HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WAZIRI NDEJEMBI ATOA ONYO KWA MKANDARASI ANAYETEKELEZA MRADI WA SONGEA–TUNDURU–MASASI

July 22, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu - Tunduru, Ruvuma


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameonesha kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Masasi kupitia Tunduru na kuagiza mkandarasi kuongeza juhudi ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa maendeleo ya mradi huo leo Julai 22, 2026, Mhe. Ndejembi amesema Serikali haitakuwa tayari kuona miradi ya kimkakati inayogusa maisha ya wananchi ikicheleweshwa bila sababu za msingi.


Amesema mradi huo ni miongoni mwa miradi muhimu ya Sekta ya Nishati inayopewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutokana na mchango wake katika kuimarisha upatikanaji wa umeme na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa Kusini.


“Maendeleo ya mradi huu hayaridhishi ukilinganisha na muda uliopita tangu utekelezaji wake uanze. Serikali inatarajia kuona kasi kubwa zaidi ya utekelezaji katika kipindi kilichobaki. Nimemuagiza Katibu Mkuu kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo haya na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa iwapo hakutakuwa na maboresho yanayoonekana,” amesema Mhe. Ndejembi.


Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Nyasa, Mhe. Boniface Magiri, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, amesema Mkoa utaendelea kushirikiana na Serikali Kuu katika kufuatilia utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha unakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati.


Naye Mhe. Sikudhani Chikambo kwa niaba ya wabunge wa Mkoa wa Ruvuma, viongozi hao wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya umeme ambayo itachochea ukuaji wa uchumi, uwekezaji na kuboresha huduma za kijamii katika maeneo ya Kusini mwa Tanzania.


Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea kupitia Tunduru hadi Masasi unatekelezwa na Mkandarasi Kalpataru Power kutoka India. Mradi huo unatarajiwa kuiunganisha Mikoa ya Lindi na Mtwara kwenye Gridi ya Taifa pamoja na kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Wilaya ya Tunduru na maeneo jirani.



HUKUMU YA TIKTOKER GHANA -SOMO KWA UHURU WA KUJIELEZA NA WAJIBU WA WATUMIAJI WA MITANDAO

July 22, 2026 Add Comment

 


Hivi karibuni, Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Accra ilimuhukumu Camilla Alhassan, mshawishi maarufu wa TikTok (Tiktoker), kifungo cha mwaka mmoja jerezani. Adhabu hii ilitolewa baada ya mshtakiwa kukiri makosa ya kusambaza taarifa za uongo na kufanya tabia ya kuudhi (offensive conduct) dhidi ya Rais John Dramani Mahama. 


Kesi hii inaashiria hatua kubwa katika udhibiti wa maudhui ya kidijitali barani Afrika na inaibua maswali muhimu kuhusu mipaka ya uhuru wa kujieleza na wajibu wa kisheria wa watumiaji wa mitandao ya kijamii.


Hukumu dhidi ya Alhassan inasimama juu ya *misingi miwili mikuu* ya kisheria inayolenga kulinda usalama wa jamii na sifa za watu


Mosi, Kusambaza Taarifa za Uongo (False News) -  Sheria za Ghana zinakataza utengenezaji au usambazaji wa taarifa ambazo mtengenezaji anajua au ana sababu ya kuamini kuwa ni za uongo, hususan kama zinaweza kusababisha hofu au taharuki miongoni mwa jamii. 


Pili, Tabia ya Kuudhi (Offensive Conduct) - Matumizi ya lugha au madai yanayolenga kudhalilisha, kuchochea chuki, au kuhatarisha amani ya umma—katika muktadha huu, kumhusisha kiongozi wa nchi na matendo ya ushirikina na kafara ya wanyama kwa malengo ya kisiasa.


Sakata hili linaangazia athari kubwa za mitandao ya kijamii katika nyanja za siasa na utulivu wa kijamii:-


*Mmomonyoko wa Imani ya Kisiasa:* Kudai kuwa Rais alifanya matambiko kwa kuzika ng'ombe 32 nchi nzima kulilenga kuchafua sifa yake na kupunguza uaminifu wake mbele ya wapiga kura, jambo linaloweza kuathiri mchakato wa kidemokrasia.


*Silaha ya Algorithm na Ushawishi:* Kama "Tiktoker," Alhassan alitumia nguvu ya ushawishi wake (clout) kupata watazamaji wengi. Katika zama za kidijitali, taarifa za kusisimua na za uzushi husambaa haraka kuliko ukweli, jambo linalofanya madhara yake kuwa makubwa na ya haraka.


*MAANA YA HUKUMU HII KWA MUSTAKABALI WA KIDIJITALI  (IMPLICATIONS)*


Uamuzi wa Jaji kukataa ombi la mawakili wa Alhassan la kupunguza adhabu una ujumbe mzito


Mahakama imeweka wazi kuwa umaarufu wa mtandaoni (social media fame) sio ngao dhidi ya sheria. Kifungo hiki kinatumika kama onyo kwa waundaji wengine wa maudhui (content creators) kuwa uhuru wa kujieleza unaambatana na wajibu.


Aidha, Kesi hii inaongeza msukumo kwa serikali za Kiafrika kuimarisha mifumo ya kufuatilia na kuchukua hatua dhidi ya uhalifu wa kimtandao (cybercrime).


*USHAURI WANGU*


Hukumu ya Camilla Alhassan ni kielelezo cha namna mifumo ya sheria inavyolazimika kubadilika ili kukabiliana na changamoto mpya zinazoletwa na teknolojia. 


