HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

MMOMONYOKO WA MAADILI KWA JAMII KWAWAIBUKA TAASISI YA SUBRA NA NUSRA KUJA NA KONGAMANO MAALUMU

January 31, 2026 Add Comment

 


Kutokana na kuporomoka  mmomonyoko wa maadili katika jamii, wanawake wa Kiislamu mkoani Tanga wameanzisha majadiliano na mikakati maalum ya kutafuta suluhisho la changamoto hiyo, sambamba na maandalizi ya kuupokea mwezi mtukufu wa Ramadhani.


Kupitia Taasisi ya Subra na Nusra, wanawake hao wameandaa kongamano maalum litakalofanyika Jumamosi hii katika Ukumbi wa Simba Mtoto, jijini Tanga, likilenga kuwaandaa wanawake kiroho na kijamii ili kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia mafundisho ya Mtume Muhammad (SAW).


Mratibu wa kongamano hilo, Bi Mwanakombo Abdallah Kipanga, alisema lengo kuu ni kutoa elimu kwa jamii, hususan wanawake, kuhusu umuhimu wa maadili mema na maandalizi sahihi ya mwezi wa Ramadhani.



“Huu si mwezi wa kawaida. Tunataka wanawake wapate elimu itakayowasaidia kuimarisha imani, malezi ya watoto na maadili ndani ya familia na jamii kwa ujumla,” alisema.




Alisema Mufti Abubakar Bin Zuberi anatarajiwa kuwa mgeni wa heshima, huku Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk Batilda Burian, akiwa mgeni rasmi. Hili litakuwa kongamano la nne kufanyika chini ya taasisi hiyo.


Bi Kipanga aliongeza kuwa jitihada hizo zimeungwa mkono pia na wanawake wenye asili ya Tanga wanaoishi Dar es Salaam, walioungana kuimarisha maandalizi ya kongamano hilo.




Miongoni mwa mada zitakazojadiliwa ni maandalizi ya wanawake katika mwezi wa Ramadhani, kujenga hofu ya Mungu, malezi bora ya watoto pamoja na umuhimu wa kuzingatia maadili mema katika maisha ya kila siku.


Aliwataka wanawake wa Kiislamu pamoja na wa dini nyingine kujitokeza kwa wingi kushiriki kongamano hilo.
Naye mjumbe wa kamati ya maandalizi, Bi Shamsi Diwani kutoka Dar es Salaam, alisema kuna haja ya dharura kwa wanawake kuungana kupambana na kuporomoka kwa maadili kunakojitokeza katika jamii.


“Ni wakati wa kusaidiana kurejesha maadili mema. Inasikitisha kuona mienendo isiyofaa na burudani zinazokiuka maadili zikizidi kushika kasi katika jamii,” alisema.


Aliongeza kuwa wako tayari kukaa pamoja na wanawake na kujadili kwa kina chanzo cha changamoto hiyo ili kupata suluhisho la kudumu.


Bi Diwani pia alielezea wasiwasi wake juu ya kuongezeka kwa migogoro ya ndoa na kuvunjika kwa familia, akisema si jambo jema kushuhudia baadhi ya wanawake wakisherehekea talaka.
“Hili si jambo la kufurahia. Ingawa talaka inaruhusiwa, si tukio la kushangiliwa,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Bi Kibibi Saidi Kibao aliwahimiza wanawake kuhudhuria ili kunufaika na mafunzo yatakayotolewa na Mashehe maarufu pamoja na mke wa Mufti wa Kwanza, Sheikh Jumaa.
Naye mjumbe mwingine wa kamati, Bi Hawa Mweri, alisisitiza umuhimu wa wanawake wa Kiislamu kudumisha maadili mema wakati wote, si kipindi cha Ramadhani pekee.
MWISHO

UDSM: WANAFUNZI WA UANDISHI WA HABARI WAKUMBUSHWA UMUHIMU WA ITHIBATI NA SHERIA

January 30, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amewahimiza wanafunzi wa uandishi wa habari kusoma, kuielewa na kuizingatia Sheria ya Huduma za Habari ili kujijenga kitaaluma na kuepuka migongano ya kisheria wanapoingia kwenye tasnia ya habari.

Wakili Kipangula ametoa wito huo wakati akitoa mhadhara kwa wanafunzi wa Mwaka wa Pili wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Shule Kuu ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano kwa Umma, uliofanyika Januari 30, 2026, chuoni hapo. Mhadhara huo ulilenga kuwaongezea uelewa wanafunzi kuhusu majukumu ya JAB na misingi ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229.

Katika wasilisho lake, Wakili Kipangula ameeleza kuwa JAB ina jukumu la kusimamia ithibati ya waandishi wa habari nchini, kulinda taaluma ya uandishi wa habari na kuhakikisha maadili na weledi vinazingatiwa. Amesisitiza kuwa wanafunzi na waandishi chipukizi wanapaswa kuifahamu Sheria ya Huduma za Habari kabla ya kuanza kazi rasmi ili kujiepusha na makosa yanayoweza kuathiri taaluma yao.

Ameeleza pia kuwa ithibati na vitambulisho vya uandishi wa habari ni muhimu kwa wanafunzi wanapokuwa kwenye mafunzo kwa vitendo (field), akisisitiza kuwa uwepo wa nyaraka hizo unatoa uhalali wa kisheria katika utekelezaji wa majukumu ya kihabari, hususan wanapokuwa wakikusanya habari katika maeneo mbalimbali.
Akijibu swali kutoka kwa wanafunzi kuhusu mafunzo katika vyombo vya habari vya vyuo, ikiwemo Mlimani Radio na Televisheni pamoja na SAUT, Wakili Kipangula amesema Sheria inatambua uwepo wa wanafunzi katika vituo hivyo kwa kipindi maalumu cha mafunzo. Amesema baada ya kukamilisha muda wa mafunzo kwa vitendo, wanafunzi wanapaswa kurejea katika ratiba yao ya kawaida ya masomo chuoni.

Mhadhara huo umeelezwa kuwa sehemu ya juhudi za JAB katika kujenga uelewa wa kisheria kwa waandishi wa habari chipukizi, hatua inayolenga kuimarisha weledi, uwajibikaji na heshima ya taaluma ya uandishi wa habari nchini.

MATI FOUNDATION YAREJESHA FAIDA KWA JAMII, KAYA 2,000 KUNUFAIKA MANYARA

January 30, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Manyara

Zaidi ya kaya 2,000 zenye uhitaji maalum mkoani Manyara zinatarajiwa kunufaika na msaada wa vyakula unaotolewa na Mati Foundation, ikiwa ni sehemu ya mpango wa kampuni ya Mati Super Brands Ltd wa kurejesha sehemu ya faida yake kwa jamii inayozunguka maeneo ya uzalishaji na biashara zake.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada wa awamu ya kwanza kwa kaya 37 katika Kata ya Bagara, Wilaya ya Babati, Meneja wa Mradi wa Mati Foundation, Isack Piganio, amesema mpango huo unalenga kusaidia makundi yaliyo katika mazingira magumu, yakiwemo kaya zenye mahitaji maalum, ili kupunguza changamoto za maisha wanazokabiliana nazo kila siku.
Piganio ameeleza kuwa msaada huo wa vyakula ni sehemu ya dhamira ya taasisi hiyo kushiriki kikamilifu katika juhudi za kijamii kwa kushirikiana na Serikali na wadau wengine wa maendeleo, huku akisisitiza kuwa lengo la sasa ni kuongeza wigo wa msaada huo ili kuwafikia walengwa wengi zaidi.

“Lengo letu ni kuhakikisha kaya nyingi zaidi zenye uhitaji zinanufaika. Tunatarajia kufikia takriban kaya 2,000 ifikapo mwisho wa mradi huu wa msaada wa vyakula,” amesema Piganio.

Baadhi ya wanufaika wa msaada huo wameeleza kufurahishwa na hatua hiyo, wakipongeza juhudi zinazofanywa na Mati Super Brands Ltd kupitia taasisi yake ya Mati Foundation kwa kuwakumbuka wananchi wenye uhitaji, hususan wale wanaoishi katika maeneo yanayozunguka kiwanda hicho.

Wanufaika hao wamesema msaada wa vyakula walioupokea utawapunguzia kwa kiasi kikubwa changamoto za kimaisha, hasa katika kipindi cha ugumu wa upatikanaji wa mahitaji ya msingi, na wameishukuru kampuni hiyo kwa moyo wa kujali na kugusa maisha ya wananchi wa kawaida.
Viongozi mbalimbali wa Serikali waliokuwa mashuhuda wa zoezi hilo wameipongeza Mati Foundation kwa moyo wa kujitolea na ushirikiano wake na Serikali katika kutatua changamoto za kijamii, wakisema mchango huo ni mfano mzuri wa sekta binafsi kushiriki katika maendeleo ya jamii.

Viongozi hao wamesisitiza kuwa ushirikiano wa aina hiyo unasaidia kuimarisha ustawi wa jamii na kupunguza mzigo kwa Serikali katika kuwahudumia wananchi wenye uhitaji.
Mati Foundation ni taasisi isiyo ya kiserikali iliyo chini ya kampuni mama Mati Super Brands Ltd, inayojihusisha na uzalishaji na usambazaji wa vinywaji changamshi mbalimbali nchini. Miongoni mwa bidhaa zinazozalishwa na kampuni hiyo ni pamoja na Strong Dry Gin, Sed Pineapple Flavoured Gin, Strong Coffee, Tai Original Portable Spirit, Tanzanite Premium Vodka na Tanzanite Royal Gin.

Kupitia Mati Foundation, kampuni hiyo imeendelea kutekeleza programu mbalimbali za kijamii zenye lengo la kuinua ustawi wa jamii na kuchangia maendeleo endelevu katika maeneo inayofanyia shughuli zake.

NGORONGORO SAKO KWA BAKO NA TAASISI ZA ELIMU KUTANGAZA VIVUTIO VYA UTALII NA ELIMU YA UHIFADHI

January 30, 2026 Add Comment


Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro leo tarehe 30 Januari, 2026 imeendelea na kampeni ya kutoa elimu ya vivutio vya utalii vilivyopo Ngorongoro na elimu ya uhifadhi endelevu kwa wanafunzi na walimu wa shule za Sekondari Manyara, Lowasa , Rift valley na Chuo cha Maendeleo ya wananchi FDC Mto wa Mbu ambapo taasisi zote zipo Wilaya ya Monduli Mkoani Arusha.




PBPA YAFUNGUA MILANGO KWA VIJANA WA UHANDISI WA MAFUTA KUTOKA UDSM NA DMI

January 30, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu- Dar es Salaam.


Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) leo tarehe 30 Januari, 2026 umepokea ugeni wa wanafunzi 30 wa Kitengo cha Petroleum Engineering kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), chini ya Chama cha wahandisi wa mafuta (Society of Petroleum Engineers -SPE),waliotembelea Wakala huo kwa lengo la kujifunza kwa vitendo kuhusu utendaji kazi wa PBPA na namna Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (BPS) unavyotekelezwa nchini.


Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Meneja wa Kitengo cha Lojistiki za Mafuta PBPA, Mhandisi Sophia Kidimwa, alisema kuwa wanafunzi hao wamepata fursa ya kuelewa mchakato mzima wa upatikanaji wa mafuta nchini kuanzia hatua za uagizaji hadi usimamizi wa lojistiki za kupokea mafuta.

“Tumepokea ugeni wa wanafunzi wa mwaka wa nne kutoka UDSM na DMI waliokuja kujifunza kuhusu taratibu zote za upatikanaji wa mafuta hapa Tanzania, jinsi mafuta yanavyoingia nchini, mchakato mzima wa uletaji wake pamoja na lojistiki za kupokea mafuta na manufaa ya Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (BPS),” alisema Sophia.

Aliongeza kuwa PBPA imekuwa ikipokea wageni kutoka taasisi mbalimbali zinazopenda kujifunza kuhusu mfumo wa BPS kutokana na mafanikio na manufaa yake kwa Taifa.

“Kama taasisi, tumekuwa tukitoa uelewa huo kwa wageni wetu na wamekuwa wakionyesha kuridhika. Tunaendelea kuwakaribisha wadau wote wanaopenda kujifunza kuhusu Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mhandisi kutoka Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA), Prudence Laurean, alisema wanafunzi hao walipitishwa katika mifumo yote ya PBPA kuanzia hatua za uagizaji wa mafuta hadi mafuta yanapofika kwenye maghala ya kuhifadhia, ikiwemo matumizi ya Mfumo wa SCADA katika ufuatiliaji wa mafuta wakati wa kushushwa kutoka melini kwenda kwenye maghala ya Serikali na binafsi.

“Mafunzo haya ni muhimu sana kwa wanafunzi kwani yanawajengea uelewa wa kina kuhusu kazi za PBPA na faida zitakazowasaidia kitaaluma hapo baadaye,” aliongeza.


Akizungumza kwa niaba ya wanafunzi, Sifrina John, mwanafunzi wa mwaka wa nne Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema ziara hiyo imelenga kuwaunganisha wanafunzi na uhalisia wa kazi katika sekta ya mafuta nchini.

“Lengo letu ni kuunganisha yale tunayojifunza darasani na mazingira halisi ya kazi katika sekta ya mafuta, na kuelewa kwa vitendo jinsi PBPA inavyofanya kazi katika uagizaji na usimamizi wa ugavi wa mafuta nchini,” alisema Sifrina.


Aliongeza kuwa wanafunzi wamefurahishwa na mafunzo waliyoyapata na namna PBPA inavyosimamia ugavi wa mafuta pamoja na mchango wake katika uchumi wa Taifa.


“Tumepata uelewa wa kina kuhusu mchakato wa uagizaji wa mafuta, usimamizi wa ugavi na mchango wa PBPA katika uchumi wa nchi. Mafunzo haya yametujenga kwa kiasi kikubwa kwa kuunganisha nadharia na vitendo,” alisisitiza.


Ziara hiyo ni mwendelezo wa juhudi za PBPA katika kuimarisha ushirikiano na wadau kutoka taasisi mbalimbali nchini sambamba na kukuza uelewa wa vijana kuhusu mifumo ya kimkakati inayosimamia sekta ya mafuta na mchango wake katika uchumi wa Taifa.

BARRICK YATOA UFADHILI KWA WANAFUNZI WATANO KUSOMA UTAALAMU WA FANI YA MADINI NJE YA NCHI

January 30, 2026 Add Comment
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) waliopata ufadhili wa kwenda kusoma nchini Afrika ya Kusini
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) , Profesa William Anangisye akizungumza na kutoa nasaha zake katika hafla ya kuwaaga wanafunzi wa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) waliopata ufadhili wa kwenda kusoma shahada ya kwanza ya Jiolojia na Madini
Meneja wa Barrick nchini , Dkt. Melkiory Ngido akizungumza na waandishi wa habari , wanafunzi waliopata udhamini kwa kwenda kusoma nchini , Afrika Kusini na wageni kwenye hafla ya kuwaaga wanafunzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam
Meneja Rasilimali watu wa Barrick nchini , Lumbu Kambula akizungumza kwenye hafla ya ufadhili wa wanafunzi watano wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) iliyofanyika jijini Dar es Salaam
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) waliopata ufadhili wa kwenda kusoma nchini Afrika ya Kusini wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Barrick na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM)

**
-Kuendelea kuwekeza katika kizazi kijacho cha wataalamu wa sekta ya madini

Kampuni ya Barrick nchini inayoendesha shughuli zake kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Twiga Minerals imetoa ufadhili kwa wanafunzi watano kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kwenda kusoma Shahada ya kwanza ya Elimu ya Madini na Jiolojia katika Chuo Kikuu cha Johannesburg Afrika ya Kusini kupitia progamu yake ya kuwezesha wasomi vijana inayotekelezwa kanda ya Afrika na Mashariki ya kati.

Akizungumza kwenye hafla ya kutangaza ufadhili huo na kuwaaga wanafunzi waliofanikiwa kupata fursa hiyo jijini Dar es Salaam , Meneja wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido amesema ufadhili huu ni ushuhuda na uthibitisho kwamba Barrick imelenga kukuza sekta ya madini kupitia uwekezaji wake sambamba na kuhakikisha sekta ya madini inatoa mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi.

“Uwajibikaji wetu hauishii kuendesha migodi yetu kwa viwango vya kimataifa bali pia tumejikita kuhakikisha tunawekeza katika kuwapatia watanzania ujuzi hususani kwa vijana ambao watakuwa wataalamu wa siku za usoni,ndio maana kupitia udhamini wa elimu kama huu kunawezesha kuwa na wataalamu wa fani ya madini na wabunifu watakaochangia kuleta maendeleo katika siku za usoni”, amesema Dkt.Ngido.

Amesema Barrick itakuwa karibu na Wanafunzi hao na pindi wakapomaliza masomo yao watapatiwa fursa ya kuwajengea uwezo wa kupata ujuzi zaidi kwa kuwapatia ajira katika migodi yake nchini.

Ameongeza kwamba dhamira ya kampuni ya Barrick ni kuendelea na ushirikiano wenye tija kwa kufanya uwekezaji endelevu wenye tija kwa Tanzania na watu wake kwa kuhakikisha kwamba katika programu hii taifa linaweza kupata wataalamu mbalimbali kwenye fani ya Uinjinia wa madini na Jiolojia hapa nchini.

Pamoja na mambo mengine amefafanua kuwa kupitia programu hiyo kampuni ya Barrick kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wataendelea na kuhakikisha wanazalisha wataalamu wapya kwenye sekta ya madini hapa nchini.

Kwa upande wake , Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Profesa William Anangisye ameshukuru kwa kampuni ya Barrick kuwapa ufadhili wanafunzi watano kutoka kwenye Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) baada ya kushindanishwa na wenzao kutoka Vyuo vikuu vingine hapa nchini.

“Tumefurahi na ufadhili huu na ni Imani yangu watakwenda kusoma kwa bidhii na hakuna atayerudishwa kwa kushindwa masomo nawataka muwe mabalozi wazuri kwa Chuo chetu na nchini kwa ujumla,” amesema Profesa Anangisye.

Amesema ufadhili wa wanafunzi hawa umekuwa baada ya mchujo wa wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali hapa nchini na hatimaye hawa wameshinda , hawa ni kati ya wanafunzi bora waliopita kwenye mchujo na kupata ufadhili kwa kwenda kusoma shahada ya kwanza kwenye madini,” .

“Ni furaha yangu kuona kwamba kati ya wanafunzi hawa waliopata ufadhili kuna wasichana hii ni moja ya sera ya pale mlimani kuweka uwiano wa jinsia kwenye masomo ili kuhakikisha watoto wa kike na wenye uwezo wanapata fursa za kusonga mbele,” amesisitiza.

Mmoja ya wanafunzi akiongea kwa niaba ya wenzake, Samson Abeid amesema programu hiyo ni fursa ya kipekee kwa wanafunzi wa kitanzania kwa kusoma kwa bidii na kuhakikisha kwamba wanatoa mchango katika maendeleo ya taifa.

“Programu hii itachochea chachu katika sekta ya elimu hapa nchini na kutoa fursa kwa wanafunzi wa kitanzania kupata elimu , maarifa na ujuzi nje ya nchini,” amesema Abeid.
Mmoja wa wanufaika akipokea nyaraka za ufadhili, katika hafla hiyo

WANANCHI MONDULI WAHAMASISHWA KUUNGA MKONO AJENDA YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

January 30, 2026 Add Comment

 


Na Mwandishi Wetu


Wizara ya Nishati imetoa wito kwa wananchi wa Wilaya ya Monduli  kuachana na matumizi ya kuni na mkaa na badala yake watumie nishati safi ya kupikia, ili  kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha ifikapo mwaka 2034, asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia kutoka Wizara ya Nishati, Nolasco Mlay kwenye ziara ya ukaguzi wa utekelezaji wa maagizo ya Ofisi ya Makamu wa Rais yanayohimiza matumizi ya nishati safi katika taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100, Wilaya ya Monduli, Mkoa wa Arusha.

Mlay amesema umefika wakati kwa wananchi kubadili mtazamo na kuachana na jitihada za kutafuta kuni au magunia ya mkaa, na badala yake kuelekeza nguvu katika matumizi ya nishati safi ambayo ni salama kwa afya na mazingira.

“Mazingira ni ajenda ya dunia nzima, na Rais wetu ni kinara wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. Hivyo ni wajibu wetu kuunga mkono dhamira yake kwa kukaa pamoja, kujadiliana na kubuni mikakati ya kuwatoa wananchi kwenye matumizi ya nishati zisizo salama na kuwapeleka kwenye matumizi ya nishati safi,” amesisitiza.

Aidha, Mlay amewapongeza viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutekeleza maagizo ya Serikali kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia katika taasisi mbalimbali.

Amesema si rahisi kwa Serikali kufahamu changamoto zilizopo katika kila eneo, hivyo mchango wa viongozi wa halmashauri ni muhimu kwani wanajitoa kwa dhati kufichua changamoto zilizopo bila hata kulipwa.


“Serikali inatambua jitihada hizi na inathamini sana taarifa za changamoto zinazowasilishwa, jambo linalowezesha kuchukuliwa kwa hatua stahiki kwa manufaa ya wananchi,” ameongeza.