HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

PROF. KABUDI AWATAKA WANANCHI KUZINGATIA TAHADHARI ZA MAAFA

August 20, 2026 Add Comment


Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu–Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amewataka wananchi kuzingatia tahadhari na maelekezo yanayotolewa na wataalamu na mamlaka husika ili kupunguza madhara yanayotokana na majanga na maafa.

Prof. Kabudi ametoa wito huo tarehe 19 Agosti, 2026 wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Watoa Huduma za Misaada ya Kibinadamu Duniani yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

“Ushiriki wa wananchi ni muhimu katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya majanga, huku akiwataka kuendelea kufuata taarifa na maelekezo rasmi kutoka kwa wataalamu na mamlaka zinazohusika na masuala ya maafa.”

Katika hatua nyingine, alisema Serikali itaendelea kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na kujenga ustahimilivu wa jamii ili kuongeza uwezo wa wananchi kukabiliana na majanga na kupunguza madhara yanayotokana na matukio hayo.

Alisema uwezo wa nchi katika kukabiliana na majanga kwa ufanisi unategemea uwepo wa mifumo madhubuti, uratibu na ushirikiano wa karibu na wenye tija kati ya Serikali na wadau wa huduma za kibinadamu.

Prof. Kabudi pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake katika kusimamia masuala ya kibinadamu na ustawi wa wananchi.

“Kupitia uongozi wa Rais Dkt. Samia, Serikali imeendelea kuhakikisha wananchi wanaokumbwa na changamoto za majanga wanapata msaada na faraja wakati wa dharura.”

Prof. Kabudi aliwataka watoa huduma za kibinadamu kuwekeza zaidi katika kuwawezesha wananchi kwa elimu na taarifa sahihi kuhusu vihatarishi vinavyowazunguka, pamoja na hatua za kuchukua kabla, wakati na baada ya janga.

Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo, Dkt. James Kilabuko, amesema maadhimisho ya siku hiyo yanatoa fursa ya kutambua na kuthamini mchango wa watoa huduma za kibinadamu ambao hujitolea kwa moyo wa huruma, ujasiri na mshikamano katika kuokoa maisha na kupunguza madhara.

Alisema ni muhimu kuendelea kuimarisha ushirikiano na mshikamano miongoni mwa Serikali, wadau wa huduma za kibinadamu na jamii katika kuhakikisha kuwa msaada unapatikana kwa wakati na unawafikia wale wanaouhitaji.

“Ni muhimu kuhakikisha kuwa katika kila hatua ya utoaji wa huduma za kibinadamu, maisha, usalama na utu wa mwanadamu vinaendelea kuwa kiini cha hatua tunazochukua.”

=MWISHO=




 

WENYE ULEMAVU WAPEWA KONGOLE KUCHANGIA UKUAJI WA UCHUMI

August 20, 2026 Add Comment

 



Na Mwandishi wetu -IRINGA


Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge,  Uratibu na Wenye Ulemavu Mhe.  Nderiananga amewapongeza watu wenye ulemavu kwa kushiriki shughuli za kiuchumi na kuongeza pato lao na Taifa kwa ujumla.


Akizungumza wakati wa ziara ya kutembelea na kukagua shughuli 

zinazofanywa na watu wenye ulemavu  katika

Kituo cha wenye ulemavu cha Neema Craft kilichopo Manispaa ya Iringa Mh. Ummy alisema kuwa Serikali inaendelea kuweka mazingira yatakayowawezesha watu wenye ulemavu

kupata elimu, mafunzo ya ufundi na mitaji ili waweze kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji.



Pia aliongeza kuwa watu wenye ulemavu wanapopata elimu ya fani mbalimbali huwajengea hali ya kujiamini, kuwa tayari kuonyesha uwezo wao na kuwa wabunifu hatimaye kupunguza wimbi la utegemezi.


" Nikipongeze Kituo hiki cha Neema Craft kwa hatua kubwa waliopiga katika kuwawezesha wenye ulemavu kwenye ujuzi mbalimbali kama tulivyoona kuna ufundi seremala, ufumaji, ushonaji, upishi na fani nyingine nyingi ambapo zote hizi zinafanywa na watu wenye ulemavu kwetu kama Serikali ni furaha kubwa," Alipongeza Mhe. Ummy



Hata  hivyo amewataka watu wenye ulemavu kutumia fursa za

mikopo, mafunzo na uwezeshaji zinazotolewa na Serikali ili

kuanzisha na kuendeleza shughuli za kiuchumi

zitakazowasaidia kujitegemea.



"Wananchi wanaponufaika na mikopo hii ni heshima kubwa kwa Mbunge pia Mkuu wa Mkoa kaka yangu Kheri James nawapongeza sana kwa namna mnavyopambana kwa ajili ya watu wenye ulemavu," alisema.


Vile vile Mhe. Ummy alifafanua kwamba baadhi ya watu wenye ulemavu wameonyesha uwezo mkubwa katika uzalishaji wa bidhaa

mbalimbali, zikiwemo samani, mikoba, mikeka na mazulia, huku bidhaa hizo zikiuzwa katika hoteli na

masoko mbalimbali.

Alisema mafanikio hayo yanaonesha kuwa watu wenye ulemavu wana uwezo wa kufanya shughuli zenye tija endapo

watapata uwezeshaji unaostahili.


"Nimetembelea hapa Neema Craft nimejionea namna watu wenye ulemavu wanavyofanya shughuli zao za ujasirimali

wanabuni na kutengeneza bidhaa nzuri ambazo hata watu wazima hawawezi na bidhaa hizo mara nyingi tunaziona katika mahoteli makubwa ambayo huwezi kuzania kwamba watu wenye ulemavu ndio wametengeneza,"Alieleza.

Aidha aliwataka wazazi na walezi kutowaficha ndani watoto wenye ulemavu badala yake kuwapeleka shule au vyuo vya ufundi na vituo vinavyotoa mafunzo ya ujuzi hatua itakayosaidia kujikwamua kiuchumi hatimaye kutoka katika hali ya kuwa omba omba mitaani.



Kwa upande wake Mkurugenzi  wa Kituo cha Neema Crafts mkoani Iringa Bwa. Joseph Adams alisema kituo hicho kilianzishwa mwaka 2003 ikiwa ni  mradi wa kijamii unaolenga kutoa mafunzo na ajira kwa watu wenye ulemavu kama vile wasiyosikia ( viziwi)  na wenye ulemavu wa viungo 

ili kuwapa heshima na kuwaepusha na kuomba barabarani. 



"Kituo hiki kinajumuisha kazi nyingi sana na zote wanafanya wao wenyewe na kuzalisha bidhaa ambazo tunaziuza kama vile Karakana za kazi za mikono, Mgahawa  unaoendeshwa na viziwi na  Nyumba ya wageni (Guesthouse),"Alisema  Mkurugenzi huyo.


Aidha aliipongeza Serikali kwa kuendelea kuonyesha upendo kwa wenye ulemavu bila ubaguzi huku akiiomba kuboresha sekta ya wakalimani kuwasaidia wenye ulemavu kupata huduma muhimu kama hospitali, taasisi za fedha, nyumba za ibada na nyinginezo.


MWISHO

NEMC YAKUTANA NA WAANDAAJI WA TANZANIA GREEN SUMMIT 2026

August 20, 2026 Add Comment
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limekutana na ujumbe wa waandaaji wa Tanzania Green Summit (TGS), inayotarajiwa kufanyika Septemba 15–16, 2026 Ukumbi wa Mlimani City, Jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kujadili mikakati ya kuhakikisha unaleta tija katika ajenda ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi.

COSTECH YAJIVUNIA MIAKA 40 YA KUZALISHA WATAALAMU

August 20, 2026 Add Comment

 








Na Oscar Assenga Tanga

TUME ya Sayansi na Teknolojia Tanzania (COSTECH), imeadhimisha miaka 40 tangu kuanzishwa kwake, ikijivunia mchango wake katika kukuza sayansi, teknolojia na ubunifu nchini, ikiwamo kuzalisha wataalamu wanaochangia maendeleo ya Taifa.

Akizungumza jana wakati wa Maonyesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayofanyika katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, mkoani Tanga, Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, alisema taasisi hiyo imepata mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka 40.

Alisema miongoni mwa mafanikio hayo ni kuwawezesha wataalamu na wabunifu mbalimbali ambao kwa sasa wanatumia ujuzi na maarifa yao kutengeneza suluhisho za changamoto zinazolikabili Taifa.

“COSTECH tunajivunia mafanikio mengi sana, lakini kubwa zaidi ni kuzalisha wataalamu mbalimbali wanaolisaidia Taifa letu,” alisema Dkt. Nungu.

Alimtaja mmoja wa wataalamu hao kuwa ni Dkt. Cecilia China, msomi kutoka Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela, ambaye kwa sasa anamiliki kampuni na anatarajia kuanzisha kiwanda cha dawa za kusindika ngozi kwa kutumia malighafi inayotokana na maganda ya korosho.

Dkt. Nungu alisema hatua hiyo ni mfano wa namna sayansi, teknolojia na ubunifu vinavyoweza kutumika kuongeza thamani ya mazao ya kilimo na kuibua fursa za kiuchumi kwa Watanzania.

Aidha, aliwataka wakazi wa Mkoa wa Tanga, hususan Jiji la Tanga, kujitokeza kwa wingi kutembelea maonyesho hayo ili kujifunza na kuona teknolojia mbalimbali zilizobuniwa na wataalamu na wabunifu wa Kitanzania.


“Niwaombe wakazi wa Mkoa wa Tanga, hususan wakazi wa Jiji la Tanga, mje kwa wingi kutembelea maonyesho haya ili muone teknolojia mbalimbali zilizobuniwa na wataalamu kutoka hapa nchini kwetu. Tupo hapa hadi Agosti 24, karibuni sana,” alisema.

Maonyesho hayo yanaendelea katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, Tanga, yakihusisha taasisi na wadau mbalimbali wa elimu, ujuzi, sayansi, teknolojia na ubunifu.

WAANDISHI CROWN MEDIA WATAKIWA KUZINGATIA WELEDI NA UADILIFU

Kajunason August 20, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imewataka Waandishi wa Habari wa Crown Media kulinda imani ya umma kwa kuzingatia weledi, maadili, uadilifu na uwajibikaji katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wito huo umetolewa wakati wa mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa na JAB kwa Waandishi wa Habari wa Crown Media, kuanzia Agosti 18 hadi 19, 2026, jijini Dar es Salaam yakilenga kuwaongezea maarifa na kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia sheria, maadili na viwango vya taaluma ya uandishi wa habari.

Akiwasilisha Mada kuhusu Msingi na Mfumo wa Kisheria unaosimamia Sekta ya Habari nchini Tanzania katika mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amewasihi Waandishi wa Habari kuthamini na kulinda taaluma yao kwa kuzingatia misingi inayowaongoza katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Waandishi wa Habari tunapaswa kuthamini na kulinda taaluma yetu wenyewe. Weledi, maadili na uadilifu ndiyo msingi wa kuaminika kwa mwandishi na sekta ya habari kwa ujumla,” amesema Wakili Kipangula. 

Kwa upande wake, Dkt. Egbert Mkoko amewataka Waandishi wa Habari kuzingatia maadili katika kila hatua ya kazi zao, akieleza kuwa maadili ndiyo msingi wa uandishi wa habari unaowajibika na wenye tija kwa jamii.

“Mwandishi wa Habari anapaswa kuzingatia maadili ya kazi katika kila hatua ya utekelezaji wa majukumu yake, kwa kuwa uadilifu na uwajibikaji ndiyo msingi wa taaluma hii,” amesema Dkt. Mkoko alipokuwa akifafanua mada Kuhusu Maadili ya Utangazaji na makosa ya kimaadili yanayofanywa mara kwa mara.

Naye Mjumbe wa JAB na Kaimu Meneja wa Huduma za Kiswahili wa Shirika la Magazeti ya Serikali (TSN), Bw. Mgaya Kingoba, akiwasilisha mada kuhusu uzalendo, amewataka Waandishi wa Habari kutumia taarifa kwa usahihi na kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maslahi ya umma.


 Wakizungumza wakati wa tathmini ya mafunzo hayo, baadhi ya Waandishi wa Habari wa Crown Media wamesema wamepata uelewa mpana kuhusu Sheria ya Huduma za Habari, hali iliyowasaidia kuondokana na fikra potofu zilizotokana na tafsiri zisizo sahihi zinazotolewa katika jamii kuhusu Sheria hiyo. Pia wameomba mafunzo kama hayo kutolewa mara kwa mara ili kuwajengea uwezo Waandishi wa Habari.

“Kwa kweli, changamoto tuliyonayo katika vyombo vyetu vya habari ni kushindwa kutofautisha maoni binafsi na uchambuzi wa kitaaluma, pamoja na kushindwa kutenganisha nafasi ya mtu binafsi na wajibu wake kama mwanataaluma. Pia kumekuwa na dhana kwamba Bodi ipo kwa ajili ya kuwadhibiti Waandishi wa Habari, pamoja na uelewa mdogo kuhusu ithibati, umuhimu wake na nafasi yake katika kulinda heshima ya taaluma,” amesema Imani Luvanga mmoja wa washiriki.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu ya JAB kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229, yanayolenga kuimarisha weledi, uadilifu, uwajibikaji na tija katika taaluma ya uandishi wa habari.

THPS YATAMBULISHA MRADI WA TANZANIA FAST HEALTH MANISPAA YA KAHAMA KUIMARISHA HUDUMA ZA VVU

August 19, 2026 Add Comment

 Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Honoratha Rutatinisibwa, akizungumza wakati wa utambulisho wa Mradi wa Tanzania FAST Health unaotekelezwa na THPS katika Manispaa ya Kahama, Mkoa wa Shinyanga, Agosti 19, 2026.Picha na Kadama Malunde

DC HAI AENDELEA KUSIKILIZA KERO ZA WANANCHI, ATATUA MIGOGORO YA ARDHI

August 19, 2026 Add Comment


Na Ashrack Miraji Kilimanjaro 

Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Mhe. Hassan Bomboko, ameendelea na ziara zake katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo kwa lengo la kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi, ikiwemo migogoro ya ardhi inayowakabili baadhi ya wananchi.

Katika ziara hizo, Mhe. Bomboko amekuwa akikutana na wananchi, viongozi wa Serikali za mitaa pamoja na wadau mbalimbali ili kupata taarifa za changamoto zinazowakabili na kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi kwa mujibu wa sheria, taratibu na haki.

Miongoni mwa changamoto zinazojitokeza katika maeneo hayo ni migogoro inayohusu matumizi na umiliki wa ardhi, ambapo Mkuu huyo wa Wilaya amesisitiza umuhimu wa wahusika kufuata taratibu za kisheria katika kutatua tofauti zao badala ya kuchukua hatua zinazoweza kuongeza migogoro katika jamii.

Mhe. Bomboko amesema Serikali itaendelea kusikiliza wananchi na kushughulikia kero zao kwa wakati, akisisitiza kuwa viongozi wana wajibu wa kuwa karibu na wananchi ili kutambua changamoto zinazowakabili na kuzitatua kwa ushirikiano.

Aidha, amewataka wananchi kutumia fursa za mikutano na ziara za viongozi kutoa changamoto zao kwa uwazi, huku akisisitiza umuhimu wa wananchi kushirikiana na Serikali katika kulinda amani, utulivu na mshikamano katika jamii.

Ziara hizo zinaendelea kuwa sehemu ya jitihada za Serikali Wilaya ya Hai za kuimarisha huduma kwa wananchi, kusikiliza kero zao na kutatua migogoro mbalimbali kwa njia ya mazungumzo na kwa kuzingatia sheria, ili kuhakikisha wananchi wanaishi kwa amani na kutumia rasilimali zao kwa maendeleo.






 

SHILINGI BILIONI 83.9 KINADAIWA KWA WATEJA MBALIMBALI WA HUDUMA YA MAJI NCHINI

SHILINGI BILIONI 83.9 KINADAIWA KWA WATEJA MBALIMBALI WA HUDUMA YA MAJI NCHINI

August 19, 2026 Add Comment




Kiasi hicho kimewasilishwa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira katika kikao chake, Bungeni jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Jackson Kiswaga (Mb) akiongoza kamati hiyo pamoja na taratibu zitakazochukuliwa, kamati imeshauri na kuelekeza madai kufanyiwa kazi ili Serikali iendelee kuimarisha huduma ya maji kwa wananchi.

Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) amesema moja ya hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kuanza kutumika kwa matumizi ya Dira janja za malipo kabla ambapo deni hukusanywa kila malipo ya huduma ya maji yanapofanyika na kufanya mazungumzo na wadaiwa ili kuona namna bora ya kupunguza madai hayo.

Waziri Aweso ameainisha kuwa ili huduma ya maji imfikie mteja, nyuma yake zipo gharama kadhaa za uendeshaji ikiwemo nishati ya umeme, dawa za kutibu maji, rasilimaliwatu, na matengenezo.

Amesema mteja anapowajibika kulipa bili ni moja ya mchango wake katika kuimarisha na kuendeleza huduma ya maji nchini.  


WASIRA ATAKA WANA CCM WAKUTANE, WASIINGIE MKENGE KWA MANENO YA MITANDAONI.

August 19, 2026 Add Comment

Mwenyekiti wa Chama cha CCM Bara Ndugu Stephen Wasira, Akizungumza na wanachama wa CCM Wilaya ya Ikungi mkoani Singida wakati wa kuanza ziara rasmi ya kikazi ya kukagua uhai wa chama Mkoani humo

_Na Mwandishi Wetu - Singida_

Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Ndugu Stephen Wasira, amewataka wanachama wa CCM kukutana mara kwa mara katika vikao rasmi vya chama ili kujadili masuala muhimu na kuepuka kupotoswa na taarifa zisizo na ukweli zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii.

Akizungumza leo tarehe 19 Agosti, 2026 Wilaya ya Ikungi mkoani Singida wakati wa kuanza ziara rasmi ya kikazi ya kukagua uhai wa chama, Wasira amesema vikao hivyo vinawapa wanachama fursa ya kupata taarifa sahihi na kuambizana ukweli.

"Wanachama wetu nchi nzima, kwa mujibu wa Katiba mna vikao vya wanachama. Mkutane muambizane. Siku hizi kwenye mitandao kuna uongo mwingi sana. Usipoangalia unaweza hata wewe kushirikishwa kusema uongo," amesema.

Amesisitiza kuwa ni muhimu wanachama kukutana na kujadili madai yanayosambaa, kisha kumtafuta mtu mwenye ujuzi awasaidie kuyafafanua.

"Kwa hiyo ni vizuri kukutana mkasema hili jambo limesemwa sana, maana yake ni nini? Mkamwita mtu anayejua akawasaidia kufafanua," ameeleza.

Makamu Mwenyekiti huyo amebainisha kuwa mikutano ya wanachama ni fursa muhimu ya kujadili masuala yanayoendelea nchini ili waweze kukitetea chama ipasavyo.

Kuhusu uhuru na umoja wa nchi, Wasira amesema CCM itaendelea kulinda urithi huo uliopatikana kwa kazi kubwa.

"Hii ndiyo CCM. Kazi ya kwanza tulipewa ni uhuru na tunalinda. Ya pili ni umoja na tunahakikisha unabaki. Yeyote anayetaka kuubomoa anabomoa msingi ambao hawezi. Anaweza kutikisa matawi lakini mizizi itabaki chini," amesema.


Ameongeza kuwa wapo wanaodai CCM haijatekeleza chochote tangu uhuru, jambo ambalo amelisema ni kinyume na ukweli.

"Wanasema hatujafanya chochote tangu uhuru. Lakini uhuru wa kusema ndio huo walionao. Mdomo una kazi mbili: kusema na kula. Mtu akisema hakuna chochote tangu uhuru, muache tu. Huyo ana matatizo anahitaji msaada," amehitimisha.

---




SHIRIKA LA GIFTED NATURE (GIFTED NATURE NGO) NA MRADI WA ‘SHUJAA PATH’

August 19, 2026 Add Comment

 

Gifted Nature NGO ni shirika lisilo la kiserikali la Tanzania lililoanzishwa mwaka 2021 na Dr. Sophia Mfaume Kizigo, linalojikita katika kuiwezesha jamii, kulinda mazingira pamoja na kutengeneza fursa kwa vijana ili waweze kuwa na maisha yenye tija na endelevu. Kupitia programu zinazolenga jamii, shirika linashughulikia changamoto za kijamii na kimazingira huku likihamasisha elimu, uongozi, ukuzaji wa ujuzi, uwajibikaji na ushiriki wa wananchi katika maendeleo.

Miongoni mwa mipango yake muhimu ni Mradi wa ‘Shujaa Path’ ulioanzishwa mwaka 2025, unaolenga hasa kuwawezesha wavulana na vijana wa kiume ambao mara nyingi hawapati uangalizi wa kutosha katika programu mbalimbali za maendeleo. Shujaa Path umeanzishwa kutokana na kutambua changamoto zinazowakabili wavulana, zikiwemo kuacha au kutoshiriki kikamilifu katika elimu, ukosefu wa malezi na ushauri wa kitaalamu, ukosefu wa ajira na fursa za kiuchumi, ushawishi hasi wa rika pamoja na ukosefu wa mazingira bora ya kukuza vipaji na uwezo wao.

Kupitia kaulimbiu “Every Boy, A Shujaa - Kila Kijana wa Kiume ni Shujaa,” Shujaa Path hailengi tu kutatua changamoto zinazowakabili wavulana, bali kuwasaidia kutambua thamani na uwezo wao, kujenga kujiamini, kuwa na maadili mema, kupata ujuzi wa maisha, ujasiriamali na ajira, pamoja na kuwa viongozi na raia wenye mchango chanya katika familia na jamii zao.

Gifted Nature NGO inaamini kuwa kumjenga kijana leo ni kuijenga jamii bora ya kesho. Kupitia ushirikiano na Serikali, shule, jamii, wadau wa maendeleo, sekta binafsi na vyombo vya habari, shirika linalenga kuendeleza na kupanua Shujaa Path ili kuwafikia wavulana na vijana wengi zaidi Tanzania.





TUZO YA MWALIMU NYERERE YAZIDI KUNG’ARA, SH MILIONI 800 KUCHAPISHA VITABU

August 19, 2026 Add Comment


Na Oscar Assenga,TANGA

TUZO ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu imeendelea ,kuonyesha mafanikio makubwa, ambapo tangu kuanzishwa kwake Watanzania 27 wamefanikiwa kushinda katika nyanja mbalimbali za uandishi bunifu.

Hayo yamesema leo na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Tanga kuelekea zoezi la ukusanyaji Miswada ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu 

Amesema mafanikio hayo yanaonyesha namna tuzo hiyo inavyoibua na kutambua vipaji vya waandishi bunifu nchini, huku idadi ya washiriki ikiongezeka kila mwaka kutoka ndani na nje ya Tanzania.

Prof. Mkenda amebainisha kuwa Serikali imewekeza takribani Shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuchapisha vitabu vilivyoshinda tuzo hizo na kuvisambaza katika shule za Tanzania Bara na Zanzibar, hatua inayolenga kuwafikia wasomaji wengi zaidi na kuhamasisha utamaduni wa kusoma.

Aidha, Waziri Mkenda amesema tuzo hizo zimeendelea kukua na kuvutia washiriki kutoka mataifa mbalimbali, jambo linaloonyesha kuongezeka kwa hadhi yake na umuhimu wa uandishi bunifu katika kukuza fasihi na lugha ya Kiswahili.

Ameongeza kuwa tuzo hizo zimekuwa jukwaa la kuwahamasisha vijana na waandishi kutumia vipaji vyao katika kutengeneza kazi zenye ubunifu na maudhui yanayoweza kuelimisha na kujenga jamii.

“Tuzo hii sasa imeingizwa rasmi katika orodha ya tuzo za uandishi bunifu duniani, ukiitafuta mtandaoni utaona tarehe 13 Aprili ni siku ya kutoa Tuzo ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu,” amesema Prof. Mkenda.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu, Prof. Penina Mlama, amesema dirisha la kuwasilisha miswada ya kazi za ubunifu limefunguliwa rasmi leo, Agosti 19, 2026, na litafungwa Novemba 30, mwaka huu.

Ameeleza kuwa waandishi bunifu wanatakiwa kutumia kipindi cha takribani miezi mitatu kuwasilisha miswada yao, huku matangazo yenye vigezo na taratibu za kushiriki yakitolewa kupitia mitandao ya kijamii ya tuzo hiyo pamoja na mitandao ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Taasisi ya Elimu Tanzania.

Prof. Mlama amesema mshiriki anatakiwa kuwa raia wa Tanzania, kazi iwe imeandikwa kwa Kiswahili na kila mwandishi anaruhusiwa kuwasilisha andiko moja tu katika nyanja atakayochagua. Aidha, mswada unaowasilishwa unatakiwa kuwa haujawahi kuchapishwa popote.

Amefafanua kuwa miswada iliyowahi kushika nafasi ya kwanza hadi ya 10 katika miaka iliyopita haitaruhusiwa kuwasilishwa tena, ingawa waandishi waliowahi kushika nafasi hizo wanaweza kushiriki kwa kuwasilisha miswada mipya. Pia, miswada iliyowahi kushinda tuzo nyingine haitazingatiwa katika ushindani wa mwaka huu.

Kwa upande wa vigezo mahususi, tamthilia ya jukwaani inapaswa kutumia vionjo vya sanaa za maonyesho za Tanzania, iwe na muda wa dakika 40–60, isiwe na maonyesho zaidi ya sita na wahusika wasiozidi sita. Ushairi unatakiwa kuwa na mashairi yasiyopungua 50 wala kuzidi 60, huku kila shairi likiwa na beti zisizozidi 15.

Kwa riwaya, urefu unatakiwa kuwa kati ya maneno 60,000 na 100,000, wakati hadithi za watoto zinatakiwa kuwa na kati ya maneno 250 na 500 kwa hadithi moja. Prof. Mlama amesisitiza kuwa kazi zinazowasilishwa zinapaswa kuwa na mawazo asilia ya mwandishi na kujikita katika masuala muhimu ya jamii.