Wakati mitandao ya kijamii ikiendelea kuwa jukwaa kuu la mijadala ya umma, kesi hii inakumbusha jamii kuwa maneno yana madhara ya kisheria, na kwamba ulimwengu wa kidijitali unapaswa kuongozwa na ukweli, maadili, na heshima kwa utu wa wengine.


Kama Tanzania Tuna paswa kuchukua hatua za wazi kwa wahalifu wa mitandao na kama nilivyo shauri mara zote tunaweza kupitia hatua tatu ili tuweze kukuza uelewa kwa wananchi na hatimae watakao kaidi zaidi tuwawajibishe kwa mujibu wa sheria za nchi


*Hatua ya Kwanza :* Wahalifu wakwamatwe na kwa uwazi watangazwe na kuonywa kisha waachiwe - Hii itakua somo kwa wengine ambao wana kawaida ya kufata mkumbo kwenye kutenda uhalifu wa kimtandao na wakidhani serikali imelala


*Hatua Ya Pili:* Mhalifu anapo rudia akamatwe tena kwa uwazi na kulipishwa faini kwa mujibu wa sheria zetu - Pesa zitakazo patikana kwneye hili ziwekwe kwenye mfuko maalum utakao saidia kuimarisha udhibiti wa uhalifu mtandao kupitia elimu ya uelewa na nyezo nyingine za udhibiti


*Hatua ya tatu:* Mhalifu anapo rudia mara ya tatu kunakua hakuna tena namna ila ni kufungwa kwa mujibu wa sheria za nchi yetu na hili liwe somo kwa wengine wote.


Naomba kuwasilisha.


*Yusuph Kileo ,*

Mtaalam wa usalama mtandao na Uchunguzio wa makosa ya Kidigitali

Dar Es Salaam, Tnazania

19 - July - 2026.

CCM YATHIBITISHA MSINGI WA KUHUDUMIA WANANCHI KWA VYAMA TAWALA AFRIKA

July 22, 2026 Add Comment

 

Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), Ndugu Rabia Abdalla Hamid , ameshiriki Mkutano Mkuu wa Chama cha Botswana National Front (BNF) unaofanyika mjini Jwaneng, Botswana, akiwakilisha Chama Cha Mapinduzi.


Akizungumza katika mkutano huo, Ndugu Rabia amesisitiza kuwa kila chama tawala kina wajibu wa kuwatumikia wananchi kwa uadilifu, kuimarisha misingi ya utawala bora, na kuendelea kutoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wananchi bila kuchoka.


Aidha, amekisii Chama cha BNF kuendelea kuzingatia maslahi ya wananchi katika utekelezaji wa sera na maamuzi yake, pamoja na kuhakikisha kuwa hakuna mwananchi anayebaki nyuma katika mchakato wa maendeleo ya taifa.

Aidha,Ndg. Rabia amempongeza Rais wa Chama cha Botswana National Front (BNF) na Rais wa Jamhuri ya Botswana, Mheshimiwa Duma Gideon Boko kwa  ushindi wa Chama chake na kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa Jamhuri ya Botswana. 


Ameeleza kuwa kuchaguliwa kwa Rais Boko na Chama cha BNF ni kielelezo cha imani waliyopewa na wananchi wa Botswana na  amewatakia mafanikio katika kuwaletea maendeleo  na ustawi wao.

DC NYAMWESE AWATAKA WAKURUGENZI KUSIMAMIA FEDHA ZA SERIKALI KWA UADILIFU

July 22, 2026 Add Comment

 



Na Oscar Assenga, Tanga


Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Salum Nyamwese, amewataka wakurugenzi wa halmashauri kuhakikisha kila fedha inayotolewa na Serikali kwa ajili ya miradi ya maendeleo inasimamiwa kwa uadilifu na kutumika kulingana na malengo yaliyokusudiwa.

Nyamwese ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Handeni amesema matumizi mabaya ya fedha za umma, rushwa na ubadhirifu vinaweza kuwa kikwazo kikubwa katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.
Alitoa kauli hiyo mjini Tanga wakati akifungua  warsha ya wadau wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo mkoa wa Tanga iliyoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), iliyowakutanisha wakurugenzi wa halmashauri, wakuu wa taasisi za umma na viongozi mbalimbali kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha uwajibikaji na usimamizi wa rasilimali za umma.

Nyamwese alisema fedha zinazotolewa na Serikali ni mali ya wananchi, hivyo viongozi wenye dhamana wanapaswa kuhakikisha kila shilingi inatumika kwa ufanisi na kuleta manufaa yaliyokusudiwa.
“Fedha zinazotolewa na Serikali ni mali ya wananchi hivyo ni wajibu wa kila mkurugenzi kuhakikisha hakuna hata shilingi moja inayopotea au kutumika nje ya malengo yaliyokusudiwa. Tunapaswa kusimamia miradi kwa uadilifu na kuhakikisha wananchi wanaona thamani ya fedha zinazotolewa,” alisema.

Alisema warsha hiyo imefanyika wakati muafaka ambapo Serikali imeanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi shindani, taasisi imara, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya rasilimali za umma.
Kwa mujibu wa Nyamwese, utekelezaji wa dira hiyo hauwezi kufanikiwa iwapo viongozi hawataweka mbele maslahi ya wananchi na kupambana kikamilifu na vitendo vya rushwa, ubadhirifu na ukiukwaji wa taratibu.

“Rushwa ni adui mkubwa wa maendeleo kwani huhujumu matumizi sahihi ya rasilimali za umma, hudhoofisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hupunguza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi na kuondoa imani ya wananchi kwa taasisi za Serikali,” alisema.

