URITHI WA UTAMADUNI WAELEZWA KUWA KIVUTIO MUHIMU CHA UTALII NCHINI

May 14, 2015

ut1
Mkurugenzi Uendeshaji na Utumishi wa Wizara ya Habari Utamaduni Utalii na Michezo Joseph Kilangi akitoa hutuba yake ya ufunguzi katika Semina ya majadiliano ya “Rasimu ya Sera ya Urithi wa Utamaduni” iliyofanyika Forodhani Mjini Zanzibar,kulia kwake ni Mkurugenzi wa Uendeshaji na Utumishi, Sera na Utafiti wa Wizara hiyo na kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Makumbusho na Mambo ya Kale Dkt. Amina Ameir Issa.
ut2
Mwalimu wa Historia Chuo Kikuu cha Taifa Suza Bi Zainab Othman akitoa mawazo ya kuiboresha Rasimu hiyo katika Semina ya kuijadili ‘Rasimu ya Sera ya Urithi wa Utamaduni’ Semina hiyo iliyofanyika Forodhani Mjini Zanzibar.
ut3
Mkurugenzi wa Sanaa Zanzibar Mdungi Ussi akichangia Rasimu ya Sera ya Urithi wa Utamaduni ambapo pamoja na mambo mengine ameshauri Sera hiyo isiingiliane na Sera zingine.Picha na Faki Mjaka
ut4
Mkurugenzi wa Idara ya Makumbusho na mambo ya kale Dkt Amina Ameir Issa akiwashukuru Washiriki kwa michango yao katika Semina ya Majadiliano ya Rasimu ya Sera ya Urithi wa Utamaduni iliyofanyika Forodhani mjini Zanzibar,kulia kwake ni Mkurugenzi wa Uendeshaji, Sera na Utafiti wa Wizara ya Habari Utamaduni Utalii na Michezo Zanzibar Mashaka Hassan Mwita na kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Magofu Zanzibar Abdallah Khamis Magofu-Picha na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar
………………………………………………………………………………….
Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar
Urithi wa Utamaduni umeelezwa kuwa ni moja kati ya Vitega uchumi muhimu ambapo kama utatumika vyema utapelekea mchango mkubwa kwa Wananchi na Serikali kwa ujumla.
Mchango huo unaweza kuwepo katika Nyanja mbalimbali ikiwemo ya Utalii,Teknolojia, Utafiti na Elimu.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Idara ya Mambo ya Kale Dkt. Amina Ameir Issa wakati wa mjadala wa Rasimu ya Sera ya Urithi wa Utamaduni uliofanyika Forodhani Mjini Zanzibar.
Amesema Nchi nyingi duniani huingiza mapato kutokana na utalii ambao kwa kiwango kikubwa hutegemea vivutio vinavyotokana na urithi wa utamaduni.
Dkt Amina ameeleza kuwa Utalii huchangia na kuongeza pato la Wananchi kutokana na kuuza bidhaa na huduma mbalimbali kwa watalii zinazotokana na Urithi wa Utamaduni zikiwemo Sanaa, Mikoba na Milango.
Amesema kukamilika kwa Sera hiyo na utekelezaji wake kutawezesha watu kutambua na kuthamini utu wao, historia na utamaduni wao jambo ambalo litapelekea watu hao kuamua kuyalinda maeneo ya Uhifadhi na utamaduni wao.
“Watu hufurahia kushuhudia Urithi wa Utamaduni wenye mahusiano na historia ya jamiii mablimbali kama vile maendeleo ya sayansi, mabadiliko ya sura ya nchi na viumbe,aina ya uburudishaji,ukarimu, huba na maisha ya watu kwenye maeneo hayo” Alisema Dkt Amina.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Uendeshaji na Utumishi wa Wizara ya Habari Utamaduni Utalii na Michezo Joseph Kilangi amesema kukamilika kwa Sera ya Urithi wa Utamaduni kutaisaidia Serikali kuanzisha Utalii wa Utamaduni wa Zanzibar ambao utakuwa ni kivutio kwa Wenyeji na Wageni mbalimbali nchini.
Amesema hatua hiyo ni miongoni mwa jitihada mbali mbali zinazofanywa na Serikali katika kuimarisha Sekta hiyo ambayo ndio tegemeo la Uchumi wa nchi.
Amesema Zanzibar ina utamaduni wake ambao unatofautiana na Nchi nyingine hivyo ipo haja ya Utamaduni huo kuenziwa na kufanywa uwe kivutio kwa Wageni ili waweze kuja nchini kwa ajili ya kujionea utamaduni huo.
“Zanzibar tuna utamaduni wetu wa Asili ikiwemo Mavazi, Tabia njema, Ukarimu, kupendana,amani na utulivu,mambo ambayo tukiyaratibu vyema katika Sera hii itakuwa kivutio cha Utalii’’ Alisema Mkurugenzi Kilangi.
Kwa upande wao Washiriki wa Semina hiyo wameipongeza Serikali kwa uamuzi wake na kuomba kufanyika kwa majadiliano mapana kutoka kwa Wadau mbali mbali hasa wa Vijijini ambao pia Sera hiyo inawahusu.
Hata hivyo Wachangiaji hao wameiomba Idara ya Makumbusho ambao ndio Wasimamizi wakuu wa Sera hiyo kuhakikisha Sera hiyo haipingani na Sera nyingine.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »