Na Raymond Mushumbusi, MAELEZO
Serikali imejipanga kujenga
machinjio ya kisasa katika eneo la Vingunguti Jijini Dar es Salaam ili
kuondoa changamoto zilizopo machinjioni hapo ikiwa ni pamoja na kulinda
afya za wachinjaji na walaji wa nyama.
.
Akiongelea mipango hiyo kwa
njia ya simu Msemaji wa Manispaa ya Ilala Bi.Tabu Shahibu amesema
Halmashauri iko katika mchakato wa kutangaza zabuni kwa makampuni
yatakayoweza kujenga machinjio hayo kwa kiwango kinachotakiwa.
“Tupo katika harakati za kutafuta mkandarasi wa kujenga machinjio na hivi karibuni tutatangaza zabuni kwa ajili ya ujenzi huo”
“ Napenda kuwahakikishia kwamba
tutafanya jitihada zote za kumpata mkandarasi mapema ili tuanze mapema
ujenzi huu wa machinjio mapya na kuondokana na changamoto zinazokabili
machinjio yaliyopo”Alisema Bi Tabu.
Aidha, Bi Tabu Shaibu amesema
kuwa kabla ya kujenga machinjio mapya wanaendelea na ujenzi wa mabanda
ya machinjio, njia za kushushia ng’ombe ,bucha na kupanua eneo la
machinjio na wameshapima na kufanya tathimini ya gharama ambazo
zitatumika katika marekebisho hayo.
Mpango huu umekuja mara baada
ya ya agizo la mawaziri, akiwemo Waziri wa Kilimo,Mifugo na Uvuvi Mhe.
Mwigulu Nchemba, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee
na Watoto Mhe. Hamis Kigwangalla na Waziri wa Nchi ofisi ya Raisi
TAMISEMI MHE. George Simbachawene walipotembelea machinjio ya Vingunguti
Januari 2 mwaka huu.
Machinjio ya Vingunguti
yalianza kutumika tangu miaka ya 1950 ikiwa inahudumia idadi ya
watumiaji wa mazao ya wanyama waliokuwa kwa wakati ule. Machinjio
hayondio bado yanatumika hadi sasa wakati idadi ya watumiaji wa mazao
ya nyama wameongezeka hivyo kukumbana na changamoto mbalimbali. Ili
kukabiliana na changamoto hiyo Serikali imepanga kuyarekebisha yaliyopo
na kujenga mapya na ya kisasa.