ZASWA FC YAWACHAPA MAVETERAN WA MJI WA CHAKE CHAKE MABAO 3-1.

April 24, 2014
Na Masanja Mabula –Pemba .24/04/2014.
 
Timu ya Wandishi wa Habari za Michezo  Zanzibar (ZASWA SC)  imekamilisha ziara yake Kisiwani Pemba kwa kuwafundisha soka Mavetarani   wa Mji wa Chake Chake kwa kuwafunga mabao 3-1, katika mchezo uliopigwa ndani ya dimba la Gombani .
 
Ushindi huo wa tatu kwa timu ya ZASWA SC ni  salamu kwa timu ambazo zitakutana na kikosi hicho cha wanahabari  kwenye michuano ya Kipwita CUP  ambapo ZASWA imepangwa kundi moja na  timu ya Miembeni FC.
 
 Katika mchezo huo  maveterani ndiyo walikuwa wa kwanza kuliona lango la ZASWA Mapema dakika ya 20 kwa bao safi lililofungwa na mchezaji Ali Kibenzi aliyeunganisha vyema krosi iliyotoka winga wa kulia.
 
Hata hivyo furaha ya maveterani ilizimwa mnamo dakika ya 35 baada ya mchezaji Abdul watif kuuwahi mpira uliotemwa na mlinda mlango wa Maveterani hao kufuatia shuti kali la umbali wa mita 28 lililopigwa na kiungo wa ZASWA Kombo Ali Kombo .
 
Kuingia kwa bao hilo kulizidisha ari kwa wachezaji wa ZASWA ambao walionekana kuutawala mchezo hali iliyosababisha  washambuliaji wa ZASWA kuweka kambi ya muda langoni kwa Maveterani hao  .
 
Wakicheza kandanda safi ZASWA waliongeza bao la pili katika 42 ambao liliwekwa ndani ya kamba na Kiungo Hilali   Banka baada ya kuichambua ngome ya maveterani na kisha kuukwamisha mpira ndani ya nyavu .
 
 Wakati akijiandaa kumpisha kiungo Khamis Dadi kuchukua nafasi yake  Kocha Mchezaji wa ZASWA SC Ali Bakar Cheupe aliiandikia timu yake bao la tatu kunako dakika ya 76 , akimalizia pasi ya Hilali Banka aliyekuwa nyota wa mchezo huo .
 
Kikosi hicho cha Wandishi wa Habari za Michezo Zanzibar kimekamilisha ziara yake  Kisiwani  Pemba ambapo kimeshinda michezo mitatu kwa kuzifunga timu za Wilaya ya Wete , Mkoani n Chake Chake huku kukipoteza mchezo katika Wilaya ya Micheweni .

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »