“African Sports kuchagua viongozi wake Agosti 15 mwaka huu”.

June 20, 2013

Na Oscar Assenga, Tanga.
MABINGWA wa Ligi kuu Tanzania Bara mwaka 1988 African Sports “Wanakimanumanu” inatarajiwa kufanya mkutano mkuu wa uchaguzi Agosti 15 mwaka huu baada ya uongozi wa muda uliopo madarakani kumaliza wakati wake.

Akizungumza na blog hii, Katibu Mkuu wa Klabu hiyo, Khatibu Enzi alisema uchaguzi huo unafanyika kutokana na kuongozwa na viongozi wa muda hivyo wakapendekeza kuitishwa mkutano huo ambao utatoa mwelekeo wa kuwapata watendaji wapya ambao watakuwa na jukumu la kuingoza klabu hiyo.

Enzi alisema fomu za kuwania nafasi katika uchaguzi huo zitaanza kutolewa kuanzia Julai 2 mwaka huu kwenye makao makuu ya klabu hiyo zilizopo barabara 12 jijini Tanga baada ya kikao cha kamati ya utendaji wanachama wao.

Katibu huyo alizitaja nafasi ambazo zitagombewa katika uchaguzi huo kuwa ni nafasi ya mwenyekiti, makamu mwenyekiti, katibu mkuu, katibu msaidizi, mweka hazina na msaidizi wake huku nafasi kumi za wajumbe watakaounda kamati ya utendaji wa klabu hiyo nazo zikiwaniwa.

Aidha katibu huyo alisema kuelekea uchaguzi huo wanatarajiwa kutoa fomu mpya za uanachama kwa wanachama wapya ambao wanataka kujiunga na klabu hiyo ambazo zitatoka kuanzia June 22 mpaka Julai 30 mwaka huu.

Mwisho.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »