Amesema tabia hiyo ya baadhi ya wafanyabiashara inachafua taswira ya nchi na kuwaweka katika mazingira magumu wafanyabiashara wengine wanaofuata taratibu na kufanya biashara kwa uaminifu.
Londo alitoa kauli hiyo jijini Tanga wakati wa kikao kazi kati ya TSB, Chama cha Wakulima wa Mkonge (SAT) na wafanyabiashara wa zao hilo.
Amesema Tanzania inaendesha uchumi wa soko huria, lakini uhuru huo haupaswi kutumiwa kama mwanya wa kufanya biashara kinyume cha sheria au kukiuka misingi ya uaminifu katika masoko ya kimataifa.

“Nimesikia hapa wafanyabiashara wakilalamika kwamba wakati mwingine wanataka kukamatwa kwa sababu kuna baadhi ya wafanyabiashara wamefanya udanganyifu kwenye soko. Mtu akifanya hivyo anashindwa kujua kwamba huku nje yeye anatambulika kama Tanzania na wala si kampuni yake,” amesema.
Amesema Serikali haiwezi kuvumilia vitendo vinavyoweza kuilazimisha nchi kutumia muda na rasilimali nyingi kurejesha uaminifu na taswira yake katika masoko ya kimataifa.
Kutokana na hali hiyo, Naibu Waziri ameiagiza TSB, kwa kushirikiana na wadau wengine wa zao hilo, kuchukua hatua mapema dhidi ya wafanyabiashara watakaobainika kufanya vitendo hivyo ili kulinda soko la mkonge na maslahi ya wafanyabiashara wanaofuata sheria.

“Pamoja na kwamba Serikali inaendelea kuweka mazingira mazuri ya kibiashara, hatuwezi kuvumilia hilo,” amesema.
TSB: WACHUKUA FEDHA, HAWAPELEKI MIZIGO
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TSB, Saddy Kambona, amesema changamoto hiyo ni miongoni mwa mambo aliyokutana nayo katika ziara zake kwenye masoko ya mkonge duniani.
Amesema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakichukua fedha kutoka kwa wanunuzi wa nje, lakini baadaye kushindwa kupeleka mizigo, hali ambayo imeanza kuchafua jina la Tanzania katika masoko hayo.

“Kwenye ziara yangu nimekutana na malalamiko kwamba kuna wafanyabiashara wamechukua fedha halafu wameshindwa kupeleka mizigo. Watu wanafanya udanganyifu kwenye masoko ya nje,” amesema Kambona.
Amesema wafanyabiashara watakaobainika kufanya vitendo hivyo wanaweza kuchukuliwa hatua, ikiwamo kufutiwa usajili au leseni zao.
Kwa mujibu wa Kambona, hatua hizo zinalenga kulinda uaminifu wa biashara ya mkonge kutoka Tanzania na kuhakikisha wafanyabiashara wanaofanya biashara kwa kufuata taratibu hawaathiriwi na vitendo vya watu wachache.

UZALISHAJI MKONGE WAPANDA
Pamoja na changamoto hiyo, Kambona amesema uzalishaji wa mkonge nchini umeendelea kuongezeka, kutoka tani 36,000 mwaka 2020 hadi kufikia tani 75,000 mwaka 2025.
Amesema mwaka 2020 wakulima wakubwa walichangia asilimia 68 ya uzalishaji wa mkonge, huku wakulima wadogo wakichangia asilimia 32.
Hata hivyo, amesema hali hiyo imebadilika kutokana na juhudi za kuwawezesha wakulima wadogo, ambapo mwaka 2025 walichangia asilimia 55 ya uzalishaji, huku wakulima wakubwa wakichangia asilimia 45.

WAFANYABIASHARA: TUNABEBESHWA DHAMBI ZA WACHACHE
Wafanyabiashara wa mkonge walioshiriki kikao hicho wamesema vitendo vya wachache vimekuwa na madhara kwa wafanyabiashara waaminifu kutoka Tanzania, ambao wakati mwingine hujikuta wakihusishwa na tuhuma au kesi zinazotokana na biashara zisizofanyika kwa uaminifu.
Gasper Daudi wa Harvest Agritech Limited amesema baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakisababisha matatizo katika masoko ya nje, hali inayowaathiri hata wale wanaofanya biashara kwa kufuata sheria.

Amesema ni muhimu Serikali na TSB kuweka mifumo madhubuti ya kuhakikisha wafanyabiashara wanaokiuka taratibu wanachukuliwa hatua mapema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Aja Tanzania Limited, Happiness Nyiti, ameomba Wizara ya Viwanda na Biashara kuweka mpango maalumu wa kurejesha uaminifu katika masoko ambayo tayari yameathiriwa na vitendo vya baadhi ya wafanyabiashara.
“Vitendo hivi vinachafua taswira ya nchi yetu. Tunaomba Naibu Waziri atusaidie kuweka mpango mzuri wa kutengeneza taswira ya nchi yetu kwenye maeneo ambayo yanaonekana waziwazi kwamba imani ya wafanyabiashara wa zao hilo kutoka Tanzania imeshuka,” amesema Nyiti.

Amesema hatua hiyo ni muhimu kwa kuwa Tanzania ina wafanyabiashara wengi wanaozingatia ubora na uaminifu, lakini juhudi zao zinaweza kuathiriwa na vitendo vya wachache.
Amesema kurejesha uaminifu katika masoko ya kimataifa kutasaidia kuongeza fursa za biashara na kuchochea zaidi uzalishaji wa mkonge nchini.