📌 Unahusisha kuongezea vijana ujuzi, kuboresha upatikanaji wa huduma za kifedha, na kuondoa vikwazo vya ujasiriamali na ajira binafsi
📌 Ataka ujuzi unaotolewa kwa vijana uende sambamba na utoaji wa mitaji
📌 Awaasa Vijana kuchangamkia fursa na kuwa waaminifu wanapopata nafasi
📌 Wanawake 6,130, Wanaume 4,905 na Makundi maalum 1,226 kufikiwa
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko leo amezindua Mpango wa Uwezeshaji wa Kiuchumi kwa Vijana (YEE) ambao unagusa maeneo yanayopitiwa na mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) ikiwa ni jitihada zinazoendelea kufanywa na Serikali katika kuhakikisha kuwa jamii zilizo karibu na miradi zinanufaika na miradi hiyo.
Akizindua mradi huo katika Kijiji cha Bukombe, wilayani Bukombe, Mkoa wa Geita tarehe 18 Agosti 2025, Dkt. Biteko amesema mradi huo wa Uwezeshaji Vijana Kiuchumi ni moja ya miradi iliyopangwa kuwezeshwa na Kampuni ya EACOP kwa kipindi cha ujenzi na baada ya ujenzi ikiwa ni sehemu ya Uwajibikaji wa Kampuni hiyo kwa jamii.
Amesema mradi huo umepangwa kuwafikia zaidi ya vijana 12,261 ambapo miongoni mwao wanawake ni 6,130; wanaume 4,905 na makundi maalumu ni 1,226 katika awamu ya kwanza inayohusisha Mikoa ya Geita, Kagera, Tabora na Tanga.
" Tunapozindua mradi huu hatuna budi kuwashukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Jamhuri ya Uganda. Viongozi wetu hawa kwa nia yao ya dhati na moyo wa uzalendo wameuendeleza na kuusimamia kikamilifu mradi huu wa EACOP ambao umefikia asilimia 65, tumefikia hapa sababu ya msukumo wao wa kutekeleza mradi huu" Amesema Dkt. Biteko
Ameeleza kuwa tangu kuanza kwa mradi wa EACOP mwaka 2022 hadi sasa, jumla ya Watanzania 9,194 wamepata nafasi za kufanya kazi ndani ya mradi na hivyo kuwa fursa kwao ya kujipatia kipato, mwaka 2024 kampuni ilitoa mafunzo maalumu kwa Vijana 170 na kuwapatia kazi kwenye mradi, Vijana wengine 110 wapo katika masomo na wanatarajiwa kujumlishwa pia katika Mradi huo pamoja na kutoa ufadhili wa Vijana 238 katika vyuo mbalimbali nchini.
Amesema wananchi wanaopitiwa na miradi wanayo haki ya kunufaika na miradi lakini wana wajibu wa kulinda miundombinu ya mradi na kuufanya kuwa ni sehemu yao kwani unachangia pia kubadilisha maisha ya wananchi.
Pia, Dkt. Biteko ameipongeza kampuni ya EACOP na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa kusimamia kwa ufanisi mradi huo huku akisisitiza kuwa, ili wananchi waone mradi huo ni sehemu yao lazima waone faida zake hivyo miradi kama ya YEE inawapa chachu wananchi kulinda miundombinu ya EACOP kwa wivu mkubwa.
Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko amesisitiza kuwa, kampuni mbalimbali zinazotekeleza miradi kuhakikisha kuwa hawaweki mkazo kwenye kuongeza ujuzi tu kwa wananchi bali wanawapatia mitaji ili waweze kufanya vizuri zaidi.
Aidha, amewaasa vijana kuchangamkia fursa zinazotokea kwenye miradi, wajitume, wawe waaminifu pale wanapopata fursa na kueleza kuwa Serikali itaendelea kuwatengenezea fursa ili wajikwamue kiuchumi na kuleta maendeleo nchini.
Kwa upande wake, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira), Mhe. Patrobas Katambi amesema Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ametengeneza mipango mikakati ya kuhakikisha vijana wanapewa fursa za ajira na mitaji kwenye maeneo mbalimbali ambapo mpango wa YEE ni kielelezo cha matokeo ya mipango hiyo.
Ameeleza kuwa, kumekuwa na programu mbalimbali ikiwemo ya uwezeshaji wananchi kiuchumi ambapo kupitia programu hiyo zaidi ya shilingi trilioni tatu zilitolewa kwa Watanzania takriban milioni 24 ikiwemo Wanawake, Vijana na Makundi maalum kwa lengo la kuwawezesha kujikwamua kiuchumi
Mkuu wa Mkoa Geita, Martine Shigella akizungumza kwa niaba ya Wakuu wa Mikoa inayopitiwa na mradi wa EACOP amesema kuwa mradi wa EACOP ni miongoni mwa miradi mikubwa ambayo wananchi wa Geita wamenufaika nayo kwa namna mbalimbali ikiwemo ajira za moja kwa moja na muda na mfupi pamoja na mnyororo wa thamani kupitia biashara ya vyakula, mbogamboga, matunda n.k
Amesema Mpango wa uwezeshaji wa vijana kiuchumi ni matunda ya Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ameendelea kuhakikisha vijana wanapata elimu na ujuzi hivyo mpango wa YEE unaongeza chachu hiyo ya utoaji elimu na ujuzi kwa wananchi wakiwemo vijana.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba amesema utekelezaji wa mradi wa EACOP wenye urefu wa km 1443 ni moja ya miradi 17 inayotekelezwa na Wizara ya Nishati ikiwemo mradi wa Julius Nyerere ( MW 2,115) ambao umekamilika, miradi ya umeme ya Ruhudji, Rumakali na Malagarasi pamoja miradi mingine ya utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia ukiwemo wa Eyasi Wembere.
Katika mradi wa EACOP amesema Serikali imechangia shilingi trilioni 1.12 ambazo ni hisa za Tanzania na kuna kampuni za kitanzania 200 ambazo zinafanya kazi mbalimbali katika mradi ambazo zitalipwa jumla ya shilingi trilioni 1.325 ikiwa ni moja ya matunda ya uwepo wa mradi huo nchini.
Akieleza sababu za kufanyika.kwa uzinduzi wa mradi wa YEE wiiayani Bukombe amesema kuwa Bukombe kuna kituo kikubwa zaidi cha kusukuma mafuta yatakayotoka nchini Uganda hadi Chongoleani Tanga, kuna kambi kubwa ya mradi wa EACOP na pia kilometa 20 za bomba hilo la mafuta zinapita katika eneo la Bukombe.
Aidha, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Mussa Makame ameeleza kuwa, TPDC imeendelea kushirikiana na kampuni ya EACOP kuhakikisha kuwa mahitaji ya wananchi yanabainishwa na kuzingatiwa katika utekelezaji wa mpango wa Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).
Ameeleza kuwa mahitaji yaliyoainishwa katika mradi wa YEE yaliandaliwa kwa kushirikiana na Serikali za Mitaa kwa ngazi ya vijiji, Kata na Halmashauri zilizopo maeneo linapopita bomba la mafuta.
Awali Clare Haule - Meneja wa Uwekezaji na Uwajibikaji kwa Jamii katika kampuni ya EACOP alisema mradi wa YEE umeanzishwa kwa kutambua kwamba zaidi ya asilimia 65 ya idadi ya watu wa Tanzania ni vijana chini ya umri wa miaka 35. Hata hivyo, vijana wengi hasa katika maeneo ya vijijini wanakumbana na vikwazo vingi kama vile ukosefu wa ajira, ukosefu wa mafunzo ya ufundi stadi , na ugumu wa kupata mitaji ya kuanzisha au kukuza biashara.
Alisema awamu ya kwanza ya Mradi wa YEE utawawezesha kiuchumi vijana katika mikoa ya Geita, Kgera, Tabora na Tanga pamoja na mikoa mingine inayobaki itanufaika katika awamu ya pili ambayo ni Singida, Shinyanga, Dodoma na Manyara ambapo vijana watapewa ujuzi unaolingana na mahitaji ya soko, kuboresha upatikanaji wa huduma za kifedha, na kuondoa vikwazo vya ujasiriamali na ajira binafsi.
Aliongeza kuwa, Mradi wa YEE ni sehemu ya Sera ya Uendelevu ya EACOP, chini ya nguzo ya Vizazi Vijavyo, inayolenga kujenga uwezo wa vijana na kuongeza upatikanaji wa fursa za kiuchumi katika jamii zinazoguswa na mradi.
Mwisho.
EmoticonEmoticon