabilitation and resumes official service in July 2026 on Lake Tanganyika. As of early May, the overhaul had reached 70% completion.

DED MBEYA DC AMSHUKURU RAIS SAMIA KWA AJIRA 259.

May 13, 2026 Add Comment

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, Bi. Erica E. Yegella amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa fursa ya ajira mpya takriabani 259 katika kipindi cha mwezi Januari na Mei 2026.

NIT YAJIPANGA KUHUDUMIA MIRADI MIKUBWA YA MAENDELEO

May 13, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO

Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) kimeendelea kutoa mafunzo kupitia kozi ndefu 49 zinazolenga kuzalisha wataalam mahiri watakaosaidia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali nchini.

WIZARA YA UCHUKUZI YAOMBA BAJETI YA SHILINGI TRILIONI 2.87 KWA MWAKA WA FEDHA 2026/27

May 13, 2026 Add Comment

 Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Wizara ya Uchukuzi imewasilisha ombi la kuidhinishiwa bajeti ya jumla ya Shilingi 2,872,738,082,000 kwa mwaka wa fedha 2026/27, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa mipango ya kuimarisha na kuendeleza sekta ya uchukuzi nchini.

Kwa mujibu wa makadirio hayo, kati ya fedha hizo, Shilingi 126,041,236,000 zimetengwa kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida, huku Shilingi 2,746,696,846,000 zikielekezwa katika Miradi ya Maendeleo, ikilenga kuboresha miundombinu ya usafiri wa anga, reli, barabara na huduma nyingine za uchukuzi.

Akizungumza bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo, Waziri wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, amesema kuwa bajeti hiyo imelenga kuharakisha utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya sekta ya uchukuzi nchini, sambamba na kuongeza ufanisi wa huduma za usafiri.

Ameeleza kuwa pamoja na hotuba hiyo, wizara imeambatisha majedwali mbalimbali yenye takwimu na taarifa za kina ili kutoa uelewa mpana zaidi kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi kuhusu hali ya utekelezaji wa sekta hiyo.

Aidha, amesema majedwali hayo ni sehemu ya hotuba rasmi ya bajeti na yanapatikana pia kupitia tovuti ya Wizara ya Uchukuzi kwa ajili ya rejea ya umma kupitia www.uchukuzi.go.tz.

Wizara hiyo inaendelea kuweka mkazo katika kuboresha miundombinu ya uchukuzi ili kuchochea ukuaji wa uchumi na kurahisisha usafirishaji wa watu na bidhaa nchini.