TPA YASIFU BENKI KUONGEZA MUDA WA KAZI

September 13, 2015


 Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo Benki Kuu, Bw. Bernard Dadi (kushoto) akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam wakati wa kutangaza rasmi mabenki kufanya kazi kwa muda wa nyongeza kuwawezesha wateja wa bandari na wadau wengine kufanya malipo hadi saa 2 usiku kwa siku za kazi na saa 8 kwa siku za mwisho wa wiki na sikukuu.  Wengine ni Kaimu Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Hebel Mhanga (wa pili kushoto), Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Uchukuzi, Bw. Gabriel Migire (wa pili kulia) na Kamishna wa Forodha wa TRA, Bw. Tiagi Kabisi (kulia). Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza ufanisi bandari hiyo.
 Kaimu Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Hebel Mhanga (kulia) akielezea jambo kwa kundi la waandishi wa habari waliotembelea bandari hiyo kuona maendeleo ya utekelezwaji wa miradi inayotekelezwa chini ya mpango wa Matokeo Makubwa Sasa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.  Inatarajiwa kuwa baada ya kukamilika, miradi hiyo itaongeza uwezo na ufanisi wa bandari hiyo.
Kaimu Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Hebel Mhanga (kulia) akiteta jambo na Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo Benki Kuu, Bw. Bernard Dadi mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam wakati wa kutangaza rasmi mabenki kufanya kazi kwa muda wa nyongeza kuwawezesha wateja wa bandari na wadau wengine kufanya malipo hadi saa 2 usiku kwa siku za kazi na saa 8 kwa siku za mwisho wa wiki na sikukuu.  Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza ufanisi bandari hiyo.

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) imeelezea kuridhishwa kwake na uamuzi wa serikali kuruhusu rasmi nyongeza ya muda wa kufanya kazi kwa benki hapa nchini na kuwa hatua hiyo ni muhimu katika kuongeza ufanisi wa bandari ya Dar es Salaam.

Hatua hii inakuja baada ya serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuruhusu kutumika kwa mfumo wa huduma baina ya taasisi za kibenki (TISS) hadi saa 2 usiku na hivyo kuwezesha wateja kufanya malipo na kuendelea na taratibu nyingine katika bandari hiyo bila tatizo.

Mfumo huo umeunganishwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Wizara ya Fedha ili kuwezesha malipo mbalimbali kama kodi kuweza kulipwa katika muda huo wa nyongeza.

Kaimu Meneja wa bandari hiyo, Bw. Hebel Mhango amesema jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki kuwa mfumo huo utaisaidia mamlaka hiyo na wadau wengine kwa kiwango kikubwa kwa kuwa utasaidia kuendana na mpango ulioanzishwa bandarini wa kufanya kazi kwa saa 24.  

Aliwakumbusha watumiaji wa bandari hasa wakala wa mizigo kuwa mfumo huo mpya unalenga kuwasaidia kuokoa muda, gharama na hivyo kuongeza ufanisi katika biashara zao.

“Tunaomba sasa wadau wengine wajitahidi kuendana na kasi ya bandari kwa kufanya pia kazi kwa muda wa saa 24. Tutaendelea kuhamasisha wadau wetu kuhusiana na mfumo huu mpya,” alisema.

Akizungumza awali, Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Uchukuzi, Bw. Gabriel Migire alisema serikali imeamua kuongezamuda wa utendaji kazi kwa mabenki ili kuruhusu wateja na wadau kulipia kodi zao hadi saa 2 usiku.

Alisema mbali na utekelezaji wa mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) katika sekta ya uchukuzi, hatua hiyo pia itarahisisha ukusanyaji wa mapato ya serikali na huduma ya mizigo.

Kwa mujibu wa takwimu, muda wa miezi sita ya majaribio iliyopita, mfumo huo umeonyesha mafanikio makubwa.

“Miezi 6 ya kipindi cha majaribio ya mfumo huu, jumla ya miamala 7,727 yenye thamani ya Tshs 382 bilioni ilifanyika,” alisema.

Alisema serikali itaendelea kutekeleza miradi ya BRN katika kuifanya bandari kuwa kivutio cha nchi za Afrika ya Mashariki na Kati.

“Wadau wote wa bandari watumie fursa hii kuleta ufanisi katika kazi zao,” alisema.

Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo BoT, Bw. Bernard Dadi alisema benki hiyo imeruhusu malipo kufanyika hadi saa 2 usiku kwa siku za kazi na kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 8 mchana mwisho wa wiki na siku za sikukuu.

“Ni vyema benki zikazingatia muda huu mpya badala ya ule zamani ambapo malipo kama hayo yalirusiwa kufanyika hadi saa 7 mchana,” alisema.

Kamishna wa Forodha wa TRA, Bw. Tiagi Kabisi alisema mamlaka hiyo inakubaliana na muda huo wa nyongeza kwani utasaidia katika ukusanyaji wa mapato ya serikali.

“TRA pia imeongeza masaa ya kuhudumia wateja wake ili kuendana na kasi ya maboresho ya bandari yanayoendelea,” alisema.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »