CCM YAUPONGEZA UBALOZI WA UINGEREZA KUHAMIA DODOMA

February 21, 2024

 Chama Cha Mapinduzi kimeumepongeza Ubalozi wa Uingereza nchini kwa kuitikia wito wa Serikali ya Awamu ya Sita wa kuzitaka ofisi za ubalozi mbalimbali zilizopo Tanzania kuhamia Dodoma.


Pongezi hizo, zimetolewa leo, tarehe 21/2/2024, jijini Dodoma na Katibu wa NEC wa Idara ya Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Ndg. Rabia Abdalla Hamid, wakati akizungumza na ujumbe wa Maafisa wa Ubalozi wa Uingereza, katika Ofisi za Makao Makuu ya CCM, Dodoma.

Ujumbe wa Maafisa wa Ubalozi wa Uingereza, ukiongozwa na Mkuu wa Ofisi ya Dodoma, Bi. Godfrida Magubo, mapema leo, umetembelea Ofisi za Makao Makuu ya CCM, Dodoma kwa ajili ya kujitambulisha na kuitambulisha Ofisi ya Ubalozi huo, iliyopo Dodoma, ambayo ilifunguliwa Januari 2024.

‘’Chama Cha Mapinduzi kinawashukuru na kuwapongeza sana kwa kuunga mkono juhudi za kuhamia Makao Makuu ya Nchi hapa Dodoma,’’ Rabia alisema akiwapongeza.

Aidha, ameutaka Ubalozi wa Uingereza wawe mabalozi wa kuhamasisha ofisi zingine za ubalozi mbalimbali nchini kuhamia Dodoma.

Ndg. Rabia ameongeza kusema, ‘’ Chama na Serikali tumehamia Dodoma moja kwa moja, na hatukusudii kurudi nyuma, hivyo natoa wito kwa ofisi zingine za ubalozi wa nchi mbalimbali kuhamia Dodoma kama ninyi mlivyofanya’’.

Katibu wa NEC Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa na ujumbe wa Maafisa wa Ubalozi wa Uingereza wamezungumza na kujadiliana mambo mbalimbali ya kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na Uingereza.





Share this

Related Posts

Previous
Next Post »