Wafanyakazi wanawake wa kampuni ya Vodacom Tanzania
PLC na taasisi yake ya kuhudumia masuala ya jamii ya Vodacom Tanzania Foundation, leo
wametembelea wodi ya wazazi katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kutoa vifaa
mbalimbali ,ukiwa ni mwendelezo wake wa kutoa vifaa vya kuokoa zaidi ya watoto 260
wanaozaliwa kabla ya wakati kila mwaka nchini.
Akiongea wakati wa kukabidhi vifaa hivyo na kutembelea wagonjwa, Mkurugenzi wa
Vodacom Tanzania Foundation, Rosalynn Mworia alisema “Tunayo furaha kuadhimisha Siku
ya Wanawake Duniani mwaka huu kwa kutembelea hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kutoa
msaada katika wodi ya wazazi vitakavyowezesha kupunguza vifo vya watoto wachanga.
Tutaendelea kuunga mkono jitihada za serikali ya Tanzania za kuboresha sekta ya afya
hususani kwa wanawake wajawazito na watoto wachanga”.
Vifaa tiba mbalimbali vya kuwasaidia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati (Njiti) vilitolewa,
baadhi ya vifaa hivyo ni vya kuwasadia watoto kupumua, kuongeza joto, kupima na kuratibu
uzito kidijitali, pampasi na khanga, [oxygen concentrators, nebulizer machines, digital weigh
scales, surfactants, infusion pumps and continuous positive airway machines, as well as
Pampers and khangas].
Mkurugenzi
wa Vodacom Tanzania Foundation, Rosalynn Mworia (wa tatu kushoto)
akikabidhi sehemu ya vifaa tiba maalum kwa ajili ya watoto wanaozaliwa
kabla ya wakati (Njiti), kwa Dkt. Mariam Kalomo aliyemwakilisha mgeni
rasmi naibu waziri, wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee, jinsia na
watoto, Dr Faustine Ndugulile. Wa pili kulia ni Muasisi wa Taasisi ya
Doris Mollel na Balozi wa Watoto Njiti, Doris Mollel.
Vodacom Tanzania Foundation inaelewa changamoto mbalimbali wanazokutana nazo
wanawake nchini, wakati wa ujauzito na wakati wa kujifungua ndio maana imeamua
kulivalia njuga changamoto zao na kuhakikisha vifo vya wanawake na watoto
vinavyosababishwa na matatizo ya uzazi vinapungua.
“Kusaidia kuboresha afya za wanawake na watoto na lishe bora ni moja ya malengo ya
taasisi yetu ya Vodacom Tanzania Foundation. Tunaamini msaada mkubwa unatakiwa
kunusuru maisha ya wanawake na watoto kutokana na changamoto mbalimbali
zinazowazunguka, tunaamini msaada huu utafanikisha kuleta matokeo chanya ya
kuboresha na kuokoa maisha ya watoto wachanga,”alisema Mworia.
Msaada huu ni mwendelezo wa taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation, kutoa vifaa vya
kisasa vinavyowezesha kuokoa maisha ya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati (Njiti)
sambamba na miradi mingine inayolenga kuboresha afya ya uzazi na kupunguza vifo vya
watoto wachanga nchini, inayotekeleza kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
Baadhi ya miradi hiyo ni kuwasafirisha wanawake wenye ugonjwa wa Fistula hadi hospitali
na kugharamia matibabu yao, kutoa jumbe za afya ya uzazi kwa wanawake wajawazito bure
kupitia simu zao za mkononi za mtandao wa Vodacom sambamba na kuwawezesha
wanawake wajawazito kuwahishwa katika vituo vya afya vyenye wataalamu wakati
wanapokaribia kujifungua, kwa ajili ya kuokoa maisha yao na watoto wanaozaliwa.
Akizungumza katika hafla hiyo, Dr Mariam Kalomo aliyemwakilisha mgeni rasmi naibu
waziri, wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee, jinsia na watoto, Dr Faustine Ndugulile
aliwapongeza Vodacm Tanzania Foundation kwa msaada huo waliojitolea huku akiwaomba
wadau wengine kujitokeza pia.
“Nawashukuruni sana kwa msaada huu, maana tuna uhakika utapunguza vifo vya watoto
wachanga kwa kiasi kikubwa, hiki mlichojitolea ni kikubwa mno kwa vile hospitali nyingi
zinakabiliwa na upungufu wa vifaa tiba, kwa hiyo tunapopokea vifaa hivi tunakuwa na
uhakika wa kuokoa maisha ya watoto wengi Zaidi,” alisema Dr Kalomo.
Kwa upande wake, Sister Zuhura Mahona aliyemuwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa hospitali
ya Taifa ya Muhimbili aliwahahakishia wafanyakazi wa Vodacom Tanzania Foundation
kwamba vifa walivyojitolea vitatumika kwa usahihi kama vilivyoombwa.
Naye mkurugenzi wa Taasisi ya Doris Mollel , Doris Mollel aliwashukuru
wafanyakazi wa Vodacom Tanzania Foundation kwa kujali watoto waliozaliwa kabla ya
wakati na kuwaokoa kwa kuwaletea vifaa tiba hivyo.
“Vifaa hivi ni muhimu sana kwa ajili ya watoto, kwa mfano ukimpatia mtoto hewa ya oxygen
unakuwa umeokoa maisha yake ambayo labda angeyapoteza kwa kukosa hewa hiyo
muhimu,” alisema Mollel.
Siku ya Wanawake Duniani huadhimishwa Machi 8 kila mwaka, ambapo hutumika kufikisha
ujumbe wa kupambana na changamoto mbalimbali zinazokwamisha kupata haki zao na
usawa na kutoa wito wa kuhakikisha maisha ya wanawake yanaboreshwa katika Nyanja
mbalimbali ikiwemo elimu, lishe bora, afya ya uzazi, na maisha bora kwa ujumla.
Vodacom Tanzania Foundation inaendelea kusaidia Wanawake na Wasichana nchini pote
kuboresha maisha yao katika Nyanja za afya, elimu bora na kuwawezesha kujikomboa
kiuchumi kupitia ujasiriamali. Kwa kushirikiana na mashirika yasiyo ya kiserikali ya hapa
nchini na wadau wengine, taasisi imesaidia zaidi ya miradi 120 mpaka sasa ikiwa imewekeza
zaidi ya shilingi Bilioni 15 kwa ajili ya kuboresha maisha ya watanzania.