RPC MALLYA AWATAKA WAUMINI WA KANISA LA MORAVIANI USHIRIKA WA SONGEA KUTOKUJIINGIZA KWENYE MADENI MAKUBWA

February 04, 2024





Na Issa Mwadangala

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe Kamishna Msaidizi wa Polisi Theopista Mallya amewataka waumini wa Kanisa la Moraviani Ushirika wa Sogea Mjini Tunduma kutojiingiza kwenye madeni makubwa ambayo hupelekea madhara ya msongo wa mawazo baada ya kushindwa kulipa madeni hayo.

Akizungumza Februari 04, 2024 na waumini wa kanisa Moravian kwa Mchungaji Emmanuel Silungwe wakati wa ibada ya jumapili Kamanda Mallya amesema madeni makubwa ni changamoto kwani husababisha msongo wa mawazo.

“Kitendo cha baadhi ya waamini kukopa mikopo mikubwa ambayo wanashindwa kumudu malipo yake kinapelekea kuwa na msongo wa mawazo na baadhi yao kujiua” alisema Kamanda Mallya.

Aidha, Kamanda Mallya amewaomba waamini wa kanisa hilo kuwa mabalozi wa kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto pamoja na kuacha vitendo vingine visivyompendeza Mwenyezi Mungu.

Sambamba na hayo amekemea suala la kuomba na kupokea rushwa jambo ambalo ni kosa kisheria lakini halimpendezi Mwenyezi Mungu kwani kuomba au kutoa rushwa kunapoteza haki ya mtu mwingine ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha waamini hao haki ya dhamana Kwa watuhumiwa pindi wanapolalamika kuwa mhalifu akikamatwa anaachiwa na Polisi vilevile alitoa elimu juu ya mgawanyo wa utendaji wa kazi za serikali kati ya Jeshi la Polisi, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na Mahakama.

Kwa upande wao waamini wa Kanisa hilo wamelipongeza Jeshi la Polisi kwa ushiriki wao katika ibada hiyo na kutoa elimu ambayo ni sehemu ya mafundisho mema ikiwa ni pamoja na kufanikisha zoezi la harambee la kupaua jengo la ofisi ya Kanisa hilo ambalo ujenzi wake bado unaendelea.

Utoaji huo wa elimu katika nyumba za ibada ni mkakati wa Jeshi la Polisi kuhakikisha viongozi wa dini wanakuwa sehemu ya kuukataa uhalifu nchini na kutumia nafasi zao katika mahubiri kutoa elimu na kukemea vitendo viovu katika jamii.


Share this

Related Posts

Previous
Next Post »