NCHI 23 WASHIRIKI JUKWAA LA TASNIA YA UFUGAJI KUKU NA NDEGE WAFUGWAO, DK.BITEKO ATOA MAAGIZO NA KUTAJA FURSA

October 18, 2024


Na Said Mwishehe, Michuzi TV

SERIKALI imesema uwepo wa Jukwaa la Tasnia ya Kuku na Ndege wafugwao katika nchi za Kusini mwa Afrika utasaidia kuweka mazingira mazuri zaidi ya ufugaji sambamba na kuboresha maisha ya wananchi kwani Takwimu zinaonesha Kaya asilimia 55 nchini zinajihusisha na ufugaji kuku.

Akizungumza wakati akifungua mkutano wa siku mbili wa Tasnia ya Kuku na Ndege wafugwao katika nchini hizo uliohusisha wadau mbalimbali Naibu Waziri Mkuu Dk.Dotto Biteko amepongeza uwepo wa jukwaa hilo na kutumia nafasi hiyo kueleza kuwa Serikali inayoongozwa na Rais Dk.Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha kuwa Watanzania wanapata fursa ya kueleza katika ufugaji kuku.

Dk.Biteko aliyekuwa amemuwakilisha Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango katika mkutano wa Jukwaa hilo ambalo limekutanisha washiriki kutoka nchi 23 amesema ufugaji wa kuku na ndege wafugwao una faida katika kuchangia usalama wa chakula na kuongeza pato la Taifa kikanda na kimataifa.

“Asilimia 55 ya kaya nchini na katika nchi mbalimbali zinajihusisha na ufugaji kuku na wanaojihusisha zaidi ni wanawake na Vijana na kwa upande wa Tanzania kuna kuku Milioni 103.1 wakiwemo kuku wa asili na wa kısasa,”amesema na kutoa maagizo kwa Wizara ya Mifugo ba Uvuvi kuanzisha mashamba ya kuku wazazi kwa ajili ya kupata vifaranga, maabara na Viwanda vya kutengeneza vyakula vya kuku.

Pia ametoa rai kwa wadau wote wa ufugaji wa kuku kuendelea kushirikiana na Serikali kutekeleza majukumu yao kwa kuwa Serikali imetoa fursa kwa kila mmoja kuweza kujishughukisha na kujiongezea kipato.

Awali Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema kuwa kufanyika kwa mkutano huo ni matokeo ya mkutano wa AGRA uliofanyika Dar es Salaaam na kuongozwa na Rais Dkt. Samia ambapo AGRA walielezwa kuhusu kuipa kipaumbele sekta ya ufugaji wa kuku kwa kuwa nchini Tanzania familia nyingi zinafuga kuku.

“ Tunawashukuru AGRA na Food Alliance kwa kutukubalia na ndio maana leo jukwaa la kwanza limefanyika hapa Tanzania na kutoa fursa kwa wafugaji wetu kujifunza na kujenga mahusiano,” amesema Waziri Ulega na kueleza takwimu zinaonesha kuwa ifikapo 2030 tasnia ya kuku itachangia asalimia 41 ya protini na kuwa watafiti nchini.

Kuhusu tafiti zinazofanywa na watafiti katika sekta ya kuku na Ndege wafugwao amesema ni vema wanaofanya tafiti wakawa wanashirikiana na Wizara hiyo ili kuwa tafiti ambazo hazitazua taharuki.

“ Kuna waatafiti walifanya utafiti kwa kutumia sampuli chache juu ya ulishaji wa kuku wanaofugwa na akina mama na vijana tafiti ile ilileta taharuki, kupitia mkutano huu Naibu Waziri Mkuu utumie fursa ya kueleza hilo kuwaambia watafiti washirikiane na Wizara ili kutotoa taarifa za taharuki kwa jamii ….

“Na kuwa Serikali inaweza kudhibiti wafugaji wasiofuata taratibu hivyo tusiharibu jitihada zinazofanywa na kukuza tasnia hii inayosaidia wafugaji wetu katika kujipatia kipato na kufanya kuwa ajira” amesema Ulega na kuongeza wanaheshimu na kuthamini kazi zao ila wanapofanya tafiti na kupeleka kwa jamii ni vema kukawa na mkakati wa pamoja wa kufikisha tafiti hizo kwa wananchi.

Kwa upande wake Waziri Mkuu wa zamani wa Ethiopia na Mwenyekiti wa Bodi ya Muungano wa Mapinduzi ya Kijani barani Afrika (AGRA), Dkt. Hailemariam Dessalegn, amesema fursa muhimu zilizopo kupitia ufugaji wa kuku ni chanzo cha protini, soko la uhakika na ajira kwa vijana na ka kushiriki katika mnyororo wa thamani.

“Jukwaa hili linatoa fursa ya kujifunza faida na changamoto katika tasnia hii na kuongeza ushirikiano. Kukuza tasnia hii katika nchi yetu inahitaji majukwaa kama haya na inahitaji utayari wa wadau mbalimbali kwa kuwa wana uwezo wa kuwekeza ili kukuza tasnia hii,” amesema Mhe. Dessalegn.

Amefafanua kwamba Tanzania ni kinara wa kuwa na njia shirikishi na ni imani yake itaendelea hivyo chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ili kufikia ajenda ya Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), haswa dhamira ya kumaliza njaa na umasikini ifikapo 2030.

Wakati huo huo Mfugaji wa kuku kutoka mkoani Tanga, Omary Mussa amesema kuwa ameanza ufugaji kupitia miradi mbalimbali na baada ya mafunzo amekuwa mfugaji tangu mwaka 2023 akianza na kuku 500 na sasa anafuga kuku 4,000 aina ya chotara na kuku wa kisasa.

“ Tanzania kufuga kuku ni utamaduni wetu tuna kazi ya kubadilisha kutoka kuwa tamaduni kuwa kibiashara nimeanzisha Kampuni ya Kuku Pesa Investment Group ili watu wafuge kuku kupata pesa,” amesema Mussa.

Kwa upande wa Grace Gondwe ambaye ni Mfugaji wa kuku nchini Malawi amesema baada ya kumaliza Chuo Kikuu nchini humo alianzisha biashara ya ufugaji wa kuku wa kisasa licha ya kukutana na changamoto mbalimbali amemudu kufanya kazi hiyo kwa miaka mitano sasa.

Ametoa ushauri kwa Vijana kuendelea kufug kuku kwani kuna fursa nyingi zinazoendana na ufugaji wa kuku.





Share this

Related Posts

Previous
Next Post »