HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

MAVUNDE AZINDUA HELIKOPTA YA KISASA YA BARRICK KWA AJILI YA UTAFITI WA KIJIOLOJIA MKOANI MARA

August 31, 2026 Add Comment

  


Muonekano wa helikopta ya kisasa ya Barrick iliyozinduliwa kwa ajili ya kufanya utafiti wa kijiolojia mkoani Mara.
Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, akikata utepe kuzindua rasmi helikopta ya kisasa ya Barrick kwa ajili ya utafiti wa kijiolojia mkoani Mara. Wengine pichani ni viongozi wa Mkoa wa Mara pamoja na viongozi wa Barrick nchini.

CHATANDA: NDEJEMBI ANA UWEZO MKUBWA WA KUMSAIDIA MAJUKUMU RAIS WETU

August 31, 2026 Add Comment

 NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, ameelezwa kuwa kiongozi mahiri, muadilifu na mzalendo, mwenye uwezo wa kumsaidia majukumu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, Agosti 30, 2026, ofisini kwake Dodoma, siku moja baada ya kukamilika uapisho wa kiongozi huyo, Ikulu ya Chamwino, Dodoma.

Chatanda ameeleza, Ndejembi ni kiongozi wa vitendo na katika majukumu aliyoaminiwa tangu akiwa Mkuu wa wilaya ya Kongwa, Mbunge, Naibu Waziri na Waziri kamili katika wizara mbalimbali.

"Kule Kongwa Dodoma akiwa Mkuu wa wilaya alifanya kazi nzuri na katika kilimo alisimamia kwa mafanikio makubwa kampeni yake aliyoiita ONJAKO yaani Ondoa Njaa Kongwa. Alihimiza wananchi kulima mazao yanayostahimili ukame kama mtama, mihogo, ufuta na alizeti ili kuwaepusha wananchi na kadhia ya njaa," amesema Chatanda.

Ameongeza kuwa, kampeni ya ONJAKO ilipokelewa vizuri na wakulima wa Kongwa kutokana na mwanzo kutilia mkazo zao la mahindi ambalo mara kwa mara walikuwa wakipata mazao kidogo kutokana na changamoto ya ukame wilayani humo.

Akisisitiza utendaji uliotukuka wa Ndejembi, Chatanda amesema, Wizara kadhaa alizohudumu zikiwemo Tamisemi, Vijana, Ardhi, Nishati, ameacha alama kubwa kwa kuwa mstari wa mbele kutatua changamoto za wananchi.

"Ndejembi si mtu wa kukaa ofisini kusubiri taarifa, anakwenda mwenyewe kujionea utekelezaji wa majukumu na maagizo mbalimbali. Ndiyo maana nasema, Rais Dk. Samia amepata msaidizi mchapakazi na hodari kwelikweli," ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo wa UWT Taifa, ametoa rai kwa wananchi kumuombea Rais Dk. Samia, Makamu wa Rais, Ndejembi na viongozi wengine ili waweze kusimamia mipango iliyopo ambayo imejikita katika kukuza ustawi na maendeleo ya wananchi.

Awali, katika uapisho huo, Rais Dk. Samia amemuasa Makamu wa Rais Mteule kuwatumikia Watanzania bila kujali tofauti zao ili kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025-2030 na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo (2050).


MAKAMU WA RAIS, ATEMBELEA OFISI YA MAKAMU WA RAIS MUUNGANO NA MAZINGIRA

August 31, 2026 Add Comment


-AWATAKA WATUMISHI KUACHA KUFANYA KAZI KWA MAZOEA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, amewataka watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kuongeza bidii, uwajibikaji na kuachana na utendaji wa kazi kwa mazoea ili kuhakikisha majukumu ya Serikali yanatekelezwa kwa ufanisi na kwa wakati.

Makamu wa Rais ametoa wito huo leo, alipofanya ziara yake ya kwanza katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), iliyopo Mtumba, jijini Dodoma, ambako alipokelewa na wafanyakazi pamoja na Menejimenti ya Wizara hiyo.

Amesisitiza umuhimu wa watumishi kubadili mitazamo na namna ya kufanya kazi, akitaka kila mmoja kuwa mbunifu na kuweka mipango inayolenga kuleta matokeo yanayoonekana kwa wananchi na Taifa kwa ujumla.

Makamu wa Rais amewasihi watumishi kutumia nafasi zao kutoa huduma yenye thamani kwa watanzania na kutambua dhamana waliyonayo katika kuwahudumia wananchi. Pia amewataka kubadili mitazamo na namna ya kufikiri, kuwa wabunifu na kuhakikisha mipango inayowekwa inaleta tija na matokeo chanya katika shughuli mbalimbali zinazotekelezwa kwa maslahi mapana ya Taifa.

Halikadhalika, amewataka kuongeza jitihada katika kudumisha Muungano kwa kuwa na mipango endelevu inayolenga kutatua changamoto mbalimbali pamoja na kutoa elimu ya fursa zilizopo katika Muungano.

Amewasihi Viongozi na Watumishi wa Wizara hiyo, kuwa na mipango endelevu katika utekelezaji wa ajenda ya ulinzi na uhifadhi wa mazingira kwa kutumia vema kampeni za upandaji miti, usafi wa majiji na miji kwa kuweka nyenzo zitakazosaidia kufanya hali hiyo kuwa endelevu. Vile vile amesisitiza umuhimu wa kuwa na Mpango maalum utakao saidia wananchi kuhama katika shughuli za kila siku zinazoharibu mazingira.

Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhandisi Hamad Masauni, amempongeza Makamu wa Rais kwa kuaminiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika nafasi hiyo na kumhakikishia ushirikiano katika kutekeleza majukumu mbalimbali yanayohusu Ofisi ya Makamu wa Rais.

Akiwasilisha taarifa kuhusu shughuli zinazotekelezwa na idara mbalimbali zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Richard Muyungi, amesema wizara hiyo ina Idara nne, Vitengo nane na Taasisi mbili zinazotekeleza majukumu mbalimbali, ikiwemo utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 katika masuala ya Muungano na Mazingira.













USALAMA WA AFCON 2027: TAEC YAONGEZA NGUVU KATIKA ULINZI WA NYUKLIA

August 31, 2026 Add Comment


Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC), kwa kushirikiana na Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu (IAEA), imeanza kuimarisha maandalizi ya usalama wa nyuklia na mionzi kuelekea Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2027, ambazo Tanzania itakuwa mwenyeji kwa pamoja na Kenya na Uganda.


Maandalizi hayo yanalenga kujenga uwezo wa kitaifa wa kuzuia, kubaini na kukabiliana na vitisho vinavyoweza kuhusisha nyenzo za nyuklia au vyanzo vingine vya mionzi wakati wa mashindano hayo, ambayo yanatarajiwa kuvutia wachezaji, viongozi, mashabiki, waandishi wa habari na wageni kutoka mataifa mbalimbali.


Akifungua rasmi jijini Arusha warsha ya siku tano kuhusu uandaaji na utekelezaji wa hatua za usalama wa nyuklia katika matukio makubwa ya umma, Mkurugenzi Mkuu wa TAEC, Profesa Najat Kassim Mohammed, amesema ukubwa na hadhi ya AFCON 2027 vinahitaji maandalizi ya kina na ushirikiano wa taasisi mbalimbali ili kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika katika mazingira salama.


Warsha hiyo, inayofanyika kuanzia Agosti 31 hadi Septemba 4, 2026, inawakutanisha wataalamu na maofisa kutoka Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Jeshi la Polisi Tanzania, vyombo vya usalama, mamlaka zinazohusika na forodha na uhamiaji, wasimamizi wa viwanja vya michezo pamoja na taasisi nyingine zenye majukumu katika ulinzi na usalama.

Profesa Najat amesema maandalizi ya mashindano yenye hadhi ya AFCON hayaishii katika ujenzi na uboreshaji wa viwanja na miundombinu mingine pekee, bali yanapaswa kwenda sambamba na kuimarisha mifumo ya usalama kwa ajili ya kulinda wananchi na wageni watakaokuwa nchini wakati wa mashindano hayo.

Amesema mikusanyiko mikubwa ya kimataifa inahitaji maandalizi yanayozingatia aina mbalimbali za vitisho na hatari zinazoweza kujitokeza, hivyo ni muhimu kwa taasisi zinazohusika kuwa na uwezo wa kubaini mapema jambo lolote lisilo la kawaida na kuchukua hatua stahiki kwa wakati.

“Ni lazima kuhakikisha kuwa vifaa vya mionzi na nyenzo nyingine zinazohusiana na nyuklia hazitumiki kwa madhumuni ya uhalifu, uharibifu au matumizi mengine yasiyoruhusiwa wakati wa AFCON 2027,” amesema Profesa Najat.

Amesisitiza kuwa usalama wa nyuklia katika matukio makubwa ya umma hauwezi kusimamiwa na taasisi moja pekee, bali unahitaji ushirikiano wa karibu, uratibu na ubadilishanaji wa taarifa kati ya taasisi zote zenye wajibu katika mfumo wa kitaifa wa ulinzi na usalama.

Kwa mujibu wa Profesa Najat, mafanikio katika eneo hilo yatategemea kwa kiasi kikubwa uwezo wa taasisi zinazohusika kufanya kazi kwa pamoja, kila moja ikifahamu wajibu wake na namna ya kushirikiana na taasisi nyingine kabla, wakati na baada ya tukio.

Amesema warsha hiyo ni sehemu ya maandalizi yanayolenga kujenga uelewa wa pamoja miongoni mwa taasisi zinazohusika, kuimarisha uwezo wa wataalamu na kuhakikisha mifumo ya uratibu inafanya kazi kwa ufanisi endapo kutatokea tukio linalohitaji hatua za kiusalama.

Tanzania tayari imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha uwezo wake katika eneo la usalama wa nyuklia na mionzi, ikiwemo matumizi ya vifaa vya kugundua mionzi katika baadhi ya maeneo muhimu na mipakani, pamoja na kuwajengea uwezo maofisa walio mstari wa mbele katika kubaini na kukabiliana na matukio yanayoweza kuhusisha vyanzo vya mionzi.

Profesa Najat amesema pamoja na uwepo wa vifaa hivyo, jambo la msingi ni kuhakikisha wataalamu wana uwezo wa kuvitumia kwa usahihi na taasisi zinazohusika zinafahamu hatua zinazopaswa kuchukuliwa baada ya kubainika kwa tukio linalohitaji uchunguzi zaidi.

Katika kipindi cha siku tano, washiriki watapatiwa mafunzo ya nadharia na vitendo kuhusu hatua za kuzuia vitisho kabla ya tukio, namna ya kuendesha operesheni za usalama katika matukio makubwa, utambuzi wa mionzi, tathmini ya tahadhari, taratibu za upekuzi na matumizi ya vifaa mbalimbali vya kugundua mionzi.

Miongoni mwa vifaa vitakavyotumika katika mafunzo hayo ni Personal Radiation Detectors (PRDs), Radioisotope Identification Devices (RIDs) pamoja na vifaa vya kugundua mionzi vinavyobebwa mgongoni. Washiriki watafundishwa namna ya kutumia vifaa hivyo, kutambua tahadhari zinazotolewa na kufanya tathmini kabla ya hatua nyingine kuchukuliwa.

Mafunzo pia yatahusisha taratibu za kufanya uchunguzi kwa watu na magari, namna ya kuthibitisha tahadhari inayotolewa na vifaa vya kugundua mionzi, pamoja na taratibu za kushughulikia vifurushi vinavyotiliwa shaka.

Profesa Najat amesema sehemu muhimu ya warsha hiyo itakuwa mazoezi ya vitendo yatakayowawezesha washiriki kutumia maarifa watakayopata darasani katika mazingira yanayofanana na hali halisi ya tukio kubwa la umma.

Washiriki watagawa majukumu katika timu mbalimbali, zikiwemo timu ya uongozi wa operesheni, timu za utafutaji na timu ya msaada wa kitaalamu wa masuala ya mionzi. Timu hizo zitafanya maandalizi ya uchunguzi wa eneo kabla ya tukio, kuandaa namna ya kukabiliana na hali mbalimbali na kugawana majukumu kulingana na wajibu wa kila upande.

Mazoezi hayo yatahusisha pia uchunguzi wa kimionzi katika mazingira ya uwanja wa michezo, ikiwemo eneo la uwanja na sehemu za kukaa watazamaji. Lengo ni kuwajengea washiriki uzoefu wa kufanya uchunguzi kabla ya tukio na kutambua mapema hali yoyote inayohitaji hatua zaidi.

Profesa Najat amesema mazoezi hayo yatasaidia kutathmini uwezo uliopo na kubaini maeneo yanayohitaji kuendelea kuimarishwa katika kipindi kilichobaki kuelekea AFCON 2027.

Amesema, hata hivyo, maandalizi hayo hayaishii katika AFCON pekee kwa sababu utaalamu, vifaa na mifumo ya ushirikiano inayojengwa sasa itabaki kuwa sehemu ya uwezo wa Taifa katika kusimamia usalama wa matukio mengine makubwa yatakayofanyika nchini.

“Uwezo tunaoujenga kupitia warsha hii utakuwa rasilimali ya kudumu kwa Taifa letu na utatumika katika kulinda mikutano ya kimataifa, mashindano ya michezo, ziara za viongozi, mikusanyiko mikubwa ya kitaifa na matukio mengine yenye umuhimu mkubwa kwa nchi,” amesema Profesa Najat.

Ameongeza kuwa moja ya mambo yanayotarajiwa baada ya warsha hiyo ni kuwa na mwelekeo wa pamoja kuhusu hatua zinazopaswa kuchukuliwa katika kipindi kilichobaki kuelekea AFCON 2027, huku kila taasisi ikifahamu eneo lake la wajibu na namna ya kushirikiana na taasisi nyingine.

Profesa Najat ameishukuru IAEA kwa kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kujenga uwezo wa wataalamu na kuimarisha mifumo ya usalama wa nyuklia, akisema ushirikiano huo umekuwa muhimu katika kupata utaalamu, mafunzo na uzoefu unaohitajika katika kukabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza.


Kwa upande wake, Kiongozi wa Timu ya Wataalamu kutoka IAEA, Lacina Saro, amepongeza Tanzania kwa kuanza mapema maandalizi ya usalama wa nyuklia kuelekea AFCON 2027, akisema tukio kubwa la aina hiyo linahitaji mipango ya kina, mafunzo na mazoezi ya kutosha kabla ya kuanza kwa mashindano.


“Uchaguzi wa Tanzania kuwa miongoni mwa wenyeji wa AFCON 2027 ni jambo la kujivunia, lakini pia unaambatana na wajibu. Mpangilio wa usalama wa nyuklia wa kiwango hiki unapaswa kuandaliwa mapema, kufanyiwa majaribio kwa kina na kutekelezwa kwa ufanisi na timu za kitaifa zilizopewa mafunzo,” amesema Saro.


Amesema IAEA itaendelea kushirikiana na Tanzania kupitia utoaji wa miongozo, mafunzo na msaada wa kiufundi unaolenga kuimarisha uwezo wa nchi katika usalama wa nyuklia.


“Tuko hapa kufanya kazi pamoja nanyi na kuunga mkono Tanzania katika kujenga uwezo wa usalama wa nyuklia ambao mnaweza kuutegemea wakati wa AFCON 2027 na hata baada ya mashindano hayo,” amesema Saro.


Naye Mkurugenzi wa Teknolojia na Huduma za Ufundi wa TAEC, Dkt. Remigius Kawala, amesema Tanzania inaendelea kujiandaa katika eneo la usalama wa nyuklia na mionzi huku Serikali ikiendelea kuwekeza katika wataalamu, vifaa na mifumo inayohitajika kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika katika mazingira salama.


Dkt. Kawala amesema Tanzania ina wataalamu wenye ujuzi pamoja na vifaa vinavyoweza kutumika katika kubaini na kukabiliana na vitisho vinavyoweza kuhusisha mionzi, huku mafunzo yanayoendelea yakilenga kuongeza uwezo wa taasisi mbalimbali kufanya kazi kwa pamoja.


Amesema maandalizi hayo yanalenga pia kujenga uwezo wa muda mrefu utakaotumika kulinda wananchi na miundombinu muhimu wakati wa matukio mengine makubwa yatakayofanyika nchini.


Dkt. Kawala amewataka washiriki kutumia kikamilifu fursa ya mafunzo hayo kuongeza ujuzi, kubadilishana uzoefu na kuimarisha uratibu baina ya taasisi zao, hatua ambayo itasaidia kuongeza utayari wa nchi kuelekea mashindano hayo.


Warsha hiyo itahitimishwa Septemba 4, 2026, baada ya washiriki kupitia mafunzo ya darasani na mazoezi ya vitendo yatakayohusisha maandalizi ya eneo, uchunguzi wa kimionzi, tathmini ya tahadhari na namna ya kuchukua hatua pale tukio lisilo la kawaida linapobainika.


TAEC itaendelea kushirikiana na taasisi za kitaifa na washirika wa kimataifa katika kuimarisha usalama wa nyuklia na mionzi nchini, huku maandalizi ya AFCON 2027 yakitumika pia kama fursa ya kuongeza uwezo wa wataalamu na kuimarisha mifumo itakayoendelea kutumika hata baada ya mashindano hayo.


Hatua hiyo ni sehemu ya jitihada za kuhakikisha Tanzania inaingia katika AFCON 2027 ikiwa imejiandaa si katika viwanja na miundombinu pekee, bali pia katika eneo la usalama, ili wananchi na wageni watakaofika nchini waweze kushiriki na kufurahia mashindano hayo katika mazingira salama.












NYUMBA INAYOGUNDUA MVUA YAWASHA MOTO WA UBUNIFU KWA VIJANA

August 31, 2026 Add Comment

Na Oscar Assenga, TANGA

IMAGINE umefua nguo zako, ukaondoka nyumbani kwa ajili ya shughuli zako, ghafla mvua ikaanza kunyesha. Badala ya kukimbia kurudi kuzianua, nyumba yenye teknolojia maalumu inagundua mvua na kuhamisha nguo hizo sehemu salama.

Hiyo ni moja ya bunifu zilizobuniwa na vijana wanaoshiriki katika mradi wa Vijana Bunifu, unaotekelezwa chini ya programu ya Tanga Yetu, kwa lengo la kuwajengea watoto na vijana uwezo wa kutumia Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati (STEM) kutatua changamoto zinazowakabili katika maisha ya kila siku.

Bunifu hiyo imeibua matumaini mapya kwamba teknolojia inaweza kutumika kutatua hata changamoto ndogo zinazoonekana kuwa za kawaida katika maisha ya kila siku, huku ikiwapa vijana nafasi ya kugeuza mawazo yao kuwa suluhisho zinazoweza kutumika na jamii.

Akizungumza kuhusu bunifu hiyo, Mohamed Mohamed, Mkufunzi wa Masomo ya STEM kutoka Project Inspire, alisema mfumo huo umeundwa kwa kuweka kihisi (sensor) kinachoweza kutambua uwepo wa mvua.

Alisema mvua inapoanza kunyesha, kihisi hutuma taarifa kwenye mfumo na kusababisha sehemu maalumu ya kukaushia nguo kuhamia upande ambao haujanyeshewa, hivyo kuzuia nguo kulowana.

“Tumewafundisha wanafunzi namna ya kutumia teknolojia kutatua changamoto zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku. Kwa mfano, mtu amefua nguo na anatakiwa kwenda kwenye kikao, lakini mvua inaanza kunyesha. Mfumo huu unatambua mvua na kupeleka nguo sehemu ambayo hazitanyeshewa,” alisema Mohamed.

Alisema mvua inapokatika, mfumo huo hutambua mabadiliko hayo na kuirudisha sehemu ya kukaushia nguo upande wenye jua ili nguo ziendelee kukauka.

Kwa Mohamed, bunifu hiyo ni mfano wa namna vijana wanavyoweza kuangalia changamoto zinazowazunguka, kuzitafakari na kutumia maarifa ya STEM kutengeneza suluhisho badala ya kusubiri majibu kutoka kwa wengine.
Vijana wafundishwa kugeuza mawazo kuwa suluhisho

Alisema lengo la mradi wa Vijana Bunifu si kuwafundisha vijana nadharia pekee, bali kuwapa uwezo wa kuunganisha elimu wanayopata darasani na changamoto halisi zilizopo katika jamii.

“Tunataka mtoto na kijana apate interest katika masomo ya STEM, kisha aweze kuchukua wazo lililopo kichwani na kulipeleka kwenye uhalisia ili liweze kutatua changamoto katika jamii,” alisema.

Alisema Project Inspire inatekeleza mpango huo kupitia mfumo unaoitwa STEM Career Radar, unaolenga kumjengea mtoto msingi wa elimu ya STEM tangu akiwa mdogo na kumwandaa kwa taaluma mbalimbali za baadaye, zikiwamo udaktari, uhandisi na Sayansi ya Kompyuta.

Kwa mujibu wa Mohamed, programu hiyo inawahusisha watoto wenye umri wa chini ya miaka mitatu hadi 12, ambao hufundishwa sayansi kwa njia ya vitendo ili kufanya ujifunzaji kuwa rahisi, wa kuvutia na wenye matokeo.
Boot Camp chachu ya ubunifu

Alisema kwa vijana wenye umri wa miaka 13 hadi 18, mradi huo unalenga zaidi kuwawezesha kuibua na kukuza mawazo ya kibunifu yanayoweza kutatua changamoto za jamii.

Vijana hao hupewa mafunzo ya vitendo kupitia programu mbalimbali, ikiwemo Boot Camp, inayowapa nafasi ya kujifunza, kujadiliana na kuendeleza mawazo yao hadi kufikia hatua ya kutengeneza bunifu.

“Katika ngazi hii tunawawezesha vijana kujifunza kwa vitendo na kutatua changamoto zilizopo kwenye jamii. Tunatumia programu mbalimbali, ikiwemo Boot Camp, ambapo vijana hupewa nafasi ya kukuza mawazo yao na kuyafanyia kazi,” alisema.
Kutoka mwanafunzi hadi kuwa mlezi wa wabunifu

Mmoja wa wanufaika wa mradi huo, Mboni Zahoro, alisema safari yake katika STEM ilianza akiwa mwanafunzi na mshiriki wa programu ya Boot Camp, kabla ya baadaye kuamua kutumia uzoefu alioupata kuwasaidia vijana wengine.

Alisema baada ya kumaliza mafunzo, aliamua kujitolea na kujifunza zaidi namna ya kuwawezesha vijana kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu katika kutatua changamoto zinazowazunguka.

Mboni alisema kupitia mradi wa Vijana Bunifu, alipata nafasi ya kuwa STEM Communicator, jukumu linalompa nafasi ya kuwasaidia vijana wengine kukuza mawazo yao na kuyabadilisha kuwa bunifu.

“Nilianza kama mwanafunzi na mshiriki wa Boot Camp, lakini baada ya kumaliza masomo niliamua kujitolea kuwasaidia vijana wenzangu. Sasa ninawasaidia kuchukua mawazo yao na kuyakuza kupitia teknolojia na ubunifu,” alisema.

Alisema uzoefu huo umemfundisha kuwa vijana wanapopewa nafasi, vifaa na mazingira sahihi ya kujifunza, wana uwezo mkubwa wa kuibua mawazo yanayoweza kuleta mabadiliko katika jamii.

Kwa mtazamo wake, kuwafundisha vijana STEM kwa vitendo ni muhimu kwa sababu kunawapa nafasi ya kujaribu mawazo yao, kujifunza kutokana na makosa na hatimaye kutengeneza suluhisho zinazoweza kutumika katika maisha halisi.

Mradi wa Vijana Bunifu unaendelea kuonyesha kwamba ubunifu hauanzi katika maabara kubwa pekee; unaweza kuanzia kwenye changamoto ndogo inayomkabili mtoto au kijana nyumbani, shuleni au katika jamii yake—na kugeuka kuwa teknolojia yenye uwezo wa kurahisisha maisha ya watu.

DKT. MUNISI: VIONGOZI WA DINI HUBIRINI MAADILI MEMA, DUMISHENI AMANI NCHINI

August 30, 2026 Add Comment
​Na. OWM (KAM) Mwanga

​Serikali imezitaka taasisi na viongozi wa dini nchini kuendelea kuwa mstari wa mbele katika kuhubiri maadili mema, mshikamano na uvumilivu ili kujenga jamii yenye amani, utulivu na uchaji wa Mungu.

DKT. SAJAD: NDEJEMBI ANA UWEZO WA KUMSAIDIA RAIS SAMIA KIKAMILIFU

August 30, 2026 Add Comment

Mtaalamu katika Sekta ya Mafuta nchini, Dkt. Sajad Habib Rai, amempongeza Makamu wa Rais, Mhe. Deogratius Ndejembi, kwa kuapishwa kushika nafasi hiyo, huku akimtabiria mambo makubwa katika utekelezaji wa majukumu yake ya kumsaidia Rais Samia Suluhu Hassan.
SHERIA YA NHIF KUPANUA WIGO WA WANACHAMA NA KUBORESHA HUDUMA

SHERIA YA NHIF KUPANUA WIGO WA WANACHAMA NA KUBORESHA HUDUMA

August 30, 2026 Add Comment

Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) uko kwenye mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Sura ya 395, kwa lengo la kupanua wigo wa wanachama, kuendana na mahitaji ya sasa ya huduma za afya na kuimarisha uendelevu wa Mfuko.

Marekebisho hayo pia yanalenga kuimarisha udhibiti wa matumizi mabaya ya Mfuko, ikiwemo udanganyifu unaoweza kufanywa na baadhi ya wanachama, waajiri na watoa huduma za afya lakini kwenda sambamba na sheria Mama ya Bima ya Afya kwa Wote.

Akizungumza  katika ukumbi wa mikutano wa NHIF, Kinondoni, Dar es Salaam, wakati wa kupokea maoni ya wadau kuhusu mapendekezo ya marekebisho ya sheria hiyo, Meneja wa Huduma za Sheria wa NHIF, Matamus Fungo, amesema sheria hiyo iliyotungwa mwaka 1999 inahitaji maboresho ili iendane na mabadiliko yaliyopo katika sekta ya afya na mwelekeo wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote.

“Tunataka sheria yetu iweze kuboreshwa ili iwezeshe watu wengi zaidi kujiunga na pia kuziba mianya ya matumizi mabaya ya kadi yanayofanywa na baadhi ya wanachama wasio waaminifu” amesema.

Amesema marekebisho hayo yanatarajiwa kuongeza idadi ya wanachama, kuimarisha uendelevu wa Mfuko na kuweka mifumo madhubuti zaidi ya kudhibiti udanganyifu na matumizi yasiyofaa ya huduma za bima ya afya.

Kuzingatia Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote

Kwa upande wake, Wakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Mwenda Tulalemwa, amesema marekebisho ya sheria yanapaswa kuzingatia mahitaji ya makundi mbalimbali ya wananchi pamoja na kuendana na Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, ili kuhakikisha hakuna mgongano wa kisheria.

Amesema wadau waliotoa maoni wamependekeza maboresho katika maeneo mbalimbali, ikiwemo mfumo wa malipo kwa vituo vya kutolea huduma za afya, huduma kwa watu wasio na uwezo na watu wenye ulemavu.

Aidha, miongoni mwa mapendekezo yaliyotolewa ni kuongeza umri wa watoto wanaotambuliwa kama wategemezi kutoka miaka 21 hadi 25, hatua inayolenga kuendana na mahitaji ya familia na mazingira ya sasa.

Naye Wakili wa Mahakama Kuu na mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Ferdinand Makole, amesema marekebisho ya sheria yanaweza kuwa fursa muhimu ya kuongeza urahisi, ufanisi na ubora wa huduma zinazotolewa na NHIF.

Amesema sheria inapaswa kuweka mazingira yatakayowezesha Mfuko kutoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wanachama na wananchi kwa ujumla, huku ikizingatia uendelevu wa Mfuko.

Kwa upande wake, Mwanasheria wa Bohari ya Dawa (MSD), Brighton Mtigani, amesema ushirikishwaji wa wananchi na wadau mbalimbali ni muhimu katika kuhakikisha sheria inayoandaliwa inaendana na mahitaji yanayobadilika ya jamii.

Amesema ushirikishwaji huo utasaidia kujenga mfumo unaozingatia usawa katika upatikanaji wa huduma za afya na kuhakikisha makundi mbalimbali yanapata huduma bila vikwazo visivyokuwa vya lazima.

Maoni ya wadau kuchangia maboresho ya rasimu

Naye Ofisa Sheria Mwandamizi kutoka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Japhes Daudi, amesema maoni yaliyotolewa na wadau yamechukuliwa na yataendelea kutumika katika kuboresha rasimu ya mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.

Kwa ujumla, mchakato huo unalenga kuhakikisha Sheria ya NHIF inaendana na mazingira ya sasa ya utoaji wa huduma za afya na mwelekeo wa Serikali wa kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya kupitia mfumo wa Bima ya Afya kwa Wote.

Marekebisho hayo yanatarajiwa kupanua wigo wa wananchi wanaoweza kunufaika na bima ya afya, kuimarisha udhibiti wa matumizi ya Mfuko, kuboresha huduma kwa wanachama na kuimarisha uendelevu wa NHIF, sambamba na kuchangia utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote nchini.

 

*Bima ya Afya kwa Wote, Jiunge sasa*

DKT. MWIGULU AWASILI KATAVI KUSHIRIKI JUBILEI YA MIAKA 25 YA JIMBO KATOLIKI LA MPANDA

August 30, 2026 Add Comment

 

Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, leo Agosti 30, 2026, amewasili Mpanda mkoani Katavi kuwa Mgeni Rasmi katika Maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 25 ya Jimbo Katoliki la Mpanda.

Maadhimisho hayo yanafanyika katika Viwanja vya Shule ya Sekondari St. Mary, Mpanda, mkoani Katavi.


WALIMU 328 WAPIGWA MSASA KUINUA UFAULU KWA SHULE ZA SEKONDARI TANGA

August 30, 2026 Add Comment

WALIMU 328 kutoka shule 10 za Sekondari katika Jiji la Tanga wanapigwa msasa kupitia semina maalumu inayolenga kuwaongezea ujuzi na mbinu za ufundishaji, hatua inayolenga kuongeza ufaulu wa wanafunzi wa Kidato cha Pili na Nne.

Semina hiyo inaendeshwa na Taasisi ya Tanzania Centre For Education kupitia mradi wa Tanga Yetu, unaofadhiliwa na Foundation Botnar na kutekelezwa kwa kushirikiana na Innovex, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kukuza ufaulu katika shule za Jiji la Tanga.

Akizungumza wakati wa semina hiyo iliyofanyika katika Shule ya Sekondari Nguvumali,   Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Centre for Education Yusuf Ogutu  alisema mafunzo hayo ni mwendelezo wa semina zilizolenga kuwajengea uwezo walimu katika masomo mbalimbali.
Alisema katika hatua hiyo walimu wa masomo ya Historia, Jiografia, Business Studies na Bookkeeping wamepatiwa mafunzo, huku awali semina ikiwa imefanyika katika Shule ya Sekondari Kihere kwa walimu wa Civics, Kiswahili, Kiingereza, Historia ya Tanzania na Maadili.

Ogutu alisema mpango huo unalenga kuhakikisha walimu wanakuwa na uelewa na lugha moja katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili wanafunzi na hatimaye kuboresha ufaulu.

“Tunawapatia walimu maarifa na mafunzo, pamoja na kuwawezesha gharama za usafiri kutoka walikotoka na kurejea. Hii ni sehemu ya mpango mpana wa kuhakikisha kampeni ya kukuza ufaulu katika Jiji la Tanga inafikia malengo,” alisema.
Alisema kampeni hiyo inatekelezwa kwa hatua mbalimbali, ambapo awamu ya kwanza iliwahusisha wanafunzi, hatua ya pili ni walimu na awamu inayofuata itawahusisha waratibu wa elimu ngazi ya kata, maafisa elimu wa wilaya pamoja na kamati za malezi na wazazi.

Kwa mujibu wa Ogutu, mpango huo unalenga kuwafanya wadau hao kuwa na uelewa unaofanana katika kuhakikisha wanashirikiana kutafuta suluhisho la changamoto zinazoathiri ufaulu wa wanafunzi.

Alisema hadi sasa walimu 85 tayari wamefikiwa kupitia mafunzo hayo, huku idadi hiyo ikitarajiwa kuongezeka hadi kufikia walimu 100 katika awamu inayoendelea, kabla ya kukamilishwa kwa mafunzo ya walimu wa masomo ya sayansi.
Ogutu alisema jumla ya walimu 328 katika shule 10 wanatarajiwa kunufaika na mpango huo, ambao unalenga kutoa mchango katika kuboresha matokeo ya wanafunzi wa Jiji la Tanga.

Wakufunzi kutoka shule bora
Aidha, alisema walimu wanaopatiwa mafunzo hayo wanafundishwa na wakufunzi wenye uzoefu kutoka baadhi ya shule zilizofanya vizuri kitaifa, hatua inayolenga kuwapatia mbinu bora za ufundishaji.

Alizitaja baadhi ya shule hizo kuwa ni Mzumbe, Marian Boys na Feza Boys, ambazo zimekuwa zikifanya vizuri katika mitihani ya kitaifa.
Alisema pia kuna wakufunzi kutoka Canossa pamoja na shule mbalimbali za Serikali zilizowahi kufanya vizuri kitaifa.

“Tunawaamini sana walimu kwa sababu wao ndiyo injini ya matokeo. Ukiwapiga msasa walimu na kuwaongezea uwezo, unakuwa umeweka msingi mzuri wa kuboresha ufaulu wa wanafunzi,” alisema.
Alisema katika semina hizo walimu wanapata nafasi ya kujadili changamoto mbalimbali za ufundishaji, ikiwemo mada ambazo zimekuwa zikiwasumbua, ili kupata ufumbuzi na kuhakikisha wanakuwa na uelewa unaofanana katika ufundishaji.

Alisema kupitia mpango huo, matarajio ni kuona walimu wakiboresha namna ya kufundisha na wanafunzi wakipata uelewa mzuri wa masomo, jambo litakalosaidia kuongeza ufaulu katika mitihani ya Kidato cha Pili na Nne.
Mpango huo ni sehemu ya juhudi za Tanga Yetu za kuwaunganisha wanafunzi, walimu, wazazi na wadau wengine wa elimu katika kutafuta njia za kuboresha kiwango cha ufaulu katika shule za Jiji la Tanga.