HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WABUNIFU WA KITANZANIA KUONYESHA TEKNOLOJIA ZAO TANGA

July 30, 2026 Add Comment
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ametangaza maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu kwa mwaka 2026, yatakayofanyika kuanzia Agosti 15 hadi 24 katika viwanja vya michezo vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga.

MAMBAMIAMBA YAINGIA RASMI KATIKA SAFARI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

July 30, 2026 Add Comment

 





Wananchi wa Kata ya Mambamiamba, Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, leo Julai 30, 2026, wamejengewa uelewa kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia wakati wa hafla ya uzinduzi wa tawi la Tanzania Women Empowerment Network (TAWEN).


Hafla hiyo imezikutanisha taasisi mbalimbali za Serikali, wadau wa maendeleo na wananchi, ambapo kila taasisi imepata fursa ya kuwasilisha huduma zake pamoja na kuelezea fursa zinazopatikana katika sekta zake. Wizara ya Nishati ilitumia fursa hiyo kutoa elimu kuhusu faida za matumizi ya nishati safi ya kupikia, ikiwemo kulinda afya, kuhifadhi mazingira na kupunguza gharama za matumizi ya nishati.


Akiwasilisha mada, Mtaalamu kutoka Wizara ya Nishati, Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia, Mha. Benezeth Kabunduguru, amesema Serikali inaendelea kutekeleza Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034), unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034, kutoka asilimia 28.6 mwaka 2025.


Amesema lengo hilo litafikiwa kupitia ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo na wananchi katika kuongeza upatikanaji wa nishati safi ya kupikia na kuendelea kutoa elimu kuhusu faida za matumizi yake. Ameongeza kuwa matumizi ya nishati safi ya kupikia yanachangia kulinda afya za wananchi kwa kupunguza athari za moshi unaotokana na matumizi ya kuni na mkaa, kuhifadhi mazingira kwa kupunguza ukataji wa miti, pamoja na kuokoa muda na gharama zinazotumika katika shughuli za kupikia, hususan kwa wanawake na watoto.


Aidha, amewahimiza wananchi wa Kata ya Mambamiamba kuchangamkia matumizi ya teknolojia mbalimbali za nishati safi ya kupikia zinazopatikana nchini ili kuongeza matumizi ya nishati hiyo na kuunga mkono juhudi za Serikali za kufikia malengo ya Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.


Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya TAWEN, Balozi Amina Salum Ali, ameipongeza Wizara ya Nishati na taasisi zake kwa kuendelea kutoa elimu na kuhamasisha jamii kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia. Amesema juhudi hizo zinaongeza uelewa wa wananchi na kuwasaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu matumizi ya nishati.


Ameongeza kuwa TAWEN itaendelea kushirikiana na Wizara ya Nishati pamoja na wadau wengine kuhakikisha elimu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia inawafikia wanawake na jamii kwa ujumla ili kuongeza matumizi ya nishati hiyo kwa manufaa ya afya, mazingira na maendeleo ya kiuchumi ya wananchi.


LILIAN LIUNDI: MAZINGIRA WEZESHI NI UFUNGUO WA KUONGEZA USHIRIKI WA WANAWAKE KATIKA SEKTA YA USAFIRI WA UMEME

July 30, 2026 Add Comment

     

Mwanzilishi wa Mradi wa Pink Ride na Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP aliyemaliza muda wake, Lilian Liundi, akizungumza wakati wa mafunzo kwa wanawake madereva wa bajaji kuhusu usafiri wa umeme na usawa wa kijinsia, yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Mwanzilishi Mradi wa Pink Ride wa Wanawake Madereva wa Magari ya Magurudumu Matatu( Bajaj) na Mkurugenzi wa Mtandao wa Jinsia Tanzania TGNP aliyemaliza muda wake, Lilian Liundi amesema mabadiliko kuelekea matumizi ya vyombo vya usafiri vinavyotumia nishati ya umeme yanapaswa kuambatana na sera na mazingira wezeshi yatakayoongeza ushiriki wa wanawake katika sekta ya usafiri na kuwawezesha kunufaika na fursa za kiuchumi zinazojitokeza.

TIBAMAZOEZI YATAJWA KUWA SULUHISHO LA MAUMIVU YA MUDA MREFU

July 30, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu

Hospitali ya Medinova Specialized Polyclinic imezindua rasmi huduma ya Tibamazoezi (Physiotherapy) ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kupanua huduma za kibingwa na kuboresha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini.

TADB YAIMARISHA NGUVU YA WAKULIMA KUELEKEA DIRA YA MAENDELEO 2050

July 30, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

BENKI ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imesema imeendelea kuimarisha nafasi yake katika kufadhili sekta ya kilimo nchini baada ya mtaji wake kuongezeka kutoka Sh bilioni 60 hadi Sh bilioni 452.16, hatua iliyowezesha kupanua utoaji wa mikopo na huduma za kifedha kwa wakulima, wafugaji na wavuvi.

WAANDISHI WA HABARI WAPATIWA MAFUNZO YA WELEDI NA MAADILI

Kajunason July 30, 2026 Add Comment

Mwandishi Wetu, Dar es Salaam, Julai 29, 2026

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imeanza rasmi kutoa mafunzo kwa waandishi wa habari nchini, yakilenga kuimarisha weledi, maadili na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa waandishi wa habari wa Bongo FM jijini Dar es Salaam, redio dada ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya JAB, Tido Mhando, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo wa kuelewa na kutekeleza matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, kwa kuzingatia weledi, maadili na uwajibikaji.

“Mafunzo haya ni utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari. Leo tumeanza rasmi na waandishi wa habari wa Bongo FM, tutaendelea kwa vyombo vingine pia kwa sababu, kutakuwa na mafunzo ya muda mfupi na ya muda mrefu. Hivyo, mafunzo haya yawe fursa ya kujenga uwezo na kuweka msingi imara wa kukuza na kulinda taaluma ya uandishi wa habari kwa kuongeza maarifa na weledi,” amesema Wakili Kipangula.

Akiwasilisha mada kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, historia na uanzishwaji wake, katika mafunzo hayo yaliyoanza leo tarehe 29 Julai, 2026 katika ukumbi wa Bodi, Wakili Kipangula amesema sheria hiyo imeweka msingi wa kuimarisha taaluma ya habari kwa kubainisha viwango vya weledi, maadili na uwajibikaji

Amesisitiza kuwa JAB itaendelea kusimamia utekelezaji wa sheria hiyo kwa kuzingatia haki, uwazi na kuheshimu uhuru wa vyombo vya habari, huku ikihakikisha taaluma ya habari inalinda maslahi ya umma..

Aidha, amewataka waandishi wa habari kuzingatia sheria na maadili katika kila hatua ya ukusanyaji, uchakataji na usambazaji wa habari ili kujiepusha na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na ukiukaji wa taaluma.

Amesema kuzingatia misingi hiyo kunajenga weledi, kunalinda heshima ya taaluma na kuimarisha imani ya jamii kwa vyombo vya habari.
Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko, akiwasilisha mada kuhusu Maadili ya Uandishi wa Habari, amesema maadili ni nguzo muhimu ya taaluma inayojengwa katika misingi ya ukweli, usahihi, haki, mizania, uwajibikaji na kutanguliza maslahi ya umma.

Amesisitiza kuwa mwandishi wa habari hapaswi kuongozwa na kasi ya kuwahi kuripoti habari, shinikizo la mitandao ya kijamii, umaarufu au maslahi binafsi, bali na ukweli na uwajibikaji.

Baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo, akiwemo Bi. Irene Kilango na Bw. Anord Philemon, wameishukuru JAB kwa kuandaa mafunzo hayo, wakisema yamewaongezea uelewa kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, maadili ya taaluma na wajibu wa mwandishi wa habari katika kutekeleza majukumu yake kwa weledi.

"Mafunzo haya yametupatia maarifa muhimu yatakayotusaidia kutekeleza majukumu yetu kwa kuzingatia maadili, sheria na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari. Tunaamini yatachangia kuboresha utendaji wetu na kuongeza uwajibikaji katika kuhabarisha umma," wamesema washiriki hao.

Mafunzo hayo ni sehemu ya mpango endelevu wa JAB wa kuwajengea uwezo waandishi wa habari nchini ili kuhakikisha wanazingatia Sheria ya Huduma za Habari, maadili, weledi na viwango vya taaluma katika utekelezaji wa majukumu yao, kwa lengo la kuimarisha ubora wa huduma za habari na kulinda maslahi ya umma.

MAHAKAMA YAMFUNGA MIAKA 30 JELA KWA KUSAFIRISHA KILO 75.15 ZA MIRUNGI

July 29, 2026 Add Comment
Mahakama ya Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga imemhukumu Isa Musini Rashidi  maarufu kama Hamidu kifungo cha miaka 30 jela baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kusafirisha kilo 75.15 za dawa za kulevya aina ya mirungi (Khat).

PSSSF YAFIKIA WATOTO WENYE MAHITAJI MAALUM TANGA

July 29, 2026 Add Comment





Tanga, Julai 28, 2026

Katika kuendeleza dhamira yake ya kuchangia maendeleo ya jamii kupitia mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSI) chini ya kampeni yake ya #PSSSFKaribuNaJamii, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umekabidhi rasmi mradi wa miundombinu wenye thamani ya Shilingi milioni 25 katika Shule ya Msingi Majani Mapana iliyopo mkoani Tanga.

Mradi huo unahusisha ujenzi wa chumba cha darasa, chumba cha mapumziko pamoja na vifaa mbalimbali vya michezo kwa ajili ya watoto wenye mahitaji maalum.


Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Bw. Kwame Temu alieleza kuwa msaada huo unalenga kuunga mkono juhudi za Serikali kwa kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalum wanapata haki yao ya msingi ya elimu. 

Alisisitiza kuwa hatua hiyo itawasaidia wanafunzi hao kujifunza katika mazingira yanayowawezesha kujifunza kwa ufanisi, kushiriki katika michezo na kukuza vipaji vyao mbalimbali.

RAIS SAMIA AONGOZA KIKAO MAALUM CHA KAMATI KUU YA CCM ZANZIBAR

July 29, 2026 Add Comment

 


Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Akiongoza Kikao Maalum cha Halmashauri  Kuu ya CCM Taifa  kilichofanyika Zanzibar Jumatano tarehe 29 Julai, 2026.





===

MANYARA YAWEKA REKODI MPYA YA HISANI, SHILINGI BILIONI 1.3 ZATIKISA DAR

Kajunason July 29, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Dar es Salaam imeandika historia mpya katika harakati za kuboresha huduma za afya baada ya Mkoa wa Manyara kufanikisha zoezi kubwa la kuchangisha fedha lililowezesha kupatikana kwa zaidi ya Shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa njiti na kuimarisha huduma za afya katika mkoa huo.

Fedha hizo zilikusanywa kupitia hafla maalumu ya chakula cha jioni cha hisani (Manyara Tanzanite Marathon Dinner Gala) iliyofanyika Julai 24, 2026 katika Hoteli ya Serena, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto, ambayo inalenga kuongeza upatikanaji wa vifaa tiba vya kisasa, kuboresha huduma za watoto wachanga na kupunguza vifo vinavyotokana na kuzaliwa njiti.

Jumla ya Shilingi 1,356,900,000 zilipatikana kupitia ahadi za michango na fedha taslimu kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo, taasisi za fedha, makampuni binafsi, viongozi wa Serikali, wabunge, wafanyabiashara na wananchi waliojitokeza kuunga mkono kampeni hiyo.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi wa kitaifa na kikanda pamoja na wadau wa sekta ya afya, ambapo mshikamano mkubwa ulionekana katika jitihada za kuhakikisha watoto wanaozaliwa njiti wanapata huduma bora na salama.

Akizungumza baada ya harambee hiyo, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Babati Vijijini, Mhe. Daniel Baran Sillo, aliyekuwa mgeni rasmi, alisema mafanikio hayo yanaonesha moyo wa uzalendo na mshikamano wa Watanzania katika kusaidia sekta ya afya.

Alisema lengo la kampeni hiyo ni kufikisha zaidi ya Shilingi bilioni 1.5, huku akiwakaribisha Watanzania kushiriki Manyara Tanzanite Marathon itakayofanyika Agosti 22, 2026 mkoani Manyara.

“Tunawashukuru wadau wote waliojitokeza na kuchangia. Kila mchango una maana kubwa katika kuokoa maisha ya watoto wetu. Tunataka kuhakikisha hospitali zetu zinakuwa na vifaa vinavyohitajika kuwahudumia watoto njiti kwa kiwango cha kisasa,” alisema Mhe. Sillo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Sendiga, alisema kampeni hiyo imeibuka kuwa jukwaa muhimu la kuunganisha nguvu za Serikali na sekta binafsi katika kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto.

Aliwataka wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kujitokeza kuchangia ili kufanikisha lengo lililowekwa, akisisitiza kuwa uwekezaji katika afya ya watoto ni uwekezaji katika mustakabali wa taifa.


“Kila mtoto ana haki ya kuishi. Tunapowekeza katika vifaa tiba na huduma za watoto njiti, tunaokoa familia, tunaimarisha jamii na tunajenga taifa lenye nguvu,” alisema Mhe. Sendiga.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Andrew Method, alieleza kuwa mkoa huo unakabiliwa na changamoto kubwa ya watoto wanaozaliwa njiti, ambapo kati ya watoto 3,000 hadi 3,200 huzaliwa njiti kila mwaka.

Alisema idadi hiyo inaweka shinikizo kubwa katika vituo vya kutolea huduma za afya, hasa katika upatikanaji wa mashine za kusaidia watoto kupumua, incubators, vifaa vya ufuatiliaji wa afya za watoto wachanga na miundombinu ya huduma maalumu.
“Watoto njiti wanahitaji uangalizi wa karibu na vifaa maalumu. Bila uwekezaji wa kutosha, tunakuwa katika hatari ya kupoteza maisha ambayo yangeweza kuokolewa,” alisema Dkt. Method.

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, kuzaliwa njiti ni miongoni mwa sababu kuu zinazochangia vifo vya watoto wachanga duniani, na huduma bora katika saa na siku za mwanzo baada ya kuzaliwa ndiyo huamua kwa kiasi kikubwa uwezekano wa mtoto kuendelea kuishi.

Wadau waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuwa kampeni hiyo imeonesha mfano wa namna matukio ya michezo yanaweza kutumika kama nyenzo ya kuchangisha fedha kwa ajili ya miradi ya kijamii na maendeleo.
Mbio za Manyara Tanzanite Marathon zimekuwa zikikua kwa kasi na sasa zinatajwa kuwa moja ya matukio makubwa ya michezo na hisani nchini Tanzania, yakilenga kuhamasisha afya, utalii na maendeleo ya jamii kwa wakati mmoja.

Waandaaji wa marathon hiyo walisema fedha zitakazopatikana zitaelekezwa katika ununuzi wa vifaa tiba, uboreshaji wa huduma za watoto wachanga na kuimarisha uwezo wa hospitali za Mkoa wa Manyara kuhudumia watoto njiti kwa ufanisi zaidi.

Kampeni hiyo pia inaunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambazo zimekuwa zikilenga kuboresha huduma za afya, kupunguza vifo vya mama na mtoto, kuimarisha ustawi wa jamii na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora katika maeneo yote ya nchi.
Waandaaji wameendelea kutoa wito kwa Watanzania kushiriki mbio hizo au kuchangia kupitia akaunti maalumu za kampeni, wakisisitiza kuwa kila mchango ni hatua muhimu katika kuokoa maisha ya mtoto mmoja au zaidi.

Michango inaendelea kupokelewa kupitia CRDB Lipa Namba 113069180 na CRDB Account No. 10401215064 (Manyara Tanzania Marathon).

Kwa mafanikio yaliyopatikana katika usiku huo wa kihistoria, Mkoa wa Manyara umeonesha kuwa mshikamano wa jamii unaweza kuwa nguvu kubwa ya kuokoa maisha, huku kampeni ya Hatua Moja Okoa Maisha ya Mtoto ikiendelea kuwa mwanga wa matumaini kwa maelfu ya watoto wanaozaliwa njiti kila mwaka nchini Tanzania.