HAKIKISHENI WALIMU WANAPANDA MADARAJA - WAZIRI JAFO

January 26, 2018
Na Nteghenjwa Hosseah, TAMISEMI.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe Selemani Jafo ameitaka Tume ya Utumishi wa Walimu(TCC) kusimamia na kuhakikisha Walimu wote wanapanda madaraja kwa wakati na kwa mujibu wa Elimu zao ili kupunguza Malalamiko ya Walimu wetu Nchini.

Waziri Jafo ameyasema hayo wakati wa Ufunguzi wa Mkutano wa Wajumbe wa Kamati ya Tume za Utumishi wa Walimu za Wilaya kwa Mikoa ya Dodoma, Morogoro na Singida uliofanyika katika Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini kilichopo Mkoani Dodoma mapema leo Tarehe 26/01/2017.

Waziri Jafo alisema kuwa kumekuwa na malalamiko, manunguniko na masononeko ya muda mrefu toka kwa Walimu kuhusu suala hili ya Upandaji wa madaraja halifuati taratibu aliyeajiriwa mwaka 2000 na anaweza kuwa sawa na yule aliyeajiriwa mwaka 2008 na wengine wamejiendeleza Kielimi lakin hakuna mabadiliko yoyote madaraja yao.

‘Tume hii ifanye kazi ya kurudisha hadhi ya Walimu, iwajengee heshima na thamani yao katika Jamii, shughulikieni malalamiko yao ya Msingi madaraja yao yapande kwa kuzingatia muda waliokaa kazini, elimu yao na Utendaji wao wa kazi; Hilo lisitegemee “favour” ya Katibu wa Watumishi wa Tume waliopo katika eneo husika’

Wakato huo huo Waziro Jafo alisisitiza  wajumbe wa Kamati za Tume ya Utumishi wa Walimu kuwa Mkutano huu utumike kupeana maarifa ya kazi, jinsi gani mnaweza kufanya kazi kwa Usahihi zaidi kwa kuzingatia Sheria iliyounda TUME YA UTUMISHI WA WALIMU ya mwaka 2015 na Kanuni zake za mwaka 2016.

‘Tume hii Ndio iwe Kimbilio la Walimu, iwe tegemeo la Utatuzi wa matatizo yote ya Walimu kwa sababu Tume ya Walimu ndio muajiri wa Walimu, Inasimamia Nidhamu za Walimu na mchakato mzima unaohusi Ajira za Mwalimu awapo kazini hivyo mfanye kazi kwa Haki, mkaepuke rushwa, Mkawe na busara na Hekima katika kutatua changamoto za Walimu’ 

Aidha Waziri Jafo hakusita kuwakumbusha wajumbe wa Tume ya Utumishi wa walimu kuhusu mgawanyo wa Walimu katika halmashauri kwa kuzingatia vipindi wanavyotakiwa kufundisha na uwekaji wa takwimu sahihi za Walimu waliopo sasa, wanaotarajiwa kustaafu kwa mwaka huu na kuweka maoteo ya ajira mpya zitakazohitajika kutokana na nafasi zitakazoachwa na wale wanaostaafu hivi karibuni.

“Takwimu zisiwe za kubahatisha tena kupitia Tume hii mhakikishe mnakuwa na Takwimu sahihi kwanza za mgawanyo wa Walimu katika kila Halmashauri je mgawanyo wa walimu waliopo Malinyi ni sawa na mgawanyo wa Walimu waliopo Manispaa sio Mwalimu wa Manispaa anafundisha vipindi viwili kwa wiki wakati anatakiwa kufundisha 20 na pia mahitaji ya walimu kulingana na masomo wanayofundisha maoteo kwa kuzingatia idadi ya wale wanaostaafu” Alisema Jafo.

 Waziri Jafo alimalizia hotuba yake kwa Tume hiyo kufanya tadhimini  ya kina  kuhusu maadili ya waalimu  na wanafunzi na kwa waalimu wanaovunja Sheria, Kanuni na maadili  ya kazi ya waalimu  ikiwemo uzembe , utoro kazini, rushwa na uhusiano wa kimapenzi na wanafunzi wachukuliwe hatua za kinidhamu.

Naye Mwenyekiti wa Tume ya  Utumishi wa Walimu Ndg.Oliva Mhaiki alisema wajumbe wa kamati za TSC Wilaya waliteuliwa rasmi na Tume katika mkutano wa Tar 20-25/02/2017 na tangu walipoteuliwa na kuanza kutekeleza majukumu yao hawakuwahi kupewa mafunzo yeyeote hivyo Sekretariet imeona upo umuhimu wa kufanya mkutano wa kazi kwa lengo la kuelekezana wajibu na majukumu yao kama kamati.
 Waziri WA Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe.Selemani Jafo akifungua Mkutano wa Kazi wa Wajumbe wa Kamati za Tume ya Utumishi wa Walimu unaofanyika katika chuo cha Mipango,Mjini Dodoma.
 Katibu wa Tume ya Walimu (kushoto aliyesimama) Mwl. Winifrida G. Rutaindurwa  akiwasilisha taarifa ya Tume katika Mkutano wa Kazi wa Wajumbe wa Kamati za Tume ya Utumishi wa Walimu unaofanyika katika chuo cha Mipango,Mjini Dodoma.
 Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Walimu, Bw.Oliva Paul Mhaiki akitoa neon la utangulizi kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufungua mkutano wa wa Kazi wa Wajumbe wa Kamati za Tume ya Utumishi wa Walimu unaofanyika katika chuo cha Mipango,Mjini Dodoma.
 Baadhi ya wajumbe wakifuatilia Mkutano wa wa Kazi wa Wajumbe wa Kamati za Tume ya Utumishi wa Walimu unaofanyika katika chuo cha Mipango,Mjini Dodoma.

Waziri WA Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.Selemani Jafo(Aliyekaa katikati) katika Picha ya Pamoja na Sekretariet ya Mkutano wa Kazi wa Wajumbe wa Kamati za Tume ya Utumishi wa Walimu unaofanyika katika chuo cha Mipango,Mjini Dodoma.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »