
Na: OWM – TAMISEMI, Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameelekeza waliokuwa wafanyabiashara 30 wa soko la ndizi Mabibo (Mahakama ya Ndizi) kurejea kufanya biashara kwa udhamini wa maandishi kutoka ofisi za Serikali za Mitaa.
Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Agosti 31, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi Ndogo ya OWM- TAMISEMI jijini Dar es Salaam, mara baada ya kupokea taarifa ya timu ya ufuatiliaji wa malalamiko ya wafanyabiashara hao wa soko la ndizi Mabibo, wakati wa kikao kazi chake na wafanyabiashara hao.
Aidha, Prof. Shemdoe ameilekeza Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo kufanya tathmini ya mali ya Bw. Frego Njovu aliyewasilisha madai ya kuomba kurejeshewa fedha alizotumia kukarabati choo kilichopo sokoni hapo ambacho alikuwa akikisimamia.
Katika kuhakikisha haki inatendeka, Prof. Shemdoe ameelekeza bidhaa za mfanyabiashara Bw. Enock Kimwayeya aliyekuwa Mwenyekiti wa Wafanyabiashara waliowasilisha malalamiko kwa Prof. Shemdoe, arejeshewe bidhaa zake alizoziacha kwenye kibanda cha biashara pindi alipoondolewa, kwani taarifa ya timu ya ufuatiliaji imeainisha kuwa Halmashauri imekiri kwamba bidhaa za mfanyabiashara huyo zipo.
Ili kuimarisha usimamizi wa soko, Prof. Shemdoe amemuelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo kumpeleka meneja wa soko mwingine kulisimamia soko hilo na aliyepo kupangiwa majukumu mengine.
Maelekezo hayo ya Prof. Shemdoe yametokana na maafikiano baina ya pande zote katika kikao kazi cha Waziri huyo na walalamikaji (wafanyabiashara) na walalamikiwa ambao ni Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo.
Malalamiko ya wafanyabiashara hao 30 yaliwasilishwa kwa Prof. Shemdoe kupitia andiko lao la tarehe 15/01/2026 lililohusu Sakata la soko la Ndizi Mabibo wakilalamikia kupigwa marufuku kuingia sokoni, kutaifishwa na kuuzwa kwa maeneo yao ya biashara, aidha Manispaa ya Ubungo iliwaondoka sokoni wafanyabiashara hao kwa tuhuma za kuhamasisha vurugu na kutoitambua manispaa hiyo kama msimamizi wa soko.

EmoticonEmoticon