TAFITI ZINAONESHA NI MUHIMU KUWEKEZA KATIKA UFUNDI STADI KUELEKEA UCHUMI WA VIWANDA-DKT MMARI

April 06, 2018

Na Said Mwishehe,Globu ya jamii

MKURUGENZI Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti ya REPOA Dk.Donald Mmari amesema kuna sababu ya kuwekeza zaidi katika kutoa elimu ya ufundi stadi nchini kwa lengo la kupika watalaamu wa fani mbalimbali ambao watashiriki kufanya kazi zenye tija na kuleta ushindani kimataifa.

Dk.Mmari ametoa kauli hiyo wakati akielezea changamoto ambazo wamezibaini kwenye warsha ya siku mbili iliyoandaliwa na REPOA kwa lengo la kujadili masuala mbalimbali katika kipindi hiki cha kuelekea Tanzania ya Viwanda.

Amesema wadau walioko kwenye warsha hiyo wamejadili kwa kina mambo mengi kwa maslahi mapana ya nchi yetu na katika mjadala huo wamebaini bado kunachangamoto ambazo ni vema zikafanyiwa kazi ili kufikia malengo ya ujenzi wa viwanda na kuwa na bidhaa zenye ushindani katika soko la kimataifa.

Ametaja moja ya changamoto ambao wameijadili ni uhaba wa wataalam katika nyanja mbalimbali na hiyo inatokana na kutowekeza zaidi kwenye elimu ya Ufundi stadi ambayo inaandaa vijana kujiajiri na kuwa watalaamu wazuri."Tumekubaliana na kutoa mapendekezo kuwa ili tuingie kwenye ushindani ipo haja ya kuhakikisha watanzania wanaalindaliwa katika elimu na ujuzi unaohusu masuala ya ufundi.

"Ni vema Serikali kwa kushirikiana na wadau wa sekta za umma na binafsi kuwekeza zaidi katika kuwajengea uwezo wananchi ambao utawafanya washiriki kikamilifu katika kufanya kazi kwenye viwanda,"amesema Dk.Mmari.Amefafanua nchi nyingi ambazo zimeendelea na zenye uwezo wa kuhimili ushindani kwenye soko la kimataifa msingi wake mkubwa wamewekeza katika elimu, ujuzi na utalaam.

"Hivyo ili kushindana nao lazima Tanzania nayo ikawekeza katika elimu, ujuzi na utaalamu kwa kuandaaa vijana watakaokuwa na ujuzi.Tumekubaliana yale ambayo tumeyaona kama changamato tumeweka na mapendekezo yetu na tumekubaliana Serikali iyapate na ikiwezekana kuyafanyia kazi,"amesem Dk.Mmari.

Amesisitiza ni vema nchi ikawekeza zaidi kwenye kujenga vyuo vya VETA ambavyo jukumu litakuwa kuandaa watalaam na kwamba kuna wakati iliingia kasumba ya kuwa na vyuo vikuu vingi ili wanaohitimu wawe na Shahada lakini elimu hiyo haina ujuzi na matokeo yake kunaibuka changamoto ya uhaba wa watalaamu.

Kwa upande wa Mlkuregenzi Mtendaji wa Tanzania Horticultural  Association (TAHA)  Jacqueline Mkindi amesema pamoja na kujadili mambo mengi kwenye warsha hiyo wamegundua ujuzi kwenye maeneo ya viwandani bado tatizo kubwa.Amesema ipo haja ya kuhakikisha wanaandaliwa watalaamu wenye ujuzi unaokubalika kimataifa kwa lengo la kuwa na bidhaa zenye ushindani na kufafanua jukumu ambalo TAHA wanafanya ni kuwaandaa vijana kujiajiri kwa kuwapatia mafunzo yenye ujuzi.

"TAHA tumebaini kuna tatizo la uhaba wa watalaam, kwa mfano kwetu inapofika kipindi cha kuchanganya mbegu maabara lazima utakuta wanaofanya kazi hiyo ni watalaamu kutoka nje."Sababu kubwa ni kwamba kwetu hawapo.Hivyo wakati nchi inajipanga kwenye ujenzi wa viwanda ni vema ikaenda sambamba na kuandaa watalaam ili kuondoa changamoto iliyopo,"amesema Mkindi.

Ameongeza cha msingi ni kuweka uratibu mzuri utakaosaidia vijana kuwajengea uwezo utakaosadia kuondoa changamoto ya uhaba wa watalaamu katika fani mbalimbali nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa Tasisi ya Utafiti Nchini, REPOA, Dk. Donald Mmari akizungumza wakati wa kufunga Warsha ya siku mbili kwa watafiti iliyoandaliwa na tasisi yake juu ya kwanini ushindani ni muhimu kuelekea uchumi wa Viwanda.

Mlkuregenzi Mtendaji wa Tanzania Horticultural Asspciation (TAHA) Jacqueline Mkindi akizungumza jambo wakati wa mkutano huo walipjadili nafasi ya kilimo katika uchumi wa Viwanda.

Mratibu na Mtafiti wa Warsha hiyo kutoka Repoa, Dk. Blandina Kilama akizungumza jambo wakati wa Mkutano huo wakati alipokuwa akiongoza meza ya majadiliano.

Mtafiti Kutoka Repoa, Dk. Lucas Katera akizungumza jambo kaatika mjadala wa Nishati kuelekea Uchumi wa Viwanda wakati wa Warsha ya siku Mbili ya Watafiti iliyoandaliwa na Repoa.

Baadhi ya Washiriki wa Warsha ya siku mbili kwa watafiti juu ya kwanini ushindani ni Muhimu kuelekea Uchumi wa Viwanda wakifatilia mada kwa makini.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »