WATAKIWA KUZIDISHA JUHUDI KUPUNGUZA UKATILI

December 12, 2023

 Na. Jeshi la Polisi Dodoma


Kamishna wa Utawala na Menejimenti ya Rasilimaliwatu CP Suzan Kaganda amewataka Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto kote nchini kuzidisha juhudi katika kutoa elimu ili kupunguza vitendo vya ukatili katika Jamii.

Kamishna Kaganda ameyasema hayo leo Disemba 12, 2023 wakati akizungumza na Watendaji wa Dawati la Jinsia na Watoto kutoka Mikoa ya Tanzania bara na Zanzibar wakati wa Kikao cha Watendaji hao kinachoendelea Jijini Dodoma

Alisema kazi inayofanyika ni kubwa ingawa bado kuna vitendo vya ukatili hivyo Watendaji hao wazidishe kutoa elimu pamoja na kubaini na kuzuia vitendo hivyo.

Aidha, aliwataka Watendaji hao kuendelea kushirikiana na wadau mambo mbalimbali ikiwemo kutoa elimu na kazi zingine ambazo zinahitaji raslimali fedha na vifaa ili kazi za Dawati ziweze kuendelea kwa kasi.

Vilevile aliwataka wote waliohudhuria kikao hicho kilichoambatana na mafunzo kuhakikisha kuwa wanakwenda kuwafundisha Watendaji na Askari ambao hawakupata fursa ya kufika Jijini Dodoma kwa ajili ya Kikao na Mafunzo hayo.

Kwa Upande wake Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto, Naibu Kamishna wa Polisi DCP Maria Nzuki alisema kutokana na kazi nzuri ya kutoa elimu kwenye nyumba za ibada iliyofanyika siku ya Jumapili katika makanisa mbakimbali Jijini Dodoma tayari Makanisa zaidi ya 20 yameomba Watendaji hao kwenda kutoa elimu Jumamosi na Jumapili ijayo.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Mahusiano ya Kimataifa, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi SACP Renata Mzinga alisema watendaji hao wamejitokeza kwa wingi kuhudhuria Kikao hicho na kila Mkoa umeleta Wawakilishi.


Share this

Related Posts

Previous
Next Post »