HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

TARURA YA KAMILISHA UJENZI BARABARA YA ESO-LONGDON KWA KIWANGO CHA LAMI

March 15, 2026 Add Comment


Arusha


Serikali kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imekamilisha ujenzi wa barabara ya Eso–Longdon yenye urefu wa kilomita 1.8 kwa kiwango cha lami katika Jiji la Arusha.


Akizungumza wakati wa ziara ya kutembelea miradi inayotekelezwa na TARURA, Meneja wa TARURA katika Halmashauri ya Jiji la Arusha, Mhandisi Godfrey Bwire amesema barabara hiyo imekamilika na kazi iliyobaki ni uwekaji wa taa za barabarani pamoja na matuta.

“Katika mwaka huu wa fedha, serikali kupitia TARURA imefanikiwa kukamilisha ujenzi wa barabara ya Eso–Longdon kwa kiwango cha lami. Kilichobaki ni uwekaji wa taa za barabarani na matuta,” amesema.


Amesema barabara hiyo imejengwa kwa kutumia mapato ya ndani na ina umuhimu mkubwa katika kupunguza msongamano wa magari, hasa katika eneo la soko la Kilombero linalojengwa kupitia mradi wa TACTIC.


Amefafanua kuwa barabara hiyo itatumika kama njia mbadala kwa watumiaji wa barabara wanaotoka Mromboo badala ya kuzunguka eneo la Sombetini, hivyo kusaidia kurahisisha usafiri na kupunguza msongamano.


Aidha, amesema utekelezaji wa miradi ya TACTIC unaendelea katika mwaka wa fedha 2025/2026, ikihusisha ujenzi wa kilomita 10.2 za barabara kwa kiwango cha lami.


Amezitaja barabara hizo kuwa ni pamoja na barabara ya Shelatoni yenye urefu wa kilomita 4.8, barabara ya Orasiti kilomita 3.96 na barabara inayoelekea Orjoro yenye urefu wa kilomita 1.475 ambako kunajengwa kituo kikubwa cha mabasi jijini Arusha.


Amesema miradi hiyo inalenga kuboresha usafiri, kupunguza msongamano wa magari na kuchochea shughuli za kiuchumi katika jiji hilo.


Pia Jiji la Arusha linaendelea kutekeleza miradi mingine kupitia TACTIC ikiwemo ujenzi wa stendi ya mabasi, masoko ya Kilombero na Moromboo pamoja na uboreshaji wa bustani ya Themi miradi hiyo ina thamani ya bilioni 30.6.


Mbali na miradi hiyo, amesema kuna miradi mingine inayotekelezwa kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara (Road Fund), ikiwemo ujenzi wa barabara kutoka Vijenge Juu hadi Ngurero, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kupunguza msongamano wa magari katika Jiji la Arusha.


Amesema mipango inaendelea ya kujenga barabara nyingine kwa kiwango cha lami ikiwemo barabara ya Kibo yenye urefu wa kilomita 3.55 kutoka Mromboo hadi Arusha Girls kupitia Uwanja wa Ndege, pamoja na barabara ya Lemala yenye urefu wa kilomita 4 kuelekea TBL na UNGA Limited.


Akizungumzia mwitikio wa wananchi, Mhandisi Bwire amesema wamepokea kwa furaha ujenzi wa barabara hizo kwani hapo awali zilikuwa na changamoto kubwa hasa wakati wa mvua na vumbi wakati wa kiangazi.


Amewataka wananchi kutunza miundombinu hiyo kwa kuepuka kutupa taka katika mitaro ya maji na kuhakikisha inasafishwa mara kwa mara ili kuruhusu maji kupita vizuri.


Pia amewahimiza kulinda taa za barabarani ili ziweze kudumu kwa muda mrefu na kusaidia kuimarisha usalama wakati wa usiku.


Amesema serikali hutumia gharama kubwa kujenga miundombinu hiyo hivyo ni wajibu wa wananchi kuilinda na kuitunza kwa manufaa ya wote.

NYAYO ZA LAETOLI FURSA YA VIWANDA VYA VIATU DUNIANI KUTENGENEZA VIATU VYA KIHISTORIA

March 15, 2026 Add Comment







Kuna methali isemayo “Asiyejua maana haambiwi maana “ lakini Ngorongoro leo itakuambia maana ya Nyayo za Laetoli.

Nyayo hizi ni za kihistoria na ni sehemu pekee duniani ambayo mafundi Viatu ulimwenguni wanaweza kufika na kutengeneza Viatu vya kihistoria vinavyoweza kushinda nishani ya Nobel kutokana na Nyayo za Laetoli zilivyo.

Katika eneo la Laetoli ndani ya hifadhi ya Ngorongoro, tarehe 24, Julai mwaka 1978, Mtafiti maarufu wa masuala ya Akiolojia Dr. Mary Leakey na timu yake iliyomhusisha Dkt. Paul Abell waligundua nyayo za zamadamu katika eneo la Laetoli zilizohifadhika katika mwamba wa jivu la volcano inayoaminika kuwa ililipuka katika mojawapo wa milima ya Ngorongoro miaka milion 3.6 iliyopita.

Wataalamu hawa wanaamini kuwa nyayo hizo ziliachwa na jamii ya watu wa kale wanaofahamika kama Australopithecus Afarensis.

Nyayo za Zamadamu katika eneo la Laetoli ni ushahidi wa pekee na wa bayana duniani kote usiopingika kwamba zamadamu (Hominin) kwa mara ya kwanza walianza kusimama wima na kutembea kwa miguu miwili katika eneo la Laetoli Ngorongoro Tanzania miaka milioni 3.6 iliyopita.

Binadamu hawa waliotembea wima kwa miguu miwili wametokana na babu/bibi mmoja aliyeishi miaka takribani millioni 7 iliyopita.

Mwanadamu aliyepo Tandahimba, Gamboshi kule Bariadi, Tandale kwa mtogole, Mbagala Zakiem na yule aliyepo Jerusalemu, Macca, Dubai, New York, London, Johannesburg, Tehran, Gaza, Misri hadi Sudan na Mumbai wametokana na babu na bibi mmoja.

Katika kuthibitisha uhai, Nyayo za zamadamu ndizo za kustaajabisha katika eneo la Laetoli, zipo nyayo za wanyama wengine wa kale kama vile nyayo za tembo, twiga, faru na wanyama ndogo kama sungura, kanga na aina za wadudu.

Kwa nyayo za Laetoli zilivyo, mafundi Viatu na wamiliki wa viwanda vya Viatu duniani wanaweza kufika katika Eneo hilo ili kupata ujuzi zaidi wa namna ya kutengeneza Viatu vya kihistoria.

Karibu kwetu Ngorongoro ambapo kila ukilala kuna ndoto ya maajabu inakuita



Muonekano wa Nyayo za Laetoli zilizoachwa na jamii za watu wa kale wanaofahamika kama Australopithecus Afarensis

WAZIRI NANAUKA -SERIKALI ITAENDELEA KUVIPA KIPAUMBELE VIKUNDI VINAVYOREJESHA MIKOPO

March 15, 2026 Add Comment

 

















Na Oscar Assenga,Muheza, Tanga

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka amesema serikali itaendelea kuvipa kipaumbele vikundi vya vijana vinavyoonyesha uwajibikaji kwa kurejesha mikopo wanayopewa ili viweze kukuza shughuli zao za kiuchumi.

Nanauka aliyasema hayo leo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyotembelea kikundi cha Vijana cha Mali Hai kilichopo wilayani Muheza mkoani Tanga kwa lengo la kukagua shughuli zao za uzalishaji pamoja na miradi iliyopata fedha kupitia mikopo ya halmashauri.

Akiwa kwenye kikundi hicho alionyesha kuridhishwa na juhudi na nidhamu ya kikundio hicho kurejesha mikopo baada ya kufanikiwa kukuza mtaji wake kutoka shilingi milioni 20 hadi kufikia zaidi ya shilingi milioni 50, hatua inayotajwa kuwa mfano bora kwa vikundi vingine vya vijana nchini.

Nanauka alisema kikundi cha Mali Hali ni miongoni mwa vikundi vichache nchini vilivyofanikiwa kurejesha mikopo kwa wakati, jambo ambalo limekifanya kupata nafasi ya kuangaliwa kwa karibu zaidi katika mipango ya kusaidiwa kuongeza mtaji na kupanua shughuli zake.

Alisema katika mchakato unaoendelea wa kusaidia wajasiriamali wadogo na kurasimisha shughuli zao, serikali itaangalia namna ya kukiweka kikundi hicho kwenye orodha ya vikundi vitakavyosaidiwa ili kuimarisha shughuli zao za uzalishaji.

Aidha, alieleza kuwa serikali inatekeleza maelekezo ya Rais ya kuhakikisha vijana wanaochukua hatua ya kufanya kazi na kuonyesha juhudi wanapatiwa mikopo na serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi na pia kutoa ajira kwa wengine.

“Vijana hawa wameonyesha mfano mzuri kwa watanzania wengine wameanza na mtaji mdogo mwaka 2008,wakapata msaada wa shilingi milioni tano mwaka 2018 na baadaye mkopo wa shilingi milioni 20 mwaka wa fedha 2020/2021. Leo hii wameongeza mtaji wao hadi kufikia zaidi ya milioni 50. Huu ni ushahidi kwamba ndoto kubwa zinaweza kuanza na mwanzo mdogo,” alisema Nanauka.

Aliongeza kuwa serikali itahakikisha vijana wenye juhudi kama hao wanapata fursa zaidi, ikiwemo mikopo mingine, pamoja na kushirikishwa katika zabuni za serikali ili waweze kukuza biashara zao.

Nanauka pia aliwashauri vijana nchini kutokudharau mwanzo mdogo na kuwa na uvumilivu wanapotekeleza ndoto zao za kimaendeleo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Hawa Mchafu, alisema kamati hiyo ipo katika ziara ya kawaida ya kukagua miradi ya maendeleo kabla ya kuanza kwa Bunge la Bajeti, ambapo wamepita katika maeneo mbalimbali kutathmini miradi iliyopata fedha za serikali.

Alisema kamati hiyo imevutiwa na kazi nzuri inayofanywa na kikundi hicho cha vijana, lakini imebaini changamoto ya eneo la uzalishaji kuwa dogo na huenda lisiweze kukidhi mahitaji yao iwapo wataongeza mtaji zaidi.

Kutokana na hali hiyo, kamati imeitaka wizara husika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuhakikisha vijana hao wanapatiwa eneo kubwa zaidi la kufanyia shughuli zao za uzalishaji ili waweze kupanua biashara zao.

“Eneo walilonalo sasa ni dogo ukilinganisha na malengo yao ya kupanua uzalishaji hivyo tunashauri wapatiwe eneo kubwa zaidi na lililopo sasa likibaki kama sehemu ya maonesho ya bidhaa wanazozalisha,” alisema Mchafu.

Pia aliishauri serikali kuangalia uwezekano wa kukipa kikundi hicho mkopo mwingine wa kifedha ili kiweze kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazokikabili, ikiwemo kununua gari kwa ajili ya shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa.

Aidha, alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha vijana nchini kutumia fursa zilizotolewa na serikali kupitia mifuko mbalimbali ya maendeleo ya vijana badala ya kujikita kwenye mfuko mmoja pekee.

Mchafu alisema kuwa Rais ametoa zaidi ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vijana kupitia wizara na taasisi mbalimbali, hivyo vijana wanapaswa kuzitumia fursa hizo kujikwamua kiuchumi.

Kamati hiyo pia imeishauri serikali kuhakikisha sheria ya manunuzi ya umma inayotaka asilimia 30 ya zabuni za serikali zitolewe kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu inatekelezwa kikamilifu ili kuwapatia vijana nafasi ya kukua kiuchumi.

Kwa sasa kikundi cha Mali Hali kinadaiwa kuajiri vijana zaidi ya 20 katika shughuli zake za uzalishaji, jambo ambalo limeelezwa kuwa linaunga mkono dhamira ya serikali ya kukuza ajira kwa vijana na kuimarisha uchumi wa wananchi.

Vijana wa kikundi hicho pia wamemshukuru Rais kwa kuendelea kutoa fursa na kuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili kufikia ndoto zao za kuanzisha kampuni kubwa inayoweza kutoa ajira kwa vijana wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini.

Mwisho.

KAMATI YA BUNGE YA SHERIA YATEMBELEA KONGANI YA BUZWAGI NA KUPONGEZA BARRICK KWA KUFUNGA MGODI KITAALAMU

March 15, 2026 Add Comment

    

Wabunge kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakitembelea maeneo mbalimbali walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ya Buzwagi ambayo ipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.
Wabunge kutoka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakitembelea maeneo mbalimbali walipofanya ziara ya kikazi ya kujionea maendeleo ya Kongani Maalum la Uwekezaji (BSEZ) ya Buzwagi ambayo ipo ndani ya mgodi wa Barrick Buzwagi ambao upo katika hatua za mwisho za ufungaji.

FCC YATOA ELIMU KWA WANANCHI WA CHALINZE

March 15, 2026 Add Comment
Maafisa wa kulinda walaji kutoka Tume ya Ushindani (FCC) wametoa elimu kwa wananchi wa Halmashauri ya Chalinze mkoani Pwani kuhusu haki na wajibu wa mlaji, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Kumlinda Mlaji duniani yanayotarajiwa kufanyika Machi 31, 2026.
Elimu hiyo imelenga kuwajengea wananchi uelewa kuhusu namna ya kutambua bidhaa na huduma zenye ubora, pamoja na hatua wanazopaswa kuchukua pale wanapokutana na udanganyifu au ukiukwaji wa haki zao kama walaji. Wananchi pia wamehimizwa kuhifadhi risiti za manunuzi na kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapobaini vitendo vya biashara visivyozingatia sheria.
Maafisa hao wameeleza kuwa lengo la utoaji wa elimu hiyo ni kuhakikisha walaji wanakuwa na uelewa wa kutosha ili kujilinda dhidi ya bidhaa bandia, bei zisizo halali na huduma zisizokidhi viwango. Aidha, wamesisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki kikamilifu katika kulinda maslahi yao kwa kufahamu haki na wajibu wao wanapofanya manunuzi au kutumia huduma mbalimbali.
Maadhimisho ya Siku ya Kumlinda Mlaji hufanyika kila mwaka duniani kote kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu haki za walaji na kuhamasisha biashara kufuata misingi ya haki, uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa bidhaa na huduma. Serikali na taasisi mbalimbali nchini huendelea kutumia maadhimisho hayo kutoa elimu kwa jamii ili kujenga mazingira salama na yenye ushindani wa haki sokoni.
 
