WANACHAMA, WASTAAFU WAIMIMINIA SIFA PSSSF KWA HUDUMA BORA

July 06, 2023

 

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, SABASABA

WANACHAMA wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) hususan Wastaafu wameelezea kuridhishwa kwao na huduma wanazozipata hivi sasa kutoka kwenye Mfuko huo ambao Agosti Mosi, 2023 utatimiza miaka Mitano tangu uanzishwe baada ya Serikali kuunganisha Mifuko minne ya Hifadhi ya Jamii ya PSPF, PPF, LAPF NA GEPF.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti walipofika kwenye banda la PSSSF kwenye Maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam Julai 5, 2023 walisema kero zilizokuwepo miaka michache iliyopita kwa sasa hawakumbani nazo.

“Wakati nafuatilia Mafao yangu nilihudumiwa vizuri, ofisi hii imebadilika sana nawaombea kwa Mungu muendelee hivyo hivyo, nawapa hongera nyingi, nasema haya kutoka moyoni mwangu, nimefika hapa na kupata huduma kwa haraka.” Alisema Mstaafu Bw. Abdallah Mandwanga.

Bw. Amana Shomari, Mstaafu kutoka Shirika la Reli Tanzania (TRC) miaka 10 iliyopita alisema kwa upande wake huduma anazozipata kwa sasa kutoka PSSSF zimeboreka sana na zimekuwa za kutia moyo.

“Nikiwa kama Mstaafu, kilichonileta hapa sabasaba kwenye banda hili la PSSSF, ni kuhakiki taarifa zangu, nimetumia si zaidi ya dakika 5 kupata huduma, hakika nawapongeza sana, nitoe wito kwa wastaafu wenzangu zoezi la uhakiki ni muhimu kwani linaondoa ucheleweshaji wa malipo ya mafao, mimi sina tatizo na malipo yangu ya kila mwezi, napokea kwa wakati haivuki tarehe 25 pesa nakutana nayo kwenye akaunti yangu.” Alisema.

Naye Bw. Stanslaus Kagaruki ambaye naye alifika kwenye banda la PSSSF amewahamasisha wastaafu wenzake kuona umuhimu wa kuhakiki taarifa zao kwani licha ya kwamba ni takwa la kisheria lakini ni huduma inayotolewa kwa muda mfupi.

“Nimechukua muda mfupi sikutarajia, nilidhani itanichukua muda mrefu, kumbe ni dole gumba, sekunde tu nimekamilisha, hivyo nawasihi wenzangu wafike kuhakikiwa ili waendelee kupokea Pensheni bila ya kikwazo.” Alisema Bw. Kagaruki.

Akizungumzia hali ya Mfuko kwa sasa, Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba alisema Mfuko umeendelea kutekeleza majukumu yake kama yalivyo ainishwa katika sheria ya Mfuko kwa umahiri na umakini mkubwa ambapo aliyataja majukumu hayo kuwa ni Kuandikisha Wanachama, Kukusanya Michango na Kuwekeza Michango hiyo na Kulipa Mafao.

“Hadi sasa tuna wanachama 780,000 na tunakusanya Michango kwa mwaka shilingi trilioni 1.65, na tunalipa Mafao shilingi trilioni 1.6 kwa mwaka,” alifafanua CPA. Kashimba.

Akifafanua zaidi Mkurugenzi huyo Mkuu wa PSSSF alibainisha kuwa, kwa sasa kuna jumla ya wanufaika wa Mafao ya kila mwezi (Monthly Pension) wanaofikia 160,000 ambao wanaolipwa Pensheni ya jumla ya shilingi bilioni 65 kila mwezi.

“Hapa utaona jinsi Mfuko unavyochachua uchumi wa nchi kwani wazee wetu hawa wanapopokea Mafao haya wanakwenda kununua huduma na mahitaji yao mbalimbali na hivyo fedha nyingi zinawafikia wananchin huko mtaani.” Alifafanua.

Aidha Mkurugenzi huyo Mkuu wa PSSSF amedokeza kuwa, Mfuko uko mbioni kuzindua mfumo mpya wa Kidijitali utakaowezesha kushughulikia masuala yote ya mafao kwa njia ya mtandao.

“Hakutakuwa na sababu ya mstaafu kuzunguka ofisini kufuatilia mafao, mstaafu mtarajiwa atajaza maombi akiwa kwenye meza yake ofisini na taarifa atakuwa anazipata kwenye simu yake ya mkononi.

“Hii yote inafanyika katika kuhakikisha tunasogeza huduma karibu kwa wanachama wetu na wastaafu kwa ujumla ili kuwaondolea adha ya kuzunguka huku na kule kufuatilia mafao yao, tunaamini kupitia mfumo huu ndani ya muda mfupi baada ya kujaza taarifa zao zitachakatwa na muhusika atakutana na fedha zake benki,” amesema Kashimba.

CPA. Kashimba amesema kupitia mfumo huo mfanyakazi anayekaribia kustaafu ataweza kujaza taarifa zake akiwa ofisini na zikachakatwa kwenye mfumo kisha kukutana na fedha zake benki. 

Alisema mafanikio yanayoonekana hivi sasa kwa sehemu kubwa yamechangiwa na juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wake Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye tangu ameingia madarakani Serikali imeongeza ajira kwa kiwango cha juu.

Wanachama wa PSSSF ni watumishi wote wa Umma, kutoka Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na Mashirika ambayo Serikali inamiliki Hisa zaidi ya asilimia 30%, alifafanua.

“Kwa kasi hii ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuongeza ajira nchini, Mfuko unatarajia ongezeko la wanachama na kufikia elfu 40 kwa mwaka.” Alifafanua.

Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba akizungumza na Wanachama waliotembelea banda la Mfuko huo kupata huduma Julai 5, 2023.
Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa ambaye leo ameyafungua rasmi Maonesho ya 46 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, akiwa katika picha ya pamoja na wakuu wa taasisi
Mwanachama wa PSSSF (kushoto) akihudumiwa 
Mwanachama wa PSSSF (kulia) akihudumiwa 


-- Khalfan Said

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »