Hafla ya Uwekaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Ukuta wa Ukingo wa Bahari hapo Mizingani Forodhani Mjini Zanzibar

January 07, 2017

 Na Othman Khamis Ame, OMPR
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema adha ya mafuriko yanayotokea kila mwaka wakati wa msimu wa Mvua za Masika na kuwakumba Wananchi yataondoka au kupungua zaidi baada ya kukamilika kwa miradi tofauti iliyonzishwa na Serikali chini ya Mradi wa huduma za Jamii Mijini.
Alisema mafanikio ya mradi huo tayari yameanza kuonekana katika ujenzi wa michirizi ya maji ya mvua kwenye maeneo ya Daraja Bovu, Mnazi Mmoja, Kijangwani na baadhi ya maeneo ya Jang’ombe  na Wananchi wake tayari wanafaidika na matunda ya mradi huo.
Balozi Seif Ali Iddi alieleza hayo wakati wa hafla ya Uwekaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Ukuta wa Ukingo wa Bahari hapo Mizingani  Forodhani Mjini Zanzibar ikiwa ni miongoni mwa harakati za shamra shamra za kusherehekea miaka 53 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar.
Alisema Serikali ya Mapinduzi imejipanga kuimarisha  miradi hiyo ikiwa sehemu ya Jududi za utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM  ya Mwaka 2015 ikilenga kuwaondoshea usumbufu unaowakumbwa wananchi walio wengi hasa wale wa maeneo ya Ng’ambo ya Mji.
Balozi Seif  alisema ujenzi wa Ukuta wa Ukingo wa Bahari hapo Mizingani  Forodhani Mjini Zanzibar ukiwa miongoni mwa miradi ya Jamii Mijini ni muhimu kwa maendeleo ya Mji Mkongwe wa Zanzibar uliobahatika kuwemo kwenye  Miji ya urithi wa Dunia  ambao unategemewa kwa uchumi wa Taifa kwa upande wa Sekta ya Utalii.
Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  Nd.  Khamis Mussa Omar alisema chimbuko la mradi wa ujenzi wa ukuta wa Mizingani umetokana na athari kubwa iliyojitokeza siku za nyuma ya kasi kubwa ya maji ya Bahari iliyoathiri eneo hilo.
Alisema Ujenzi  wa Ukuta huo ulioanza Tarehe 22 April 2015  ukiwa na urefu wa Mita 320, upana Mita sita na ongezeko na mita sita kuelekea usawa wa Bahari unatarajiwa kukamilika rasmi ndani ya Mwaka huu wa 2017.
Alieleza kwamba asilimia 65% ya ujenzi huo imekamilika kwa upande wa ukuta wenyewe na kazi iliyobaki na kuendelezwa kwa hivi sasa ni ujenzi wa bustani pamoja na bara bara ya watembeao kwa miguu.
Akimkaribisha Balozi Seif kuzindua ujenzi huo wa Ukuta, Waziri wa Fedha na Mipango Dr. Khalid Salum Mohamed alisema uimarishaji wa Mji Mkongwe kupitia mradi wa Jamii Mijini utakuwa chachu ya kuimarika kwa Sekta ya Utalii Nchini.
Dr.  Khalid aliwaomba Wamiliki Binafsi wa majengo yaliyomo ndani ya Mji Mkongwe kushirikiana na Serikali Kuu katika kuyaweka kwenye mazingira bora yatakayotoa haiba nzuri ya Mji wa Zanzibar unaotegemewa katika makusanyo ya Mapato ya Taifa kupitia sekta hiyo ya Utalii.
Ujenzi wa Ukuta wa Ukingo wa Bahari hapo Mizingani  Forodhani Mjini Zanzibar  unasimamiwa na Wizara ya Fedha na Mipango ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Mkono wenye masharti nafuu wa shilingi Bilioni 7,222,577,890 kutoka Benki ya Dunia.
Kampuni ya  Seyani Brothers ya Mjini Dar es salaam ndio iliyopewa jukumu la kujenga Ukuta huo chini ya Msimamizi  Mshauri muelekezi Kampuni ya Aurecon kutoka Nchini Afrika Kusini.
Balozi Seif akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi, wahandisi wa ujenzi wa ukuta,  watendaji wa Wizara ya Fedha  pamoja na washauri walekeza wa ujenzi huo mara baada ya kukamilisha kwa hafla hiyo.
Kulia ya Balozi Seif waliokaa vitini ni Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mh. Zubeir Ali Maulid, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha Nd. Khamis Mussa, Kamishna wa Polisi Zanzibar Kamanda Hamdan Makame.
Kushoto ya Balozi Seif  ni Waziri wa Fedha Dr. Khalid Salum,  Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Mh. Ayoud Mohamed Mahmoud na Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Mh. Rashid  Ali Juma.
Makamu wa Pili a Rais wa Zanzibar Balozi Seif akiweka jiwe la Msingi la Ujenzi wa Ukuta wa kuzuia maji ya Bahari hapo Mizingani Forodhani Mjini Zanzibar ikiwa ni shamra shamra za kusherehekea miaka 53 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Wa kwanza kushoto ni Waziri wa Fedha na Mipango wa SMZ Dr. Khalid Salum Mohamed ambapo wa nyuma yake ni Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Mh. Zubeir Ali Maulid. Picha na OMPR – ZNZ.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »