Mabadiliko ya bei za mafuta nchini kwa mwezi Aprili 2026 yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na vita inayoendelea kati ya Marekani kwa kushirikiana na Israeli dhidi ya Irani iliyoanza tarehe 28 Februari 2026, mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imesema jana.
“Kushambuliwa kwa visima vya mafuta, maghala ya kuhifadhi mafuta na viwanda vya kusafisha mafuta (refineries) pamoja na Irani kufunga Lango la Hormuz linalopitisha takriban asilimia 20 ya mafuta yanayosafirishwa kwenda kwenye masoko mbalimbali duniani, imeathiri hali ya uzalishaji mafuta kwenye nchi za Mashariki ya Kati ambako Tanzania inaagiza kwa kiasi kikubwa; imeongeza gharama za usafirishaji kutokana na kukosekana kwa meli za kusafirisha mizigo na imeongeza gharama za bima za meli za mizigo kutokana na vita,” imeeleza taarifa iliyosambazwa kwenye vyombo vya habari jana.
Kwa mwezi Aprili 2026, gharama za kuagiza mafuta (premiums) katika Bandari ya Dar es Salaam zimeongezeka kwa wastani wa asilimia 15.3 kwa mafuta ya petroli na asilimia 10.8 kwa mafuta ya dizeli na hakuna mabadiliko ya gharama kwa mafuta ya taa.
EWURA imesema ongezeko hilo ni janga la kidunia na Tanzania kama sehemu hiyo inachukua hatua mbalimbali kuhakikisha usalama wa upatikanaji wa mafuta nchini na bei himilivu ili kupunguza madhara ya kiuchumi na kijamii. Kutokana na hali hiyo, EWURA imewashauri wananchi kutumia mafuta kwa uangalifu na ufanisi mkubwa.
EmoticonEmoticon