 
 

NAIBU WAZIRI ARDHI AITAKA NHC KUONA NAMNA YA KUANZISHA MIRADI MIKUBWA KILA WILAYA NCHINI

March 15, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga,TANGA


NAIBU Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi,Kaspar Mmuya amelitaka Shirika la Taifa la Nyumba (NHC) waanze kufikiria namna ya kuanzisha miradi mikubwa ambayo inaweza kutoa huduma kwa wananchi kwenye kila mikoa na wilaya ili wajipambanue utofauti wao na mashirika mengine.

Mmuya aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea mradi wa Jengo la Kitega Uchumi unaosimamiwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mkwakwani Plaza ambapo alisema kutokana na uwepo wa mahitaji yake kwa wananchi waliopo maeneo mbalimbali hapa nchini.

Mradi huo ni moja ya miradi mingi NHC wanafanya nchini na unagharimu kiasi cha Sh.Bilioni 8.6 fedha ambazo zilizopitishwa na Bunge katika Bajeti ya Mwaka 2025/2026 ambapo ulianza mwaka jana mwezi wa sita na utakamilika kwa muda wa miezi 24 na wanategemeaJune mwakani utakamilika .

Mpaka sasa mradi huo umetekelezwa kwa asilimia 37 na fedha zilizotumika ni zaidi ya Bilioni 2 ambao utakuwa na ghorofa tatu za mwanzo za biashara za kawaida,ya pili na tatu ni kutakuwa na ofisi mbalimbali na ya nne mpaka nane hizo ni kwa ajili ya makazi watajenga nyumba 20 ambazo nyumba 10 zitakuwa na vyumba viwili pamoja na master, jiko na vitu vingine na vyumba 10 zitakuwa na vyumba vitatu.

“Kwa kweli nimetembelea mradi huu nimeridhika kwa maana nimeona thamani ya fedha iliyotumika mpaka asilimia ya utekelezaji kuna uwiano mkubwa nimeangalia ubora na umahiri wa mafundi waliokuwepo nimejiridhisha kuna unadhifu mkubwa kwenye kazi yao”Alisema Naibu Waziri huyo.

Alisema pia ujenzi wa Jengo hilo umezingatia mazingira rafiki kwa watu wote kwamba litakuwa na lifti mbili ambazo zitatoa huduma za kijamii katika ghorifa ya tatu na kuna lifti ambayo watakuwa wanatumia watu watakaokuwa wanakaa juu kwenye nyumba za makazi na nyumba hizo hazitakodishwa zitauzwa kwa mtu yoyote mwenye uwezo wa kununua na matangazo tiyari wamekwisha kuwekwa.

Alisema kuna umuhimu wa uwepo wa miradi kama hiyo katika wilaya mbalimbali ikiwezekana mradi unaofanana nao waweke kwenye majimbo yote 272 ili wakitembea wajumbe NHC wapo katika maeneo ambayo wapiga kura wa Rais,Wabunge na Madiwani wanapotokea lakini niwapongeze kwa mradi huu.

Hata hivyo alimshukuru Rais Dkt.Samia Suluhu kwa kulifanya shirika hilo liwe imara kiuchumi lakini lijielewe sasa linabidi lisonge mbele katika kuwekeza zaidi katika ujenzi wa makazi.

Ambapo zaidi ya nyumba milioni 3 kila mwaka ni mapungufu ama mahitaji ambayo yanahitajika kwenye nchi na wanavyoelewa idadi ya watu inaongezeka kwa kiasi kikubwa na mahitaji ya nyumba yanaongezeka.

“Wito nyie wenyewe mmejionea mradi upo asilimia 37 na zaidi ya asilimia 70 ya Jengo hilo tayari watu wameanza kuchukua nafasi kununua hivyo kuna mahitaji makubwa ya nyumba hapa Tanga ushauri wangu anzeni kufikiri kuanza miradi mikubwa inayoweza kutoa huduma kwa wananchi ili kujipambanua na kujitofautisha na mashirika mengine “Alisema

Kwa upande wake Msimamizi mkuu wa Mradi huo kutoka NHC Ephahim Msigwa alisema mradi huo unatumia fedha za ndani na una ghorofa nane ambapo ghorofa tatu zitakuwa kwa ajili ya biashara na tano za makazi ya watu ambapo mpaka sasa wamekwisha kutumia Bilioni 2.1.

Mradi huo ni wa miaka miwili ambapo ulianza kutekelezwa mwezi juni mwaka 2025 na kwamba unatarajiwa kukamilika ukamilike mwezi juni 2027 ambapo mpaka sasa upo asilimia 37.9 huku wananchi zaidi ya 189 wa Mkoa wa Tanga wakinufaika na ajira kwenye mradi huo.

Mwisho

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA NISHATI NA MADINI YAIPONGEZA TANESCO UTEKELEZAJI WA MRADI WA UMEME JUA KISHAPU

March 15, 2026 Add Comment

 



📌 Watembelea mradi kuona ufanisi wake

📌 Shilingi bilioni 118 zatumika kutekeleza mradi

📌 Watoa rai awamu ya pili kuanza kwa kasi


Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imelipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa usimamizi na utekelezaji mzuri wa Mradi wa Uzalishaji Umeme kwa nguvu ya Jua wa Kishapu wenye uwezo wa Megawati 50 unaotekelezwa katika Mkoa wa Shinyanga.

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Subira Mgallu, mara baada ya Kamati kutembelea mradi huo tarehe 13 Machi, 2026 kwa lengo la kujionea maendeleo ya utekelezaji wake pamoja na ufanisi wa matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mhe. Mgallu alisema mradi huo ni hatua muhimu katika mageuzi ya sekta ya nishati nchini kutokana na matumizi ya teknolojia ya nishati jadidifu.

“Tumetembelea mradi huu wa uzalishaji wa umeme kwa kutumia teknolojia ya jua na tunaona ni mapinduzi makubwa katika sekta ya nishati nchini. Hii ni hatua muhimu kwani kwa mara ya kwanza Tanzania inapata Megawati 50 za umeme kutoka kwenye nishati ya jua,” alisema Mhe. Mgallu.

Alisema Kamati imeridhishwa na namna fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo zimetumika ipasavyo na kufanikisha utekelezaji wa mradi huo kwa ufanisi.

“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, tumeridhishwa na matumizi ya fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya mradi huu. Tunaona wazi kuwa fedha hizo zimetumika vizuri katika utekelezaji wa mradi huu wenye thamani ya takribani shilingi bilioni 118,” alieleza.

Aidha, alisema mradi huo tayari umeanza kuchangia Megawati 50 katika Mfumo wa Gridi ya Taifa, hatua inayochangia kuongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini pamoja na kuimarisha vyanzo mseto vya nishati.

“Utekelezaji wa mradi huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kunakuwa na vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme. Hii inaongeza uhakika wa upatikanaji wa nishati ya umeme nchini,” alisema.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, alisema mradi wa Kishapu unatekelezwa kwa awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme katika Gridi ya Taifa.

“Mradi huu una awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 tayari imekamilika na imeanza kuingiza umeme kwenye Gridi ya Taifa. Awamu ya pili itahusisha uzalishaji wa Megawati 100 zaidi na kufanya jumla ya Megawati 150 kutoka katika mradi huu,” alisema Mhe. Ndejembi.

Kamati hiyo imetoa Rai kwa Wizara ya Nishati na TANESCO  inaendelea kuendelea na  mikakati ya kuanza utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi huo ili kuongeza zaidi uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini.

KAMATI YA BUNGE YARIDHISHWA KASI YA USAMBAZAJI UMEME VITONGOJI 15 KILA JIMBO

March 15, 2026 Add Comment

 


📌 Yasema utekelezaji wa mradi huo umeboresha upatikanaji wa umeme vijijini.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeipongeza Wizara ya Nishati kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kasi ya utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 15 kwa kila jimbo nchini ili kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi wa maeneo ya vijijini.

 Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe.Subira Mgalu ametoa kauli hiyo katika ziara ya Kamati hiyo walioambatana na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, kukagua utekelezaji wa miradi ya umeme katika vitongoji vya Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mhe. Mgalu amesema kuwa Bunge liliidhinisha bajeti ya Wizara ya Nishati kwa mwaka wa fedha 2025/2026 kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji 15 kwa kila jimbo Tanzania Bara kupitia REA, mpango ambao umeanza kuonyesha matokeo chanya katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Amesema katika Mkoa wa Shinyanga pekee, umeme tayari umefika katika vitongoji 90, jambo linaloonyesha juhudi kubwa za Serikali katika kuhakikisha wananchi wa vijijini wanapata huduma muhimu ya nishati.

“Tunaipongeza Wizara ya Nishati kwa kazi nzuri ya kusimamia mradi huu kupitia REA. Kasi ya usambazaji wa umeme vitongojini inaendelea kuleta matumaini makubwa kwa wananchi na kuboresha maisha yao,” amesema Mhe. Mgalu.

Aidha, ameihimiza REA kuendelea kuongeza juhudi katika kupeleka umeme kwenye taasisi muhimu za umma kama zahanati, vituo vya afya, shule za msingi na sekondari, miradi ya maji pamoja na taasisi za dini ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wananufaika na huduma hiyo.

Amesisitiza Wizara hiyo kusimamia wananchi kuunganishiwa huduma ya umeme katika vitongoji kwa gharama ya Sh.27,000 ili kutimiza maono ya Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha umeme unafika katika vitongoji vyote nchini ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome amesema utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme katika vitongoji mkoani Shinyanga unaendelea vizuri na tayari umeanza kuleta manufaa kwa wananchi, hususan katika shughuli za uzalishaji na huduma za kijamii, hali inayoleta tabasamu kwa wananchi.

Amesema ataendelea kushirikiana na Waziri wa Nishati, Mhe.Deogratius Ndejembi, kusimamia maelekezo ya Rais kuhakikisha umeme unawashwa katika vitongoji vyote, sambamba na kauli mbiu ya wananchi wa Mkoa wa Shinyanga ya 'Salome Makamba, Washa umeme'.

Katika ziara hiyo, Kamati ya Bunge pia ilikagua na kuwasha umeme katika Zahanati ya Mine iliyopo Jimbo la Msalala, pamoja na kuwasha huduma ya umeme katika mashine ya kusaga na kukoboa katika Jimbo la Kahama Mjini, huduma zilizopatikana kupitia mradi wa kusambaza umeme vitongoji 15 kwa kila jimbo (HEP IIA).

KAMATI YA BUNGE YAITAKA WMA KUHAKIKI MITA ZA UMEME KWA MUJIBU WA SHERIA

KAMATI YA BUNGE YAITAKA WMA KUHAKIKI MITA ZA UMEME KWA MUJIBU WA SHERIA

March 15, 2026 Add Comment

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeiagiza Wakala wa Vipimo (WMA) kuhakikisha mita za umeme zinahakikiwa kikamilifu kabla ya kufungwa kwa ajili ya matumizi, kwa kuzingatia sheria zilizopo ili kulinda haki za watumiaji.

Aidha, Kamati hiyo imeipongeza WMA kwa jitihada za uhakiki na ukaguzi wa vipimo mbalimbali, ikiwemo mita za maji, huku ikiitaka Wakala hiyo kuendelea kusimamia kwa ukaribu vipimo katika sekta ya ujenzi ili kupunguza malalamiko ya wananchi yanayotokana na bidhaa hizo.

Hayo yameelezwa leo Machi 14, 2026, na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Deodatus Mwanyika, wakati wa ziara ya kikazi katika Kituo cha WMA cha Uhakiki wa Vipimo Misugusugu mkoani Pwani kwa lengo la kukagua miradi ya maendeleo na kujionea shughuli za uhakiki wa vipimo zinavyotekelezwa kituoni hapo.

Akizungumza katika ziara hiyo, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, aliihakikishia Kamati kuwa wizara itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa.

Alisisitiza kuwa azma ya Serikali ni kuhakikisha WMA inasimamia matumizi ya vipimo sahihi katika uzalishaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali, pamoja na Uhakiki wa mita za umeme na maji, ili kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson Simon, akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, alibainisha kuwa uhakiki wa vipimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa mkoa huo. Alieleza kuwa kwa sasa Mkoa wa Pwani una jumla ya viwanda 1,688, vikiwemo viwanda vikubwa 199 na vidogo sana 1,017, hivyo uhakiki wa usahihi wa Vipimo ni nyenzo muhimu katika kuvutia uwekezaji zaidi.

Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Bw. Alban Kihulla, alisema kuwa ukaguzi na uhakiki wa vipimo una nafasi kubwa katika kuhakikisha haki na usawa baina ya pande mbili zinazofanya biashara.

Pia, aliwahimiza wananchi kuhakikisha wanatumia vipimo vilivyohakikiwa, huku akiwasihi watoa huduma kuzingatia uadilifu kwa kutoa huduma kupitia vipimo sahihi ili kuleta usawa na kuhakikisha bidhaa zinazonunuliwa zinaendana na thamani halisi ya fedha.

MTENDAJI MKUU ADEM AFUNGUA KIKAO KAZI CHA CHAMA CHA KUTETEA HAKI ZA WALIMU

March 14, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefungua kikao kazi cha Chama cha Kulinda na Kutetea Haki za Walimu (CHAKUHAWATA) kinachofanyika jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wadau mbalimbali wa sekta ya elimu ili kuimarisha uongozi, utawala bora na udhibiti wa ubora wa elimu nchini.

KAMATI YA BUNGE YAKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA KAMPASI YA CHUO KIKUU MZUMBE TANGA

March 14, 2026 Add Comment
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Mhe. Husna Juma Sekiboko (Mb) akiongoza Wajumbe wa Kamati hiyo kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi ya Tanga, unaotekelezwa kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET).

GRIDI YA TAIFA YA MAJI ITACHOCHEA MAENDELEO KWA KASI

March 14, 2026 Add Comment




Na: Dk. Reubeni Lumbagala, Tanga


Maji ni kimiminika muhimu kwa maisha na uhai wa viumbei. Maji hutumika kuanzia asubuhi, mchana, jioni hadi usiku. Hutumika kwa matumizi ya nyumbani kama kupikia, kufulia na kuogea. Hutumika katika shughuli za kiuchumi kama viwandani, mashambani, migodini, masokoni kutaja kwa uchache. Maji hayana mbadala, panapohitajika maji, hakuna namna nyingine bali kuyatafuta na kukidhi haja yake. Hakuna siku inaweka kupitia bila kutumia maji. Maji ni uhai na maji ni maisha. Binadamu anahitaji maji kila siku. 

Tanzania imebarikiwa kuwa na vyanzo vingi vya maji. Mathalani; bahari, maziwa, mito, mabonde. Vyanzo hivi husaidia kupata maji kwa matumizi mbalimbali. Kutokana na ongezeko kubwa la watu nchini na shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi, mahitaji ya huduma ya maji pia yameongezeka sana. Wizara ya Maji yenye dhamana ya usambazaji wa huduma ya maji katika maneno mbalimbali nchini ina wajibu mkubwa wa kuhakikisha maji yanawafikia wahitaji ili kuchochea shughuli mbalimbali za kimaendeleo nchini.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ni mdau mkubwa wa sekta ya maji. Anatambua umuhimu wa maji kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Kutokana na hilo, amekuwa akiongeza fedha katika bajeti ya Wizara ya Maji kila mwaka, jambo linalosaidia utekelezaji wa miradi ya maji ambayo inakwenda kutatua changamoto za maji katika maeneo mbalimbali nchini na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwani maji ni kiungo muhimu sana. Mathalani kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Bajeti ya Wizara ya Maji ilikuwa Sh. 1.01 trilioni ambapo katika fedha hizo, Sh. 943.22 bilioni zilikuwa ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Hii inaonyesha namna Wizara ya Maji ilivyojizatiti kutatua kero za wananchi kwa kupeleka fedha nyingi kwenda kwenye miradi ya maji.

Rais Dk. Samia pia ameelekeza Wizara ya Maji kufanikisha mradi kabambe wa Gridi ya Taifa ya Maji kama ilivyo Gridi ya Taifa ya Umeme inayosimamiwa na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha nchi inakuwa na uhakika wa maji kwa shughuli mbalimbali za maendeleo. Kwa nchi yetu yenye utajiri wa vyanzo vya maji, mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji ni suala muhimu hasa kipindi hiki ambacho dunia inapitia changamoto ya mabadiliko ya tabia ya nchi. 

Gridi ya Taifa ya Maji itakusanya maji kutoka vyanzo mbalimbali vya maji nchini kwa matumizi ya kimaendeleo. Kilimo ambacho ndiyo uti wa mgongo wa uchumi wetu kinahitaji sana raslimalimaji kwa ajili ya umwagiliaji. Kilimo cha kutegemea maji ya mvua pekee hakitoi uhakika kwa kupata mavuno kwani endapo kutatokea ukame au uhaba wa mvua, mazao yatanyauka na kufa kabisa. Uwepo wa maji ya kutosha unatoa uhakika wa kuvuna, kupata chakula na fedha baada ya kuuza mazao ndani na nje ya nchi. Maji yanawezesha pia uzalishaji wa umeme wa nguvu za maji (Hydo-Electric Power - HEP).

Maji ya uhakika yanatoa uhakika wa uendelevu wa shughuli za ufugaji. Wanyama na ndege watapata maji ya kunywa na majosho ya kuogeshea wanyama. Uvuvi unategemea uwepo wa maji, ukosefu wa maji unarudisha nyuma shughuli za uvuvi ambazo ni muhimu kwa uchumi wetu. Maeneo ya biashara kama masokoni vilevile wanahitaji maji kwa ufanisi wa shughuli zao. Wachimbaji wa madini na wahandisi wa ujenzi nao wanahitaji maji katika shughuli zao. Maeneo ya taasisi kama shule na hospitali, nao bila maji maisha hayaendi.


Katika kufanyia kazi maelekezo ya Rais Dk. Samia kuhusiana na mradi wa Gridi ya Taifa ya Maji, hivi karibuni Waziri wa Maji Jumaa Aweso, Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Mwajuma Waziri pamoja na watendaji wa sekta ya Maji walifanya ziara katika Jimbo la Shan Dong Kaskazini mwa China kuona na kujifunza namna walivyofanikiwa kuviunganisha vyanzo vya mito na maziwa katika Gridi ya Taifa ya Maji kutoka Kaskazini hadi Kusini mwa China.


Kimsingi, mpango uliopo nchini ni kuviunganisha vyanzo mbalimbali vya maji nchini kama vile Maziwa ya Viktoria, Tanganyika na Nyasa pamoja na mito ya Rufiji, Kagera, Kiwira, Wami, Pangani, Ruvu na Ruvuma na vyanzo vingine ili kuwa na uhakika wa maji kwa maendeleo ya sekta mbalimbali. Katika kutekelekeza miradi huu, ni vyema wananchi tukawa mabalozi wazuri wa kutunza vyanzo vya maji vilivyopo na kutunza mazingira kwa ujumla. Tukumbuke maji hayana mbadala, kila mtu anahitaji maji. Kwa hakika, mafanikio ya kuwa na Gridi ya Taifa ya Maji ni uhakika wa kupata maendeleo endelevu. Tuunge mkono mradi huu muhimu kwa manufaa ya kizazi cha leo na kijacho. Tafakari.


Maoni: 0620 800462.

MZIKI WA DKT.AGNES GIDNA WAIKUNA KAMATI YA BUNGE

March 14, 2026 Add Comment




Kamati ya kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imempongeza Afisa Uhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Dkt. Agnes Gidna kutokana na umahiri, umakini, kujiamini na uchambuzi wake mkubwa wa masuala ya mambo kale na jiolojia.


Wakiongozwa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Timotheo Mnzava wabunge hao wametoa pongezi hizo baada ya kukagua na kupata maelezo ya mradi wa makumbusho ya _Urithi Geopark Museum._ 


Wabunge wamepongeza kazi kubwa iliyofanywa na serikali ya Tanzania na China ambapo hawakusita kuelezea hisia zao kutokana na mtaalam huyo  alivyowakonga nyoyo kwa kuelezea historia kuhusa kutokea kwa kreta ya Ngorongoro, milpuko ya volkano, maumbile ya dunia, chanzo cha binadamu wa kale na masuala mengine.


Kamati ya Bunge imeielekeza wizara ya Maliasili na Utalii kuitumia makumbusho hiyo kama bidhaa ya utalii na kitovu cha elimu kwa vijana wa kitanzania na kimataifa.


Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt.Ashatu Kijaji aliwashukuru wabunge kwa pongezi hizo na kuwahakikishia kuwa wizara yake itasimamia kwa karibu maendeleo ya Urithi Geopark Museum.


Dkt.Agnes Gidna, mtaalam wa makumbusho, mambo kale na urithi wa utamaduni amekuwa kiungo muhimu  katika makumbusho hayo kutokana na umahiri wake wa kitaaluma na kitaalam kuihadithia yaliyopo kwenye makumbusho hiyo.

MIRADI SEKTA YA MAFUTA NA GESI ASILIA IKAMILIKE KWA WAKATI-DKT.MATARAGIO

March 14, 2026 Add Comment


📌*Asisitiza kuhusu uwekezaji wa vitalu vipya vya Mafuta na Gesi Asilia*


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio, ameitaka Menejimenti ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuhakikisha kuwa miradi ya mafuta na gesi asilia inayoendelea nchini inatekelezwa na kukamilika kwa wakati ili iweze kuendelea kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Dkt. Mataragio ametoa maelekezo hayo leo wakati alipokutana na menejimenti ya TPDC  kwa lengo la kujadili fursa zilizopo katika sekta ya Mafuta  na Gesi Asilia, changamoto pamoja na kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha sekta.

Aidha, Dkt. Mataragio ameiagiza TPDC, kuongeza vitalu vipya vya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia.


“Ni muhimu TPDC ikaendelea kupanua maeneo ya uwekezaji ili kuvutia wawekezaji zaidi katika shughuli za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia kama mnavyofahamu rasilimali hii ni muhimu katika kutoa uhakika wa nishati nchini mfano kwenye  uzalishaji wa umeme na kukuza uchumi wa viwanda." Amesisitiza Dkt.Mataragio


Kwa upande wake, Kamishna wa Petroli, Goodluck Shirima, amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia ili kuongeza matumizi yake katika sekta mbalimbali ikiwemo majumbani, viwandani na katika uzalishaji wa umeme.



Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kutenga na kuandaa maeneo kwa ajili ya ushiriki wa sekta binafsi kwenye miradi ya usambazaji wa gesi, akibainisha kuwa miradi hiyo ni miongoni mwa miradi mikubwa ya kimkakati (flagship projects) inayolenga kuongeza matumizi ya gesi asilia.


Naye,  Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Mussa Makame amesema Shirika hilo litaendelea kutekeleza maagizo  yanayotolewa na viongozi wa Wizara kwa lengo la kuzidi kuiimarisha sekta ya Mafuta na Gesi Asilia.


“TPDC itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara ya Nishati ili kuhakikisha miradi ya gesi asilia na mafuta inatekelezwa kwa ufanisi na kwa manufaa ya Watanzania wote."  Amesema Makame


Ziara ya Dkt. Mataragio TPDC ni muendelezo wa ziara zake katika Taasisi zinazosimamia Sekta ya Mafuta na Gesi Asilia ikiwa ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Nishati kuimarisha usimamizi wa taasisi zake ili ziendelee kutekeleza majukumu kwa ufanisi lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wananufaika  na rasilimali zilizopo nchini.