TOENI ELIMU ZAIDI KWA WANANCHI JUU YA UGONJWA WA MPOX;WAZIRI MHAGAMA

August 21, 2024

 Na WAF, Namanga- Arusha

Waziri wa Afya, Mhe. Jenista Mhagama amewataka wataalamu wa Afya nchini kuongeza kasi ya kutoa elimu ya ugonjwa wa Mpox ili wananchi wawe na uelewa mpana dhidi ya ugonjwa huo.

Waziri Mhagama ametoa agizo hilo leo Agosti 21, 2024 wakati wa ziara kwenye Kituo cha Forodha cha Mpaka wa Namanga Halmashauri ya Wilaya ya Longido mkoani Arusha alipofika kuona utayari wa kukabiliana na ugonjwa wa Mpox.

“ Nimezungumza na mmoja wa wasafiri lakini hajui dalili za za ugonjwa wa Mpox hivyo ipo haja ya kuongeza kasi ya utoaji elimu kwa wananchi ili kuwa na uelewa juu ya ugonjwa huo”, ameeleza Mhe. Mhagama na kuongeza

“Kuwe na mabango na vipeperushi vinavyotoa elimu juu ya ugonjwa kuelezea Dalili, unaambukizwaje na namna ya kujikinga ili kila msafiri anayeingia na kutoka nchini awe na uelewa mpana” amesisitiza Waziri Mhagama.

Mhe. Mhagama amesema kwa sasa mpaka Tanzania ni Salama na hakuna mgonjwa yeyote aliyebainika kuwa na ugonjwa huo hivyo wananchi waendelee kuchukua tahadhari juu ya ugonjwa wa Mpox .

“ Natoa wito kwa wananchi kila mmoja awe mlinzi kwa mwenzake pale atakapo ona dalili za ugonjwa huo kwa mtu basi atoe taarfa kwa wataalamu wa afya, Kituo cha kutolea huduma za afya kilichopo karibu yake au kuwasiliana na Wizara ya Afya kwa Namba ya 199 ili kuhakikisha nchi inakuwa salama”, ametoa wito.

Akihitisha ziara yake Waziri Mhagama amewahakikishia watanzania kuwa Wizara yake imejipanga kikamilifu kwa kuimarisha Huduma za uchunguzi na maabara maeneop ya mipakani ili kuhakikisha ugonjwa huo hauingii nchini    

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »