WAZIRI MKUU AWATAKA VIONGOZI WA DINI KUSHIRIKIANA NA SERIKALI KUPAMBANA NA RUSHWA, UFISADI

June 13, 2016

MAJLI 
Waziri Mkuu, Kassim Majliwa akiwa katika picha ya pamoja na Maaskofu wa Kanisa katoliki katika sherehe za kumsimika Askofu wa jimbo la Geita, Flavian Kassala  (kushoto kwake) zilizofanyika kwenye kanisa kuu katoliki mjini Geita Juni 12, 2016.(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
……………………………………………………………………………………………………….
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka viongozi wa dini kushirikiana na Serikali katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili zikiwemo za rushwa, ufisadi na matumizi mabaya ya fedha za umma.
Amesema siku zote kumekuwa na ushirikiano mzuri kati ya Serikali na Asasi mbalimbali ikiwa ni pamoja na madhehebu ya Dini katika kuwapatia huduma za kijamii kama vile, afya, elimu, maji, utunzaji wa mazingira na nyingi nyingine.
Waziri Mkuu Majaliwa ameyasema hayo leo mchana (Jumapili, Juni 12, 2016) wakati alipomuwakilisha Mheshimiwa Rais Dk. John Magufuli katika Ibada ya kuwekwa wakfu  na kusimikwa kuwa Mhashamu  Askofu Flavian Kassala kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki Geita.
“Serikali inatambua jitihada kubwa zilizowekwa na Kanisa Katoliki katika Jimbo hili la Geita na Tanzania kwa ujumla hivyo wito wangu kwa Baba Askofu na Waumini wa Kanisa kwa ujumla wenu ni kuwaomba muendelee na kazi hii nzuri ya kutoa huduma muhimu kwa jamii,” amesema.
Amesema maendeleo ya nchi yanawategemea wote hivyo ushirikiano  kati ya Kanisa na Serikali utawezesha maendeleo ya Taifa kupatikana kwa kasi zaidi na kunufaisha wananchi wote.
Waziri Mkuu amesema jukumu la Serikali ni kuweka mazingira wezeshi ambayo yatasaidia Mtanzania kujikomboa na umaskini na kwamba kazi kubwa ya viongozi wa dini kuunganisha jamii na wala siyo kuwatenganisha.
Hata hivyo Waziri Mkuu amesema kinachotakiwa kufanywa na wote ni kumwuomba Mwenyezi Mungu awawezesha kuwaelewa viongozi walioko madarakani na kutii maelekezo yanayotolewa kwani hata vitabu vya dini vinaelekeza kutii mamlaka.
Amesema iwapo waumini watatii na kuzingatia mafundisho ya kiroho yanayotolewa na viongozi wao wa dini ni dhahiri kwamba yatajenga imani miongoni mwao na upendo utatawala katika jamii nzima.
Waziri Mkuu amesema Serikali itaendelea kushirikiana na Madhehebu yote katika kuwahudumia Watanzania wote bila ubaguzi, hivyo aliwasihi waendelee kuwekeza katika huduma za jamii ikiwemo Shule, Vyuo, Zahanati kwa kuwa wana jukumu la kushirikiana kwa pamoja kujenga taifa.
Wakati huo huo Waziri Mkuu aliwaomba wote kwa pamoja waunge mkono juhudi za Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli katika kupambana na uzembe, ubadhirifu na wote wanao kiuka maadili ya utendaji wa kazi.
Kwa upande wake Askofu Renatus Nkwande wa Jimbo la Bunda ambaye alikuwa msimamizi wa Kitume Jimbo Katoliki Geita amewaomba waumini kumpa ushirikiano Askofu mpya wa jimbo hilo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »