VIWANDA 7 VYA KUCHAKATA MAZAO YA ASALI VYAJENGWA

February 02, 2024





Na. Anangisye Mwateba- Dodoma

Serikali imewezesha ujenzi wa viwanda saba (7) vya kuchakata na kufungasha asali katika Wilaya za Sikonge, Mlele, Nzega, Tabora, Manyoni, Kibondo na Bukombe vitakavyotumika kuongezea thamani asali inayozalishwa na kuuzwa katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Haya yamebainika wakati Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dunstan Kitandula(Mb) akijibu swali la Mhe. Athuman Almas Maige Mbuge wa Tabora Kaskazini katika kikao cha cha tatu cha Mkutano wa 14 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaondelea jijini Dodoma aliyetaka kujua Je Serikali ina mpango gani wa kufanya asali kuwa moja ya zao la kimkakati?

Mhe. Kitandula aliongeza kuwa ufugaji nyuki ni moja ya shughuli muhimu za kijamii, kiuchumi na kiutamaduni kwa makabila mengi hapa nchini, Afrika na katika maeneo mengi duniani.
- Advertisement -


Aidha, ufugaji nyuki una mchango mkubwa katika kuhakikisha usalama wa chakula kupitia uchavushaji. Ufugaji Nyuki ni miongoni mwa shughuli za kiuchumi hasa kwa jamii inayoishi kando kando na maeneo yaliyohifadhiwa.

‘Kwa kutambua umuhimu wa shughuli hii, Serikali imechukua hatua kadhaa za kufanya asali kuwa zao la kimkakati. Hatua hizo ni pamoja na: Kuimarisha mifumo ya usimamizi pamoja na kutunga na kutoa miongozo mbalimbali inayohusu ufugaji nyuki; kuwezesha wafugaji nyuki kwa kuwapatia mizinga ya kisasa. Mathalan katika kipindi cha miaka mitano (5) iliyopita zaidi ya mizinga ya kisasa 64,593 imetolewa kwa vikundi vya wafugaji nyuki kutoka katika mikoa mbalimbali”. Mhe. Kitandula alisema.

Mhe. Kitandula aliongeza kuwa Serikali inatekeleza programu na miradi mbalimbali ya kuwezesha kuongeza uzalishaji wa asali sambamba na kutafuta masoko mapya ya asali katika nchi za Umoja wa Ulaya na Asia.

Pia aliongeza kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau wa Maendeleo inatekeleza mradi wa kuwezesha ufugaji nyuki katika mikoa mitano (Tabora, Singida, Katavi, Kigoma na Shinyanga) kwa upande wa Tanzania Bara na Kisiwa cha Pemba kwa upande wa Zanzibar.

Vilevile, Serikali inakamilisha Mpango wa Kuendeleza Sekta ya Ufugaji Nyuki ambao utachochea uzalishaji, mauzo ya asali nje ya nchi pamoja na ajira hasa kwavijana na wanawake.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »