TAARIFA KUTOKA NDANI YA SHIRIKISHO LA SOKA TANZANIA TFF.

December 28, 2017
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

DESEMBA 28, 2017

RELEASE NAMBA 438,439,440,441 NA 442



LIGI KUU BARA MZUNGUKO WA 12 KUENDELEA KESHO



Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) mzunguko wa 12 katika msimu wa 2017/2018 inaendelea wikiendi hii baada ya kusimama kwa wiki tatu kupisha michuano ya CECAFA huko Kenya na mechi za raundi ya pili ya Azam Sports Federation Cup (ASFC).



VPL ambayo wadhamini wenza ni Kituo cha Televisheni cha Azam (Azam Tv) na KCB - Benki inayotoa huduma zake kisasa, itaanza kesho Ijumaa Desemba 29, 2017 kwa mchezo kati ya Azam FC na Stand United kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam kuanzia Saa 1:00 usiku.



Jumamosi Desemba 30, kutakuwa na michezo mitatu - Lipuli na Tanzania Prisons ya Mbeya kwenye Uwanja wa Samora mkoani Iringa kuanzia saa 8:00 mchana; Mtibwa Sugar na Majimaji ya Songea katika dimba la Manungu, Turiani mkoani Morogoro ilihali Ndanda itaikaribisha Simba kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona - Mtwara. Mechi hizo mbili zitachezwa kuanzia saa 10:00 jioni.



Jumapili, mabingwa watetezi wa VPL, Young Africans watakuwa wageni wa Mbao FC kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza kuanzia saa 10:00 jioni huku Njombe Mji FC na Singida United wakitangulia kwa mchezo utakaoanza 8:00 mchana Uwanja wa Saba Saba, Njombe.



VPL itakamilisha mechi za mzunguko wa 12 katika mechi zitakazopigwa mwakani, Januari mosi  ambako Mbeya City wakiikaribisha Kagera Sugar Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya  na Mwadui wakiikaribisha Ruvu Shooting zote kuanzia saa 10:00 jioni.



Baada ya mechi hizo, Ligi Kuu itasimama tena kupisha mechi za Kombe la Mapinduzi visiwani Zanzibar na raundi ya tatu ya Azam Sports Federation Cup (ASFC) itakayochezwa kati ya Januari 5 na 7 mwakani kabla ya kuingia kwenye mzunguko wa 13 wa ligi kuanzia Januari 13 na 17, 2018.





TFF KURASIMISHA MASHINDANO YASIYO RASMI



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) lipo kwenye mkakati madhubuti wa kuyarasimisha mashindano yasiyo rasmi ili kuweza kutambuliwa.



Kumekuwa na upotoshaji unaofanywa kwa makusudi kuwa Rais wa TFF Wallace Karia amefuta mashindano yote ya aina hiyo taarifa ambazo sio sahihi alichokisema Rais Karia wakati akizungumza na Wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari ni kuwa TFF inaandaa kanuni ili mashindano yote ya aina hiyo yachezwe kwa kukidhi vigezo katika utaratibu mzuri na watapata vibali kupitia FA wilaya na mikoa baada ya kutimiza vigezo vitakavyowekwa wakati yale yenye sura ya kitaifa yatapata kibali kutoka TFF.



Nia ya TFF ni njema yenye lengo ya kuufanya Mpira wa Tanzania kuwa katika muelekeo mmoja wenye kufuata utaratibu wenye tija na wenye kuchochea maendeleo ya mchezo wa soka hapa nchini.



WATANZANIA WAENDELEA KUJITOKEZA KUNUNUA TIKETI ZA FAINALI ZA KOMBE LA DUNIA ZA RUSSIA.



Watanzania wameendelea kujitokeza kununua tiketi za Kombe la Dunia zitakazochezwa mwakani nchini Russia.



Mpaka sasa kati ya tiketi 290 zilizotolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) tiketi za Fainali tayari zimemalizika zikiwa zimebakia tiketi za nusu fainali na hatua ya makundi.



Hatua ya makundi ya fainali hizo za Kombe la Dunia ndio yenye tiketi nyingi zaidi zikiwa zimetolewa tiketi 250.



Yeyote mwenye nia ya kununua tiketi awasiliane na Idara ya mashindano ya TFF mwisho Januari 15, 2018.



KADI MAALUMU ZA KUINGILIA UWANJANI KWA WAANDISHI



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) inaendelea kusisitiza utaratibu kwa Waandishi wa Habari za Michezo wa namna ya kuingia kuripoti mechi za fainali za kombe la Dunia zitakazofanyika Russia mwakani.



Mwandishi anayehitaji kuripoti fainali hizo awasiliane moja kwa moja na Idara ya Habari na Mawasiliano TFF ili kuweza kupata kadi hizo maalumu (Accreditation) ambazo zinapatikana kupitia link maalumu inayosimamiwa na   idara hiyo.



Mwisho wa kuomba kadi hizo maalumu kwa waandishi ili kuweza kuthibitishwa FIFA ni Januari 15, 2017.



TFF, OFISI YA MKUU WA MKOA KUWANOA MAKOCHA



Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania TFF kesho anatarajia kuzindua rasmi kozi ya ukocha kwa Walimu wa Shule za Msingi na Sekondari iliyoanza leo Desemba 28, 2017.



Kozi hiyo iliyoandaliwa kwa ushirikiano wa TFF na Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Dar Es Salaam itakayochukuwa muda wa siku 10 itafanyika kwenye vituo viwili vya Makao Makuu ya TFF, Karume – Ilala na Viwanja vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.



……………………………………………………………………..……………..……

IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA



Share this

Related Posts

Previous
Next Post »