WALIMU 3,153 WASHIRIKI SHINDANO LA STADI ZA UFUNDISHAJI

June 02, 2026


Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetangaza kuwa jumla ya walimu 3,153 wamejisajili kushiriki Shindano la Taifa la Nne la Stadi za Ufundishaji kwa Walimu wa Shule za Awali na Msingi pamoja na Shindano la Pili la Stadi za Ufundishaji kwa Walimu wa Shule za Sekondari Tanzania Bara,ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuendelea kuimarisha ubora wa ufundishaji na ujifunzaji nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 2, 2026, jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Hafidh Ameir, amesema kuwa hafla ya utoaji wa zawadi kwa washindi wa mashindano hayo itafanyika Juni 6, 2026 katika Ukumbi wa Maktaba Mpya wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Amesema mashindano hayo yanatoa fursa kwa walimu kuonesha umahiri wao wa kitaaluma, ubunifu na matumizi ya mbinu bora za ufundishaji darasani, huku yakitumika pia kama sehemu ya utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Mafunzo Endelevu ya Walimu Kazini (MEWAKA).

"Kati ya walimu 3,153 waliosajiliwa kupitia Mfumo wa National Teaching Skills Competition System (TSCS), walimu 1,263 walitimiza masharti yote ya ushiriki kwa kuwasilisha video za ufundishaji pamoja na maandalio ya masomo kwa ajili ya tathmini."amesema Mhe.Ameir

Amesema mchakato wa tathmini umekamilika na tayari orodha teule ya walimu watano bora imepatikana katika kila eneo la ushindani, huku mgeni rasmi katika hafla ya utoaji wa zawadi akitarajiwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe.

Mhe. Ameir ameeleza kuwa mshindi wa kwanza katika kila kundi atazawadiwa Shilingi milioni 2.5, cheti cha pongezi, cheti cha ushindi pamoja na kompyuta mpakato. Aidha, shule anayofundisha mshindi huyo itapatiwa projekta kwa ajili ya kuimarisha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji.

Katika hatua nyingine, amesema shule zitakazotoa washindi wa kwanza katika maeneo ya Kusoma kwa Darasa la Awali, Kiingereza kwa Darasa la Kwanza na Ufaraguzi wa Zana kwa Darasa la Pili zitapatiwa vibao vya kielektroniki 100 vyenye thamani ya Shilingi milioni tano.

Serikali inaendelea kutumia mashindano hayo kama nyenzo ya kuhamasisha ubunifu, kuongeza ari ya utendaji kwa walimu na kuibua mbinu bora za ufundishaji zitakazochangia kuinua viwango vya elimu nchini.

Kaulimbiu ya shindano la mwaka huu ni “UFUNDISHAJI BORA, TAIFA IMARA.

 

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »