
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, tarehe 21 Oktoba, 2025 Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo, amesema mafanikio hayo yametokana na operesheni zilizofanyika katika kipindi cha mwezi Septemba na Oktoba 2025 katika maeneo mbalimbali nchini.
Kamishna Jenerali Lyimo amesema katika operesheni iliyofanyika eneo la Kariakoo, Dar es Salaam, Mamlaka ilikamata dawa za kulevya aina ya mirungi zenye uzito wa kilogramu 40.32 zilizokuwa zimekaushwa na kufungwa kama viungo (spices) katika paketi 80 zenye maandishi ya “Dry Basil Leaves”. Dawa hizo zilikuwa zikisafirishwa kwenda nchini Canada na Italy kupitia makampuni ya usafirishaji.
Ametaja waliokamatwa kuhusiana na dawa hizo kuwa ni Yusuphu S. Kibaha (35) na Mohamed H. Ramadhan (41), na uchunguzi wa awali umebaini dawa hizo ziliingizwa nchini kwa njia za kificho kutoka nchi jirani.
“Uchunguzi wetu umeonesha uwepo wa mtandao wa usafirishaji wa mirungi unaotumia bodaboda na baadhi ya mawakala wa kampuni za usafirishaji ili kurahisisha kusafirisha dawa hizo bila kutiliwa shaka. Mtandao huu unaweza kuathiri taswira ya nchi yetu kimataifa, na sisi hatutalifumbia macho suala hili” alionya Kamishna Jenerali Lyimo.
Katika tukio jingine lililofanyika eneo la Mlalakuwa, Kinondoni, Mamlaka iliwakamata watuhumiwa wanne wakiwa wanatengeneza biskuti za bangi kwa ajili ya house party ya wanafunzi wa vyuo vikuu. Watu hao ni Bright A. Malisa, Humphrey G. Safari, Novatus A. Kileo, na Chriss P. Mandoza, wote wakiwa na umri wa miaka 26.
“Watuhumiwa hao walikutwa na biskuti 140 za bangi, puli nane, na paketi tisa za bangi zenye jumla ya kilo 2.858. Hii inaonesha namna vijana wetu wanavyohatarisha maisha yao kwa kujihusisha na utengenezaji wa bidhaa zenye dawa za kulevya kwa ajili ya starehe,” alisisitiza Lyimo.
Aidha, amesema Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya inaendelea na uchunguzi wa matumizi ya bangi kwenye bidhaa mbalimbali ikiwemo vinywaji, vyakula, vipodozi na sigara za kielektroniki (vapes), ambapo baadhi ya bidhaa zimebainika kuwa na viambata vya bangi.
Akizungumzia operesheni zilizofanyika mikoani, Lyimo alisema DCEA kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama imefanikiwa kukamata bangi kilo 9,164.92, mirungi kilo 1,555.46, skanka gramu 367, na heroin gramu 7.498, pamoja na kuteketeza ekari 11.5 za mashamba ya bangi.
Aidha, amewaonya bodaboda, wamiliki wa kampuni na mawakala wa usafirishaji kuwa makini na mizigo wanayobeba au kusafirisha ili kuepuka kujikuta kwenye mgogoro wa kisheria. Pia ametumia fursa hiyo kuwaonya wanafunzi wa vyuo vikuu kuacha mara moja kujihusisha na dawa za kulevya na badala yake kutumia muda wao katika masomo ili kutimiza ndoto zao.
“Vijana wetu ndio nguvu kazi ya taifa. Tunataka waishi maisha yenye afya, wasikubali kudanganywa na makundi yanayotumia dawa za kulevya kama sehemu ya starehe. Mamlaka haitasita kuchukua hatua kali kwa yeyote atakayehusishwa na uhalifu huu,” alisisitiza Lyimo.
EmoticonEmoticon