HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

FCC YAONGEZA UHAMASISHAJI KUELEKEA SIKU YA UDHIBITI WA BIDHAA BANDIA

FCC YAONGEZA UHAMASISHAJI KUELEKEA SIKU YA UDHIBITI WA BIDHAA BANDIA

June 24, 2026 Add Comment

Tume ya Ushindani Tanzania (FCC) imeendelea kuimarisha kampeni ya utoaji elimu kwa umma kuhusu madhara ya biashara ya bidhaa bandia, ikisisitiza kuwa utengenezaji, usambazaji na uuzaji wa bidhaa hizo ni kosa la jinai linaloadhibiwa kwa mujibu wa sheria za nchi.

Akizungumza leo Juni 22, 2026, katika eneo la Kariakoo Jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa FCC, Bi. Roberta Feruzi, amesema bidhaa bandia zina athari kubwa kwa uchumi, afya na usalama wa wananchi, huku zikidhoofisha ushindani wa haki katika biashara.

Amesema watu watakaobainika kujihusisha na biashara ya bidhaa bandia wanaweza kukabiliwa na adhabu ya kifungo cha kati ya miaka minne hadi 15 jela pamoja na faini inayofikia kati ya Shilingi milioni 10 na milioni 50, kulingana na masharti ya sheria husika.

Bi. Feruzi ameeleza kuwa FCC inaendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali za ndani na kimataifa katika kudhibiti bidhaa bandia ili kuhakikisha haziingii nchini, hazisambazwi katika soko la ndani, wala kutumiwa kama njia ya kupitishwa kwenda mataifa mengine kupitia mifumo ya usafirishaji.

Amebainisha kuwa nafasi ya Tanzania kama lango muhimu la biashara na usafirishaji katika ukanda wa Afrika Mashariki inaifanya nchi kuwa miongoni mwa maeneo yanayoweza kutumiwa na wahalifu kusafirisha bidhaa bandia, hali inayohitaji ushirikiano wa karibu kati ya serikali, sekta binafsi na wananchi katika kupambana na tatizo hilo.

Kwa mujibu wa Bi. Feruzi, biashara ya bidhaa bandia si changamoto ya Tanzania pekee, bali ni tatizo la kimataifa linalosababishwa na watu wasio waaminifu wanaotafuta faida kwa kutumia kazi, ubunifu na alama za biashara za wengine kinyume cha sheria.

Ametoa wito kwa wananchi na wafanyabiashara kuwa makini wanaponunua au kuuza bidhaa, huku akiwahimiza kutoa taarifa kwa mamlaka husika wanapobaini uwepo wa bidhaa zinazohisiwa kuwa bandia.

Vilevile, amesema Tanzania itaadhimisha Siku ya Kitaifa ya Udhibiti wa Bidhaa Bandia Juni 25, 2026, yakiwa na  kauli mbiu isemayo: "Linda Maisha na Masoko Dhidi ya Pombe, Vilainishi na Sigara Bandia" ambapo maadhimisho hayo yatatumika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu athari za bidhaa bandia na kuimarisha juhudi za kitaifa na kimataifa za kupambana na biashara hiyo haramu.

Amesisitiza kuwa mafanikio ya vita dhidi ya bidhaa bandia yanategemea ushirikiano wa wadau wote, ikiwemo Serikali, wafanyabiashara , wazalishaji na wananchi, ili kulinda uchumi wa taifa, afya za watumiaji na mazingira ya biashara yenye ushindani wa haki.

TAEC YATOA ELIMU YA MATUMIZI SALAMA YA MIONZI KWA WANANCHI

June 23, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu - Dodoma


Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imehitimisha kwa mafanikio ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyofanyika katika Viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, ambapo ilitoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi salama ya mionzi na mchango wa teknolojia ya nyuklia katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

Katika kipindi chote cha maonesho hayo, banda la TAEC lilitembelewa na wananchi, wanafunzi, wataalamu na wadau mbalimbali waliopata fursa ya kujifunza kuhusu majukumu ya Tume katika kusimamia matumizi ya mionzi nchini pamoja na kuhakikisha teknolojia ya nyuklia inatumika kwa kuzingatia viwango vya usalama vinavyolinda afya za binadamu na mazingira.

Wataalamu wa TAEC walitoa elimu kuhusu usimamizi na udhibiti wa matumizi ya vyanzo vya mionzi, utoaji wa vibali kwa watumiaji wa teknolojia hiyo pamoja na ukaguzi wa mara kwa mara unaofanyika katika taasisi na maeneo mbalimbali yanayotumia vifaa vya mionzi ili kuhakikisha usalama unaendelea kuzingatiwa wakati wote.

Aidha, wananchi walipata uelewa kuhusu matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, viwanda, migodi, maji na utafiti wa kisayansi. Elimu hiyo ilibainisha mchango mkubwa wa teknolojia hiyo katika kuboresha huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa, kuongeza uzalishaji katika sekta za uzalishaji na kusaidia matumizi endelevu ya rasilimali za taifa.

Vilevile, TAEC ilitoa ufafanuzi kuhusu nafasi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati ya umeme, ikieleza namna teknolojia hiyo inavyoweza kuchangia upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa ajili ya kuendeleza shughuli za viwanda, biashara na ukuaji wa uchumi wa taifa.

Katika sekta ya afya, wananchi walielimishwa kuhusu matumizi ya mionzi katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali, huku katika sekta ya chakula wakipata maelezo kuhusu matumizi ya teknolojia ya mionzi katika uhifadhi wa mazao na bidhaa za chakula kwa kuzuia uharibifu unaosababishwa na wadudu na vimelea, hivyo kuongeza muda wa matumizi na kupunguza upotevu wa mazao baada ya kuvunwa.

Mbali na kupata elimu, washiriki wa maonesho hayo walipata fursa ya kuuliza maswali na kufanya majadiliano ya moja kwa moja na wataalamu wa TAEC kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu usalama wa mionzi, hatua za tahadhari zinazopaswa kuzingatiwa pamoja na mchango wa Tume katika kulinda jamii dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na matumizi yasiyo salama ya mionzi.

TAEC imeeleza kuwa ushiriki wake katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma umeendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi, kutoa taarifa sahihi kuhusu huduma zake na kuongeza uelewa wa umma kuhusu matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyohitimishwa leo yameendelea kutoa fursa kwa taasisi za umma kuwasilisha huduma zao kwa wananchi, kuimarisha uwajibikaji, kujenga imani ya umma na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu mchango wa taasisi hizo katika maendeleo ya Tanzania.











SAUTI ZA VIJANA ZAPELEKEWA MEZANI

June 23, 2026 Add Comment

 

Wataalamu wa afya, watafiti, viongozi wa vijana na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani na nje ya Afrika wamekutana jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha huduma na sera za afya kwa vijana balehe barani Afrika.

Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na Mtandao wa ARISE kupitia Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Afya ya Umma, Dkt. Mary Mwanyika Sando, Juni 22, 2026, inaeleza kuwa Mkutano wa 2026 wa Afya ya Vijana Balehe Kusini mwa Jangwa la Sahara (CAH-SSA) pamoja na Mikutano ya Mwaka ya Mtandao wa Utafiti, Sayansi ya Utekelezaji na Elimu Afrika (ARISE), unafanyika kuanzia Juni 22 hadi 25, 2026 Jijini Dar es Salaam.


Mkutano huo unafanyika chini ya kaulimbiu “Kuonesha Mafanikio ya Afua Endelevu za Afya ya Vijana Balehe Zinazoongozwa na Jamii”, ukiwa na lengo la kuonesha matokeo ya tafiti na kujadili mbinu bora za kuboresha afya ya vijana.

Mgeni rasmi katika mkutano huo ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Tanzania, Dkt. Seif Abdallah Shekalaghe, ambaye amezungumzia namna matokeo ya tafiti yanavyoweza kutumika kuboresha sera za afya, kuimarisha huduma kwa vijana na kuongeza ushiriki wa vijana katika ubunifu na utekelezaji wa afua zinazowahusu.

Mkutano huo umewakutanisha wadau mbalimbali wakiwemo Serikali, washirika wa maendeleo, viongozi wa vijana, watafiti, taasisi za utafiti na sekta binafsi kwa lengo la kujenga ushirikiano wa kuongeza matokeo chanya katika afya ya vijana barani Afrika.

Katika mkutano huo, vijana pia wamepewa nafasi kupitia Wawakilishi wa Bodi ya Ushauri ya Vijana Balehe na Vijana kwa ujumla (AYAB), akiwemo Mtanzania Bi. Mariam Surve na Bi. Mariam Yusuff kutoka Nigeria, ambao wanawakilisha sauti na mahitaji ya vijana katika uundaji na utekelezaji wa programu za afya.

Miongoni mwa maeneo yatakayojadiliwa ni matokeo ya miradi ya DASH na ARISE-NUTRINT inayolenga kuboresha afya ya vijana katika maeneo ya lishe, mazoezi, afya ya uzazi na afya ya akili. Miradi hiyo imefadhiliwa na Serikali ya Ujerumani pamoja na Umoja wa Ulaya.

Aidha, mkutano huo unalenga kuimarisha mipango ya Mtandao wa ARISE kwa kipindi cha mwaka 2026–2027 kwa kuweka mikakati itakayowezesha afua za afya kwa vijana kuwa endelevu kifedha na kutekelezwa kwa upana katika ngazi za jamii, kitaifa na kikanda.

Wakizungumza kuhusu umuhimu wa mkutano huo, viongozi wa ARISE wamesema jukwaa hilo ni muhimu katika kuunganisha tafiti, matokeo yake, sera na utekelezaji wa programu zinazolenga kuboresha maisha ya vijana barani Afrika.

Mtandao wa ARISE ni ushirikiano wa taasisi za Afrika na mabara mengine unaolenga kuimarisha uwezo wa utafiti wa afya ya umma na kuendeleza utekelezaji wa afua zenye msingi wa ushahidi, ukiwa na zaidi ya taasisi 22 kutoka nchi mbalimbali Kusini mwa Jangwa la Sahara.








RC MTANDA: ONGEZENI MAPATO, FUTENI HOJA ZA CAG

June 23, 2026 Add Comment



Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda ameutaka Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema kuongeza juhudi katika ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kuimarisha utoaji wa huduma na kuhakikisha halmashauri inapata uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Mhe. Mtanda ametoa kauli hiyo wakati akizungumza katika Mkutano wa Baraza Maalumu la kujadili hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), amesisitiza kuwa mapato ndiyo msingi wa uendeshaji wa halmashauri na huwezesha watumishi na madiwani kupata stahiki zao kwa wakati.

Aidha, ameutaka Uongozi wa Halmashauri kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo ili kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana na wananchi wanapata manufaa yaliyokusudiwa kupitia miradi inayotekelezwa katika maeneo yao.

Kuhusu maagizo ya Kamati za Bunge, RC Mtanda amesema Halmashauri inapaswa kuandaa taarifa za kina kuhusu utekelezaji wa maelekezo hayo badala ya kutoa taarifa za jumla zisizoonyesha hatua zilizofikiwa. Ameongeza kuwa atawaita viongozi husika ili wajieleze kuhusu utekelezaji wa maagizo yote yaliyotolewa.

Pia amesisitiza kuwa hoja zote za ukaguzi zilizobaki zinapaswa kujibiwa na kufutwa kwa wakati, akieleza kuwa uwepo wa hoja ambazo hazijafungwa unaathiri taswira ya halmashauri na utendaji wake.

Sambamba na hilo, Mkuu huyo wa Mkoa ametaka madeni yote yanayodaiwa na halmashauri yakusanywe na kulipwa kwa wakati, akibainisha kuwa ukusanyaji wa madeni utachangia kuongeza uwezo wa kifedha na kuwezesha utekelezaji wa miradi zaidi ya maendeleo.

Vilevile, amewahimiza Viongozi kuhamasisha wananchi kujiunga katika vikundi mbalimbali vya kiuchumi ili waweze kukidhi vigezo vya kupata mikopo kutoka halmashauri na taasisi za fedha, hatua itakayosaidia kuongeza shughuli za uzalishaji na kuinua uchumi wa wananchi.

Akihitimisha RC Mtanda pia amewapongeza Wahe. Madiwani wa halmashauri hiyo na kuwataka kuendelea kuhamasisha wananchi kudumisha amani na utulivu, akisisitiza kuwa maendeleo ya kweli hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mazingira ya amani na mshikamano katika jamii.





 

RC MTANDA AKABIDHI PIKIPIKI 18 KWA VIKUNDI 2 VYA VIJANA BUCHOSA

June 23, 2026 Add Comment



Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. Said Mtanda leo tarehe 23 Juni, 2026 amekabidhi pikipiki 18 zenye thamani ya Tshs. Milioni 54.9 vya vikundi viwili vya vijana vya Bodaboda Lugasa na Waungwana Group Mbugani.


Akiongea kwenye hafla ya makabidhiano hayo Mhe. Mtanda ameipongeza halmashauri hiyo kwa kuendelea kufanya vizuri kwenye eneo la matumizi ya fedha za mapato ya ndani kwa maendeleo ya wananchi.

Halmashauri ya Buchosa inafanya vizuri sana , kwanza kwenye kukusanya mapato na pili kwenye kutumia kwa ajili ya maendeleo ya wananchi kwa kutumia mapato yao kununua vyombo kama pikipiki na kukopesha kwa vijana. Amesema Mkuu wa Mkoa.

Aidha, ametoa wito kwa halmashauri hiyo kusimamia urejeshaji wa mikopo hiyo ili itumike kununua zingine na kuwezesha makundi mengine yaweze kukopeshwa.

Aidha, amewataka vijana walionufailka na mkopo huo kuheshimu sheria za usalama barabarani kwa kuendesha kwa staha kwa usalama wao na wa watumia barabara wengine aidha kuzitumia pia kwa malengo mahsusi na sio kuzizidishia matumizi.

"Hii siyo sadaka huu ni mkopo na dawa ya deni ni kulipa, wasiolrejsha mkopo wakamatwe wapelekwe polisi hadi walipe ili ikawasaidie wengine kuweza kukopeshwa" Ameongeza Mkuu wa Mkoa.





 

WIZARA YA NISHATI YASISITIZA USHIRIKIANO KUFIKIA ASILIMIA 80 YA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA IFIKAPO 2034

June 23, 2026 Add Comment










Wizara ya Nishati imesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kufanikisha lengo la Taifa la kufikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Wito huo umetolewa na Mjiolojia Mkuu wa Wizara ya Nishati, Bw. Ngereja Mgejwa, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, wakati akifungua Maonesho na Kongamano la Nishati Safi ya Kupikia 2026 (Clean Cooking Expo 2026), Juni 23, 2026 katika Ukumbi wa EACLC jijini Dar es salaam.

Akizungumza katika kongamano hilo, Bw. Mgejwa amesema nishati safi ya kupikia ni ajenda muhimu ya kitaifa inayohitaji ushirikiano wa wadau wote ili kuleta mabadiliko ya kudumu katika sekta ya nishati. Amesema matumizi ya nishati safi yana mchango mkubwa katika kulinda afya za wananchi, hususan wanawake na watoto, kuhifadhi mazingira, kuinua elimu kwa watoto wa kike na kuongeza tija ya kiuchumi.

Ameeleza kuwa kazi iliyopo mbele ni kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi ya kupikia iliyo nafuu, salama na endelevu ikiwemo gesi oevu (LPG), majiko banifu, gesi asilia, umeme, bayogesi na bayoethanoli.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya nishati safi pamoja na kutoa elimu kwa umma ili kubadili matumizi ya nishati za jadi kwenda kwenye nishati safi.

Bw. Mgejwa amepongeza Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TABWA) kwa kuandaa kongamano hilo, akisema majadiliano yatakayofanyika yataibua suluhisho na mapendekezo yatakayochochea ongezeko la matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Ameongeza kuwa kongamano hilo litahitimishwa kwa Mbio za Nishati Safi ya Kupikia zitakazotumika kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi kwa afya na uhifadhi wa mazingira.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa ya Wafanyabiashara Wanawake Tanzania(TABWA) Bi. Noreen Mawalla amesema maonesho hayo yameandaliwa chini ya kaulimbiu ya "Linda Afya, Hifadhi Mazingira, Okoa Muda kwa Uchumi Endelevu" kwa lengo la kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuunga mkono utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia.

Amebainisha kuwa Clean Cooking Expo 2026 itafanyika kwa siku tatu na itajumuisha mafunzo, mijadala na maonesho ya teknolojia mbalimbali za nishati safi zitakazowakutanisha wadau kutoka sekta ya umma na binafsi.

Amewakaribisha wananchi kutembelea mabanda ya maonesho ili kupata elimu na taarifa sahihi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia, huku akieleza kuwa Mbio za Nishati Safi ya Kupikia zitafanyika Jumamosi na zinatarajiwa kuongozwa na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi.