.........................................................................
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamisi Kigwangalla ameonana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Saudi Arabia na Kuwait pamoja na Msimamizi wa Jumuiya ya Makampuni ya Albawardi inayoendesha hoteli mbalimbali za kitalii nchini ikiwemo Hyatt Regency na Four Season Serengeti ofisini kwake Jijini Dodoma jana.
Mazungumzo hayo yaliyolenga kujadili mambo mbalimbali ya kuimarisha sekta ya uhifadhi na utalii kwa maslahi ya nchi hizo tatu. Mabalozi hao ni Bandar Abdulla wa Saudi Arabia, Mohammad Rashed Alamiri wa Kuwait na Fouad Mustafa Msimamizi wa Makampuni ya Albawardi ya Umoja wa Falme za Kirabu kwa upande wa Tanzania na Afrika ya Mashariki.
Dk. Kigwangalla aliwaomba mabalozi hao kupitia jumuiya zao za uwekezaji kuwekeza katika miundombinu ya hoteli za kitalii Jijini Dodoma na kwenye Mapori ya Akiba katika Sakiti ya Kaskazini, Kusini na Magharibi hususan Pori la Akiba la Burigi.
Naye Msimamizi wa Jumuiya ya Makampuni ya Albawardi, kwa upande wa Tanzania na Afrika ya Mashariki, Fouad Mustafa alisema jumuiya hiyo ipo tayari kutoa ushirikiano kwa Serikali ya Tanzania katika ujenzi wa miundombinu ya barabara inayounganisha Hifadhi ya Ngorongoro na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
Alisema mbali na uwekezaji uliopo hivi sasa jumuiya hiyo inajenga hoteli nyingine za kitalii tatu katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Hifadhi ya Ngorongoro na katikati ya Jijini la Arusha ambapo ameiomba Serikali kuzifungua kupitia viongozi wake wa juu pale ujenzi wake utakapokamilika hususan Mhe. Rais.