VETA YAKUTANA NA WADAU WA VIWANDA VYA UMEME NA MAGARI KUJADILI KUHUSU MRADI WA MAFUNZO YANAYOTOLEWA NA VETA KWA KUSHIRIKIANA NA VIWANDA

March 09, 2015

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi (VETA) imekutana na wadau wa viwanda vya umeme na magari jijini Dar es Salaam kujadili utekelezaji wa mradi wa mafunzo yanayotolewa na VETA kwa kushirikiana na viwanda ujulikanao kama Dual Apprenticeship Training Project.

Mradi huo uliopo kwenye majaribio tangu kuanzishwa kwake mwaka 2011 kwa ushirikiano kati ya Hamburg Chamber of Skills Craft ya Ujerumani na VETA,unalenga kuandaa idadi kubwa ya mafundi stadi wenye ujuzi zaidi kwa vitendo kwa kuwa sehemu kubwa ya mafunzo hayo inafanyika viwandani.

Akifungua rasmi warsha hiyo mgeni rasmi Mkurugenzi wa Mafunzo ya Ufundi-VETA Leah Lukindo alisema kwamba ni muhimu kwa vyuo vya ufundi stadi kutoa stadi zinazohitajika na viwanda kwa kuwa viwanda vinategemea nguvu kazi hiyo ili kufanikisha malengo yake.

Alisema kukosekana kwa ushirikiano kati ya vyuo vya ufundi stadi na viwanda kunasababisha malalamiko mara kwa mara kutoka viwandani ya kutoridhishwa na utendaji kazi wa wahitimu wa mafunzo ya ufundi stadi nchini.

Alisisitiza kuwa mfumo wa Dual Apprenticeship Training unamwezesha kijana kupata ujuzi wa fani husika wakati anafanya kazi kwenye kiwanda hivyo kumuwezesha kwa kiasi kikubwa kujifunza zaidi kwa vitendo na kuendana na mahitaji ya soko la ajira pmaoja na kupata uzoefu na uelewa wa mazingira halisi ya kufanyia kazi.

Aliwataka wenye viwanda kuonyesha ushirikiano kwa kujiunga na mradi huu ambao una faida kubwa kwao kwani unawasaidia kupata mfanyakazi mwenye ujuzi unaotakiwa pamoja na uzoefu wa kazi kwa kuwa muda mmwingi wa masomo anakuwa kwenye kiwanda husika.
Mkurugenzi wa Mafunzo ya Ufundi Stadi-VETA Leah Lukindo akizungumza wakati akifungua rasmi warsha hiyo katika ukumbi wa hoteli ya Giraffe-Dar es Salaam.
Washiriki wa warsha hiyo ambao ni wadau wa viwanda vya umeme na magari wakisikiliza kwa makini hotuba ya mgeni rasmi.
Mratibu wa mradi huo Francis Komba akisisitiza jambo kwa washiriki wakati akiwasilisha mada inayohusu wajibu wa wadau wa viwanda katika utekelezaji wa mradi.
Meneja mradi Martin Mac Mahon akiwasilisha mada juu ya utekelezaji wa mradi tangu kuanzishwa kwake mwaka 2011 na mikakati iliyopo kuhakikisha mradi huo unafikia malengo waliyojiwekea.
Baadhi ya washiriki wa warsha hiyo wakifuatilia mada mbalimbali zilizotolewa kuhusu mradi.
Mshauri wa mradi Ahmed Athuman (kulia) akijadili jambo juu ya mradi na Mkuu wa chuo cha VETA-Dar es Salaam Samuel Ng`andu wakati wa mapumziko.
Washiriki wa warsha wakiwa katika picha ya pamoja na mgeni rasmi Mkurugenzi wa Mafunzo ya Ufundi Stadi-VETA Leah Lukindo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »