HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

TANZANIA KUENDELEA KUTUMIA AKILI UNDE KATIKA KUKABILIANA NA MAAFA

May 11, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu, Masvingo - Zimbabwe

TANZANIA imesema itaendelea kutumia teknolojia ya Akili Unde (AI) katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa maafa nchini ili kuongeza ufanisi wa utoaji wa tahadhari za mapema na kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga mbalimbali.


Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Dkt. Jim Yonazi, wakati wa mkutano wa maandalizi ya Mkutano wa Sita wa Kawaida wa Kamati ya Mawaziri Wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika Mei 11, 2026 mjini Masvingo, Zimbabwe.

Alisema matumizi ya AI yatasaidia uchakataji na ufuatiliaji wa taarifa mbalimbali zinazoripotiwa kuhusu masuala ya maafa nchini, hatua inayolenga kuongeza uwezo wa Serikali katika kufanya maamuzi ya haraka wakati wa majanga.


“Matumizi ya teknolojia ya Akili Unde yatawezesha uchambuzi wa taarifa kwa haraka, kutabiri hatari zinazoweza kujitokeza na kusaidia hatua za mapema za kukabiliana na maafa,” alisema Dkt. Yonazi.


Dkt. Yonazi alisema Serikali inaendelea kuweka mkazo katika maeneo muhimu yatakayosaidia kuwa na usimamizi wenye tija wa maafa ikiwemo utafiti wa kisayansi, matumizi sahihi ya Akili Unde, ushirikiano katika uhifadhi wa taarifa za matukio pamoja na matumizi ya menejimenti ya maarifa.

Aidha alisema Tanzania imeendelea kuwa mfano katika ukanda wa Kusini mwa Afrika kutokana na uwezo wake wa kuratibu na kusimamia maafa kwa mafanikio huku ikiendelea kuzuia, kupunguza madhara, kujiandaa na kurejesha hali pindi majanga yanapotokea.

Alifafanua kuwa mafanikio hayo yamechangiwa na uwepo wa Kituo cha Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Majanga na Tahadhari ya Mapema ambacho hufanya kazi saa 24 kupokea, kufuatilia na kuchambua taarifa za majanga kwa wakati halisi.


“Kituo cha Operesheni ya Maafa kimekuwa msaada mkubwa kwani kimerahisisha upatikanaji wa taarifa za mapema, uchambuzi wa takwimu za wakati halisi na upangaji wa mikakati ya kurejesha hali pamoja na kutoa elimu kwa umma kuhusu namna ya kujiandaa na kukabiliana na maafa,” alisisitiza.


=MWISHO=

MENEJIMENTI YA WIZARA YA NISHATI YATEMBELEA MRADI WA EACOP TANGA, WAFIKIA 85% YA UTEKELEZAJI.

May 11, 2026 Add Comment

Menejimenti ya Wizara ya Nishati imetembelea mradi wa kimkakati wa kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani mkoani Tanga nchini Tanzania wa EACOP (East African Crude Oil Pipeline) katika leo tarehe 11 Mei 2026.

Menejimenti hiyo ikiongozwa na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga imepokea taarifa ya utekelezaji wa mradi huo pamoja na kujionea ujenzi wa kituo cha kupokea, kuchakata na ujenzi wa gati la kupakia mafuta.

Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amesema Wizara ya Nishati imejionea kazi nzuri inayoendelea kufanyika ambapo mradi huo unatekelezwa kwa wakati na umefikia asilimia 85 ya utekelezaji.

“Tumeridhishwa na utekelezaji wa mradi huu. Umezalisha ajira kwa Watanzania katika fani mbalimbali, pia umefungua fursa nyingi kwa wananchi wa Mkoa wa Tanga moja kwa moja na Taifa kwa ujumla, ikiwa ni pamoja na ushiriki wa wazawa. vile vile mradi huu umesaidia jamii kupitia ukarabati wa barabara, miradi ya maji na miradi mingine ya kijamii,” amesema Kamishna Luoga.

Akitoa maelezo ya mradi huo, Mhandisi wa Mradi wa Kituo cha Kuhifadhi Mafuta, Mhandisi Musa Msafiri amesema utekelezaji wa upande wa matenki ya kuhifadhi mafuta umefikia asilimia 94, ambao ni ujenzi wa matenki manne yenye uwezo wa kubeba mapipa 2,000,000.

Kwa upande mwingine, Mhandisi wa Ujenzi wa gati, Fred Mahenge amesema utekelezaji wa mradi wa upande wa kituo cha kupakia na kusafirisha mafuta baharini (Jet) ni zaidi ya asilimia 90.

Mradi huu umezalisha jumla ya ajira 1,834, ambapo Watanzania wamepata asilimia 84 ya nafasi zote za ajira.

Aidha mradi huu unahusisha ujenzi wa bomba la mafuta lenye urefu wa kilomita 1,443 kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani mkoani Tanga, ambapo mafuta yatapakiwa na kusafirishwa kwenda soko la dunia.







BALOZI MTEULE TANZANIA NCHINI KOREA AANZA RASMI MAJUKUMU

May 11, 2026 Add Comment
Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Jamhuri ya Korea Mheshimiwa Noel Kaganda amepokelewa rasmi katika Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini Seoul kuanza rasmi majukumu yake ya uwakilishi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Jamhuri ya Korea.

KAMISHNA KUJI AZINDUA MRADI WA KUSAFIRISHA NA KUSAMBAZA UMEME KATIKA HIFADHI YA TAIFA MIKUMI

May 11, 2026 Add Comment


Na. Philipo Hassan - Mikumi

Mwisho mwa wiki ikiyopita, Kamishna wa Uhifadhi TANAPA CPA Musa Nassoro Kuji alizindua rasmi mradi wa kusafirisha na kusambaza umeme wa TANESCO ndani Hifadhi ya Taifa Mikumi. Mradi huo unaolenga kuboresha utoaji wa huduma ndani ya hifadhi, kuimarisha shughuli za uhifadhi na utalii, kuboresha matumizi ya nishati ya umeme kwa watumishi wa hifadhi na kuongeza fursa za uwekezaji katika sekta ya utalii.

Usambazaji wa umeme wa TANESCO ndani ya hifadhi utaboresha na kuleta mapinduzi makubwa kwenye upatikanaji wa nishati hiyo kwa watumishi, watalii, wawekezaji waliopo ndani ya hifadhi hiyo pamoja na wananchi ambao nao wamefaidika na umeme huo ambao pia umepita kwenye maeneo yao wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Uzinduzi huo ulihudhuriwa na Menenejimenti ya hifadhi, Maafisa na Askari wa uhifadhi wakiongozwa na Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Augustine Masesa ambaye ndiye Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Mikumi, Meneja wa TANESCO Morogoro Kusini Mhandisi Lugata Masingija pamoja na wananchi wa maeneo jirani na hifadhi hiyo.

Kamishna Kuji aliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuidhinisha bajeti ya mradi huo pia Bodi ya Wadhamini ya TANAPA kwa usimamizi wa karibu wa shughuli za Shirika ikiwemo utekelezaji wa mradi huo.

Aidha, Kamishna Kuii aliupongeza uongozi wa TANESCO kwa utekelezaji wa mradi huo ambapo mbali na kuunga mkono jitihada za Serikali za uwepo wa nishati safi utaongeza kasi ya maendeleo kwa wananchi wa vijiji jirani vilivyonufaika na mradi huu,” alisema Kamishna Kuji.

Mradi huo unaweka historia mpya katika Hifadhi ya Taifa Mikumi kwa kuimarisha matumizi ya nishati safi na uhakika, hatua inayotarajiwa kuongeza ubora wa huduma, kuchochea uwekezaji wa utalii na kuendelea kufungua fursa za maendeleo kwa jamii zinazozunguka hifadhi hiyo.











WAZIRI MKUU DKT.MWIGULU AKUTANA NA RAIS WA IFAD,NAIROBI

May 11, 2026 Add Comment


*Wajadili Kilimo himilivu na uendelezaji wa Kilimo Biashara*


WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 11, 2026 amekutana na Rais wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo ya Kilimo (IFAD), Alvaro Lario, jijini Nairobi, Kenya, ambapo wamejadili maeneo mbalimbali ya ushirikiano katika sekta ya kilimo na uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.


Katika mazungumzo hayo, Dkt. Mwigulu amesema Tanzania itaendelea kushirikiana na IFAD katika maeneo mbalimbali ikiwemo kilimo himilivu cha tabianchi, maendeleo ya kilimo biashara, mapinduzi ya kidijitali katika sekta ya kilimo pamoja na uwezeshaji wa vijana na wanawake kiuchumi.

Aidha, Waziri Mkuu amesema Tanzania inatarajia kuendelea kushirikiana na IFAD katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ya kilimo ikiwemo mpango wa kuongeza uzalishaji wa alizeti ili kusaidia kuongeza upatikanaji wa mafuta ya kula nchini.

“Kimekuwa ni kikao kizuri kwa sababu tumekuwa na ushirikiano nao kwa muda mrefu, ambapo katika kipindi kilichopita tumeshirikiana nao katika miradi mbalimbali, na hasa miradi katika sekta za uzalishaji”.


“Lakini pia tumedhamiria kuendelea kushirikiana katika kuendeleza mazao ya mchanganyiko ambayo katika miaka ya nyuma ilikuwa inachukuliwa kuwa ni mazao ya chakula peke yake, kwasasa mazao haya niya biashara na tunayafanya sehemu ya kukuza biashara ambayo Tanzania inafanya na nchi nyingine”


Ameongeza kuwa Tanzania inatarajia kuendelea kushirikiana na IFAD katika sekta ya mifugo na mazao ya baharini kwa upande wa Zanzibar. 


“Sambamba na hayo, tunategemea kushirikiana nao katika utekelezaji wa kilimo endelevu ambacho kinasaidia kampeni yetu ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi nchi”. Amesisitiza Dkt. Mwigulu


Kwa upande wa Rais wa IFAD Alvaro Lario, amesema kuwa wataendelea kuhakikisha mipango na utekelezaji wa IFAD vinaendana na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Tanzania 2050


“Kwasasa tunasubiri kusikia vipaumbele ya Tanzania ili tujue namna gani tunaweza kusaidia katika maeneo vya utoshelevu na usalama wa chakula pamoja na uongezaji thamani wa mazao”

KIPINDI CHA MWAKA 2021-2026 HUDUMA ZA AFYA ZIMEONGEZEKA, ZIMEIMARIKA

May 11, 2026 Add Comment


Na Hassan Kimweri, WAF - Dodoma

Sekta ya afya nchini imepata mafanikio makubwa katika kipindi cha awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yaliyoongeza upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa vifaa tiba, uoatikanaji wa dawa pamoja na huduma za kibingwa na za dharura nchini.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema hayo leo Mei 11, 2026 wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azan Zungu.

"Eneo la vituo vya kutolea huduma za afya vimeongezeka kutoka elfu 10,153 mwaka 2021/22 hadi elfu 13,683 kufikia Machi 2026, sawa na ongezeko la vituo 3,530, Zahanati zimeongezeka kutoka elfu 7,189 hadi elfu 8,706 huku hospitali zikiongezeka kutoka mia 404 hadi mia 475 mwaka 2026," amesema Waziri Mchengerwa

Aidha, Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeongeza majengo mapya katika hospitali mbalimbali zikiwemo Hospitali ya Muhimbili, KCMC, BMH, Bugando, Mirembe, pamoja na Kibong'oto huku ikiwa imejenga hospitali mpya 10 za rufaa za mikoa, kukarabati hospitali kongwe 50, kukamilisha maboma 980 ya zahanati na kujenga vituo vya afya 390.

Amesema, katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto, Serikali imeongeza wodi za watoto wachanga kutoka 80 hadi 438 pamoja na vituo vya upasuaji wa dharura kutoka 445 hadi 630 ambayo ni mafanikio yaliyochangia kupungua kwa vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 556 mwaka 2016 hadi vifo 104 mwaka 2022 kwa kila vizazi hai 100,000.

"Katika huduma za uchunguzi na matibabu ya kibingwa, Serikali imenunua na kusimika vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi bilioni 241.6 ambapo mashine za MRI zimeongezeka kutoka 7 hadi 13, CT Scan kutoka 12 hadi 45 pamoja na Digital X-ray kutoka 147 hadi 559," amesema Waziri Mchengerea

Kwa upande wa chanjo, amesema watoto waliopata chanjo ya Pentavalent dozi ya tatu wameongezeka kutoka watoto milioni 2,093,412 hadi milioni 3,186,979 huku kiwango cha chanjo kikiongezeka kutoka asilimia 93 hadi 96, juu ya lengo la kimataifa la asilimia 90.

"Upatikanaji wa dawa na bidhaa za afya umeimarika, Serikali imetoa Shilingi trilioni 1.4 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba, viwanda vipya 11 vya dawa na vifaa tiba vimeanzishwa huku 'Tanzania Pharmaceutical Industries kikifufuliwa kwa ajili ya uzalishaji wa dawa za VVU nchini," amesema Waziri Mchengerwa

SERIKALI YATOA BILIONI 48.8 BIMA YA AFYA KWA WOTE

May 11, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu , Dodoma


Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya zisizo na uwezo kwa kutoa Shilingi bilioni 48.8 kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa makundi maalum kupata huduma za afya kwa uhakika. Kupitia utekelezaji huo, jumla ya kaya 172,297 tayari zimefikiwa na kuingizwa kwenye mpango huo, huku wanufaika 463,228 wakianza kupata huduma mbalimbali za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa nchini.

Akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52 kwa mwaka 2026/27 Waziri wa Afya Mhe. Omary Mchengerwa amesema kuwa, utekelezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila kujali hali yake ya kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea huduma jumuishi za afya kwa wananchi wote.

Katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na utekelezaji wa mpango huo, mabaraza na bodi za kitaaluma yameendelea kusimamia ubora wa huduma kwa kusajili wataalam wa afya 14,310, hatua inayoongeza nguvu kazi muhimu kwa utoaji wa huduma nchini.

Amesema kuwa kuhusu upatikanaji wa huduma za matibabu, jumla ya maduka ya dawa 330 yamesajiliwa pamoja na watarajali 3,004, huku vituo vya kutolea huduma za afya 3,643 vikisajiliwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma karibu na wananchi.

Katika kuhakikisha taaluma na maadili yanaendelea kuzingatiwa hususan wakati huu wa kuhudumia wananchi wengi zaidi kupitia mfumo wa Bima ya Afya, vituo binafsi vya afya 654 vimekaguliwa ili kuhakikisha vinakidhi viwango na kutoa huduma salama kwa wananchi.

Mafanikio hayo yanaakisi hatua kubwa ya Serikali katika kujenga mfumo imara wa afya unaojali usawa, ubora na upatikanaji wa huduma kwa wote, huku Bima ya Afya kwa Wote ikiendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

BARRICK YAWEZESHA WANAFUNZI VYUO VIKUU MBEYA KUTAMBUA FURSA KUPITIA KONGAMANO LA AIESEC 2026

May 11, 2026 Add Comment

 

Naibu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Mbeya University of Science and Technology ( MUST) Prof. Said Wai akifungua kongamano la AIESEC 2026 lililofanyika katika chuo hicho.
Afisa Mwandamizi wa AIESEC Tanzania, Joshua Samwel akiongea na wanafunzi katika kongamano hilo.

BODI YA REA YAFANYA ZIARA KWENYE KAMPUNI ZA NISHATI SAFI YA KUPIKIA ARUSHA

May 11, 2026 Add Comment


-Mradi wa Nishati Safi ya Kupikia waongeza ajira kwa vijana

Bodi ya Nishati Vijijini (REB) leo Mei 10, 2026 imefanya ziara katika Kampuni zinazozalisha, kusambaza bidhaa za nishati safi ya kupikia katika Mkoa wa Arusha.

Bodi hiyo ikiwa imeongozwa na Mwenyekiti wake, Mhe. Balozi Meja Jenerali (mstaafu), Jacob Kingu pamoja na Wajumbe wa Bodi hiyo, Mhe. Radhia Msuya na Mhandisi Sophia Mgonja waliweza kutembelea kampuni ya Ignate Energy Access yenye bidhaa za My Sol pamoja na kampuni ya HannyG Investment.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti Kingu, amezipongeza kampuni hizo kwa kuunga mkono kampeni ya Serikali ya Nishati Safi ya Kupikia kwa kuanza kutengeneza pamoja na kusambaza bidhaa za nishati safi ya kupikia huku akitoa wito kwa makampuni mengine kuendelea kuunga mkono kampeni hiyo ili malengo yaliyowekwa ya ifikapo 2034, Asilimia 80 ya Watanzania wawe wanatumia nishati safi ya kupikia.

Awali akitoa taarifa ya utendaji wa kampuni ya My Sol, Meneja Uendeshaji wa Mitambo, Joe Chambua, amesema kuwa pamoja na huduma zingine zinatolewa na kampuni hiyo ikiwamo huduma ya ufungaji wa umeme jua, kampuni hiyo imeanza kutekeleza mradi wa nishati safi ya kupikia kwa kuja na teknolojia rahisi na ya gharama nafuu ya mtambo wa biogasi.

Amesema kuwa wamefanikiwa kufunga mitambo ya biogasi katika taasisi mbalimbali nchini ikiwemo Magereza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa kampuni ya Hanny G Investment, Hanny Mbaria, ambao wanajishughulisha na utengenezaji wa majiko banifu pamoja na mkaa mbadala ameishukuru Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kuipa kampuni hiyo kazi ya kusambaza majiko banifu na mkaa mbadala katika shule 53 Tanzania Bara.

Mbaria amesema licha ya mradi wa nishati safi ya kupikia kulinda mazingira lakini pia mradi huo umetoa ajira kwa vijana wengi.

“Kwa sasa kampuni yetu imekua zaidi na tumeajiri vijana wengi zaidi tofauti na hapo awali. Kwa sasa tuna wafanyakazi zaidi ya 120 wenye ajira za kudumu na wasio na ajira za moja kwa moja ni 1000,” amesema Mbaria.








DKT. MWIGULU KUMUWAKILISHA RAIS DKT. SAMIA MKUTANO WA USHIRIKIANO AFRIKA NA UFARANSA, NCHINI KENYA

May 11, 2026 Add Comment

 WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Mei 10, 2026 ameondoka nchini kuelekea Nairobi, Kenya ambako anatarajia kumuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Mkutano wa Ushirikiano wa Afrika na Ufaransa (Africa Forward: Africa–France Partnership for Innovation and Growth Summit) utakaofanyika Mei 11–12, 2026.

Lengo la mkutano huo ni kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Afrika na Ufaransa katika sekta mbalimbali ikiwemo biashara, teknolojia, nishati, afya, Akili Unde (AI), kilimo, uchumi wa buluu pamoja na viwanda.

Aidha, mkutano huo unalenga kukuza uwekezaji mpya kati ya Afrika na kampuni za Ufaransa, kujenga ushirikiano unaotajwa kuwa wa usawa, pamoja na kujadili mageuzi ya mfumo wa fedha na maendeleo endelevu ya Afrika.

Mkutano huo wa Wakuu wa Nchi na Serikali unawakutanisha wadau wa maendeleo, wawekezaji pamoja na sekta binafsi, na umeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Rais wa Jamhuri ya Kenya, Mheshimiwa William Samoei Ruto, na Rais wa Jamhuri ya Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron.



BARABARA YA TOGO IKAMILIKE JUNI, MKATABA UJENZI WA BARABARA YA KIMARIO (BRAZIL) USAINIWE MEI 25 - PROF. SHEMDOE

May 11, 2026 Add Comment



Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ameilekeza TARURA na Manispaa ya Kinondoni kuhakikisha ujenzi wa barabara ya Togo unakamilika mwezi Juni, 2026 na mkataba wa ujenzi wa barabara ya Kimario (Brazil) unasainiwa Mei 25, 2026, ili kuwaondolea adha wananchi wa Kinondoni na watumiaji wengine wa barabara hizo zinazojengwa kwa kiwango cha lami kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo leo Mei 10, 2026 Kinondoni Jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na ofisi yake kupitia Wakala ya Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), aliyoifanya kutokana na ombi la wananchi wa Kinondoni kupitia kwa Mbunge wao Mhe. Abbas Tarimba.

“Tunaondoka hapa tukikubaliana kwamba barabara ya Togo itakamilika Juni 2026 na mkataba wa ujenzi wa barabara ya Kimario (Brazil) utasainiwa Mei 25, 2026 hivyo waheshimiwa Madiwani mfuatilie utekelezaji wa maelekezo haya,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amemtaka Meneja wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam Mhandisi Geofrey Mkinga na Meneja wa TARURA Wilaya ya Kinondoni Mhandisi Edwin Kabwote kuhakikisha wanasimamia barabara hizo zikamilike kwa wakati ili kuwaondolea adha wananchi wa Kinondoni na watumiaji wote wa barabara hizo hususani kipindi hiki cha mvua.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amemshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha ujenzi wa barabara 17 za DMDP II katika wilaya ya Kinondoni zilizogharimu Shilingi Bilioni 97.7 ambazo zina jumla ya urefu wa wa kilometa 36.483.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni Mhe. Abbas Tarimba amemshukuru Waziri wa TAMISEMI Prof. Riziki Shemdoe kwa kufanya ziara ya kukagua miradi hiyo ya maendeleo na kutoa maelekezo mahususi ya kuikamilisha, na kuongeza kuwa wananchi wamejionea wenyewe usikivu wa Waziri huyo wa Serikali ya Awamu ya Sita ambaye ametembelea miradi ya maendeleo jimboni kwake ikiwa ni siku ya jumapili ambayo anapaswa kupumzika.