WASUSIA SHUGHULI ZA MAENDELEO BAADA YA LAMBALAMBA KUFUKUZWA KIJIJINI.

April 14, 2014
NA HAMISI RAMADHANI,MKINGA.
 
 BAADHI ya wakazi wa Kata ya Mhinduro iliyopo wilaya ya Mkinga mkoani Tanga wamesusia kushiriki katika shughuli zote za maendeleo huku wengine wakitishia kurudisha kadi za Chama cha Mapinduzi (CCM) kufuatia serikali kupiga marufuku shughuli za kundi la watu wanaodaiwa kufichua wachawi maarufu kama Lambalamba.
 
Hasira hiyo imefuatia baada ya wananchi wanaoishi katika vijiji vilivyomo ndani Kata hiyo  kuchanga fedha zaidi ya shilingi laki nane kwa ajili ya kuwaleta Lambalamba kwenye maeneo yao ili aweze kuwaondolea kero ya vitendo vya kishirikina ambavyo wamedai kuwa vimekuwa vikichangia kurudisha nyuma jitihada zao za kujiletea maendeleo.
 
Zoezi la mgomo dhidi ya shughuli zote za maendeleo limeingia siku ya saba tangu kundi hilo la Lambalamba kupigwa marufuku na serikali ili kuzuia uvunjifu wa amani unaoweza kujitokeza miongoni mwa jamii.
 
Kutokana na mgomo huo Mkuu wa wilaya ya Mkinga Mboni Mgaza alijikuta akihutubia watoto wadogo na watumishi wa serikali tu  kwenye sherehe za zoezi la upandaji miti zilizofanyika katika Kijiji cha Churwa wilayani humo baada ya wananchi kukataa kutoka majumbani mwao.
 
“Mheshimiwa Mkuu wa wilaya hii iliyojitokeza leo ndiyo hali halisi iliyopo hapa Kijijini tangu serikali ilipopiga marufuku kuendelea kwa zoezi la Lambalamba wananchi hawa wamekuwa wakikataa kushiriki shughuli zote za maendeleo “,alisema Anthon Mlola Mwenyekiti Serikali Kijiji cha Churwa.
 
Akielezea hatua hiyo baada ya wananchi kususia mkutano wake pamoja na shughuli za maendeleo  Mkuu wa wilaya ya Mkinga Mgaza alisema serikali itaendelea na msimamo wake wa kupiga marufuku watu hao wanaojiita ni watoa uchawi ikiwa ni hatua moja wapo ya kupingana na vitendo vinavyoashiria uvunjifu wa amani.
 
“Pamoja na mgomo huo lakini niwaombe wananchi watambue kuwa serikali haitakubaliana na maamuzi hayo ya kuwaleta lambalamba na kusababisha uvunjifu wa amani hivyo nawaomba viongozi wa Kamati ya ulinzi na usalama kwa ngazi zote kuhakikisha wanaendelea kusimamia agizo hili la kupiga marufuku vikundi vya aina hii”,alisema Mgaza.
 
 
Kufuatia hatua hiyo Askari Mgambo na wale wa kutoka kikosi cha 838 KJ cha Maramba JKT walilazimika kushiriki zoezi la upandaji miti ambapo zaidi ya miti 39,000 ilipandwa katika misitu mitatu ya hifadhi ya asili wilayani humo.
 

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »