RAIS DKT.SAMIA :SERIKALI IMEPIGA HATUA KUBWA UJENZI WA MIRADI YA UMEME

March 09, 2025


▫️Asisitiza Mradi wa JNHPP utachochea Ajenda ya Nishati Safi


Na Josephine Maxime -Arusha


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema  Serikali imepiga hatua kubwa katika ujenzi wa miradi ya umeme, hususan Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere, ambalo litazalisha megawati 2115 litakalochangia upatikanaji wa umeme wa uhakika.


Mheshimiwa Rais ameyasema hayo lMachi 8, 2025, wakati wa Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, yaliyofanyika kitaifa katika Viwanja vya Sheikh Amri Abeid Jijini Arusha.

Katika hotuba yake, Rais Samia amesema  kukamilika kwa miradi mbalimbali ya kimkakati ya uzalishaji  umeme kutachangia kusukuma ajenda ya Serikali kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo amefafanua kuwa licha ya Mradi mkubwa wa JNHPP bado kuna miradi mingine midogo  ambayo inazalisha Umeme .

"Tanzania imefanya kazi kubwa katika suala la Nishati. Tulikuwa tunafaidi Umeme mijini pekee, lakini sasa umesambazwa katika vijiji vyote. Tunapozungumza kuhusu Nishati, pia tumelenga nishati safi. Tumefanya kazi kubwa kujenga Bwawa la Julius Nyerere, ambalo litazalisha megawati 2115, pamoja na mabwawa mengine madogo yanayozalisha umeme katika maeneo mbalimbali nchini," alisisitiza Rais Samia.


Kuhusu Usawa wa Kijinsia Mheshimiwa Rais amesema kuwa kumeshuhudiwa Wanawake katika Mashirika mbalimbali likiwemo Shirika la Umeme Taanzania TANESCO wanavyoshiriki katika shughuli za uzalishaji Umeme

Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani  mwaka huu yamepambwa na Kauli mbiu isemayo, "Wanawake na Wasichana 2025: Tuimerishe Haki, Usawa na Uwezeshaji.



Share this

Related Posts

Previous
Next Post »