>Sheria Isichague Chama
NA OSCAR ASSENGA, TANGA
Katibu Mkuu wa Chama cha NLD, Doyo
Hassan Doyo, amesema mjadala unaoendelea kuhusu hatua zinazochukuliwa na Ofisi
ya Msajili wa Vyama vya Siasa umeonyesha jinsi baadhi ya Watanzania wanavyotoa
hukumu za haraka bila kutafakari misingi ya sheria.
Doyo alisema kumekuwa na mtazamo
kwamba Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inalenga zaidi vyama vya upinzani,
huku ukweli ukiwa ni kwamba taasisi hiyo inasimamia sheria bila kuangalia
itikadi ya chama husika.
Akizungumza wakati wa ziara ya chama
hicho mkoani Tanga, alisema hatua zilizochukuliwa hivi karibuni dhidi ya baadhi
ya viongozi wa kisiasa zinatokana na matamshi yaliyotafsiriwa kuwa na viashiria
vya uvunjifu wa sheria za vyama vya siasa.
“Sheria iko wazi. Chama au kiongozi
anayekiuka taratibu anaweza kupewa adhabu ya faini, kusimamishwa shughuli au
hata kuchukuliwa hatua nyingine za kisheria. Hii siyo kwa chama fulani pekee,”
alisema.
Alieleza kuwa baada ya viongozi wa Chama
cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoa kauli zilizozua mjadala, Ofisi ya
Msajili iliwaandikia barua ya kutaka maelezo. Hatua hiyo, kwa mujibu wa Doyo,
ilitafsiriwa vibaya na baadhi ya wananchi pamoja na wanaharakati waliodai kuwa
upinzani unaonewa.
Hata hivyo alisema hali hiyo
imebadilika baada ya mmoja wa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) naye
kuandikiwa barua kufuatia matamshi yake ya kisiasa.
“Watu walidhani sheria inafanya kazi
kwa upande mmoja, lakini sasa imeonekana wazi kuwa anayevunja sheria ndiye
anayechukuliwa hatua, bila kujali anatoka chama gani,” alisema.
Doyo alisema vyama vya siasa
vinapaswa kutambua kuwa vimesajiliwa kwa mujibu wa sheria na hivyo vina wajibu
wa kuendesha shughuli zake ndani ya mipaka ya kisheria.
Alionya kuwa siasa zisizo na nidhamu
zinaweza kupelekea uvunjifu wa amani na kuhatarisha usalama wa Taifa.
“Ukianza kufanya siasa nje ya
sheria, maana yake unaondoka kwenye misingi ya kisiasa na kinachofuata ni
migogoro na vurugu. Taifa haliwezi kujengwa kwa misingi ya shinikizo na
vitisho,” alisema.
Aidha, aliitaka Ofisi ya Msajili wa
Vyama vya Siasa kuendelea kusimamia sheria kwa uthabiti bila kuogopa presha za
kisiasa kutoka kwa wanasiasa au wanaharakati.
Kwa mujibu wa Doyo, uwepo wa taasisi
imara zinazotekeleza sheria kwa haki ndiyo msingi wa kulinda amani na utulivu
wa nchi.
Katika ziara hiyo ya NLD iliyoanzia
Pangani na kuelekea Lushoto, chama hicho kimesema kinaendelea kutoa elimu kwa
wananchi kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria, taratibu na kanuni za kisiasa ili
kuimarisha demokrasia na mshikamano wa Taifa.




EmoticonEmoticon