Tanga Warriors yaiadhiri City Kings yaibamiza Vikapu 46-37.

June 02, 2013

  Na Oscar Assenga,Tanga.
TIMU ya Mpira wa Kikapu ya Tanga Warriors mwishoni mwa wiki iliifunga City Kings vikapu 46-37 katika bonanza la Michezo ambalo liliandaliwa na Bandari Tanga lengo likiwa ni kuwaweka vijana pamoja na kuinua michezo.

Katika mchezo huo Tanga Warriors walionekana kucheza kwa kujipanga na kupeleka mashambulizi mara kwa mara kwenye lango la City Kings ambapo mpaka mzunguko wa kwanza unamalizika Tanga Warriors walikuwa wanaongoza kwa vikapi 37-22 kwenye mechi hiyo ambayo ilichezwa viwanja vya Bandari jijini Tanga.

Baada ya kumalizika mechi hiyo ilifuatiwa na mchezo wa Pete ambapo timu ya Umiseta Tanga iliweza kuumana na Bandari Tanga na kumalizika kwa Bandari Tanga kuibuka na ushindi wa mabao 24-19,katika mchezo ambao ulikuwa na upinzani wa hali ya juu.

Bonanza hilo ambalo lilikuwa la aina yake kutokana na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa michezo mkoani ambapo kwenye mchezo wa kikapu timu ya  Umiseta Tanga waliweza kuifunga Bandari kwa vikapu 24-17.

Mechi ya mwisho ambayo ilikuwa na upinzani mkubwa ni ya kuvuta kamba ambapo timu ya City Kings iliweza kuibuka kidede baada ya kuwavuta Tanga Warriors seti 2-1 michezo ambayo ilichezwa viwanja vya Bandari jijini Tanga.

Nyota wa bonanza hilo alikuwa ni Adam Mkondo kutoka timu ya Tanga Warriors ambaye alichangia kwa kiasi kikubwa kuipa ushindi timu yao kwenye mechi hiyo .

Akizungumza kabla ya kuanza bonanza hilo mgeni rasmi, Kaimu Meneja wa Bandari Tanga,Moshi Mtambalike Chawala alisema lengo la bonanza hilo lilikuwa kuwapa hamasa vijana kupenda michezo pamoja na kuwataka vijana kupenda kujituma na kucheza kwa moyo kwani michezo ni ajira ambayo inaweza kuwainua katika maisha yao.

Kwa upande wake, Afisa Utumishi wa Bandari ya Tanga, Teckla Malombe alisifu viwango vya wachezaji walioshiriki bonanza hilo na kuwataka vijana kuendelea kupenda michezo na kuipa kipaumbele.

Nae Mratibu wa Bonanza hilo, Dr.Omari Khupe alisema Bonanza hilo ni endelevu ambalo hufanyika kila wiki ya mwishoni mwa mwezi lengo ni kuwakutanisha wanamichezo pamoja na kuinua viwango vya michezo.

Mwisho.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »