MAISHA BORA HAYAPATIKANI KWA KUKAA VIJWENI-KISAUJI.

December 17, 2013
IMEWEKWA DESEMBA 17,2013 SAA 2:15.
Na Oscar Assenga,Tanga.

MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (MNEC) wilaya ya Tanga,Salim Kassim Kisauji amesema maisha bora kwa kila mtanzania yataenda na ufanyaji wa kazi na sio kukaa vibarazani kwa kupiga soga.


Kisauji ambaye pia ni Meya  wa zamani wa Jiji la Tanga alitoa kauli hiyo wakati akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika kata ya Ngamiani kusini ikiwa ni ziara ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana Mkoa wa Tanga(UVCCM) Abdi Makange wilayani hapa ulioendana sambamba na ufunguzi wa matawi.


Kisauji alisema watanzania wengi wamejijengea mazoea ya kuacha kufanya kazi kwa bidii badala yake wamekuwa wakitumia muda mwingi kukaa vijiweni na kusema wanamaisha magumu huku wakiacha kutumia vema fursa zilizopo ili kuweza kujipatia maendeleo.


Alisema kutokana na hali hiyo vijana wengi wameacha kufanya kazi na kugeuka kuwa omba omba kitendo ambacho ni hatari kubwa sana hasa katika mustakabali wao na jamii zinazowazunguka.


    “Mara nyingi mnadanganyika kwa kuambiwa vijana mnatekelezwa sio kweli tokeni sasa fanyeni kazi kwa bidii na matunda yake mtayaona lakini kama mkiendelea kukaa vijiweni kila siku maisha yatakuwa  magumu kwenu “Alisema Kisauji.


Aidha aliwataka wazazi na walezi mkoani hapa kuwahimiza vijana wao kuacha kukaa mitaani badala yake watoke wakafanye kazi ili waweze kujiongezea pato ambalo litasaidia jamii zao kujikwamua kimaisha.


Akizungumzia suala la watendaji wa wazembe,Kisauji alisema dawa yao iko jikoni kwa kuhakikisha wanawashughulikia ipasavyo lengo likiwa ni kuwa na watendaji wenye kujua wajibu wa kutekeleza majukumu yao kwa wananchi na sio vyenginevyo.


Aidha aliwataka madiwani kuhakikisha wanalisimamia kikamilifu suala la mikopo ya vijana na wakina mama asilimia 10 inayotokana na makusanyo ya halmashauri kila mwezi ili yaweze kufika kwa walengwa waliokusudiwa.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »