Serikali yasaidia viwanda vidogo 48,996

July 17, 2016

DSC_1141 
Jacquiline Mrisho – MAELEZO
Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania imesaidia jumla ya viwanda vidogo 48,996 kwa kuvipa huduma muhimu zinazowawezesha wajasiriamali kusimama wenyewe ili kuondokana na lindi la umasikini.
Takwimu hizo zimetolewa na Mkurugenzi wa Viwanda Vidogo na vya Kati kutoka Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Dkt. Consolatha Ishebabi alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hii kuhusu mikakati ya Serikali juu ya kuendeleza viwanda vidogo pamoja na umuhimu wa viwanda hivyo.
Dkt. Ishebabi amesema kuwa Viwanda Vidogo vikiendelezwa ndio mwanzo wa kuwa na viwanda vya Kati na Vikubwa na hiyo ndio sababu kubwa inayoifanya Serikali kutilia mkazo na kuzidi kuweka mikakati mingi ya kuviinua viwanda hivyo ili vikue na kufikia viwanda vya kati au vikubwa.
“Kwa mujibu wa Sensa ya Viwanda ya mwaka 2013, Tanzania ina jumla ya viwanda vidogo 48,996 ambavyo vimesaidia kutoa jumla ya ajira 156,476 kwa wananchi, hivyo tunaona umuhimu wa viwanda vidogo katika suala la kutoa ajira na kupunguza umasikini kwa kiasi kikubwa”, alisema Dkt. Ishebabi.
Mkurugenzi huyo amefafanua kuwa viwanda vidogo sio mali ya Serikali bali Serikali iko pamoja na viwanda hivyo katika kuvisaidia ili viendelee na kuhakikisha vinakuwa kufikia viwanda vya kati au vikubwa hivyo, kazi ya Serikali ni kuwahamasisha wananchi na kuwapa misaada ya elimu, mikopo pamoja na kuwawezesha maeneo ya kufanyia shughuli hizo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Masoko na Habari wa Shirika la Kuhudumia Viwanda Viwanda Vidogo (SIDO), Janeth Minja amesema kuwa Shirika hilo ni kubwa na liko katika Mikoa yote Tanzania, linawasaidia wajasiriamali kwa kuwapa huduma za aina 4 ambazo ni; mafunzo, teknolojia, mikopo pamoja na kuwatafutia masoko ya bidhaa zao.
“Napenda kutoa rai kwa wananchi hasa vijana na wanawake wasio na ajira kuwa wasijibweteke tu majumbani bali watumie fursa zinazotolewa na SIDO ili waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na umasikini, kama mtu ana wazo la biashara anatakiwa awasiliane na ofisi zetu za SIDO zilizopo kwenye Mkoa husika”, alisema Janeth.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »