MSTAHIKI MEYA JERRY SILAA AWATAKA WAKAZI WA MKOA WA LINDI KUJITOKEZA KWA WINGI KUJIANDIKISHA KATIKA DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA

February 01, 2015


111112 
Wakazi wa mkoa wa Lindi wametakiwa kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura ili waweze kushiriki kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika mwishoni mwa mwaka huu. Rai hiyo imetolewa jana na Mjumbe wa Kamati kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jerry Silaa wakati akiongea kwenye kilele cha sherehe za kutimiza miaka 38 ya chama hicho mkoani Lindi zilizofanyika katika tawi la Mnazi Mmoja lililopo kata ya Mingoyo wilaya ya Lindi mjini. Silaa mbaye pia ni Mstahiki Meya wa Manispaa ya Ilala alisema iwapo mtu atajiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura atashiriki katika uchaguzi mkuu ujao hivyo basi wakati ukifika ni jukumu la mabalozi kuwahimiza wananchi kujiandikisha ili wasipoteze haki yao ya msingi ya kupiga kura. Aidha Meya Silaa aliwapongeza wana CCM kwa ushindi wa asilimia 77 walioupata wakati wa uchaguzi wa Serikali za mitaa, vijiji na vitongoji uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana na kuwataka kuwa makini katika kuteua viongozi wanaokubalika na wananchi na kuachana na makundi yanayokibomoa chama hicho kwa kufanya hivyo itawawezesha kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi ujao. Kwa upande wa vijana aliwahimiza kujishughulisha katika shughuli za kimaendeleo ili waweze kujipatia maendeleo kwani mkoa wa Lindi uko katika dira ya maendeleo kwa kuwa na ardhi yenye rutuba, barabara nzuri na gesi. Silaa alisisitiza, “Nawashauri vijana wenzangu mjiunge na CCM chama kinachowasaidia vijana kuwaletea maendeleo ukilinganisha na vyama vingine vinavyowapotezea muda na kurudisha nyuma maendeleo yenu”. Alikipatia kikundi cha Zamira ambchi kinajishughulisha na kilimo na ujasiriamali shilingi laki tano ili ziweze kuwasaidia kuinua mtaji. Naye Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kupitia wilaya ya Lindi mjini Mama Salma Kikwete alisema sherehe hizo zina umuhimu wa kipekee kwa wana CCM kwani zimeangukia mwaka wenye matukio muhimu na makubwa kwa nchi ambayo ni kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais. Mama Kikwete ambaye ni Mke wa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema mwaka 2015 ni mwaka wa kuhitimisha utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2010-2015 ambapo Chama hicho kiliwaomba wananchi wakichague ili kiwafanyie kazi watanzania ambao walikiamini na kukichagua. “Matokeo yake watanzania wameyaona , miundombinu ya barabara, shule na vyuo vimejengwa na watoto wengi hivi sasa wapo mashuleni. Huduma za afya zimeboreka kwa kujengwa Hospitali, vituo vya afya na Zahanati”. Lakini hata kwa yale ambayo hayakuwepo kwenye Ilani na yalikuwa ni matakwa ya wananchi chama chetu sikivu hakikusita kuyakubali kwani yalikuwa ni kwa ajili ya maslahi ya Taifa na vizazi vyetu”, alisema Mama Kikwete. Kuhusu Katiba inayopendekezwa MNEC huyo alisema itapigiwa kura ya maoni mwaka huu mwezi wa nne hivyo basi aliwataka wanaCCM na watanzania wote kwa ujumla kuipigia kura ya ndiyo katiba pendekezwa kwani inakidhi matakwa ya watanzania kwa kuwa imegusa katika maeneo yote. Akiwasalimia wananchi waliohudhuria sherehe hizo Mkuu wa wilaya ya Lindi Dkt. Nassoro Hamidi aliwahimiza wazazi kuhakikisha watoto walioandikishwa darasa la kwanza na wale waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza wanaenda shule kuanza masomo ili waweze kupata elimu itakayowasaidia katika maisha yao. Katika kilele cha sherehe hizo zilizoenda sambamba na wiki ya Chama na Jumuia zake kauli mbiu yake ni Umoja ni ushindi, Katiba yetu, Taifa letu jumla ya wanachama wapya 448 walijiunga na chama hicho ambapo saba walitoka vyama vya upinzani, Chama cha Wananchi (CUF) watano na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wawili

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »