Naibu Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii avutiwa na Kamati ya Ulinzi wa Mtoto Stendi ya Nyegezi, Mwanza

August 21, 2024
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu amekagua shughuli za kamati ya ulinzi wa watoto wanaoishi mazingira magumu/ mitaani iliyopo stendi Kuu ya Mabasi Nyegezi jijini Mwanza.

Mdemu amekagua shughuli za kamati hiyo Jumanne Agosti 20,2024 akiwa kwenye mwendelezo wa ziara yake ya kukagua miradi na shughuli mbalimbali za maendeleo ya jamii mkoani Mwanza.

"Nimevutiwa sana na kamati hii, sote tukiungana na kuwajibika pamoja, tutafanikiwa kuwalinda watoto na vitendo vya ukatili wa kijinsia lakini pia kuwaondoa katika maeneo ya stendi" amesema Mdemu huku akipongeza wazo la uanzishaji wa kamati hiyo akisema linaweza kusaidia kuwa na kamati za aina hiyo katika stendi mbalimbali nchini.

Awali akiwasilisha taarifa ya utendaji kazi wa Kamati hiyo, Afisa Ustawi wa Jamii Kata ya Ngegezi, Edith Ngowi amesema tangu mwaka 2021 kamati hiyo imewaokoa watoto 297 katika stendi ya mabasi Nyegezi.

"Kwa kushirikiana na shirika la Railway children Africa na Jeshi la Uhamiaji, watoto 230 wameunganishwa na familia zao ingawa tumepata changamoto ya watoto 30 ambao wamerejea tena mitaani baada ya kuumganishwa na familia zao huku wengine wakitoa taarifa ambazo si sahihi na hivyo kushindwa kuwapata ndugu zao" amesema Ngowi.

Aidha Ngowi amebainisha kuwa watoto hao wamekuwa wakifika stendi kwa njia mbalimbali ikiwemo kudandia malori na mabasi kutoka mikoani huku wengine wakitumikishwa kazi za usafi wa kuosha magari hayo kwa ujira mdogo wa hadi shilingi 500.

"Hali hiyo inawashawishi kuvutiwa kubakia stendi hivyo tunaendelea kutoa elimu kwa makondakta kuacha kuwatumia watoto hasa wa kiume kwenye kazi za kuosha magari" amesema Ngowi akibainisha kuwa wengi wana umri kati ya miaka saba hadi 14.

Kamati hiyo inaundwa na viongozi mbalimbali wakiwemo maafisa maendeleo ya jamii, wenyeviti wa Serikali za mitaa, polisi, uongozi wa stendi ya Nyegezi, wafanyakazi kwenye mabasi na shirika la kutetea haki za watoto wanaoishi mazingira magumu la Railway Children Africa ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa afua za Jukwaa la Kizazi Chenye Usawa chini ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum.
Na George Binagi- GB Pazzo, BMG
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu akizungumza na kamati ya ulinzi wa mtoto stendi ya Nyegezi jijini Mwanza.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu akizungumza na kamati ya ulinzi wa mtoto stendi ya Nyegezi jijini Mwanza.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu akizungumza na kamati ya ulinzi wa mtoto stendi ya Nyegezi jijini Mwanza.
Afisa Ustawi wa Jamii Kata ya Ngegezi, Edith Ngowi akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa kamati ya ulinzi wa mtoto Stendi ya mabasi Nyegezi jijini Mwanza.
Baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi wa mtoto Stendi ya mabasi Nyegezi jijini Mwanza.
Baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi wa mtoto Stendi ya mabasi Nyegezi jijini Mwanza.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu (katikati) akiwasili Ngudu wilayani Kwimba kuendelea na ziara ya kukagua afya mbalimbali zinazotekelezwa na Wizara hiyo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »