DKT. MAGUFULI AWANYIMA LIKIZO YA PASAKA WAKANDARASI MPAKA BARABARA ZILIZOHARIBIWA NA MAFURIKO ZIKAMILIKE

April 15, 2014

WAZIRI wa Ujenzi, Dk. John Magufuli, amewataka wahandisi wote nchini kutokwenda likizo kwa ajili ya Sikukuu ya Pasaka hadi miundombinu iliyoharibiwa na mvua itakapokamilika kukarabatiwa.
Dk. Magufuli alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam jana wakati wa kuiaga na kuizindua Bodi mpya ya Ushauri ya Wakala wa Ufundi na Umeme (Temesa).
Alisema kutokana na kuharibika kwa miundombinu mbalimbali nchini hakuna haja ya mhandisi kwenda likizo hata akiwa katika hali ngumu.
“Watanzania wanategemea miundombinu ya barabara na madaraja katika kupitisha mizigo na vyakula pamoja na shughuli za maendeleo, hivyo kazi hii inapaswa kufanyika na kukamilika haraka,” alisema.
Alisema kunahitajika nguvu za ziada katika kutekeleza hilo, ndiyo maana ameamua kukatisha likizo za wahandisi ili kufanikisha hilo.
“Nafanya ziara za ukaguzi katika maeneo yote yaliyoathrika na nikibaini kuna mhandisi kaenda likizo basi afungashe virago vyake huko huko na asirudi tena,” alisema.
Alitaja baadhi ya madaraja yaliyoanza kukamiliki na kutumika kuwa ni Daraja la Lindi linaloungana na Kongowe, Daraja la Mpiji Magohe na Bagamoyo ambalo hadi sasa limekamika katika tuta kiasi cha mita 75 pamoja na Daraja la Ruvu ambalo linatumika upande mmoja.
Mbali na hayo, aliitaka Bodi mpya ya Temesa kuwa makini katika shughuli zake, kwani ni miongoni mwa wahusika wakubwa pia wanaowajibika katika utekelezaji wa  miundombinu nchini.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »