Kocha mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars)
inayodhaminiwa na bia ya Kilimanjaro, Charles Mkwasa ametoa orodha ya
wachezaji 22 watakaosafiri usiku wa jumapili kuelekea nchini Uturuki kwa
kambi ya wiki moja kujiandaa na mchezo dhidi ya Nigeria Septemba 05,
2015.
Orodha hiyo ya wachezaji 22 imetoka katika kikosi kilichotangazwa
wiki mbili zilizopita na kocha mkuu wa Taifa Stars, ambapo walipata
nafasi ya kufanya mazoezi kwa takribani wiki moja katika uwanja wa
Karume.
Wachezaji wote waliochaguliwa timu ya Taifa wanapaswa kuripoti
kambini Tansoma Hoteli siku ya jumapili saa 5 asubuhi kwa maandalizi ya
mwisho ya safari hiyo.
Wachezaji waliochaguliwa ni All Mustafa (Yanga SC), Aishi Manula
(Azam FC), Said Mohamed (Mtibwa Sugar), walinzi Shomari Kapombe (Azam
FC), Abdi Banda, Mohamed Hussein, Hassan Isihaka (Simba SC), Juma Abdul,
Haji Mngwali, Kelvin Yondani, Nadir Haroub (Yanga SC).
Viungo Mudathir Yahya, Himid Mao, Frank Domayo (Azam FC), Salum
Telela, Deus Kaseke (Yanga SC), Said Ndemla (Simba SC), Washambuliaji
John Bocco, Farid Musa, (Azam FC), Rashid Mandawa (Mwadui FC), Saimon
Msuva (Yanga SC), na Ibrahim Ajib (Simba SC).
Taifa Stars inatarajiwa kuondoka jumapili usiku kwa usafiri wa
shirika la ndege la Uturuki (Turkish Airlines), na kufika jumatatu
asubuhi jijini Istambul, ambapo timu itaelekea katika mji wa Kocael
ambapo itaweka kambi ya wiki moja katika hoteli ya Green Park Kartepe.