HABARI ZETU
Loading...

HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

MAKATIBU WAKUU WAKUTANA KUPITIA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA MUDA WA KATI WA PROGRAMU YA AFDP

September 15, 2026 Add Comment



Na; Mwandishi Wetu- Dar es Salaam

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi ameongoza Kikao cha Makatibu Wakuu kutoka katika  Wizara  zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP), Wakuu wa Taasisi pamoja na Wakurugenzi wa Sekta, pamoja na wataalam kutoka katika sekta hizo  na Ujumbe Kutoka Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) katika ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu Mtaa wa Magogoni Jijini Dar es Salaam tarehe 15 Septemba 2026.

Kikao hicho kimefanyika baada ya ziara maalumu ya wataalamu kutoka IFAD na AFDP kukamilisha ziara ya kutembelea maeneo yanayotekeleza Programu ya kuendeleza Kilimo na Uvuvi ya kupima matokeo utekelezaji wa program ya muda wa kati (MTR)

Pamoja na mambo mengine IFAD wamepongeza Serikali kwa Kusimamia vyema Shughuli za Programu kwa kuleta matokeo chanya kwa wananchi..Aidha  kikao hicho kimepokea wasilisho la dondoo lnayoainisha hoja za makubaliano yaliyopendekezwa kuhusiana na mwenendo wa utekelezaji wa Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP).



GASTECH 2026: GESI YA TANZANIA KUIWEKA NCHI KATIKA RAMANI YA DUNIA

GASTECH 2026: GESI YA TANZANIA KUIWEKA NCHI KATIKA RAMANI YA DUNIA

September 15, 2026 Add Comment


BANGKOK, Thailand:


Tanzania imeeleza dhamira yake ya kuchukua nafasi muhimu katika kuunda kizazi kijacho cha uzalishaji na usambazaji wa gesi asilia duniani, kwa kuendeleza rasilimali zake kwa viwango vya juu na kujenga mnyororo jumuishi wa thamani wa gesi.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, wakati akishiriki mjadala wa kimataifa wenye mada “The New Energy Powers: Who Will Shape the Next Era of Gas Supply?” katika Mkutano wa Gastech 2026 unaofanyika Bangkok, Thailand.

Mjadala huo umeangazia mabadiliko yanayoendelea katika soko la gesi duniani, changamoto za kijiografia na kisiasa, mabadiliko ya mahitaji ya nishati, kuibuka kwa vyanzo vipya vya usambazaji wa gesi pamoja na namna nchi zenye rasilimali ya gesi zinavyoweza kujipanga kuwa miongoni mwa wazalishaji na wasambazaji muhimu kuelekea kizazi kipya.

Akizungumza katika mjadala huo, Mhe. Salome amesema uzoefu wa Tanzania umeonyesha kuwa na rasilimali kubwa ya gesi pekee hakutoshi, bali thamani ya rasilimali hiyo huonekana pale inapoweza kubadilishwa kuwa nishati ya uhakika, yenye ushindani na inayochochea maendeleo ya kiuchumi.

Amesema historia ya gesi nchini Tanzania, ikiwemo ugunduzi wa gesi katika Songo Songo katika miaka ya 1970 na kuanza kwa uzalishaji wa kibiashara mwaka 2004, inatoa fundisho kwamba ugunduzi wa rasilimali pekee hauleti thamani bila uwekezaji, miundombinu, sera rafiki kwa uwekezaji, soko linalokua na dhamira ya pamoja kati ya Serikali na sekta binafsi.

Tanzania kwa sasa ina zaidi ya trilioni 57 za futi za ujazo za gesi asilia zilizogunduliwa, huku sehemu kubwa ya rasilimali hizo ikiwa katika maeneo ya bahari kuu.

Pamoja na rasilimali hizo kubwa, Tanzania imeendelea kutumia gesi ya nchi kavu na maji ya kina kifupi kama kichocheo cha maendeleo ya Taifa.

Kwa mujibu wa Mhe. Salome, Songo Songo na Mnazi Bay zimekuwa nguzo muhimu katika mfumo wa nishati wa Tanzania, zikichangia uzalishaji wa umeme na kuwezesha matumizi ya gesi katika viwanda, taasisi, kaya na sekta ya usafirishaji kupitia matumizi yanayokua ya gesi asilia iliyobanwa (CNG).

Kuunganisha Gesi na Soko la Dunia Mhe. Makamba amesema moja ya mafanikio muhimu ya Tanzania ni kuanza kuunganisha rasilimali za gesi na masoko ya Dunia, huku matumizi ya gesi yakipanuka kutoka katika uzalishaji wa umeme hadi viwanda, taasisi, kaya na sekta ya usafirishaji.

Amesema kwa sasa, matumizi ya gesi nchini katika uzalishaji wa umeme ni asilimia 69 huku asilimia 27 ikitumika viwandani, asilimia 3 katika usafirishaji na asilimia 1 katika taasisi na kaya.

Amesema mgawanyo huo unaonyesha kuwa Tanzania haitumii gesi kama rasilimali ya nishati pekee, bali pia kama kichocheo cha maendeleo ya viwanda, kuimarisha usalama wa nishati na kukuza uchumi wa Taifa.

Aidha Mhe. Salome amesisitiza kuwa matumizi ya gesi katika soko la ndani na utekelezaji wa miradi mikubwa ya kuuza gesi nje ya nchi havipaswi kuonekana kama mikakati inayokinzana, bali kama sehemu ya mkakati mpana wa kukuza soko la gesi na kuongeza thamani ya rasilimali hiyo kwa Taifa.

Amesema masoko ya ndani na kikanda yanaweza kutoa manufaa ya kiuchumi kwa haraka, kujenga miundombinu na kuongeza uwezo wa ndani, wakati miradi mikubwa ya kuuza gesi katika masoko ya kimataifa inafungua fursa za uwekezaji mkubwa, teknolojia na upatikanaji wa masoko ya kimataifa.

Tanzania katika kizazi kipya cha gesi duniani

Akijibu swali la msingi la mjadala kuhusu nchi zitakazokuwa mstari wa mbele katika kizazi kipya cha usambazaji wa gesi duniani, Mhe. Makamba amesema si lazima ziwe nchi zenye rasilimali nyingi zaidi, bali zile zitakazokuwa na mikakati bora ya uwekezaji, miundombinu ya usambazaji, upatikanaji wa masoko ya kimataifa na ushirikishwaji mpana wa wananchi katika mnyororo wa thamani wa gesi.

Amesema Tanzania ina fursa ya kuwa miongoni mwa nchi hizo kutokana na ukubwa wa rasilimali zake, nafasi yake ya kimkakati katika ukanda wa Afrika Mashariki, ongezeko la mahitaji ya nishati pamoja na juhudi zinazoendelea za kuendeleza miundombinu na masoko ya gesi.

Mhe. Makamba amesema Tanzania inalenga kuhakikisha kuwa rasilimali ya gesi inatumika kuongeza usalama wa nishati nchini, kuchochea uwekezaji na viwanda, kuongeza ajira na mapato ya Taifa, huku ikiiwezesha nchi kushiriki kikamilifu katika mnyororo wa thamani wa gesi wa kikanda na kimataifa.

Amesema hatua hizo zinaifanya Tanzania kuwa na nafasi ya kutumia rasilimali zake za gesi si kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya sasa pekee, bali pia kujenga msingi wa ushindani wa Taifa katika kizazi kijacho cha soko la gesi duniani.




DKT JAKAYA KIKWETE AHANI MSIBA WA NDUGU WA MBUNGE WA ZAMANI WA NKASI

DKT JAKAYA KIKWETE AHANI MSIBA WA NDUGU WA MBUNGE WA ZAMANI WA NKASI

September 15, 2026 Add Comment




Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, amemtembelea na kumpa pole Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Nkasi, Mhe. Ally Mohamed Keissy, kufuatia msiba wa shimeji yake – dada wa mkewe uliotokea hivi karibuni.

Dkt Kikwete akioneshwa nyumba aliyowahi kushi akiwa afisa wa CCM miaka ya 1980 alipomtembelea na kumpa pole Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Nkasi, Mhe. Ally Mohamed Keissy, kufuatia msiba wa shimeji yake – dada wa mkewe uliotokea hivi karibuni.

NCAA YAWAPIGA MSASA MALAIGWANAN

September 15, 2026 Add Comment

 

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro imeendesha mafunzo ya ujasiriamali kwa Malaigwanani ,wazee na kina mama maarufu wapatao 33 kutoka kata 11 za ndani ya eneo la hifadhi Ngorongoro ili kuwajengea uwezo wa kutambua fursa mpya za kiuchumi.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Kamishina Msaidizi Mwandamizi anayeshughulikia huduma za jamii bi Gloria Bideberi amesema lengo la semina hiyo ni kuhakikisha Malaigwanani na wazee hao wanapata elimu ya kutosha kuhusu ujasiriamali na namna ya kutumia fursa zinazopatikana katika maeneo yao.

Bi. Gloria alieleza kwamba elimu hiyo itakwenda sambamba na ziara za kujifunza kwa vitendo, ambapo washiriki watatembelea maeneo mbalimbali ya uzalishaji wa bidhaa ikiwemo kiwanda cha uzalishaji wa bidhaa za maziwa Tanga Fresh kilichopo Mkoani Tanga ili kujifunza namna bidhaa zinavyozalishwa, kuendelezwa na kufikishwa katika masoko.

“Lengo la mafunzo haya ni kuhakikisha kuwa wananchi hawa wanapata elimu ya kutosha na kuwawezesha kutembelea maeneo mbalimbali ya uzalishaji wa bidhaa ili kujifunza kwa vitendo zaidi,” alisema Gloria

Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro katika kuwawezesha wananchi kiuchumi na kuimarisha ushiriki wa jamii katika maendeleo endelevu ya eneo la Hifadhi Ngorongoro.









RISITI YA SH1.4 MILIONI YAMUINGIZA MATATANI

September 15, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu, LUSHOTO

MAHAKAMA ya Wilaya ya Lushoto imemtia hatiani mfanyabiashara wa vifaa vya ujenzi katika eneo la Soni, Issack Vitales Msigiti, kwa kosa la rushwa baada ya kushindwa kutoa risiti ya EFD yenye thamani ya Sh1,497,057.

Mshtakiwa huyo amehukumiwa kulipa faini ya Sh500,000 au kutumikia kifungo cha miaka mitatu jela baada ya kupatikana na hatia katika Shauri la Rushwa Na.17811/2026.

Akizungumza katika Taarifa yake hivi karibuni Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Tanga Ramadhani Ndwatah alisema hukumu  hiyo ilitolewa Agosti 11, 2026, mbele ya Hakimu Kavumo Masewa Mndeme, ambaye alisikiliza shauri hilo lililoendeshwa na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), John Chihangala.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka TAKUKURU, Msigiti alikutwa na hatia kwa kujipatia manufaa kwa kutotoa risiti ya EFD ya Sh1,497,057, jambo lililosababisha kukadiriwa kwa kiwango pungufu cha kodi katika makadirio ya mwaka uliofuata.

Taarifa hiyo ilisema suala hilo lilianza kubainika kupitia taarifa za kiintelijensia zilizopokelewa Agosti 5, 2026, na baadaye kufanyika kwa uchunguzi maalumu uliodumu kwa siku tatu, kuanzia Agosti 8 hadi 10, 2026.

Mshtakiwa alishtakiwa kwa kosa la rushwa kinyume na Kifungu cha 15(1)(a) na (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCA), Sura ya 329, Marejeo ya 2024.

Baada ya mahakama kumtia hatiani, ilimpa chaguo la kulipa faini ya Sh500,000 au kwenda jela miaka mitatu.

Hata hivyo, Msigiti alilipa faini hiyo na hivyo kuepuka kutumikia kifungo.

TAKUKURU imeendelea kusisitiza umuhimu wa wafanyabiashara kuzingatia sheria na taratibu za kodi, ikiwamo utoaji wa risiti za EFD, ili kuepusha migogoro na hatua za kisheria.


TAKUKURU (M) TANGA – LUSHOTO

Septemba 15, 2026

JK AONDOKA MKOANI TABORA BAADA YA ZIARA YAKE YA SIKU NNE

September 15, 2026 Add Comment


Muasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF), Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiondoka leo Septemba 16, 2026 baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku nne mkoani Tabora kwa kutembelea na kukagua zahanati pamoja na nyumba mbili za watumishi zilizojengwa katika Kijiji cha Gengesita, Kata ya Kizengi, Wilaya ya Uyui.

 Katika Uwanja wa ndege wa Tabora amesindikizwa na Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Dr Jafaar Seif na Mkuu wa Wilaya ya Urambo Dkt. Khamis Mkanachi na viongozi wengine wa wilaya na mkoa.

Muasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF), Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiondoka leo Septemba 16, 2026 baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku nne mkoani Tabora kwa kutembelea na kukagua zahanati pamoja na nyumba mbili za watumishi zilizojengwa katika Kijiji cha Gengesita, Kata ya Kizengi, Wilaya ya Uyui. Katika Uwanja wa ndege wa Tabora amesindikizwa na Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Dr Jafaar Seif na Mkuu wa Wilaya ya Urambo Dkt. Khamis Mkanachi na viongozi wengine wa wilaya na mkoa.
Picha ya pili Dkt Kikwete akisalimiana na wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) wanaohiudumu katika Uwanja wa Ndege wa Tabora wakati akiondoka mwishoni mwa ziara yake ya siku nne ya mkoa huo leo Septemba 15, 2026

TUME YA TAIFA YA UNESCO YASHIRIKI JUKWAA LA NNE LA KIMATAIFA LA MAADILI YA AKILI UNDE RIYADH RIYADH, SAUDI ARABIA:

September 15, 2026 Add Comment



 Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inashiriki katika Jukwaa la Nne la Kimataifa la Maadili ya Akili Unde linaloendelea mjini Riyadh, Saudi Arabia, likiwakutanisha wawakilishi kutoka nchi mbalimbali duniani kujadili namna ya kuhakikisha maendeleo na matumizi ya akili unde yanaongozwa na maadili, uwajibikaji na kuhudumia maslahi ya jamii.

Jukwaa hilo linatoa nafasi kwa nchi na wadau mbalimbali kubadilishana uzoefu na kujadili masuala yanayohusu mustakabali wa akili unde, ikiwemo namna ya kuimarisha mifumo ya sera na utawala, kujenga uwezo na kuhakikisha teknolojia hiyo inatumika kwa kuzingatia haki za binadamu, usalama, usawa na uwajibikaji.

Kwa Tume ya Taifa ya UNESCO, ushiriki huo ni sehemu ya kuendelea kuunganisha Tanzania na UNESCO katika mijadala na ajenda za kimataifa zinazohusu sayansi, teknolojia, elimu, utamaduni na maendeleo ya jamii.

Tume inawakilishwa katika jukwaa hilo na Bi Fides Mallya, Afisa Programu kutoka Sekta ya Sayansi Jamii ya Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anayeshiriki katika shughuli na mijadala mbalimbali inayoendelea katika jukwaa hilo.

TUME YASHIRIKI MJADALA WA AFRIKA

Katika jukwaa hilo, Tume ya Taifa ya UNESCO inashiriki pia katika mjadalawa viongozi na wadau kutoka Afrika unaolenga kujadili namna bara hilo linavyoweza kuwezeshwa ili kunufaika kikamilifu na maendeleo ya teknolojia ya akili unde.

Mjadala huo unaangazia umuhimu wa Afrika kuimarisha uwezo wake katika sayansi, teknolojia, utafiti, ubunifu na ujuzi wa kidijitali, pamoja na kujenga mazingira bora ya kisera na kitaasisi yatakayowezesha matumizi salama na yenye tija ya akili unde.

Kwa kushiriki katika mjadala huo, Tume inaendelea kufuatilia mwelekeo wa kimataifa kuhusu akili unde na kuchangia katika mijadala inayolenga kuhakikisha maendeleo ya teknolojia hiyo yanazingatia mahitaji ya jamii na yanachangia maendeleo jumuishi na endelevu.

USHIRIKI WA TUME WAIUNGANISHA TANZANIA NA UNESCO

Ushiriki wa Tume katika jukwaa hilo unaonesha nafasi yake muhimu kama kiungo kati ya Tanzania na UNESCO, kwa kuwezesha ushiriki wa nchi katika mijadala, programu na ajenda za UNESCO katika ngazi ya kimataifa.

Kupitia majukwaa hayo, Tume inaendelea kufuatilia maendeleo na mwelekeo wa kimataifa katika maeneo ya UNESCO, kubadilishana uzoefu na nchi nyingine na kutafuta fursa za ushirikiano zinazoweza kuchangia maendeleo ya Tanzania.

Katika eneo la akili unde, ushiriki huo unaipa Tume fursa ya kufuatilia mijadala kuhusu maadili, utawala na matumizi yanayowajibika ya teknolojia hiyo, huku ikiendelea kuhusisha mijadala ya kimataifa na mahitaji ya maendeleo ya Tanzania.

UJUMBE WA TUME WAKUTANA NA BALOZI

Katika mwendelezo wa ushiriki wa Tume katika jukwaa hilo, ujumbe wa Tanzania unaoshiriki katika shughuli za jukwaa umepata fursa ya kufanya kikao na Balozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia.

Kikao hicho kimekuwa fursa ya kubadilishana taarifa kuhusu ushiriki wa Tanzania katika jukwaa hilo na kuimarisha uratibu kati ya ujumbe wa Tanzania na Ubalozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia katika masuala yanayohusu shughuli za kimataifa.

Jukwaa la Nne la Kimataifa la Maadili ya Akili Unde linaendelea mjini Riyadh likiwa sehemu ya juhudi za kimataifa za kuimarisha ushirikiano katika kuhakikisha maendeleo ya akili unde yanaenda sambamba na maadili, uwajibikaji, haki za binadamu na maendeleo jumuishi.


PROF. SHEMDOE AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA MADARASA LINDI

PROF. SHEMDOE AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA MADARASA LINDI

September 15, 2026 Add Comment

Na: OWM – TAMISEMI, Mchinga – Lindi

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa madarasa manne na ofisi moja ya Mkuu wa Shule ya Msingi Mkwajuni, Kata ya Kitomanga, Manispaa ya Lindi, ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo yake ya kuhakikisha shule hiyo inarejeshewa miundombinu iliyoharibiwa na maafa.

Shule hiyo ilikumbwa na maafa Januari 29, 2026, ambapo madarasa mawili, ofisi ya Mwalimu Mkuu, nyumba mbili za walimu na vyoo vya wanafunzi viliezuliwa, huku darasa moja likiangukiwa na mkorosho.

Prof. Shemdoe ameweka jiwe la msingi katika mradi huo Septemba 14, 2026, alipofika shuleni hapo kukagua maendeleo ya ujenzi wa madarasa hayo na ofisi ya Mkuu wa Shule, unaogharimu Shilingi Milioni 96. Ujenzi huo ulianza baada ya hoja iliyowasilishwa Bungeni na Mbunge wa Jimbo la Mchinga, Mhe. Salma Rashid Kikwete, akiomba Serikali kutoa usaidizi wa haraka kufuatia maafa yaliyolikumba shule hiyo. 

Kufuatia hoja hiyo, Prof. Shemdoe alimuagiza Mkurugenzi wa Manispaa ya Lindi kuhakikisha fedha zinapatikana kwa haraka kwa ajili ya ujenzi wa madarasa hayo manne, agizo ambalo lilitekelezwa.

Akizungumza baada ya kukagua mradi huo, Prof. Shemdoe amesema Serikali imeonesha utayari wa kuchukua hatua za haraka pale wananchi wanapokabiliwa na changamoto zinazohitaji suluhisho la dharura.

“Mhe. Mkuu wa Mkoa, tuliomba ridhaa kwa Mhe. Rais ya kuomba fedha za kujenga madarasa haya manne ziletwe mara moja, na leo hii wote tumeshuhudia madarasa manne mazuri pamoja na ofisi ya Mkuu wa Shule hii ya Mkwajuni yaliyotokana na juhudi za Mbunge Mhe. Salma Rashid Kikwete za kuomba usaidizi wa haraka,” amesema Prof. Shemdoe.

Aidha, Prof. Shemdoe amewahakikishia wananchi wa Kata ya Kitomanga kuwa OWM–TAMISEMI italeta fedha nyingine kwa ajili ya kujenga madarasa zaidi katika shule hiyo, ili hatimaye shule hiyo iwe na madarasa mapya na kuondokana na matumizi ya madarasa ya zamani yaliyopo katika hifadhi ya barabara.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mchinga, Mhe. Salma Rashid Kikwete, amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kuweka jiwe la msingi katika katika Shule ya Msingi Mkwajuni, huku akimuomba kuendelea kusaidia upatikanaji wa majengo mengine ya madarasa na ofisi ili walimu wapate mazingira bora zaidi ya kufanyia kazi na wanafunzi kujifunza katika mazingira salama na rafiki.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mhe. Adam Kighoma Malima, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kumuamini na kumpa jukumu la kusimamia upatikanaji wa maendeleo kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi.

Mhe. Malima pia amemshukuru Mhe. Rais kwa utayari wake wa kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akiahidi kuendelea kuwatumikia wananchi wa Lindi kwa bidii na moyo wa uzalendo.

Katika ziara yake mkoani Lindi Septemba 14, 2026, Prof. Shemdoe pia ametembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo, ikiwemo Mradi wa Bandari ya Uvuvi ya Kilwa Masoko; Mradi wa ujenzi wa Jengo la Wazazi (Maternity Ward) na Jengo la Wodi ya Matibabu ya Watoto Wachanga (NCU) katika Hospitali ya Wilaya ya Kinyonga; Mradi wa ujenzi wa Shule ya Msingi katika eneo la Sekondari Mkunyule, Kata ya Mandawa; pamoja na Mradi wa ujenzi wa Shule ya Msingi Kitomanga ‘B’.        

SERIKALI HAITAVUMILIA WAFANYABIASHARA WA MKONGE WANAOFANYA UDANGANYIFU KATIKA MASOKO YA NJE

September 15, 2026 Add Comment

 




Na Oscar Assenga, TANGA

NAIBU Waziri wa Viwanda na Biashara ,Dennis Londo amesema Serikali haitawavumilia wafanyabiashara wa mkonge wanaofanya udanganyifu katika masoko ya nje huku akiitaka Bodi ya Mkonge Tanzania (TSB) kuchukua hatua za haraka dhidi ya wafanyabiashara wanaodaiwa kuchukua fedha kutoka kwa wanunuzi wa nje bila kupeleka bidhaa walizoahidi, ikisema vitendo hivyo vinahatarisha uaminifu wa Tanzania katika masoko ya kimataifa.

Amesema tabia hiyo ya baadhi ya wafanyabiashara inachafua taswira ya nchi na kuwaweka katika mazingira magumu wafanyabiashara wengine wanaofuata taratibu na kufanya biashara kwa uaminifu.

Londo alitoa kauli hiyo jijini Tanga wakati wa kikao kazi kati ya TSB, Chama cha Wakulima wa Mkonge (SAT) na wafanyabiashara wa zao hilo.

Amesema Tanzania inaendesha uchumi wa soko huria, lakini uhuru huo haupaswi kutumiwa kama mwanya wa kufanya biashara kinyume cha sheria au kukiuka misingi ya uaminifu katika masoko ya kimataifa.




“Nimesikia hapa wafanyabiashara wakilalamika kwamba wakati mwingine wanataka kukamatwa kwa sababu kuna baadhi ya wafanyabiashara wamefanya udanganyifu kwenye soko. Mtu akifanya hivyo anashindwa kujua kwamba huku nje yeye anatambulika kama Tanzania na wala si kampuni yake,” amesema.

Amesema Serikali haiwezi kuvumilia vitendo vinavyoweza kuilazimisha nchi kutumia muda na rasilimali nyingi kurejesha uaminifu na taswira yake katika masoko ya kimataifa.

Kutokana na hali hiyo, Naibu Waziri ameiagiza TSB, kwa kushirikiana na wadau wengine wa zao hilo, kuchukua hatua mapema dhidi ya wafanyabiashara watakaobainika kufanya vitendo hivyo ili kulinda soko la mkonge na maslahi ya wafanyabiashara wanaofuata sheria.




“Pamoja na kwamba Serikali inaendelea kuweka mazingira mazuri ya kibiashara, hatuwezi kuvumilia hilo,” amesema.
TSB: WACHUKUA FEDHA, HAWAPELEKI MIZIGO

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TSB, Saddy Kambona, amesema changamoto hiyo ni miongoni mwa mambo aliyokutana nayo katika ziara zake kwenye masoko ya mkonge duniani.

Amesema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakichukua fedha kutoka kwa wanunuzi wa nje, lakini baadaye kushindwa kupeleka mizigo, hali ambayo imeanza kuchafua jina la Tanzania katika masoko hayo.




“Kwenye ziara yangu nimekutana na malalamiko kwamba kuna wafanyabiashara wamechukua fedha halafu wameshindwa kupeleka mizigo. Watu wanafanya udanganyifu kwenye masoko ya nje,” amesema Kambona.

Amesema wafanyabiashara watakaobainika kufanya vitendo hivyo wanaweza kuchukuliwa hatua, ikiwamo kufutiwa usajili au leseni zao.

Kwa mujibu wa Kambona, hatua hizo zinalenga kulinda uaminifu wa biashara ya mkonge kutoka Tanzania na kuhakikisha wafanyabiashara wanaofanya biashara kwa kufuata taratibu hawaathiriwi na vitendo vya watu wachache.


UZALISHAJI MKONGE WAPANDA

Pamoja na changamoto hiyo, Kambona amesema uzalishaji wa mkonge nchini umeendelea kuongezeka, kutoka tani 36,000 mwaka 2020 hadi kufikia tani 75,000 mwaka 2025.

Amesema mwaka 2020 wakulima wakubwa walichangia asilimia 68 ya uzalishaji wa mkonge, huku wakulima wadogo wakichangia asilimia 32.

Hata hivyo, amesema hali hiyo imebadilika kutokana na juhudi za kuwawezesha wakulima wadogo, ambapo mwaka 2025 walichangia asilimia 55 ya uzalishaji, huku wakulima wakubwa wakichangia asilimia 45.


WAFANYABIASHARA: TUNABEBESHWA DHAMBI ZA WACHACHE

Wafanyabiashara wa mkonge walioshiriki kikao hicho wamesema vitendo vya wachache vimekuwa na madhara kwa wafanyabiashara waaminifu kutoka Tanzania, ambao wakati mwingine hujikuta wakihusishwa na tuhuma au kesi zinazotokana na biashara zisizofanyika kwa uaminifu.

Gasper Daudi wa Harvest Agritech Limited amesema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakisababisha matatizo katika masoko ya nje, hali inayowaathiri hata wale wanaofanya biashara kwa kufuata sheria.



Amesema ni muhimu Serikali na TSB kuweka mifumo madhubuti ya kuhakikisha wafanyabiashara wanaokiuka taratibu wanachukuliwa hatua mapema.



Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Aja Tanzania Limited, Happiness Nyiti, ameomba Wizara ya Viwanda na Biashara kuweka mpango maalumu wa kurejesha uaminifu katika masoko ambayo tayari yameathiriwa na vitendo vya baadhi ya wafanyabiashara.


“Vitendo hivi vinachafua taswira ya nchi yetu. Tunaomba Naibu Waziri atusaidie kuweka mpango mzuri wa kutengeneza taswira ya nchi yetu kwenye maeneo ambayo yanaonekana waziwazi kwamba imani ya wafanyabiashara wa zao hilo kutoka Tanzania imeshuka,” amesema Nyiti.



Amesema hatua hiyo ni muhimu kwa kuwa Tanzania ina wafanyabiashara wengi wanaozingatia ubora na uaminifu, lakini juhudi zao zinaweza kuathiriwa na vitendo vya wachache.

Amesema kurejesha uaminifu katika masoko ya kimataifa kutasaidia kuongeza fursa za biashara na kuchochea zaidi uzalishaji wa mkonge nchini.

TBS YATAHADHARISHA MATUMIZI YA VIPODOZI VYENYE VIAMBATA SUMU

September 14, 2026 Add Comment
Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeonya wananchi kuhusu matumizi ya vipodozi visivyo salama, likisema bidhaa hizo zinaweza kusababisha madhara makubwa kiafya, ikiwemo magonjwa sugu kama saratani.

ENG.JOYCE BARAVUGA- SHULE ZIHAKIKISHE MAFUNZO YA TEHAMA YANAENDELEA

September 14, 2026 Add Comment

Mratibu wa Mafunzo ya Kidijitali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Eng. Joyce Baravuga, amesema mafanikio ya Mradi wa Kuziba Pengo la Kidijitali: Kuhakikisha Elimu ya Ujuzi wa Kidijitali Inayozingatia Usawa wa Kijinsia kwa Wanawake na Wasichana (Closing the Digital Divide: Ensuring Gender-Transformative Digital Skills Education for Women and Girls) yatategemea kwa kiasi kikubwa utayari wa shule kuendeleza mafunzo na shughuli za Klabu za TEHAMA (ICT Clubs) baada ya kumalizika kwa Kambi ya Mafunzo (Boot Camp).

Eng. Baravuga amewapongeza wakuu wa shule zilizochaguliwa kushiriki katika programu hiyo, akisema utayari na uthubutu wa shule ni miongoni mwa vigezo vilivyozingatiwa katika uteuzi.

Amesema shule hizo zinapaswa kuwa wadau muhimu wa programu hiyo kwa kuhakikisha maarifa na ujuzi unaopatikana kupitia mafunzo unaendelea kutumika shuleni na kuwafikia wanafunzi wengine.

Amewataka walimu na wakuu wa shule kuhakikisha Klabu za TEHAMA zinaendelea baada ya wanafunzi kurejea shuleni, ili kuwapa wasichana nafasi ya kuendelea kujifunza, kufanya mazoezi na kuendeleza ubunifu wao katika teknolojia.

Aidha, amewataka walimu, hususan wanaohusika na TEHAMA, kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo na kuhakikisha maarifa yanayopatikana hayabaki kwa wanafunzi walioshiriki pekee, bali yanawafikia wanafunzi wengine shuleni.

Eng. Baravuga pia amesisitiza umuhimu wa kukusanya taarifa za utekelezaji wa shughuli za mafunzo kila siku, akisema taarifa hizo zitasaidia kupima mafanikio ya programu, kubaini changamoto na mapungufu, pamoja na kuweka msingi wa kuboresha utekelezaji katika hatua zijazo.

Amesema ukusanyaji wa taarifa kwa wakati utasaidia pia kutambua maeneo yanayohitaji kupewa msukumo zaidi na kuhakikisha malengo ya programu yanafikiwa.

Vilevile, amesisitiza umuhimu wa wanafunzi kuchaguliwa kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa bila upendeleo, ili kuhakikisha fursa zinazotolewa kupitia programu hiyo zinawafikia walengwa kwa usawa.

Eng. Baravuga amesema ushiriki wa shule, walimu na viongozi wa shule ni muhimu katika kuhakikisha Kambi ya Mafunzo haibaki kuwa tukio la muda mfupi, bali inakuwa mwanzo wa kujenga mazingira endelevu ya kujifunza, kutumia na kubuni kupitia TEHAMA miongoni mwa wanafunzi.

DR.FAITH SHAYO : LER US BUILD GIRLS INTEREST IN ICT

September 14, 2026 Add Comment

MOROGORO. Dr. Faith Shayo has called for greater efforts to build girls’ interest, confidence and enthusiasm in Information and Communication Technology (ICT), saying that creating interest is an important first step towards encouraging more girls to participate in technology.

Speaking during preparations for the ICT Boot Camp in Morogoro, Dr. Shayo said the programme is not primarily about providing girls with digital devices, but about helping them develop an interest in technology and understand its potential to improve their lives and communities.

She said access to devices remains important, but the immediate priority is to give girls the opportunity to learn, explore technology and develop the confidence to use it creatively.

“We want to build girls’ interest and enthusiasm in ICT. We want them to see that they can use technology to develop solutions to challenges in their communities,” she said.

Dr. Shayo said a key outcome of the programme is the establishment and strengthening of ICT Clubs in participating schools, providing girls with a space where they can continue learning, practising their skills and developing innovative ideas beyond the Boot Camp.


The programme is expected to reach 500 girls, with activities continuing after the Boot Camp. The girls will return to their schools and continue participating in ICT Club activities under the guidance of teachers and school leaders.

She said experts will continue visiting the schools to follow up on the progress of the clubs, while Project Coordinator Mr. Ginarious Ernest will also visit selected schools as part of the follow-up process.

Dr. Shayo said the practical nature of the Boot Camp is intended to help girls move beyond simply learning about technology and begin exploring how ICT can be used to address real challenges in their communities.

The Boot Camp is scheduled to officially begin tomorrow at Kilakala Secondary School in Morogoro, bringing together girls from 10 schools as part of the UNESCO-BNU project, “Closing the Digital Divide: Ensuring Gender-Transformative Digital Skills Education for Women and Girls.”