WATUMIAJI WA BARABARA WASHAURIWA KUTOTUMIA VIVUKO VILIVYOZUILIWA

January 31, 2024




Dar es Salaam

Watumiaji wa barabara mkoani Dar es Salaam wameshauriwa kutotumia barabara au vivuko ambavyo vimewekwa vizuizi katika kipindi hiki ambacho mvua zinaendelea kunyesha nchini.

Wito huo umetolewa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam Mhandisi Geofrey Mkinga wakati wa ukaguzi wa madaraja ya Luhufi na Tanganyika katika Wilaya ya Kinondoni.

Mhandisi Mkinga amesema katika kipindi cha mvua barabara nyingi huharibika zaidi na usalama kuwa mdogo hivyo wanaweka vibao watu wasipite au wapite kwa tahadhari kwa maana barabara ni nyembamba

“Kwa kipindi hiki cha mvua, barabara nyingi zinakuwa zimeharibika hivyo tunapoona usalama ni mdogo huwa tunaweka alama za tahadhali, kwa hiyo tunaomba watumiaji wa barabara wazingatie hizo alama” Alisisitiza Mhandisi Mkinga.

Ameongeza kusema kwamba kumekuwa na tabia kwa baadhi ya watu kutaka kupita kwa ngazi au magogo vitendo ambavyo ni hatarishi.

“Tunafahamu hali ilivyo kwenye daraja hadi kufikia hayo maamuzi hivyo vile tulivyoweka alama wasijaribu kupita kwani sio salama”. Amesisitiza.

Akitolea mfano wa daraja la Msumi-Madale ambalo kwa sasa hivi halipitiki kabisa na limefungwa ila bado kuna majaribio ya watu kutaka kupita kwa magogo kitu ambacho ni hatarishi.

Ameongeza kusema kwamba TARURA inaenda kujenga kivuko cha kutembea kwa miguu daraja la Msumi-Madale na litawasadia kuvuka ila wasijaribu kutumia njia zingine za kupanga mawe au miti kwani ni hatari kwa kuwa mvua zinaweza kunyesha na kusababisha kingo kuanguka na hivyo kuhatarisha maisha yao.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »