MUHEZA YAANZA MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2026

June 06, 2026

 

DC awapongeza wananchi kwa mwitikio mkubwa wa Jogging

Na Oscar Assenga, Muheza

MAANDALIZI ya kuupokea Mwenge wa Uhuru 2026 katika Wilaya ya Muheza yamezidi kushika kasi baada ya wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki mazoezi ya Jogging yaliyoandaliwa ikiwa ni sehemu ya kujiandaa na tukio hilo muhimu la Kitaifa.

Akizungumza baada ya mazoezi hayo, Mkuu wa Wilaya ya Muheza Ayoub Sebabili  aliwapongeza wananchi kwa mwitikio wao mkubwa, akisema ushiriki huo unaonyesha utayari wa wakazi wa wilaya hiyo kuupokea Mwenge wa Uhuru unaotarajiwa kuwasili Juni 23 mwaka huu.

Alisema mazoezi hayo yamelenga kuwaweka wananchi katika hali nzuri ya afya, kuimarisha mshikamano na kuwaandaa kimwili na kiakili kuelekea mapokezi ya mwenge huo.

“Tunawashukuru wananchi wote waliojitoa kushiriki mazoezi haya. Hii ni ishara nzuri ya ushirikiano katika maandalizi ya tukio muhimu la kitaifa ambalo Wilaya ya Muheza itakuwa mwenyeji wake,” alisema.

Mkuu huyo wa wilaya alibainisha kuwa jogging nyingine itafanyika Juni 13 mwaka huu na kutoa wito kwa wananchi ambao hawakupata nafasi ya kushiriki safari hii kujitokeza kwa wingi ili kuwa sehemu ya maandalizi hayo.

Alisisitiza kuwa mazoezi hayo ya kilomita tano yanafanyika kwa mwendo wa kawaida ili kuwezesha kila mwananchi kushiriki bila kujali umri au hali yake ya kiafya.

“Tunawakaribisha vijana, wanawake, wazee pamoja na watu wenye ulemavu kushiriki mazoezi haya. Lengo letu ni kuona wananchi wote wanakuwa sehemu ya maandalizi ya kuupokea Mwenge wa Uhuru 2026,” alisema.

Muheza inatarajia kuupokea rasmi Mwenge wa Uhuru Juni 23, huku maandalizi mbalimbali yakiendelea kufanyika kuhakikisha tukio hilo linafanyika kwa mafanikio na kuacha alama chanya kwa wananchi wa wilaya hiyo.

Share this

Related Posts

Latest
Previous
Next Post »