HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts
WASTAAFU WAONYWA DHIDI YA MATAPELI KUPOTEZA MAFAO YAO
Na Marco Maduhu, SHINYANGA
WASTAAFU nchini wametakiwa kuwa makini na watu wanaojitambulisha kama mawakala wa Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSSSF), wakihimizwa kutumia njia rasmi za mfuko huo katika kuhakiki taarifa zao na kufuatilia mafao yao ili kuepuka kutapeliwa na kupoteza fedha zao.
Tahadhari hiyo imetolewa leo, Septemba 18, 2026, na Afisa Msimamizi wa PSSSF Mkoa wa Simiyu, Salum Mwegelo, wakati wa semina ya PSSSF kwa waandishi wa habari kutoka Klabu za Waandishi wa Habari za Shinyanga na Simiyu pamoja na Mtandao wa Wanablogu Tanzania (Tanzania Bloggers Network – TBN), iliyofanyika mjini Shinyanga.
Mwegelo amesema baadhi ya wastaafu wamekuwa katika hatari ya kutapeliwa kutokana na kutumia watu wasio rasmi wanaodai kuwa wanaweza kuwasaidia katika taratibu za kuhakiki taarifa, kufuatilia au kupata mafao yao.
![]() |
Amesema watu hao wanaweza kuomba taarifa nyeti za wastaafu, ikiwemo namba za siri za akaunti za fedha na taarifa nyingine binafsi, ambazo zinaweza kutumiwa kufanya miamala bila ridhaa ya wahusika.
“Mawakala hao huwarubuni wastaafu na kuomba namba za siri na taarifa muhimu, ikiwemo taarifa za akaunti zao, na kisha kuzitumia kufanya miamala bila ridhaa ya wahusika na kusababisha kupoteza mafao,” amesema Mwegelo.
Mwegelo amesisitiza kuwa PSSSF haina mawakala wanaotoa huduma kwa niaba ya mfuko huo, hivyo wastaafu wanapaswa kuwa na tahadhari dhidi ya mtu yeyote anayejitambulisha kama wakala wa PSSSF na kuwaomba taarifa zao za siri.
Amesema wastaafu wanapaswa kutumia njia rasmi zinazotolewa na PSSSF, ikiwemo kufika katika ofisi za mfuko huo au kutumia mifumo ya kidijitali inayowawezesha wanachama na wastaafu kufuatilia na kuhakiki taarifa zao kwa usalama.
Amesema matumizi ya mifumo ya kidijitali ni miongoni mwa njia zinazoweza kuwasaidia wanachama kupata taarifa zao kwa urahisi bila kulazimika kuwapa watu wengine taarifa zao binafsi au za kifedha.
Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa PSSSF, Abdul Njalo, amewataka waandishi wa habari na wanablogu kutumia taaluma yao kuwafikishia wananchi taarifa sahihi kuhusu huduma za mfuko huo, hususan elimu inayohusu haki, wajibu na taratibu za kupata mafao.
Njalo amesema vyombo vya habari, blogu na majukwaa ya kidijitali vina nafasi kubwa katika kuhakikisha elimu hiyo inawafikia wanachama na wastaafu kwa lugha rahisi na inayoeleweka, huku akiwataka waandishi na wanablogu kuthibitisha taarifa kabla ya kuzifikisha kwa umma.
Amesema elimu sahihi inaweza kusaidia kuwawezesha wanachama na wastaafu kutambua njia halali za kupata huduma za PSSSF na kuchukua tahadhari dhidi ya watu wanaoweza kutumia mwanya wa ukosefu wa taarifa kuwahadaa.
Naye Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga, Greyson Kakuru, amesema semina hiyo imekuwa na umuhimu mkubwa kwa waandishi wa habari na wanablogu kwa kuwa imewapa uelewa zaidi kuhusu huduma za PSSSF na masuala yanayowahusu wanachama na wastaafu.
Kakuru amesema maarifa yaliyopatikana yatawasaidia waandishi na wanablogu kuandaa na kusambaza habari zenye usahihi, huku wakitoa elimu kwa jamii kuhusu namna ya kutumia huduma za PSSSF na kujilinda dhidi ya utapeli.
Amesema ushirikiano kati ya PSSSF na vyombo vya habari pamoja na wanablogu ni muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi kwa wakati na kutumia huduma za hifadhi ya jamii kwa uelewa zaidi.
Naye Mratibu wa Tanzania Bloggers Network (TBN) Kanda ya Ziwa, Kadama Malunde, amepongeza PSSSF kwa kuandaa semina hiyo, akisema mafunzo kama hayo ni muhimu kwa waandishi wa habari na wanablogu kwa kuwa yanawaongezea uelewa wa masuala wanayopaswa kuyafikisha kwa jamii.
Malunde amesema waandishi na wanablogu wana wajibu mkubwa wa kuhakikisha kila taarifa wanayoitoa kwa umma inathibitishwa, ina usahihi na inatoka katika vyanzo vinavyoaminika, hususan katika kipindi hiki ambacho taarifa za kidijitali zinaweza kusambaa kwa kasi kubwa.
“Semina kama hii ni muhimu kwa sababu inatupa nafasi ya kujifunza na kuongeza uelewa. Tukiwa waandishi na wanablogu, jukumu letu si kuchapisha taarifa tu, bali kuhakikisha taarifa tunazowafikishia wananchi ni sahihi, zimehakikiwa na zina manufaa kwa jamii,” amesema Malunde.
SERIKALI YAAGIZA UKAGUZI MAENEO YA UWEKEZAJI NCHINI
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, amewaagiza Makamishna wa Ardhi Wasaidizi katika mikoa yote nchini kufanya ukaguzi wa maeneo ya uwekezaji yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli mbalimbali kwa lengo la kubaini maeneo yasiyoendelezwa na kutoa taarifa ili hatua stahiki zichukuliwe
Dkt. Akwilapo ametoa agizo hilo Septemba 18, 2026, mara baada ya kuhitimisha ziara yake katika maeneo ya uwekezaji ya Kongani ya Viwanda ya KAMAKA pamoja na kiwanda cha Nondo cha Gain Company Limited kilichopo Mlandizi, Wilaya ya Kibaha, Mkoa wa Pwani.
Amesema Wizara ya Ardhi, imebaini kuwepo kwa maeneo ambayo yalipewa wawekezaji kwa ahadi ya kuanzisha viwanda au shughuli nyingine za uzalishaji, lakini hayajaendelezwa kwa muda uliokubaliwa.
“Tuna taarifa kuna waliochukua maeneo wakasema watatengeneza viwanda lakini bado hawajafanya hivyo. Natoa maelekezo makamishna kufanya ukaguzi na kuwasilisha taarifa ili hatua stahiki zichukuliwe kwa maeneo yasiyoendelezwa kadri ya mikataba waliyoingia,” amesema Dkt. Akwilapo.
Aidha, Waziri huyo amewataka wamiliki wote wa ardhi ambao hawazingatii masharti ya uendelezaji maeneo waliyopewa kuhakikisha wanayaendeleza kwa wakati, vinginevyo wizara itachukua hatua kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo.
Amesisitiza kuwa, hatua hizo zitawahusu wawekezaji wazawa na wa kigeni, akieleza kuwa kwa wawekezaji wazawa hatua inaweza kujumuisha kubadilisha milki za ardhi walizopewa, huku kwa wawekezaji wa kigeni wizara ikishirikiana na taasisi husika, ikiwemo TISEZA, katika kushughulikia masuala ya umiliki na uwekezaji.
Dkt. Akwilapo amesema, hatua hiyo inalenga pia kujibu malalamiko kutoka kwa wananchi ambao maeneo yao yalichukuliwa kwa ajili ya uwekezaji, lakini baadaye hayakuendelezwa.
Ameeleza kuwa, hali hiyo imekuwa ikisababisha wananchi kuhoji sababu za maeneo kutolewa kwa wawekezaji ambao hawajaanza shughuli za maendeleo kwa muda mrefu.
Awali Mhe Dkt Akwilapo alielezwa kuwa eneo la Kongani ya Viwanda Mlandizi wilayani Kibaha mkoa wa Pwani linakabiliwa na changamoto kadhaa kama vile upatikanaji wa maji na ubovu wa barabara hali waliyoieleza kuwa inayosababisha kero katika usafirishaji bidhaa na malighafi.
Hata hivyo, Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) wameeleza kuanza kuchukua hatua za dharura kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa ufumbuzi wa muda mfupi na mrefu
Ziara ya Dkt. Akwilapo katika Mkoa wa Pwani imelenga kujionea kwa karibu shughuli za uwekezaji na matumizi ya ardhi katika maeneo hayo, pamoja na kutathmini namna bora ya kuendeleza maeneo ya uwekezaji kwa kuzingatia mipango ya matumizi ya ardhi na maendeleo endelevu.
Aidha, ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi za kutambua fursa na changamoto zinazohusiana na ardhi na uwekezaji, kwa lengo la kuimarisha matumizi bora ya ardhi, kuvutia uwekezaji na kuchochea maendeleo ya wananchi.
----------mwisho---------
Green Acres yajivunia umahiri wa taaluma
HABARIROSTAM AZIZI: UONGOZI IMARA, SERA BORA NA MIFUMO THABITI VITAAMUA MUSTAKABALI WA UWEKEZAJI AFRIKA MASHARIKI
HABARIMAKAMU WA RAIS AAGIZA MAWAZIRI WATATU KUTATUA MGOGORO WA MIPAKA PUGU NDANI YA SIKU SABA
Na: OWM–TAMISEMI, Dar es Salaam.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, amewaagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI), Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na Waziri wa Maliasili na Utalii kufika ndani ya siku saba katika Dampo la Pugu kwa ajili ya kutatua mgogoro wa muda mrefu wa wananchi kuhusu mipaka ya kiutawala na mpaka wa Msitu wa Kazimzumbwi.
Makamu wa Rais ametoa agizo hilo Septemba 18, 2026, jijini Dar es Salaam, wakati akizungumza na wananchi wa Pugu mara baada ya kufanya ziara katika Dampo la Pugu, linalohudumia Mkoa wa Dar es Salaam kwa kupokea taka, na kusikiliza kero zinazowakabili wananchi wa eneo hilo.
“Nikiwa Dampo kuna wazee wangu waliwasilisha malalamiko juu ya kubuguziwa katika Msitu wa Kazimzumbwi, wakidai hawajui kama wako eneo gani la utawala, Pwani au Dar es Salaam. Hivyo, ninawaelekeza Mawaziri wa TAMISEMI, Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na wa Maliasili na Utalii kuhakikisha ndani ya siku saba wawe wamefika hapa kutatua changamoto hiyo ya wananchi kubuguziwa,” amesema Mhe. Ndejembi.
Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka mawaziri hao watakapofika katika eneo hilo kuzungumza na wananchi na kuhakikisha katika kutatua changamoto hiyo wanatumia taarifa rasmi ya Serikali kuhusu mipaka ya kiutawala, yaani Government Notice (GN) iliyochapishwa katika Gazeti la Serikali, kama msingi wa kubaini mipaka husika.
Akizungumza kwa niaba ya mawaziri wenzake, Waziri wa Nchi, OWM–TAMISEMI, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameahidi kutekeleza maelekezo hayo ya Makamu wa Rais kwa kufika katika eneo hilo ndani ya siku saba na kuzungumza na wananchi kwa ajili ya kutafuta suluhisho la mgogoro huo.
“Mhe. Makamu wa Rais, tumepokea maelekezo yako ya kutatua mgogoro huu wa wananchi wa mipaka ya kiutawala na Msitu wa Kazimzumbwi ndani ya siku saba. Hivyo, mimi Prof. Riziki Shemdoe, Waziri wa TAMISEMI, Dkt. Akwilapo, Waziri wa Ardhi, na Dkt. Ashatu Kijaji, Waziri wa Maliasili, tutakuja kuzungumza na wananchi ili kutatua mgogoro huo,” amesema Prof. Shemdoe.
Aidha, Prof. Shemdoe ameahidi kutekeleza maelekezo ya Makamu wa Rais ya kuzisimamia Halmashauri zote za Mkoa wa Dar es Salaam kuleta vitendea kazi, ikiwemo tingatinga (bulldozer), kwa ajili ya kuboresha mazingira na kuongeza ufanisi wa huduma ya upokeaji wa taka katika Dampo la Pugu.
Prof. Shemdoe amesema tayari amemwelekeza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kuanza kufuatilia utekelezaji wa agizo hilo ili kuhakikisha vitendea kazi vinapatikana na hatua zinazohitajika zinachukuliwa.
Prof. Shemdoe ametumia fursa hiyo kumshukuru na kumpongeza Makamu wa Rais, Mhe. Deogratius Ndejembi, kwa kufanya ziara katika Dampo la Pugu, kusikiliza kero za wananchi na kutoa maelekezo ya hatua za haraka kuchukuliwa kwa ajili ya kuongeza ufanisi wa utendaji kazi wa dampo hilo linalohudumia Mkoa wa Dar es Salaam.
TANZANIA KUWA MWENYEJI WA KONGAMANO LA MITAALA AFRIKA
HABARITPi YASHIRIKIANA NA JAMII KUIMARISHA USAFI WA MAZINGIRA
HABARIJAB YAWANOA WAANDISHI WA WASAFI MEDIA MEDIA KUHUSU SHERIA NA MAADILI

ORYX GAS YAKABIDHI MITUNGI YA GESI 600 KWA WANANCHI NAMTUMBO
HABARISTAMICO YAWAANDAA WATUMISHI KUKABILIANA NA MVUA ZA EL NIÑO
HABARITMDA YAZIWEKEA MKAKATI DAWA TIBA ZISITUMIKE KINYUME CHA MIONGOZO
HABARINEMC YATAKIWA KUONGEZA UFANISI KATIKA UKAGUZI WA MAZINGIRA
habTanzania, UNESCO Bolster Collaboration in Education, Science, Culture and Information
HABARIPhoto: Tanzania National Commission for UNESCO
JEZI ZA TAIFA STARS: MAKONDA AIBUKA MKATABA, MAPATO NA UBORA
HABARINa Mwandishi Wetu, Dodoma.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda, ametangaza kutoutambua mchakato wa kubadilisha jezi za timu za taifa, akisema umefanyika bila kuishirikisha Wizara licha ya maelekezo aliyoyatoa Februari 2026.
Sambamba na hatua hiyo, Waziri Makonda ameagiza kuundwa kwa kamati maalumu itakayochunguza mikataba ya wazabuni wa jezi hizo, manufaa yake kwa timu za taifa pamoja na mapato yanayotokana na mauzo yake.
Uamuzi huo umetangazwa siku mbili baada ya Waziri Makonda kukataa hadharani jezi mpya zilizoonekana zikivaliwa na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, akisema hazikuwa na ubora unaoendana na hadhi ya Taifa Stars.
“Hii siyo jezi ya Taifa Stars. Taifa Stars kwa ubora wake hatuwezi kuwa na jezi za kiwango cha chini hivi. Acheni kutumia picha za Naibu wangu huku ofisi yangu haina taarifa. Tuheshimiane,” alisema Waziri Makonda kupitia mitandao ya kijamii.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara leo, Septemba 18, 2026, uchunguzi huo unalenga kubaini iwapo mikataba iliyopo inanufaisha timu za taifa kwa kiwango kinacholingana na fedha nyingi zinazotolewa na Serikali kugharamia timu hizo.
Wizara imeeleza kuwa Februari 2026, Waziri Makonda alitoa maelekezo ya kuboresha jezi za timu za taifa ili ziakisi utambulisho wa Tanzania na kuzalisha manufaa mapana kwa nchi.
Hatua hiyo imeelezwa kuwa muhimu kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika maandalizi ya timu za taifa zinazoshiriki mashindano ya kimataifa, pamoja na Tanzania kuwa mwenyeji mwenza wa Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027).
Kamati hiyo pia itachunguza mapato yanayotokana na mauzo ya jezi na mchango wake katika kugharamia uendeshaji wa timu za taifa.
TBS, HALMASHAURI KUIMARISHA USHIRIKIANO KULINDA AFYA ZA WANANCHI
HABARITANESCO IMEJIPANGA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NINO -MD TWANGE
NishatiNa Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limesema limejipanga kukabiliana na athari za mvua za El Niño kwa kuimarisha miundombinu, kuandaa timu za dharura na kuchukua tahadhari katika mabwawa ya kuzalisha umeme.
Akizungumza katika kipindi cha Aridhio cha TBC, Septemba 17, 2026, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema shirika limefanya tathmini ya miundombinu yake na kubaini maeneo hatarishi.
“Tumefanya kikao na Mamlaka ya Hali ya Hewa na tathmini ya miundombinu yetu, hivyo maeneo hatarishi tunayafahamu na tumeanza kuchukua hatua,” amesema Bw. Twange
Amesema maandalizi hayo yameanza pia katika maeneo mbalimbali, ikiwemo Dar es Salaam, kwa kuimarisha nguzo za umeme zilizoonekana kuwa katika hali ya kuchoka.
“Kama Dar es Salaam tumeanza, kwa ajili ya kurekebisha nguzo za miti ambazo zina dalili ya kuchoka ili tuweze kuweka nguzo nyingine,” ameongeza Bw. Twange.
Aidha, amesema TANESCO imeandaa timu za dharura zitakazoshughulikia changamoto za wateja endapo zitatokea wakati wa mvua hizo.
“Tumeziandaa timu zetu za dharura kwa maana ya _“emergency”_ team zetu kwa maana ya kushughulika wateja wetu watakapokuwa wanatupigia simu,” amethibitisha.
Kwa upande wa mabwawa ya kuzalisha umeme wa maji, amesema TANESCO inafuatilia hali ya maji katika mabwawa yake, huku ikitambua uwezekano wa El Niño kusababisha ongezeko kubwa la maji.
“Sisi tuna eneo jingine la vituo vyetu vya kuzalisha umeme wa maji. Mabwawa kama Mwalimu Nyerere, Mtera, Kidatu, Kihansi. Maji kwetu ni huduma muhimu na tunayafurahia kwa ajili ya kuwa na kiwango cha kutosha cha maji kinachotuwezesha kuzalisha umeme,” amesema.
Hata hivyo, amesema maji mengi kupita kawaida yanaweza pia kuwa na madhara kwa wananchi wanaoishi karibu na mabwawa hayo, hivyo TANESCO imeanza kutoa elimu na kuchukua tahadhari.
“Lakini kutokana na El Niño huenda tukapata maji mengi kuliko ilivyo kawaida. Na maji yale yanaweza kuleta madhara kwa majirani ambao wanazunguka maeneo ya mabwawa yetu,” ameongeza
“Tumeshaanza kazi kwa kushirikiana na viongozi wa maeneo hayo kutoa elimu kwa wananchi lakini ni sisi wenyewe kuchukua tahadhari ili maji yatakapokuwa mengi basi yasije yakaleta madhara kwa majirani na wananchi walio karibu na mabwawa yetu ya kuzalisha umeme,” ameongeza Twange.
TANESCO imesema itaendelea kuchukua tahadhari na kuimarisha utayari wake kukabiliana na athari za El Niño, huku wananchi wakihimizwa kushirikiana na shirika hilo kwa kutoa taarifa mapema na kuzingatia usalama wa umeme.
RC TANGA: WASTAAFU LINDENI MAFAO YENU, TUMIENI MIFUMO YA KIDIJITALI
biashara
Mkuu wa mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian akizungumza katika semina ya PSSSF kwa maafisa Rasilimaliwatu wa mkoa wa Tanga kilichofanyika mapema leo Septemba 17, 2026 ikiwa na lengo la kuwaelimisha huduma mbalimbali zitolewazo na Mfuko na hasa kuwahamasisha kuwasilisha madai ya wanachama kwa wakati na matumizi ya kidigitali.NA MWANDISHI WETU, TANGA
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian amewataka wastaafu kulinda mafao yao dhidi ya matapeli, huku akiupongeza Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) kwa kuhamasisha matumizi ya mifumo ya kidijitali inayorudisha heshima na tabasamu kwa wastaafu.
Akifungua semina ya PSSSF kwa waajiri iliyofanyika jijini Tanga iliyowakutanisha Maafisa Rasilimaliwatu na Utawala 120 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali, Balozi Dkt. Batilda alieleza kuwa maboresho hayo yanaendana na maagizo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutoa huduma bora, za haraka na bila vikwazo. "Niwapongeze sana PSSSF kwa hatua hii inaowezesha Mafao kulipwa kwa haraka," alisema.

Meneja wa PSSSF Kanda ya Kaskazini Mashariki, Kwame Temu, aliwahimiza waajiri kutoa taarifa za watumishi wapya ndani ya siku 30 ili wasajiliwe mapema na kuwahamasisha watumishi kutumia kikamilifu mifumo ya kielektroniki. Kwa upande wake, Afisa Mfawidhi wa Mkoa wa Tanga, Bi. Hanim Babika, alisisitiza waajiri kufanyia kazi changamoto ya kugongana kwa taarifa na kuhakikisha wafanyakazi wa mikataba kusajiliwa.
Akitoa ushuhuda, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Mchatta alisema elimu inayotolewa na PSSSF imebadili kabisa maisha ya wastaafu wa sasa, kwani wanatoka utumishi wakiwa wanajiamini na wenye uelewa mpana wa uwekezaji. "Sekretari wangu alipostaafu, alikuja ofisini kwangu mwenye furaha, ananieleza habari za fursa za uwekezaji tu baada ya kupata mafunzo ya PSSSF," alisema Katibu Tawala.

PSSSF inaendelea kuwasihi wanachama na wastaafu nchini kutumia mifumo rasmi ya kielektroniki ili kupata huduma kwa haraka, uwazi na usalama zaidi ambayo ni PSSSF Member Portal na PSSSF Kiganjani, aidha wawawe na changamoto kutumia simu ya bure kuwasiliana na Mfuko ambazo ni 0800110055.
Meneja wa PSSSF Kanda ya Kaskazini Mashariki, Bw. Kwame Temu akizungumza katika semina kwa maafisa Rasilimaliwatu na Utawala wa Mkoa wa Tanga.


.jpg)











































