Afande Prisca Komba atwaa Tuzo ya Mwanamke mwenye Mafanikio Tanzania 2014

March 09, 2015

 Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni anayesimamia Dawati la Jinsia, Inspekta Prisca Komba (pichani), ameibuka mshindi wa Tuzo ya Mwanamke mwenye Mafanikio Tanzania kwa mwaka 2014.
 
Inspekta Komba, alishinda pia Tuzo ya Mwanamke wa Mwenye Mafanikio katika Sekta ya Umma.

Wengine waliopata tuzo mbalimbali ni pamoja na Debora Mwenda, aliyepata tuzo ya Mwanamke mwenye mafanikio ya maisha, Penina Mlama, alipata tuzo ya Utamaduni na Sanaa, Mary Gitanho, Tuzo ya Ustawi wa Jamii.

Sharmillah Bhatt, tuzo ya Sayansi na Teknolojia, Jennifer Shigoli, tuzo ya Mwanamke mdogo mwenye Mafanikio, Blandina Sembu, tuzo ya Habari na Mawasiliano.

Pia Dk. Wineaster Anderson, tuzo ya Taaluma, Nahida Esmail, tuzo ya Elimu, Devotha Likokola, Biashara  na Ujasiriamali, Jacqueline Mkindi, tuzo ya Kilimo, Mpendwa Chihimba,tuzo ya Afya na Angel Eaton, tuzo ya Michezo.

Tuzo hizo, zilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Taasisi ya Tuzo za Wanawake Wenye Mafanikio Tanzania (TWAA) inayoandaa tuzo hizo zilizokutanisha wanawake zaidi ya 700.

 Rais na Mwandaaji wa tuzo hizo, Irene Kiwia, akikabidhi tuzo hizo alisema  jumla ya Wanawake 36 waliingia tatu bora katika vipengele 12 vilivyokuwa vinashindaniwa na kati ya hizo jumla ya tuzo 14 zimetolewa.

“Katika kuelekea siku ya wanawake duniani ambayo inafanyika kitaifa  kesho (leo) tumeona ni vyema tukawapatia tuzo wanawake ambao wameleta mabadiliko chanya ndani ya jamii,kwani mafanikio yao yanaleta hamasa kwa wanawake wengine wenye malengo,”alisema Kiwia.

Alivitaja vipaumbele vya mwanamke ambaye anataka kuleta mabadiliko ndani ya jamii kuwa ni ndoto,uthubutu,kufuatilia ndoto,uvumilivu na ustahimilivu.

Akizungumzia tuzo hiyo, Ispekta Komba, ameishukuru jamii kwa kutambua umuhimu na kazi ambazo amekuwa akizifanya ndani ya jamii na kwamba amepata nguvu ya kuendelea kufanya kazi hiyo kwa ufanisi zaidi.

“Sikutegemea kupata tuzo hii na nimelia kwa chozi la furaha,namuomba Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP), Ernest Mangu, pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe, kutoa vyeo kwa wakati ili kuongeza motisha wa kufanya kazi,”alisema Komba

Aliitaka serikali na mahakama kuhakikisha inasimamia kesi za udhalilishaji na ukatili wa kijinsia zinatolewa hukumu mapema ili kumaliza vitendo hivyo ndani ya jamii na pia kupunguza kasi ya udhalilishaji ambayo inatokana na watuhumiwa kutochukuliwa hatua kwa wakati.
 
Raisi  wa Taasisi ya Tuzo ya Wanawake Wenye Mafanikio Tanzania, Irene Kiwia akizungumza katika hafla ya Utoaji wa tuzo hizo uliofanyika katika  Ukumbi wa Serena Hotel jijini Dar es salaam.
Debora Mwenda Mwanahabari mkongwe wa Redio Tanzania  akizungumza baada ya kupokea tuzo ya Mwanamke  mwenye mafanikio ya maisha, akielezea ni jinsi gani alivyofanikiwa kuelimisha jamii kupitia kipindi chake cha (Mama na mwana) kilichokuwa kikirushwa hewani Redio Tanzania.
Sharmillah Bhatt, Kushoto akipokea tuzo ya Sayansi na Teknolojia katika ukumbi wa Serena Hotel Leo Jijini Dar es salaam.
 
Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni anayesimamia Dawati la Jinsia, Inspekta Prisca Komba (kushoto) akifurahia kushinda tuzo kwa kupiga saluti sambamba  na Rais wa tuzo za wanawake wenye mafanikio Tanzania (TWAA), Irene Kiwia.
 
Baadhi ya wahudhuriaji katika tuzo ya Mwanamke Mwenye Mafanikio Tanzania wakifuatilia  utolewaji wa tuzo hizo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »