WAZIRI SANGU: MSHIKAMANO NA AMANI NDIO NGUZO YA MAENDELEO YA TAIFA
habariMRADI WA EACOP UMETOA ZAIDI YA AJIRA 3,000 MKOANI SINGIDA-MHE.SALOME
habariIramba, Singida
Zaidi ya ajira 3,000 zimetolewa mkoani Singida kupitia utekelezaji wa Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP), huku wananchi wakinufaika pia kwa kutoa huduma mbalimbali ikiwemo kuuza vyakula, kukodisha vyombo vya usafiri na kutoa huduma nyingine zinazohitajika wakati wa utekelezaji wa mradi huo, hatua inayochangia kuongeza kipato kwa jamii zinazouzunguka mradi.
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema hayo leo Juni 13, 2026 wilayani Iramba mkoani Singida wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba.
Amesema dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni kuhakikisha kuwa Mradi wa EACOP hauwi tu mradi wa kukuza uchumi wa nchi bali unakuwa chachu ya kubadilisha maisha ya wananchi mmoja mmoja kupitia fursa za ajira na biashara.
Katika hatua nyingine, Mhe, Salome amesema kuwa ifikapo mwaka 2030 vitongoji vyote wilayani Iramba vitakuwa vimefikiwa na umeme ambapo kati ya vitongoji 393 vilivyopo tayari vitongoji 165 vina umeme na kwa sasa wakandarasi wanaendelea na kazi ya kusambaza umeme katika vitongoji 65.
Ameongeza kuwa Serikali imetoa shilingi milioni 285 kwa ajili ya ujenzi wa ofisi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wilayani humo ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi, mradi unaotarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu.
Vilevile amesema Serikali imetoa shilingi bilioni 1.085 katika mwaka huu wa fedha unaoisha kwa ajili ya maboresho ya miundombinu ya umeme wilayani Iramba, ikiwemo kupunguza urefu wa laini za umeme na kuongeza transfoma ili kuboresha upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi.
Kuhusu matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia, Mhe. Salome amesema Wilaya ya Iramba imepokea majiko banifu zaidi ya 1,000 na majiko ya gesi zaidi ya 2,000 ikiwa ni hatua za uhamasishaji wa nishati safi ya kupikia, huku akitoa wito kwa wanaume kuwaunga mkono wanawake kwa kununua na kuhamasisha matumizi ya majiko hayo ili kuwawezesha kina mama kupata muda zaidi wa kushiriki katika shughuli za uzalishaji mali na maendeleo ya familia.
OFISI YA WAZIRI MKUU NA OMDTZ ZAIMARISHA UTAYARI WA JAMII KUKABILIANA NA MAFURIKO DAR ES SALAAM
habari
Na, mwandishi wetu - Dar es Salaam
Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na Taasisi OpenMap Development Tanzania (OMDTZ), kupitia mradi wa Ramani Zetu, Sauti Zetu imeendesha warsha ya kupitia na kuthibitisha Mipango ya Kujiandaa na Kukabiliana na Maafa kwa kata tano za Makurumula, Mabibo, Keko, Ubungo na Tabata jijini Dar es Salaam.
Warsha hiyo imewakutanisha viongozi wa serikali za mitaa, Kamati za Usimamizi wa Maafa za Kata, wataalamu wa usimamizi wa maafa, waratibu wa maafa wa mkoa na wilaya pamoja na wadau mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha mipango hiyo inakidhi mahitaji halisi ya jamii zinazokabiliwa na hatari ya mafuriko Dar es Salaam.
Akifungua warsha hiyo Mkurugenzi Msaidizi wa Operesheni za Maafa kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Kanali Selestine Masalamado amesema kuwa ubora wa mpango wa maafa hupimwa kwa uwezo wake wa kutekelezeka na kuleta matokeo chanya kwa wananchi, huku akisisitiza umuhimu wa mipango hiyo kuzingatia mazingira halisi, rasilimali zilizopo na uwezo wa taasisi husika.
“Mradi huu unaofadhiliwa na Zayed Sustainability Prize kupitia Taasisi ya Open Map Development Tanzania (OMDTZ), kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – Idara ya Usimamizi wa Maafa, umekuja wakati sahihi na tunamatarajio makubwa katika kuleta matokeo chanya kuhakikisha tunaimarisha masuala ya usimamizi wa maafa nchini, ”alisema Kanali Masalamado
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa OMDTZ, Bw. Innocent Maholi, alisema taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na Serikali katika kuimarisha ustahimilivu wa jamii dhidi ya maafa kupitia matumizi ya teknolojia, uchoraji ramani shirikishi na uwekezaji katika mifumo ya tahadhari ya mapema katika maeneo hatarishi.
Naye Mratibu wa Maafa wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Gerald Sondo, amepongeza ushirikiano huo akieleza kuwa mipango hiyo itasaidia kuongeza utayari wa jamii, kuboresha uratibu wa mwitikio wa dharura na kupunguza athari za mafuriko katika Jiji la Dar es Salaam.
“Kwa kipindi cha miezi mitatu iliyopita, kamati za usimamizi wa maafa katika kata husika zimefanya tathmini ya vihatarishi, kubainisha njia za uokoaji na maeneo salama, kuandaa mifumo ya mawasiliano na uratibu pamoja na kupendekeza hatua za tahadhari ya mapema zinazoshirikisha jamii,”alisema Bw. Sondo.
Aliongezea kuwa, Mipango iliyothibitishwa itatumika kama mwongozo wa vitendo kwa jamii kabla, wakati na baada ya maafa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha usalama wa wananchi na ustahimilivu dhidi ya mafuriko na majanga mengine.
WATHIBITI UBORA WA SHULE WAASWA KUSIMAMIA KWA WELEDI MATUMIZI YA NeST
habari
Wathibiti Ubora wa Shule nchini wametakiwa kusimamia kwa weledi matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi wa Umma (NeST) ili kuhakikisha manunuzi yote ya Serikali yanafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.
Rai hiyo imetolewa Juni 11, 2026 jijini Arusha na Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Fredrick Salukele, akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, katika ufunguzi wa mafunzo kuhusu matumizi ya Mfumo huo.
Dkt. Salukele amesema mafunzo hayo yatawawezesha washiriki kutumia mfumo huo kwa ufanisi katika usimamizi wa fedha za uchangiaji, ununuzi wa bidhaa na huduma mbalimbali pamoja na malipo ya shughuli za tathmini za shule.
Amewasisitiza washiriki kusimamia kwa ufanisi rasilimali zilizopo, ikiwemo rasilimali watu na miundombinu, sambamba na kuimarisha huduma bora za elimu.
Aidha, Dkt. Salukele amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri na Wathibiti Ubora wa Shule kuhakikisha taasisi za elimu zinazingatia taratibu zote za uendeshaji ikiwemo masuala ya malazi, chakula na usalama wa wanafunzi.
Naye, Miurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule kutoka Wizara hiyo Dkt. Ephrahim Simbeye amesisitiza uzingatiaji wa miongozo ya elimu, akitaka kukomeshwa kwa adhabu zisizokubalika na kuhakikisha kuna mazingira bora ya ufundishaji na ujifunzaji kwa wanafunzi.
Wakizungumza kuhusu mafunzo hayo, Bi. Lilian Kasenga Mthibiti Ubora kutoka Manispaa ya Temeke pamoja na Emmanuel Hangaya kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema, wametaja mbinu wanazotumia kufikia malengo huku wakisema mafunzo hayo yatakwenda kuwaongezea ufanisi kazini.













