div class="separator" style="clear: both; text-align: center;">
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Financial Intelligence Unit (FIU) zimesaini hati ya makubaliano ya kubadilishana taarifa (Data Sharing Agreement), hatua inayolenga kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa na utakatishaji fedha haramu nchini.
Hafla ya kusaini makubaliano hayo imefanyika leo Septemba 24,2025 katika Makao Makuu ya TAKUKURU jijini Dodoma, ikihudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Francis Chalamila na Kamishna wa FIU, Bw. Majaba Shabani Magana pamoja na wakurugenzi kutoka taasisi hizo.
Akizungumza katika tukio hilo, Bw. Chalamila amesema hatua hiyo ni mwendelezo wa ushirikiano wa muda mrefu kati ya taasisi hizo mbili, ulioanza tangu kusainiwa kwa makubaliano ya ushirikiano (MoU) mwaka 2015.
“Makubaliano haya mapya yanayohusu ubadilishanaji wa taarifa ni utekelezaji wa matakwa ya Sheria ya Serikali Mtandao ya mwaka 2023, ambayo inazitaka taasisi zinazoshirikiana kuhakikisha zinasaini Data Sharing Agreement endapo zitahusiana katika kubadilishana taarifa,” amesema Bw. Chalamila
Aidha amefafanua kuwa madhumuni makuu ya makubaliano hayo ni kurahisisha na kuwezesha ubadilishanaji wa taarifa kati ya TAKUKURU na FIU ili kuongeza ufanisi wa uchunguzi na udhibiti wa vitendo vya rushwa na utakatishaji fedha haramu.
Bw. Chalamila alisema kwa kipindi cha mwaka 2022 hadi 2025, TAKUKURU imepokea taarifa fiche 47 za miamala yenye mashaka kutoka FIU, ambapo kati yake 36 zilifanyiwa uchunguzi. Aidha, kwa miaka ya 2023 hadi 2025, TAKUKURU iliomba taarifa 141 kutoka FIU kwa ajili ya kusaidia uchunguzi mbalimbali.
“FIU imekuwa msaada mkubwa katika kufanikisha uchunguzi wetu. Ushirikiano huu umewezesha chunguzi kufanyika kwa wepesi na kwa matokeo chanya,” amesema .
Aidha, ametoa wito kwa wadau wengine kuendelea kushirikiana na TAKUKURU ili kufanikisha azma ya taifa ya kupambana na rushwa.
“Tunasisitiza kuwa kila Mtanzania akitimiza wajibu wake, tunaweza kutokomeza tatizo la rushwa nchini. Ndiyo maana kaulimbiu yetu inasema: Kuzuia Rushwa ni Jukumu Lako na Langu; Tutimize Wajibu Wetu,” amesisitiza Bw. Chalamila.
Kwa upande wake, Kamishna wa Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu (FIU), Bw. Majaba Magana, amesema kuwa hatua hiyo itasaidia kutatua changamoto ya ukosefu wa mfumo wa kitaifa wa kielektroniki wa kuhifadhi takwimu za uhalifu.
Bw.Magan amebainisha kuwa awali takwimu hizo hazikuwa na muunganiko wa moja kwa moja, jambo lililosababisha kutosomana na hivyo kukwamisha juhudi za kupata picha kamili ya mwenendo wa uhalifu wa kifedha nchini.
EmoticonEmoticon