Aliwataka wakurugenzi kushirikiana kwa karibu na Takukuru katika kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ndani, kuongeza uwazi katika matumizi ya fedha za umma na kuchukua hatua mapema dhidi ya viashiria vya ubadhirifu.
Nyamwese alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuelekeza uwekezaji mkubwa katika Mkoa wa Tanga kwa lengo la kuboresha huduma za kijamii na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Alieleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2025/2026, Mkoa wa Tanga umepokea zaidi ya Sh trilioni 3 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali katika sekta za elimu, afya, maji, kilimo, mifugo, uvuvi, biashara, uwekezaji, miundombinu ya barabara, nishati, ardhi na uwezeshaji wananchi kiuchumi.
Hata hivyo, alisema kiasi hicho kikubwa cha fedha hakitakuwa na maana bila kuwepo kwa usimamizi mzuri, ufuatiliaji wa karibu na uwajibikaji wa viongozi wanaosimamia miradi hiyo.

“Fedha pekee hazileti maendeleo. Kinacholeta maendeleo ni usimamizi mzuri, ufuatiliaji wa karibu na uwajibikaji wa viongozi wanaosimamia utekelezaji wa miradi,” alisisitiza.
Aliwataka wakurugenzi kufanya tathmini za mara kwa mara za miradi inayotekelezwa katika maeneo yao, kuhakikisha kazi zinafanyika kwa viwango vinavyotakiwa na kuchukua hatua dhidi ya watumishi au wakandarasi watakaobainika kukiuka sheria.
Akizungumzia fursa za maendeleo zilizopo mkoani Tanga, Nyamwese alisema mkoa huo unatarajiwa kuwa kitovu kikubwa cha biashara na uwekezaji kutokana na utekelezaji wa miradi ya kimkakati, ikiwemo uboreshaji wa Bandari ya Tanga, reli ya kisasa (SGR) pamoja na Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Alisema miradi hiyo itaongeza shughuli za kiuchumi na kuvutia wawekezaji wengi zaidi, hivyo viongozi wa halmashauri wanapaswa kuhakikisha mazingira ya uwazi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya rasilimali yanaendelea kuimarishwa.
Awali, akizungumza katika warsha hiyo, Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ( TAKUKURU) Ramadhan Ndwatah alisema taasisi hiyo imefanya tathmini ya miradi inayotekelezwa ndani ya Mkoa wa Tanga na kubaini baadhi ya changamoto zinazotokana na usimamizi usioridhisha.

Alisema changamoto hizo ni pamoja na ucheleweshwaji wa miradi, matumizi yasiyo sahihi ya fedha, ongezeko la gharama zisizo za lazima na kupungua kwa manufaa yaliyotarajiwa kwa wananchi.

“Licha ya mafanikio yaliyopatikana kwenye miradi ya maendeleo, bado kuna changamoto ya udhaifu katika utekelezaji wa miradi, ucheleweshwaji wa miradi kwabaadhi ya wadau wenye dhamana, kuongeza gharama zisizo za lazima na kupunguza manufaa yanayotarajiwa kwa wananchi,” alisema.

Alisema kutokana na changamoto hizo, wameona ni muhimu kukutana na wadau wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ili kuwakumbusha wajibu wao katika kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa ufanisi.
Aliwataka wadau wote wenye dhamana ya kusimamia miradi kushirikiana na TAKUKURU ili kutimiza azma ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo kupitia miradi mbalimbali.

Mkurugenzi Tanga Jiji atoa ushauri kuhusu BOQ

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Tanga, Mhandisi Juma Hamsini, aliiomba Serikali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI kuzingatia thamani halisi ya vifaa vinavyotumika wakati wa kuandaa BOQ za miradi mbalimbali ya ujenzi, ikiwemo madarasa.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha gharama zinazowekwa kwenye miradi zinaendana na hali halisi ya soko na kusaidia utekelezaji wa miradi yenye ubora na thamani kwa wananchi.



TANZANIA MGENI RASMI MAONESHO YA UFUGAJI NYUKI AFRIKA NCHINI ALGERIA

July 21, 2026 Add Comment

  



Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe Mobhare Matinyi, akizungumza na vyombo vya habari vya Algeria wakati akitangaza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi katika Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika (Africa Bee Expo) yatakayofunguliwa jijini Algiers mnamo Septemba 3, 2026.

WAZIRI SANGU: BONDE LA ZIWA RUKWA NI HAZINA YA AJIRA KWA VIJANA

July 21, 2026 Add Comment
Mbunge wa Jimbo la Kwela ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Deus Sangu akipata Maelezo kutoka kwa msimamizi wa mradi wa ujenzi wa madarasa Noble Helium ambayo Inafanya shughuli za utafiti na uchimbaji wa gesi ya helium Christian Temba (20 Julai 2026) alipokuwa akikagua miradi ya Maendeleo katika Kijiji cha Kinambo Kata ya Milepa Wilaya ya Sumbawanga.

NEWALA KUNUFAIKA NA UMEME WA UHAKIKA

July 21, 2026 Add Comment



📌*Ni baada ya kukamilika kwa njia ya kusafirisha umeme ya kilovoti 33 Masasi - Mtwara*


📌*Mradi umeimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi wa Wilaya ya Newala na maeneo jirani.*


📌*MD Twange asema thamani ya mradi ni takribani shilingi bilioni 4.65*



📍Newala, Mtwara | Julai 22, 2026


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amezindua rasmi mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 33 kutoka Masasi hadi Newala, akieleza kuwa mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na kuweka mazingira wezeshi kwa ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Newala.


Akizungumza wakati wa uzinduzi wa njia hiyo, Mhe. Ndejembi amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaendelea kuwekeza katika miradi ya kimkakati ya umeme ili kuhakikisha huduma ya nishati inawafikia wananchi wengi zaidi na kuwa chachu ya maendeleo.

"Njia hii ya umeme ni msingi wa kukuza uchumi, kuongeza uzalishaji, kuvutia uwekezaji na kuboresha upatikanaji wa umeme kwa Wilaya ya Newala," amesema Mhe. Ndejembi.


Aidha, Waziri Ndejembi amesema Serikali itaendelea kuhakikisha Mikoa ya Lindi na Mtwara inapata umeme wa uhakika ikiwa ni pamoja na kuiunganisha Mikoa hiyo na umeme wa gridi ya Taifa.

Akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mkuu wa Wilaya ya Newala, Mhe. Mwangi Kundya amesema miradi mbalimbali imeendelea kutekelezwa Mkoa wa Mtwara.


"Mheshimiwa Waziri niipongeze Serikali kwani Vijiji vyote vya Mkoa wa Mtwara 785 vinapata huduma ya umeme". Amesema Mhe. Mwangi.



Ameongeza kuwa katika kuboresha huduma kwa wateja mkoa wa Mtwara umepokea vitendea kazi yakiwemo magari kumi na moja, bajaji nne na pikipiki tisa.

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mha. Felchesmi Mramba amesema Serikali imekuwa ikiboresha uwekezaji na upatikanaji wa umeme Mikoa ya  Mtwara na Lindi.


"Mahitaji ya Lindi na Mtwara yameendelea kuongezeka na Serikali imewekeza kwenye uzalishaji na hivi sasa Mkoa wa Mtwara tunazalisha zaidi ya megawati 50". Amesema Mha. Mramba.

Awali akitoa taarifa za utekelezaji wa mradi Mkurugenzi Mtendaji TANESCO, Bw. Lazaro Twange amesema ujenzi wa njia hiyo umetekelezwa kwa shilingi bilioni 4.56 kwa umbali wa Kilometa 76 kutoka Masasi hadi Newala.

"Mheshimiwa mgeni rasmi kabla ya mradi huu kutekelezwa Wilaya ya Newala ilikuwa ikipata umeme kutokea Mtwara kupitia Nanyumbu umbali wa kilometa 170, hali iliyochangia tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara". Amesema Bw. Twange.



Ameongeza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa njia hiyo ya umeme kumeimarisha upatikanaji wa umeme na kuondoa changamoto ya kukatika kwa umeme kwa Wilaya hiyo.



Aidha, Serikali kupitia TANESCO imetenga takribani shilingi bilioni 5.27 kwa ajili ya kujenga kituo cha kubadilishia umeme (Switching Station) kitakacho saidia kuboresha upatikanaji wa umeme na kukidhi mahitaji ya sasa na ya badaye ya wananchi na wawekezaji wa Wilaya ya Newala. 


Mbunge wa Newala Vijijini Dkt. Yahaya Nawanda kwa niaba ya Wabunge wa Mkoa wa Mtwara ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme Mkoa wa Mtwara.

KIKWETE AITAKA AFRIKA KUBADILI AHADI ZA AFYA KUWA UTEKELEZAJI WENYE BAJETI

July 21, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu, Accra, Ghana

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, amezitaka nchi za Afrika kuacha kutegemea matamko na ahadi zisizoambatana na utekelezaji, badala yake ziongeze uwekezaji wa ndani, uwajibikaji na matumizi ya ubunifu ili kuimarisha mifumo ya afya barani humo.

Dk. Kikwete alitoa kauli hiyo Julai 20, 2026, wakati akizungumza katika Mjadala wa Ngazi ya Juu wa Sera uliofanyika katika Hoteli ya Kempinski jijini Accra, Ghana, pembezoni mwa Mkutano Maalumu wa Umoja wa Afrika kuhusu Afya.

Mjadala huo uliwakutanisha mawaziri, watunga sera, taasisi za kikanda, washirika wa maendeleo, viongozi wa sekta binafsi na wataalamu wa afya kutoka mataifa mbalimbali, ukiandaliwa kwa ushirikiano kati ya African Renaissance Trust, Wakfu wa Jakaya Mrisho Kikwete, Tume ya Umoja wa Afrika na wadau wengine.

Akizungumza katika mkutano huo, Dk. Kikwete alisema utegemezi wa muda mrefu wa misaada ya nje katika kugharamia sekta ya afya hauwezi kuendelea kuwa msingi wa mifumo ya afya ya Afrika, hasa wakati misaada ya maendeleo inapopungua na mahitaji ya huduma bora za afya yakiongezeka.

Alisema bara hilo linapaswa kuongeza uwezo wa kugharamia huduma zake za afya kupitia mapato ya ndani, matumizi yenye ufanisi wa rasilimali na uwajibikaji katika matumizi ya fedha za umma.


“Ujumbe kutoka Eswatini hadi Accra ni mmoja; Afrika lazima igharamie, izalishe na ilinde mustakabali wake wa afya,” alisema.

Dk. Kikwete alikumbusha kuwa ni miaka 25 sasa tangu kupitishwa kwa Azimio la Abuja la mwaka 2001 lililozitaka nchi wanachama wa Umoja wa Afrika kutenga angalau asilimia 15 ya bajeti zao kwa sekta ya afya, lakini nchi nyingi bado hazijafikia lengo hilo.

Alisema hali hiyo imeendelea kuchangia mzigo mkubwa wa magonjwa kama UKIMWI, kifua kikuu, malaria, pamoja na vifo vinavyoweza kuzuilika vya wajawazito na watoto wachanga.

Katika hotuba yake, Dk. Kikwete alieleza kuwa usalama wa afya ya mama na mtoto unapaswa kuwa kipaumbele kikuu, akibainisha kuwa takribani wanawake 260,000 hufariki kila mwaka duniani kutokana na matatizo yanayohusiana na ujauzito na kujifungua, huku karibu asilimia 70 ya vifo hivyo vikirekodiwa barani Afrika.

Alisisitiza kuwa changamoto si ukosefu wa maarifa, dawa au teknolojia, bali ni kushindwa kuzifikisha huduma hizo kwa wananchi wanaozihitaji.


“Mama anaporudi nyumbani salama, ni kwa sababu fedha, ushahidi wa kisayansi na utoaji wa huduma vimefanikiwa kukutana,” alisema.

Akitoa mfano wa Tanzania, Dk. Kikwete alisema ushirikiano kati ya Wakfu wa Jakaya Mrisho Kikwete, Wizara ya Afya na taasisi za utafiti umechangia kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto kupitia tafiti na mikutano ya kisayansi inayofanyika kila baada ya miaka miwili.

Alisema juhudi hizo zimechangia kupungua kwa vifo vya wajawazito kutoka zaidi ya vifo 550 kwa kila watoto 100,000 wanaozaliwa hai hadi vifo 104, hatua inayoiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya kufikia lengo la Maendeleo Endelevu la kupunguza vifo hivyo hadi 70 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, alisema mafanikio ya sekta ya afya hayapaswi kupimwa kwa kiwango cha fedha kinachotengwa pekee, bali kwa matokeo yanayowafikia wananchi.

“Swali si tunatumia kiasi gani katika afya. Swali ni kama uwekezaji wetu unawafikia wananchi wanaouhitaji zaidi,” alisema.

Katika mkutano huo pia ulizinduliwa mfumo wa African Renaissance Health Financing Insights Dashboard, utakaosaidia serikali kufuatilia ahadi za kifedha, matumizi ya bajeti, mapungufu ya fedha pamoja na matokeo ya uwekezaji katika sekta ya afya.

Dk. Kikwete alisema mfumo huo utasaidia kuimarisha uwajibikaji na ushirikiano kati ya wizara za afya na wizara za fedha ili kuhakikisha fedha zinazotengwa zinaleta matokeo yanayotarajiwa.

Pia alihimiza Afrika kupunguza utegemezi wa dawa na chanjo kutoka nje kwa kuwekeza katika uzalishaji wa ndani, kuimarisha Wakala wa Dawa wa Afrika na kutumia fursa za biashara ya kikanda kuimarisha usalama wa afya.

Katika mapendekezo yake, Dk. Kikwete aliwasilisha vipaumbele vitano ambavyo ni kuifanya afya kuwa uwekezaji wa kimkakati, kuongeza mapato ya ndani kupitia bima na kodi bunifu, kulinda huduma muhimu wakati misaada inapopungua, kuimarisha uwajibikaji na kuongeza ushirikiano wa kikanda.

Kwa upande wake, Kamishna wa Umoja wa Afrika anayeshughulikia Afya, Masuala ya Kibinadamu na Maendeleo ya Jamii, Balozi Amma Twum-Amoah, alisema mafanikio ya sera za afya yanapaswa kupimwa kwa maboresho yanayoonekana katika maisha ya wananchi.

Akihitimisha hotuba yake, Dk. Kikwete alisema Afrika haina upungufu wa mikakati wala ubunifu, bali changamoto iliyopo ni utekelezaji wa maamuzi yaliyokwishafikiwa.


“Tuondoke Accra tukiwa na dhamira ya kubadili ahadi kuwa bajeti, bajeti kuwa programu, programu kuwa matokeo yanayopimika, na matokeo kuwa maisha marefu, yenye afya na uzalishaji zaidi kwa wananchi tunaowahudumia,” alisema.

MASAUNI: UWEKEZAJI WA VIWANDA UZINGATIE SHERIA YA MAZINGIRA

July 20, 2026 Add Comment
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni (kulia) akimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge mara baada ya kuwasili mkoani humo kwa ajili ya ziara ya kikazi ambayo anatarajia kuifanya kuanzia leo Julai 20,2026.

SANGU: WALIOFUJA FEDHA ZA SHULE MFINGA WAFIKISHWE MAHAKAMANI

July 20, 2026 Add Comment
Mbunge wa Jimbo la Kwela ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akizungumza na Viongozi na Wananchi mara baada ya kukagua mradi wa Shule ya Msingi Mfinga iliyopo Sumbawanga, Mkoani Rukwa tarehe 19 Julai, 2026.

WAZIRI KAKURWA ATOA MWELEKEO WA KUTATUA CHANGAMOTO ZA WAFANYABIASHARA WA MIFUGO

July 19, 2026 Add Comment
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Balozi Dkt. Bashiru Ally Kakurwa, akizungumza na wafanyabiashara wa mifugo na mazao yake wakati wa kikao kilichoandaliwa na Umoja wa Wafanyabiashara wa Mifugo na Mazao Yake Temeke (UWAMIMATE), kilichofanyika Julai 19, 2026 katika Ukumbi wa Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Temeke, Dar es Salaam. Katika kikao hicho, wafanyabiashara waliwasilisha changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya biashara ya mifugo na mazao yake, huku Waziri akiahidi kuzifanyia kazi kwa kushirikiana na wizara na taasisi husika

TRAMEPRO YAENZI URITHI WA NELSON MANDELA, YATAKA JAMII KUJENGA AMANI

Kajunason July 19, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu

SHIRIKA la Dawa Asilia na Ulinzi wa Mazingira Tanzania(TRAMEPRO Tanzania ) limetoa mwitokwa Watanzania, Waafrika na jumuiya ya kimataifa kuendelea kujenga jamii inayoheshimu utu wa kila mtu, kuwekeza katika elimu, afya, sayansi, mazingira na amani.

TRAMEPRO imetoa mwito huo leo Julai 18,2026 katika kukimbizi ya kuzaliwa kwa Hayati Nelson Mandela aliyekuwa Rais wa nchi ya Afrika Kusini.

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu TRAMEPRO Tanzania Boniventura Mwalongo amesema wanaungana na mataifa ya Afrika na dunia kuadhimisha kumbukizi ya kuzaliwa kwa Hayati Nelson Mandela mmoja wa viongozi mashuhuri waliobadilisha historia ya dunia kwa kupigania uhuru, usawa, haki za binadamu na maridhiano.

Pia amesema mambo ya kujifunza kupitia kutoka kwa Nelson Mandela ni kwamba elimu ni silaha yenye nguvu zaidi ya kubadilisha dunia, msamaha ni nguvu, si udhaifu; hujenga taifa lenye umoja.

Mengine ni uvumilivu na subira vinaweza kushinda hata changamoto kubwa, Uongozi ni huduma, si nafasi ya kutawala wengine, haki na usawa ni msingi wa maendeleo endelevu.

"Mandela anatufundisha pia umoja wa Waafrika na kuheshimiana ni nguzo ya maendeleo ya bara letu. Afya, mazingira na maendeleo vinapaswa kwenda pamoja kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho, " amesema Mwalongo.

Akieleza zaidi amesema kwa waratibu asili Asili,TRAMEPRO Tanzania inaona mafunzo makubwa kutoka kwa Mandela katika kujenga umoja wa sekta, kuzingatia maadili ya taaluma, kuendeleza utafiti, kuhifadhi mimea tiba, kulinda mazingira na kushirikiana na taasisi za kisayansi ili tiba asili ichangie kikamilifu afya na maendeleo ya jamii.

Kuhusu historia ya Nelson Mandela alizaliwa Julai 18, 1918 katika kijiji cha Mvezo, Mkoa wa Eastern Cape, Afrika Kusini. Jina lake la asili, Rolihlahla, katika lugha ya Kixhosa humaanisha mtu anayetikisa tawi la mti, na kwa maana ya kawaida huashiria mtu mwenye kuhoji au kupinga hali iliyopo.

Alipoanza shule ya msingi, mwalimu wake alimpa jina la Nelson, kama ilivyokuwa desturi ya wakati huo katika shule nyingi za kikoloni.

Mandela alizaliwa katika familia ya kifalme ya kabila la Thembu. Baba yake aliitwa Gadla Henry Mphakanyiswa Mandela, aliyekuwa mshauri wa mfalme wa Thembu, na mama yake aliitwa Nosekeni Fanny Mandela.

Kutoka kwa wazazi wake alijifunza heshima, uwajibikaji, uongozi na umuhimu wa kuitumikia jamii.

Katika elimu, Mandela alianza masomo katika shule za wamisionari, akaendelea katika Chuo cha Healdtown, kisha akasoma katika Chuo Kikuu cha Fort Hare.

Baadaye alisomea sheria katika Chuo Kikuu cha Witwatersrand, ambako alijiandaa kuwa mwanasheria na mtetezi wa haki za wanyonge. Elimu yake ilimpa msingi wa kuelewa sheria na kuitumia kutetea usawa na utu wa binadamu.

Mandela aliongoza mapambano dhidi ya mfumo wa ubaguzi wa rangi (Apartheid). Kutokana na msimamo wake, alifungwa gerezani kwa miaka 27, lakini hakukata tamaa wala kuacha kuamini kuwa amani na maridhiano vinaweza kushinda chuki. Baada ya kuachiwa huru mwaka 1990, aliongoza mazungumzo yaliyoweka msingi wa Afrika Kusini mpya yenye demokrasia.

Mwaka 1994, Nelson Mandela aliingia katika historia kwa kuwa Rais wa kwanza mweusi wa Afrika Kusini aliyechaguliwa kidemokrasia. Uongozi wake ulijengwa juu ya maridhiano, msamaha na umoja wa kitaifa. Mwaka 1993, alitunukiwa Tuzo ya Amani ya Nobel kwa mchango wake katika kumaliza Apartheid kwa njia ya amani.

UANAGENZI UTAWATOA VIJANA KIMAISHA: WAZIRI SANGU

July 19, 2026 Add Comment
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu akifuatilia maelezo ya Kijana Mnufaika wa Mafunzo ya Uanagenzi Fani ya Ufundi Bomba, Ismail Mbogo alipotembea Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST), kampasi ya Rukwa.

St Anne Marie Academy yasomesha waliofiwa na wazazi tangu mwaka 2029

July 19, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu

Waziri wa zamani wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka ameangalia maonesho ya sayansi wataka wakaguzi wa shule kutenda haki kwa shule binafsi na kuziona kama mshirika wa maendeleo badala ya mshindani.

MASAUNI: UHIFADHI WA UDONGO NI MSINGI WA MAENDELEO ENDELEVU

July 19, 2026 Add Comment
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni, akizungumza na wadau mbalimbali wa mazingira kabla ya kushiriki matembezi yaliyolenga kuhamashisha jamii katika Uhifadhi na Utunzaji wa Mazingira yaliyofanyika Julai 19, 2026 jijini Dar es Salaam.

BODI YA NISHATI VIJIJINI YARIDHISHWA NA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA GEREZA LA MANYONI

July 19, 2026 Add Comment
Bodi ya Nishati Vijijini (REB) imeridhishwa na hatua, ubunifu na kasi ya mageuzi yanayotekelezwa na Gereza la Manyoni, mkoani Singida, katika kuachana na nishati isiyo safi na kuanza kutumia bidhaa na teknolojia za Nishati Safi ya Kupikia.

SHIRIKA LA FROM HEARTS 2 HANDS LAJENGA MAKTABA YA KISASA KUNUFAISHA WANAFUNZI 737 WA JAMII YA KIMASAI , MONDULI

July 19, 2026 Add Comment

   

Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Gloriana Kimath akipata maelezo mbalimbali kuhusu Maktaba hiyo kutoka kwa mwanzilishi wa From Hearts 2 Hands , Dkt. Briana Greene (kushoto) wakati wa uzinduzi rasmi wa maktaba wilayani Monduli.
Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Gloriana Kimath (kulia0 akipata maelezo mbalimbali kuhusu Maktaba hiyo kutoka kwa mwanzilishi wa From Hearts 2 Hands , Dkt. Briana Greene wakati wa uzinduzi rasmi wa maktaba wilayani Monduli.
Mkuu wa Wilaya ya Monduli , Gloriana Kimath akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa maktaba mpya iliyojegwa na Shirika la From Hearts 2 Hands kupitia mwanzilishi wake , Dkt. Briana Greene (kulia kwa Mkuu wa Wilaya) ambayo inafungua fursa ya kujifunza , utamaduni wa kujisomea , kupanua maarifa na kuongeza ufaulu wanafunzi wa Shule ya Msingi Lendikinya ya jamii ya wafugaji wa kimasai wilayani Monduli.
Mkuu wa Wilaya ya Monduli , Gloriana Kimath akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa maktaba mpya iliyojegwa na Shirika la From Hearts 2 Hands kupitia mwanzilishi wake , Dkt. Briana Greene (kulia kwa Mkuu wa Wilaya) ambayo inafungua fursa ya kujifunza , utamaduni wa kujisomea , kupanua maarifa na kuongeza ufaulu wanafunzi wa Shule ya Msingi Lendikinya ya jamii ya wafugaji wa kimasai wilayani Monduli.
Sehemu ya muonekano wa ndani wa maktaba hiyo ya kisasa
Sehemu ya muonekano wa ndani wa maktaba hiyo ya kisasa.
Sehemu ya muonekano wa nje wa maktaba hiyo ya kisasa.
***

SHIRIKA la From Hearts 2 Hands kupitia mwanzilishi wake , Dkt Briana Greene limezindua maktaba ya kisasa ambayo inaweza kuhudumia wanafunzi 737 wa Shule ya Msingi Lendikinya kutoka jamii ya wafugaji wa kimasai wilayani Monduli.

Akizungumza kwenye uzinduzi huo , Mkuu wa Wilaya ya Monduli (DC), Gloriana Kimath ameipongeza taasisi hiyo kwa kujenga maktaba ambayo ni miongoni mwa maktaba bora zaidi katika Mkoa wa Arusha.

Amesema ushirikiano kati ya Serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali umeendelea kuleta matokeo chanya katika kuboresha huduma za jamii, hususan sekta ya elimu hapa nchini.

"Ninatamani wakuu wa wilaya nyingine waje waione maktaba hii na wajifunze. Ni mradi wa mfano ambao umeongeza thamani kubwa katika elimu ya Wilaya ya Monduli," ameongeza.

Kimath amefafanua kwamba pamoja na uzuri wa jengo hilo, jambo muhimu zaidi ni kuhakikisha maktaba inatumika ipasavyo kwa kujenga utamaduni wa watoto kujisomea vitabu na kujifunza maarifa mapya.

Amesema ndani ya maktaba hiyo kuna vitabu vya historia, sayansi, lugha, sanaa na vifaa vya kujifunzia vitakavyowawezesha watoto kukuza vipaji na ubunifu wao.

Amewataka wazazi kuhakikisha watoto wanaendelea kujisomea hata wanaporejea nyumbani badala ya kuacha jukumu hilo kwa walimu pekee.

"Wazazi wana nafasi kubwa ya kuwajengea watoto utamaduni wa kusoma. Mtoto akitoka shuleni aendelee kupata muda wa kujisomea nyumbani," amefafanua.

Kimath amewahimiza wazazi wa jamii ya Kimasai kutowabagua watoto wa kike katika kupata elimu, akisema wao pia wana uwezo wa kufikia nafasi mbalimbali za uongozi.

"Mimi ni mtoto wa kike na leo nimekuwa Mkuu wa Wilaya wa kwanza mwanamke Monduli. Kama wazazi wangu wasingenisomesha, nisingefika hapa. Mtoto wa kike anaweza, tusimkatize ndoto zake kwa ukeketaji, ndoa za utotoni au vitendo vingine vinavyomnyima haki ya elimu," amesema.

Pia amewataka wananchi na viongozi wa kijiji kuilinda maktaba hiyo ili idumu kwa vizazi vijavyo, akisisitiza ni mali ya jamii nzima na si ya mtu mmoja ili kufanya vizuri kitaaluma.

Amewahimiza wakazi wa Monduli kuendelea kuwekeza katika elimu, akibainisha kuwa wilaya hiyo imeendelea kufanya vizuri kitaaluma.

"Elimu ndiyo ufunguo wa maisha. Katika matokeo ya Kidato cha Nne Mkoa wa Arusha, Monduli iliongoza, na katika matokeo ya Kidato cha Sita hatukuwa na Daraja la nne wala sifuri. Tukishirikiana Serikali, wazazi na walezi, tunaweza kufanya vizuri zaidi hadi ngazi ya taifa," amesema.

Akizungumza baada ya uzinduzi huo, Dk. Briana Greene amesema uwekezaji katika elimu ni njia bora ya kubadilisha maisha ya watoto wa jamii ya wafugaji na kuwapa nafasi ya kufikia ndoto zao.

Ameongeza kwamba alianza kusaidia shule hiyo kwa kujenga tenki hilo la na miundombinu ya maji baada ya kubaini changamoto zilizokuwepo, kabla ya kuendelea na ujenzi wa maktaba kupitia taasisi yake ya From Hearts 2 Hands.

"Elimu ndiyo msingi wa maendeleo ya jamii yoyote,tunataka watoto wa Lendikinya wapate fursa sawa na watoto wengine duniani. Hii ndiyo sababu tuliamua kujenga maktaba yenye vitabu na vifaa vitakavyowasaidia kujifunza kwa njia mbalimbali," amesema.

Amesema maktaba hiyo imejengwa baada ya kuona umuhimu wa wanafunzi kupata vitabu karibu ili vifungue fursa ya kujifunza zaidi.

"Nakumbuka nilikuja Lendikinya na niliona watoto wakihitaji maji,tukatengeneza tenki la maji nikaona wanahitaji maktaba waweze kujisomea vitabu,nikaamua kuijenga hapa nashukuru kwa Serikali kwa ushirikiano wa kufanikisha hili".

"Natumaini utamaduni mzuri wa kimasai ikifanikiwa huku watoto wakipata fursa ya kupanua mawazo yao na kupata maarifa mapya yanayoweza kuleta maendeleo katika jamii yao ninafuraha kubwa kukutana nanyi na kuweza kutoa mchango wangu kwa jamii,"ameongeza.

Amewataka wazazi wa jamii ya Kimasai kuhakikisha wanawapeleka watoto wote shule, hususan wasichana, akisema elimu ndiyo njia ya kuvunja mzunguko wa umaskini na kuwawezesha watoto kujitegemea baadaye.

"Pia nawaomba wanafunzi kuitunza maktaba hii na vifaa vyote vilivyomo. Hii ni rasilimali yenu na itawasaidia kukua kielimu na kutimiza ndoto zenu," amesema.

Akizungumza kwa niaba ya wazazi, diwani wa Kata ya Sepeko Joseph Kimaay, ameshukuru kwa ujenzi wa maktaba hiyo na kuwa itasaidia kukuza na kuboresha elimu.

"Katika kata na wilaya yetu kwa ujumla hakuna maktaba kama hui,tunashukuru kwa msaada huu na tunaamini bila ushirikiano mzuri wa Serikali na wadau binafsi leo tusingekuwa na jengo kama hili,tunaamini itaboresha elimu ya watoto wetu,"ameongeza.

Akisoma risala kabla ya uzinduzi huo, Mwalimu Mkuu Solomon. Godfrey amesema mradi huo ni wa kipekee katika Wilaya ya Monduli na unatarajiwa kubadilisha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi wa shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 1977.

Amesema shule hiyo ina wanafunzi 737, wakiwemo wavulana 331 na wasichana 406, pamoja na walimu wanane.

Godfrey ameongeza kuwa maktaba hiyo imewekewa samani, vitabu vya aina mbalimbali, vifaa vya michezo, muziki, sanaa, kompyuta na maeneo maalumu ya watoto kujifunzia kwa vitendo na kuwa uwepo wa maktaba hiyo utasaidia kuongeza utamaduni wa kujisomea kwa wanafunzi, walimu na jamii, kuchochea ubunifu, kuboresha mazingira ya kujifunzia na kuongeza kiwango cha ufaulu kutoka asilimia 86.02 kilichofikiwa mwaka 2025.

Mbali na maktaba hiyo, amesema shirika hilo limekuwa likitekeleza miradi mingine ya maendeleo katika kijiji hicho ikiwemo ujenzi wa tanki la maji lenye uwezo wa kuhifadhi lita 100,000, ugawaji wa matenki ya maji kwa wananchi, ujenzi wa nyumba za kuvunia maji ya mvua na ugawaji wa chupa 700 za kubebea maji kwa wanafunzi.

Naye mwanafunzi wa Darasa la Sita, Riziki Papaking, amewashukuru wadau wa elimu kwa kufanikisha ujenzi wa maktaba hiyo, akisema itawawezesha kupata mazingira bora ya kujisomea na kuongeza ufaulu wao.

"Tunawashukuru wadau wa elimu kwa kutujengea maktaba hii. Itatupa nafasi ya kujisomea zaidi, kuongeza maarifa, kufanya vizuri katika masomo na kutimiza ndoto zetu," amesema Riziki.

Wanafunzi 737 wa Shule ya Msingi Lendikinya wilayani Monduli wanatarajiwa kunufaika na maktaba ya kisasa iliyojengwa na shirika la From Hearts 2 Hands, huku wadau wakisema mradi huo utakuza utamaduni wa kujisomea, kuongeza ufaulu na kuwapa watoto wa jamii ya wafugaji fursa sawa za elimu.