
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI

NA MWANDISHI WETU, DODOMA
Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, ameelezwa kuwa kiongozi mahiri, muadilifu na mzalendo, mwenye uwezo wa kumsaidia majukumu Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.
Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake wa Chama Cha Mapinduzi (UWT) Taifa, Mary Chatanda, Agosti 30, 2026, ofisini kwake Dodoma, siku moja baada ya kukamilika uapisho wa kiongozi huyo, Ikulu ya Chamwino, Dodoma.
Chatanda ameeleza, Ndejembi ni kiongozi wa vitendo na katika majukumu aliyoaminiwa tangu akiwa Mkuu wa wilaya ya Kongwa, Mbunge, Naibu Waziri na Waziri kamili katika wizara mbalimbali.
"Kule Kongwa Dodoma akiwa Mkuu wa wilaya alifanya kazi nzuri na katika kilimo alisimamia kwa mafanikio makubwa kampeni yake aliyoiita ONJAKO yaani Ondoa Njaa Kongwa. Alihimiza wananchi kulima mazao yanayostahimili ukame kama mtama, mihogo, ufuta na alizeti ili kuwaepusha wananchi na kadhia ya njaa," amesema Chatanda.
Ameongeza kuwa, kampeni ya ONJAKO ilipokelewa vizuri na wakulima wa Kongwa kutokana na mwanzo kutilia mkazo zao la mahindi ambalo mara kwa mara walikuwa wakipata mazao kidogo kutokana na changamoto ya ukame wilayani humo.
Akisisitiza utendaji uliotukuka wa Ndejembi, Chatanda amesema, Wizara kadhaa alizohudumu zikiwemo Tamisemi, Vijana, Ardhi, Nishati, ameacha alama kubwa kwa kuwa mstari wa mbele kutatua changamoto za wananchi.
"Ndejembi si mtu wa kukaa ofisini kusubiri taarifa, anakwenda mwenyewe kujionea utekelezaji wa majukumu na maagizo mbalimbali. Ndiyo maana nasema, Rais Dk. Samia amepata msaidizi mchapakazi na hodari kwelikweli," ameongeza.
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo wa UWT Taifa, ametoa rai kwa wananchi kumuombea Rais Dk. Samia, Makamu wa Rais, Ndejembi na viongozi wengine ili waweze kusimamia mipango iliyopo ambayo imejikita katika kukuza ustawi na maendeleo ya wananchi.
Awali, katika uapisho huo, Rais Dk. Samia amemuasa Makamu wa Rais Mteule kuwatumikia Watanzania bila kujali tofauti zao ili kufanikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025-2030 na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo (2050).
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)

.jpeg)














Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) uko kwenye mchakato wa kufanya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Sura ya 395, kwa lengo la kupanua wigo wa wanachama, kuendana na mahitaji ya sasa ya huduma za afya na kuimarisha uendelevu wa Mfuko.
Marekebisho hayo pia yanalenga kuimarisha udhibiti wa matumizi mabaya ya Mfuko, ikiwemo udanganyifu unaoweza kufanywa na baadhi ya wanachama, waajiri na watoa huduma za afya lakini kwenda sambamba na sheria Mama ya Bima ya Afya kwa Wote.
Akizungumza katika ukumbi wa mikutano wa NHIF, Kinondoni, Dar es Salaam, wakati wa kupokea maoni ya wadau kuhusu mapendekezo ya marekebisho ya sheria hiyo, Meneja wa Huduma za Sheria wa NHIF, Matamus Fungo, amesema sheria hiyo iliyotungwa mwaka 1999 inahitaji maboresho ili iendane na mabadiliko yaliyopo katika sekta ya afya na mwelekeo wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote.
“Tunataka sheria yetu iweze kuboreshwa ili iwezeshe watu wengi zaidi kujiunga na pia kuziba mianya ya matumizi mabaya ya kadi yanayofanywa na baadhi ya wanachama wasio waaminifu” amesema.
Amesema marekebisho hayo yanatarajiwa kuongeza idadi ya wanachama, kuimarisha uendelevu wa Mfuko na kuweka mifumo madhubuti zaidi ya kudhibiti udanganyifu na matumizi yasiyofaa ya huduma za bima ya afya.
Kuzingatia Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote
Kwa upande wake, Wakili wa Serikali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Mwenda Tulalemwa, amesema marekebisho ya sheria yanapaswa kuzingatia mahitaji ya makundi mbalimbali ya wananchi pamoja na kuendana na Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, ili kuhakikisha hakuna mgongano wa kisheria.
Amesema wadau waliotoa maoni wamependekeza maboresho katika maeneo mbalimbali, ikiwemo mfumo wa malipo kwa vituo vya kutolea huduma za afya, huduma kwa watu wasio na uwezo na watu wenye ulemavu.
Aidha, miongoni mwa mapendekezo yaliyotolewa ni kuongeza umri wa watoto wanaotambuliwa kama wategemezi kutoka miaka 21 hadi 25, hatua inayolenga kuendana na mahitaji ya familia na mazingira ya sasa.
Naye Wakili wa Mahakama Kuu na mwanachama wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Ferdinand Makole, amesema marekebisho ya sheria yanaweza kuwa fursa muhimu ya kuongeza urahisi, ufanisi na ubora wa huduma zinazotolewa na NHIF.
Amesema sheria inapaswa kuweka mazingira yatakayowezesha Mfuko kutoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wanachama na wananchi kwa ujumla, huku ikizingatia uendelevu wa Mfuko.
Kwa upande wake, Mwanasheria wa Bohari ya Dawa (MSD), Brighton Mtigani, amesema ushirikishwaji wa wananchi na wadau mbalimbali ni muhimu katika kuhakikisha sheria inayoandaliwa inaendana na mahitaji yanayobadilika ya jamii.
Amesema ushirikishwaji huo utasaidia kujenga mfumo unaozingatia usawa katika upatikanaji wa huduma za afya na kuhakikisha makundi mbalimbali yanapata huduma bila vikwazo visivyokuwa vya lazima.
Maoni ya wadau kuchangia maboresho ya rasimu
Naye Ofisa Sheria Mwandamizi kutoka Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Japhes Daudi, amesema maoni yaliyotolewa na wadau yamechukuliwa na yataendelea kutumika katika kuboresha rasimu ya mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.
Kwa ujumla, mchakato huo unalenga kuhakikisha Sheria ya NHIF inaendana na mazingira ya sasa ya utoaji wa huduma za afya na mwelekeo wa Serikali wa kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya kupitia mfumo wa Bima ya Afya kwa Wote.
Marekebisho hayo yanatarajiwa kupanua wigo wa wananchi wanaoweza kunufaika na bima ya afya, kuimarisha udhibiti wa matumizi ya Mfuko, kuboresha huduma kwa wanachama na kuimarisha uendelevu wa NHIF, sambamba na kuchangia utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote nchini.



*Bima ya Afya kwa Wote, Jiunge sasa*
WALIMU 328 kutoka shule 10 za Sekondari katika Jiji la Tanga wanapigwa msasa kupitia semina maalumu inayolenga kuwaongezea ujuzi na mbinu za ufundishaji, hatua inayolenga kuongeza ufaulu wa wanafunzi wa Kidato cha Pili na Nne.