UFINYU wa BAJETI katika mradi wa Damu.

June 24, 2013

Na Oscar Assenga, Tanga.
IMEWEKWA JUNE 24 saa 12:11
UFINYU wa Bajeti ya kutosha katika mradi wa uhamasishaji jamii kuhusu uchangiaji damu kwa hiari katika wilaya za Korogwe, Mkinga na Tanga ni miongoni mwa changamoto zilizojitokeza wakati wa zoezi hilo likiwa linafanyika katika maeneo hayo hali ambayo ilipelekea kutokufikia malengo yaliyokusudiwa.

Hayo yalisemwa na Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa habari mkoani Tanga,(TPC)Hassani Hashimu hivi karibuni wakati akisoma taarifa ya uhamasishaji huo kwa waandishi wa habari kwenye majumuisho ya uchangiaji wa damu yaliyofanyika katika viwanja vya Tangamano jijini Tanga .

Hashimu alisema katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi huo ulifanikiwa kukusanya uniti 210 za damu kati ya makadirio ya kukusanya uniti 450 ambapo kati yao wanaume waliochangia ni 183 na wanawake walikuwa 27.

Aliongeza kuwa kutokana na uhamasishaji huo uliofanywa na chama hicho katika kipindi chote cha utekelezaji wa mradi huo kupitia vyombo vya habari vya ndani na nje ya mkoa wa Tanga wataalamu wa damu salama kutokana kanda ya kaskazini wameweza kukusanya uniti 450 kati ya lengo walilojipangia la kukusanya uniti 1000.

Alisema kikwazo kingine ni kukosekana kwa elimu ya kutosha kuhusu umuhimu wa uchangiaji wa damu ndani ya jamii sambamba na kukosekana kwa msukumo kutoka kwenye mamlaka husika katika kuvifanya vilabu vya wachangiaji damu kuwa endelevu.

Aidha aliiomba serikali ya mkoa wa Tanga kupitia mganga mkuu wa mkoa kuweka utaratibu mzuri ambao utawezesha wachangiaji damu wanaojitolea kwa hiari kutambulika na kupewa huduma kwenye hospitali bila kikwazo pale inapohitajika.

“Tunaaamni kuwa huduma bora hiyo itawafanya wachangiaji damu kuwa na ari ya kuendelea kujitolea kutokana na kuwa na uhakika wa kupata huduma wakati wote wanapokuwa wakihitaji wao pamoja na ndugu zao “Alisema Hashimu.

Alisema ombi hilo linatokana na kuwepo kwa malalamiko kutoka kwa wachangiaji damu kuwa wamekuwa wakikosa huduma stahiki na ikibidi kununua damu hasa wanapohitaji huduma hiyo kwenye hospitali za mkoani hapa.

Kampeni hiyo ilizinduliwa mei 23 mwaka huu ambapo lengo kuu ilikuwa ni kukabiliana na changamoto ya upungufu wa damu unaozikabili benki za damu katika hospitali za mkoa wa Tanga hususani hospitali ya rufaa ya mkoa ambayo ni Bombo.

Mradi huo ulianzishwa na Chama cha Waandishi wa habari mkoa wa Tanga( Tanga Press Club) kwa kufadhiliwa na Kampuni ya simu za Mikononi ya Vodacom kwa kiasi cha shilingi milioni sita 6,000,000.

Mwisho.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »