Showing posts with label habari. Show all posts
Showing posts with label habari. Show all posts

NAIBU WAZIRI ARDHI AITAKA NHC KUONA NAMNA YA KUANZISHA MIRADI MIKUBWA KILA WILAYA NCHINI

March 15, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga,TANGA


NAIBU Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi,Kaspar Mmuya amelitaka Shirika la Taifa la Nyumba (NHC) waanze kufikiria namna ya kuanzisha miradi mikubwa ambayo inaweza kutoa huduma kwa wananchi kwenye kila mikoa na wilaya ili wajipambanue utofauti wao na mashirika mengine.

Mmuya aliyasema hayo wakati wa ziara yake ya kutembelea mradi wa Jengo la Kitega Uchumi unaosimamiwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mkwakwani Plaza ambapo alisema kutokana na uwepo wa mahitaji yake kwa wananchi waliopo maeneo mbalimbali hapa nchini.

Mradi huo ni moja ya miradi mingi NHC wanafanya nchini na unagharimu kiasi cha Sh.Bilioni 8.6 fedha ambazo zilizopitishwa na Bunge katika Bajeti ya Mwaka 2025/2026 ambapo ulianza mwaka jana mwezi wa sita na utakamilika kwa muda wa miezi 24 na wanategemeaJune mwakani utakamilika .

Mpaka sasa mradi huo umetekelezwa kwa asilimia 37 na fedha zilizotumika ni zaidi ya Bilioni 2 ambao utakuwa na ghorofa tatu za mwanzo za biashara za kawaida,ya pili na tatu ni kutakuwa na ofisi mbalimbali na ya nne mpaka nane hizo ni kwa ajili ya makazi watajenga nyumba 20 ambazo nyumba 10 zitakuwa na vyumba viwili pamoja na master, jiko na vitu vingine na vyumba 10 zitakuwa na vyumba vitatu.

“Kwa kweli nimetembelea mradi huu nimeridhika kwa maana nimeona thamani ya fedha iliyotumika mpaka asilimia ya utekelezaji kuna uwiano mkubwa nimeangalia ubora na umahiri wa mafundi waliokuwepo nimejiridhisha kuna unadhifu mkubwa kwenye kazi yao”Alisema Naibu Waziri huyo.

Alisema pia ujenzi wa Jengo hilo umezingatia mazingira rafiki kwa watu wote kwamba litakuwa na lifti mbili ambazo zitatoa huduma za kijamii katika ghorifa ya tatu na kuna lifti ambayo watakuwa wanatumia watu watakaokuwa wanakaa juu kwenye nyumba za makazi na nyumba hizo hazitakodishwa zitauzwa kwa mtu yoyote mwenye uwezo wa kununua na matangazo tiyari wamekwisha kuwekwa.

Alisema kuna umuhimu wa uwepo wa miradi kama hiyo katika wilaya mbalimbali ikiwezekana mradi unaofanana nao waweke kwenye majimbo yote 272 ili wakitembea wajumbe NHC wapo katika maeneo ambayo wapiga kura wa Rais,Wabunge na Madiwani wanapotokea lakini niwapongeze kwa mradi huu.

Hata hivyo alimshukuru Rais Dkt.Samia Suluhu kwa kulifanya shirika hilo liwe imara kiuchumi lakini lijielewe sasa linabidi lisonge mbele katika kuwekeza zaidi katika ujenzi wa makazi.

Ambapo zaidi ya nyumba milioni 3 kila mwaka ni mapungufu ama mahitaji ambayo yanahitajika kwenye nchi na wanavyoelewa idadi ya watu inaongezeka kwa kiasi kikubwa na mahitaji ya nyumba yanaongezeka.

“Wito nyie wenyewe mmejionea mradi upo asilimia 37 na zaidi ya asilimia 70 ya Jengo hilo tayari watu wameanza kuchukua nafasi kununua hivyo kuna mahitaji makubwa ya nyumba hapa Tanga ushauri wangu anzeni kufikiri kuanza miradi mikubwa inayoweza kutoa huduma kwa wananchi ili kujipambanua na kujitofautisha na mashirika mengine “Alisema

Kwa upande wake Msimamizi mkuu wa Mradi huo kutoka NHC Ephahim Msigwa alisema mradi huo unatumia fedha za ndani na una ghorofa nane ambapo ghorofa tatu zitakuwa kwa ajili ya biashara na tano za makazi ya watu ambapo mpaka sasa wamekwisha kutumia Bilioni 2.1.

Mradi huo ni wa miaka miwili ambapo ulianza kutekelezwa mwezi juni mwaka 2025 na kwamba unatarajiwa kukamilika ukamilike mwezi juni 2027 ambapo mpaka sasa upo asilimia 37.9 huku wananchi zaidi ya 189 wa Mkoa wa Tanga wakinufaika na ajira kwenye mradi huo.

Mwisho

KAMATI YA BUNGE YAITAKA WMA KUHAKIKI MITA ZA UMEME KWA MUJIBU WA SHERIA

KAMATI YA BUNGE YAITAKA WMA KUHAKIKI MITA ZA UMEME KWA MUJIBU WA SHERIA

March 15, 2026 Add Comment

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo imeiagiza Wakala wa Vipimo (WMA) kuhakikisha mita za umeme zinahakikiwa kikamilifu kabla ya kufungwa kwa ajili ya matumizi, kwa kuzingatia sheria zilizopo ili kulinda haki za watumiaji.

Aidha, Kamati hiyo imeipongeza WMA kwa jitihada za uhakiki na ukaguzi wa vipimo mbalimbali, ikiwemo mita za maji, huku ikiitaka Wakala hiyo kuendelea kusimamia kwa ukaribu vipimo katika sekta ya ujenzi ili kupunguza malalamiko ya wananchi yanayotokana na bidhaa hizo.

Hayo yameelezwa leo Machi 14, 2026, na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Deodatus Mwanyika, wakati wa ziara ya kikazi katika Kituo cha WMA cha Uhakiki wa Vipimo Misugusugu mkoani Pwani kwa lengo la kukagua miradi ya maendeleo na kujionea shughuli za uhakiki wa vipimo zinavyotekelezwa kituoni hapo.

Akizungumza katika ziara hiyo, Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dennis Londo, aliihakikishia Kamati kuwa wizara itatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa.

Alisisitiza kuwa azma ya Serikali ni kuhakikisha WMA inasimamia matumizi ya vipimo sahihi katika uzalishaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali, pamoja na Uhakiki wa mita za umeme na maji, ili kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson Simon, akitoa salamu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, alibainisha kuwa uhakiki wa vipimo ni uti wa mgongo wa uchumi wa mkoa huo. Alieleza kuwa kwa sasa Mkoa wa Pwani una jumla ya viwanda 1,688, vikiwemo viwanda vikubwa 199 na vidogo sana 1,017, hivyo uhakiki wa usahihi wa Vipimo ni nyenzo muhimu katika kuvutia uwekezaji zaidi.

Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa WMA, Bw. Alban Kihulla, alisema kuwa ukaguzi na uhakiki wa vipimo una nafasi kubwa katika kuhakikisha haki na usawa baina ya pande mbili zinazofanya biashara.

Pia, aliwahimiza wananchi kuhakikisha wanatumia vipimo vilivyohakikiwa, huku akiwasihi watoa huduma kuzingatia uadilifu kwa kutoa huduma kupitia vipimo sahihi ili kuleta usawa na kuhakikisha bidhaa zinazonunuliwa zinaendana na thamani halisi ya fedha.

MTENDAJI MKUU ADEM AFUNGUA KIKAO KAZI CHA CHAMA CHA KUTETEA HAKI ZA WALIMU

March 14, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM), Dkt. Maulid J. Maulid, amefungua kikao kazi cha Chama cha Kulinda na Kutetea Haki za Walimu (CHAKUHAWATA) kinachofanyika jijini Dodoma, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya wadau mbalimbali wa sekta ya elimu ili kuimarisha uongozi, utawala bora na udhibiti wa ubora wa elimu nchini.

KAMATI YA BUNGE YAKAGUA MAENDELEO YA UJENZI WA KAMPASI YA CHUO KIKUU MZUMBE TANGA

March 14, 2026 Add Comment
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Mhe. Husna Juma Sekiboko (Mb) akiongoza Wajumbe wa Kamati hiyo kukagua maendeleo ya mradi wa ujenzi wa Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi ya Tanga, unaotekelezwa kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET).

VIJIJI VINNE MBULU VYAANZA KUNUFAIKA NA MRADI WA MAJI WA BILIONI 41

March 13, 2026 Add Comment

Wananchi na wakazi wa Hydom wilayani Mbulu mkoa wa Manyara wamemshukuru Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kufuatia Wizara ya Maji kupitia RUWASA kutekeleza mradi mkubwa wa Majisafi ya bomba wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 41 na tayari vijiji vinne vimeshaanza kunufaika na mradi huo.

Wametoa pongezi hizo wakati wa ziara ya kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira alipotembelea na kukagua mradi huo ikiongozwa na Mwemyekiti wake Mhe. Jackson Kiswaga (Mb) katika eneo la Hydom lilipo tangi kubwa la ujazo wa lita 2,000,000 la mradi huo.

Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA Mha. Wolta Kirita aliieleza Kamati hiyo kuwa tayari wananchi zaidi 800 wameshasajiliwa na kupatiwa kadi za malipo kabla ya matumizi kwani mradi huo unaenda sambamba na ufungaji wa dira za maji za malipo ya kabla, ambapo mwananchi anaweza kuchota maji kwenye kituo muda wowote anapokuwa anahitaji huduma hiyo.

Mkurugenzi Mkuu Kirita alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika Novemba 2027.

Kwa mujibu wa Meneja wa RUWASA mkoa wa Manyara Mha. James Kionaumela alisema mradi huo umeshaanza kutoa huduma katika vijiji vinne na ukikamilika utahudumia zaidi ya wakazi 100,000 wa eneo hilo.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbulu Mhe. Michael Semindu akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Sendiga alisema kwa sasa wananchi wa wilaya hiyo wanapata maji kwa saa 12 kwa siku huku akiipongeza RUWASA kwa kazi nzuri katika kutekeleza mradi huo.